Mikataba ya Mwinyi, Kikwete kufilisi nchi

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797




mwinyi_233.jpg




VIONGOZI walioingiza serikali katika mikataba mikubwa mitatu ya utata, wameliandalia taifa mzigo mkubwa wa madeni yasiyolipika hata katika miaka 50 ijayo, MwanaHALISI limeelezwa.
Wakati Dowans wanadai Sh. 94 bilioni, IPTL wanadai zaidi ya Sh. 248.6 bilioni kwa serikali/TANESCO kuvuruga mkataba wake.
Mikataba yenye utata na inayotishia kuangamiza taifa ni ile ya kuzalisha umeme ya makampuni ya IPTL, Richmond na Dowans iliyosainiwa wakati wa utawala wa Rais Ali Hassani Mwinyi na rais Jakaya Kikwete.
Pamoja na makampuni hayo kukaba koo serikali na kuifikisha katika mahakama na tume mbalimbali za kimataifa za usuluhushi, gharama za serikali kujitetea zinaendelea kuongezeka.
Katika kipindi cha miaka mitano tu iliyopita, serikali imetumia zaidi ya Sh. 23 bilioni kujitetea, kwa kulipa makampuni ya uwakili. Gharama hizi zinaongezeka mwaka hadi mwaka kufuatia kesi kuchukua muda mrefu na hata kufumuka kwa kesi mpya.
Sehemu ya mabilioni hayo ya shilingi imelipwa kwa makampuni ya wanasheria ya Mkono and Company Advocates ya Tanzania na Hunton and William ya Marekani kwa kutetea TANESCO iliyoshitakiwa na kampuni ya Independent Power Tanzania Limited (IPTL).
Mabilioni mengine yamelipwa kwa makampuni ya mawakili ya Rex Attorney ya Tanzania na Reed Smith ya Uingereza kwa kutetea TANESCO katika kesi iliyofunguliwa na kampuni ya Richmond Development Company (LLC).
Rex Attorneys na Reed Smith wamelipwa au watalipwa pia mabilioni ya shilingi kwa kutetea TANESCO katika shauri lililofunguliwa na makampuni ya Dowans Holdings S.A na Dowans Tanzania Limited (DTL) katika mahakama ya kimataifa ya usuluhishi wa kibiasha (ICC).
Nyaraka zinaonyesha kuwa tayari Mkono and Company Advocates na Hunton and William wamelipwa na TANESCO kiasi cha dola 11,818,542.89 (sawa na karibu Sh. 17 bilioni).
Kampuni ya Mkono and Company Advocates inamilikiwa na mbunge wa Musoma Vijijini (CCM), Nimrod Mkono.
Aidha, kampuni ya Mkono imelipwa pia kiasi cha Sh. 8.5 milioni kwa kusimamia shauri lililofunguliwa na benki ya Standard Chartered Bank ya Hong Kong dhidi ya serikali katika shauri la kukatisha mkataba wa IPTL. Serikali na IPTL waliingia mkataba mwaka 1994.
Nyaraka zinaonyesha kuwa Rex Attoney na mwenzake walilipwa kiasi cha dola 3,574,351.51 (karibu Sh. 5 .2 bilioni) katika shauri lililofunguliwa na makampuni ya Dowans Holdings S.A na Dowans Tanzania Limited (DTL) katika mahakama ya kimataifa ya usuluhishi wa kibiasha (ICC).
Mawakili hao pia wamelipwa dola 860,056.71 (karibu sawa na shilingi 1.2 bilioni) kwa kazi ya kutetea TANESCO dhidi ya kesi iliyofunguliwa na kampuni ya Richmond Development Company (LLC) na kusikilizwa katika Falme za Kiarabu.
Kuibuka kwa taarifa hizi kumekuja mwezi mmoja baada ya mbunge wa Bumbuli (CCM), January Makamba kuibua kile kilichoitwa, “taarifa juu ya upatikanaji wa umeme nchini,” ambapo tarehe 3 Februari 2011 alitaka waziri wa nishati na madini, William Ngeleja kueleza hatua zinazochukuliwa na TANESCO katika kukabiliana na mgawo wa umeme na mzigo wa kesi unaolikabili.
Katika barua hiyo, Makamba anasema, “Katika viambatanisho vya hukumu ya ICC, kama ilivyosajiliwa mahakama kuu ya Tanzania zipo nyaraka zinazoonyesha kwamba mwanasheria aliyeishauri TANESCO kuvunja mkataba na Dowans – kwa kusema kwamba siyo mkataba halali na kwamba hakuna madhara ya kisheria kuuvunja – ndiye huyohuyo pia aliyeshauri benki ya Stanbink kutoa mkopo wa dola za 120 kwa Dowans – kwa kusema kwamba ni kampuni halali, inakopesheka na ina mkataba halali na TANESCO.”
Anasema, “Ni mwanasheria huyohuyo aliyewakilisha TANESCO kwenye kesi iliyofunguliwa na Dowans, kesi ambayo ilitokana na ushauri wake, na baada ya hukumu ndiye huohuyo, kwa mujibu wa maelezo yako mheshimiwa waziri ya tarehe 6 Januari 2011, aliyetoa ushauri kwamba hakuna njia nyingine zaidi ya kuilipa Dowans.”
Makamba alitaka serikali kueleza suala hilo kwa ufasaha ili kuondoa kile alichoita, “picha inayoweza kuonyesha serikali ilikosa umakini kwenye jambo hili zima na maadili hayakuzingatiwa.”
Alisema itakuwa vema taarifa ya serikali ikieleza ni wanasheria gani waliotumiwa na TANESCO kwa kila hatua katika shauri lake Dowans kwa kuanzia kwenye ushauri na kabla ya kuvunjwa kwa mkataba.
Akijibu hoja za Makamba, Ngeleja anakiri kuwa benki ya Standard Chartered ya (Hong Kong) ambayo ni benki tanzu ya Standard Chartered ya Uingereza inayomiliki asilimia kubwa ya hisa za IPTL Tanzania Ltd., wameishitaki serikali kwa madai ya kutumia mitambo yake ya kuzalisha umeme kupitia Provisional Liquidator hivyo kukiuka Bilateral Investment Treaty (BIT) kati yake na serikali ya Uingereza.
Kesi hizo ni Na. ARB /10/20 iliyofunguliwa na Standard Chartered Bank (Hong Kong) dhidi ya TANESCO, tarehe 1 Oktoba 2010 na kesi Na.ARB/10/12 iliyofunguliwa tarehe 11 Juni 2010.
Katika shauri hilo, IPTL wanataka mahakama “iamuru serikali kutoa tamko la kukiri kukiuka mkataba wa uwekezaji wa kimataifa – Bilateral Investment Treaty (BIT) na kulipa fidia ya dola 118.6 milioni, pamoja na kulipa gharama zote za uwekezaji - capacity charges – ambazo shirika hilo hazijazilipa tokea mwaka 2007 pamoja na fidia ya dola 130 milioni.”
Ngeleja anasema chimbuko la kesi hizo ni mgogoro wa awali kati ya Taneso na na IPTL ambao uliwasilishwa ICSID, Novemba mwaka 2007. Kesi zilizotajwa ziko katika hatua za awali na zinatarajiwa kuanza kusikilizwa Aprili mwaka huu.
Akijibu madai ya njia iliyotumika kupatikana kwa makampuni ya wanasheria, Ngeleja anasema “TANESCO iliona ni busara kuendelea kuwatumia mawakili walewale (Mkono and Company Advocates) kwa kuwa wana taarifa muhimu kuhusiana na kesi husika.
Anasema, “Kampuni ya Mkono ilianza kushughulikia shauri la IPTL tangu mwaka 2007 baada ya kupendekezwa na serikali kuwa washauri wa Kamati ya serikali ya ununuzi wa deni la IPTL. Kutokana na uelewa wa mawakili hao juu ya IPTL, ilionekana ni busara waendeshe kesi hiyo.”
Kuhusu kampuni ya wanasheria ya Rex Attorney, Ngeleje anasema, ilipewa kazi ya ushauri baada ya ushindani uliohusisa kampuni tatu za FK Law Chambers, IMMA Advocates na Mkono. Anasema katika shauri la Dowans, TANESCO waliamua kuichukua tena Rex kwa ilikuwa na uzoefu na mkataba huo.
Katika shauri hilo, mahakama ya ICC imeamuru TANESCO kulipa kiasi cha dola 94 milioni (Sh. 134 bilioni) kutokana na kushindwa katika kesi hiyo.
Kwa mujibu wa uchunguzi wa MwanaHALISI, kampuni ya Mkono ililipwa na TANESCO – miezi miwili kabla ya uchaguzi, 19 Agosti 2010 kiasi cha dola 1,088,550.00 (karibu Sh.1.6 bilioni). Malipo hayo yalifanywa kupitia ankara Na. 124/10.
Aidha, kabla ya Mkono kuchukua kitita hicho cha fedha, tarehe 15 Julai 2009, TANESCO walilipa mwanasheria huyo kiasi cha dola 2,177,100.00 (karibu Sh. 3.7 bilioni). Fedha hizo zililipwa kupitia ankara Na. 069/09 kwa kile kilichoitwa kazi za usuluhishi kati ya TANESCO na IPTL.
Nayo Rex Attonery, imelipwa na TANESCO kiasi cha dola 47,552.25 kupitia ankara Na. 456/10 ya 28 Septemba 2010 kwa kazi za ushauri katika kesi Na. 15910 iliyofunguliwa na kampuni ya Richmond katika mahakama ya ICC dhidi ya TANESCO. Malipo mengine ya dola 472,000.00 yamefanyika 23 Juni 2010 kupitia ankara Na. 34/10 kwa ajili ya masuala ya usuluhishi katika kesi Na. 15910 kati ya TANESCO na Richmond. Dola 83,504.46 zililipwa tarehe 9 Aprili 2010 kama gharama za kukodishia chumba cha kusikilizia usulihushi kati ya TANESCO na Richmond kwa kesi hiyohiyo.
 
Back
Top Bottom