Ndugu zangu mtakumbuka kwamba wakati wa Kampeni, Rais John Pombe Magufuli, (JPM) alionekana kujitenga na chama chake cha CCM. ukiachia magwanda ya kijani aliyokuwa anayavaa (ambayo sijamuona kuyavaa tena toka ameapishwa), kauli zake, vibwagizo, vyote vililenga kujenga hoja kwamba siyo CCM inayoomba kura bali ni MAGUFULI. "SERIKALI YA MAGUFULI" , "CHAGUA MAGUFULI". Matarajio ya wengi, nadhani hata wanaccm, ni kwamba kwa kuwa CCM imechafuka mbele ya wananchi, ni sawa kuiweka pembeni kwanza, lakini mara ingetokea akawa mshindi, basi CCM ingechukua nafasi yake kama kawaida.
Baada ya kuapishwa, Magufuli hakuonesha jitihada ya pekee kujishughulisha na CCM, na katika hatua zake za mwanzo ambapo alifanya ziara kadhaa za ghafula, akatoa hotuba ya bunge ambapo alimshambulia waziwazi mtangulizi wake, rais mstaafu Jakaya Kikwete, ambaye alimbatiza jina la "mzee wa maisha bora" (kejeli?) tena kwa takwimu kuhusu safari zake za nje. hili lilikuwa jambo ambalo wapinzani na wanaharakati walilipigia kelele sana lakini CCM na serikali yake walitetea kwamba safari hizi zina tija. kurugenzi ya mawasiliano ikulu ilifanya kazi yake kutetea hili kwa nguvu zote. sasa leo Rais JPM analisema mbele ya vigogo wa ccm, na JK mwenyewe, tena kwa kusisitiza kwamba hataki kuwa mnafiki, ilikuwa ni ngumi nzito sana siyo kwa JK tu bali kwa CCM pia.
Tumeshuhudia hali ya ubaridi usio wa kawaida kwa upande wa CCM. tulizoea kuona kauli za kupongeza na maandamano ya kuunga mkono. safari hii kimya. lakini kilichonifanya kutoa mchango wangu kwenye hili jambo, ni ile hotuba ya Rais JPM kwa wafanyabiashara jana. wakati pekee ambapo aliitaja CCM, ilikuwa ni katika mabaya. ni pale alipokuwa anaeleza kuhusu ufisadi katika ubinafsishaji wa viwanda kule Morogoro, ambapo alisema kwamba viongozi wa CCM walihusika katika ubinafsishaji huu ambapo viwanda vimegeuzwa mahali pa kulala mbuzi. Hii hali ya kutoitaja kabisa CCM, au inapobidi aitaje, basi anaitaja katika mabaya, inanikumbusha mgomo wa wanahabari kwa aliyekuwa katibu mwenezi wa CCM wakati huo, na waziri wa mambo ya ndani, Ramadhani Mapuri (sijui yuko wapi siku hizi). wanahabari waliamua kususa kuandika habari yoyote kuhusu Mapuri, isipokuwa tu pale itakapokuwa ni habari mbaya! ilibidi msemaji wa CCM awe Mangula wakati huo kama sikosei, aliyekuwa katibu mkuu.
Katika hotuba yake kwa wafanyabiashara, kuna wakati amesisitiza kwamba serikali ipo, na kwamba serikali hii - (siyo ya CCM, bali ) ni ya JPM. hiyo ilikuwa ni ngumi nyingine kwa CCM. kwamba amekusudia kujitenga kabisa na CCM kadiri anavyoweza. na kusisitiza zaidi hilo, akasema pia kwamba hakuchukua fedha ya mfanyabiashara yoyote. sasa mimi sina hakika kama wale waliokuwa wanabandika matangazo walitumia fedha kutoka wapi. fulana na kofia zilitoka wapi. na je, kampeni yake aligharimia yeye mwenyewe? maana kama ni chama kiligharimia, kuna uhakika gani kwamba wafanyabiashara na wengine hawakupenyeza rupia zao? lakini la muhimu ni kwamba hata kama hayo yalifanyika, yeye hayatambui na hii siyo serikali ya CCM bali ni ya JPM. kwa maana hiyo, hata kama kuna vigogo katika CCM walipokea fedha kwa ajili ya kampeni, ili baadae wakikaa kugawana nyama ya mzoga, wapate mgao wao, basi imekula kwao. JPM hatambui hayo.
Ni kweli kwamba kwa kasi aliyonayo mpaka hivi sasa, Rais Magufuli anavifanya vyama vyote vya siasa kuonekana kama havina umuhimu, kikiwemo chama chake cha CCM. na kwa kutekeleza yale ambayo yalikuwa yanapigiwa kelele sana na vyama vya upinzani, anapunguza nguvu ya vyama hivyo, ambayo imekuwa ikikua kwa kasi miongoni mwa watanzania hasa kutokana na kiburi cha CCM.
sasa je, JPM anawezaje kujitenga kabisa na CCM? tuseme kikatiba na kisheria JPM ana wigo mpana kiasi gani kuiweka CCM pembeni? na CCM nayo je, itamwangalia tu bila kufanya mbinu za kumrejesha kundini? mahali ambapo CCM wanaweza kumkaba koo ni katika bunge. ambapo wabunge walio wengi wa CCM wanaweza kutaka "kumtia adabu". lakini hapo nadhani UKAWA wanaweza kugeuka na kumuunga mkono? lakini kwa uchaguzi tulioshuhudia, hivi kuna kundi linaweza kuthubutu kufanya kinyume na matarajio ya wananchi? naomba tujadili.