Kwa Wana CCM na Wenye Mapendo na Taifa Letu

August

JF-Expert Member
Jun 18, 2007
8,386
4,045
Naomba kuwauliza ndugu zangu wa CCM, kuanzia ngazi ya juu mpaka ya Chini, kwamba wanapopitisaha eg Miswada ya Bunge wanajua maana yake na madhara yake kwa nchi au ndio kusindikiza Bwege wakati wenzao wana Faidika na Hiyo Miswada.
Mojawapo ni hiyo ya Madini, Ubinafsishaji, hata hizi sheria za kutangaza Mali wakati ukiomba faili lenyewe hupewi, Miswada ya Kodi nakadhalika, au ndio kudanganyika na elfu kumi kumi za vikao na kupewa uenyekiti au ujumbe kwenye Bodi ndiko kunako wadanganya?
Pia hivi karibini tuliona Umoja wa Vijana wa CCM wakipokea 400m kutoka kwa mfadhili moja , Je hii fedha imekuja kwa nia nzuri, na inajenga taifa kikweli kweli au inajenga nchi kama Ice cream jua likija ina yayuka.
NNi mengi yapo yanafanyika na yanapitishwa na Vikao halali vya CCM au katika Bunge letu ambayo ni ya kuiua au kuiangamiza nchi yetu, au kuwanufaisha wachache lakini inapigiwa kura na wengi wetu. Sasa sisi/hao wanaopigia kura maamuzi mabovu au kupitisha kiongozi mbovu, je wanaelewa kwamba wanajiangamizi wenyewe?
Mifano Nyingine inaweza kuwa Ubinafsi shaji wa TRC, ATC, Bandari nk
 
kumbuka walivyofanya kwenye issue ya buzwagi... hatuna watu hapa, hawafai wote!!!
 
Unategemea nini wakati una wabunge wengi wa darasa la saba.? Si hivyo tu, wengi wao wanaqualifications za kugushi; wanajiita DR. kumbe wamenunua hizo title kwenye internet. Kushangaza zaidi wengine wanachaguliwa kuwa mawaziri na manaibu mawaziri. Kwa mtindo huu ujue ukipanda bangi huwezi kuvuna mpunga!! CCM inabariki uzandiki wote huu na jitihada za kutaka kuweka minimum qualifications kuwa mbunge awe angalau na degree ya kwanza zinapingwa kwa kutumia mizengwe lukuki.
 
Nape asema Makamba anakumbatia mafisadi

2008-12-11 13:16:07
Na Simon Mhina

Kada machachari wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Nape Nnauye, amesema kauli ya Katibu Mkuu wa chama hicho, Yusuf Makamba, kwamba mjadala juu ya mafisadi wa Akauti ya Malipo ya Madeni ya Nje (EPA) katika Benki Kuu ya Tanzania (BoT) ufungwe, inaashiria kuwakumbatia mafisadi.

Mwanasiasa huyo chipukizi ambaye yupo katika kipindi cha mapambano na makada wenzake ndani ya Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM), kutokana na kuvuliwa uanachama kwa kupinga mradi wa Jengo Jipya la Umoja huo, alisema hatua ya Makamba kuweka mizengwe mapambano dhidi ya ufisadi inawavunja moyo watendaji wa serikali ambao wapo mstari wa mbele kushughulikia tatizo hilo.

Nape ambaye bado ni Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM (NEC), alisema kauli ya Makamba ni sawa na ya mtu anayeogopa kivuli chake.

Hata hivyo, Nape katika mazungumzo na Nipashe jijini Dar es Salaam jana, alisema kimsingi Makamba hana uwezo wala madaraka ya kuzuia mjadala juu ya mafisadi.

Nape alisema ingawa hana uhusiano wowote na watu wanaopiga makelele juu ya ufisadi, lakini anafikiri wanafanya hivyo kutokana na machungu makubwa ya umasikini wanayopata Watanzania kutokana na mafisadi.

Alihoji: ``Hivi Mzee Makamba mafisadi wakisemwa vibaya yeye anakerwa na nini?

Hivi kinachomkera ni kipi, mafisadi waliopora fedha za wavuja jasho au wavuja jasho wanaopiga makelele juu ya mafisadi kuwaibia?``

Alisisitiza kuwa katika hali ya kawaida, hakuna Mtanzania ambaye atanyamazia ufisadi kutokana na uzito wake.

Nape alihoji tena: ``Ina maana Mzee Makamba anajua idadi ya mafisadi wote nchini?``

Akifafanua, alisema kazi ya kuwashughulikia wahalifu hao ipo chini ya serikali na vyombo vyake vya dola na sio jambo la kisiasa.


Wakati huo huo, Mbunge wa Moshi Mjini kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Philimon Ndesamburo, amesema chama chake `kitafunga mdomo` kuhusu ufisadi, iwapo Rais wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa, atakamatwa na kufikishwa mahakamani.

Alisema Mkapa ni hazina kubwa ya mafisadi nchini na siku akifikishwa kortini janga hilo litakuwa limefikia tamati.

``Chadema hatutaacha kupiga kelele juu ya ufisadi kama anavyosema Makamba hadi hapo Mkapa ambaye ni hazina ya mafisadi atakapopelekwa kortini, mambo yote yaliyofanyika yalikuwa chini ya utawala wake na alikuwa anayajua na alishiriki, lazima akamatwe,``alisema Ndesamburo.

Mbunge huyo alisema mafisadi ndani ya CCM na serikali yake, hawajamalizika hivyo lazima waendelee kusakwa.
Alisema asilimia 10 tu ya mafisadi wote nchini ndio wamekamatwa, lakini asilimia 90 akiwemo `baba lao` bado wapo mitaani.

Ndesamburo alisema japokuwa Makamba amelenga kuwasaidia baadhi ya mafisadi, lakini kwa hili anatakiwa aone aibu.

``Yaani wakati huu ambao Rais Jakaya Kikwete ameridhia watu waliokuwa mawaziri wafikishwe Mahakamani yeye anasimama kutetea ufisadi, namuomba angalau aone aibu, hata kama amelambishwa asali,`` alisema.

Kuhusu Operesheni Sangara, Ndesamburo alisema itaendelea kwa nguvu zote licha ya Makamba kuibeza, kwa vile inalenga kuwafumbua macho Watanzania.

Alisema operesheni hiyo si uchochezi wala nguvu ya soda, bali Makamba ametoa shutuma hizo, baada ya kushindwa kujibu hoja zinazotolewa na Chadema.

Makamba alinukuliwa katika vyombo vya habari jana akisema kwamba mjadala wa EPA kwa sasa umefungwa kwa kuwa watuhumiwa wote wamefikishwa kortini.

Hata hivyo, ukweli ni kwamba bado watuhumiwa wengine wakiwamo wamiliki wa Kagoda Agriculture Ltd hawajafikishwa kortini.
Habari zaidi soma ukurasa wa pili.

SOURCE: Nipashe
 
Date::12/12/2008
Mbunge: Makamba ana jambo EPA
Na Ally Sonda, Moshi
Mwananchi

MBUNGE wa Viti Maalumu wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo(Chadema), Lucy Owenya ameliomba Jeshi la Polisi kumuhoji katibu mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Luteni Yusuph Makamba kuhusu kauli yake ya kutaka mjadala dhidi ya mafisadi nchini ufungwe.

Wakati viongozi wa juu wa serikali wakisema kuwa uchunguzi katika wizi wa fedha kwenye Akaunti ya Malimbikizo ya Madeni ya Nje (EPA) bado unaendelea licha ya watu 20 kufikishwa mahakamani kujibu tuhuma na kwamba "mengi zaidi yatafichuka", katibu huyo wa CCM alishauri mjadala huo ufungwe kwa kuwa suala hilo limeshakwisha.

Rai yake imepokelewa kwa hisia tofauti na watu wa kada mbalimbali, wengi wakimshutumu mkuu huyo wa zamani wa mkoa wa Dar es salaam kwa kutaka kutumia ushawishi wake ili kuzima mjadala wa kashfa hiyo, akiwemo Owenya ambaye alisema kauli ya Makamba ina mengi yaliyojificha.

Owenya alitoa ombi hilo alilodai linamlenga mkuu wa jeshi hilo nchini, Inspekta Saidi Mwema, wakati akizungumza na Mwananchi mjini hapa na kudai kuwa Makamba ana jambo analotaka kuficha kuhusu sakata la wizi wa fedha kwenye Akaunti ya Malimbikizo ya Madeni ya Nje (EPA) ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT).

"Ni dhahiri kuwa kigogo huyo wa CCM anazo taarifa nyingi za mafisadi, ukiwemo wizi wa fedha za EPA. Ni vema sasa akahojiwa ili baadaye awe shahidi mwema mbele ya mahakama," alisema Owenya.

Alisema kauli yake ni ya kutia aibu na ni dhihaka kwa Watanzania wengi maskini wanaoishi kwa kula mlo mmoja kwa siku huku baadhi ya vigogo wa CCM na wa serikali wakichota kwa wizi mabilioni ya fedha ambayo yangewajengea msingi imara wa maisha yao.

Alimtaka Makamba atambue kuwa Tanzania ina maskini wengi ambao wanashindwa kusafiri kwa kukosa barabara vijijini, watoto wao kukosa elimu bora kwa sababu hakuna shule bora, kukosa maji safi na salama na wengine kukosa tiba kwa kuwa vituo vingi vya afya na zahanati hazina dawa.

Owenya amemtaka Makamba kuwaomba radhi watanzania kwa kutoa lugha yenye harufu ya Uchochezi ambayo inaweza kuwafanya wananchi hususan maskini wakaichukia serikali yao halali iliyopo madarakani.

Lakini akasisitiza zaidi kuwa anapaswa kumuomba radhi mwenyekiti wake wa CCM, Rais Jakaya Kikwete na waziri wake Mkuu kwa kutoa kauli inayopingana na vita waliyoitangaza vita dhidi ya mafisadi ambayo wamesema haina kikomo.

Makamba alitoa kauli hiyo wakati akizungumza kwa nyakati tofauti na wakazi wa wilaya za Karatu na Ngorongoro mkoani Arusha ambako aliomba mjadala wa tuhuma za ufisadi wa EPA ufungwe kwa vile tayari watuhumiwa wote wamefikishwa mahakamni.

"Ndugu zangu mjadala wa EPA na Ufisadi umekwisha... Rais Kikwete tayari amechukua hatua watuhumiwa wapo mahakamani. Sasa hili jambo kila siku kuendelea kulizungumza ni ajabu sana," alisema Makamba kwenye mkutano wa hadhara.
 
Sijui CCM wanangoja nini kumtimua Makamba kwenye Ukatibu Mkuu wa Chama..!!!

Nape ananifurahisha sana anapoweza kuita koleo, koleo bila kumungunya.
 
mropokaji makamba!!! ataua chama... hana tofauti na mapuri!!!
 
I like this!

``Yaani wakati huu ambao Rais Jakaya Kikwete ameridhia watu waliokuwa mawaziri wafikishwe Mahakamani yeye anasimama kutetea ufisadi, namuomba angalau aone aibu, hata kama amelambishwa asali,`` alisema.

Huyu mzee hana aibu kabisa...!

Hii ni nzuri zaidi kama Kijana kama Nape anaiona hiyo na kuisema kama alivyoisema..!

Makaba ni kama hategemei kusemwa na mwana ccm mwenzake kama hivyo...lakini kashasemwa ....!!!

Sidhani huyu mzee anajua utamaduni wa namna hiyo!!

Hii ingewafanya hata wana ccm wengine kumuiga Nape!!
 
Sijui CCM wanangoja nini kumtimua Makamba kwenye Ukatibu Mkuu wa Chama..!!!

Nape ananifurahisha sana anapoweza kuita koleo, koleo bila kumungunya.

Makamba si wa kitimua muda huu , ila wamwache awatibue hadi mwaka 2010 tuone itakuwaje .Hongera Makamba endelea kuwa kambakamba na makamba yako .
 
Bubu habari hii iliandikwa kwa makosa, maneno mengi yaliongezwa kwa makusudi na kuleta mgongano mkubwa sana huko ndani juzi na jana, ingawa it is about time sasa Makamba akaondoka,

Lakini tarehe 13 anasimama mbele ya kamati ya bunge ya ethics kujibu mashitaka kutoka kwa mbunge mwanamama mmoja, itakua saaafi sana.
 
Nape umesahau msemo wenu wa CCM 'kelele za mlango,hazimzuii mwenye nyumba kulala'.
Unavyozidi kupiga kelele ndivyo rufaa yako inavyozidi kuchelewa
Pole sana mkuu!!!
 
Date::12/13/2008
Zitto azidi kuwaka, asisitiza Kagoda mali ya CCM

* Adai fedha ilizochotwa EPA zilitumika uchaguzi mkuu 2005

Na Kizitto Noya
Mwananchi

MBUNGE wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe amesisitiza kuwa Chama Cha Mapinduzi (CCM) hakiwezi kukataa uhusiano wake na Kampuni ya Kagoda Agricultural Limited iliyochota zaidi ya Sh40 bilioni kwenye Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA) katika Benki Kuu ya Tanzania.

Zitto aliyekuwa anajibu mapigo ya CCM iliyomshutumu juzi kwa kuipaka matope kwa kuihusisha na Kagoda, alisisitiza kuwa CCM haiwezi kujivua gamba la Kagoda kwa kuwa ndiyo inayomiliki kampuni hiyo, ikiwa miongoni mwa kampuni 22 zilizochota jumla ya Sh133 bilioni katika Benki Kuu ya Tanzania (BoT).

"CCM ndiyo inayomiliki Kagoda na Kagoda ni ya CCM. Fedha za Kagoda ndizo zilizotumika kwenye kampeni za CCM katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2005. Huu ndio ukweli," alilisitiza Zitto.

Alisema kauli ya chama hicho iliyotolewa juzi na Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, John Chiligati kuikana kampuni ya Kagoda, ililenga kujisafisha lakini pamoja na jitihada hizo, ukweli utaendelea kubaki kuwa kampuni ya Kagoda ni mali ya CCM.

Kwa mujibu wa Kabwe, endapo CCM inataka kutakata inatakiwa kumruhusu Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kukagua hesabu zake za mwaka 2004/2005 na ieleze wapi ilipata fedha za uchaguzi mkuu mwaka 2005 uliomwingiza Rais Jakaya Kikwete madarakani.

"Kama ni kujisafisha njia nzuri kwao si kutoa matamko, chama hicho kinatakiwa kumruhusu Mkaguzi Mkuu akikague na baadaye waseme fedha walizotumia katika uchaguzi mkuu mwaka 2005 zilizotoka wapi," alisema.

Alisema hakuna mantiki wala uhalali kuwaondoa mafisadi wa EPA katika uhusiano na CCM, kwani sehemu ya fedha iliyochotwa kwenye akaunti hiyo, zilitumiwa na CCM kwenye uchaguzi mkuu mwaka 2005.

"Mimi nasema hii ni spinning (kupindisha ukweli), kama mtu amechota Sh40 bilioni na sehemu ya fedha hizo zikatumika kwenye uchaguzi wa CCM utawezaje kukiondoa chama hicho kwenye ufisadi huo?" alihoji na kuendela:

"Kama CCM wataweza kuthibitisha kwa ushahidi kwamba hawahusiki na ufisadi huo na kwa ushahidi wa taarifa ya mkaguzi mkuu kuhusu chama hicho, niko tayari kuwajibika na maelezo yangu," alisema.


Katika hatua nyingine Zitto alisema Chadema inatarajia kutoa tamko kuhusu kauli ya Chiligati kwamba vijana wanatakiwa kuacha kuifuatafuata CCM kwa kuwa walizaliwa wakaikuta ikiwa imara na watakufa na kuiacha ikiwa imara.

Alisema kauli hiyo ni hatari kwa usalama wa vijana wa aina yake wanaotetea maslahi ya umma hivyo chama chake cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) lazima kitoe msimamo wake katika hilo.

"Labda nimalizie kwa kusema kwamba Chiligati anaposema sisi vijana tunaoifuata fuata CCM tutakufa na kuiacha CCM imara ni very serious. Kama chama (Chadema), leo (jana) tutaitolea tamko kauli hiyo kwani tunahisi wanataka kutuua," alisema.

Kabwe alitoa kauli hiyo siku moja baada ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kutoa tamko rasmi kuiruka kampuni ya Kagoda Agricultral Limited ikisema kuwa haina uhusiano nayo.

Chiligati aliwaambia waandishi wa habari juzi kuwa chama hicho hakina uhusiano wa aina yoyote na kampuni hiyo na kwamba hata kama kuna mwanachama anayehusika, ni suala lake binafsi na sio kwa mwavuli wa chama.

Tangu kuibuliwa kwa tuhuma hizo baadhi ya wanasiasa wamekuwa wakiihusisha CCM na Kampuni ya Kagoda inayodaiwa kuchota Sh40 bilioni kwenye akaunti hiyo na miongoni mwa watuhumiwa wa EPA waliokwishafikishwa mahakamani, yumo Mweka Hazina wa CCM Mkoa wa Kigoma, Shaaban Maranda

Juzi Chiligati ambaye ni Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM alitoa tamko la kukisafisha chama hicho na kashfa hiyo akisema haina uhusiano wowote na wala hawaitambui kampuni ya Kagoda.

"Vita dhidi ya ufisadi na rushwa nyingine ielekezwe kwa mtu mmoja mmoja na siyo CCM kwani haiwezekani wana-CCM wote wakaenda benki kuiba fedha hizo pamoja," alisema Chiligati na kuongeza: "kampuni ya Kagoda haina uhusiano wa aina yoyote na CCM na wala CCM hatuijui".

Alisema kwa muda mrefu viongozi wa vyama vya upinzani wamekuwa wakifanya juhudi za makusudi kutaka kuihusisha kampuni hiyo na CCM na kutoa mfano kwamba, hivi karibuni Kabwe alinukuliwa akisema kwamba kuisha kwa suala la EPA kwa kiwango kikubwa kunategemea Kagoda itakavyochukuliwa hatua za kisheria.

Chiligati alisema Zitto pia alinukuliwa akisema kushindwa kwa serikali kuchukua hatua dhidi ya Kagoda kuna maana moja tu na kwamba kampuni hiyo ndiyo inayoijengea CCM Kaburi.

Katibu mwenezi huyo alisema shutuma zinazotolewa na Zitto na wapinzani wengine ni siasa zenye takataka zinazolenga kuipaka matope CCM na kwamba ni za uzushi na uzandiki.

Alisema CCM ni chama chenye kuheshimika, makini na safi, hivyo vijana wadogo iliowalea kuanza kukipaka matope ni kutafuta laana na njama zao hazitafanikiwa.
 
Hii ni nzitto kweli kweli...

"...Kama CCM wataweza kuthibitisha kwa ushahidi kwamba hawahusiki na ufisadi huo na kwa ushahidi wa taarifa ya mkaguzi mkuu kuhusu chama hicho, niko tayari kuwajibika na maelezo yangu..."

Could this be a political demise?(with ambiguity)

Change is coming and I can proudly say, I am part of it!
See my avatar!!!
 
Muheshimiwa Kabwe amemwaga manyanga ya ukweli.
Kagoda ni CCM, na CCM ni kagoda.

Kagoda ni kiti anachotumia mtawala fulani katika jamii. CCM wanajiona wao ni watawala mpaka mwisho wa dunia, hivyo wakaamua kutumia jina hilo na kuliibia taifa.
Aliyekuwa gavana wa BOT, Daudi Balali alilazimishwa kutoa pesa hizo katika kikao cha CCM kule Dodoma na katika kuzima soo Balali asiseme basi CCM ikaona isiwe tabu ni bora kumpa sumu na kummaliza.
 
....hivi kila kampuni si ina accounts books ambazo kisheria lazima ziwepo?kwa ajiri ya Tax na mengine,sasa vipi hao kagoda watuonyeshe books zao tujue in/outs ya pesa zote zilizopitia kwao...so simple lakini ufisadi,abuse of power,kutofuata sheria vitazuia kila kitu na hakuna kitu tutajua lakini makelele ya Zitto is a good start na yatashika moto kwa wananchi,watu kama Chilligati hawana akili na hawajui matendo yao ndio yatafanya vizazi vyao vijavyo kuendelea kuishi kwenye umaskini mkubwa,anatetea CCM ambayo hata kesho inaweza kufutika tuu lakini Taifa litaendelea kuwepo...hawa watu inabidi wabadilishe thinking yao la sivyo watajiangamiza wenyewe!
 
Haya uliyoyasema wewe nayo ni mazito...

Muheshimiwa Kabwe amemwaga manyanga ya ukweli.
Kagoda ni CCM, na CCM ni kagoda.

Kagoda ni kiti anachotumia mtawala fulani katika jamii. CCM wanajiona wao ni watawala mpaka mwisho wa dunia, hivyo wakaamua kutumia jina hilo na kuliibia taifa.
Aliyekuwa gavana wa BOT, Daudi Balali alilazimishwa kutoa pesa hizo katika kikao cha CCM kule Dodoma na katika kuzima soo Balali asiseme basi CCM ikaona isiwe tabu ni bora kumpa sumu na kummaliza.

Una uthibitisho? Ama, uko tayari kijasiri, kuthibitisha uliyoyasema "uko tayari kuwajibika na maelezo yako?



Kidatu,
Maneno ya Mh. Zitto, yana uzito ndani yake, inamaana kuna cheche...,

"Kama CCM wataweza kuthibitisha kwa ushahidi kwamba hawahusiki na ufisadi huo na kwa ushahidi wa taarifa ya mkaguzi mkuu kuhusu chama hicho, niko tayari kuwajibika na maelezo yangu," alisema.

Haya aliyoyasema ni mazito, peke yake, siyo kujadiliwa juu juu, they have dismal contents and the consequences can be not so very good and good.

Vinginevyo anaomba Ukaguzi, na mkaguzi mkuu kuhusu chama hicho.

Hatahivyo, anadai ana maelezo, kwahivyo, atawajibika. Kwa maana nyingine yuko tayari kumwaga haya manyanga? Au kujiuzulu? 'Spinning' uh?'


Mh. Zitto ameonyesha ujasiri mkubwa, nafikiri kwa hilo nampa tano!
My best bet is to see how this unfolds now.

Anyway, nafikiri litakuwa duru safi sana la kuanzia mwaka 2009 na mwaka 2010.
 
Kuna mambo kadhaa hapa yafaa tujiulize na kuyatafakari kwa kina;

- tunailaumu serikali lakini tunamsifu Raisi wake.
- tunashangilia juhudi zake za kusafisha serikali lakini tunalaumu wasaidizi wake anaowateua yeye.
- tunailaumu CCM lakini tunamsifu Mwenyekiti wake.
- tunashangilia juhudi zake za kusafisha chama lakini tunawalaani wasaidizi wake anaoshirikiana nao.

Sasa kichekesho ni kuwa kiongozi wa serikali si ndiye huyo huyo anaongoza CCM ?
Sasa Padre Kalugendo akituita sisi wananchi walemavu wa fikra atakuwa amekosea ?
 
Pilipili imewekwa kwenye kidonda, sikiliza kilio.
Pamoja na akili yake ndogo,Nzi hukwepa kutua juu ya moto, sembuse Mifisadi ya CCM.
Mkalia kuti kavu huanguka pwaaa.
Za mwizi 39, ya 40 anapigwa pingu tu.
Nyani kakaa juu ya jiwe la moto na makalio wazi, kesho harudii tena.
Operesheni Sangara ipo Nyanza, Mipapa ya CCM inatafunana yenyewe huko bahari ya Hindi hii hii hiihi!!.

Dogo Zitto mwaga vitu watu tujidai.
 
Kuna mambo kadhaa hapa yafaa tujiulize na kuyatafakari kwa kina;

- tunailaumu serikali lakini tunamsifu Raisi wake.
- tunashangilia juhudi zake za kusafisha serikali lakini tunalaumu wasaidizi wake anaowateua yeye.
- tunailaumu CCM lakini tunamsifu Mwenyekiti wake.
- tunashangilia juhudi zake za kusafisha chama lakini tunawalaani wasaidizi wake anaoshirikiana nao.

Sasa kichekesho ni kuwa kiongozi wa serikali si ndiye huyo huyo anaongoza CCM ?
Sasa Padre Kalugendo akituita sisi wananchi walemavu wa fikra atakuwa amekosea ?

Swali lako atakaye diriki kujibu lazima akutoe golini kwanza,lazima atengeneze maswali upya ndio ayajibu hayo si haya ni nondo hizi.
 
Back
Top Bottom