Simba waifuata TP Mazembe kibabe Send to a friend Wednesday, 16 March 2011 21:10
Clara Alphonce
WACHEZAJI wa timu ya Simba wanaondoka kesho kwenda DR Congo huku wakiwa na matumaini makubwa ya kufanya vizuri katika pambano lao dhidi ya TP Mazembe huko.Mchezo huo ni wa kwanza wa raundi ya kwanza ya Ligi ya Mabingwa Afrika, mchezo utakaofanyika Stade Municipal de Lubumbashi ambao wakati mwingine huitwa Uwanja wa Kenya wenye uwezo wa kuchukua mashabiki 35,000.
Kuingia hatua hiyo, Simba iliitoa Elan de Mitsoudje ya Comoro kwa jumla ya mabao 4-2, katika mchezo wa kwanza, timu hizo zilitoka suluhu na Simba kumaliza kazi Dar es Salaam. TP Mazembe inaanza raundi ya kwanza kwa kuwa ni bingwa mtetezi.
Mabingwa hao wa Tanzania wanaondoka na kundi la wachezaji 20 tayari kwa mchezo wao wa Jumapili huku mshambuliaji wake, Mussa Hassan Mgosi na Juma Kaseja wakiwataka wachezaji wenzao kujituma zaidi katika mchezo huo.
Akizungumza na Mwananchi jana, Mgosi alisema kuwa mechi hiyo itakuwa ngumu kwa kuwa TP Mazembe wako vizuri kifedha, kimpira na wanacheza kwenye uwanja wa nyumbani na wamekwishachukua ubingwa wa Afrika mara mbili.
Hata hivyo, Mgosi alisema kuwa pamoja na yote hayo wachezaji wenzake hawatakiwa kuhofia na wanachotakiwa ni kuhakikisha wanajituma na kujitolea katika mechi hiyo.
''Yaani naomba Mungu aendelee kunijalia uzima mpaka siku hiyo kwani kwa sasa nimejiandaa vya kutosha na hakuma mechi niliyoipania kama hivyo hivyo nataka niwahakikishie Wanasimba kuwa bado nipo na nitapigana kuakikisha nawafunga au tunawafunga,'' alisema Mgosi.
Naye kipa wa timu hiyo, Juma Kaseja alisema kuwa wanachotakiwa ni kujituma kwani uwezo wa kuwafunga upo kama wakionyesha nia ya kufanya hivyo japo mchezo utakuwa mgumu kwa pande zote mbili.
Alisema wao hawakuanza tu na kuwa mabingwa wa Afrika walianzia chini hivyo hawatakiwi kukata tamaa bali kujituma na kujiamini na kuona wanacheza na timu ya kawaida.
Mshambuliaji wa timu hiyo, Emmanuel Okwi amewatoa hofu mashabiki wake katika mchezo wao dhidi ya TP Mazembe na kudai hakuna linaloshindikana endepo watacheza kwa kujiamini huku akiwataka wachezaji wenzake kuelekeza nguvu katika pambano hilo litakalofanyika mapema mwishioni mwa juma hili mjini Lubumbashi.
Okwi ambaye amejigamba kurudi katika kiwango chake baada ya kuwa majeruhi alisema ana imani kubwa na timu yake na kwamba iko imara na itawashangaza mashabiki wake kwa kufanye kweli katika mchezo wao utakaofanyika ugenini kabla ya marudiano hapa nyumbani.
Akizungumza na Mwananchi, shambuliaji huyo alisema wamejipanga vyema na watahakikisha wanaiwakilisha vema Tanzania katika mchezo huo.
"Ni mchezo mgumu hakuna asiyefahamu TP Mazembe na historia yake ya kufanya vizuri lakini ukweli ni kwamba kila kitu ni maandalizi na sisi kama wachezaji tunatambua tunapaswa kufanya nini," alisema Okwi.
Aidha Okwi aliwataka wachezaji wenzake kuendelea na ushirikiano waliuonyesha katika mechi zao za ligi hasa katika kipindi hiki ambacho wanakabiliana na jukumula kuwakilisha nchi kuahidi kuwapa Watanzania kile wanachosubiri.Katika msafara huo, Simba itawakosa Abdulhamid Humoud, Hilal Echessa, Joseph Owino na Uhuru Seleiman ambaye ni majeruhi wa muda mrefu.
Wengine ambao wataachwa ni wachezaji wawili waliowapandisha kutoka timu B Faraji Kabari ambaye yupo kambi ya timu ya Taifa ya vijana chini ya miaka 20 na Kelvin Charles.Wachezaji ambao wanatarajia kuondoka na timu hiyo ni Juma Kaseja, Ally Mustapha 'Barthez' ambao ni makipa wakati washambuliaji Mussa Hassan Mgosi, Mbwana Samatta, Emmanuel Okwi, Ahmed Shibori na Shija Mkina.
Viungo ni Amri Kihemba, Mohamed Banka, Rashid Gumbo, Patrick Ochan, Nico Nyagawa huku mabeki wakiwa Amir Maftah, Kelvin Yondan, Juma Nyosso, Jerry Santo, Juma Jabu, Meshack Abel, Haruna Shamte na Salum Kanoni.Hata hivyo Makamu Mwenyekiti wa klabu hiyo Godfrey Nyange 'Kaburu' alisema kuwa leo watatoa utaratibu wote wa safari yao ya kesho japo awali walisema kuwa timu hiyo inatarajia kuondoka kwa ndege maalumu.
Alisema kuwa maandalizi ya safari yamekamilika wanachosubiri sasa ni majina ya wachezaji watakaokuwa kwenye msafara huo wa kesho baada ya kumaliza mazoezi ya jana jioni.Timu hiyo ambayo ilikuwa mjini Arusha kwa kambi ya siku tano wanatua leo Dar es Salaam tayari kwa maandalizi ya safari hiyo.