MEDUSA: Malkia wa Damu

SEHEMU YA 07.

Ilikuwa ni lazima Nasria atoke ndani ya chumba hicho na kurudi nyumbani kwake lakini hakujua ni kwa namna gani angeweza kuondoka bila kugundulika. Yule mwanamke jini lilipotea na kutimka zake, lilimwacha ndani ya chumba kile huku akiwa na mwili wa Kamulika tu.
Hakujua afanye nini na kutoka, kumfuata dada wa mapokezi na kumwambia yule mwanaume alikufa chumbani kwake angeaminika kwa kuwa kweli amekufa na mwili wake kuonekana kitandani ila suala la kumwambia ni jini ndilo lililomuua, hakia kingekuwa kichekesho na kila mtu angemuona alikuwa akijitetea.
Kurudi mapokezi na kumwambia mhudumu kwamba kulikuwa na maiti lingekuwa jambo gumu sana na kitu alichokifikiria ni kuondoka chumbani humo. Kitu cha kwanza kabisa alichokifanya ni kufuta alama zote za vidole kwa kutumia kitambaa kilichokuwa na unyevunyevu.
Alifanya hivyo kwa kuwa alipenda sana kusoma simulizi za kipelelezi, pale wauaji walipokuwa wakimmaliza mtu, kitu cha kwanza kilikuwa ni kufuta alama za vidole vyao ili kuwapa kazi polisi kuwatafuta, naye alifanya hivyo.
Alipomaliza, akahakikisha hajasahau kitu, akakishika kitasa na kuufungua mlango, halafu akafuta tena alama za vidole vyake na kuanza kutembea kuelekea mlango wa nyuma. Alitaka kutoroka kupitia huko. Kwenye loji nyingi huwa na mlango wa nyuma ambao huwa mahususi kwa wazinzi wote ambao hawakutaka kuonekana mlango wa mbele, hasa wale waliokuwa wakiingia na wake za watu ama walikuwa wakifahamika sana.
Alikwenda huko, akakutana na geti, huku akionekana kutokujiamini, akalifungua na kuondoka zake, sasa akawa anatembea kwa mwendo wa haraka kutafura bodaboda. Akiwa njiani ndipo akaanza kukumbuka kilichokuwa kimetokea chumbani mule, akaanza kulia, hakika aliumizwa na hakujua lile jini lilifanya nini mpaka kumuingia.
Aliliota usiku huo, likampa mhemko mkubwa wa kufanya mapenzi, akamtafuta Kamulika lakini kilichotokea, likajitoa mwilini mwake na kumuua. Machozi yalikuwa yakilowanisha macho yake, aliumizwa moyoni, hakuamini kama alisababisha kifo cha mwanaume huyo.
Huku akiwa anaendelea kuomboleza, sasa akaanza kuwa na hofu wa watu wengine kufahamu kilichotokea, ilikuwa ni lazima watu wagundue kama yeye ndiye aliyesababisha hilo kama tu Kamulika aliwapigia simu marafiki zake usiku ule na kuwaambia alikuwa akimfuata.
“Ningechukua na simu yake!” alijisemea.
Alifanya kosa kuiacha kwani namba yake ingeonekana humo, uchunguzi wa polisi ungefanyika hata kupitia kwa simu ya Kamulika, na endapo namba yake ingeonekana, tena akiwa amempigia simu basi lingekuwa tatizo.
Alichokijua polisi wangeanza na yule mhudumu, angeelezea kilichotokea na baada ya hapo, wangetaka kumfahamu mwanamke aliyekuwa humo. Ili kumfahamu ilikuwa ni lazima kuchukua simu yake na kuangalia namba iliyoingia muda huo, ilikuwa ni lazima kuiona namba yake, angepigiwa simu na kutakiwa kituo cha polisi, endapo angefika huko na kukutana na yule mhudumu, ilikuwa ni lazima kumkumbuka.
“Nifanye nini?” akajiuliza huku akiwa na hofu.
Kurudi kule loji lilikuwa jambo lisilowezekana hata kidogo, kurudi huko ilimaanisha alikuwa akiyarudia matatizo yake, alihisi inawezekana mhudumu ama watu waliochukua vyumba vya jirani tayari walijua kilichotokea, endapo angejifanya kurudi, angedakwa na kupelekwa polisi.
“Kurudi ni upumbavu!” alijisemea.
Moyo wake ukaingia kwenye mateso makubwa na hofu nzito, hakujua ni kipi hasa alitakiwa kufanya, alijiona kuanza kupitia kwenye matatizo makubwa mno, hakutaka kufungwa jela wala kupata tatizo lolote lile, alikuwa na pesa, biashara zake, alitaka kuona zikiendelea na kuwa tajiri mkubwa.
Mwanamke jini.
Huyo ndiye aliyempa maswali makubwa, hakuwahi kuwa na jini, alisoma madrasa tangu akiwa binti mdogo tu, alishiriki kwenye shughuli zote za Kiislamu zikiwemo Maulidi lakini kote huko hakuwahi kuona ama kuambiwa alikuwa na jini, hilo jini lilitoka wapi na nini kilitokea?
Hakumfikiria mume wake wala kumuwaza kwa lolote baya, alichokijua ni kwamba walimalizana na wakati ndiyo kwanza mwanaume huyo alikuwa ameanza. Alitembea mpaka alipofika katika Barabara ya Shekilango sehemu iitwayo Sinza Makaburuni na kuita bodaboda.
Akataka apelekwe Manzese Tip Top, hilo halikuwa tatizo, akachukuliwa na kupelekwa huko kulipokuwa na klabu ya usiku. Alifanya hivyo makusudi kwa kuwa hakutaka kugundulika kabisa, bodaboda ilichukua dakika kadhaa, ikafika, akamlipa dereva na kuondoka zake.
Akasimama kwa dakika kadhaa, kulikuwa na watu wengi kiasi waliokuwa wakiendelea na mambo yao, hakutaka kujishughulisha nao sana, kwa jinsi alivyokuwa, muonekano wake kila mmoja alihisi alikuwa mmoja wa wanawake waliokuwa wakijiuza.
Akaenda mbele mpaka alipoona bodaboda nyingine na kuichukua ambayo ilimpeleka Tandale. Kila kitu alichokuwa amekifanya kilitokana na simulizi mbalimbali za kipelelezi alizowahi kuzisoma.
Kama mtu amefanya kosa sehemu na aliona baada ya hapo angetafutwa, mara baada ya kuchukua usafiri ilikuwa ni lazima kubadilishabadilisha, hilo lingewafanya hata watu kumpa kuwa vigumu.
Kwa alichokifanya, hata kama asubuhi ingegundulika maiti halafu kuifuatilia, hata kama wangempata dereva ambaye alimpeleka Manzese, angesema yeye alimpeleka huko na kuondoka kumbe mwenzake alichukua bodaboda nyingine na kumpeleka Tandale, tena si bodaboda ya eneo aliloachwa.
Alipofikishwa Tandale, akateremka na kufungua geti na kuingia chumbani kwake, sehemu ya kwanza kwenda ilikuwa ni bafuni, akaoga na kwenda chumbani. Usingizi haukuja, alikuwa na hofu tele na alikuwa akifikiria kile kilichokuwa kimetokea.
Hakika kilimtisha, hakuamini kama kwenye maisha yake siku moja angemuona mtu akifa

Je, nini kitaendelea?

Sent from my SM-A107F using JamiiForums mobile app
Sehemu hii ni ijayo....sehemu iliyotakiwa kupostiwa ni hii hapa chini

Ukishaisoma hiyo ya chini ndio uje hiyo ya juu. Nimejichanganya kuposti.

Sent from my SM-A107F using JamiiForums mobile app
 
Sehemu ya 7 ilitakiwa kuwa ya 8 na hii ya 8 ilitakiwa kuwa ya saba. Hivyo anza na hii kwanza, ukimaliza nenda kaisome hiyo ya juu.

SEHEMU YA 08

Kilikuwa ni chumba kikubwa kilichotapakaa damu mbichi sakafuni iliyoonyesha kulikuwa na kiumbe hai kilichochinjwa ama kujeruhiwa kwa kukatwakatwa. Katikati ya chumba kile kulikuwa na bakuli kubwa ambalo ndani yake mulikuwa na damu nyingine mbali na ile iliyokuwa imetapakaa sakafuni.
Pembeni kabisa ndani ya chumba kile alisimama msichana mmoja, alikuwa na nywele ndefu mpaka mabegani, alivalia kaniki nyeusi huku akionekana kuwa na hofu kuongea ama kuuinua uso wake.
Alikuwa akitetemeka pale alipokuwa amekaa, mwili wake ulitapakaa damu kana kwamba yeye ndiye ambaye alijeruhiwa na kumwaga damu ile kiasi cha kusema ilikuwa ni rahisi kukadiria ilikuwa zaidi ya lita tatu.
Pumzi ndefu na nzito zilikuwa zikisikika kutoka kwa msichana huyo aliyekuwa amesimama pembezoni kabisa ya chumba kile. Alitamani kuzungumza kitu lakini alishindwa kabisa, alionekana kuogopa kitu fulani hivi mahali pale alipokuwa.
Huku akiwa amesimama mahali hapo, ghafla akasikia mlango ukifunguliwa, kwa hofu nzito akasogea pembeni zaidi ya chumba kile na kusimama, kutetemeka kwa mwili wake kukaongezeka zaidi, alitamani kukimbia lakini akashindwa kufanya hivyo.
Mtu aliyeingia ndani ya chumba hicho alikuwa mwanamke mmoja wa makamo, kichwani alikuwa na nywele timutimu na kwa jinsi alivyoonekana, hata naye mwili wake ulitapakaa damu, yaani ni kama kulikuwa na mtu aliyekwenda na kidumu kilichokuwa na damu na kummwagia.
Akaenda mpaka kulipokuwa na bakuli lile lililokuwa na damu na kulichukua kisha kuinywa ile, alipomaliza tu, akayainua macho yake na kumwangalia msichana huyo aliyesimama pembeni ya chumba kile, akaanza kutoa kicheko cha sauti kubwa, kicheko kilichoonyesha dhihaka kubwa aliyokuwanayo dhidi ya msichana huyo.
Akaanza kuongea maneno fulani ambayo ilikuwa ni vigumu sana kumuelewa lakini lafudhi yake ilikuwa ni ya Kiarabu, aliongea kwa dakika moja tu, ghafla, umbo lake likaanza kupungua na hatimaye kubaki mdogo hewani, yaani hakukanyaga chini wala kugusa juu, akiwa hivyohivyo, kama mshale uliochomoka, akatoka hapo na kwenda kumuingia msichana huyo.
Ghafla Nasria alikurupuka kutoka kitandani, alikuwa amepiga kelele lakini kutokana na kuwa peke yake ndani ya nyumba alichokuwa, ilikuwa ni vigumu kwa watu wengine kumsikia, madirisha na milango ya vioo yalizuia sauti yake kutoka ndani ya nyumba ile.
Alikuwa akihema kama mtu aliyekimbia mbio fupi kwa kasi kubwa, jasho lililokuwa likimtoka ingawa feni liliendelea kupuliza kama kawaida. Akaanza kuangalia huku na kule, chumba kilikuwa na mwanga hafifu uliotoka kwenye taa ya uyoga iliyokuwa pembeni ya kitanda.
Haraka sana akaichukua simu yake na kuangalia saa. Ilikuwa ni saa nane ya usiku. Huku akionekana kama mtu aliyekuwa na haraka fulani hivi, akaanza kuangalia sehemu yenye majina ya watu aliowasevu kwenye namba yake, alipoliona jina la Kamulika, haraka sana akampigia, simu ikaanza kuita.
“Halo!” ilisikika sauti ya Kamulika ikiita.
“Kamuleka!”
“Ni Kamulika!”
“Nasria hapa! Upo wapi?”
“Nyumbani! Mbona usiku sana?”
“Tunaweza kuonana Sinza Lion?”
“Sinza Lion?”
“Ndiyo!”
“Usiku wote huu?”
“Unaogopa? Basi acha nimtafute mtu mwingine!” alisema na kukata simu.
Alifanya hivyo makusudi kabisa, hakuwa na mtu mwingine wa kumpigia simu zaidi ya huyo, alijua alipendwa mno na mwanaume huyo hivyo ilikuwa ni lazima kumpigia tu.
Mwili wake ulikuwa kwenye hali ya tofauti kabisa, alisikia muwasho fulani chini ya kitovu, yaani katikati ya mapaja yake na alichokuwa akihitaji ni kufanya mapenzi na mwanaume yeyote yule na mtu rahisi ambaye aliamini angemsaidia kwenye hilo alikuwa huyo Kamulika.
Alitamani kuonana naye sehemu na kuuridhisha mwili wake, kipindi hicho hakuwa na akili zake, alipelekezwa na tamaa ya mwili wake. Alisikilizia simu ya Kamulika, baada ya sekunde kumi, ikaanza kuita.
“Mbona umenikatia simu jamani? Yaani kuuliza imekuwa kosa. Aya niambie upo wapi mama,” alisema Kamulika kwa sauti ya unyonge kabisa iliyoonyesha alikuwa tayari kwa kila kitu.
“Sinza Lion, hapa kuna loji inaitwa Komamanga, inatazamana na hoteli ya Mambosasa. Njoo hapo haraka sana. Ukifika niambie,” alisema na kukata simu, hakutaka kuendelea kuongea.
Haraka sana baada ya kumaliza, akainuka, akavaa sketi yake laini kabisa iliyoonyesha mpaka maungo yake na kwa juu alivalia blauzi ambayo ilikuwa nyepesi kutoka mwilini, baada ya kumaliza, hakutaka kubaki ndani, alijipulizia manukato na kutoka chumbani humo.
Kadiri muda ulivyokuwa ukizidi kwenda mbele ndivyo ambavyo hamu yake ya kufanya mapenzi na mwanaume ilivyozidi kumshika, haraka sana alipotoka ndani, kama bahati kwake akaiona bodaboda ikipita, akaisimamisha na kumwambia dereva alitaka kupelekwa Sinza Lion.
“Buku tatu!”
“Wewe twende!” alisema, akapanda na kuondoka zake.
Njiani alikuwa na mawazo tele kuhusu ndoto ile, hakujua ilikuwa ikimaanisha nini na mwanamke yule aliyeingia ndani ya chumba kile alikuwa nani. Alijua dhahiri kwamba yule mwanamke aliyekuwa amesimama pembeni ya chumba kile alikuwa yeye, ila huyo mwingine hakuwa akimfahamu kabisa.
Ukiachana na hilo pia akaanza kujiuliza kuhusu damu zile, zilikuwa za nani na ilikuwaje mpaka ziwe ndani ya chumba kile. Moyo wake uliogopa mno, hakuamini kama yeye ndiye aliyekuwa ameota ndoto ile mbaya na kuogopesha mno.
Mbali na hayo yote jambo ambalo lilimfanya kuwa kwenye mshangao mkubwa ni kwa namna alivyokuwa na muhemko wa kufanya mapenzi. Hakuwahi kuwa kwenye hali hiyo kwa kiasi kikubwa kama ilivyokuwa siku hiyo, ilikuwa ni tofauti kabisa kiasi cha kushangaa.
Alisikia hamu kubwa, mwili wake ulikuwa mpaka ukitetemeka na mwanaume aliyemfikiria kwa haraka sana alikuwa Kamulika na ndiyo maana aliamua kumpigia simu na kumwambia akaonane naye huko Loji, Sinza.
“Dada tumefika,” alisema dereva bodaboda, walikuwa wamesimama barabarani, akashtuka na kuangalia eneo hilo.
“Kata kulia tuingie kwa ndanindani,” alimwambia na dereva kufanya hivyo.
Sasa macho yake yakawa makini kuangalia kila kona, walipofika mbele ambapo kulikuwa na baa ya Lion, akamtaka kukata kushoto na kuelekea sehemu iliyokuwa na hoteli ya Mambosasa ambapo kwa pembeni ndipo kulipokuwa na loji ya Komamanga.
“Nimefika,” alimwambia dereva, akateremka na kumlipa pesa, akaingia zake ndani.
Ilikuwa ni lazima afike ndani ya loji hiyo kabla ya Kamulika, alitaka kuyazoea mazingira ya chumba hicho kwanza. Akaenda mpaka mapokezi na macho yake kutua kwa mhudumu aliyekuwa hapo, alikuwa dada fulani wa makamo, aliyekuwa na shepu yake na kwa nyuma alikuwa na kile kitu ambacho kingewafanya wanaume wote waseme ‘Mashallah’.
“Nahitaji chumba,” alimwambia dada yule.
“Haina shida. Bei zinatofautiana!”
“Kuna cha shilingi ngapi na ngapi?” aliuliza.
“Elfu thelathini, arobaini na hamsini,” alijibiwa.
“Naomba cha elfu hamsini!” alimwambia.
“Sawa.”
Hilo halikuwa tatizo, akapewa ufunguo wa chumba hicho na kuelekea ndani. Alipofika, kitu cha kwanza kilikuwa ni kwenda bafuni, alitakiwa kuuweka mwili wake safi kabla ya Kamulika kufika mahali hapo.
Akavua nguo zake zote na kujiangalia, alivutia mpaka mwenyewe kuanza kujitamani. Alikuwa tayari kwa kila kitu muda huo, na mtu aliyekuwa akimsubiri alikuwa Kamulika tu.
Baada ya kumaliza akatoka na kusikia simu yake ikianza kuita, alipokiangalia kioo, alikutana na jina la mwanaume huyo, akaachia tabasamu, akaipokea simu na kuipeleka sikioni.
“Nimefika!”
“Mwambie dada wa mapokezi unakuja kwa mwanamke aliyeingia sasa hivi chumba namba nane,” alimwambia.
“Sawa,” alisema Kamulika na kukata simu.
Baada ya kukata simu, akachukua taulo na kulivaa, ndani ya dakika kama mbili hivi akasikia mlango ukigongwa, alikuwa Kamulika ambaye alitangulizana na yule dada, alipohakikisha mgeni amefika, akarudi mapokezi na kuwaacha wawili hao.
Kamulika alimwangalia Nasria, mwanamke huyo alivutia, alijaribu kumfananisha na kila mwanamke mzuri ambaye aliwahi kukutana naye kwenye maisha yake lakini hakujua alitakiwa kumfananisha na nani.
Kama watu walisema mwanamuziki Beyonce alikuwa mrembo sana, basi Kamulika alihisi alikuwa mbele ya mwanamke aliyekuwa mrembo mno kuliko huyo, kila alipomwangalia, hakuisha hamu, alibaki akimtamani kupita kawaida.
“Utaanza kula ama kuoga?” aliuliza msichana huyo kauli iliyokuwa na utata mkubwa.
“Nadhani kula kabla ya kuoga ni vizuri zaidi,” alisema Kamulika huku akimwangalia Nasria.
Hakutaka kubaki kama sanamu tu, ilikuwa ni lazima kama mwanaume anayejiweza, rijali amsogelee msichana huyo na kuanza kufanya utundu wake.
Kichwa chake kilikuwa kinafikiria mambo mawili tu. Kwanza ni uzuri wa msichana huyo, yaani alikuwa akienda kufanya mapenzi na mwanamke mrembo, aliyevutia, aliyenukia kama alilala kwenye bustani ya maua mengi ya waridi.
Nasria hakuwa na kinyongo, yeye ndiye aliyempigia simu mwanamke huyo, alifika mahali hapo kwa ajili ya kuimaliza haja ya mwili wake. Wakaanza kushikana hapa na pale huku wote wakiwa kama walivyotoka matumboni mwa mama zao.
Huku kila kitu kikiwa tayari, ghafla Nasria akahisi kama kitu kimemkaba kooni, alishtuka, haikuwa kawaida kuwa kwenye hali hiyo, akashika koo lake, mara yule mwanamke aliyemuona kwenye ndoto akatoka mwilini mwake na kusimama pembeni ya kitanda kile.
Aliogopa, alishtuka kupita kawaida. Mwanamke yule alimwangalia Kamulika aliyekuwa amelala kitandani huku akisikilizia raha ya kushikwa na Nasria hapa na pale, aliyafumba macho yake na kuhisi alikuwa peponi, tayari ameletewa wanawake saba wa kuwa naye.
Mara baada ya mwanamke yule ambaye kwa kifupi angeitwa jini kumwangalia Kamulika, kijana huyo akaanza kujishika kooni na kuanza kuhangaika kitandani pale. Nasria aliogopa, akaelekea pembeni na kuangalia.
Alikuwa akipiga kelele, alijiona kabisa akipiga kelele lakini sauti yake haikuwa ikitoka kabisa, ni kama alikuwa akimnong’oneza mtu.
Alishangaa! Akaona haiwezekani, akaanza kuufuata mlango kwa lengo la kuufungua na kutoka ndani ya chumba kile ili kwenda kuomba msaada, ilishindikana kabisa kuufikia mlango, yaani aliuona haukuwa mbali na mahali aliposimama lakini kila alipousogelea, nao ulisogea, sasa akaanza kuukimbiza lakini hakuwa akiufikia.
Wakati hayo yote yakiendelea, bado Kamulika alikuwa kitandani pale akiyaokoa maisha yake. Macho yake yakaanza kuwa mekundu, mapovu yakaanza kumtoka mdomoni na mwili wake kuanza kukakamaa huku akitetemeka kama mtu aliyekuwa amepatwa na kifafa.
“Aauughh...” ni sauti ambayo aliweza kuitoa, baada ya auti hiyo, akanyamaza na kutulia, sasa mwili wake ukawa umekakamaa na kuwa mgumu kama jiwe la kuchoma.
“Mungu wangu!” alisema Nasria, huku akiwa hajui afanye nini! Ghafla jini lile likapotea chumbani mule na kumuachia msala.
Hakujua ni kwa namna gani angejichomoa ndani ya chumba kile, hakuamini kama angeaminika endapo angezungumza kile kilichotokea, kila mtu angemuona muongo na kumchukulia yeye ndiye aliyemuua mwanaume yule.

Je, nini kitaendelea?

Sent from my SM-A107F using JamiiForums mobile app
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom