Manchester Utd na kilichotokeaa mwaka 1999

Vw Jr

JF-Expert Member
Apr 2, 2017
377
338
MANCHESTER UNITED NA KILICHOTOKEA MWAKA 1999.

Na Tom Thomas

Mwaka 1999 unabaki kuwa mwaka bora kwenye historia ya Manchester United. Mafanikio yaliyopatikana yanaufanya kuwa mwaka bora na wa kipekee sana. Ni mwaka ambao klabu ilifanikiwa kushinda mataji makubwa matatu. UEFA Champions League, Premier League na FA Cup. Hakuna klabu nyingine iliyowahi kufanya hivi.

Mafanikio haya yalimfanya Kocha wa Manchester United wakati huo, Alex Ferguson atunikiwe heshima maalumu na utawala wa Kifalme nchini Uingereza chini ya Malkia Elizabeth II. Heshima iliyomfanya atambulike kwa jina la Sir Alex Ferguson.

Mafanikio haya hayakupatikana kirahisi. Manchester United walipitia njia ngumu sana kuyapata. Haikuwa kazi rahisi kushinda kila ubingwa ilioupata. Hii ni sababu nyingine inayoufanya mwaka huu uonekane kuwa wa kipekee sana.

PREMIER LEAGUE.
Manchester United walianza harakati za kuutafuta ubingwa huu kwa kucheza mechi ya nyumbani dhidi ya Leicester City. Ikiwa haijashinda ubingwa wowote msimu uliokua umepita, walilazimisha sare ya magoli 2-2 ndani ya uwanja wao wa Old Trafford.

Mpaka dakika ya 78 Leicester City walikua mbele kwa magoli mawili. Magoli ya Emile Heskey na Tony Cotee. Magoli mawili ya Teddy Sheringham na lile la dakika ya 90 la Kiungo David Beckham yaliinusuru Manchester United isipoteze mchezo wake huu wa kwanza wa ligi.

Mechi ya pili ugenini dhidi ya West Ham mambo bado yalikua magumu. Mechi ilimalizika kwa sare ya 0-0. Manchester United walisubiri hadi mechi ya tatu dhidi ya ‘vibonde’ Charlton Athletic ili waweze kupata ushindi wao wa kwanza. Ushindi wa magoli 4-1. Magoli mawili ya Ole Gunnar Solskjaer na Dwight Yorke aliyefunga magoli mawili mawili pia.

Mechi ya tano ugenini dhidi ya Arsenal, walipokea kichapo cha kwanza. Arsenal wakiwa ndani ya uwanja wao Highbury walipata ushindi wa magoli 3-0. Hali ikawa mbaya sana kwa Manchester United ukizingatia mchezo uliokua unafuata ulikua dhidi ya wapinzani wao Liverpool.

Walifanikiwa kushinda mechi hiyo iliyofuata dhidi ya Liverpool. Kuanzia hapo wakaendeleza rekodi nzuri ya kufanya vizuri kwenye mechi zilizofuata. Walipoteza mechi mbili tu tangu siku hiyo, mechi dhidi ya Sheffield Wednesday na ile dhidi ya Middlesbroug.

Mzunguko wa pili, mechi nne kabla ya msimu kumalizika, Arsenal walikua wanaongoza Ligi. Manchester United wakiwa nafasi ya pili, Chelsea akishika nafasi ya tatu. Manchester United walicheza mechi ya ugenini dhidi ya Liverpool. Ilikua ni mechi muhimu itakayotoa mustakabli kuelekea ubingwa.

Dakika ya 60, Manchester United walikua wakiongoza kwa magoli 2-0. Liverpool walipambana sana ndani ya uwanja wao wa nyumbani. Mpaka dakika 90 zinamalizika, matokeo yakawa 2-2. Liverpool walisawazisha kwa magoli ya Jamie Redknapp la lile la dakika za mwisho la Kiungo Paul Ince.

Wakati huohuo, Arsenal wao walishinda mechi yao dhidi ya Tottenham Hotspur, Chelsea pia waliifunga Leeds United goli 1-0. Mbio za ubingwa zilikua kali sana. Arsenal akiendelea kuongoza ligi. Mechi tatu zikabaki.

Mechi iliyofuata ilikua dhidi ya ‘wagumu’ Middlesbrough. Kumbuka mechi ya kwanza, Manchester United walipoteza nyumbani Old Trafford. Mechi hii ilikua ndani ya uwanja wa Riverside Stadium. Mechi ngumu iliyomalizika kwa Man United kupata ushindi wa goli 1-0. Goli la Dwight Yorke.

Arsenal wao walipoteza mechi iliyofuata dhidi ya Leeds United, kitendo kilichoipa nafasi kubwa Manchester United kushinda ubingwa. Mechi iliyofuata, Manchester United walihitaji ushindi kutangaza ubingwa. Haikua hivyo. Mechi ilimalizika kwa sare. 0-0 dhidi ya Blackburn Rovers. Ikawa imeshindikana.

Ikabidi isubiriwe hadi wiki ya mwisho ili iamue ni nani atakua bingwa kati ya Arsenal na Manchester United. Mechi hizo za mwisho Manchester United walicheza dhidi ya Tottenham Hotspur, Arsenal dhidi ya Aston Villa.

Magoli ya Andy Cole na David Beckham yaliipa ubingwa Manchester United kwenye ushindi muhimu wa magoli 2-1 licha ya Arsenal kupata ushindi pia. Msimu ukamalizika Manchester United wakatwaa ubingwa kwa tofauti ya pointi moja dhidi ya Arsenal walioshika nafasi ya pili.

FA CUP.
Njia waliyopita Manchester United kwenye FA Cup ilikua ngumu vilevjle kama ile ya Premier League. Walicheza dhidi ya timu ‘ngumu’. Middlesbrough, Chelsea, Liverpool na Arsenal kwenye hatua za mtoano pamoja na Newcastle United kwenye fainali.

Walianza harakati za kuwania ubingwa huu kwa kucheza dhidi ya Middlesbrough. Kumbuka Middlesbrough walishinda mechi ya Old Trafford kwenye ligi. Mechi hii ilikua ndani ya Old Trafford tena. Sekunde chache baada ya kipindi cha pili kuanza Andy Townsend aliifungia Middlesbrough goli la kwanza, baadae Man United walirudi na kupata ushindi wa magoli 3-1.

Hatua iliyofuata ilikua dhidi ya Liverpool. Kwenye mechi hii, dakika ya tatu ya mchezo, Michael Owen aliipatia Liverpool goli la kuongoza. Mpaka dakika ya 87, Manchester United bado walikua nyuma kwa goli hilo moja huku wakiwa wamepoteza nafasi nyingi za kufunga.

Wakati mpira ukielekea kumalizika. Dwight Yorke akaipatia Man United goli la kwanza, dakika ya 88 kabla ya Ole Gunnar Solskjaer kufunga goli la pili dakika ya 90. Mechi ikamalizika. Manchester wakasonga mbele. Mechi iliyofuata ilikua dhidi ya Fulham. Ilimalizika kwa ushindi mwembamba wa goli 1-0.

Hatua ya sita. Manchester United walicheza dhidi ya Chelsea. Mechi ya kwanza nyumbani Old Trafford, mechi ngumu iliyowashuhudia Paul Scholes na Roberto Di Matteo wakitolewa nje kwa kadi nyekundu. Mechi ikaisha kwa sare. 0-0. Ikabidi ichezwe mechi nyingine Stamford Bridge. Mechi iliyomalizika kwa Man United kupata ushindi wa magoli 2-0. Magoli ya Dwight Yorke.

Hatua iliyofuata ilikua ni ya nusu fainali. Mechi dhidi ya Arsenal. Mechi ya kwanza, Old Trafford ilimalizika kwa sare, 0-0 baada ya dakika 90. Zikaongezwa dakika 30 pia matokeo yalikua vilevile. 0-0. Ikaamuliwa mechi nyingine ichezwe siku tatu baadae.

Mechi ya pili iliyochezwa April 14, 1999 inabaki kuwa mechi kali kuwahi kuzikutanisha Arsenal na Man United. Ni mechi iliyochezwa ndani ya uwanja wa Highbury. Alianza David Beckham kufunga goli la kwanza kabla ya Dennis Bergkamp kusawazisha.

Mshambuliaji wa Arsenal Nicolas Anelka alifunga goli lakini halikuruhusiwa kwani mwamuzi alisema Anelka alikua ‘offside’. Dakika ya 74, Kiungo wa Manchester United Roy Keane alitolewa uwanjani kwa kadi nyekundu na kuwafanya Man United wabaki 10 uwanjani kwenye mechi hii ngumu.

Dakika ya 90, beki Phil Neville alimchezea faulo kiungo wa Arsenal Ray Parlour ndani ya eneo la box. Mwamuzi akaamuru ni penati. Golikipa Peter Schmeichel akaicheza penati ya Dennis Bergkamp. Mechi ikamalizika kwa sare, 1-1.

Zikaongozwa dakika 30. Ndani ya dakika hizo Kiungo wa Manchester United, Ryan Giggs alifunga moja kati ya magoli yake bora kabisa kwenye maisha yake ya soka. Alifunga goli baada ya kukimbia na mpira kutoka nyuma akiwapiga chenga wachezaji wa Arsenal kisha kumfunga golikipa David Seaman. Mechi ikaisha kwa ushindi wa goli 2-1. Man United wakafuzu hatua ya fainali.

Mechi ya fainali dhidi Newcastle United ndani ya Wembley ilikua ni ya mwisho kabla ya uwanja huo kufungwa. Mechi ilimalizika kwa Man United kupata ushindi wa magoli 2-0. Magoli ya Teddy Sheringham na Paul Scholes. Manchester United wakashinda ubingwa wa pili.

UEFA CHAMPIONS LEAGUE.
Kwanza kabisa, Manchester United walijikuta kwenye wakati mgumu baada ya kupangwa kundi moja dhidi ya Bayern Munich na Barcelona. Klabu nyingine ilikua ni Brøndby kutoka Denmark. Lilikua ni ‘kundi la kifo’.

Manchester United walimaliza mechi za makundi wakiwa na pointi 11. Wakipata sare nne, mbili dhidi ya Bayern Munich, mbili dhidi ya Barcelona. Walipata pointi sita dhidi ya Brøndby. Bayern Munich waliongoza kundi, Man United wakashika nafasi ya pili. Nafasi iliyofanya wafuzu hatua ya robo fainali.

Ilikua ni dhidi ya Inter Milan. Mechi ya kwanza, Old Trafford iliisha kwa Man United kupata ushindi wa magoli 2-0. Mechi iliyofuata kule Milan ikamalizika kwa sare 1-1. Mechi ya nusu fainali ilikua dhidi ya Waitaliano pia, Juventus.

Mechi ya kwanza, Old Trafford, Kiungo na nahodha wa Juventus Antonio Conte aliianza kwa kufunga goli la kwanza. Mpaka dakika 90 zinamalizika, bado Juventus walikua mbele kwa goli 1-0. Kwenye dakika za nyogeza, Ryan Giggs akafunga goli la kusawazisha kutokana na pasi ya David Beckham.

Mechi ya pili kule Turin. Mpaka dakika ya 11, Juventus walikua mbele kwa magoli mawili ya Filippo Inzaghi. Manchester United walihitaji kufanya ‘come back’ na kupindua matokeo. Mwisho, mechi ikamalizika kwa ushindi wa magoli 3-2. Magoli ya Roy Keane, Dwight Yorke na lile la ushindi dakika za mwisho la Andy Cole. Wakaingia fainali.

Fainali. Mechi dhidi ya Bayern Munich ndani ya Camp Nou mjini Barcelona. Kumbuka Bayern Munich na Manchester United walikutana kwenye makundi, mechi zote mbili zilimalizika kwa sare. Mechi hii ya mwisho ilikua ni ya kuamua nani ashinde ubingwa wa Ulaya.

Manchester United iliwakosa viungo wake muhimu, Roy Keane na Paul Scholes. Hivyo ilibidi David Beckham acheze kama kiungo wa kati pamoja na Nicky Butt. Hii ilikua ni mechi ya mwisho ya golikipa Peter Schmeichel kama mchezaji wa Manchester United. Mechi iliamuliwa na ‘referee’ bora kabisa kuwahi kutokea duniani. Muitaliano Pierluigi Collina.

Dakika ya sita tu mchezo. Mario Basler akaipatia Bayern Munich goli la kwanza. Goli liliodumu hadi dakika ya 90. Zikaongezwa dakika tatu. Manchester United wakapata kona alipigwa na David Beckham dakika ya 91. Mpira wa kona uliokolewa vizuri, ukamkuta Ryan Giggs aliyepiga krosi kuelekea ndani ya box, mpira ukamkuta Teddy Sheringham aliyefunga goli la kusawazisha.

Dakika mbili baadae, Manchester United wakapata kona nyingine iliyopigwa na David Beckham tena, ni kona iliyozaa goli la pili na la ushindi lillofungwa na Ole Gunnar Solskjaer. Mechi ikamalizika kwa Manchester United kupata ushindi wa magoli 2-1. Ushindi ulioipa ubingwa wa pili wa UEFA Champions League.

Msimu ukamalizika. Manchester United wakatengenezea historia ya kuwa klabu ya kwanza kushinda mataji makubwa matatu ndani ya msimu mmoja nchini England. Hii ni rekodi ambayo inadumu hadi leo.

Sent using Jamii Forums mobile app
 
na mwaka huu yuko na timu ngumu ngumu kila mchuano labda tusubiri historia kujirudia

maana naona epl timu zina mbwela mbwela tu
 
Hii record ýa 1999 ndo ikanifanya niipende na kuwa shabiki wa Man U mpaka leo. Hii historia itajirudia tu siku za mbele

GGMU
 
Back
Top Bottom