Katika hili la Samata, lawama TFF haziepukiki
Tullo Chambo
KARIBUNI tena katika Jumatatu hii ya Uwanja wa Kuchonga, kama kawaida ni kupeana changamoto za kimichezo ili kuchochea ufanisi katika sekta hii muhimu katika jamii ya Michezo.
Bila shaka mu wazima wa afya njema na mnaendelea na makukumu yenu halali ya kila siku, kwa Wakristo naendelea kuwatakia maadhimisho mema ya sikukuu hii ya Pasaka, ambayo leo ni ‘Jumatatu ya Pasaka',.
Kama ilivyo ada na kwa manufaa ya wale ambao kwa namna moja ama nyingine hatukuwa pamoja Jumatatu iliyopita Uwanjani, tupeane dondoo kidogo ya mada ya iliyopita. Wiki iliyopita Uwanjani, tulizungumzia jinsi ubabaishaji ama ubovu, udhaifu au ulaghai unaofanywa na baadhi ya kampuni ambazo hivi sasa zinajishughulisha na shughuli ya kuandaa mapambano ya ngumi za kulipwa hapa nchini.
Kwa takribani miaka kadhaa sasa, mchezo wa ngumi, hususan zaidi ngumi za kulipwa umekuwa ukijipunguzia mashabiki na hata kukubalika kwake katika jamii ya kitanzania kutokana na kutawaliwa na vitendo visivyo vya kiungwana na ambavyo hata wakati mwingine ni kinyume cha sheria, hivyo kupoteza maana nzima ya michezo.
Katika kuzidi kujipambanua kwa mambo hayo, hivi karibuni ilizidi kujidhihirisha kuwa ngumi za kulipwa ni ubabaishaji mkubwa na mchezo usio wa kistaarabu, baada ya kuzidi kugubikwa na vurugu badala ya furaha na upendo, kama ilivyo dhana nzima ya michezo.
Tulilazimika kulaani tabia hizi katika ngumi za kulipwa pale, kwa mara nyingine iliposhuhudiwa katika pambano lililowakutanisha mabondia maarufu, Mada Maugo na Japhet Kaseba kugubikwa na vurugu na uvunjifu wa amani.
Basi, baada ya ukumbusho huo kwa ufupi, sasa turejee katika mada yetu ya leo. Hivi sasa imeshuhudiwa anga la michezo likigubikwa na masuala ya usajili hivi sasa hapa nchini.
Lakini kubwa lililonisukuma leo, ni suala la malumbano ya uhalali wa klabu ambayo inammiliki mchezaji chipukizi mwenye kipaji, ambaye hivi sasa ametokea kuliteka wimbi la usajili hapa nchini, Mbwana Samatta anayekipiga klabu ya Simba ya jijini Dar es Saalam.
Mchezaji huyu ambaye amecheza nusu msimu katika klabu ya Simba, baada ya kushindwa kuafikiana na uongozi wa klabu hiyo msimu wa kwanza, ambako alikuwa akitokea African Lyon pia ya jijini Dar es Salaam, hivi sasa ameibua malumbano makubwa juu ya uhalali wake, hasa baada ya klabu ya TP Mazembe ya DRC kutangaza kumnyakua kwa kitita cha dola 100,000 za Marekani baada ya kukunwa naye wakati walipokutana katika mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika.
Mara baada ya klabu ya Simba kuweka bayana mipango yake ya kumuuza Samatta TP Mazembe, African Lyon ambayo asili yake ni iliyokuwa Mbagala Market, iliibuka na kudai kuwa mchezaji huyo ni wa mali yao na kuwa ndio wenye kustahili kupokea kitita hicho kutoka Mazembe.
Kwanza suala hili unaweza kuliona kama sinema, ambayo hadi sasa ilipofikia, Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), ndilo muhusika mkuu katika uhalali wa sakata hili lilivyoibuka.
Lakini kwa haraka haraka, embu jiulize, inakuwaje Samatta ambaye TFF ilimpitisha msimu uliopita wa usajili kuwa ni halali kuichezea Simba, leo baada ya kuibuka suala la neema ya ‘faranga' kupitia chipukizi huyu, Lyon inakuja na kudai ni mali yake! Inashangaza sijui wakati wote wa Ligi ilipoanza ilikuwa wapi?
Lakini, wao TFF tayari kupitia katibu mkuu wake, Angetole Osiah imeabainisha kuwa, kwa mujibu wa taratibu zao za usajili, Samatta ni mali ya Simba na kulikuwa kuna kipengele cha makubaliano kati ya klabu hizo mbili, Lyon basi wawasilishe vielelezo katika Shirikisho hilo ili iweze kuapta haki yake.
Inashangaza! Kama TFF inasema Samatta ni hali Simba, inakuwaje kuitaka Lyon iwasilishe vielelezo vingine, ina maana Shirikisho hili ambalo linaendeshwa na watu walioaminika na wadau na kuchaguliwa au kupewa dhamana ya ajira, kufanya kazi kwa ubabaishaji na udhaifu wa hali ya juu.
Bila shaka kanuni, miongozo na sheria za usajili TFF ziko wazi kabisa, leo hii inakuwaje zinashindwa kusimamiwa ipasavyo na kuepuka malumbano yasiyo na maana na hata kulidhalilisha soka la Tanzania na hata ikiwezekana kumuharibia mipango yake mchezaji husika.
Nasisitiza kuna udhaifu mkubwa katika baadhi ya watendaji wa TFF kushindwa kusimamia na kuzitekeleza kanuni na taratibu zinazohusiana na usajili, kutokana na baadhi ya vielelezo ambavyo Lyon ilivianika hewani siku moja tu, baada ya Osiah kuwataka kufanya hivyo.
Lakini kilichonisukuma zaidi kuitupia lawama TFF, ni baada ya kuona baadhi ya nyaraka za Lyon, ambazo kimsingi zinaweza kutowahalalisha kuwa Samatta ni wao asilimia 100, ambazo ndizo zinawapa kiburi cha leo kulianzisha hili, ingwaje sijui nusu msimu mzima tangu aanze kuichezea Simba hawakuwahi kuibuka kudai taratibu hazikukamilishwa au kufuatwa.
Baadhi ya vielelezo hivyo ni kama ile barua ya Novemba 15, 2010 ya Lyon kwa TFF kuomba kibali cha mchezaji huyo kufanya majaribio katika klabu ya Lisboa ya Ureno, kupitia barua yenye kumbukumbu ALFC/KB/TFF/15-2010, ikieleza majaribio yake yaanze Desemba 3 hadi Januari mwaka huu. TFF ilishughulikia suala hili, ambako pia lilikuwa likumuhisha mchezaji mwingine Hamis Thabit yenye kumbukumbu namba TFF/ADM/Vs-10/32, ya Novemba 20, ikiwatambua ni wachezaji wa African Lyon kwa msimu wa 2010/11.
Lakini pia, katika kuonyesha kuwa kulikuwa na longolongo au baadhi ya makubaliano hasa ya malipo hayakuwa yamekamilishwa ndani ya muda muafaka, kulikuwa na vikao vya kumalizia usajili vichochoroni, kimojawapo kikiwa cha Julai 21, 2010 cha viongozi wa Lyon na Simba ambacho kiliwashirikisha Kassim Dewji, Mohamed Dewji ‘Mo', Crencentius Magori, Godfrey Nyange ‘Kaburu' na Mulamu Ng'ambi, ambako inadaiwa ilikubaliwa uandaliwe utaratibu wa kuwalipa kupitia mechi mbili, ambazo ni African Lyon na Simba na ile ya Simba na Yanga, lakini hakuna mafanikio.
Inasikitisha, lakini ndivyo mambo yalivyo, ambako wakati huo Lyon nao hawakudiriki kupaza hewani sauti zao kulalamika kuwa wanadhulumiwa au kuna sheria zimepindishwa. Huu ndio usanii unaobarikiwa na TFF kwa baadhi ya vigogo na hatimaye kuja kuibuka mitafaruku kama hii.
TFF ingekuwa makini katika kusimamia utekelezaji wa kanuni na sheria zake, muda wa usajili ukipita basi umepita na kutoruhusu mikataba ya pembeni ambayo hata yenyewe haikumbuki kuisajili, bila shaka kwa kuwa inafanyika kinyume na taratibu, masuala kama haya ya Samatta yasingeibuka na kuleta matatizo haya.
Haya Lyon mbali ya Samatta, imeibuka na madai mengine kuwa, hata mchezaji mwingine Rashid Gumbo naye si halali kwa Simba bali mali yao, kazi nyingine hiyo, lakini kimsingi ni udhaifu wa usimamizi na utekelezaji ndani ya TFF.
Hivi ikija kuthibitika malalamiko ya Lyon yana hoja hasa kutokana na kujikanganya kwenyewe kwa TFF athari zake mbele zikoje? Sijui kama wanaliona hili, au wanategemea yale yale ya uungwana na kusaidiana kumalizana nje ya taratibu.
Yote kwa yote, ubabaishaji TFF ndio chanzo cha malumbano au matatizo haya ya uhalali wa Samatta na iwe tayari kupokea lolote litakalotokea. Kila la heri, tukutane wiki ijayo.