Mahakama ya hakimu Mkazi Kisutu imeelekeza bondia maarufu nchini Hassan Mwakinyo kupelekewa wito wa kufika mahakamani kupitia gazeti la Mwananchi kufuatia kesi ya madai inayomkabili mahakamani hapo.
Uamuzi huo umetolewa leo na hakimu mkazi mkuu wa mahakama hiyo Amir Msumi baada ya Mwakinyo kukataa kupokea hati ya wito wa kufika mahakamani iliyowasilishwa kwake na msambaza nyaraka wa mahakama.
Mwakinyo alifunguliwa kesi ya madai na kampuni ya PAF Promotion, ambapo pamoja na mambo mengine iliwasilisha madai manane mahakamni hapo likiwemo la kuilipa kampuni hiyo TSH milioni 150 ikiwa ni madhara ya jumla baada ya bondia huyo kushindwa kupanda ulingoni tofauti na mkataba wake aliosaini.
Wakili anayeiwakilisha kampuni ya PAF promotion, Herry Kauki amedai kesi hiyo ilipangwa leo Novemba 13, 2023 kwa ajili ya kutajwa na kuangalia kama bondia huyo amepewa wito wa kufika mahakamani.
Wakili Kauki alisema wao walipeleka wito serikali ya mtaa, lakini Mwakinyo aligomea wito wa kufika Mahakamani.
Pia walimtuma msambaza nyaraka za mahakama maalumu kwa ajili ya kupeleka viapo lakini Mwakinyo pia aligomea kupokea wito huo, hivyo msambaza nyaraka wa mahakama hiyo alikula kiapo kuelezea haya maelezo kuwa amepeleka wito lakini Mwakinyo amekataa kusaini wala kupokea wito huo.
Kutokana na hali hiyo hakimu Msumi alitoa amri kwa upande wa mlalamikaji ambaye ni kampuni hiyo kutangaza wito wa mahakama kupitia gazeti la Mwananchi, ukimtaka Mwakinyo kufika mahakamani hapo Novemba 20, 2023 ili kusikiliza kesi yake.
Chanzo: Mwananchi