mawazomgala
JF-Expert Member
- Sep 30, 2014
- 342
- 212
Ni Profesa John Thornton aliyekuja nchini kuonana na Rais JPM wakati wa sakata la makinikia.
Athibitisha msimamo wa tume ya makinikia kuwa ACACIA imekuwa na tabia ya kukwepa kodi Tanzania.
Asikitika kampuni hiyo kusababisha kuharibika kwa mahusiano ya kibiashara na serikali.
NA Mwandishi maalum
MWENYEKITI Mtendaji wa Kampuni ya Barrick Gold Corporation, Profesa John Thornton, amesema kampuni yao ya Acacia Mining inayofanya kazi Tanzania, haijawahi kulipa kodi ya mapato (Coporate Income Tax) kwa serikali ya Tanzania kutokana na shughuli za uchimbaji wa dhahabu nchini suala ambalo limeathiri uhusiano baina ya kampuni hiyo na serikali.
Kauli hiyo ya Prof. Thornton inaleta matumaini kwa serikali ya Tanzania katika majadiliano yanayoendelea baina yake na Barrick juu ya tozo na kodi ambazo wanatakiwa kuilipa serikali kutokana na usafirishaji wa makinikia kwa miaka 19 tangu Acacia kuanza shughuli zake za uchimbaji nchini.
Tayari kampuni ya Barrick imeshakubali kulipa Tanzania dola milioni 300 kama utayari wa kushirikiana wakati majadiliano yakiendelea baina ya pande hizo.
Kwa mwaka mmoja na nusu sasa serikali imezuia usafirishaji wa makinikia (gold concentrate) nje ya nchi suala ambalo limeathiri utendaji kazi wa kampuni ya Acacia nchini kwa kiasi kikubwa pamoja na kusababisha kuporomoka kwa hisa zake katika soko la hisa la London.
Akizungumza katika mahojiano na The Globe and Mail mwanzoni mwa mwezi Septemba mwaka huu alisema Migodi ya Barrick inayomilikiwa na Acacia kwa asilimia 64 nchini Tanzania “hajalipa kodi ya mapato kwa Tanzania” zaidi ya kulipa mirabaha na kodi za mishahara tu.
Hata hivyo si Barrick wala Thornton ambao wamekanusha kuhusu ukweli wa kauli hiyo zaidi ya Barrick kujaribu kufafanua kuwa wanafikiri kuwa Mwenyekiti huyo alitia chumvi wakati akimaanisha kuwa kiasi kilicholipwa kwa serikali ya Tanzania ni kidogo sana ikilinganishwa na mapato ya Acacia katika shughuli za uchimbaji dhahabu nchini.
Kauli hiyo imeleta mgongano baina ya Barrick na Acacia baada ya Acacia kuipinga na kusema wanashangazwa na taarifa hiyo isiyo sahihi ya Thornton.
Kwa mujibu wa Globe, Acacia ikiwa imetolewa kwenye mazungumzo kati ya serikali ya Tanzania na Barrick, mafaili kwaajili ya kuunda mkataba mpya yamekabidhiwa kwa Kevin Thomson ambaye Mtendaji Mwandamizi wa Mikakati wa Barrick.
Kampuni ya Acacia iliingia katika kashfa ya usafirishaji wa makinikia na kuisababishia serikali hasara ya mabilioni ya fedha kwa mujibu wa tume ya uchunguzi iliyoundwa na Rais John Magufuli kuchunguza ukweli wa kiasi na thamani ya madini yaliyopo katika makontena ya makinikia yaliyozuiliwa.
Kamati hiyo ilibaini kuwepo kwa viwango vingi vya juu vya dhahabu ndani ya makinikia yaliyofanyiwa uchunguzi. Viwango hivyo ni kati ya 671 g/t hadi 2375 g/t, sawa na wastani wa 1400 g/t.
“Wastani huo ni sawa na 28 kg za dhababu kwenye kontena moja lenye tani 20 za makinikia. Hivyo, kwenye makontena 277 ya makinikia yaliyozuiliwa Bandari ya Dar es Salaam na Bandari Kavu yatakuwa na wastani wa tani 7.8 za dhahabu yenye thamani ya TZS bilioni 676 (USD 307,292,720),” ilisema taarifa hiyo iliyotolewa Mei mwaka jana na kuongeza;
“Aidha, kwa kutumia kiwango cha juu kilichopimwa kwenye kontena moja lenye shehena ya tani 20 za makinikia (47.5 kg), kiasi cha dhahabu katika makontena 277 kitakuwa 13,157.5 kg ambazo thamani yake ni Sh trilioni 1.146 (USD 521,300,150).
“Hivyo, thamani ya dhahabu katika makontena 277 yaliyozuiliwa bandarini ni kati ya TZS bilioni 676 na bilioni 1,147.”
Kutokana na taarifa hiyo ya Kamati ya Mkinikia, Prof. Thornton alikutana na Rais Magufuli Juni 14 2017 na kufanya mazungumzo ambapo aliahidi kuwa Barrick ipo tayari kufanya majadiliano na serikali ili kulipa fedha ambazo Tanzania imezipoteza kutokana na kuendesha shughuli zake hapa nchini.
Julai 31 2017 majadiliano baina ya pande hizo mbili yalianza huku upande wa Tanzania ukiongozwa na Waziri wa Katiba na Sheria Profesa Palamagamba Kabudi na baadae Barrick ikakubali kuilipa Tanzania Dola za Marekani Milioni 300 sawa na Sh bilioni 600.
Hatua hiyo ilifikiwa Oktoba mwaka jana wakati kamati mbili za majadiliano ile ya Tanzania na ya Barrick zilipokuwa zikiwasilisha ripoti ya mazungumzo yao kwa Rais Magufuli ambapo ikiwa ni mara yake ya pili kukutana na Rais Prof. Thornton alitoa salamu za shukrani na kusema kampuni yao italipa kiasi cha dola za Marekani milioni 300 kama njia ya kuonesha utayari wake na uaminifu kwa Serikali ya Tanzania.
Thornton alisema licha ya kuwa kwa sehemu kubwa wameafikiana masuala mengi, lakini suala ya tozo ya malimbikizo ya kodi bado hawajakubaliana kikamilifu na kwamba wameliweka kiporo wakati akiwasiliana na wanahisa wengine ili kufikia makubaliano zaidi.
Kauli yake ya sasa inaleta matumaini makubwa kwa serikali ya Tanzania kuwa huenda kiasi cha zaidi ya Trilioni 400 kilichokadiriwa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), kikalipwa na kampuni hiyo.
Baada ya Globe kuchapisha kauli hiyo ya Thornton, Mkurugenzi Mtendaji wa Acacia, Peter Geleta aliibuka na kukanusha taarifa hiyo akisema kuwa si taarifa sahihi.
“Tulishangazwa sana na taarifa zisizo sahihi za Thornton na tumetaka Barrick watoe ufafanuzi,” aliiambia Globe.
Geleta alitoa ufafanuzi kwa wafanyakazi wake kupitia tangazo la ndani la Septemba 18 mwaka huu kuwa Acacia na kampuni zake tanzu umelipa dola bilioni 1 kama kodi na mrabaha kwa serikali kwa miaka zaidi ya 15.
Alisema kwa nusu ya mwaka huu wamelipa kodi ya mapato ya dola milioni 23.3 na mwaka jana dola milioni 34.6 na kwamba kwa miaka 15 wamelipa jumla ya dola milioni 140 kama kodi.