Maamuzi yoyote magumu huwa yana gharama zake, lakini suala zuri kwenye maamuzi magumu ni kwamba ni maamuzi ambayo yanakupeleka kwenye heshima na mafanikio, sasa swali la kujiuliza kwa mtu yoyote yule anayetaka kuchukua maamuzi magumu ni kwamba, je uko tayari kuzikabili gharama zake ? na suala hili wakati mwingine linahitaji ujitoe kwelikweli na wakati mwingine linaweza hata kukukatisha tamaa kwa kufikiria kwamba labda uamuzi huo ulioufanya sio sahihi kutokana tu na gharama zitakazokuwa zinakukabili, lakini kitu kizuri ni kwamba wahenga walisema kwamba : ''Ukiona usiku unakolea ujue asubuhi inakaribia''. Sasa swali la kujiuliza ni kwamba : Je ni wazalendo wangapi wa nchi yetu ambao wako tayari kulivulimia giza hili totoro la usiku ili kuingojea asubuhi ? Wakati mheshimiwa rais wetu Jakaya Kikwete alipokuwa anatolewa maneno ya kejeli na dharau toka kwa viongozi wa Rwanda na vyombo vya habari vya nchi ya Rwanda (nukuu taarifa mbalimbali za vyombo vya habari) naamini kwamba watanzania wengi waliumia kusikia maneno haya ya kejeli na ya dharau hasa ukizingatia kwamba utamaduni wa mtanzania mara nyingi unamfanya kumheshimu mtu mwingine yoyote na hasa mtu huyo anapokuwa mgeni kutoka nchi nyingine. Ile ilikuwa ni dharau ambayo watanzania wengi hawakuitegemea na naamini kwamba mpaka leo hii wapo atu ambao hawaamini maneno yale yalisemwa. Ndio hawaamini, lakini ukweli utabaki kuwa ukweli, Rais wetu amekejeliwa na kudharauliwa na hii ni kejeli na dharau kwetu sisi wote watanzania. Kinachotuponza sisi ni utamaduni wetu wa kuheshimu utu na udugu kati ya watu, hili sasa naweza kutamka wazi kwamba ni KOSA, hili ni kosa na limetugharimu na litaendelea kutugharimu kama tusipoamua kuliacha na kuchukua maamuzi magumu. Tumeanza kuchukua maamuzi magumu lakini kama ilivyo maamuzi magumu yoyote yana gharama, itakapofikia kuanza kulipa gharama hizo inatubidi tuwe tayari kwani faida za maamuzi haya magumu ni kubwa kuliko gharama hizo ambazo tunatakiwa tuzilipe. Gharama hizi ni za muda tu na wala zisitukatishe tamaa. Gharama hizi zimewekwa na maadui zetu ili watukatishe tamaa, lakini hata wao wanajua kwamba baada ya muda fulani gharama hizi zitakuwa hazina maana tena, lakini kitu kitakachotusaidia kuzikabili gharama hizi ni UZALENDO, uzalendo wa wananchi katika kuzivumilia na kutafuta mbinu mbadala na uzalendo wa viongozi katika kuwawezesha wananchi kuzikabili gharama hizi huku suluhu ya kudumu ikitafutwa, narudia tena kusema kwamba KITU KITAKACHOTUSAIDIA KUZIKABILI GHARAMA HIZI NI UZALENDO, watanzania tunatakiwa tufahamu kuwa tunapita katika moja ya vipindi vigumu katika nchi yetu na kitakachoweza kutusaidia kupita katika kipindi hiki kigumu ni UZALENDO KWA NCHI YETU.
Kwahiyo sitegemei wakazi wa mkoa wa Kagera waanze kulialia kuhusu suala la mgawo wa umeme, waelewe kwamba ndio wanaanza hivyo kulipia gharama za maamuzi magumu kama itakavyokuwa kwa Watanzania wengine wote nchini.
Kwani mlifikiri kwamba Rais Paul Kagame aliposema kwamba muda sahihi ukifika atampiga Rais Jakaya Kikwete (''when the right time will come i will hit him'') mlifikiri kwamba atampiga kwa ngumi za mikono yake ?, je mlishawahi kuona maraisi wa nchi wakipigana ngumi hadharani ?
NAOMBA KUWASILISHA.