WATU 16 wamenusurika kufa baada ya boti waliyokuwa wakisafiria ya mv Nasebwa katika Ziwa Victoria kuzama. Watu hao walifanikiwa kuokoa maisha yao baada ya kuvaa maboya.
Taarifa zinasema kwamba boti hiyo iliyokuwa ikitokea Maisome kwenda Kaunda ilizama baada ya kugonga mwamba na kuanza kuingiza maji, lakini kutokana na boti kuwa na vifaa vya uokoaji, watu wote walivaa maboya yaliyowasaidia kuelea majini hadi walipookolewa.
Meneja Mawasiliano kwa Umma wa Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Majini na Nchi Kavu (Sumatra), David Mziray alisema boti hiyo inayomilikiwa na Msita Francisco wa Kisiwa cha Maisome Sengerema ilipata ajali hiyo Jumapili iliyopita majira ya saa nane mchana.
Mziray alisema, tukio kama hilo la okoaji linaonyesha umuhimu wa vyombo vya usafiri wa majini kuwa na vifaa vya kutosha vya kujiokolea kama maboya ambavyo mara kunapotokea ajali, abiria au wafanyakazi wa chombo husika wanaweza kuokolewa na kuwa salama.
Alisema Sumatra inaendelea kusisitiza kuwa wamiliki na waendesha vyombo vya majini ili kuepuka ajali kuzingatia kuwa chombo chochote hakiruhusiwi kuanza safari kama hakijakaguliwa na kupewa cheti au hakijasajiliwa au kimepakiwa kuzidi uwezo wake.
Pia chombo kisicho na mitambo (injini) hakiruhusiwi kubeba abiria huku chombo chochote hakiruhusiwi kuanza safari kama hakina vifaa vya kuokolea maisha, hasa majaketi kwa ajili ya wasafiri wake.
Mziray alisema chombo kabla ya kuanza safari ni lazima kupata taarifa ya hali ya hewa na kutoanza safari pale inapobainika kuwa hali ya hewa ni mbaya katika sehemu yoyote ile ya njia inayotarajiwa kutumiwa na chombo na mengineyo.
Source: Habari Leo