Kisa cha Nelson Chisale na Simba wa Mokwalo…!

Mtambuzi

Platinum Member
Oct 29, 2008
8,810
15,398
192646_714440.jpg
192646_714437.jpg

Mark Scott-Crossley
192646_713142.jpg
Mathebule Richard.jpg
Marehemu Richard Mathebula
192646_714416.jpg
Simon Mathebula
192646_714417.jpg
Richard Mathebula na Simon Mathebula
192646_714402 (1).jpg
Masalia ya nguo na mifupa ya Nelson Chisale

murder_wideweb__430x285.jpg
kaburi la Nelson Chisale

Mnamo mwanzoni mwa mwaka 2003 Nelson Oupa Chisale wakati huo akiwa na umri wa miaka 41 alipata kazi kama fundi seremala katika kampuni moja ya ujenzi iliyokuwa ikimilikiwa na tajiri mmoja nchini Afrika ya Kusini Mark Scott-Crossley, 37. Hata hivyo badala ya kuajiriwa kwa kazi aliyoomba, aliajiriwa kwa kazi isiyo ya ujuzi ya kufanya kazi shambani, katika shamba la tajiri huyo lililoko katika mji mdogo wa Hoedspruit uliopakana na Mbuga ya wanyama ya Kruger takriban kilometa 500 kutoka Johannesburg. Aliahidiwa kupata ujira mnono mara 10 kuzidi ule aliokuwa akiupata wakati akifanya kazi katika jiji Johannesburg.

Alikubaliana na mwajiri wake kwamba kiasi fulani cha fedha kiwekwe kwenye akaunti ya mpwa wake kwa ajili ya familia yake kujikimu lakini maelekezo yake hayakufanyiwa kazi. Alizungumza na Bosi wake bwana Mark Scott-Crossley, juu ya jambo hilo, na akamuahidi kulifanyia kazi swala lake. Hadi kufikia miezi nane tangu aanze kazi pale shambani, hakuna kiasi chochote cha fedha kilichotumwa kwa mpwa wake kulingana na maelekezo yake. Chisale alichukuwa uamuzi wa kuripoti jambo lile kwenye vyombo vinavyohusika ambapo alimshitaki bosi wake kwa kosa la kukiuka mkataba wake na kuvunja sheria za kazi.

Kutokana na kuripoti swala hilo, alianza kupata matatizo pale kazini na mwezi mmoja baadae, mnamo Novemba 2003, alifukuzwa kazi kwa kile kilichoelezwa kwamba ni mwizi, na alionywa asije akakanyaga katika eneo lile tena. Pamoja na kufukuzwa kazi, pia nguo zake zilichomwa moto zikiwemo namba za simu za mpwa wake aitwae Fetsang Jafta, ambaye ndiye aliyemuandikisha ili awe anatumiwa sehemu ya mshahara wake kila mwezi.

Mnamo siku ya Jumamosi ya Januari 31, 2004, Chisale alirudi shambani hapo ili kuchukuwa vyombo vyake vya kupikia, baada ya kupata kazi mahali pengine, lakini alipofika alikamatwa na wafanyakazi watatu waliotajwa kwa majina ya Robert Mnisi, Richard Mathebula, 41, na Simon Mathebula, 43, (hawa Mathebula sio ndugu), ambapo walimshambulia kwa mapanga na kisha kumfunga kwenye mti kwa masaa 6 au 7 hivi huku damu zikimvuja kutokana na majeraha. Walimuita Bosi wao Mark Scott-Crossley ambapo alifika akiwa ameongozana na mwanae wa kiume aliyekuwa na umri wa miaka 12. Alipofika alimuelekezea Chisale bunduki kichwani na kuanza kumhoji sababu ya kuingia shambani kwake ilhali alifukuzwa kazi na kuamriwa asirudi tena katika eneo hilo. Chisale alijitetea kwamba alifika pale kuchukuwa vyombo vyake alivyoviacha baada ya kupata kazi mahali pengine. Kwa mujibu wa wafanyakazi hao, Chisale alifumba macho kusali, akidhani atauawa kwa bunduki hiyo iliyoelekezwa kichwani mwake. Lakini Bosi wao alimpiga kwa kitako cha bunduki hadi akapoteza fahamu.

Chisale atupwa ndani ya zizi la Simba.........

Aliwaamuru kina Mathabula wampakie Chisale kwenye gari na akiwa na wafanyakazi hao aliendesha umbali wa kilometa 20 hadi kwenye shamba la kutunza na kuzalisha Simba weupe ambao ni adimu nchini humo, katika eneo la Mokwalo. Shamba hilo linamilikiwa na mtu mmoja aliyetajwa kwa jina la Albert Mostert.

Walipofika katika shamba hilo ilidaiwa kwamba Scott aliwaagiza Robert Mnisi, Simon Mathabula na Richard Mathabula, wamtupe Chisale ndani ya uzio ule walipohifadhiwa Simba zaidi ya 20, ambapo walimshambulia na kumla akiwa mzima.

Mnamo siku ya Jumapili ya Februari 1, 2004, wafanyakazi wa shamba hilo waliona mabaki ya mwili wa Binadamu ikiwepo fuvu la kichwa, vidole, mifupa kadhaa ya miguu na mbavu na nguo zilizoraruliwa. Waliripoti kwa Bosi wao ambapo Polisi walijulishwa kuhusu tukio hilo.

Polisi walipofika walikusanya mabaki ya mwili ule pamoja na nguo za marehemu zilizoraruliwa na kwa kutumia vidole vya marehemu yule waliweza kutambua kwamba mabaki yale ni ya nani. Kwa mujibu wa alama za vidole, waligundua kwamba mwili ule ulikuwa ni wa Nelson Oupa Chisale, baba wa watoto watatu.

Awali Chisale aliripotiwa kupotea siku tatu zilizopita, na waliomuona kwa mara ya mwisho walidai kumuona akiingia katika shamba hilo la Mark Scott-Crossley, ambapo hakuonekana tena akiwa hai.
Kesi hii ni mwaka 2004, iliyotokea huko nchini Afrika ya Kusini katika mji wa Phalaborwa, mji mdogo uliopo umbali wa kilometa 450 kaskazini magharibi mwa Johannesburg katika jimbo la Limpopo ambapo raia mmoja wa Kizungu aitwae Mark Scott-Crossley, pamoja na wafanyakazi wake wawili waliojulikana kwa majina ya Simon Mathebula na Richard Mathebula walishitakiwa kwa kosa la kuhusika na mauaji ya aliyekuwa mfanyakazi wake Nelson Chisale kwa kumtupa kwenye zizi la simba akiwa hai ambapo aliliwa na simba hao na kubaki mifupa.

Watuhumiwa Kizimbani............................

Mshitakiwa wa nne katika kesi hiyo Robert Mnisi aligeuka kuwa shahidi muhimu wa upande wa mashitaka katika kesi hiyo kwa makubaliano maalum kwamba aondolewe kwenye orodha ya washitakiwa.
Waliofikishwa mahakamani hapo ni Mark Scott-Crossley pamoja na wafanyakazi wake Simon Mathebula na Richard Mathabula. Katika hati ya mashitaka iliyosomwa hapo mahakamani ilielezwa kwamba mnamo Januari 31, 2004, Mark Scott-Crossley aliwaamuru wafanyakazi wake wampige na kumtesa Chisale ambapo walimshambulia kwa mapanga na kisha kumfunga kwenye mti. Baadae akishirikiana nao walimpakia kwenye gari na kwenda kumtupa kwenye zizi la simba akiwa hai ambapo aliliwa na simba hao na kubaki mifupa.

Awali washitakiwa hao walikana mashitaka, lakini wakati kesi hiyo inaanza kusikilizwa, mshitakiwa mmoja, Richard Mathebula alikiri kuhusika na mauaji hayo lakini alidai kwamba alikuwa anatekeleza amri ya bosi wake yaani Mark Scott-Crossley.

Hata hivyo baadae mshitakiwa Richard Mathebula kesi yake iliahirishwa kutokana na kuumwa kifua kikuu (TB), iliamuliwa kuwa atashitakiwa akiwa peke yake atakapopona. Kesi hii ilitikisa serikali ya ANC, na matamko mbalimbali yalitolewa kulaani mauaji hayo. Miongoni mwa matamko hayo yalikuwemo yale yaliyotolewa na chama cha wafanyakazi wa mashambani pamoja na kiongozi wa umoja wa vijana wa ANC.

"Tupo hapa ili kuhakikisha kuwa haki inatendeka." Alisema Abitha Malatji, kiongozi wa umoja huo kisha akaendelea…. "Tunataka wote wafungwe kifungo cha maisha na ijumlishwe na miaka 100. Lazima wote watatu waozee jela."

Naye waziri wa kazi wa nchi hiyo wa wakati huo Membathisi Mdladlana alilaani vikali mauaji hayo. Nalo shirikisho la wafanyakazi nchini humo nalo lililaani mauaji hayo na msemaji wa shirikisho hilo alisema kwamba mauaji hayo yanadhihirisha wamiliki wa mashamba nchini humo ambao wengi ni wazungu, wanawanyanyasa sana na kuwatendea vitendo vibaya wafanyakazi wao ambao wengi ni weusi kuliko hata ilivyokuwa wakati wa serikali ya kibaguzi.

Nje ya mahakama hiyo kulikuwa na maandamano ya wakazi wa eneo hilo wakiwa na mabango yaliyokuwa na ujumbe unaolaani mauaji hayo. Ulinzi nje na ndani ya Mahakama hiyo ulikuwa umeimarishwa kiasi cha kutosha kuhofia kutokea kwa fujo wakati wa kusikilizwa kwa kesi hiyo.

Kesi hii ilisikilizwa na Jaji mweusi aitwae George Maluleke ambapo wananchi wengi wa nchi hiyo walikuwa na imani kubwa juu yake kuwa atatenda haki. Ukweli ni kwamba bado kuna malalamiko mengi ya wananchi wengi weusi wa nchi hiyo ya kutokuwa na imani na Majaji wazungu kutokana na kuonekana kuendelea kuendesha kesi nyingi zinazowahusisha wazungu wakiwa bado wanafuata misingi ya kibaguzi.

Kesi hii ilikuwa kama pigo kwa jamii ya wazungu waliozoea kuwanyanyasa weusi na wasichukuliwe hatua miaka ya nyuma wakati serikali ya kibaguzi ikiwa madarakani, lakini tangu kupatikana kwa uhuru wa nchi hiyo na serikali ya ANC kushika madaraka, bado ile tabia ya wazungu kujiona wako juu ya weusi kwa kila kitu haijafutika vichwani mwao.

Hata kitendo cha Scott-Crossley kufikishwa mahakamani kwa kosa la kutuhumiwa kwa mauaji ya mtu mweusi kwa wazungu walio wengi waliliona jambo hilo kama kitu kisichowezekana.

Na hata wakati Scott-Crossley alipokuwa akifikishwa mahakamani hapo mara kwa mara kusikiliza kesi yake hakuonekana kujali wala kujuta na alikuwa akijiamini kupita kiasi, kama vile hakuna kilichotokea. Upande wa mashitaka katika kesi hiyo ulitakiwa kuthibitisha kama Mark Scott-Crossley aliwaamuru wafanyakazi wake wamuue Chisale au kama Chisale alikuwa hai wakati anatupwa ndani ya zizi la simba.

Kwa mujibu wa mfanyakazi wake mmoja wa shambani hapo aliyetajwa kwa jina la Robert Mnisi ambaye alikuwa ni mmoja wa watuhumiwa aliyegeuka kuwa shahidi muhimu kwa upande wa mashitaka katika kesi hiyo ambayo ilivuta hisia za watu wengi nchini humo, aliiambia mahakama kwamba, siku hiyo ya mauaji bosi wao Scott-Crossley alimpiga Chisale na kitako cha bunduki mpaka akapoteza fahamu kabla ya kumpakia kwenye gari (Pick up) ambapo waliondoka pamoja na wafanyakazi wenzie hadi kwenye zizi walipohifadhiwa simba weupe ambao ni adimu nchini humo na kumuamuru yeye na wenzie wamtupe Chisale ndani ya zizi hilo ili aliwe na simba hao.

"Dokta, mnyanyue (yaani Chisale) na umtupe huko ndani ya zizi la simba." Alisema Mnisi akimnukuu bosi wake Scott-Crossley.

Mnisi alidai kwamba wakati bosi wake anamuamrisha alikuwa amemuwekea bunduki kichwani ili kumtisha.

"Hey kama hutaki kutii amri yangu nitakuua, panda kwenye gari haraka usipoteze muda." Mnisi alimnukuu bosi wake Scott-Crossley wakati anamuamrisha kutekeleza amri yake.

Mnisi alidai pale mahakamani kwamba Chisale alikuwa hai wakati anatupwa ndani ya zizi hilo la Simba, kwani alimsikia akikoroma, kitu ambacho kilionyesha kwamba alikuwa hajakata roho. Naye mpwa wa marehemu Chisale Fetsang Jafta akitoa ushahidi wake pale mahakamani alisema kwamba, alilitambua fuvu la kichwa kirahisi kwamba ni la Chisale kwa sababu meno yake ya mbele yalikuwa na mwanya.

Hata hivyo dhamana ya kiasi cha paundi 30,000 alichopewa Mark Scott-Crossley kilitenguliwa baada ya kumshika shati shahidi mmoja katika kesi hiyo na kumtisha kwa maneno ndani ya mahakama, na hivyo kuendelea kukaa rumande wakati kesi yake inaendelea kusikilizwa. Awali Mark Scott-Crossley aliahidi kuilipa familia ya Chisale kiasi cha dola 6,300 kwa ajili ya kugharamia mazishi na dola 21,000 kwa ajili ya ujenzi wa nyumba ya familia hiyo na mshahara wa dola 210 kwa mwezi kwa miaka kumi, kama wataridhia atolewe gerezani. Pendekezo hilo lilikataliwa.

Mtaalamu wa serikali wa kuchunguza maiti Dr. Donald Mabunda alithibitisha kwamba Chisale alikuwa hai kabla ya kutupwa ndani ya zizi la simba ambapo alifariki baadae baada ya kushambuliwa na kuliwa na simba hao.

Lakini mtaalamu wa kuchunguza maiti wa kujitegemea Dr. Leon Wagner ambaye aliletwa na wakili wa Mark Scott-Crossley kuufanyia uchunguzi mwili huo ili kuondoa utata, akitoa ushahidi wake pale mahakamani alisema kwamba, Chisale alikwisha kufa hata kabla ya kutupwa ndani ya zizi la simba.

Wakili wa Simon Mathebula, Matthews Kekana, alikiri kwamba, ni kweli mteja wake alishiriki kumpiga Chisale na panga na baadae kumfunga kwenye mti lakini akimtetea alidai kwamba mteja wake alikuwa anatekeleza amri ya bosi wake, yaani Scott-Crossley. Naye wakili aliyekuwa akimtetea Scott-Crossley, Johann Engelbrecht aliiambia mahakama kwamba, mteja wake hakuhusika na mauaji ya Chisale, bali alishiriki tu kwenda kuutupa mwili huo baada ya kutishiwa kuuawa na mmoja wa wauaji wa Chisale.

Utetezi wa mtuhumiwa waibua mapya.............

Akitoa utetezi wake Scott-Crossley aliieleza mahakama kwa kirefu kwamba, alikuwa akihusihwa na tuhuma mbalimbali hapo kabla na mara nyingi zimekuwa zikimletea matatizo. Aliendelea kusema kwamba, siku ya tukio alifika katika shamba lao la familia majira ya mchana na kumkuta Simon Mathebula akiwa getini ambapo alionekana akiwa katika hali ya wasiwasi. Alipomwangalia vizuri aligundua kwamba alikuwa na matone ya damu katika mavazi yake.

Akidhani kwamba, kuna wawindaji haramu wamevamia eneo lake la kuwindia, alimwita Robert Mnisi, akiamini kwamba ni mtaalamu wa kupambana na majangili kwa sababu alikuwa ni dereva mahiri wa magari ya uwindaji. Hata hivyo alipofika katika nyumba wanayoishi wafanyakazi wa shamba lake, alimkuta Nelson Chisale akiwa amefungwa na waya katika mti, lakini binafsi hakufurahishwa na jambo lile.

Alipomchunguza Chisale aligundua kwamba, alikuwa na majeraha ya kukatwa na panga kichwani na shingoni. Alimuuliza kwamba amefuata nini pale shambani kwake, Chisale alimjibu kuwa amefuata vyombo vyake vya kupikia. Lakini yeye alimjibu kwamba hakuna kitu chochote alichoacha pale shambani kwake. Akiendelea kutoa utetezi wake Scott-Crossley, aliieleza mahakama kwamba alimtuma kijana wake wa kiume aliyekuwa na umri wa miaka 12 akamletee bunduki yake iliyokuwa ndani ya nyumba ambapo alimuonesha Chisale bunduki ile na kumuonya kuwa kile ndicho atakachokipata atakaporejea tena pale. Scott-Crossley alitoa maelezo yale akipinga maelezo ya Robert Mnisi kwamba alimshambulia Chisale na kitako cha bunduki kichwani.

Baadae alimpa mwanaye bunduki ile ili airejeshe ndani, kisha akawaleleza kina Mathebula washughulikie jambo lile kwa jinsi watakavyoona, kwa sababu hakuona kwamba ni busara kushughulika na jambo lile, halafu akaondoka zake. Scott-Crossley aliendelea kuileza mahakama kwamba kila mfanyakazi wake anajua ni nini majukumu yake, na kamwe hakuthubutu kutoa maelekezo kwa kina Mathebula kuwa wamkamate Nelson Chisale pindi atakaporejea pale shambani.

Aliporejea usiku pale shambani alielezwa na Mnisi kwamba kuna tatizo limetokea pale shambani na alipoangalia kwenye mti ambapo ndipo alipofungwa Chisale, hakuona mtu. Alipouliza alipo Chisale alielezwa na Richard Mathebula kwamba Chisale yupo bafuni na amekwishakufa.

Scott-Crossley alidai kustishwa na taarifa ile na alipoenda bafuni aliukuta mwili wa Chisale ukiwa umelala na alipopima mapigo ya moyo hakuona dalili za Chisale kuwa hai. Scott-Crossley alisema hayo kupinga maelezo ya Robert Mnisi kwamba, Chisale alikuwa hai wakati akitupwa kwenye zizi la simba. Alimgeukia Mnisi ambaye alisimama katika mlango wa bafuni na kumuuliza nini cha kufanya, Mnisi alimjibu huku akiwa amemkazia macho katika hali ya kuogofya na kumwambia, "kwa kifupi hakuna mtu aliyeuwa na hakuna mtu aliyekufa."

Na katika hali ya kuonesha kwamba, walikusudia kuficha mauaji yale, Mnisi alitoa mawazo mawili ya namna ya kuutupa mwili ule ili usionekane. Kwanza alisema mwili ule unaweza kutupwa kwenye ngema ya ufukweni mwa bahari (cliff) au kwenye shamba walipohifandhiwa simba. Mnisi alimweleza Scott-Crossley kwamba walimuuwa Chisale ili kumsaidia yeye na sasa ni zamu yake kuwasaidia kwenda kuutupa mwili ule, la sivyo watamuuwa yeye na mtoto wake pia.

Scott-Crossley aliendelea kuileza mahakama kwamba, Mnisi aliendelea kumtisha kwamba Chisale ni mtu ambaye ametokea katika jamii iliyopo jirani na shamba lake, kwa hiyo ajaribu kutafakari namna wanajamii watakavyokuja juu pindi watakapojua kwamba Chisale ameuawa katika shamba lake.

Na hapo ndipo alipojua kwamba yeye na familia yake watakuwa matatizoni iwapo jambo lile litakuja kujulikana na wanajamii hasa ikichukuliwa kwamba bado jamii ya watu weusi nchini humo wana vidonda vya kutawaliwa chini ya utawala wa ubaguzi wa rangi kwa miaka mingi. Wazo la kwenda kuutupa mwili wa Chisale kwenye ngema (cliff) tuliliona kuwa ni la hatari kwa sababu kama tungekutana na askari wa doria tukiwa na mwili ule ndani ya gari ungetuletea matatizo zaidi, hivyo tuliamua kwenda kwenye eneo walipohifadhiwa simba. Tulipofika katika eneo hilo, mimi, Mnisi, na Mathebula tulisaidiana kuushusha mwili ule katika gari na kuutupa ndani ya zizi la simba.

Alipoulizwa kama hakusikia sauti yoyote kutoka kwa Chisale kuashiria kwamba alikuwa hajakata roho, Scott-Crossley alikanusha kusikia sauti yoyote toka kwa Chisale wakati wakiutupa mwili wake ndani ya zizi la simba. Akimalizia kutoa utetezi wake Scott-Crossley aliiambia mahakama kwamba, aliishiwa na nguvu kabisa baada ya kujulishwa kwamba Chisale amekufa, hivyo baada ya kutishiwa maisha yake na ya mwanaye aliona ni vyema aungane nao ili kuondoa mwili ule mahali pale.

Hukumu ya kushangaza iliyoweka historia...........................

Kesi hiyo ambayo ilichukuwa takriban mwaka mmoja iliisha kusikilizwa kwake hapo mnamo April 28, 2005. Siku ya hukumu, mahakama ilifurika umati wa watu na kulizuka hali ya wasiwasi miongoni mwa wananchi. Hata hivyo hukumu ilichelewa kusomwa kwa nusu saa ili kuruhusu mtuhumiwa Scott-Crossley afunge ndoa na mwanamke mmoja aliyetajwa kwa jina la Simonetta Strydom ambaye alikutana na Scott-Crossley wakati alipomtembelea gerezani. Mume wa Simonetta Strydom alipoteza maisha katika mahakama hiyo.

Katika hukumu yake hakimu aliyesikiliza kesi hiyo George Maluleke alikubaliana na ushahidi uliotolewa na Robert Mnisi ambapo alimhukumu Scott-Crossley kifungo cha maisha na Simon Mathebula alihukumiwa kifungo cha miaka 15 jela.

Hukumu hiyo ilipokelewa kwa nderemo na vifijo na wakazi wa mji huo mdogo wa Phalaborwa na walimpongeza Jaji aliyehukumu kesi hiyo Mheshimiwa Jaji George Maluleke.

Akizungumzia hukumu hiyo mpwa wa Nelson Chisale, Fetsang Jafta alionekana kuridhishwa na hukumu hiyo.

Naye Mark Scott-Crossley akizungumzia hukumu hiyo alisema, "tulitegemea hukumu ya namna hii tangu awali, kwa hiyo sikushangazwa na hukumu hii. Nasikitika kwamba familia ya Chisale ilikataa pendekezo langu la kuwalipa fidia kwa kile kilichotokea. Si kwamba nilikuwa na lengo la kuwapa rushwa ili kuepuka hukumu hii, bali nilikuwa nawasikitikia kwa kupoteza mpendwa wao…. Hata hivyo tutakata rufaa kupinga hukumu hii na ninaamini haki itatendeka……."

Mshitakiwa mwingine katika kesi hiyo Richard Mathebula ambaye kesi yake iliahirishwa kusikilizwa kutokana na kuugua TB aliripotiwa kufariki akiwa katika Hospitali ya gereza la Nelspruit muda mfupi tu baada ya kesi yake kuanza kusikilizwa.

Hata hivyo mnamo Septemba 28, 2007, mahakama ya rufaa ya nchi hiyo ilitengua hukumu ya Scott-Crossley ya kifungo cha maisha na badala yake akahukumiwa kifungo cha miaka mitano jela, kwa madai kwamba upande wa mashitaka katika kesi hiyo ulishindwa kuthibitisha pasi na shaka kwamba Chisale alikuwa hai wakati anatupwa kwenye zizi la simba.

Mnamo Septemba 2008 Mark Scott-Crossley alitolewa kwa msamaha wa Parole ambapo aliungana na familia yake na kuanza maisha mapya uraiani. Msamaha huo ulizua malalamiko mengi miongoni mwa jamii ya watu weusi likiwemo shirikishao la wafanyakazi nchini humo.

 
Haya wadau kama kawaida ni Ijumaa nyingine tena nawaletea simulizi ya kesi hii iliyotokea nchini Afrika ya Kusini mwaka 2004..... Ni kesi ambayo ilivuta hisia za watu wengi nchini humo na nje ya nchi, lakini zaidi walikuwa ni raia weusi wa nchi hiyo ambao walishuhudia utawala wa kibaguzi kwa karne kadhaa kabla ya kupata uhuru na kuitishwa uchaguzi huru uliyoiweka serikali ya chama cha ANC madarakani..........

Hili lilikuwa ni tukio la kwanza la kibaguzi lililotokea baada ya kukomeshwa kwa ubaguzi wa rangi, na kesi hii iliwagawa wananchi wa nchi hiyo kwa misingi ya rangi zao kila upande ukiuangalia upande mwingine kama adui........ lakini serikali ya nchi hio ilimudu kutuliza hali hiyo na amani ikaendelea kuwepo.................

Ni kisa kizuri ambacho kinafundisha na kuhuzunisha pia...................

Tukutane juma lijalo.
 
Habari ndeeefu, afu mbona sioni uhusiano wake na jukwaa hili,au kuua mtu,kushtakiwa,kuliwa na simba n.k ni Mahusiano na mapenzi? Kizunguzungu ati!
 
yaani badala ya kusema anyongwe wanatengua hukumu na kumpa miaka mitano na wabebe laana ya huyo muuaji,jamani watu wengine si binadamu,embu angalia raisi wa syria nani ataniambia ni binadamu
 
Mmmh japokua sijui sheria lakini katika hali ya kawaida baada ya kukata rufaa mzungu kapendelewa aisee haiwezekani mauaji ya kikatili namna hiyo mtu afungwe miaka 5 then apate msamaha na kudunda mtaani bila shida!nchi za africa zote zinafanana!tunaabudu sana hawa watu weupe khaa!
 
Thanks Gusta,
Mh kwa kweli inaonyesha ni vipi mnyonge jhana haki!

Huyu mzungu anaonyesha jeuri ya kutaka kununua uhai wa mtu kwa mali, hovyo kabisa.
Nawapongeza ndugu kukataa ile offer.

But hukumu baada ya rufaa haikuwa haki nkabisaaaaaaa!
Huyu angefungwa maisha na ingekuwa fundisho kwa watu wengine wenye tabia kama yake.
 
Habari ndeeefu, afu mbona sioni uhusiano wake na jukwaa hili,au kuua mtu,kushtakiwa,kuliwa na simba n.k ni Mahusiano na mapenzi? Kizunguzungu ati!

Baba V huoni kama kulikuwa na mahusiano hapo?
Mtu na wafanyakazi wake wanaamua kuua mfanyakazi mwenzao wa zamani.

Mapenzi: muuaji amua kuoa katikati ya hukumu!
Hadi hapo hujaona kama hili ni jukwaa lake kabisa?
 
Una mnyanyasa mwafrika mwenzio wakati kampuni ni ya mzungu. Kuna yule mwanamuziki aliimba mzungu hapa alikuja kumalizia tu hawa weusi walishafanya kitendo kibaya cha kumkatakata chisale. (ukimpa mwafrika bunduki atauwa waafrika wenzake).
 
Hawa vimburu wana roho mbaya kama sura zao, ikiwa mfanyakazi aliyekuwa akipokea amri alihukumiwa miaka 15 iweje muuaji mkuu ahukumiwe miaka 5 na msamaha juu? sisi waafrika akili zetu fupi ka nywele zetu. Mtambuzi mjukuu wako TaiJike anakupa hi leo amekabwa mpaka penati maana yuko busy kuliko ulimi wa nyoka.
 
Last edited by a moderator:
Habari ndeeefu, afu mbona sioni uhusiano wake na jukwaa hili,au kuua mtu,kushtakiwa,kuliwa na simba n.k ni Mahusiano na mapenzi? Kizunguzungu ati!
Wewe ni mgeni wa hili jukwaa?? Mbona kuna mahusiano hapo kwenye hiyo kesi Baba V....??
Wenzako tuna zaidi ya nusu mwaka kila wiki tunapata habari hizi habari humu....!!
 
Last edited by a moderator:
Back
Top Bottom