Kuparaganyika kwa Utawala Wao - Mwanzo wa Mwisho

Mzee Mwanakijiji

Platinum Member
Mar 10, 2006
33,476
39,995
Na. M. M. Mwanakijiji

Huwezi kutawala wananchi bila maono. Huwezi kuwatawala watu bila kuwapa mwelekeo wa wapi unataka kuwapeleka nawe badoukajiita "kiongozi mzuri". Naam, utawala usio na maono ya pamoja yenye kushirikisha matamanio na njozi za wananchi hugeuka na kuwa utawala wa kuburuzana, kutishana, kubishana na kubabaishana. Ni utawale wa kibabe.

Utawala ambao msingi wake ni vitisho, hadaa, matumizi ya dola au vyombo vya usalama ni utawala ambao umetengeneza ndani yake mbegu za kuvunjika kwake. Jamii zote za watu duniani ambazo zimewahi kujaribu kujenga tawala zisizo na maono ya pamoja zimeishia kuparaganyika. Zilijaribu kudumu kwa muda lakini kwa vile mbegu za kuparaganyika zinapandwa na kumwagiwa maji na ukosefu wa maono basi tawala hizo hufika mahali huanza kujivunjavunja zenyewe kama biskuti zilizomwagiwa maji.

Hili ni kweli kuanzia utawala wa enzi za Waajemi na Wakaldayo kama ilivyokuwa katika utawala wa Warumi na Wagiriki na kama ilivyokuwa katika tawala za Wamisri wa kale na tawala nyingine nyingi duniani. Tawala zinapofikia mahali pa kufanikiwa huanza kutengeneza ndani yake chembechembe za ukosefu wa maono kwani kila mmoja anaanza kutenda kwa manufaa yake mwenyewe na baada ya muda wanajikuta kundi kubwa la watu wao likiwa limetupwa nje ya baraza la mafanikio.

Hili ndilo lililosababisha Mapinduzi ya Ufaransa na baadaye kuvunjavunja nguvu za Mfalme kule Uingereza na hata kuchochea kwa kiasi kikubwa mapinduzi adhimu ya Marekani ambayo yalibainisha uwezo na haki ya wananchi kuikamata nchi na utawala wao mikononi mwao.

Katika taifa letu watawala wetu wameanza kuparaganyika. Sababu kubwa inayokoleza na kuharakisha kuvunjika vunjika kwa utawala wao siyo ufisadi tu - kwani ufisadi hasa ni dalili ya sababu yenyewe bali hasa ni Uroho. Wenzetu wanaita "greed"

Uroho kama nitakavyokuja kuonesha huko mbeleni tukijaaliwa ndio msingi wa kuvunjika na kumeguka kwa watawala kwani kila mmoja wao anataka kukusanya zaidi kwake na kwa familia yake na kwa jamaa yake. Uroho siyo wa madaraka tu - kwani huo upo na wote tunauona bali uroho mali na vitu. Kwa kadiri ambavyo waroho hawa wanazidi kujikusanyia pasi wenyewe kujua wanajikuta wanawanyangánya wananchi wao vitu vyao vingi kwa kutumia "sheria na taratibu".

Hata hivyo huwezi kuwanyangánya wananchi kila kitu. Unaweza kuwanyangánya ardhi, unaweza kuwanyangánya nafasi za kufanikiwa, unaweza kuwapora hata nguvukazi yao lakini kuna vitu viwili huwezi kuwapora na ni vitu hivyo ambavyo huwezi kuwapora ndivyo ambavyo tumeviona vikisababisha mabadiliko makubwa huko Afrika ya Kaskazini na Mashariki ya kati. Vitu hivyo ni Utu na Uhuru.

Mwanadamu ni kama paka ambaye umemuweka kwenye kona na kuanza kumpiga au kumnyanyasa. Utaweza kufanya hivyo kwa muda fulani lakini anapofikia mahali ambapo kizingiti cha woga kinapaswa kuvukwa mwanadamu hana cha kuogopa kwani nini kitaweza kumtokea zaidi ambacho tayari hakimtokei? Ndio utaona kuwa wanadamu katika mazingira hayo hawaogopi kifo wala mateso kwani hivyo vyote vinaweza kuhimiliwa isipokuwa ukosefu wa Utu na uhuru.

Ni hili ndilo liliwafanya kina Mandela kwenda kifungoni, Martin Luther King Jr. kutembea kule Selma, Alabama na hata kina Nyerere kukubali kufikishwa mahakamani kwa makosa ya uchochezi. Ni hili la kutambua tunu isiyo kifani ya utu na uhuru wa mwanadamu vilivyowafanya wananchi wa Zanzibari kuinuka dhidi ya utawala dhalimu wa Sultani na vibaraka wake na hatimaye kuweka utawala wa wananchi na kurudisha utu na uhuru wao.

Ni hili ndilo tunaloliona Syria leo hii ambako vikosi vya Bashar vinajitahidi sana kuzima maasi. Tatizo ni kuwa Bashar na wengine wenye kutegemea dola wanasahau kuwa mwanadamu akishavuka kizingiti cha woga hakuna risasi, pingu, wala jela inayoweza kuzima fikra zake zinazolia "mabadiliko mabadiliko". Wamisri baada ya kumfunga Khaled kwa wiki mbili wakati wa vuguvugu la mabadiliko lililomuondoa Mubarak miezi michache tu iliyopita walidhania kuwa kwa kufanya hivyo basi kijana yule angeweka manyanga chini na kwenda kujificha na familia yake.

Hawakutarajia kumuoja Khaled akizungumza kwenye TV na kusema kuwa yuko tayari kupoteza vyote alivyokuwa navyo - pamoja na familia yake - kama kwa kufanya hivyo kungempatia hadhi na utu na uhuru wake kama mwanadamu. Hii dhana watawala waliolewa madaraka hawaielewi. Sote tunakumbuka kilichotokea masaa machache baadaye kwani wale Wamisri ambao tayari walishaanza kukata tamaa walipata nguvu mpya na hatima kufanya kile kinachoitwa "the final push" iliyomtoa Mubarak madarakani.

Ndugu zangu, utawala wa CCM nchini umeparaganyika. Hawana maono ya pamoja na hawana mwelekeo wa pamoja - wanatuongoza kutoka katika hulka na siyo kutoka katika mtima wa kiakili. Wanaongozwa kama na hisia na wamepoteza uwezo wa kushika gidamu ya farasi wa mabadiliko na sasa mabadiliko yanaanza kuwaperekesha puta. Wameparaganyika kiasi kwamba sasa wanaanza kuumana na kutafunana wenyewe kwa wenyewe huku wakijiaminisha kuwa wanaongoza!

Naam, tunachoshuhudia ni mwanzo wa mwisho wa utawala ambao zamani uliwahi kuwapa wananchi wetu tumaini; tunashuhudia mwisho wa kizazi ambacho kilipewa nafasi ya kutuongoza kikashindwa na hata jaribio la kupitisha mikoba yao kwenda kizazi kingine linaonekana kushindwa vile vile kwa sababu badfo wanaamini ni wao pekee ndio wenye kustahili kutawala. Siyo hivyo tu wanaamini wanatakiwa kutawala bila kuulizwa, wafuje bila kukatazwa, wale bila kunyangánywa na wagawane bila watu wengine kusema kwanini.

Watanzania wameshavuka kizingiti cha woga; wanadai mabadiliko. Mabadiliko ambayo msingi wake ni Uhuru na Utu. Huko ndiko tulikoanzia kama taifa. Naam huko ndiko tunarudia. Nje ya hapo ni uadui wa kudumu kati yetu na wao. Wanyakyusa wanasema "tukufumusya ubulughu, bwitu naabene". Yaani tunatangaza ugomvi kati yetu na wao. Ni ugomvi wa kudumu. Mpaka wao wasalimu amri.
 
Ni kweli uyasemayo Mwanakijiji, Hawa watu wamelewa madaraka kama pombe ya Mwanzi inavyolewesha au kama pombe aina ya Gongo number one! inavyolewesha. Ila wanasahau kwamba wananchi wamechoshwa na karaha ya halufu ya pombe yao waliyokunywa bila mpango. Wananchi wanakeleka na matapishi ya pombe yao ya Gongo waliyokunywa bila mpango.

Tunahitaji mabadiliko ya kweli na tutayadai bila kuchoka.
 
Kuna kitu kimoja najiuliza kila siku bila majibu. Hivi huko CCM hakuna msafi? yaani hakuna maono? Hivi maprofessor na pHD holders wote huko hawana maono? Hivi siasa kwao ni kutumikia wananchi au familia zao? hizo familia zao kwao ni hapa TZ? Hivi wanaitazama nchi hii na hatma yake ni next few years?

Mungu tubariki, asante mwanakijiji.
 
huu mtindo wa kujivua magamba unapumbaza...dawa hapa ni kutumia njia ya mkato tu...kukata kichwa cha hili joka........
 
Kuna kitu kimoja najiuliza kila siku bila majibu. Hivi huko CCM hakuna msafi? yaani hakuna maono? Hivi maprofessor na pHD holders wote huko hawana maono? Hivi siasa kwao ni kutumikia wananchi au familia zao? hizo familia zao kwao ni hapa TZ? Hivi wanaitazama nchi hii na hatma yake ni next few years?

Mungu tubariki, asante mwanakijiji.
Mwanzoni Kingunge alijifanya kiziba mapengo ya MWALIMU baadae tukamshtukia ni bonge la fisadi, by this time KINGUNGE hana heshima yeyote ajifie zake tupungukiwe mafisadi.
CCM hamna wasomi wafikao kumi bali ni watu walioenda shule kwa levo mbalimbali.Hivi Prof Peter Msolwa naye msomi??alikitafuna SUA akageuka mchawi mtu wa kuogea ofisini kila jtatu ya mwanzo wa mwezi, amekutwaga makaburini (near SUA forestry garden)akiwa na sanda usiku yaani noma.
Watoto wa kutoka kwa mkewe wa ndoa wanaBULLEY kwa hiyo aliwageuza wake wa viprofesa vingine wake wa kumzalia watoto.
 
Kwa kuongezea tu mkuu, siku zote tawala zilizoparaganyika hu-survive kwa kununua affection (Kupendwa) hivyo basi mwisho wa siku watawala hujikuta wanaamini kila kitu, mtu, jamii wana bei zake na pesa(materials) ndiyo kila kitu. Ndiyo maana huwa inawawia vigumu kuamini kwamba wanaweza kupingwa au kukosolewa hivi hivi tu. Lazima wajiaminishe kwamba wapingaji wamenunuliwa. Na wanapojaribu kutafuta mnunuzi ni nani na kugundua hakuna basi wako tayari kufabricate kwa kutumia hela (materials) kuiaminisha jamii kwamba hata wapinzani wao wana bei...
 
Nakubaliana na hoja. Wamechanganyikiwa watawala wa sasa kiasi cha kuongoza kwa kudandia dandia hoja wanazodhani kuwa pengine zitawawezesha kukubalika. MMMMMMMMMh, tulishafikia ukomo! CCM huwezi aminika tena, huwezi jisafisha na ufisadi, huwezi waletea watu utu na uhuru, huwezi kuleta mageuzi ya kimaendeleo kwa watanzania. Na kwa tanzania ya sasa, hakuna kilichobakia, bali ni kuungana wote kuwatoa watawala wa sasa na kuanza njia yetu mpya ya kulikomboa taifa hili ki-upya. Kaza buti CDM-kukomboa watanzania-kwa maendeleo ya haraka na kweli!!!
 
Du, Mwanakijiji anatufikirisha mifano zaidi ya tawala zilizoshamiri lakini hatimaye zikaporomoka kama vile Ghana, Mali na Songhay. Kumbe somo la historia linakuza fikra kwa wenye kufikiri
 
Du, Mwanakijiji anatufikirisha mifano zaidi ya tawala zilizoshamiri lakini hatimaye zikaporomoka kama vile Ghana, Mali na Songhay. Kumbe somo la historia linakuza fikra kwa wenye kufikiri
Tatizo kubwa ni kuwa CCM na mashabiki wake wamejiaminisha kuwa kanuni zilizovunja tawala nyingine za kale haziwahusu wao. Kama Nyambala alivyosema manaamini wanapendwa sana. Wazo la kwamba kuna wananchi wanawachukia kutoka moyoni haliwaingii akilini kabisa.
 
Na. M. M. Mwanakijiji ... Ni hili ndilo liliwafanya kina Mandela kwenda kifungoni, Martin Luther King Jr. kutembea kule Selma, Alabama na hata kina Nyerere kukubali kufikishwa mahakamani kwa makosa ya uchochezi. Ni hili la kutambua tunu isiyo kifani ya utu na uhuru wa mwanadamu vilivyowafanya wananchi wa Zanzibari kuinuka dhidi ya utawala dhalimu wa Sultani na vibaraka wake na hatimaye kuweka utawala wa wananchi na kurudisha utu na uhuru wao.....Watanzania wameshavuka kizingiti cha woga; wanadai mabadiliko. Mabadiliko ambayo msingi wake ni Uhuru na Utu. Huko ndiko tulikoanzia kama taifa. Naam huko ndiko tunarudia. Nje ya hapo ni uadui wa kudumu kati yetu na wao. Wanyakyusa wanasema "tukufumusya ubulughu, bwitu naabene". Yaani tunatangaza ugomvi kati yetu na wao. Ni ugomvi wa kudumu. Mpaka wao wasalimu amri.

Ni Kweli, kuna tatizo la ujinga wa mwanadamu kutokuelewa UASILI wa viumbe hai. Na siku tatizo hili litakapomalizika mafanikio na maisha bora havitazuilika kwa namna yeyote ile.

Jiulize ..Jogoo anaweza kukosea kuwika? Kobe anaweza kukosea kuwa kobe?

La hasha!

Jogoo anafuatia uasili wake tu ..unaompa msukumo wa kuwa jogoo na hata kuwika kwake sio yeye kama anavyotaka ..ila ni uasili wake unampa msukumo huo. Mimea na hata wanyama wote ... wanatii uasili wao tu na maisha yao yanafikia kilele cha mafanikio yote.. Kobe hana uchaguzi wa kuwa kobe kwani Uasili wake ndio unamfanya kobe kuwa kobe... na si vinginevyo..na anafikia kilele cha mafanikio ya maisha yake.

Umeshajiuliza uasili wa mwandamu ni upi? Umeshajiuliza siku akiutambua na kuuenzi, kuujenga , kuulinda na kuutetea kwa kila hali nini kitatokea?

Kama ambavyo mbuyu haukosei kuwa mbuyu na mafanikio yote ya maisha ya mbuyu yanafikiwa ...ndivyo itakavyo kuwa kwa Taifa la Tanzania... Karibuni litafikia kilele cha mafanikio yasiyozuilika kwa namna yeyote ile.


Uasili wa mwandamu sio mimea, sio unyama ni UTU HURU!!

Siku Watanzania watakapo UTAMBUA NA KUENZI ... MAMALAKA YA UASILI HUU. SIKU UTU HURU UTAKAPO ANZA KUFOKA NA KUCHUKUA HATAMU ... hapatakalika.. nafuu usikie volakano na mtikisiko wa hiroshima...

Mamalaka ya Utu huru ... hayazuliki kwa Kikundi kidogo cha CCM au Viongozi wengine wote duniani wanvyojaribu kufanya..."KUUZUIA"

Hivi nani anajua maana ya Utanzania... Nani anajua siri ya Utanzania ..
UTANZANIA NI UTU HURU uliolala ..uko mbioni kuamka..na hakuna wa kuzuia ...
Kiongozi awaye yote ..kutoka chama chochote kama anajiheshimu ... mara moja aunge mkono ..dhana ya utu huru ..na aitekeleze kwa fikra, kauli na matendo ..vingine ahame nchi hii sio yake... sio kwa sababu nimesema ..ni kwa kuwa waasisi wa Taifa la Tanzania NI WAONA MBALI walikuwa na maarifa ya siri ya utu. Walifungasha kila kitu kwenye asili kuu ya mwandamu ..walikuwa na hekima na busara...kinachoatakiwa ni kuanza kwa vuguvugu dogo tu ... kurejea kwenye UTU NA UHRU WA MTANZANIA ... the rest you will not have to ask .. you will see!!
 
Tatizo kubwa kwa CCM ni 'over confidence' na kutokubaliana na hali halisi (unrealistic). Miaka nenda rudi CCM imekuwa inapandikiza mamluki kwenye vyama vya upinzani, kuhonga fedha nyingi na hata vyeo ili mtu/watu wawaunge mkono. Na wakati mwingine kutishia (i.e wafanyabiashara) ili wasikikatae chama hicho. Hizi tricks zimekuwepo kwa miaka na cha ajabu hawaonekani kukubali kuwa vyote hivyo haviwezi kumfanya mtu akakipenda chama kwa dhati. Ni sawa na forced marriage.

Hii inanikumbusha issue ya CIA Marekani kutumia water-boarding technic kama njia ya kupata information toka kwa wafungwa wa Guantamo Bay. Ukweli ni kwamba mfungwa kwa kuhofia mateso atasema chochote mmarekani anataka kusikia ili mradi apone lakini haaminishi alichosema ni kweli - kwa maana nyengine flawed information.

CCM wanajitapa wanapendwa lakini angalia namna walivyo busy kuhonga ili ionekane hivyo. Watu wanabebwa na fusso kwenda kwenye mikutano yao, T-shirt kila mahali, kanga ndio usiseme. kama wanapendwa yote hii ya nini?. Ukiangalia kwenye majukwaa wamekaa watu wazito, wanene wanatokwa na majasho kwa shibe.Lakini angalia umma ulioletwa na fusso, watu wamepauka na bila aibu utakuwa CCM wamewageuza kuwa 'mobile billboards kwa kuwavalisha t-shirt za manjano. Dhihaka.

CDM on the other hand wanaonekana kuwa sumaku, hakuna fusso, hakuna taarab, hakuna t-shirt wala kanga ila watu wanajitokeza tena kwa wingi mno. Nini kinawavuta? hope, hope for a better future.

Chema chajiuza, kibaya chajitembeza.
 
  • Thanks
Reactions: Ame
Iko siku kitaeleweka tu bongo. Ccm na watu wake watakuwa chama cha upinzani!

Ebu fanya tathimini upya Mkuu!

Mi naona kama haipo kabisa; sasa hivi ambacho wananchni kupitia chadema wanapambana nacho siyo chama cha siasa kwa maana ya CCM, CCM ili kwisha shindwa na CDM siku nyingi sana, sasa CDM wanapambana na Utawala uliopo ambao ulijiingiza katika siasa kupitia kwa nguvu za dola na hao ndio walioibomoa nchni; yaani Mafisadi, Baadhi ya wanasiasa wastafuu pamoja na Usalama wa Taifa na system yake (maana hawa ndio waliyoharibu CCM na hata hivyo hawajui hatima yao baada ya Tanzania kuzaliwa upya) ndio maana utakuta hata wanapo tafuta majibu ya maswali yanayosumbua Jamii wana shindwa kutofautisha kati ya utawala, Siasa na utendaji!

CCM na vyombo vya dola vilifanya kosa moja kubwa sana la kuwa wanafki baada ya kuanzishwa kwa siasa za vyama vingi nchni! CCM ilikubali vyama vingi kwa shingo upande na hivyo kufanya ubia wa kijasusi na UWT kwa ajili ya kujiaminisha kutawala milele; hawakujua madhara ya muda mrefu ni kukosa imani kwa wananchni, Siku zote vyama vilivyofanya ubia na vyombo vya dola vinakuwa na kiburi na kusahau wanyonge na wananchni wao, ukisha kuwa mbia na vyombo vya dola huwezi kufungua sikio kwa wanyonge. CCM ilikuwa na kiburi cha kuaminishiwa na Dola ndio maana uchaguzi wa 2010 Utakuta wakina Shimbo wanalazimika kutumika kutishia wananchni, wakina Mwema wanalazimika kuuwa Watanzania eti kwa vile wameandamana katika ardhi ya nchni yao tena bila hata silaha yoyote! Wakina Tendwa wanatishia kuifuta CDM hati kwavile haikubali kuwa kibaraka wa CCM!

Genekai, CCM haipo wala haitakuwepo tena baada ya ukombozi, angalia hata wakati CDM inafanya maandamano ya siasa kwa kuzunguka nchni bnaadhi ya mikoa kuomba ridhaa na kuelimisha Jamii juu ya madhara ya CCM wao wakitumia zaidi vitisho na kutegemea nguvu za Dola! na asasi zake za kidini; Sasa wanataka kujaribu kuadaa watu kuwa wao ni chama cha siasa kwa maneno matupu kuwa CCM imevua gamba ili kudanganya kuwa hiyo ni siasa lakini hamna kitu humo, Hilo neno kuvua gamba halikuwamo katika ahadi lukuki za Kikwete! CCM haiwezi kuibuka na kazi mpya ya kushaurisha jamii juu ya ahadi walizotoa lukuki ambazo zinasubiriwa kwa hamu kwa propaganda rahisi hivyo! Swala la kushughulikia Mafisadi haliwezi kutungiwa methali wakati vyombo vya dola vipo na ndio kazi zao, methali yanini tena hapo?

Hakuna haja ya kuleta methali mpya ilikudanganya kuwa CCM ipo Biz na kazi ya kuvua gamba wakati hiyo siyo kazi yao na hawaiwezi, wanajichunguza vipi waowenyewe! Vyombo vya Dola vilivyo huru vinatosha kushughulikia mambo yote ya Ufisadi bila ujanja ujanja. Mi naona watakuwa Biz miaka mitano tena na hii methali yao + zile ahadi za raisi + Ilani ya CCM sijui gap litakuwa kubwa kiasi gani?
 
Mwanzoni Kingunge alijifanya kiziba mapengo ya MWALIMU baadae tukamshtukia ni bonge la fisadi, by this time KINGUNGE hana heshima yeyote ajifie zake tupungukiwe mafisadi.
CCM hamna wasomi wafikao kumi bali ni watu walioenda shule kwa levo mbalimbali.Hivi Prof Peter Msolwa naye msomi??alikitafuna SUA akageuka mchawi mtu wa kuogea ofisini kila jtatu ya mwanzo wa mwezi, amekutwaga makaburini (near SUA forestry garden)akiwa na sanda usiku yaani noma.
Watoto wa kutoka kwa mkewe wa ndoa wanaBULLEY kwa hiyo aliwageuza wake wa viprofesa vingine wake wa kumzalia watoto.

This is too much my Merytina hata kama ni chuki haipaswi kuwa kiasi hiki huu ni zaidi ya uchawi ndugu yangu maana hapo ukweli, hisia na majungu yamejichanganya kiasi huwezi kujua which is which. Kwa uchache wa ninavyo mfahamu huyu uliyeiua personality yake kwakiasi hiki; Yeye pamoja na kina marehemu Chachage, Prof J. Maghembe na maprof wengine wamesaidia saana wasomi kupewa hadhi nchi hii hasa wanataaluma. Ungejua wanataaluma hali zao zilikuaje kuanzia 2003 kurudi nyuma basi ungempa moyo kwakusimamia kidete mslahi ya wanataaluma pamoja na kuwa alistaafu kabla ya kufaidi mafao ya uzeeni waliyoya pigania hata hivyo amekuwa compansated na package ya ubunge. And to be frank wasomi walianza kuanza kufikiriwa wakati drs and profs walipoingia kwa wingi bungeni (siyo wale wa degree za Puw no!), imagine kama hali ni mbaya hata sasa kabla ilikuaje?
 
Na. M. M. Mwanakijiji

Ndugu zangu, utawala wa CCM nchini umeparaganyika. Hawana maono ya pamoja na hawana mwelekeo wa pamoja - wanatuongoza kutoka katika hulka na siyo kutoka katika mtima wa kiakili. Wanaongozwa kama na hisia na wamepoteza uwezo wa kushika gidamu ya farasi wa mabadiliko na sasa mabadiliko yanaanza kuwaperekesha puta. Wameparaganyika kiasi kwamba sasa wanaanza kuumana na kutafunana wenyewe kwa wenyewe huku wakijiaminisha kuwa wanaongoza!
.

Nimeipenda hii !
 
Viongozi wetu hawawezi kuwa na maono kwani wengi wanatumia muda mwingi na pesa nyingi kujiandaa kutwaa madaraka na sio kujiandaa kuwatumikia wananchi. Wote tunaona jinsi ligi ya 2015 ilivyoshika kasi. Unategemea kuna mtu kati yao anayefikiria anataka kuwafanyia nini watanzania? Kwao sasa ni wakati wa mapambano na akifanikiwa kupata nafasi 2015 atabaki anashangaa na hatakuwa na jipya la kuwafanyia watz. Watu wa namna hiyo utawagundua kwa msemo '..kwanza nitaendeleza yale yote mazuri ya awamu iliyopita'. Mtu anayesema hivyo hajui anaenda kufanya nini ikulu, maana tunapomchagua mtu hatutegemei aharibu mazuri aliyoyakuta. Nguvu nyingi inaelekezwa kwenye uchaguzi na sio utumishi kwa wananchi. Wakati mwingine inakuwa heri miongo michache iliyopita ambapo kiongozi mtarajiwa alikuwa anajulikana/andaliwa mapema, leo kila mtu anayetaka 'kuuza sura' anagombea urais. China wana viongozi wao watarajiwa, hatokei mtu 'out of blue'.

Ukitaka kujua viongozi wana mchango kiasi gani kwenye maendeleo ya wananchi, fuatilia yanayotendeka Rwanda. Huko vitendo vinaongea. Hawana mafuta, wala lundo la madini kama nchi zingine, lakini maono ya mbali ya kiongozi mmoja tu yamewezesha kubadilisha maisha hata ya watu wa chini (mfano: kupungua kwa rushwa- hii ndio inayotesa watu wa chini). Hapa tusilete kisingizio cha nchi ndogo, maana hata ushelisheli na Lesotho ni nchi ndogo, vile vile Sudan na China ni nchi kubwa. Pamoja na mfumo mzima kuharibika kutokana na mauaji ya halaiki, leo wanafanya mambo na kuweka mikakati ambayo sisi wenye amani tele hatuwezi hata kuota ndotoni.

Tunahitaji Kiongozi ambaye njaa yake ni kuona anailetea mafanikio nchi yake. Ajue anataka kutufanyia nini na atafikaje hapo. Hatuhitaji Kiongozi ambaye kazi yake itakuwa kujaza hela kwenye mifuko yake, rafiki na ndugu zake.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom