Mbinu, mikakati kuamua ushindi Arsenal, Barca leo
Tuesday, 15 February 2011 19:47
LONDON, Uingereza
MBINU na mikakati sahihi ya makocha na wachezaji wao ndiyo itatoa mshindi katika mchezo wa leo wa Ligi ya Mabingwa Ulaya baina ya Arsenal na Barcelona kwenye Uwanja wa Emirates jijini London.
Ukiondoa matokeo ya mwaka jana ambayo Barcelona iliitoa Arsenal kwa jumla ya mabao 6-3 katika hatua ya robo fainali ya michuano hiyo na fainali ya ligi hiyo mwaka 2006, ambayo Barca iliifunga Arsenal pungufu kwa mabao 2-1 mjini Paris, Ufaransa na kutwaa ubingwa, mchezo wa leo utakuwa wenye ushindani.
Kwa upande wake, kocha Arsene Wenger amejipa matumaini kwamba vijana wake wanaweza kutengeneza nafasi za mabao, kisha kuifunga Barcelona, akiwataka kwa muda wote wasiwaachie wapinzani wao nafasi ya kuchezea mpira wapendavyo.
"Tukiwaweka katika shinikizo, Barca hawawezi kucheza, msimu uliopita walituonyesha. Tulipobaini mbinu yao, tukawadhibiti," alisema Wenger.
Lakini, kocha huyo alieleza kuwa vijana wake hawana budi kucheza mchezo wao wa kawaida, wakishambulia na kuitia msukosuko ngome ya Barca na mabao yatapatikana.
"Ninaamini, tukifanikiwa kuwaweka katika shinikizo, tutakuwa na nafasi ya kutengeneza nafasi za kufunga mabao," alieleza.
"Kimsingi, hiki ndicho nimewaagiza vijana wangu kabla ya mchezo. Ni mchezo ambao hawana budi kuuchukulia kwa umakini, nina matumaini tutafaulu.
"Swali gumu ni mchezo ujao kwenye Uwanja wa Nou Camp ambako hatuna budi kubadilika. Tutacheza zaidi kwa kushambulia."
Kiungo Abou Diaby, hata hivyo amewaonya wenzake kutomfikiria zaidi mshambuliaji Lionel Messi
"Kama tunataka ushindi, tusimwangalie Messi, bali tujihami kama timu moja, matokeo yatakuwa tofauti," alieleza Diaby.
Messi, ndiye aliyeiadhiri Arsenal kwa mabao manne kwenye mchezo wa marudiano wa mwaka jana wa robo fainali kwenye Uwanja wa Nou Camp.
Akizungumzia mchezo huo wa leo, Messi alieleza: Ninataka kuzidi kuwa bora mbele yao."
Messi, alieleza kuwa atachungwa na jeshi la viungo, Abou Diaby, Alex Song au hata kikosi kizima, lakini atawasumbua.
"Ninaamini mchezo wangu dhidi yao mwaka jana utawachochea kunikamia, lakini nitajitahidi kusaka mabao," alieleza Messi.
"Mchezo wa mwaka jana ulikuwa maalum kwangu. Maoni yaliyotolewa na wengi baada ya mchezo ule yanaoyesha kwamba nilifanya vizuri.
"Haitokei mara nyingi kufunga mabao manne katika mchezo mmoja, tena kufanya hivyo kwenye michuano kama ya Ligi ya Mabingwa Ulaya, hatua ya robo fainali dhidi ya timu imara, tena katika mchezo ambao kila upande ulitaka kusonga mbele baada ya mchezo mgumu wa kwanza, ni jambo la kushangaza kwangu.
"Ninapenda kuwaona Arsenal wakicheza, nawafuatilia kwenye televisheni kwani wanacheza kama sisi, ninaupenda mchezo wao , lakini naamini sisi (Barca), ni wazuri kwa mbinu za mchezo kuliko kila mmoja. Lakini, tutaonyesha hilo kwa matokeo mazuri."
Aliongeza. "Zipo timu ambazo ni ngumu kwetu kukabiliana nazo, lakini Arsenal na Manchester United zinataka kucheza na kutushinda kwa mchezo ambao unafanana na ule wa kwetu, ndiyo maana inakuwa vigumu kucheza nao.
"Hatuichukulii kirahisi Arsenal hata kwa dakika moja, kwani mwaka jana walituonyesha kwamba wanaweza kuwa hatari ukipoteza umakini wakati wowote unapocheza dhidi yao.
Vijana hao wa Pep Guardiola, wamekuwa wakipewa nafasi kubwa ya kushinda mchezo, wakiendeleza utawala wao wa soka wa Hispania kwingineko Ulaya.