ManiTek TV
JF-Expert Member
- Jun 3, 2011
- 410
- 155
Apple  ni kinara wa gajeti za mkononi, hayati Steve Jobs katika katika mkutano wa watengeza Apps na wanahabari WWDC aliweka wazi kuwa Apple ni kampuni ya kutengeza vifaa vya aina hiyo. Hata hivyo miaka ya karibuni wachambuzi wa masoko, fedha na teknolojia wamekuwa wakiiwekea alama ya kuuliza kampuni hiyo iwapo imefanza kuporomoka na wakati wake wa kutamba imefikia kilele.
Kabla ya kuzungumzia kuporomoka kwa Apple  kwanza tukumbushe mafanikio makubwa wa kampuni hii, katika kipindi cha pili cha uongozi wa Steve Jobs, yaani katika kipindi cha miaka kumi baina ya 2000 na 2010 thamani ya hisa Apple imeongezeka kwa wastani wa 600%. Apple imeleta mapinduzi ya matumizi na muonekano wa gajeti za muziki mwaka 2001 walipotoa iPod Classic ya Kwanza, waliuacha Ulimwengu mzima hoi, kuanzia hapo watu walianza kubadilika kwa jinsi wanavyosikiliza na kununua muziki. Miaka michache sote tumesahau kama kulikuwa na kitu kinaitwa Walkman zilizokuwa zinatolewa na Sony.
Mwaka 2007 iPhone ya kwanza ilikonga nyoyo za wanateknolojia na kuufanya ulimwengu mzima wa simu uanze kuangalia Apple  wanafanya nini ili na wao wafanye, pamoja na Google kutangaza kwamba Android Cup Cake ilikuwa tayari, iliwachukua karibu mwaka mzima kutoa simu ya kwanza ili walau iikaribie iPhone.
Mwaka 2010 katika WWDC Steve Jobs alizindua "magical device" ya mwisho mpaka sasa, tunakumbuka mara baada ya kutokea kwenye skrini ya Keynote, Jobs alisema "...and we call it the iPad". Kwa mara nyingine Makampuni mengine yakaanza kutengeneza tablets kwa kasi. Hatusemi kuwa iPad ilikuwa tablet ya kwanza. Sote tunafahamu kwamba tablet ya kwanza ni ile aliyopewa Nabii Musa (Moses) ikiwa na amri kumi. Lakini tangu tablet ile ulimwengu haukuwa ni wenye shauku kubwa na tablet mpaka ilipotoka iPad.
Lakini cha msingi ni kwamba Apple wamefanya maksoa kadhaa katika kipindi cha miaka kama mitano au sita ya mwisho ya mafanikio haya. Sasa hebu tuangalie ni mambo gani yaliyowapelekea wachambuzi kuanza kupata fikra kuwa huenda Apple wanaanza kuteremka na hasa kwa upande wa iPhone.
Mambo ambayo huenda yataiangusha Apple 
Awali, Apple wamekuwa na mtindo wa kutoa simu moja kila miaka miwili. Tunasema simu moja kila miaka miwili kwa sababu iPhone 3G, iPhone 3GS na iPhone 4S sio simu mpya. Ni simu ambazo ziliendeleza mauzo ya simu zile zile kwa kuziongezea kasi tu. Kwa jinsi ushindani ulivyopata kasi hasa kutoka kwa Samsung, Apple haiwezi kuendelea kuongoza kwa muda mrefu iwapo wataendelea kutoa simu moja kila miaka miwili.
Pili, Kufukuzwa kwa Makamu wa Rais wa iOS Scott Forstall kunaashiria wazi kuwa ndani ya Apple mambo si shwari. CEO mpya amekuwa akiyumbishwa na baadhi ya vigogo ndani ya Apple. Apple imeyumba katika sehemu mbili ambazo tutazizungumzia kwenye nukta zijayo. Scott Forstall hakufukuzwa peke yake bali yeye pamoja na Mkuu wa Mauzo John Browett.
Tatu, Apple ilipata skendo kubwa walipotoa iPhone 4, skendo iliyojulikana kama "Antenna-Gate" katika skendo hii watu wanaotumia mkono wa kushoto walipata matatizo ya simu zao kupoteza signal kwa vile wanapozikama walikuwa wanaunganisha sehemu ambayo haikutakiwa kuungana, Apple walizima "Antennagate" kwa kutoa bure mabampa kwa wanunuzi wote wa mwanzoni.
Nne, Kilichopelekea Scott Forstall kuondolewa kama Makamu wa Rais wa iOS ni kukataa kuomba radhi baada ya skendo nyingine kubwa katika kipindi cha miaka mitatu, skendo hiyo ni Ramani iliyotoka na iOS 6. Ramani hii ilikuwa ni aibu kwa kampuni hii. Hatimaye Apple waliomba radhi na kuwajulisha watumiaji wao wasitumie ramani hiyo badala yake kutafuta nyingine kwenye AppStore. Muda si mrefu Google Maps ilirudishwa kwenye AppStore kama mkombozi.
Tano, Wakati watengenezaji wote wa simu walianza kutoa simu kubwa kutoka 3.5" kwenda 3.7, 4", 4.2", 4.5", 4.7" hadi 5 Apple walikuwa wamelala. Imewachukua muda mrefu sana Apple kugundua kuwa ulimwengu wa simu unakwenda kwenye "Phablet", yaani masimu makubwa makubwa. Apple wameongeza ukubwa simu yao toleo la mwaka jana, yaani iPhone 5 kwenda 4". Kwa maoni yetu hapa walichelewa sana.
Sita, baada ya miaka 3 ya kuongeza ukubwa (iPhone 5) na kupunguza ukubwa (iPad Mini) Apple inahitaji kuuhakikishia ulimwengu kuwa kitengo cha utafiti na maendeleo (R&D) kinafanya kazi kwa ufanisi, ulimwengu unahitaji kuona bidhaa mpya ambayo itabadili tena dunia, la si hivyo Apple na Samsung wote ni sawa, hakuna kiongozi madhubuti.
Saba, wakati Apple bado inaendelea kupata faida katika kila biashara inayofanya, ripoti za fedha za Apple zinaonyesha kwamba kampuni hiyo inaendesha maduka zaidi ya 400 katika nchi 14 tofauti kwa hasara. Hii ndio iliyopelekea kufukuzwa kwa John Browett kama mkuu wa mauzo.
Nane na mwisho thamani ya hisa za Apple sasa imeanza kushuka, hivi karibu kampuni kubwa ya uwekezaji Morgan Stanley wameiondoa Apple kama miongoni mwa kampuni yenye hisa bora. Mpaka sasa Apple imeshuka thamani katika soko la hisa kwa jumla ya $226 bilioni. Hili ni pigo kubwa na mwokozi ni "magical device" kama vile iWatch au iTelevision, gajeti ziwe na uweoz wa kuubadili ulimwengu katika moja ya fani hizo. Utabiri wetu ni kwamba Apple bado haitatoa Apple TV (sio STB, TV hasa) hivi karibuni lakini wako karibu kutoa saa ya mkononi. Je saa hiyo itaushangaza ulimwengu?
Toa Mcango wako, Apple ndio inakwenda au itaendelea kutamba? Tueleze na sababu unazoziona wewe!