Uhuru yalazimisha sare kwa Mwananchi FC Send to a friend Sunday, 20 March 2011 20:44
Imani Makongoro
TIMU ya Mwananchi FC, imelazimishwa sare ya 1-1 na Uhuru Publication katika mchezo wa kwanza wa Kundi C la michuano ya Wiki ya NSSF, mchezo uliofanyika kwenye Viwanja vya Chuo Kikuu cha Ualimu, DUCE.
Mchezo huo ambao Mwananchi FC walicheza kwa nguvu lakini mshambuliaji wake, Abdallah Masoud alikosa mabao mengi ya wazi akiwemo nafasi muhimu dakika ya 85 akiwa na kipa Said ambua.
Mwananchi ambayo haikuwa na wachezaji wa akiba kutokana na baadhi kuwa majeruhi huku na wengine wakiwa katika majukumu, walikwenda mapumziko wakiwa mbele kwa bao 1-0.
Mwananchi FC ndiyo walizifumania nyavu za wapinzani wao katika dakika ya 39 baada ya mchezaji wake, Ibrahim Masoud aliyeingia badala ya William kupiga shuti la mbali na kipa wa Uhuru alichupa bila mafanikio.
Kipindi cha pili Mwananchi FC ilicheza kandanda safi huku mshambuliaji wake Abdallah Masoud kukosa magoli ya wazi mara nane mfululizo na Uhuru kuitumia nafasi hiyo kujipatia goli la kusawazisha dakika 18 kabla ya filimbi ya mwisho kupitia kwa Fred Mpokigwe.
Katika mchezo mwingine, Radio Kheri ilitoka suluhu na Habari Zanzibar, mchezo uliofanyika kwenye Viwanja vya TCC Chang'ombe.Kwa upande wa netiboli, Mwananchi Queens leo inashuka dimbani kucheza na New Habari ikiwa ni mchezo wa kwanza wa Kundi B la michuano hiyo.
Queens ambao ni washindi wa pili katika mashindano hayo mwaka jana imejigamba kushinda mchezo huo wa Kundi B..
Kocha wa timu hiyo, Noel Kiunsi alisema kuwa timu yake imejiandaa vya kutosha na iko kamili kwa ajili ya mechi hiyo na nyingine na kuongeza kuwa lengo si kuwa washindi pili kama mwaka jana bali ni kutwaa ubingwa.