mafuriko yameelekezwa baharini!
Upinzani umefanya makosa mengi ya msingi na wengi wameshaandika haya - kuna kupokea makapi, kuna kuweka mayai yote kapu moja (kuachiana), kuna kushindwa kutangaza sera hata siku ya ufunguzi wa kampeni, kuna kudhulumiana ndani ya ushirika, kuna kutowafikia wananchi wengi vijijini kwa kupenda starehe na misifa ya helikopta, kuna kutokujibu tuhuma nzito dhidi ya afya ya mgombea wao, kuna kutojibu tuhuma kuhusu chama kikuu ndani ya Ukawa kununuliwa, kuna kudharau mpinzani wao mkuu kana kwamba kazeeka au kachoka sana, kuna kudharau umuhimu wa watumbuizaji katika jamii ya kiafrika na kuwaita fiesta, n.k. Makosa ni mengi mno. Ila hii ilitokana na nini? UNYUMBU!
Nyumbu inasadikika ndiye mnyama mwenye IQ (ufahamu) mdogo kuliko wanyama wengi mbugani. Ni mnyama ambaye mwindaji hasumbui akili yake sana japo nyumbu ana maguvu na mapembe makali! Kichwani hamna kitu! Nyumbu hujihami kwa kuotea! Huota kuwa simba au mwindaji mwingine yeyote akija atamla jirani yake na si yeye! Kwa hiyo aendapo nyumbu mwenzie na yeye huenda! Nyumbu mwenzie akipiga kona na yeye hupiga kona! Nyumbu mwenzie akisimama na yeye husimama! Nyumbu mwenzie akiruka na yeyehakawii!
Ndio maana katika lile ajabu mojawapo la dunia litokealo mtoMara kule Serengeti mamba hujilia nyumbu hadi wanakinai! Akitokea nyumbu mmoja akaruka mtoni au akamsukuma mwenzie basi nyumbu wote watarukia mtoni au watasukumana hadi wadumbukie mtoni.
Tabia hii ya nyumbu tumeiona katika kampeni za Ukawa! Wenyewe kwa vinywa vyao tumewasikia wakijinadi ALIPO NA SISI TUPO! Yaani hata akitumbukia mtoni na wao watajiloweka humo! Hata pale ilipokuwa dhahiri kipenzi chao ni mgonjwa taabani tumewasikia wakisema TUTAMPA KURA HUYOHUYO HATA KWA MACHELA TUTAMPELEKA IKULU! Ni unyumbu ulikuwa upo kazini! Ndioo! Nyumbu hawanamuda wa kufikiri hata kidogo! Husukumana na huigana matendo!
Ni katika unyumbu huu watu walishindwa kufanya tafakuri yakina! Hata pale nyumbu mkuu aliposema atawaachia watu waliohukumiwa na mahakama ya juu kabisa nchini kwa makosa mazito kabisa bado nyumbu wadogo walirukaruka kushangilia!Si nyumbu? Hata pale wawindaji walipotuhumu kuwa nyumbu mkubwa nimgonjwa badala ya kuweka mkakati wa kuwaaminisha wapigakura kuwa nyumbu mkuu yuko ngangari wao ndio kwanza wanasema TUNATAKA HUYO HUYO MGONJWA!
Tabia hii ya unyumbu imesababisha anguko kuu nililolitabiri liwe kweli! Hili ni anguko kuu kwa kuwa hakika mwaka 2020 watu watasita kugeuka nyumbu! Bahati mbaya sana barani Afrika ili upinzani uweze kushika dola unyumbu unahitajika.
Kwa kawaida huwa anatokea almaarufu (celebrity) ambaye anatengeneza manyumbu wengi! Huyu Almaarufu akijua kucheza politics of wildbeasts anawashangaza watawala. Akishindwa huwa anatoweka kama alivyochomoza! Ni kwa kuwa kwa bahati mbaya zaidi unyumbu haujirudii! Ukipita umepita.