semmy samson
Member
- Dec 20, 2010
- 85
- 0
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera na Uratibu), William Lukuvi, akiwa na Mkuu wa Wilaya ya Ngorongoro, Elias Wawalali na Rose Nyerere (katikati) baada ya kuwasili katika Uwanja wa Ndega wa Wasso, Liliondo, jana asubuhi. Rose alitua na ndege nyingine akiwa na mdogo wake anayeumwa, Mazembe Nyerere.Waziri Lukuvi na msafara wale walielekea kijijini Samunge kwa Mchungaji Ambilikile Masapile
WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera na Uratibu), William Lukuvi, amekiri kuwa mkusanyiko mkubwa wa watu wanaokwenda kunywa dawa kijijini Samunge, Loliondo mkoani Arusha ni tukio la kihistoria ambalo halijawahi kutokea kabla na baada ya Uhuru wa Tanzania.
Waziri Lukuvi alitoa kauli hiyo jana kijijini hapa, alipokwenda kufuatilia utekelezaji wa maagizo aliyotoa kwa niaba ya Serikali siku kadhaa zilizopita kuhusu uboreshaji wa mazingira ya utoaji huduma.
"Jamani kama kuna mtu ambaye anapuuza hiki kinachoendelea hapa Loliondo kwa kweli ni vigumu kumuelewa, haiwezekani watu wote hawa waje huku wakati hakuna kitu.
"Kwa kumbukumbu zangu sahihi, sikumbuki ni lini katika nchi yetu kuliwahi kutokea mkusanyiko mkubwa kama huu wa watu wa rika zote, wenye vipato, elimu na utaifa tofauti kama hili la kwa Mchungali Ambilikile, huu ni muujiza.
"Kama nilivyokwisha sema hapo awali, sisi kama Serikali kamwe hatutaingilia huduma ya huyu mzee, lakini kwa sababu watu ni wengi sana hapa hatuwezi kukaa pembeni, ni lazima tuje tusaidie kuboresha mazingira ili wananchi wengi iwezekanavyo wapate hii huduma," alisema.
Waziri huyo alitumia fursa hiyo kulipongeza Jeshi la Polisi kwa kuimairisha ulinzi na kulinda amani, hasa kwa kuzingatia umati mkubwa wa watu na mazingira duni kiutendaji yaliyopo kijijini Samunge.
Mbali na pongezi kubwa kwa Jeshi hilo, alimsifu Mkuu wa Wilaya ya Ngorongoro, Elias Wawalali pamoja na wasaidizi wake kwa kufanya kazi usiku na mchana kuhakikisha mambo yanakwenda sawa.
Katika ziara hiyo jana, Waziri Lukuvi alikutana na kupeana mkono na Mchungaji Mstaafu Ambilikile Masapile, na kisha alipewa dawa akanywa pamoja na mkewe na wageni wengine.
Lukuvi, alimwomba Mchungaji Masapile, aeleze mambo ambayo angependa Serikali iyafanye.
Akijibu swali hilo, Mchungaji Masapile ambaye huzungumza taratibu, aliiomba Serikali imsaidie kumpatia sufuria kubwa tatu na maturubai ya kutosha.
Alisema sufuria hizo ni kwa ajili ya kuchemshia dawa na maturubai ni kwa ajili ya kuwasaidia maelfu ya watu wanaofika kupata dawa, hasa wakati huu wa mvua kubwa. Pia aliomba apatiwe tanki kubwa la kuhifadhia maji. Samunge kuna mfumo wa maji safi na salama ya bomba. Sufuria anazoomba zina uwezo wa kuhifadhi lita zaidi ya 400 kwa kila sufuria moja.
Kwa sasa Halmashauri ya Ngorongoro, imetoa gari linalotumika kusomba kuni, na pia kuna gari la kuhudumia wagonjwa wanaohitaji huduma ya dharura kutoka kwenye msururu mrefu mno wa magari.
Bila kuchelewesha mambo, Lukuvi alimkabidhi Mkuu wa Wilaya ya Loliondo, Sh milioni moja kwa ajili ya kununulia sufuria na tanki la kuhifadhia maji.
Aidha, alisema wiki ijayo Serikali itapeleka maturubai na viti ili viweze kusaidia maelfu kwa maelfu ya watu wanaomiminika nyumbani kwa Mchungaji Masapile kunywa dawa.
"Kwa kweli huyu mzee ni mtu wa Mungu, jamani hana makuu kabisa, nimeuliza gharama za masufuria na matanki ya maji nimeambiwa hazizidi Sh milioni moja, kwa hiyo nimekabidhi fedha hizo.
"Naondoka kwenda Dar es Salaam kukutana na wenzangu kwa ajili ya kushughulikia suala la mahema na viti kwa ajili ya watu kupumzika, kwa sababu wengine ni wagonjwa sana hivyo hawawezi kusimama kwa muda mrefu wakisubiri dawa.
"Mchungaji ameniambia uwezo wake ni kuhudumia watu 2,000 kwa siku, sasa itabidi kwa kushirikiana na uongozi wa mkoa na wilaya tuweke utaratibu ambao kwa siku wataruhusiwa watu 2,000 kufika kwake na kunywa dawa.
"Haileti maana mtu kushinda porini kwa siku nne hadi tano, kwa sababu kwa kufanya hivyo shughuli nyingine za maendeleo zinasimama. Kwa mfano gari nyingi zinazotumika hapa ni zile zinazobeba watalii, ni lazima tutafute utaratibu mzuri," alisema.
Pia aliwaonya wenye magari mabovu, ambao kutokana na tamaa ya pesa wamekuwa wakibeba abiria kuwapeleka kwa Mchungaji Masapile, kuacha kuyatumia.
Alisema magari hayo yamekuwa yakiharibika au kupinduka na kusababisha adha kubwa kwa wananchi.
Alisema ataagiza magari yote yanayokwenda kijijini Samunge, yakaguliwe na askari wa Kikosi cha Usalama Barabarani kabla ya kuanza safari ili kuhakiki ubora, na gari likishakaguliwa litapewa namba maalumu.
Jana watu wa kawaida na watu maarufu waliendelea kumiminika Samunge.
Miongoni mwao waliokunywa dawa jana ni Katibu Mkuu Kiongozi Mstaafu, Balozi Paul Rupia na mkewe; pamoja na Rosemary Nyerere ambaye ni mtoto wa Baba wa Taifa, Rosemary alimpeleka mdogo wake, Mazembe Joseph Nyerere, ambaye anasumbuliwa na maradhi ya figo.
Pia walikuwapo Watanzania wengi wenye asili ya Kiasia ambao wote, pamoja na watoto wao, walikunywa dawa.
Hali ilikuwa ya shangwe kwa watu wote hao waliobahatika kuonana na Mchungaji Masapile. Wengi walimshika mkono na kutaka kupiga picha naye.
Leo, makamanda wa polisi wa mikoa karibu yote nchini wanatarajiwa kuwapo Samunge kwa ajili ya kujionea hali halisi na kumalizia safari yao kwa kupata dawa.
Msururu wa magari ni mrefu, na kwa taarifa za jana ulikuwa umefikia urefu wa kilomita 20.
Habari hii imeandikwa na Manyerere Jackton, Masyaga Matinyi na Eliya Mbonea, ambao kwa zaidi ya wiki moja sasa wapo Samunge wakiripoti tukio hili kubwa na la aina yake kuwahi kutokea nchini.