Herbalist Dr MziziMkavu
Platinum Member
- Feb 3, 2009
- 43,074
- 34,844
Mbunge wa Kisesa (CCM), Luhaga Mpina
Mbunge wa Kisesa (CCM), Luhaga Mpina, amesema hataiunga mkono bajeti ya serikali ya 2013/2014 kwa sababu haina jipya ikiwamo kukosekana kwa vyanzo vipya vya mapato na nidhamu katika upangaji wa matumizi.
Mpina akizungumza na waandishi wa habari mjini Dodoma, alisema baada ya kuisoma kwa makini bajeti hiyo amebainikuwa ina mapungufu mengi ikiwamo kutotengewa fedha za kutosha kwa mpango wa maendeleo wa miaka mitano.
Pia sababu nyingine ilikuwa ni matumizi ya kawaida hususani matumizi mengineyo-OC kutengewa fedha lukuki.
Nimepitia kwa kina bajeti na kugundua kuwa bajeti hiyo haipishani sana na bajeti zilizowahi kuwasilishwa miaka ya nyuma kutokana na sababu mbalimbali sitaiunga mkono kama serikali haitachukua hatua ya kuirekebisha, alisema.
Alizitaja sababu za kutoiunga mkono bajeti hiyo kuwa ni matumizi mengineyo kuendelea kutengewa fedha nyingi badala ya matumizi mengineyo kupungua kama ambavyo serikali imekuwa ikiahidi mara kwa mara.
Alisema katika bajeti hii matumizi mengineyo yameongezeka toka Sh. trilioni 4.07 hadi Sh. trilioni 4.5 hii ni ongezeko la Sh. bilioni 430 sawa na ongezeko la 10.7%.
Hali hii haiwezi kuendelea kukubalika fedha za umma kuendelea kutumiwa na wajanja wachache katika posho, semina huku Watanzania wengi wakiendelea kuteseka katika lindi la umasikini, miradi ya maendeleo kukosa fedha za kutosha, alisema.
Kwa mujibu wa Mpina, katika mjadala wa bajeti unaoendelea baada ya serikali kubanwa na wabunge ikakubali kupunguza matumizi mengineyo kwa kiasi cha Sh. bilioni 283.5 na fedha hizo kupangiwa miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo Maji, Uchukuzi, Viwanda, Vijana.
Kuhusu misamaha ya kodi, Serikali imekuwa ikiahidi kuchukua hatua ya kupunguza misamaha ya kodi katika hotuba za bajeti za serikali za tangu 2008/2009. lakini hadi sasa hakuna kilichofanyika hadi kufikia ju Sh. trilioni 1.8 ikiwa ni 4.3% ya pato la taifa.
Kwa upande wa Deni la Taifa, limekua toka Sh. trilioni 20.27 (Machi 2012) hadi Sh. trilioni 23.67 (Machi 2013) ikiwa ni ongezeko Sh. trilioni 3.40 sawa na 17%.
Katika mwaka wa fedha 2012/2013 kiasi cha Sh. trilioni 2.7 kilitengwa kulipia deni la taifa wakati mwaka wa fedha ujao 2013/2014 kiasi cha Sh. trilioni 3.3 zimetengwa.
Swali la kujiuliza ni kwanini Deni la Taifa likue kwa kasi kiasi hicho wakati kila mwaka tunatenga fedha kulipa deni pamoja na riba zake? alihoji.
CHANZO: NIPASHE