Hon. Rev. Luckson Ndaga Mwanjale
Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii niweze kuchangia katika sheria hii ya mimea au ya mbegu za mimea kama ambavyo imeletwa. Kidogo nilikuwa na wasiwasi na mambo haya ya mimea kwa sababu ninakotoka huko kumekuwa na shida wakati mwingine kwamba, mimea inawaletea shida kweli wakulima. Nimeona hiyo kwa sababu kuna nchi nyingi ambazo zimepata matatizo hayo hasa mbegu hizi mpya ambazo zinakuwa introduced kwa wakati huu.
Nafahamu kwamba kuna nchi nyingi ambazo hata wale watu ambao wanagundua nchi kama Marekani au Canada au South Africa ambako kumekuwa na mimea mingi ambayo inagunduliwa kila wakati, lakini wananchi wake wakati mwingine wamelalamika kwa sababu hii mimea au mbegu au vyakula ambavyo vinatokana na hiyo mimea vinaleta madhara kwa wananchi.
Mheshimiwa Spika, nakumbuka wakati mmoja huko Zambia walipeleka msaada wa mahindi na watu wa Zambia wakayakataa yale mahindi kwa sababu yametengenezwa kwa GMO (Genetic Modified Foods and Organism). Lakini nataka kusema hivyo kwa sababu nakumbuka hapo zamani, kwetu huko Mbeya tulikuwa na mbegu ambayo ukipanda mwaka kesho tena unaweza ukachambua mbegu hiyo ukapanda na ikaota, lakini kwa wakati huu mbegu ambazo ziko kwenye soko ukipanda mara moja mwaka kesho huwezi ukazipanda tena. Hiyo ndiyo inaleta wasiwasi kwa sababu wananchi wengi wakati mwingine wanashindwa kuzinunua mbegu kila mwaka. Miaka yote ya nyuma na tangu tunazaliwa mbegu zilikuwa zinachambuliwa hizo hizo.
Mheshimiwa Spika, sasa nilikuwa naomba kuuliza kwamba: Je, inakuwaje? Kwanini mbegu zile za zamani zisiboreshwe hizo hizo ambazo ziko kuliko tukang'ang'ania kupata mbegu kutoka nchi ambazo ni kama nilivyosema huko Canada, Marekani na South Africa wanachukua mbegu, lakini watu wale hawana furaha na kile chakula kwa sababu wanasema wakati mwingine kimesababisha hata watu kupata kansa?
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nilikuwa nataka kutoa angalizo kwamba hizi mbegu naomba zinapokuja isiwe kwamba watu wanafanya biashara hapa, tunachezewa tunafanyiwa biashara, watu wanataka ku-monopolize biashara yote hapa kwamba ni lazima uende ukanunue mbegu kwao wakati zamani tulikuwa tunajitafutia wenyewe. Unajua kwamba nikilima mwaka huu nitachambua, nitapata mbegu nzuri, nitapanda tena. Lakini sasa hivi kuna wafanyabiashara ambao kwa kweli wanatufanyia biashara mbaya sana. Unapanda mbegu mara moja na hurudii tena kuipanda, maana yake ni kwamba mwaka huo ule, iishe, umeshakwisha. Kwa kweli tutafika hapo?
Mheshimiwa Spika, nilikuwa naomba nitoe angalizo kwa Serikali kwamba, Taasisi hizi ambazo zinafanya mpango wa kugundua hizi mbegu zijaribu kuangalia mbegu hizi za asili ambazo tunazo, ambazo wakati mwingine unahitaji tu kuchambua na kuweza kuzipanda tena. Kwanini tuletewe mbegu ambazo mimi nafikiri kuna mchezo tunachezewa hapa?
Mheshimiwa Spika, kuna mchezo tunachezewa hapa na watu ambao wanafanya biashara ya mazao hayo duniani. Wanatuletea mbegu ambazo hutanunua mbegu mahali kwingine kokote kule. Nitoe mfano mmoja, ukilima na ukapanda viazi, pale kuna dawa ambayo inapigwa pale, kiazi kitaota lakini majani yale mengine hayaoti. Sasa unafikiri hapa kuna kitu gani kinafanyika?
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nilikuwa na wasiwasi kwamba haya mambo ya mbegu, mimea hii tukawa tunafanyiwa biashara bila sisi kujua kwamba hapa tunachezewa mchezo mbaya.
Kwa hiyo, natoa angalizo kwa Serikali iwe macho inapofanya ugunduzi wowote wa mimea hii, ihakikishe kwamba hiyo mimea kwa kweli itawasaidia wananchi na siyo inawadidimiza. Kwa sababu siyo wananchi wote kila mwaka watakuwa wana uwezo wa kununua mbegu hizo. Wananchi wengine wanashindwa, walizoea kuweka huko juu anaikausha kwa moshi huko lakini akipanda mwaka kesho mbegu iko safi.
Kwa hiyo, naomba kutoa angalizo hapo kwa ndugu zangu ambao wanafanya ugunduzi huu kwa sababu kama nilivyosema, hata nchi hizo ambazo kwa kweli wamefanya mambo hayo, bado hata wananchi hawakubaliani nayo kwa asilimia mia moja. Canada pale wanakataa, Marekani wanakataa na South Africa wamekataa, wanasema jamani mbegu hizi mnazotugundulia hizi mbona zinaleta shida! Ni kama zinaleta ugonjwa fulani. Kwa hiyo, sisi nchi ndogo ambazo ndiyo tunaendelea tunapokea tu, mradi tumeshapata msaada. Nilikuwa naomba kwamba tuangalie hilo.
Mheshimiwa Spika, halafu mimea ya sasa hivi hata mahindi ukilima unashangaa, mwaka mmoja tu mahindi yameshaoza. Zamani tulikuwa tunaweka mahindi yanakaa mwaka mzima. Sasa hivi miezi mitatu mahindi yameshaingiliwa na wadudu. Hizo mbegu zinatusaidia nini? Mbona zinaleta gharama kubwa?
Nilikuwa naomba kuweka angalizo kwa Serikali kwamba iwe macho inapoleta na ku-introduce mambo kama haya na mimea kama hii ijaribu kutafiti kwamba yale ya zamani yako wapi? Sasa hivi imekuwa ni mzigo mkubwa tu na kwa bahati mbaya sasa yanapoliwa unaweka dawa ndiyo unaweka sumu zaidi kwa wananchi kwa sababu sasa hivi watu wanapulizia sumu za kila ajabu, halafu elimu ya kutosha kuweza kuwaelimisha wananchi wajue namna gani ya kuhifadhi mazao yao haitolewi. Kila mwananchi anajinunulia tu sumu hii, anaweka kwenye mahindi, mahindi hayo, yanawekwa kwenye soko, yanapelekwa Dar es Salaam. Wewe unanunua kumbe unanunua sumu.
Nilikuwa naiomba Serikali iwe macho katika kuleta Muswada huu kwa sababu ni muhimu kabisa kujua sisi ni binadamu na sisi tulikuwa na mimea yetu. Hivyo ni vizuri pia iangaliwe hiyo mimea yetu ambayo tulikuwa nayo zamani. Hii ya ugunduzi tu na kusema itatusaidia kuleta chakula kingi, lakini wakati huo inaleta gharama kubwa ya kutunza. Haina maana yoyote! Unaona ni afadhali hata ungetumia mbegu ya zamani ya asili kuliko kutumia ya sasa hivi kwa sababu ya asili mimi naweza kuweka miaka hata miwili wala haiharibiki. Lakini leo hii, vijidudu vimejaa, hata sasa hivi mimi nina mahindi pale karibu gunia mia na kitu, lakini yote yanaharibika, inabidi uyatoe tena uanze kuweka dawa, hiyo ina faida gani?
Kwa hiyo, ndiyo maana nasema wazi kwamba natoa angalizo kwa Serikali tuwe macho kuhakikisha hii mimea ambayo inagunduliwa tuwe tumefanya utafiti wa kutosha kwamba inatusaidia nini? Ina faida gani kwa mwananchi? Inaleta madhara gani? Tusiangalie tu upande wa kupata fedha, upande wa biashara kwamba tutafanya biashara, lakini tuangalie na madhara yake pia.
Mheshimiwa Spika, hayo ndiyo nilitaka nichangie hoja hiyo na ninaomba nimalizie hapo. Ahsante sana.