Chilojnr
JF-Expert Member
- Jul 5, 2012
- 302
- 1,306
MANARA, KAMA HUUWEZI UTANI, USITANIE WENZAKO
Mpira ni mchezo mmoja mtamu sana, yaani sasa hivi unacheka lakini itakuchukua sekunde moja tu, unabadilika na kuwa mwenye huzuni tele.
Ipo hivyo, timu inapofanya vizuri, ni yetu sote lakini inapofanya vibaya mzigo wote anaangushiwa kocha. Si Bongo tu, hata Ulaya huwa ipo hivyo, siku zote shabiki anataka kucheka tu, matokeo ya kusuluhu ama kufungwa wala hayataki kabisa.
Ni siku chache zilizopita nilimsikia msemaji wa Klabu Kubwa, Simba SC, Haji Manara akilalamika kwa madai ya kudhihakiwa kutokana na uwalimu wake wa masomo ya Kiislamu, Madrasa huku akiwataka Wanasimba wote tumjie juu aliyekuwa msemaji wa Yanga, Jerry Muro kwamba kaukashifu Uislamu. Nilipomsikiliza tu, nikabaki nacheka sanaaaaa.
Wakati namsikiliza alivyokuwa akilalamika kwa kulialia, nikawa nayakumbuka maneno yake ya kipindi cha nyuma akiwataka Wanayanga wasilalamike wanavyodhihakiwa kwani wao ni watani wa Simba tu, hata iweje ni lazima watulie kama walivyo.
Wanayanga wakatulia japokuwa wengine waliendelea kuja juu, wiki kadhaa mbele, huyuhuyu Manara ambaye anawakumbusha Wanayanga kwamba Simba ni watani wao wa jadi, leo analia kwa sababu tu kataniwa kwa kiasi kikubwa, utani mmoja tu ukamfanya kulalamika mbele ya waandishi wa habari.
Nimkumbushe tu Manara kwamba mkiwa watani wa jadi huwa haiangalii upo kwenye tukio gani, unafanya nini, mtu akitaka kukutania, kama ni mtani wako wa jadi, tulia akutanie anavyoweza.
Ukienda kwenye makabila, unaweza kuona umefiwa, nyumba nzima mnalia kwa uchungu halafu mtani wako ambaye ni nyumba ya pili tu ameweka muziki, wanaselebuka na wanakuja mpaka msibani na kucheza kwa shangwe na kuwaambia acheni ujinga wa kulialia na nyie nyanyukeni mcheze nao.
Utani huu unakwenda mbali zaidi hata kipindi cha kwenda kuzika. Mtani wako analizuia jeneza na kudai apewe pombe ndipo ataruhusu mwili uende kuzikwa. Ni utani lakini anamaanisha, msipompa pombe, hamuendi kuzika kweli, mtatafuta pombe ilipo, mtampa, atawaacha mkazike maiti yenu.
Huo ni utani wa jadi ambao alikuwa anauzungumzia Manara kila siku na kuwakumbusha Wanayanga. Nilichokigundua Manara hajui nini maana ya utani wa jadi, ni mtu mwenye hasira, ni mtu ambaye hataki kuguswa.
Kuwa mwalimu wa madrasa si tusi, ni heshima kubwa sana, leo mtu akiwa imamu wa msikiti fulani na kusema ustadhi fulani alinifundisha madrasa, ni heshima kubwa kwake.
Jerry Muro aliingizia hilo kama sehemu ya utani lakini bado Manara anakasirika. Akitaniwa kwamba alisaidiwa pesa za matibabu, anakasirika...kiukweli kabisa Manara hajui utani anapenda kutania watu lakini yeye hapendi kutaniwa.
Uwezo wa Yanga umeshuka kwa sasa, hawana la kumtania Manara zaidi ya kukumbushia yaliyopita ambapo tayari yameonyesha ni kwa namna gani yanamchukiza sana.
Ukimsikiliza Jerry Muro, alijimwambafai kidogo akasema yeye ni mkuu wa wilaya na ana uwezo wa kumuweka Manara ndani kwa saa 48.
Huo ni utani tu kwa kuwa ikitokea amefanya hivyo bila Manara kufanya kosa kila mmoja atamshangaa, si sisi tu bali hata Rais John Pombe Magufuli atamshangaa, lakini utani huohuo alivyouzungumzia Manara utagundua ni kwa kiasi gani amekasirika...mishipa ya shingo ikamtoka...Manara umesahau kwamba aliyekwambia hivyo ni mtani wako? Tena yule unayemuita wa jadi? Hasira za nini mzee baba?
Unapopenda kutania watu, wanapokasirika kwa sababu ya utani wako basi na wewe siku ukitaniwa usije juu, unaita waandishi wa habari na kutokwa povu, kwa nini uambiwe urudi kufundisha Madrasa? Kwa nini ukumbushwe jinsi ulivyosaidiwa ulipokuwa unaumwa? Kwa nini uambiwe Yanga ilikulea kwa sababu mzee Sunday Manara alikuwa mchezaji wa Yanga, pesa alizokuwa akilipwa zilikusomesha na kutatua ya hapa na pale?
Huo wote ni utani Manara! Hata kama mtu kaongea kwa jazba, bado ni utani, mnataniana, usitokwe na mishipa ya shingo, uanze kuingiza udini kwenye utani ilimradi tu Waislamu wamchukie Jerry Muro, nadhani si sahihi.
Jerry Muro hakutukana Uislamu kama unavyotaka kutuaminisha, aliikumbusha tu kazi yako ya zamani na kukutaka urudi huko kuendelea nayo na uachane na soka, kama angesema kauli mbaya, ya uchochezi basi angechukuliwa hatua kwa kuleta udini.
Manara mshikaji wangu, Mwanasimba mwenzangu! Kama huwezi utani, basi usitanie watu! Wengine mnakuwa mashuhuri kutania watu ila mkitaniwa nyie tu, mnatoka povu.
Najaribu kujiuliza siku ambayo Manara anatokwa na povu, Jerry Muro angekuwa pembeni, halafu huyo Manara angekuwa na bastola kiunoni, unadhani nini kingetokea?
Kama huuwezi utani, acha kutania wenzako.
Nyemo Chilongani
Sent using Jamii Forums mobile app