Mkapa hakuzuia mjadala - Msekwa; Akiri kasoro ya Bunge, asema maji yakimwagika …

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797
KASHFA YA RADA

Mwandishi Wetu

Toleo la 255
22 Aug 2012


  • Akiri kasoro ya Bunge, asema maji yakimwagika …
  • Zitto asema Bunge lilipaswa kuunda kamati ya kuchunguza
  • Kuharibika kwa rada hiyo kwatonesha upya machungu

KUHARIBIKA wiki iliyopita kwa rada iliyonunuliwa kwa bei kubwa katikati ya nyendo za kifisadi sasa kumeibua lawama kwa Bunge lililopita, lililokuwa chini ya Spika Pius Msekwa, Raia Mwema limebaini.


Kinachohojiwa sasa ni vipi Bunge wakati huo halikuamka usingizini kuungana na baadhi ya wabunge wa Uingereza, akiwamo Waziri wa Maendeleo ya Kimataifa, Clare Short, waliopaza sauti kupinga Tanzania isinunue rada hiyo kwa bei hiyo mbaya.


Katikati ya maoni hayo, yapo pia maoni mengine yanayotokana na kauli zinazokinzana na viongozi wa juu kabisa serikalini wengine wakisema wahusika wa ununuzi huo wafikishwe mbele ya sheria na wengine wakisema watu hao hawana cha kujibu na kwamba kesi ya rada haiwezi kuendeshwa Tanzania kwa vile ilikotokea, Uingereza, ilikwishakufungwa.


Ukiacha kwamba ununuzi huo uligubikwa na wimbi la ufisadi unaotajwa kuwahusisha wakubwa katika serikali ya Tanzania wakati huo, wafanyabiashara na kampuni ya uuzaji silaha ya Uingereza, BAE Sytems, wabunge wa Uingereza walikuwa wakisema pia ya kuwa teknolojia ya rada hiyo ilikuwa imepitwa na wakati.


Aidha, wiki mbili zilizopita, taarifa ya Ubalozi wa Uingereza kuhusiana na suala la rada hiyo ilisema Tanzania ina sheria zake na hivyo si hoja kwamba sheria za Uingereza zikiharamisha jambo, linaweza kuwa limeharamishwa Tanzania pia.


Msekwa, wiki hii akizungumza katika mahojiano na Raia Mwema kuhusu ukimya wa Bunge wakati huo kuhusu rada hiyo ambayo imekwisha rudisha fidia ya kiasi cha shilingi bilioni 78 nchini, fedha hizo zikipewa majina mengi kama vile chenji ya rada na rushwa ya rada, alisema tayari "maji yamemwagika, hayazoleki".


Mahojiano kati ya Msekwa, ambaye sasa ni Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi-Tanzania Bara yalikuwa hivi:


Mwandishi: Mheshimiwa Msekwa, wewe ndiye uliyekuwa Spika wakati mjadala kuhusu Tanzania kununua rada kutoka BAE-Systems ulivyopamba moto katika Bunge la Uingereza. Wabunge wa Uingereza walipinga lakini Bunge la Tanzania lilikaa kimya. Huoni kwamba hakumtanguliza maslahi ya Watanzania?


Mzee Msekwa: Ni kweli ...lakini yaliyopita si ndwele, tugange yajayo. Maji yamekwishamwagika, hatuna la kufanya.


Mwandishi: Huoni kwamba ukimya wenu ulikuwa kasoro kubwa sana na hamkuwatendea haki Watanzania mliokuwa mnawawakilisha?


Mzee Msekwa: Ni bahati mbaya tu, narudia kwamba hayo yamekwishatokea. Maziwa yakimwagika ndiyo hivyo tena.


Mwandishi: Kuna madai kwamba Rais Benjamin Mkapa ambaye alikuwa akitetea ununuzi wa rada hiyo kwa kushawishiwa na aliyekuwa Waziri Mkuu wa Uingereza, Tony Blair, ndiye aliyeshinikiza Bunge kutojadili suala hilo na hata kuunda kamati teule ya uchunguzi. Ni kweli?


Kwa swali hilo Mzee Msekwa alijibu: "Hapana. Ni kwamba hakuna hoja yoyote iliyowasilishwa bungeni na mbunge yeyote. Hata serikali haikuwahi kabisa kulileta suala hilo bungeni. Mimi ndiye niliyekuwa Spika, hilo suala halikufika kabisa ndani ya Bunge. Unajua bungeni kuna taratibu zake za kuwasilisha suala fulani."


Aliendelea: "Kuna kuwasilisha kwa njia ya hoja binafsi na taratibu nyingine. Hayo hayakufanyika, ndiyo maana nasema maji yamekwishamwagika, hayazoleki na yaliyopita si ndwele tugange yajayo."


Itakuwa kazi kubwa kunyamazisha kabisa suala hili la rada kwa vile wapo wanaoamini kwamba wahusika bado wanaweza kufikishwa mbele ya sheria ambazo huwabana wengine na hasa watu wadogo.


Kati ya hao ni Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Kabwe Zitto anayeamini kwamba Bunge la Msekwa lilapaswa kuwa makini zaidi na kutenda zaidi badala ya kukaa kimya.


Kwa mujibu wa Kabwe, kelele tu za wabunge wa Uingereza akiwamo Waziri wao Short aliyetishia hata kujiuzulu, zilitosha kuamsha Bunge la Tanzania kwa kuunda kamati ya uchunguzi ili kujiridhisha au kuokoa fedha za wananchi.


Katika kuonyesha makosa ya Bunge hilo la nane, Zitto anasema skandali hiyo ya rada ilihitaji kuundwa kwa kamati maalumu ya Bunge ya kuchunguza.


"Skandali ya rada ilihitaji parliamentary inquiry. Inasikitisha pia kwamba mjadala huu wa rada umekuwa ni kuhusu chenji na Andrew Chenge (amekuwa akituhumiwa kuhusika), lakini suala la ubora wa rada yenyewe halikupewa uzito unaostahili.


"Nadhani jambo la kufanya kwa sasa ni Serikali kuueleza umma hali halisi kuhusu rada hiyo na ubora wake na usalama wa nchi ukoje," alisema Zitto na kuongeza:


"Hata kama kutafikiwa uamuzi wa kununua rada mpya inabidi kuwa makini sana, tusiwape tena nafasi mafisadi kujinufaisha katika suala zima la ununuzi. Leo hii usalama katika anga letu ni wa shaka, hatuna uwezo wa kuona ndege hata za adui kama tukivamiwa".


Sasa, licha ya kununuliwa kwa fedha nyingi hadi kufikia hatua ya kurudisha kiasi cha fedha kilichozidi, rada hiyo ni mbovu na kuna njia mbili tu za kuirejesha ifanye kazi.


Njia hizo mbili kwa mujibu wa Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Fadhili Manongi, ni ama kuagiza kifaa kipya kutoka katika kampuni iliyouza rada hiyo au kukifanyia matengenezo kifaa hicho kilichoharibika ambacho kazi yake katika rada hiyo ni kusambaza umeme (power supply unit).


Rada hiyo iliyonunuliwa kwa Dola za Marekani milioni 40 na Serikali ya Tanzania kutoka BAE Systems ya Uingereza, haifanyi kazi tangu Agosti 3, mwaka huu, baada ya kutokea hitilafu katika kifaa cha kusambaza umeme.


Katika kashfa hiyo ya ununuzi wa rada, viongozi na wafanyabiashara kadhaa wamekuwa wakihusishwa.


Uchunguzi kuhusu ununuzi wa rada hiyo ulifanywa na Taasisi ya Makosa Makubwa ya Jinai (SFO) ya Uingereza, na kubaini kuwa Tanzania ilinunua rada hiyo kwa fedha nyingi kinyume cha bei halisi.











 
Hawa CCM bado kidogo watatajana VIZURI; naona baadhi yao Wamechoja JELA; Wengine Wameona CCM inaanguka na WENGI

Wasipotoka CLEAN CHAMA kingine kikichukuwa 5 star hotel yao itakuwa GEREZA la UKONGA kwa MAISHA yao; Hawawezi

Kukimbilia NJE watarudishwa na MAPOLISI wa NJE...
 
Hawa CCM bado kidogo watatajana VIZURI; naona baadhi yao Wamechoja JELA; Wengine Wameona CCM inaanguka na WENGI

Wasipotoka CLEAN CHAMA kingine kikichukuwa 5 star hotel yao itakuwa GEREZA la UKONGA kwa MAISHA yao; Hawawezi

Kukimbilia NJE watarudishwa na MAPOLISI wa NJE...

Wanasheria wanatakiwa kuliangalia hili kwa kina. kwani hii inaonekana wazi kabisa kuwa ni uhujumu uchumi kama si matumuizi mabaya ya ofisi je kinga ya raisi ni kwa kila jambo au ni kwamambo yanayo husu maslahi ya Taifa tu.
 
Back
Top Bottom