Mgogoro wa Ukraine umeendelea kwa zaidi ya miezi miwili. Baraza la Wawakilishi la Bunge la Marekani hivi karibuni lilipitia mpango wa msaada wa takriban dola bilioni 40 kwa Ukraine. Mpango huo utakabidhiwa kwa Baraza la Seneti, ambapo unatarajiwa kupitishwa kwa mafanikio.
Takwimu zilizotolewa na Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani zinaonesha kuwa, tangu Joe Biden aingie madarakani, misaada iliyotolewa na Marekani kwa Ukraine imezidi dola bilioni 4.3 za Kimarekani. Lakini badala ya kusaidia Ukraine, misaada hiyo itatatiza zaidi nchi hiyo inayokumbwa na mzozo wa kijiografia.
Kwa mujibu wa CNN, Rais Joe Biden wa Marekani ametaka bunge la nchi hiyo kupitisha mpango huo wa kuisaidia Ukraine mara moja, kwa kuwa msaada wa sasa utaisha hivi karibuni. Licha ya hayo, Biden siku hiyo hiyo pia amesaini muswada wa sheria wa Ukodishaji wa Ulinzi wa Kidemokrasia kwa Ukraine, ambao ulipitishwa mwezi Aprili na mabaraza ya Wawakilishi na Seneti ya bunge la Marekani. Mswada huo utakapoanza kutekelezwa, utarahisisha sana mchakato wa Marekani kutoa msaida wa kijeshi na misaada mingine muhimu kwa Ukraine.
Je, kwa nini Marekani inatoa kiasi kikubwa cha fedha kuiunga mkono Ukraine? Na misaada hiyo inaweza kuisaidia Ukraine kujiondoa katika mgogoro na Russia?
Wachambuzi wanaona kuwa, Marekani kuendelea kutoa silaha na fedha kwa Ukraine si kwa ajili ya demokrasia, uhuru au haki ya kimataifa kama inavyodai, lengo lake halisi linalofichwa ni kwamba Marekani inatumai kuzidisha mzozo kati ya Russia na Ukraine, ili kupunguza nguvu na ushawishi wa Russia. Licha ya hayo, kupitia misaada hiyo yenye thamani kubwa, mashirika ya silaha nchini Marekani yatapata faida kubwa.
Kwa upande wa Ukraine, kile kinachoitwa kama “mkono wa msaada” uliotolewa na Marekani utaitatiza zaidi nchi hiyo inayokumbwa na vita na Russia, ambayo ni moja ya nchi yenye nguvu zaidi ya kijeshi duniani. Kati ya misaada iliyotolewa na Marekani, mingi ni ya kijeshi, ili Ukraine iendelee kuwa mstari wa mbele wa Marekani kukabiliana na Russia, na kuendelea kumwaga damu kwenye vita.
Serikali ya Marekani inapaswa kubeba jukumu kubwa kwa kuzuka kwa mzozo wa Russia na Ukraine. Mwandishi wa gazeti la New York Times Thomas Friedman amesema, makosa makubwa ya Marekani ya kufanya maamuzi juu ya upanuzi wa NATO yalisababisha kuzorota kwa uhusiano kati ya Russia na Ukraine, na serikali ya Marekani inapaswa kubeba jukumu la vita kati ya nchi hizo mbili.
Profesa mstaafu wa Taasisi ya Utafiti wa Kiuchumi katika Chuo Kikuu cha Jawaharlal Nehru nchini India Prabhat Patnaik amesema, Mgogoro kati ya Russia na Ukraine ni uthibitisho mwingine wa umwamba wa Marekani, na chanzo kikubwa cha mgogoro huo ni kwamba, Marekani haipendi nchi za Ulaya kuendeleza uhusiano wa karibu wa kiuchumi na Russia.
Watu wengi duniani wanaona kuwa mzozo kati ya Russia na Ukraine unatokana na ubinafsi wa nchi za Magharibi zinazoongozwa na Marekani katika miaka 30 iliyopita. Ikiwa kwenye kitovu cha dhoruba, Ukraine haitaweza kunufaika na misaada ya Marekani, bali itazamishwa zaidi katika tatizo la kisiasa la kijiografia.