Na kwa taarifa ya wasiojua, aliyewambia wanamtwara wagombe ni Mbatia. Mmwagieni tu matusi kwa kufuata upotoshaji wa gazeti la uhuru, lakini historia itasema ukweli.
Soma ushahidi huu, wa alichosema akiwa huko huko Mtwara, miezi takriban tisa kabla ya wanamtwara kuandamana
Msikubali gesi kupelekwa Dar, asema Mbatia
Thursday, March 8, 2012
MWENYEKITI wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia amewataka wananchi wa Mkoa wa Mtwara, wasiruhusu gesi inayozalishwa mkoani humo, kusafirishwa kwenda Dar es Salaam na maeneo mengine ya nchi kabla ya hawajanufaika nayo. Wito huo unakuja wakati Serikali imeshaamua kujenga bomba kwa ajili ya kusafirishia gesi kutoka Msimbati, nje kidogo ya mji wa Mtwara kwenda Dar es Salaam, ukiwa ni mkakati wa kupunguza tatizo la umeme linaloikabili taifa. Hata hivyo baadhi ya wanasiasa wa upinzani, wanaupinga mpango huo.Tayari viongozi wa CUF mkoani humu, wameshatangaza azma ya kupinga uamuzi huo kwa maandamano na kuhujumu mradi huo. Akihutubia mkutano wa hadhara uliofanyika jana katika Uwanja wa Soko Kuu la mjini Mtwara, Mbatia alisema watu wa Mtwara lazima watumie uwezo wao kupinga mpango huo wa Serikali vinginevyo, wataendelea kuwa maskini. "Lazima mseme hapana tena kwa hasira kubwa, msiruhusu gesi hii kwenda Dar es Salaam kabla ya kuwanuisha wenye rasilimali," alisema Mbatia huku akishangiliwa na umati wa watu. Akizungumzia hali ya maisha, mwenyekiti huyo alisema wakati taifa linajiandaa kufanya tathimini ya utekelezaji wa malengo nane ya maendeleo, Mkoa wa Mtwara umevuka kiwango cha umaskini na kufikia kiwango cha ufukara. "Wakati maeneo mengine wakisonga mbele kupunguza umaskini, Mtwara kiwango cha umaskini kimekithiri na kuvuka mipaka na sasa ni ufukara," alisema Mbatia huku akiungwa mkono na wananchi. Katika mkutano huo Mbatia alimpokea mwanachama mpya, Uledi Abdallah aliyekuwa mgombea ubunge wa Mtwara Mjini, kupitia CUF mwaka 2010 kabla ya kujiondoa uanachama wiki mbili zilizopita. Akizungumza katika mkutano huo Uledi ambaye muda wote alikuwa akishangiliwa alisema baada ya kupitia sera za vyama vyote vya siasa nchini amejiridhisha kuwa NCCR-Mageuzi ndicho chama chenye mwelekeo wa kuwakomboa watu wa Mtwara.
Chanzo - Mwananchi