...
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kimeamua kuwatosa mawaziri saba wanaotajwa kuwa ni mizigo kwa serikali inayoongozwa na chama hicho.
Hatua hiyo ya kuwatosa mawaziri hao waliohojiwa na Kamati Kuu (CC), iliyokutana juzi mkoani Dodoma, inalenga kukinusuru chama katika uchaguzi mkuu unaotarajia kufanyika mwaka 2015.
Kikao cha CC kilichoketi juzi, kimemtupia mzigo wa kuwangoa mawaziri Rais Kikwete ambaye ndiye aliyewateua.
Akizungumza na waandishi wa habari, jana jijini Dar es Salaam, Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, alisema CC imetoa mapendekezo kwa Rais Kikwete ambaye ndiye mwenye hatima ya mawaziri hao.
Alisema Rais Kikwete ni mamlaka ya uteuzi wa mawaziri na ndiye atakayeamua kuwaadabisha, kuwasukuma au kuwaondoa madarakani mawaziri mizigo.
Aliyewaweka ndiye atakayewaondoa, Kamati Kuu haijamwabia awaondoe, inachokifanya ni kushauri tu. Lakini madaraka yote anayo rais aliyewachagua, alisema Nape.