Michezo magazetini leo...

Michezo magazetini leo...

Status
Not open for further replies.
Azan ampa pole Mzee Yussuf


na Abdallah Menssah


amka2.gif
MBUNGE wa Kinondoni, Idd Azan amemtumia salamu za pole, Mfalme wa mipasho na Mkurugenzi Mkuu wa kundi la Jahazi Modern Taarab, Mzee Yussuf, kutokana na kuugua kwake.
Azan alitoa salamu hizo za pole ofisini kwake jijini Dar es Salaam jana katika mazungumzo maalumu na mwandishi wa habari hizi.
Alisema kuwa amelazimika kumtumia Yussuf salamu za pole kwa sababu yeye ni Mbunge wa Kinondoni anakoishi msanii huyo na anathamini pia mchango wake katika muziki na sanaa kwa ujumla.
"Unajua, muziki ni kati ya vyanzo vya maendeleo hapa nchini, hivyo hatuna budi kuwafariji wanamuziki wetu na kuwa nao bega kwa bega wanapopatwa na matatizo kwa kuwa wao ndio wanaofanya muziki uwepo," alisema Azan.
Aidha, Azan alisema kuwa pia anawaomba wapenzi, mashabiki pamoja na wadau wengine wote wa muziki kuzidi kumuombea Yussuf apate nafuu haraka.
Alisema kwa kuonyesha anawajali na kuthamini mchango wa wasanii wilayani Kinondoni, amepanga kuhudhuria onyesho la kwanza kwa Yussuf kupanda jukwaani akiwa na kundi lake la Jahazi.
"Kadhalika, kama siku mbili hizi kama nitapata nafasi, basi nitakwenda kumjulia hali huko kisiwani Zanzibar alikopumzika kabla hajaanza kazi," alisema Azan.
Onyesho la kwanza kwa Yussuf kupanda jukwaani ni lile lililopangwa kurindima katika mkesha wa Siku ya Wapendanao ‘Valentine's Day', kwenye ukumbi wa Travertine Hotel, Magomeni, jijini Dar es Salaam.
 
Waziri afagilia Tamasha la Pasaka kusaidia yatima


na Mwandishi wetu


amka2.gif
NAIBU Waziri wa Uchukuzi, Dk. Athuman Mfutakamba, amelisifia tamasha la Pasaka kwa kusema kwa kitendo cha sehemu ya fedha hizo kusomesha yatima na kuwasaidia yatima, hilo ni zaidi ya tamasha.
Akizungumza jijini Dar es Salaam juzi, Mfutakamba alisema amepata faraja kubwa na Msama Promotions inayoratibu tamasha hilo kuyajali makundi hayo maalumu kwenye jamii.
"Nimefarijika mno na muamko huu, kwakweli huu ni mfano wa kuigwa kwani ni watu wachache mno wanaoweza kuandaa matamasha kama haya na fedha zinazopatikana kuwasaidia watoto yatima na wajane," alisema Mfutakamba.
Aidha, Mtufakamba amesema kwamba kwa kiasi kikubwa, tamasha hilo pia litasaidia kupunguza tatizo la ajira kwa vijana, kwani wengi hivi sasa wameamua kujikita katika muziki wa injili kwa ajili ya kumuimbia Mungu na kujipatia kipato.
"Unapokuwa na watu wenye uzalendo kama Msama Promotions kwa hakika kabisa vijana wengi watajitokeza na watahamasika kujiingiza katika muziki huu, kwani watakuwa na uhakika wa kujipatia kipato," alisema Mfutakamba.
Tamasha kubwa la Pasaka linatarajiwa kufanyika Aprili 24 mwaka huu siku ya Sikuu ya Pasaka katika Ukumbi wa Diamond Jubilee jijini Dar es Salaam na baadaye kufanyika mjini Shinyanga Jumatatu ya Pasaka, Aprili 25 na jijini Mwanza Aprili 26, lengo lake kubwa mwaka huu ni kwa ajili ya kuwasomesha watoto yatima na kuwasaidi mtaji wa biashara wanawake wajane.
Msama Promotions chini ya Mkurugenzi wake, Alex Msama, ndiyo imechangia kwa kiasi kikubwa kukua kwa muziki wa injili nchini kupitia matamasha mbalimbali kama ya Krismasi na Pasaka, achilia mbali yale ya uzinduzi wa albamu mbalimbali.
 
Miwa yailewesha Yanga
• Mashabiki wawashukia viongozi, wachezaji

na Ruhazi Ruhazi


amka2.gif
WAKATA miwa wa Mtibwa Sugar ya Manungu Turiani, Morogoro jana walitibua rekodi ya Yanga ya kutopoteza mechi katika Ligi Kuu Bara baada ya kuichapa bao 1-0 kwenye Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam.
Bao pekee lililoizamisha Yanga lilifungwa na mtokea benchi, Juma Javu, dakika ya 70, akiunganisha krosi ya Juma Abdu, aliyeambaa na mpira wingi ya kulia na kumimina krosi iliyowapita walinzi wa Yanga na kumkuta mfungaji.
Kuingia kwa bao hilo kuliwafanya Yanga kuzinduka na kupeleka mashambulizi mengi langoni mwa Mtibwa, lakini kukosa umakini na mbinu kwa washambuliaji wao kukawagharimu kushindwa kusawazisha.
Vincent Barnabas aliyeingia badala ya Ally Mohammed nusura aipigie Mtibwa bao la pili dakika ya 80 lakini shuti lake likambabatiza mlinzi wa Yanga, Chacha Marwa.
Mlinzi chipukizi wa Yanga anayecheza pembeni kushoto Zuberi Ubwa, nusura aipatie Yanga bao la kusawazisha dakika za lala salama lakini shuti lake la mita 30 lilipanguliwa na kipa Shaban Kado na kuwa kona ambayo haikuzaa matunda.
Hadi mwamuzi Alex Mahagi kutoka Mwanza anamaliza pambano hilo, ni Mtibwa Sugar waliotoka kidedea wakijikusanyia pointi zote tatu, huku mashabiki wa Yanga wakirusha maneno makali nje ya uwanja huo.
Huu ni mchezo wa kwanza wa Ligi Kuu kwa Yanga kucheza chini ya Fred Minziro, baada ya Kocha aliyeifikisha hapo Kostadin Papic kuiacha timu hiyo wiki iliyopita.
Baada ya mechi hiyo kumalizika, mashabiki waliokuwa na hasira walitaka kumshusha kwenye gari la wachezaji, kiungo wao Godfey Bonny ‘Ndanje', kwa madai kuwa alikuwa akimnyima pasi za kufunga mshambuliaji Mzambia Davies Mwape, kabla ya Jerry Tegete kuokoa jahazi kwa kuwaambia kuwa watakwenda kuyamaliza wenyewe mambo hayo.
Baada ya kumkosa Bonny, mashabiki hao walimvaa Makamu Mwenyekiti, Davis Mosha ambaye alijifungia ndani ya gari lake aina ya Noah, ingawaje mashabiki hao walifanikiwa kuvunja kioo cha nyuma na kumtwanga jiwe akiwa ndani kabla ya gari hilo kuondolewa kwa kasi na kutoweka eneo hilo la uwanja.
Mashabiki hao, ambao walikuwa wamegawanyika makundi kila moja likilaumu baadhi ya viongozi, pia walimweka kati mjumbe wa Kamati ya Utendaji, Mohammed Bhinda kwa madai hayo hayo ya kuwashawishi wachezaji kucheza chini ya kiwango, lakini alijitetea na kupona kupokea kibano.
Mosha akizungumzia hali hiyo, alisema itafika wakati wataachia Yanga hao, kwani anaona hakuna kitu kinachoendelea, ingawa yeye yuko hapo kwa ajili ya kutetea masilahi ya wanachama ambao ndio waliomchagua.
Vikosi Yanga, Nelson Kimathi, Fred Mbuna, Abuu Ubwa, Chacha Marwa, Nadir Haroub ‘Cannavaro', Godfrey Bonny, Juma Seif, Jerryson Tegete, Davies Mwape na Kigi Makasi/Nsa Job.
Mtibwa Sugar, Shaban Kado, Juma Abdu, Yussuf Nguya, Obadia Mungusa, Salum Swedi, Julius Mrope, Faustin Lukoo, Omari Matuta, Ally Mohammed/Vincent Barnabas na Lameck Dayton/Yussuf Mgwao/ Hussein Javu.
Leo Simba inashuka katika dimba hilo kuvaana na African Lyon katika mfululizo wa ligi hiyo.
 
Yanga: Papic katoroka


na Dina Ismail


amka2.gif
UONGOZI wa Yanga umesema kuwa aliyekuwa Kocha wake Mkuu, Mserbia Kostadin Papic, ametoroka na mamilioni ya fedha za klabu hiyo hivyo wanafanya taratibu za kisheria ili kumnasa.
Papic inadaiwa alitoroka nchini juzi usiku kwenda kwao Serbia, huku uongozi wa timu hiyo ukisema kwamba hatAweza kuondoka mpaka pale atakapojibu shutuma mbalimbali zinazomkabili.
Mwenyekiti wa Yanga, Wakili Lloyd Nchunga, aliwaambia waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana kwamba Papic aliamua kujiuzulu na kutoroka baada ya kuona huenda aliyoyafanya yataweza kumletea matatizo.
Alisema, Papic alifanya usajili wenye utata kwa kuwalipa wachezaji fedha pungufu za usajili, wakati hela zote zilitolewa, huku akimtolea mfano Omega Seme, ambaye alimpa sh milioni 10 badala ya 15 zilizotolewa.
Nchunga pia alisema, kocha huyo alichakachua fedha za usajili wa Mghana Kenneth Assamoh kwa kuidanganya klabu aliyotoka kuwa Yanga imemsajili kwa mkopo, wakati fedha za usajili wake zilitolewa.
Kama hiyo haitoshi, Papic alitumia fedha za kumsajili kipa kutoka Serbia, Ivan Knezevic, huku pia akiondoka na dola 3,000 alizokopa Agosti mwaka jana.
"Tutamfuatilia kwa namna moja ama nyingine yeye pamoja na wengine wanaohusika katika sakata hili, tutawachukulia hatua za kisheria," alisema Nchunga.
Hata hivyo, habari zilizopatikana jana zinadai kuwa mmoja wa viongozi wa Yanga anahusika katika mchakato wa kumtorosha Papic.
Katika hatua nyingine, makocha wanne kutoka nchi mbalimbali wamejitokeza kuomba kibarua cha kumrithi Papic.
Nchunga alisema tayari wameishafanya mazungumzo na mmoja kati ya hao, Sam Timbe, ambayo yanakwenda vizuri lakini hatima yake itajulikana katika kikao hicho.
Aliwataja makocha wengine ambao wametuma wasifu wao (cv), kuwa ni Roy Barego wa Uingereza anayeishi nchini Afrika Kusini, ambaye aliwahi kuinoa timu ya taifa ya Zimbambwe, wengine wanatoka Yugoslavia na Serbia.
Pia Nchunga alimtangaza Mwesigwa John Selestine kuwa kaimu katibu mkuu wa klabu hiyo mpaka pale mchakato wa kumpata katibu wa kudumu utakapokamilika, ajira hiyo imeanza Februari mosi.
 
Wagosi wazidi kutakata Ligi Daraja la Kwanza


na Safari Chuwa, Tanga


amka2.gif
WENYEJI wa Ligi Daraja la Kwanza hatua ya tisa bora, Coastal Union ‘Wagosi wa Kaya' wa hapa, jana walizidi kupalilia njia ya kurejea Ligi Kuu Bara msimu ujao baada ya kuwafumua Moro United mabao 2-1.
Kwa matokeo ya mechi hiyo iliyochezwa kwenye Uwanja wa Mkwakwani, Coastal Union wamefikisha pointi sita baada ya kushinda mechi zote mbili.
Kabla ya kukutana na Moro United, Coastal Union waliwafunga Villa Squad ya Kinondoni bao 1-0.
Katika mechi ya jana ambayo ilichezwa mapema, wenyeji Moro United walikuwa wa kwanza kuziona nyavu za Coastal Union dakika ya 16 mfungaji akiwa Henry Ngonye, baada ya beki wa Coastal Union, Mohamed Danstan, kukawia kuokoa mpira katika eneo la lango lake.
Hata hivyo, Coastal Union walicharuka na kufanikiwa kusawazisha bao hilo dakika ya 20, likifungwa na Daniel Lyanga akimalizia mpira uliotemwa na kipa wa Moro United, Lucheke Mussa, kutokana na shuti la Kibabu Chandiga.
Bao hilo liliwapa nguvu Coastal Union ambao waliongeza kasi ya mchezo na dakika ya 35, walifunga bao la pili, likiwekwa wavuni na Shafii Kaluwani kwa pasi ya Mohamed Issa.
Licha ya timu hizo kushambuliana kwa nguvu, lakini hadi mapumziko, Coastal Union walikuwa mbele kwa mabao hayo 2-1.
Kipindi cha pili kiliendelea kuwa cha mashambulizi makali, lakini hadi filimbi ya mwisho, matokeo yalibaki kuwa 2-1.
Coastal Union: Godson Mmasa, Said Nassor, Paul John, Konji Mayega, Jamal Machelenga, Mohamed Danstan, Mohamed Issa, Daniel Lianga, Moses Lutandika na Ally Hassan.
Moro Union: Lucheke Mussa, Musiba Selemani, Jeofrey Isdori, Said Fundikira, Hassan Kibweni, Adam Simba, George Mkoba, Henry Ngonye, Benedict Ngassa, Erick Mawala, Bakar Mpakala.
Katika mechi ya pili, Villa Squad walifanikiwa kuvuna pointi zote tatu kwa kuwafunga Morani FC mabao 2-0.
Villa walipata bao la kwanza dakika ya 29, likiwekwa wavuni na Stahimili Kebe kwa mkwaju wa penalti ambalo lilidumu hadi mapumziko.
Dakika ya 52, Villa Squad walipata bao la pili likiwekwa wavuni na Yahya Daruweshi aliyeambaa na mpira kabla ya kupiga shuti na kutinga wavuni.
Ligi hiyo itaendelea tena kesho kwa mechi kati ya maafande wa Prisons ya Mbeya dhidi ya wenzao wa JKT Oljoro katika mechi ya kwanza kabla ya wavaa buti wengine Rhino Rangers ya Tabora kupigishana kwata na Polisi Moro.
 
Kagasheki ahimiza ushiriki kongamano la michezo


na Asha Bani, Bukoba


amka2.gif
MBUNGE wa Bukoba Mjini, Balozi Khamis Kagasheki, amewataka wadau mbalimbali wa michezo kujitokeza kwa wingi katika kongamano la michezo litakalofanyika katika ukumbi wa Linas mjini hapa Februari 6 mwaka huu. Akizungumza na vyombo vya habari mara baada ya kukabidhi mchango wake wa sh milioni moja kwa timu ya maveterani ambao ndio waandaji wa kongamano hilo, Balozi Kagasheki alisema ni vema wadau wakajitokeza kwa wingi ili kutoa maoni yao katika nyanja mbalimbali za michezo.
Alisema, Mkoa wa Kagera kwa sasa uko nyuma katika michezo kwa ujumla, ukilinganisha na hali ilivyokuwa zamani, hivyo aliwataka wadau kujitokeza ili waweze kuelezea kinachotakiwa kufanyika ili kuhakikisha sekta hiyo mkoani hapa inapanda chati kama zamani.
"Viwango vya michezo vimeshuka chini sana katika mkoa huu, hivyo kuna haja wananchi wapenda michezo wakakusanyika na kujadili nini kifanyike na kwa nini tumefikia hapa tulipo, hakuna riadha, mpira wa kikapu, michezo yote viwango vyake viko chini kabisa," alisema Balozi Kagasheki.
Naye Kocha wa timu hiyo, Benny Kampambe, alimshukuru Balozi Kagasheki ambaye pia ni mlezi wa timu hiyo kwa kuwasaidia na kumtaka kutokata tamaa kuendelea kufufua michezo mjini hapa kwa njia yoyote ile.
Alisema, wao kama maveterani wana malengo makubwa ya kuhakikisha kuwa soka inasonga mbele sambamba na michezo mingine na kwa kuanza wameweza pia kununua sehemu ya kiwanja kwa ajili ya kujenga miradi mbalimbali ikiwa kama ni kitega uchumi katika michezo yao.
Aliongeza kuwa, kwa sasa wana mafanikio makubwa kutokana na kuwa na ongezeko la wanachama 82, ambao wako katika michezo mbalimbali.
 
Simba Silaha wahimizwa mshikamano


na Chile Kasoga


amka2.gif
WANACHAMA wa tawi la Simba la Silaha lililopo Mtoni Manispaa ya Temeke wametakiwa kujenga ushirikiano na mshikamano kwa lengo la kuiletea ushindi klabu yao.
Mwenyekiti wa tawi hilo, Mathias Nyanda, alitoa wito huo juzi wakati wa mkutano wake na wanachama wa tawi hilo.
"Endapo wanachama wenyewe ndani ya tawi tutakuwa hatuna umoja na ushirikiano, hatutaweza kuwa na muda wa kuweza kujadili maendeleo ya klabu," alisema Nyanda.
Aliwataka wanachama hao, kujiepusha na migogoro na badala yake wapange mikakati ya kuweza kuisaidia klabu ya Simba ili iweze kutetea ubingwa wa Ligi Kuu.
Hata hivyo alibainisha kuwa, tawi hilo lina mpango wa kuongeza wanachama wapya watakaokuwa na kadi halali za uanachama mara baada ya kuwafanyia upya uhakiki.
Wanachama wa tawi hilo, walikutana mwishoni mwa wiki kujadili jinsi ya kuweza kupata jengo la kudumu la tawi lao, ambako kila mwanachama ameombwa kuchangia sh 7,000.
 
Mtambo wa Gongo amtwanga Mroso kwa pointi


Na Addolph Bruno

BONDIA Maneno Osward 'Mtambo wa Gongo' amefanikiwa kumchapa Robert Mroso 'Cobra' wa Arusha kwa pointi 98-97 katika pambano lao lisilo la ubingwa lililofanyika
juzi katika Ukumbi wa Amana Ilala, Dar es Salaam.

Pambano hilo ambalo lilikuwa la kg. 72 uzani wa kati (middle) raundi 10 lilikua na upinzani mkali ingawa, Osward anayemzidi Mroso kwa kg. mbili alimwotea katika raundi ya tatu na nne.

Katika pambano mabondia wote walianza kwa nguvu sawa katika raundi ya kwanza na ya pili, ambapo kwenye raundi ya tatu na ya nne, Mroso alionekana kuzidiwa na kumpa nafasi mpinzani wake kushinda.

Ushindi wa Oswald ulionekana dhahiri katika raundi ya tano baada ya kumrushia konde nzito Mroso, hadi kupasuka juu ya jicho na kusababisha kuvuja damu nyingi.

Licha ya kupasuka huko, Mroso aligeuka na kuonesha upinzani mkali katika raundi zilizosalia wakirushiana makonde mazito kwa zamu na kusababisha majaji wa mchezo huo, Ali Bakari 'Chapion', Nassoro Kondo, Omari Yazidu na Sakwe Mtulya kutoa ushindi kwa Osward mchezo ulipomalizika.
 
India bingwa wa kriketi wa Dunia,


*Yailaza Sri Lanka

MUMBAI, India

INDIA imetwaa Ubingwa wa Kriketi wa Dunia, baada ya kuifunga Sri Lanka kwa wiketi 277-4 kwa 274-6 katika mechi ya fainali iliyochezwa katika Uwanja wa
Wankhede juzi mjini Mumbai.

Ushindi huo wa kwanza tangu mwaka 1983 ulizua nderemo, vifijo na shangwe nchini India inayofahamika kuwa na uwendawazimu wa mchezo huo katika bara la Asia.

Mchezaji wa Sri Lanka, Mahela Jayawardene alicheza vizuri na kuisaidia timu yake kupata alama 103 katika mipigo 91 katika Overs za mwisho na kupata alama 274-6 mjini Mumbai.

India haikuwa na wachezaji wake nyota, Virender Sehwag na Sachin Tendulkar, lakini Gautam Gambhir na Mahendra Dhoni waliimarisha timu katika mitupo.

Gambhir alitolewa nje akiwa na 97, lakini nahodha Dhoni akiwa na 91 bila kutolewa aliisaidia timu kutofungwa na ikashinda huku ikiwa na akiba ya mipira 10 ya kurusha.

Nahodha huyo, hakuwa katika kiwango cha juu katika mashindano hayo lakini alicheza kwa kujitolea maisha katika fainali na kuisaidia timu kuibuka na ushindi na kufanya mashabiki kulipuka kwa furaha uwanjani na sehemu mbalimbalia, ambako walikuwa wakifuatilia kwenye runinga.

Ilikuwa ni mechi iliyokuwa na ushindani mkubwa, lakini ni India ilikuja kuibuka na ushindi.

Washindi wengine waliowahi kutwaa taji hilo na miaka yao ni kama ifuatavyo: 1975: West Indies, 1979: West Indies, 1983: India 1987: Australia, 1992: Pakistan 1996: Sri Lanka, 1999: Australia, 2003 na 2007.
 
Hodgson afurahia West Brom kuifunga Liverpool


LONDON, Uingereza

KOCHA Roy Hodgson amesisitiza kuwa amefurahi mno kwa kuiongoza timu ya West Brom na kuibuka na ushindi dhidi ya timu yake ya zamani ya Liverpool.Hodgson alitimuliwa
na Reds Januari mwaka huu, baada ya kuiongoza kwa miezi sita lakini alikuja kuchukuliwa Baggies wiki tano baadaye.

Vijana wa Kenny Dalglish, ndiyo walioanza kuongoza kufunga goli katika mechi hiyo iliyochezwa juzi kupitia kwa Martin Skrtel katika Uwanja wa Hawthorns lakini Chris Brunt, alikuja kufunga magoli mawili kwa penalti na kuipatia ushindi timu yake.

Hodgson alisema kuwa yeye alimalizana na waajiri wake wa zamani na kwamba amefurahia timu yake mpya kuibuka na ushindi.

Alisema: "Nimepata furaha ya ziada kwa kuifunga Liverpool. Niliongeza marafiki wengi sana nikiwa Liverpool.

"Nina muda mwingi sana kuwaheshimu wachezaji na timu ya makocha, wengi kati yao walifanya kazi na mimi na tulifanya kazi kwa uaminifu mkubwa.

Alisema anafurahi kuifunga Liverpool kwa kuwa si kitu ambacho kilizoeleka katika siku za nyuma.

Ushindi huo umeipaisha West Brom hadi katika naafasi ya 12 katika msimamo na Hodgson amefurahia uchezaji wa timu yake.Alisema: "Nimeridhishwa sana. Nimeridhishwa sana na uchezaji.

Alisema hata wapinzani wao walicheza soka nzuri sana, ukiondoa dakika 15 za kwanza.

"Tulianza kufungwa, ilikuwa ni kipindi kigumu katika mchezo. Lakini ilikuwa ni maendeleao makubwa kwa wachezaji kusahau kila kitu na kuendelea kucheza na kufunga magoli mawili.

"Magoli yote mawili ilikuwa ni matokeo ya presha kuwa iliwekwa kwenye goli la Liverpool na kusababisha makosa yaliyozaa penalti za magoli."
 
AC Milan yaichapa 3-0 Inter Milan


MILAN, Italia

TIMU ya AC Milan imejiweka katika nafasi nzuri ya kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu ya Italia, Serie A baada ya kuwatandika Inter Milan kwa mabao 3-0 na kuongeza
pengo la pointi tano dhidi ya mahasimu wao.

Katika mechi hiyo ya juzi, mchezaji Alexandre Pato ndiye aliifungia timu yake mabao mawili huku beki, Cristian Chivu akitolewa nje kwa kadi nyekundu baada ya kumwangusha Mbrazil huyo mapema kipindi cha pili.

Pato alipachika bao lake dakika za kwanza za mchezo huo kabla ya kupachika la pili, muda mfupi baada ya Inter Milan kubaki na wachezaji 10 uwanjani.

Bao la tatu na la ushindi lilifungwa na Antonio Cassano kwa mkwaju wa penalti, ikiwa imesalia dakika moja mpira umalizike.

"Tulibaki kuwa watulivu na kucheza soka," alisema Allegri. "Hatukuwaachia Inter wapate nafasi nyingi za kufunga na kwa upande wetu pia tulipata nafasi nyingi," aliongeza mchezaji huyo.

Timu zote mbili zimebakiza mechi saba na Inter Milan, huenda ikapitwa na Napoli kama itakuwa imeshinda mechi yake ya jana dhidi ya Lazio.

"Sidhani kama mchuano umemalizika, lakini pointi tano ni pointi tano ambazo ni nyingi," alisema kocha wa Inter Leonardo. "Kwa ujumla bao la mapema liliathiri mno mechi na liliwapa AC Milan kujiamini. Endapo tungeweza kusawazisha kabla ya kwenda mapumziko tungeweza kubadili mechi," aliongeza.
 
Simba kwa kheri Afrika Send to a friend Sunday, 03 April 2011 20:33

okwi-akimtoka.jpg
Mshambuliaji wa Simba, Emmanuel Okwi akijaribu kumtoka beki wa TP Mazembe, Stopila Sunzu wakati wa mechi ya Ligi ya Mabingwa Afrika kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.Picha na Jackson Odoyo.

Sosthenes Nyoni
NDOTO ya mabingwa wa Tanzania, Simba kusombe kwenye michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika imebaki hadithi baada kupokea kipigo cha mabao 3-2 kutoka kwa TP Mazembe jana kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

Mabingwa hao mara mbili wa Afrika, waliuanza mchezo huo kwa kasi na kufanikiwa kupata bao la kuongoza dakika ya 18, kupitia mshambuliaji wake Given Singuluma aliyeunganisha vizuri mpira wa kona uliopigwa na Patou Kabangu.

Shija Mkina aliyeingia kipindi cha pili kuchukua nafasi ya Juma Jabu aliyeumia alipatia Simba bao la kusawazisha dakika 58, kufutia mpira wake wa krosi kwenda moja kwa moja wavuni na kumwacha Kidiaba Robert asijue la kufanya.

Mshambuliaji Allan Kaluyituka alipatia Mazembe bao la pili dakika 63, baada ya kuwazidi ujanja mabeki wa Simba, kabla ya Mbwana Samatta kuisawazishia tena Simba dakika ya 65, akiunganisha kwa kichwa mpira wa kona wa Amri Maftah kufanya matokeo hayo kuwa 2-2.

Nyota wa Zambia, Singuluma alimaliza ubishi kwa kupachika bao la tatu dakika 73, baada ya kupokea pasi nzuri ya Kaluyituka na kupiga shuti lilomshinda Juma Kaseja na kujaa wavuni.

Simba watajilaumu wenye kwa kupoteza nafasi nyingi za kufunga katika kipindi cha kwanza baada ya washambuliaji wake Samatta, Emmanuel Okwi na Mussa Mgosi kupoteza nafasi nyingi za wazi.

Dakika ya 3, Mgosi alishindwa kumalizia kona ya Okwi baada ya mpira wake wa kichwa kupaa juu, lakini mashabiki wa Simba wataikumbuka nafasi nzuri aliyokosa Samatta baada ya kumtoka beki wa Mazembe, Stopila Sunzu na kubaki yeye na kipa, lakini shuti lake lilidakwa na Robert Kidiaba.

Katika mchezo huo Simba walitawala sana sehemu ya kiungo na kufanya mashambulizi mengi, huku wapinzani wao wakicheza kwa kujihami na kufanya mashambulizi ya kushitukiza na kupiga mashuti ya mbali.

Awali mashabiki wanaodaiwa kuwa wa TP Mazembe walipambana na Polisi wakati wakijaribu kuingia kwenye jukwaa ambalo hakustahili kukaa.
 
Status
Not open for further replies.

Similar Discussions

Back
Top Bottom