Candid Scope
JF-Expert Member
- Nov 8, 2010
- 11,890
- 6,898
Mishahara na marupuru ya wabunge kwa nchi masikini Kusini mwa Jangwa la Sahara, Tanzania ikiwamo imeelezwa kuwa ni mzigo kwa wananchi wanaowaongoza, utafiti umebaini.
Kutokana na hali hiyo, utafiti huo umependekeza kuwa nchi hizo ziunde taasisi huru ya kupanga mishahara na marupurupu ya wabunge, mawaziri, rais na watumishi wengine wa kada ya juu kwenye utumishi wa umma, ili kudhibiti gharama hizo.
Akiwasilisha matokeo ya utafiti ulioangalia kama Afrika inaweza kumudu gharama za demokrasia, Mtafiti wa Taasisi ya Utafiti wa Kuondoa Umaskini (Repoa), Dk. Theodore Valentine, alisema wabunge wanapata pato kubwa kwa sababu wana uhuru wa kujiongezea mishahara na posho.
Alisema jambo hilo linafanya demokrasia kuwa ghali zaidi kwa nchi masikini zilizo Kusini mwa Jangwa la Sahara kutokana na mishahara na marupurupu makubwa yanayotolewa kwa wabunge na watumishi wengine wa umma wakiwamo marais, bila kuangalia hali halisi ya Pato la Taifa.
Alisema kuundwa kwa Taasisi huru kutasaidia kupanga mishahara hiyo kulingana na uchumi wa nchi na pia itaongeza uwazi wa kipato cha watumishi wa umma.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Repoa, Profesa Samuel Wangwe, alisema ni Taasisi huru ndiyo itasaidia kupanga mishahara ya wabunge kulingana na uchumi wa nchi ikizingatiwa kuwa wananchi wengi bado ni masikini.