Huwezi kujenga umoja kama wasiojulikana wataendelea kuwepo na kupewa nguvu.
Huwezi kujenga umoja kama watu wataendelea kubambikiwa kesi za uhujumu uchumi na utakatishaji fedha.
Huwezi kujenga umoja kama watu wataendelea kutazamwa kikanda.
Huwezi kujenga umoja kama Polisi, mahakama na Bunge vitaendelea kutumika kama vyombo vya watu binafsi na CCM.
Huwezi kujenga umoja kama maDC na maRC wataendelea kuwaweka watu korokoroni kwa ubabe, uonevu na kukomoana.
Huwezi kujenga umoja kama utaendelea kuwaona wasio wanaCCM ni raia daraja la pili.
Huwezi kujenga umoja kama Polisi wataendelea kufanya kazi kama kikundi cha kigaidi. Kazi kubwa ya magaidi ni kujenga hofu. Leo polisi badala ya kuwakamata watuhumiwa, wanawateka watuhumiwa. Polisi wamebakia na kazi ya kuwaziba watu na kuwanyima watu haki zao za kikatiba.
Umoja wa kitaifa hauji kwa kauli bali kwa matendo. Mazuri mengi tuliyokuwa nayo zamani, yaliyokuwa yakilitambulisha Taifa letu yamevurugwa awamu hii. Kama hili limegundulika sasa, na kuna dhamira ya kuliondoa, ianze kufanyika kazi katika hayo niliyoyataja. Bila hivyo umoja wetu utaendelea kutetereka zaidi na zaidi, na uchaguzi wa mwakani utaongezea maradufu.