Mbunge ataka juhudi za kuongeza maprofesa

Roving Journalist

JF Roving Journalist
Apr 18, 2017
2,812
11,988
Fuatilia yanayojiri kwenye Bunge la 12, Mkutano wa 12, Kikao cha 6, leo Septemba 5, 2023.


Mbunge wa Muleba Kusini (CCM), Dk Oscar Ishengoma amehoji idadi ya maprofesa wanaozalishwa nchini na wale wanaostaafu, huku Serikali ikisema hadi kufikia mwaka 2022, Tanzania ilikuwa na maprofesa 226.

Naibu Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia, Omary Kipanga, amesema:Profesa ni ngazi ya kitaaluma, ambayo mhadhiri au mtumishi wa taasisi za elimu ya juu huifikia baada ya matokeo ya kazi za kitaaluma ikiwemo kufanya machapisho na ufundishaji,” amesema na kuongeza;

“Hivyo kupanda cheo kwa mwanataaluma kunatokana na jitihada za mhusika katika ufundishaji, kufanya tafiti na kuchapisha maandiko yake katika majarida yanayokubalika kitaifa na kimataifa.”

Kipanga amesema kuongezeka kwa idadi yao kunategemea zaidi jitihadi za mtu binafsi katika utekelezaji wa majukumu yake na kukubalika kwa jitihada hizo kwa wanataaluma wenziwe kwa kuzingatia miongozo waliyojiwekea.

Amesema hadi kufikia mwaka 2022 tulikuwa na jumla ya maprofesa 226, kati yao 163 wakiwa ni maprofesa washiriki (Associate Professors) na 63 ni maprofesa kamili (Full Professors).

Amesema suala la kustaafu linahusu zaidi vyuo vikuu vya umma ambapo umri wa kustaafu ni miaka 65.

Amesema kwa takwimu za mwaka 2022 idadi ya maprofesa kamili waliostaafu ni wanne na wanaotarajia kustaafu kwa mwaka 2023 ni watano, mwaka 2024 ni wawili na mwaka 2025 ni sita.

Kipanga amesema maprofesa washiriki waliostaafu kwa mwaka 2022 ni mmoja na wanaotarajiwa kustaafu kwa mwaka 2023 ni 18, mwaka 2024 ni wanne na mwaka 2025 ni sita.

Katika swali la nyongeza Ishengoma ametaka umri wakustaafu kwa maprofesa kuongezeka kutoka miaka 65 hadi 70, huku pia akihoji kama kuna mpango wa kuongeza maslahi kwa maprofesa ili kuvutia vijana wengi kusoma kufikia ngazi hiyo ambako kwa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), wanahitajika 161 lakini wapo tisa tu.

Akijibu swali hilo nyongeza, Kipanga amesema kuwa suala la kuongeza umri limechukuliwa kwa ajili ya kufanyiwa kazi na suala la maslahi wamekuwa wakiendelea kuongeza.

Chanzo: Mwananchi
 
Back
Top Bottom