Any updates za hawa mabondia?au ndo kusema wameshahukumiwa kifungo huko?
Mabondia waliokamatwa na mihadarati nje...Polisi: Walitumwa na kigogo wa Dar
sogeza Habari Zinazoshabihiana
Maiti aokotwa akielea bonde la Msimbazi 08.04.2008 [Soma]
Siri za Uchaguzi Mkuu zaanza kufichuka 17.04.2006 [Soma]
Msambaza mihadarati mstaafu ajitokeza 02.12.2006 [Soma]
*Wamo wanajeshi wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania
*Walidakwa mtaani Morisi wakiiuza kwenye 'rambo'
*Jeshi lataka maelezo BFT walikwendakwendaje huko
Na Joyce Magoti
JESHI la Polisi nchini limethibitisha kukamatwa kwa mabondia watatu na raia wawili Watanzania nchini Morisi (Mauritius) wakiwa na mihadarati na kusema walitumwa na mfanyabiashara wa Dar es Salaam.
Mabondia hao, Fills Ramadhani (30) mwenye pasipoti namba AB 226128 ya Tanzania, Ally Rajabu (36) pasi namba AB 288440, Nathaniel Elias (39) pasi namba AB 279681 na Emilian Patrick (27) mwenye pasi namba AB 082456.
Wengine ni Petro Charles (30) mwenye pasi namba AB 083452 na Irenge Nasoro Mareo (43) pasi namba AB 080729 na walikamatwa pamoja na mwanamke wa Kenya Bi. Prisila Wanja 'Nyeri' mwenye pasi namba A 1039833 ya Kenya, wakiwa na pipi 373 za dawa ya kulevya aina ya heroin zenye uzito wa kilo sita.
Hayo yalisemwa jana Dar es Salaam na Naibu Kamishna wa Polisi, Bw. Peter Kivuyo, wakati akitoa taarifa ya kuthibitisha kukamatwa kwa wanamasumbwi hao nchini Morisi wakiwa na dawa za kulevya.
Alisema upelelezi uliofanywa na Polisi, ulibaini kuwa dawa hizo ni mali ya mfanyabiashara wa Dar es Saalam, ambaye yuko katika mtandao wa watu wanaojihusisha na biashara ya dawa za kulevya.
Bw. Kivuyo alisema Jeshi lake lilishindwa kutoa taarifa mapema kutokana na kosa hilo kuwa la jinai na kuhitaji muda ili kupata taarifa sahihi na za kweli, hadi taarifa hiyo ilipotumwa kutoka Morisi ikiambatana na picha za watuhumiwa.
Alisema watuhumiwa hao kabla ya kwenda Morisi wakitokea Nairobi kwa ndege ya Morisi namba MK 5355 walipekuliwa katika viwanja vya ndege vya Nairobi na Morisi bila kupatikana na kitu chochote mpaka wakafika na kuchukua vyumba viwili vya kulala katika hoteli ya Mount View.
Alisema kutokana na taarifa za shaka za nyuma zilizokuwapo juu yao, askari wa nchi hiyo waliendelea kuwafanyia uchunguzi na Juni 11 mwaka huu, wawili kati yao walikamatwa mtaani wakiwa na mfuko mweusi wenye dawa hizo.
"Baada ya watu hao wawili kukamatwa, walipelekwa hotelini na kuunganishwa na wenzao wanne na baada ya mahojiano, walimtaja mwanamke raia wa Kenya waliyesafiri naye ndege moja huku yeye akiwa amepandia Nairobi," alisema.
Bw. Kivuyo alisema uchunguzi ulionesha kuwa watu hao walisafirisha dawa hizo kwa kuzimeza zikiwa katika vifuko vyeusi, hali ambayo ni vigumu kuonekana katika vipimo vya usalama katika uwanja wa ndege.
Alisema watuhumiwa wote walikuwa na paspoti halali na walifikishwa katika Mahakama nchini humo na kwamba Watanzania hao wanashitakiwa kuingiza nchini humo dawa za kulevya na Mkenya anashitakiwa kwa kusaidia kuingiza dawa hizo nchini humo.
"Baada ya Jeshi letu kufanya uchunguzi wa kina, tumebaini kuwa dawa hizo zilitoka hapa na ni mali ya mfanyabiashara ambaye tumepata jina lake na namba zake za simu na ni mkazi wa Dar es Salaam, ambaye pia yuko katika mtandao wa wauzaji wa dawa za kulevya," alisema.
Alisema hadi sasa hawajapata taarifa sahihi kuhusu lini kesi hiyo itasikilizwa, lakini akasema itategemea na kukamilika kwa upelelezi ikiwa ni pamoja na kasi ya usikilizaji wa kesi wa Mahakama hiyo.
Katika taarifa nyingine iliyotolewa jana na Makao Makuu ya Jeshi la Wananchi Tanzania (MMJKT), ilisema miongoni mwa watuhumiwa hao, watatu ni wanajeshi.
Wanajeshi kwa mujibu wa taarifa hiyo ni Ofisa Mteule Daraja la Kwanza wa JWTZ, Nassoro Michael ambaye Polisi imemtaja kama Irenge Nassoro Mareo, ambaye ni kocha wa timu ya Taifa ya ngumi; Koplo Usu Petro Mtagwa au Petro Charles na Praiveti Emilian Patrick.
Taarifa ilisema mabondia hao waliombwa na Shirikisho la Ngumi (BFT) kwa ajili ya maandalizi ya timu ya Taifa ya Ngumi kwa michezo ya Olimpiki itakayofanyika China Agosti mwaka huu.
Ilisema JWTZ kwa kutambua umuhimu wa michezo na ushirikiano wa muda mrefu na BFT, iliwapa kibali cha kujiunga na timu ya Taifa kwa ajili ya maandalizi hayo.
"Hata hivyo, wachezaji hao waliporuhusiwa kujiunga na timu hiyo kwa muda wote wa mazoezi, walikuwa chini ya uangalizi wa karibu wa BFT, kwa vile muda wote walikuwa nao katika kambi ya mazoezi.
"BFT walikuwa na mamlaka ya kuwatumia katika michezo ya majaribio ndani na si nje ya nchi. Kwa kutambua hilo, BFT iliandika barua yenye kumbukumbu BFT/GC/Vol 2/44 ya Mei 28 mwaka huu, ikiomba kuwatumia wachezaji hao nchini Morisi katika mashindano ya pili ya Afrika yaliyoanza Juni 12-22 mwaka huu," ilisema taarifa.
Iliongeza kuwa ombi hilo lilikataliwa na JWTZ kwa barua yenye kumbukumbu namba MMJKT/3095-3 ya Juni 6 mwaka huu na kwamba utaratibu wa mwanajeshi yeyote kwenda nje ya nchi ni lazima uwe na kibali cha Mkuu wa Majeshi.
"JWTZ ilipata taarifa ya kukamatwa kwa wachezaji hao kupitia vyombo vya habari vya ndani na nje ya nchi, ambao walikwenda nje bila kibali cha mwajiri wao.
"JWTZ itahitaji maelezo kutoka BFT ni vipi mabondia hao ambao ni wanajeshi, walisafiri nje ya nchi bila idhini ya Mkuu wa Majeshi," ilisema.
Jeshi la Wananchi, ilisema taarifa, limeanza uchunguzi ili kubaini mazingira ya utoro wa wanajeshi hao ili hatua zinazostahili ziweze kuchukuliwa.
Source: majira
JE HUYU KIGOGO NI NANI?