Roving Journalist
JF Roving Journalist
- Apr 18, 2017
- 4,783
- 14,975
Chama cha ACT Wazalendo kimesema kuwa kipaumbele cha Chama hicho kwa sasa ni kupigania mageuzi ya mfumo wa uchaguzi na kurejesha thamani ya kura ya kila Mtanzania kwenye uchaguzi.
Msimamo huo umeelezwa na Kiongozi wa Chama Mstaafu wa ACT Wazalendo, Ndugu Zitto Kabwe, ambaye alikuwa mgeni rasmi katika Kongamano la Uzinduzi wa Operesheni ya Chama, Operesheni Linda Demokrasia, lililofanyika katika Jimbo la Lindi Mjini leo tarehe 29 Machi 2025.
Ndugu Zitto Kabwe amesema kwamba Operesheni Linda Demokrasia inalengo la kurudisha thamani ya kura kwa Mtanzania. Alisema haya akilaani ukiukwaji wa sheria na misingi ya haki katika chaguzi tatu zilizopita.
"Kwa chaguzi tatu mfululizo thamani ya kura imepotea. Uchaguzi wa Serikali za Mitaa 2019 hakukuwa na kura, takribani wagombea wote wa upinzani walienguliwa. Mwaka 2020 tuliona kwa mara ya kwanza kura feki zikozagaa hovyo barabarani. Mwaka 2024 wakafanya kama mwaka 2020" alisema Zitto Kabwe.
"Tume ya Uchaguzi yenye wajumbe kama Omari Mapuri ambaye amewahi kuwa Mwenezi wa CCM inawezaje kutenda haki kwa watu wote? Sheria ya sasa ya Tume Huru ya Uchaguzi imeweka utaratibu kuwa angalau wajumbe wa Tume ya Uchaguzi wapatikane kwa ushindani. Watu waombe na wafanyiwe usaili. Serikali ya CCM haitaki kutekeleza jambo ambalo wamelitunga wenyewe."
Zitto Kabwe amesema kutokana na kuvurugwa kwa demokrasia nchini, matokeo yake ni kuporomoka kwa uzalendo miongoni mwa wananchi.
"Kwa wizi wa kura CCM wanadhani wanatukomoa CCM. CCM wanalikomoa Taifa. Mapenzi kwa Taifa yanaporomoka, watu hawajivunii tena Utanzania, wanavumilia kwa sababu hawana pa kwenda." alisisitiza Zitto Kabwe.
"Kulinda demokrasia ni wajibu namba moja wa raia. Raia wanapokosa uhuru wa kuamua nani awe kiongozi wao wanakuwa watumwa ndani ya nchi yao," alisisitiza Ndugu Mchinjita.
Chama cha ACT Wazalendo kinaendelea na programu mbalimbali za Operesheni Linda Demokrasia ikiwemo Makongamano ya kufafanua dhana hiyo kwenye Mikoa mbalimbali na ziara kwa wadau mbalimbali wa demokrasia.
Imetolewa na Shangwe Ayo,
Naibu Katibu wa Habari, Uenezi na Mahusiano na Umma, ACT Wazalendo
29 Machi 2025