Mathanzua
JF-Expert Member
- Jan 4, 2017
- 15,848
- 20,697
Picha ya Rais Donald Trump na wahasimu wake.
Rais Donald Trump wa Marekani anakabiliwa na tishio la kuwa rais wa 3 wa Marekani kushitakiwa, pale ambapo baraza la wawakilishi la Marekani litapiga kura ya kihistoria ambayo itafungua milango ya mashitaka dhidi yake.
Wabunge wa Democratic wanatarajiwa kuidhinisha mashitaka mawili dhidi ya rais wa Republican siku ya Jumatano.
Bwana Trump anajandaa kufika mbele ya Seneti mwezi ujao, lakini bunge hilo linadhibitiwa na wanachama wengi wa chama chake na huenda lisipige kura ya kumuondoa madarakani.
Rais ametaja mchakato huo kuwa "jaribio la mapinduzi" na "hujuma.
Katika barua ya kurasa sita aliyoandika mkesha wa kura hiyo, Bwana Trumpa anadai kuwa alinyimwa haki "kuanzia mwanzo wa sakata la kutaka kumuondoa madarakani".
Aliwazuia washirika wake kufika mbele ya kamati ya bunge kutoa ushahidi na pia kupuuzia mbali ombi la kumtaka afike yeye mwenyewe mbele ya kamati hiyo siku ya Jumanne. Spika wa hilo Bunge Nancy Pelosi, alitangaza kwamba,baraza la wawakilishi litapiga kura leo kuamua kuhusu mashitaka yote mawili.
Picha ya Nancy Pelosi
Baraza la Wawakilishi litatumia moja ya mamlaka muhimu sana, ambayo limepewa kikatiba wakati wabunge watakapopiga kura dhidi ya rais wa Marekani.
Bi Pelosi aliwasilisha ujumbe kwa wenzake wa chama cha Democratic, akisema kuwa Baraza la wawakilishi litatumia moja ya mamlaka muhimu sana, ambayo limepewa kikatiba wakati wabunge watakapopiga kura kuidhinisha vifungu viwili vya mashtaka dhidi ya rais wa Marekani.
Spika huyo pia aliongeza kuwa katika kipindi hicho muhumi katika historia ya taifa hilo, lazima wabunge wailinde katiba ya nchi,dhidi ya maadui wote wa nchi na ndani ya Marekani.
Wabunge watakutana asubuhi 09:00 majira ya huko (14:00 GMT) siku ya Jumatano. Kura hiyo inatarajiwa kupigwa kati ya 18:30 na 19:30.
Bunge linapojiandaa kwa kura hiyo muhimu, Rais Trump atazuru eneo la Michigan kwa hafla ya "Krismasi" pamoja na makamu wake Mike Pence.
Rais Trump akiwa katika picha ya pamoja na Rais wa Ukraine na mchekeshaji Volodymyr Zelensky.
Trump anashutumiwa kuacha kutoa usaidizi wa kijeshi kwa Ukraine ili kuilazimisha nchi hiyo imchunguze hasimu wake kisiasa
Mashitaka ni yapi ?
Baada mjadala wa saa kadhaa wiki iliopita, kamati ya masuala ya haki inayoongozwa na Democrats iliidhinisha mashitaka mawili dhidi ya Rais Trump.
Trump anakabiliwa na tuhuma za matumizi mabaya ya madaraka kwa kuiagiza Ukraine kumchunguza makamu wa rais wa zamani wa Marekani Joe Biden, ambaye yuko katika kinyang'anyiro cha kuwania urais kwa tikiti ya chama cha Democratic.
Hatua hiyo ikitajwa kuwa kama njama ya kumpinga asiweze kuwania urais katika uchaguzi wa 2020 wa Marekani.
Trump pia anakabiliwa na shitaka la kufanya njama za kuvuruga uchunguzi wa bunge dhidi yake katika tuhuma hiyo kwa kuwazuia maafisa kutoa ushahidi wao pamoja na kuficha baadhi ya nyaraka.
Vifungu viwili vya mashitaka vinatarajiwa kupitishwa na baraza la wawakilishi ambalo linadhibitiwa na chama cha Democratic.
Kama mchakato utakwenda kama inavyotarajiwa kesi yake itafunguliwa Januari mwakani.
Picha ya Rais Donald Trump.
Je, inawezekana kumvua madaraka Rais wa Marekani?
Ikiwa kura ya bunge kama inavyotarajiwa Jumatano sambamba na mirengo ya kisiasa,Bwana Trump atakua Rais wa tatu katika historia ya Marekani kuchunguzwa.
Baadae atashtakiwa katika Seneti, ambako maseneta kutoka vyama vyote wanapaswa kutekeleza wajibu wao wa kutoa hukumu kwa uhuru.
Bunge la Seneti linadhibitiwa na chama cha rais cha Republican. Kiongozi wa Seneti Mrepublican Mitch McConnell aliwaudhi Democrats wiki iliyopita aliposema Maseneta wa Republican watashughulikia uchunguzi wa Trump kwa "utaratibu kamili" na na kupiga kura kupinga mchakato.
Chuck Schumer, kiongozi wa walio wachache katika bunge la Seneti alisema :"Kama vipengele vya uchunguzi vitatumwa katika Senati, kila Seneta atakula kiapo cha kutoa 'haki bila upendeleo '.
Kuhakikisha Seneti inaendesha kesi ya haki na ya kweli inayoruhusu ukweli wote unajitokeza ni jambo muhimu."
Mapema Jumanne, wakili binafsi wa Bwana Trump Rudy Giuliani alionekana kuthibitisha kwamba alifanya juhudi za kumuondoa balozi wa Marekani nchini Ukraine, Marie Yovanovitch, ili kutoa fursa kwa ajili ya uchunguzi.Hilo linaweza kuwa jambo la maana kisiasa kwa Bwana Trump.
Bwana Giuliani aliliambia gazeti la New York Times kuwa alimfikishia Bwana Trump "mara kadhaa" taarifa juu ya namna Bi Yovanovitch anaweza kuwa alihusika kwa njia fulani katika uchunguzi.
"Nilihitaji Yovanovitch atoke," Bwana Giuliani aliliambia gazeti hilo la New York.
Marais wawili wa Marekani wamepigiwa kura ya kutokuwa na imani ni Andrew Johnson mwaka 1868 na Bill Clinton mwaka 1998 lakini katika matukio yote mawili bunge la Seneti halikupiga kuwalazimisha kung'atuka madarakani.
Richard Nixon alijiuzulu Agosti mwaka 1974 wakati ilipojitokeza wazi kwamba anapigiwa kura yakutokwa na imani naye na kung'atuliwa madarakani na Congress baada ya kutokea kwa kashfa ya Watergate.
Makundi ya waandamanji wanaotaka Trump apigiwe kura ya kutokuwa na imani naye, wameandamana katika miji mikuu kote nchini Marekani leo Jumanne.
Baadhi ya wananchi wa Marekani wakiandamana wakitaka Donald Trump aondolewe madakani.
Raia wa Marekani wamegawanyika kuhusu mchakato mzima wa uchunguzi wa kutaka kumuondoa madarakani Rais Trump.
Wengi wao walikuwa wameshika mabango yanayosema "Muondoeni Trump" na kuandika hashtagi #ImpeachTrumpNow.
Wachambuzi wanasema kwamba Marekani imegawanyika.
Tovuti ya kisiasa ya Marekani inaonesha kuwa kura za maoni 538 za kitaifa, zinaonesha kwamba asilimia 47 ya watu wanaunga mkono mchakato wa Trump kupigiwa kura ya kutokuwa na imani naye, huku asilimia 46.4 wakipinga mchakato huo.
Chanzo: BBC Swahili