esther mashiker
JF-Expert Member
- May 29, 2018
- 616
- 555
KUANZIA Mei Mosi mwaka huu, kila Mtanzania atatakiwa kusajili laini kwa alama za vidole kwa kutumia kitambulisho cha Taifa, ambako kila mtu atakuwa na laini moja kwa mtandao mmoja. Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Atashasta Nditiye alitoa ufafanuzi huo baada ya Mbunge wa Rombo, Joseph Selasini (Chadema) kuuliza swali bungeni jana.
Selasini alisema katika usajili huo wa Mei Mosi, amesikia kwamba naibu waziri alitangaza mtu anatakiwa kusajili kwa alama za vidole laini moja tu wakati katika baadhi ya maeneo baadhi ya mitandao haipatikani. Naibu Waziri Nditiye alisema ni kweli kuanzia Mei Mosi usajili wa alama za vidole utaanza, ambako kila mtu atasajili laini yake kwa mtandao mmoja.
Alisema alinukuliwa vibaya kwamba mtu anatakiwa kusajili laini moja tu, bali kinachotakiwa hapo ni kuhakikisha kwamba kila mtu anamiliki laini moja kwa mtandao mmoja. “Lengo la usajili huo ni kupunguza utitiri wa laini nyingi ambazo nyingine hazina tija na zinaongeza gharama kwa Watanzania,” alisema Nditiye. Alisema kwa wabunge watasajili laini zao wakiwa wanaendelea na shughuli za Bunge.
Alisema ataomba wamiliki wa kampuni za mitandao ya simu, kupeleka madawati yao hapo bungeni ili wabunge wasajili laini zao. Akijibu swali la msingi la Mbunge wa Viti Maalumu, Anna Gidirya (Chadema) aliyetaka kujua ni lini serikali itapeleka huduma hiyo katika vijiji vya Yorotonik, Endagwe, Hoshan na Endakiso katika Jimbo la Babati Vijijini, alisema serikali inaendelea kuratibu utekelezaji wa jitihada muhimu za kuwezesha maeneo yote nchini kukiwa na huduma za mawasiliano, sawa na maelekezo ya Sera ya Taifa ya Tehama ya mwaka 2016.
Kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote, serikali itavianisha vijiji hivyo kwa kuangalia ukubwa wa eneo, idadi ya wakazi wake na kufanya tathmini ya mahitaji halisi ya ruzuku kwa ajili ya kukisha huduma ya mawasiliano. Baada ya tathmini kukamilika, vijiji hivyo vitajumuishwa katika orodha ya miradi itakayoingia katika zabuni zinazotarajiwa kutangazwa katika mwaka wa fedha 2019/20.