Kibanda - Sio Ufisadi, Ni Urais 2015

RaiaMbishi

JF-Expert Member
Jan 18, 2012
252
125
Mwaka 2009, Kibanda wakati ule akiwa mhariri mtendaji wa gazeti la Tanzania Daima alianzisha mfululizo wa makala zenye kichwa kisemacho - Tuendako: Sio Ufisadi, Ni Urais 2015. Katika makala hizo, Kibanda alishambulia sana mtandao uliomwingiza Kikwete madarakani. Makala hizi zilileta mtikisiko mkubwa sana kwa walengwa hali ambayo iliweka maisha ya Kibanda hatarini lakini kilichokuwa kinamlinda Kibanda ni uwepo wake kwenye gazeti linalomilikiwa na mmoja wa viongozi wa Chadema (Freeman Mbowe, suala ambalo lilifanya iwe vigumu kwa mtu yoyote wa CCM kumdhuru Kibanda bila ya kuchafua hali ya hewa ambatyo ingepelekea CCM kudhoofika na Chadema kuzidi kupanda chati.

Ni makala hizi ndio zimemletea matatizo, na nina uhakika kwamba kwa vile vile mwenyezi mungu amemuokoa na umauti, siku atakapopata nafuu na kuamua kufunguka, atakuja kuthibitisha uhusiano wa makala zake hizi na janga lililompata. Ni muhimu kwa vyombo vya usalama kuunganisha makala hizi na ujasusi aliofanyiwa Kibanda, la sivyo itakuwa ni michezo ya kuigiza. Zifuatazo ni mfululizo wa makala husika - msomaji, kuwa makini zaidi na sehemu zilizopigwa rangi nyekundu.
-------------------------------------------------------------------------------------

Makala ya Kwanza


Tuendako: Si ufisadi, ni urais 2015

Absalom Kibanda

Jumatano, 8 Aprili 2009
MAMBO ya ajabu na yanayostaajabisha yameanza kujitokeza katika nchi hii, katika siku na miezi ya hivi karibuni, kiasi cha kusababisha kuzuka kwa maswali mengi yasiyo na majibu.

Matukio ya hivi karibuni kabisa kisiasa yanayojumuisha kauli za kitatanishi zilizotolewa na wenyeviti wastaafu wa mikoa wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na kabla ya hapo matamshi makali ya Makamu Mwenyekiti mstaafu wa chama hicho tawala, John Malecela, yanaonyesha dhahiri kwamba, kuna kasoro kubwa katika mwenendo mzima wa kiuongozi hapa nchini.

Kwa maneno rahisi kabisa, kitendo cha wazee hao wa CCM kujitokeza hadharani na kuchomeka hoja za kumtetea na kumsafishia njia Rais Jakaya Kikwete wakati wa kinyang'anyiro cha urais mwakani, ni kielelezo cha wazi cha kuwapo kwa tatizo kubwa zaidi nyuma ya kauli za wazee hao.

Ingawa ni kweli kwamba kauli za namna hii za kumsafishia njia Kikwete zilishapata kutolewa kabla ya hapo na watu wengine kadhaa wazito, akiwamo mfanyabiashara maarufu, Reginald Mengi na Waziri Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye, bado kuibuka kwake upya na tena kwa nguvu kubwa kunaweza kuashiria dalili za kuwapo kwa hali ya kukata tamaa katika jamii.

Ni jambo la bahati mbaya sana kwamba, wazee hawa wa CCM na watu wengine mashuhuri wa kabla yao na pengine wengine watakaoibuka baada yao, wanajitokeza leo, wakati dalili zimeshaanza kujionyesha wazi kwamba, ile hatari iliyokuwa ikimnyemelea Kikwete miezi au zaidi ya mwaka mmoja uliopita ya kumfanya awe rais wa kwanza ndani ya CCM kuongoza kwa muhula mmoja tu, ikiwa imeshaanza kutoweka.

Wasomaji wa safu hii ni mashahidi wazuri kwamba, miezi kadhaa kabla ya azimio hilo lisilo rasmi la kuibuka kwa kutumwa kwa wazee hao, limekuja wakati tayari nikiwa mmoja miongoni mwa wadadisi wa mambo ambao nilieleza bayana kuhusu uhakika wa Kikwete kushinda kwa mara nyingine tena urais kwa muhula wa pili wakati wa Uchaguzi Mkuu wa Oktoba mwakani.

Hata hivyo, napenda kueleza mapema kabisa kwamba, matukio yaliyosababisha kufunguka upya kwa njia ya Kikwete kuendelea na awamu yake ya pili ya utawala wake hakujasababishwa au kuchagizwa kwa namna yoyote ile na hatua zozote makini za kimaamuzi au za kiutawala alizochukua, bali matakwa na mahitaji, kama si nusura ya kimazingira yanayolikabili taifa kwa hivi sasa.

Kwa upande mwingine, naweza kusema pasipo shaka kwamba, nusura ya Kikwete ya kuondoka madarakani mwaka 2010 kwa kiwango kikubwa imechagizwa na kuyeyuka kwa namna isiyo na maelezo fasaha kwa upinzani dhidi yake ndani ya chama chake na nje ya CCM.

Wafuatiliaji wazuri wa siasa za nchi hii wanaweza wakawa mashahidi wazuri kwamba, kusambaratika kwa genge haramu la mtandao ndani ya CCM ambalo lilipigana kufa na kupona kuhakikisha Kikwete anashinda uteuzi na hatimaye urais mwaka 2005 likicheza rafu mbaya na za hatari kwa kiwango cha kutishia mustakabali wa umoja na mshikamano wetu kitaifa, ilikuwa ni dalili ya kwanza iliyoanza pole pole kumjengea msingi wa ushindi kiongozi huyo.

Msambaratiko huu ambao leo hii umewaweka katika kundi moja wana mtandao wa aina ya Edward Lowassa, Andrew Chenge, Rostam Aziz, Nazir Karamagi na wenzao wengine huku ukiwatenganisha na kuwakosanisha maswahiba wao wa zama zile wa aina ya, Samuel Sitta na Bernard Membe, kwa kiasi kikubwa ulimtenganisha Rais Kikwete na madhambi yote ya mtandao, ambao ulijenga maadui wengi ndani na nje ya CCM.

Kumeguka kwa genge hilo kulisababisha wana CCM wengine ambao awali hawakuwa sehemu ya wanamtandao kujikuta ama wakishikamana na kundi la kwanza na wengine wakajikuta wakiungana na kuunda mtandao mpya na kundi jingine jipya.

Katika mparaganyiko huu, Lowassa, Rostam, Karamagi na wenzao wakajikuta wakiwa majeruhi wa kwanza wa hali hii ambayo kwa upande mwingine iliwapandisha chati na kuwajengea ushujaa wana mtandao wenzao wachache wa aina ya Sitta na Membe.

Ufa huu wa kwanza uliomuacha Kikwete akiwa shuhuda, uliwaunganisha katika kundi moja kina Sitta na Membe na wanasiasa wenzao kadhaa ndani ya CCM wa aina ya Dk. Harrison Mwakyembe, Anne Kilango Malecela, William Shellukindo, Lucas Selellii, Christopher ole Sendeka na wenzao wengine wengi ambao leo wanajitambulisha na kutambulika kijamii kuwa wanaharakati wa vita dhidi ya ufisadi.

Kuundwa kwa kundi hili jipya ambalo lilijipatia nguvu kubwa kuanzia Februari mwaka jana kulifanikisha azima ya kiharakati ya CCM ya kuzima mapambano dhidi ya ufisadi yaliyokuwa yameanzishwa na kambi ya upinzani ndani ya Bunge yaliyokuwa yakiongozwa na kina Hamad Rashid Mohammed, Wilbrod Slaa, Zitto Kabwe, Halima Mdee, Habib Mnyaa na wenzao wengine wengi.

Kuibuka kwa mwelekeo huo mpya wa mambo ndiko ambako wakati fulani kupitia katika safu hii nilikuelezea kuwa ni hatua mahususi ya makada wa CCM kuiteka nyara vita takatifu ya ufisadi kutoka katika himaya ya wapinzani na kuifanya ichukue sura tofauti na iliyoiweka chini ya himaya ya chama hicho tawala. Hii ilikuwa ni salama ya tatu ya Rais Kikwete.

Tukio la hivi majuzi la Serikali ya Marekani kumpa tuzo ya mwanamke jasiri, Mama Kilango, kwa namna alivyoweza kukabiliana na vitendo vya ufisadi, ni ushahidi mmojawapo na wa wazi wa namna CCM ilivyofanikiwa kuizima ndoto ya mafanikio ya kambi ya upinzani waliyojijengea miaka miwili ya mwanzo ya utawala wa Kikwete, ambayo ilianza kutoa dalili za kumfanya aonekane kuwa ni rais wa awamu moja tu.

Mafanikio haya ya awali ya kuwapora wapinzani turufu moja nzuri ya kisiasa dhidi ya chama tawala ndani ya Bunge, iliwawezesha makada mashujaa wa ndani ya CCM waanze kuimarisha msingi imara wa kujipanga kwa ajili ya safari ya kumrithi Rais Kikwete wakati atakapomaliza muhula wake wa uongozi.

Mtandao huu mpya wa ‘mashujaa' wa CCM, kwa umakini mkubwa walifanikisha azima yao ya kumtenganisha kikazi na kiharakati Kikwete na maswahiba wake wakuu wawili, Lowassa na Rostam, wakianza kwa kujijengea uhalali wa kimaadili machoni mwa wanachama wenzao wa chama tawala na kisha jamii kwa ujumla, kabla ya kubuni mbinu mbalimbali za kulainisha moyo wa rais na watendaji wengine wa serikali uwaelekee wao. Hii ilikuwa hatua ya nne ya kumjengea JK uhalali ulioanza kutokomea.

Mtandao huo mpya wa mashujaa wa ufisadi, ambao ulijumuisha watu waliokuwa wakijua mbinu za chini chini za kujijenga na kujilinda wakati wanapotaka kufanikisha ajenda zao za kimamlaka, ulilazimika kuongeza juhudi za kujiweka karibu zaidi ya Kikwete na serikali yake, baada ya kuanza kuona kuwapo kwa dalili za tishio la wazi na la siri kutoka katika kundi la majeruhi wa kisiasa wa ndani ya CCM, ambao kwa bahati mbaya walikuwa wakionekana kuwa ni watu wenye nguvu kubwa za kiuchumi.

Huku wakitambua ukweli huo, ajenda dhidi ya ufisadi iliyobebwa juu juu na kina Sitta, Membe, Kilango, Sendeka, Mwakyembe na wenzao ikajikuta ikipata baraka za kuungwa mkono waziwazi na mfanyabiashara maarufu anayemiliki mtandao wa vyombo vya habari, Reginald Mengi.

Ubia huo wa kiajenda kati ya mashujaa hao wa ufisadi wa ndani ya Bunge na mfanyabiashara huyo ulikuwa ni pigo baya zaidi kwa kundi la majeruhi wa vita ya ufisadi, kutokana na nguvu kubwa ya kihabari waliyoanza kujijengea kina Sitta, Kilango, Sendeka, Sellelii na wenzao wengine wa mtandao huo mpya.

Wafuatiliaji wazuri wa habari na makala katika magazeti, televisheni na redio wanaweza wakawa mashahidi wazuri wa namna habari zinazowahusu kina Sitta, Sendeka, Kilango, Shellukindo, Sellelii na wenzao wengine wengi zilivyoanza kuripotiwa kwa namna ya kuwabainisha kuwa wanaharakati wazuri wa vita dhidi ya ufisadi.

Wakati hayo yakiendelea, kwa bahati mbaya sana, vita takatifu ya ufisadi iliyoanzia katika vyombo vya habari kabla ya kuingizwa bungeni na wabunge wa upinzani kabla ya kutekwa nyara na kupindishwa na ‘mashujaa' hao wa CCM ikaanza taratibu kugeuka na kuchukua mkondo tofauti kabisa na ule uliolenga kuubomoa kabisa mfumo wa kifisadi uliojistawisha ndani ya serikali kupitia katika chama tawala.

Haraka haraka, mashujaa hao feki wa CCM wakafanikiwa kukisafisha chama chao na kumuepusha kabisa rais na viongozi wengine wa juu wa chama hicho katika tuhuma za kifisadi na kulifanya suala hilo lianze kuonekana kuwa ni matendo binafsi ya kikundi cha watu wachache walafi ambao waliamua kutumia fursa zao za kimamlaka kujinufaisha wao wenyewe.

Hali ilipofikia hatua hiyo, ndipo ghafla taifa likashuhudia watuhumiwa kadhaa wakifikishwa mahakamani wakihusishwa na vitendo vya ufisadi kupitia kashfa ya wizi wa fedha katika Akaunti ya Malipo ya Madeni ya Nje (EPA), Alex Stewarts, na kisha Richmond. Hiyo ilikuwa hatua ya tano iliyosaidia kuisafisha nyota ya Kikwete iliyoanza kufifia.

Wakati haya yote yakitendeka, leo hii taratibu, siri imeanza kufichuka kwamba, nyuma ya pazia, baadhi au majemedari wote wa mtandao mpya wa vita dhidi ya ufisadi, walikuwa wameamua kuyatumia mapambano haya kama mbinu mahususi ya kuzima kile kilichoanza kuonekana kuwa ni dalili za wazi za kumuandaa Lowassa kuwa mrithi wa Kikwete ama mwaka 2010 au 2015.

Kufichuka kwa siri hii ambayo wanasiasa wengi wa ndani ya CCM hawataki kuiweka wazi, kumesababisha ghafla majna ya watu wanaotajwa kuingia katika orodha hiyo ya urais kuongezeka kila kukicha, ikiwataja Membe, Masha, Mengi, Lowassa, Nchimbi na wengine wengi ama kwa kupotosha lengo na wakati mwingine kubainisha ukweli.

Tukutane wiki ijayo wakati tutakapoanza kufichua siri hizi hatua kwa hatua.
-----------------------------------------------------------------
makala hii pia inapatikana katika tovuti ifuatayo:

Si ufisadi, ni urais 2015
 
Makala ya Pili

Tuendako: Si ufisadi, ni urais 2015 (2)

Absalom Kibanda
Jumatano, Aprili 15, 2009
HII ni wiki ya pili nikiwa katika mada hii inayohusu tafsiri yangu binafsi na kimsingi mtazamo wangu kuhusu mwenendo wa masuala ya siasa katika nchi hii.
Nilianza kuandika mada hii wiki iliyopita, nikieleza japo kwa muhtasari - mambo hasa yaliyokuwa yameanza kujitokeza nyuma ya pazia la vita dhidi ya ufisadi iliyoanza miaka miwili au mitatu iliyopita. Vita hiyo ina lengo jema la kukabiliana na vitendo vinavyojumuisha ukiukwaji wa maadili ya kimadaraka ndani ya serikali, kupitia katika mtandao mahususi ndani ya chama tawala.

Makala yangu ya wiki iliyopita iliibua maswali, kebehi, furaha, hasira na changamoto kutoka kwa watu wa karibu na wa kutoka miongoni mwa watu na wadadisi wanaowakilisha makundi mbalimbali ya kijamii, kisiasa na kiuchumi.

Mgawanyiko huo wa kimtazamo ulikuwa mkali zaidi miongoni mwa makada wa makundi mbalimbali ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), kutokana na namna ilivyowagusa kwa namna ya kuwaumiza, kuwaridhisha, kuwaogopesha na wakati mwingine kutishia mustakabali wa kimakundi ndani ya chama hicho tawala.
Pamoja na kupokea changamoto zenye miguso inayotofautiana na kukinzana, bado ni ukweli kwamba mambo yote haya yalinitia hamasa zaidi kuendelea kuwaandikia Watanzania wenzangu wanaofuatilia mwenendo wa mambo haya, kupata fursa ya kuzifungua bongo zao na kupima kwa makini zaidi kitu hasa kilichokuwa kikiendelea katika nchi yetu hii.

Mmoja wa watu wa mwanzo kuwasiliana nami na kuijadili makala yangu alikuwa mwanahabari mwenzangu na rafiki yangu wa siku nyingi. Hivi sasa maandishi yake na kazi za kihabari anazozifanya zimemfanya ajipambanue kimatendo kuwa mwanaharakati mkubwa wa vita dhidi ya ufisadi. Mwahabari huyo ambaye msimamo wake dhidi ya ufisadi si wa kutiliwa shaka hata kidogo, alinieleza bayana jinsi anavyosumbuliwa na hoja zangu zilizokuwa zikionyesha dhahiri kutofurahishwa na uamuzi wangu wa kuukosoa waziwazi msimamo wa baadhi ya wanasiasa wa ndani ya CCM - ambao katika siku za hivi karibuni wamejipambanua kuwa watu walio mstari wa mbele katika vita dhidi ya ufisadi.

Kwa maneno yake mwenyewe, pamoja na kukubaliana na msingi wa hoja yangu, mwanahabari mwenzangu huyo aliniasa kuachana na hoja hiyo, kwani ingeweza kudumaza na kufisha vita takatifu ya ufisadi ambayo kila mwananchi mzalendo alipaswa kuiunga mkono. Katika maelezo yake, mwahabari huyo alikiri kukubaliana na ukweli kwamba msimamo wa kikundi kidogo cha wabunge wa CCM ‘waliojitoa mhanga' kuupiga ufisadi, ulichagizwa kwanza na matakwa yao ya kimakundi ndani ya chama hicho tawala na malengo yao ya kisiasa ya siku zijazo na si uchungu walio nao kwa nchi yao.

Mwanahabari alikwenda mbele zaidi na kuwaita wanasiasa hao wanaharakati wa vita ya ufisadi kuwa ni mamluki au askari wa kukodiwa katika vita takatifu. Malengo ya msingi ya mamluki hayafanani kwa namna yoyote ile na wanaharakati halisi na wa kweli wa vita ya ufisadi. Na hao si wengine bali ni wanasiasa wachache wa vyama vya upinzani na wanahabari wenye mawazo huru na ya kizalendo.

Mtu mwingine aliyewasiliana nami na kujadili hoja hiyo aliniomba sana nifanye kila ninaloweza kuwalinda baadhi ya wanasiasa wa kundi hilo, akisema - japo walikuwa wakifanya hivyo kwa sababu tu ya kujitafutia umaarufu wao binafsi - bado kwa kufanya kwao hivyo angalau walisababisha baadhi ya mambo kubadilika na tatizo la ufisadi kuanza kupungua serikalini.

Lakini msomaji wa tatu wa ile makala yangu alitofautiana na hao wawili na hata mimi binafsi. Alikwenda mbele zaidi na kuuponda mtazamo wangu akisema - tena kwa kujiamini - kwamba makala yangu ilikuwa ikijaribu kuwatetea mafisadi waliolitafuna taifa hili kwa miaka mingi. Binafsi baada ya kukaa chini na kutafakari changamoto hizo tatu na nyingine nyingi nilizotumiwa kwa njia moja au nyingine, nilijikuta nikilazimika kuzikataa na kuendelea na uamuzi wangu wa kuwaeleza Watanzania kile kilichokuwa kikitokea katika taifa hili hivi sasa.

Wiki iliyopita nilihitimisha makala yangu kwa kuyataja baadhi ya majina ya watu yaliyoanza kutajwatajwa na kuhusishwa ama na urais kwa kupitia CCM au nje ya chama hicho tawala kwa ajili ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 au 2015. Awali, kabla sijafikia hatua hiyo nilieleza mapema kwamba kwa hali ilipofikia sasa, kwa kiwango kikubwa (si kiwango chote), kulikuwa na nafasi ndogo kwa mtu mwingine kutoka ndani ya CCM kupata fursa ya kumng'oa Kikwete katika urais wake mwaka ujao.

Ukweli kuhusu hali hiyo ya sasa ndiyo ambayo kwa hakika iliwafanya wazee kadhaa wa CCM kwa mafungu na kwa wakati tofauti wajikute wakianza kujitokeza sasa na kujifanya wakianza kumuunga mkono Kikwete, hata kufikia hatua ya kusema eti alikuwa amefanikiwa kusimamia ipasavyo Ilani ya Uchaguzi ya chama hicho.

Ni jambo la wazi kwamba baadhi ya wazee hao au wote walifikia hatua ya kusema hivyo si kwa sababu walikuwa wakiridhishwa na namna Kikwete alivyokuwa akiiingoza serikali, la hasha, bali kutokana na matakwa ya sasa ya kimazingira na mustakabali mwema wa chama chao katika siku za usoni.

Watu wanaojua vyema siasa za kimakundi ndani ya CCM ni mashahidi wazuri kwamba, baadhi ya wazee hao ambao leo hii wamekuwa wakijidai kumuunga mkono Kikwete ndiyo hao hao, katika vikao visivyo rasmi vya majumbani mwao na katika vijiwe vyao, wamekuwa mstari wa mbele kueleza kukerwa kwake na namna serikali na hususan rais mwenyewe anavyoiendesha nchi.

Lakini kikubwa zaidi kinachoweza kuzusha maswali mengi, ni kitendo cha wazee hawa hawa ambao leo wanajifanya wakiwa mstari wa mbele kumtetea Kikwete, hata kumpa sifa za kuwa jemedari wa vita dhidi ya ufisadi kuwa na rekodi ya kufanya kila linalowezekana kwa maneno na vitendo vya kumtenganisha kabisa kiongozi huyo na kundi la makomredi zake ambao kwa namna moja au nyingine ndiyo waliokuwa nyuma ya ajenda ya sera, mwelekeo na hata uandishi wa ilani ya uchaguzi iliyomwingiza madarakani zaidi ya miaka mitatu iliyopita. Huu ni unafiki wa hatari wa siasa za ndani ya CCM.

Kwa hakika kikundi hiki cha wanasiasa wanaojifanya kuwa wanaharakati wa vita ya ufisadi, ndiyo ambao baadhi yao miaka miwili tu iliyopita walikuwa wameshaanza kuhaha wakipita mitaani na kuwahamasisha wapinzani wajipange sawasawa kwa ajili ya kuwasaidia kumng'oa Kikwete wakati wa uchaguzi mkuu wa 2010.

Aina hii ya wana-CCM ndiyo ambao katika mazingira ya kushangaza wakati huo walikuwa wakihimiza umoja, mshikamano, ushirikiano na ikibidi muungano wa vyama vya upinzani na baadhi yao wakafikia hatua ya kujaribu kujenga mazingira ya kuviunganisha vyama vya CUF na CHADEMA, eti ili viweze kusimamisha mgombea mmoja bora wa urais mwaka 2010.
Kama hiyo haitoshi, wanasiasa hawa wa CCM na wafadhili wao kadhaa wafanyabiashara, wakiwamo watu wazito kabisa walifikia hatua kuviunga mkono vyama vya upinzani katika harakati za kusaka ubunge wakati wa chaguzi ndogo, Kiteto, Tarime na baadaye Mbeya Vijijini. Baadhi ya wanasiasa hao wa CCM wakiwamo wabunge, wajumbe wa Halmashauri Kuu na si ajabu Kamati Kuu (CC), walifikia hatua ya kushiriki katika mikakati ya ushindi ya vyama vya upinzani na wengine wakachangia hata fedha, kwa kiwango cha kuonyesha namna walivyokuwa na uzalendo kwa taifa lao. Kwa hakika hawa ni matapeli wa kisiasa.

Watu tunaowajua vyema wanasiasa hawa, tunaweza kusema pasipo shaka kwamba, wengi miongoni mwa wanasiasa hawa ambao leo wanajibandika ubia na Kikwete nyuma ya pazia la ufisadi, ndiyo ambao muda si mrefu uliopita walikuwa wakijaribu kujenga ushawishi ambao ungewawezesha wanasiasa wenzao wa ndani ya CCM wa aina ya Profesa Mark Mwandosya kuchukua fomu za kukabiliana na Kikwete mwakani na si kusubiri hadi mwaka 2015.

Kwa maneno yao wenyewe wanasiasa hawa, waliopokuwa wakiulizwa ni kwa nini basi walikuwa wamefikia hatua hiyo ya kumuona rais wao wa CCM kuwa ni kutawala katika kipindi kimoja, majibu waliyokuwa wakiyatoa yalikuwa rahisi kabisa; ameshindwa kazi.

Baada ya ajenda zao hizo kuanza kuonekana si chochote si lolote ndani ya chama chao na kisha kuonekana zikisaidia kuvijenga vyama vya upinzani ambavyo vilishaanza kupanda majukwaani na kufichua uoza wa kutisha ndani ya CCM na miongoni mwa viongozi wa serikali, vinyonga hawa wa kisiasa kwa ustadi mkubwa wakaamua kujitafutia uhalali mpya ndani ya chama chao.

Wakati wakianza kujitafutia uhalali wa kisiasa, kiuchumi na kimadaraka ndani ya chama chao, wakabaini kwamba juhudi zao hizo zilikuwa haziwezi kamwe kufanikiwa wakati wanasiasa wa aina ya Edward Lowassa, Rostam Aziz, Yussuf Makamba na Nazir Karamagi wakiwa bado na nafasi kubwa kimamlaka ndani ya chama hicho.

Zilipoibuka hoja za Buzwagi, Richmond na EPA ndani na nje ya Bunge na kugeuka kuwa ajenda dhidi ya CCM, zikiratibiwa na vyombo vya habari na wanasiasa wa kambi ya upinzani, kundi hilo la mamluki wa kisiasa wa ndani ya CCM, mara moja wakauona mwanya wa wazi wa kuanza kutimizwa kwa malengo yao ya kisiasa. Huku wakijua kile wanachokitaka, wakapata uhalali wa kuwashughulikia ipasavyo wabaya wao wote wa kisiasa, lengo lao la awali likiwa ni kumfikia hata Rais Kikwete mwenyewe kabla ya mipango yao hiyo kuvurugwa kiufundi na mtandao wa kiusalama unaomzingira rais.

Walipobaini kwamba wamekwama kumfikia rais, haraka haraka wakatafuta kufanya naye ubia wa kimkakati, hatua ambayo kwa bahati njema, katika hatua za mwanzo, Kikwete mwenye akaonyesha dhahiri kuungana na kundi hilo. Hatua hii ya Kikwete kuungana na kundi hili lililianza kujijenga ndani ya Bunge na nje na miongoni mwa makada viongozi na wafanyabiashara wa chama hicho tawala, ikalipa mwanya kundi hilo kuanza kujipanga upya kwa ajili ya ajenda mpya ya kisiasa ya siku zijazo.

Katika hali ya ustadi mkubwa, wanasiasa wawili wa kundi la mtandao - Samuel Sitta na Bernard Membe - wakaamua kujitanabaisha na kundi hili, wakijipenyeza na kuwaacha wabia wao wa miaka mingi - Lowassa, Rostam, Karamagi, Msabaha na wenzao wengine wengi wakishangaa. Wakati kila mmoja miongoni mwao akitafuta kujiweka mahali salama kisiasa, Membe, mwanaharakati na mwanamtandao anayezijua mbinu za kiusalama kujiimarisha akaamua kutumia turufu yake binafsi na akajipambanua kuwa mwanasiasa anayeweza kuwa tegemeo na tumaini jipya na safi la kumrithi Kikwete, baada ya kuwaengua kina Lowassa.

-------------------------------------------------------------------------------------
Makala hii pia inapatikana katika tovuti ifuatayo:
Si ufisadi, ni urais 2015 (2)
 
Makala ya Tatu

Tuendako: Si ufisadi, ni urais 2015 (3)


Absalom Kibanda

Jumatano, Aprili 22, 2009

SIHITAJI kuweka msisitizo kuwaandikia Watanzania wenzangu wanaosoma safu yangu hii kila wakati kwamba, joto la kuelekea Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010 linapanda kila kukicha.

Kupanda kwa joto hili la kisiasa kwa wakati huu, kumesababisha kuibuka kwa matukio mengi makubwa na yasiyo makubwa ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na miongoni mwa wanasiasa wa kambi ya upinzani.

Kimsingi, sina haja ya kuanza kuyaeleza tena baadhi ya matukio ya kisiasa ambayo niliyazungumzia katika makala zangu mbili zilizopita, ambazo zote zilikuwa zikigusia mada hii ya leo.

Niseme mapema katika hatua hii ya leo kwamba, hata baada ya kuandika kile nilichokiandika kwa wiki mbili zilizopita, ikiwa ni pamoja na kupokea changamoto zenye ladha zinazokinzana, bado msimamo na imani yangu katika kile nilichokiandika unabakia kuwa thabiti.

Uthabiti wa kile ninachokiandika, ninauona ukiwa bayana katika dhana kubwa mbili; uhusiano wa moja kwa moja uliojijenga katika dhana mbili zilizotawala siasa za nchi hii katika siku na miaka ya hivi karibuni, yaani, ufisadi na urais wa baada ya Jakaya Mrisho Kikwete.

Wakati nikiandika haya, nilikuwa nikitambua vyema kwamba, majemedari wa vita halisi ya ufisadi wa kimfumo na kidola, uliojijenga hapa nchini tangu kuingia kwa mfumo wa soko huria mwanzoni mwa miaka ya 1990, ni baadhi ya wanasiasa wa kambi ya upinzani na vyombo vya habari.

Pengine ambacho sikupata fursa ya kukieleza au kukitolea ufafanuzi wa kina na kwa uthabiti, ni ukweli mwingine kwamba, vita halisi ya ufisadi kamwe haiwezi ikapiganwa katika misingi ya haki na makada wa CCM, ambao mpaka leo hii bado wanaendelea kung'ang'ania ndani ya chama hicho kwa gharama kubwa. Hili nitaanza nalo wiki hii.

Kutokana na kutambua kwangu hilo, ndiyo maana kila mara ninapopata fursa ya kujadili masuala ya kisiasa, hususan haya yanayohusu mapambano dhidi ya ufisadi, nimekuwa nikisisitiza kuwa, ufisadi unaopigiwa kelele nyingi katika taifa letu sasa, ni ufisadi uliostawishwa na mfumo wa kimadaraka na kimamlaka (institutionalised corruption).

Ninaweza kusema kwa kujiamini kwamba, kwa hakika mfumo wa ufisadi huu hapa nchini, haufanani kwa namna yoyote ile na ule wa nchini Kenya wa zama za Daniel arap Moi, wala ule wa Zimbabwe unaofanywa na viongozi kadhaa katika serikali ya Rais Robert Mugabe.
Tofauti kubwa ni kwamba, wakati ufisadi katika nchi nyingine za Kiafrika kama ule ambao umesikika miongoni mwa viongozi binafsi wa juu nchini Malawi, Zambia, Zimbabwe na Kenya, wa hapa nchini umejijenga katika misingi ya kimkakati kidola (state sponsored corruption), ukiwa na baraka za watendaji wakuu na kusimamiwa na viongozi wenye mamlaka mazito ndani ya chama tawala na serikalini.

Ni kwa sababu hiyo basi, ndiyo maana limekuwa ni jambo rahisi kuwafikisha mahakamani akina Chiluba na Bakili Muluzi huko Zambia na Malawi, ilihali ikiwa vigumu sana kwa jambo kama hilo kufanyika hapa nchini.

Ukweli huo ndiyo ambao umekuwa ukinipa jeuri kusema bayana kwamba, kwa mahali ilipofikia CCM, na namna ilivyojijengea uhalali ndani ya dola, ikipenya mioyo, nafsi na akili za watendaji wakuu serikalini, wakiwamo wakuu wa idara nyeti zinazopaswa kusimamia masuala ya ulinzi na usalama wa taifa hili, kupona kwetu kutawezeshwa pale tu, chama hicho kitakaposambaratika katika mapande makubwa mawili au zaidi ya hayo, na kuzaa vyama vingine au kuungana na vyama vingine vya upinzani vilivyopo sasa.

Ingawa mara nyingi maneno ya namna hii ninapoyaandika au kuyasema yamekuwa yakisababisha ukakasi mwingi miongoni mwa viongozi wa serikali, hata wale wa chama tawala, bado ukweli unabakia pale pale kwamba, tiba ya kirusi cha ufisadi unaolikabili taifa hili itapatikana iwapo tu, Watanzania kwanza watatambua kuwa, chimbuko la tatizo hili liko ndani ya CCM na serikali yake, na si miongoni mwa kada au kiongozi mmoja mmoja kama wanavyotaka kutuaminisha baadhi ya wanafiki.

Ni kwa sababu ya ukweli huo basi, ndiyo maana kwangu mimi limekuwa ni jambo lisiloingia akilini, kwa kiongozi aliyepata kushika nafasi za juu ndani ya CCM au serikalini kwa miaka mingi, na ambaye kwa namna moja au nyingine alishiriki moja kwa moja au kwa njia ya ushauri katika matukio yaliyozaa vitendo vya hatari vya kifisadi, yeye mwenyewe leo hii akaamua kujibadilisha rangi kwa staili ya kinyonga na kujipambanua kuwa mwanaharakati hodari wa vita hiyo takatifu, pasipo kwanza kufanya toba ya kisiasa ya wazi kwa Watanzania wenzake.

Katika mwelekeo huo huo, limekuwa ni jambo ambalo fikra zangu zimekataa katakata kuwatilia maanani pasipo unafiki, baadhi ya wanasiasa waliopata kuwa ndani ya kundi la mtandao uliomwingiza Rais Kikwete madarakani mwaka 2005, ambao eti leo hii wakitumia ujinga na wepesi wa kusahau wa Watanzania, wamejipanga kutuhadaa ili ghafla tuwaone kuwa ni mashujaa katika vita dhidi ya ufisadi.

Kama hiyo haitoshi, akili zangu zinakataa katakata kuwasadiki pasipo kudadisi kwa kina, baadhi ya wanasiasa wa ndani ya CCM ambao rekodi zao za kihistoria zinathibitisha pasipo shaka kwamba, kwa namna moja au nyingine walipata kushiriki katika hadaa za kisiasa za chama tawala, wakifanya ubia na watawala kwa nyakati tofauti kwa ajili tu ya kuyaangalia matumbo yao.

Katika mtiririko huo huo, limekuwa ni jambo linaloumiza sana kwa wanasiasa ambao wamepata kuwa watendaji wakuu katika mfumo wa serikali za CCM na wakati mwingine ndani ya chama tawala, leo hii kujitokeza wakijifanya ‘wameokoka' na kujivisha joho la utakatifu unaowapa uhalali wa kuwanyoshea vidole wenzao wengine wa ndani ya chama chao, wakiwamo watu waliopata kuwa maswahiba na wanaharakati wenzao katika ajenda nyingi chafu zilizopata kulihujumu kama si kuliumiza taifa.

Kwa hakika ni mtazamo na tafakuri hiyo hiyo ambayo ilinifikisha katika hitimisho la kuwakataa baadhi ya wanasiasa ambao leo wanawaaminisha Watanzania kwa kila njia kuwa, ni watu safi na wenye nia njema na nchi hii wakati rekodi zao tangu tuwafahamu wakiwa katika kilinge cha siasa za kitaifa na kimataifa, hulka zao siku zote zimelenga kuwachafua wenzao kwa gharama za kujihakikishia pepo za kisiasa mbele ya safari.

Ni kwa sababu hiyo, ndiyo maana kabla sijafikia hatua ya kuandika lolote kwa kina, nilijipa kazi ya kupitapita mitaani na kukutana na watu wazito na wanaowakilisha maslahi ya makundi tofauti, ili kujua ni kitu gani hasa kilikuwa kimejificha nyuma ya pazia hili la vita dhidi ya ufisadi.

Udadisi huo kwa kiwango kikubwa ndiyo ambao hatimaye uliniwezesha kubaini kuwa, vita hii ambayo baadhi ya watu wamejitoa mhanga kuipigania, imeshatekwa nyara na kundi la wanasiasa wenye malengo yao binafsi.

Hitimisho langu hilo lilibainisha pasipo shaka kwamba, msingi wa mparaganyiko huo ndani ya CCM, uliozaa makundi mapya na kustawisha mengine ya siku zote, ni kisasi, kujipatia umaarufu, uchu wa kujitwalia madaraka, kujisafishia njia, kugombea ukaribu na Kikwete na wakati mwingine kusaka uwaziri, ukiwamo uwaziri mkuu.

Kama hiyo haitoshi, udadisi huo ukanifunulia hatua kwa hatua namna makundi hayo ndani ya CCM yalivyokuwa yameshaanza kujipanga kwa ajili ya kutafuta mrithi wa Kikwete, baadhi wakilenga kufanya hivyo mwakani na wengine 2015, kabla upepo wa kisiasa haujabadilika na wote kuamua kuiweka kando ajenda ya 2010 na kuangalia mbele zaidi.

Ni kutokana na ukweli huo basi, ndiyo maana katika makala yangu ya wiki iliyopita, nilihitimisha mada yangu kwa kuweka bayana kwamba, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe alikuwa tayari ameshaanza kuhusishwa na harakati za kuwa mrithi wa Rais Kikwete.

Nilipozisikia habari hizi kwa mara ya kwanza, sikuzitilia maanani na nikaendelea na udadisi wangu ambao ulinipa fursa ya kutambua kwamba, jina la Membe lilikuwa moja miongoni mwa mengine mengi kama Samuel Sitta, Edward Lowassa, Lawrence Masha, Prof. Mark Mwandosya, Frederick Sumaye na Emmanuel Nchimbi, kwa kuwataja wachache.

Wakati majina yote hayo ya wanasiasa yakitajwa, likaibuka pia jina la mfanyabiashara mashuhuri, Reginald Mengi, kwanza akihusishwa na CCM na baadaye CHADEMA kabla yeye mwenyewe kujitokeza mbele ya rais na kukanusha uvumi huo.

Hadi ninapoandika makala hii leo, ni Membe peke yake ambaye hajakabiliana na shutuma za wazi dhidi yake, tangu vita dhidi ya ufisadi itekwe nyara na wanasiasa wanafiki wachache wa ndani ya CCM. Kusitirika huko kwa Membe hadi leo hii ambako kwa hakika bado naendelea kukufanyia utafiti, japokuwa kulikuwa na jitihada za kujaribu kumhusisha na mradi wa zabuni ya vitambulisho vya taifa, hakuondoi ukweli kwamba, mwanasiasa huyo aliyepata kuwa swahiba mzuri wa akina Rostam Aziz na Lowassa, anaweza akawa ameshaanza safari kwa ajili ya kumrithi Kikwete au vinginevyo.

Kwa mtu anayemfahamu Membe sawasawa, anaweza akawa mpuuzi iwapo ataamua kuzipuuzia hoja zinazomhusisha mwanasiasa huyo mwenye historia ya ukachero na harakati za urais wa mwaka 2015, ama kwa nafasi yake binafsi au ya mtu anayemuamini sana.

Baadhi yetu tunakumbuka vyema namna Membe alivyoshiriki kikamilifu na pasipo kuyumba katika harakati za miaka 10 za kuhakikisha Kikwete (mwenyewe humwita Jakaya), rafiki yake mkubwa wa tangu zama za Chuo Kikuu cha Dar es Salaam wa miaka ya 1970, anakuwa rais, kwanza mwaka 1995 na kisha 2005.

Waandishi wenzangu wa habari za uchunguzi ni mashahidi wa namna Membe na wenzake wa kundi la mtandao walivyoshiriki kikamilifu nyuma ya pazia katika kuhakikisha kwamba, safari ya Kikwete kuingia Ikulu inaondolewa vikwazo vyote dhidi yake serikalini.

Ninaweza kusema pasipo shaka kwamba, ingawa harakati kubwa za kumpeleka Ikulu Kikwete zilizohusisha mikakati katika vyombo vya habari, ndani ya CCM, serikalini na hadi Ikulu ziliratibiwa na akina Rostam, Lowassa, Sitta na wenzao wengine, bado ni ukweli kwamba, Membe hakupata kuachwa nje ya mzingo mpana wa harakati hizo.

Zama hizo, wakiwa Dodoma na Dar es Salaam, lilikuwa ni jambo la kawaida kukutana na Membe akiwa bega kwa bega na Rostam ama ana kwa ana na wakati mwingine katika mawasiliano yao ya simu.

Kwa hakika kuanguka kisiasa kwa wanasiasa wa kariba ya Hassy Kitine, Prof. Simon Mbilinyi na Iddi Simba kutoka serikalini kwa staili ya kutenganishwa na Benjamin Mkapa aliyekuwa rais wa zama hizo, na mtu aliyewaamini kwa kiwango kikubwa watu hao, hakuwezi kutenganishwa na harakati za wanamtandao akiwamo Membe.

Leo hii anapoangushwa Lowassa, Rostam na wenzao wengine waliokuwa karibu mno kimkakati na Kikwete, na kufuatiwa na kutengana kisiasa kwa watu hao na wanaharakati wenzao kama Membe na Sitta kwa kiwango cha kupoteza mawasiliano ya kidugu na kirafiki waliyokuwa nayo kabla na baada ya ‘mtu wao' kuingia Ikulu, ni ushahidi wa mwanzo kwamba, ugomvi huu wa sasa unafanana na ule wa zama za akina Mbilinyi, Kitine na Simba.

Tutaendelea wiki ijayo.
------------------------------------------------------------------------------------
Makala hii inapatikana katika tovuti ifuatayo:
Si ufisadi, ni urais 2015 (3)
 
Makala ya Nne
Si ufisadi ni urais 2015 (4)

Jumatano, Aprili 29, 2009

Absalom Kibanda
TANZANIA imekuwa ni nchi yenye mtiririko wa matukio makubwa makubwa ya kisiasa, hususan yale yanayozungumzia ufisadi katika siku, miezi na miaka ya hivi karibuni. Nimepata kuliandika hili na kwa kweli nalazimika kulirejea tena wiki hii.

Kila Mtanzania anayefuatilia masuala yanayohusu tuhuma za ufisadi, ni shahidi mzuri kwamba kati ya wiki iliyopita na leo hii, kumetokea masuala mazito katika taifa hili yanayogusa masuala hayo ya ufisadi.

Kubwa kuliko yote ni lile linalomhusu mfanyabiashara maarufu na mwenye jina kubwa hapa nchini, Reginald Mengi, ambaye wiki iliyopita aliamua kujitoa mhanga kwa namna ambayo si rahisi kuieleza, akataja majina ya watu watano ambao aliwahusisha na tuhuma za ufisadi na kwa maneno yake mwenyewe, akawaita ‘mafisadi papa'.

Kishindo cha kauli hiyo ya Mengi, kikasikika kwa namna yake katika vyombo vya habari na kwa hakika, vile ambavyo yeye mwenyewe anavimiliki, vikalipa uzito wa kipekee suala hilo. Hili sina haja ya kulifafanua.

Udadisi binafsi nilioufanya kwa kusikia maoni ya moja kwa moja toka kwa watu mbalimbali, umenithibitishia jambo moja kubwa kwamba, kauli ya Mengi imeibua mjadala mkubwa mitaani, maofisini na majumbani.

Na kwa namna ya ajabu, kauli hiyo imeweza kuthibitisha pasipo shaka namna mfanyabiashara huyo alivyoweza kuibua mgawanyiko wa wazi wa kimaoni, kuhusu kile alichokisema. Wako wanaompinga na wako wanaomuunga mkono.

Aidha, kwa upande mwingine na kwa mtazamo wangu, kauli hiyo ya Mengi imezidi kuweka ‘chumvi katika kidonda' ambacho nimekuwa nikikizungumzia katika makala zangu tatu zilizopita, na pengine hii ya leo.

Kwa hakika kwa kauli yake, nimejiridhisha pasipo shaka kwamba, vita ya ufisadi ambayo Watanzania tumeiunga mkono kwa dhati, inaendelea kuonyesha kila dalili za kuanza kupoteza mwelekeo kama si kupotoshwa.

Naweza kusema pasipo kusita kwamba, uamuzi wa Mengi, mfanyabiashara ambaye nguvu zake katika umma ni kubwa, kuwataja watu watano kwa majina akisema wao ndio mafisadi papa, umefanikiwa kuvuruga ukweli wa wazi unaogusa mfumo mzima wa utawala wa nchi, unaoongozwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM) na tuhuma nzito za ufisadi.

Sina sababu ya kurejea kwa kina kile nilichokieleza wiki iliyopita, kwamba aina ya ufisadi unaolitafuna taifa letu ni ule uliojistawisha na kujizatiti katika mfumo wetu wa kimadaraka, ambao huwatumia watu wachache katika kufanikisha azma za watawala.

Lakini pengine kikubwa ambacho nilikiona na nimeendelea kukiona kutokana na matamshi hayo ya Mengi ni kwamba, kidogo kidogo, ukweli kwamba vita dhidi ya ufisadi imeanza kupenyezwa kisiasa, ikilenga kustawisha kundi jipya linalojipanga kuamua hatima ya urais wa baada ya Kikwete, umeanza kujidhihirisha.

Kwa hakika sina uhakika iwapo Mengi anayo mapenzi ya dhati na imani ya kweli kwa Rais Kikwete, na kwamba anamuunga mkono kiongozi huyo katika kile anachokiita kuwa ni mapambano yake dhidi ya ufisadi.
Sababu kubwa ya kutokuwa kwangu na uhakika, ni namna vita hii inayoongozwa na wazee wetu kama akina Mengi, inavyojaribu kupiganwa kwa njia ya kumwacha rais akibakia mpweke wakati wasaidizi wake wakuu kikazi, wakiwamo mawaziri na wakati mwingine marafiki zake, wanapoanza kunyofolewa kwa namna ya kushambuliwa mmoja baada ya mwingine.
Mashaka yangu kuhusu jambo hilo yako wazi, na ndiyo maana nilianza mapema hata kabla Mengi hajajitokeza na kusema kile alichokisema kuhusu namna kunyofolewa kwa maswahiba wa Kikwete kunavyofanywa ili tu kuhalalisha matakwa fulani fulani ya kisiasa. Kwangu mimi, staili hii ya kutafuta watu uchawi ni ya hatari kubwa.
Watu ambao wamekuwa wakisoma safu yangu hii na pengine wale ambao wamekuwa wakifuatilia makala zangu, ni mashahidi wazuri wa namna ambavyo nimekuwa siku zote nikipinga siasa za watu kuwindana, kushikana mashati na kushambuliana.
Ni kwa sababu hiyo, ndiyo maana wakati baadhi ya watu walipokuwa wakiwashambulia watu kama Mengi mwenyewe miezi kadhaa iliyopita kwa dhamira iliyoonekana waziwazi kumlenga kwa nia ya kumhujumu, niliwapinga na nikamtetea mfanyabiashara huyo mzalendo kwa nguvu kubwa.

Katika mlolongo huo huo wa kimtazamo, nitakuwa msaliti wa dhamira yangu iwapo leo hii tena, nitaamua kuondoka katika misingi hiyo na kuunga mkono harakati za Mengi za kujibu mapigo, kulipiza kisasi au kuwawinda baadhi ya watu kwa staili ile ya kutafuta wachawi.

Kwangu mimi usaliti wa namna hiyo si tu kwamba utagusa hisia zangu, bali pia naona wazi kwamba, utajenga msingi wa kuhalalisha aina mpya ya siasa zilizoanzishwa na kundi la mtandao lililomuunga mkono Kikwete katika harakati zake za urais, ambalo moja ya mikakati yake mikubwa ilikuwa ni kuchafua watu kwa staili ile ile ya kutafuta wachawi.

Ni jambo la kusikitisha sana leo kwamba, maadui wa kisiasa wa Rais Kikwete; Edward Lowassa, Rostam Aziz, Jeetu Patel, Tanil Somaiya na wengine, leo wamejikuta nao wakinaswa katika mtego huo huo wa hoja za kushangilia wabaya wao kushambuliwa, pasipo kuangalia na kujiuliza iwapo kwa kufanya hivyo wanaendeleza dhambi ile ile iliyopaswa kufanywa na wanasiasa na wafanyabiashara wengine miaka michache tu iliyopita.

Lakini pengine jambo baya zaidi ni ukweli kwamba, baadhi ya watu ambao wanaonekana kujitokeza na kuwa mstari wa mbele leo hii wakiunga mkono vita hii ya ufisadi mpya iliyojengwa chini ya misingi ya kutafuta wachawi, wanafanya hivyo si kwa sababu nyingine yoyote, bali wakilenga kujiandalia mrithi wanayeamini atawafaa baada ya Kikwete. Hakika siasa za aina hii ni usaliti mbaya kwa taifa.

Pengine niseme mapema kwamba, utaratibu huu mpya wa baadhi ya wazee na viongozi wetu kama alivyo Mengi, Samuel Sitta, Christopher ole Sendeka, Lucas Selelii na wenzao wanaosema wamejitoa mhanga kupambana na ufisadi (vita ninayoiunga mkono), wa kuanza kutafuta wabaya wao ili kuhalalisha mapambano yao, unaweza siku moja ukasababisha taifa likaingizwa katika hatari ya kupandikizwa kwa chuki na uhasama, ambao suluhu yake itakuwa shida kuipata kwa njia za amani. Hatutaki watufikishe huko.

Wakati nikisema hayo, pengine niseme mapema kwamba, makala zangu zilizopita zilizaa maoni tofauti kutoka kwa wasomaji.
Mmoja wa wasomaji hao, ambaye wiki ijayo natarajia kutoa majibu ya hoja alizozitoa akizungumzia hoja yangu alikuwa na haya ya kusema: Ndugu yangu Kibanda, Salaam. Nimesoma makala zako, hasa sehemu ya pili na ya tatu na kuvutiwa na mada husika. Kwa kweli mada yenyewe ni nyeti na yenye kujuza, hasa kama utafiti uliofanywa ni wa kina. Kwa aina ya magazeti yetu, ni moja ya makala zenye mtiririko wa kuvutia, lakini pia yenye kuacha maswali mengi kwa watu (nadhani), labda ni vema nijisemee mimi binafsi.

Mada inasema si ufisadi bali urais wa 2015. Inaweza kuwa kweli au hapana, kuendana na hitimisho lako litakavyokuwa, japokuwa kwa eneo ulilofika hadi sasa, unaonyesha kana kwamba unaamini hakuna vita ya kweli.

Binafsi napata shida kidogo katika mambo mawili haya; vita ya ufisadi na hizo mbio za 2015 au hata labda tuseme 2010 (kwa wanaodai kuna mpango wa mapema hivyo).
Nijuavyo mimi, ufisadi ni kitu kibaya, ufisadi wa aina yoyote ile na unaofanywa na mtu yeyote yule haufai. Ana heri anayeupiga vita ufisadi huo kama ilivyo wenye heri wanaojitahidi kuzuia uhalifu, dhambi au kwenda mchomo kwa watu kwenye mambo mbalimbali (yaani kuepusha mabaya).

Kwa hiyo, vita ni vita, madhali tunakubaliana kwamba ufisadi ni mbaya, maana sidhani hata kidogo kwamba wewe unaweza kuwa mmoja wa watu wanaounga mkono mafisadi, lazima ufisadi huo na wanaoutenda wapigwe vita, ili hatimaye tubakiwe na nchi safi yenye watu safi, mipango safi na mwenendo safi.

Watu wenye mikono misafi tu ndio waruhusiwe kuendesha nchi yetu kwa kupewa ofisi zetu takatifu. Kwa mtiririko wa uchambuzi wako, nakwazwa kwa sababu inaonekana kana kwamba unasema kuna haja ya kudharau vita dhidi ya ufisadi, au kuuacha ufisadi uendelee, maana wanaoupiga vita wana ajenda binafsi.

Mimi nadhani vyama vyote vya siasa na dini zote za kweli na zenye watu walio na dhamiri safi lazima wapige vita ufisadi kwa nguvu zote na kutoka kila upande. Sasa hili la kusema ajenda imebinafsishwa, si sahihi. Sikubaliani na yeyote yule, awe kutoka chama cha upinzani, chama tawala, serikalini au katika vyombo vya habari atakayelalamika kwamba ajenda yake (yao) ya kupambana na ufisadi imebinafsishwa au imeibwa na mtu au kundi fulani.

Mimi nadhani usahihi ni kwamba, yeyote atakayejiunga katika kupiga vita ufisadi akaribishwe kwa mikono miwili na jitihada zifanyike ili wengi kadiri itakavyowezekana wajiunge upande wa kupiga vita ufisadi kwa sababu kuna uwezekano mkubwa zaidi kwa wengi kuwashinda wachache kuliko kinyume chake. Hata hivyo, wachache wanaweza kutumia nguvu ya akili, ujanja, uzoefu na hata fedha na mali kuushinda upande mwingine. Ndiyo maana nasema hakuna mantiki mmoja kulalamika kwamba vita 'yake' dhidi ya ufisadi imechukuliwa na wengine.

Huu ni mzigo mzito ambao hata Mnyamwezi hawezi kuubeba peke yake. Ni dude kubwa ambalo lazima wengi wajipange kulisukuma mpaka litumbukizwe kwenye shimo la kina kirefu, lisiweze tena kutoka na kuja kuwasumbua watu.

Pengine kinachotuhangaisha katika muktadha huu, na hasa katika vyombo vya habari na kwa wanasiasa, ni inapofikia kutoa hukumu. Ni vizuri tuelewe jambo moja kwanza na tukubaliane - wote hatutaki ufisadi. Au yupo anayeutaka? Ajitokeze hadharani atuambie mimi naunga mkono ufisadi. Sijapata kuona wala kusikia, na kama wapo wanayasemea kwenye sakafu za mioyo yao.

Hata kama kuna ajenda binafsi za kutafuta urais, ni vema wote tuungane upande mmoja kwa sababu nchi ni yetu wote, ikiliwa tunaumia sisi (isipokuwa wale wanaopata gawio kutoka kwa hao mafisadi) na mwisho nchi yetu inaangamia na tunabaki na umasikini. Kwa hiyo, wote kwa pamoja tukiingia kwenye mchakato wa kupambana na ufisadi itapendeza.
Huwezi kusema huyu aache kupambana nao maana ana ajenda ya siri kwapani, hatutafika. Aache kwa vipi? Nani atakuwa hakimu au jaji wa kusema fulani sawa apige vita ufisadi na fulani aache maana ana ajenda ya siri? Vita inapokuwa ni moja dhidi ya ufisadi, mambo mengine yanaendelea.

Ni vigumu kutekeleza jambo moja na kuacha mengine. Masuala haya ni mtambuka na lazima yaende pamoja. Ndiyo maana wakati rais wa nchi anaendelea kuongoza wananchi wote bila kubagua itikadi (ndivyo inatakiwa), anaendelea kuongoza vikao vya chama chake, kufanya uteuzi na kukiandaa chama kwa chaguzi zijazo.

Kadhalika wapinzani wapo bungeni kama kioo cha serikali ikichafuka ijisafishe, ikitoka barabarani ijirudishe na wakati huo huo vyombo vya kusimamia sheria na vile vya ku-adjudicate vinaendelea na kazi yake kwa mujibu wa sheria, huku nyingine zikitungwa ili kuboresha utendaji wa vyombo vyetu. Kwa hiyo, kama wapo wenye ajenda ya siri ya kuumiza wengine, watajulikana tu mwisho wa siku na nadhani hawatapewa nafasi ya uongozi, na huenda hata vyama vyao havitawapa fursa za kuwania nafasi husika.
Tuendelee na safari yetu ya kujenga Tanzania yenye umoja, amani, mshikamano, utulivu, maendeleo endelevu na hatimaye asali na maziwa kwa kila mtu. Ni kazi nyingi, na katika kuyafikia haya yote, lazima ufisadi usukumwe kando pamoja na mafisadi wenyewe. Tangu serikali ya awamu ya nne iingie madarakani, ni hoja yangu kwamba imekuwa na kazi ya kuweka mambo sawa kuliko kujenga mapya.

Imekuwa kama mtu anayetaka kujenga nyumba, lakini eneo la kujenga nyumba kuna miti mikubwa, tena yenye mizizi mirefu, kuna lundo la takataka ngumu na majimaji na pia labda kuna tatizo jingine la kurekebisha. kwa hiyo lazima kwanza kuondoa vyote hivyo ili kuweza kuanza kuchimba msingi kwa vipimo takikana na kuanza ujenzi wa nyumba yenyewe.

Na wakati hayo yakiendelea, mwaka wa nne huu hapa na wa tano unaanza, kipindi cha kwanza kinaisha. Ni juu ya Watanzania kuangalia kama wameweza kuchimba kwa kasi inayotakiwa miti husika, kuondoa uchafu na kusawazisha eneo (na katika haya kuna huo ufisadi, hali mbaya ya uchumi, matatizo yanayozuilika na mengine ya kujitakia kwa uzembe na mengine ya asili yasiyozuilika).

Kwa hiyo wote kama Watanzania, tuwe na kazi moja, kupambana na ufisadi. Kwa hiyo ukimwona yeyote anapiga vita ufisadi usibadili ajenda na kumwandama yeye kama mtu. Kila mtu aangalie udhaifu uliopo, kama upo kwako nausema, upo kwangu unausema. Be thy brother's keeper.

Msaidie mwenzio aondoe boriti nawe atakuonyesha kibanzi chako. Mtu si rahisi kuona uchafu ulio mgongoni au kisogoni mwake, mwingine ndiye ataona na kumwonyesha, naye anamwambia nawe pia tazama u mchafu eneo hili. Jisafishe, jitakase ili uweze kuingia hekaluni kwa mwanakondoo baada ya kuvaa mavazi meupe, masafi na mwili na roho isiyo na mawaa!

Kwa kufanya hivyo tutakwenda, lakini kuanza kusema hakuna hili wala lile, au fulani kaiba ajenda yangu ya kupiga vita ufisadi, itakuwa ubinafsi. Ujanja wa kisiasa lazima uwapo, kutumia fursa zinazojitokeza kujinadi kupo, na historia inaonyesha hakukwepeki, lakini tusitumie kigezo hicho kuwapiga vita wanaopiga vita ufisadi, tukae nao pamoja tushirikiane kwa silaha mbalimbali kuuangamiza, maana nyumba yetu ni moja kugombea fito hakutusaidii hata kidogo." Mwisho wa kunukuu.

Wiki ijayo nitajibu sehemu ya hoja zake, ikiwa ni pamoja na kuweka sawa pale ninapoamini ama mimi au msomaji wangu alikuwa ameteleza.

Makala hii inapatikana katika tovuti ifuatayo:
Si ufisadi ni urais 2015 (4)
 
Makala ya Tano

Tuendako: Sio Ufisadi, Ni Urais 2015 (5)

Absalom Kibanda

Jumatano, 6, Mei, 2009
NISEME mapema kwamba, hii ni sehemu ya mwisho ya makala zangu zinazozungumzia mada inayojaribu kuonyesha kuwapo kwa uhusiano wa karibu kati ya ajenda ya zama hizi ya vita dhidi ya ufisadi na harakati za kusaka urais wa mwaka 2015 ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Namshukuru sana Mungu kwamba, nimefikia tamati katika mjadala huu katika wiki ambayo tumeshuhudia vita kubwa ya hoja na vielelezo ya mafahali wawili wafanyabiashara wenye ushawishi mkubwa, Reginald Mengi na Rostam Aziz.
Ninaona fahari kusema kwamba, wakati makala zangu zikiwa katikati, mwelekeo wa hoja zake kwa sababu ambazo si rahisi kuzieleza kwa maneno, zilishabihana kwa kiwango kikubwa, na matamshi yaliyotolewa na mwanasiasa mwanazuoni na bingwa wa uchumi, Profesa Ibrahim Lipumba.
Sote wawili, Lipumba na mimi, tulijikuta pasipo kuwahi kukaa pamoja na kujadili, tukiguswa na kuamini kwamba ufisadi unaolitafuna taifa leo hii, umejengwa na kustawishwa katika mfumo wa kimamlaka ukiunganisha mitandao ya rushwa iliyopenya ndani ya Serikali ya CCM.

Katika medani za kisomi, uchambuzi wetu wawili, ulitupa hitimisho kubwa moja kwamba, aina ya rushwa inayolitafuna taifa hivi sasa, hata kusababisha watu wazito kuingia katika malumbano, ni ile ya kimfumo, yaani, ufisadi wa kitaasisi au kwa kimombo rahisi; institutionalised corruption.

Kwa sababu hiyo basi, hatua za msingi ambazo Watanzania kama taifa tulikuwa tukipaswa kuanza kuzichukua sasa ili kukabiliana na hatimaye kushinda vita dhidi ya rushwa, zilikuwa hazina budi kuanza kuchukuliwa katika mwelekeo wa kuudondosha kwa namna ya kimapinduzi, mfumo huo wa kifisadi uliojistawisha kwa miaka nenda, miaka rudi.

Ninaamini tena kwa dhati kwamba, tatizo hili la kimfumo ambalo limejijenga kwa miaka mingi na kustawi, ndilo ambalo katikati ya miaka ya 1990, wakati akiwa hai, Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere, alipata kulisemea pale alipotamka kuwa, "upinzani wa kweli utatoka ndani ya CCM."

Watu wanaokumbuka vyema kauli hiyo ya Mwalimu, ambaye zama hizo akiwa kiongozi mstaafu alibakia kuwa mwanafalsafa wa masuala ya siasa, alikwenda mbele zaidi na kusema hilo lingewezekana tu iwapo CCM ingemegeka katika makundi makubwa mawili.
Ukizichukua kauli hizo za Mwalimu na kuangalia namna alivyokuwa akikerwa na rushwa ndani ya chama chake hicho, ambacho wakati huo alifikia hatua ya kukiponda akikifananisha na kokoro linalosomba kila aina ya uchafu na kisha akasema angeweza hata kukiacha kwa kuwa hakikuwa mama yake, utabaini kirahisi kwamba, alikuwa akiamini kwamba, tiba ya matatizo mengi hapa nchini, likiwamo lile kubwa la rushwa, ingepatikana iwapo tu chama hicho kingemegeka.

Wakati fulani nikifanya mazungumzo ya kawaida na mwasisi na Mwenyekiti wa kwanza wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Edwin Mtei, mzee huyo ambaye sasa ni mstaafu, alinieleza pia jinsi Mwalimu Nyerere alivyopata kuwaeleza dhamira yake hiyo ya kuona CCM ikimegeka wakati walipokwenda kumtembelea nyumbani kwake Butiama miaka ya mwanzo ya 1990.

Ni jambo la kusikitisha kwamba, tangu Mwalimu aeleze ndoto zake hizo njema kwa mustakabali wa taifa, viongozi na makada wa CCM wamekuwa wakifanya kila linalowezekana kukinusuru chama chao kufikwa na msambaratiko ambao hatimaye ungeweza kujenga upinzani wenye nguvu. Wamefanikiwa kwa kiwango kikubwa.
Pengine hali hiyo huwa ni ya kusikitisha zaidi wakati jitihada za wazi za vyama vya upinzani - hususan viwili vyenye ushawishi unaowiana vya CUF na CHADEMA – kujiimarisha, zinapokwamishwa ama na ujinga, wivu na ubinafsi wa viongozi wa vyama hivyo au kwa njia ya mikakati ya hila ya makada na viongozi wa CCM na wale wa serikali.
Mambo haya mawili yanapotokea, lile la CCM kushindwa kumegeka ili kumuenzi Mwalimu na hili la pili la kuendelea kuudhoofisha upinzani kwa kila hila za wazi na za siri, kikubwa kinachoendelea ni kustawi na kukomaa kwa misingi ya ufisadi wa kitaasisi ambao hatima yake hutuhujumu Watanzania wote.

Ni kutokana na misingi hiyo, ndiyo maana katika makala zangu zote nimekuwa nikipambana na kutofautiana sana na wale wote ambao wamekuwa wakijaribu kunishawishi nikubaliane na mbinu chafu zinazotumiwa na viongozi, wabunge, wapambe na makada wa CCM katika kuendesha vita dhidi ya ufisadi, kwa dhamira ya kukiponya chama chao ambacho safari ya utimilifu wa unabii wa kisiasa wa Mwalimu Nyerere ilikuwa ikikaribia kabisa kutimizwa.

Ni kwa sababu hizo ndiyo maana nilisema huko nyuma na ninasema tena kwamba, aina ya mikakati inayoendeshwa na kundi la wana CCM wanaotamba kwamba wamejitoa mhanga kukabiliana na ufisadi na ambao siku zote jitihada zao zimekuwa zikilenga kukilinda chama chao, serikali yao na rais wao, ni haramu na ambayo kwa watu wenye akili timamu si ya kuungwa mkono hata kidogo.

Watu wenye akili timamu watakubaliana nami kwamba, kazi kubwa iliyofanywa na Kamati Teule ya Bunge iliyoongozwa na Mbunge wa Kyela, Dk. Harrison Mwakyembe kuchunguza kashfa ya Richmond, iliishia katika kuhakikisha serikali, rais na CCM vinabakia imara.
Kulithibitisha hili wala hakuhitaji akili nyingi, kwani ni jambo rahisi kwani ilibidi aliyekuwa Waziri Mkuu Edward Lowassa aanguke au aangushwe ili kuinusuru CCM, serikali na Rais Jakaya Kikwete.

Ni kwa sababu hizo hizo, ndiyo maana wabunge wa CCM waliokuwa wakijua kwamba, wapinzani walikuwa wameshajitwalia sifa katika kashfa ya Buzwagi kutokana na hoja nzito za mbunge kijana wa CHADEMA, Zitto Kabwe, wakahakikisha wanaungana kuwafikisha kule walikokuwa wakitaka kumpeleka Lowassa akina Nazir Karamagi na Dk. Ibrahim Msabaha. Katika hili wakafanikiwa.

Mkakati huo ulipofanikishwa, ndipo hapo ghafla mashujaa wapya wa vita dhidi ya ufisadi, akina Luca Selelii, William Shellukindo, Christopher ole Sendeka, Anna Kilango, Samuel Sitta na Mwakyembe wakaibuka kwa nguvu kubwa wakiwaweka kando akina Dk. Wilibrod Slaa, Hamad Rashid Mohammed, Halima Mndee na Zitto. Hii ilikuwa chenga ya kwanza ya mwili na akili.

Mwanzo huu wa kuinusuru CCM ukaendelea kujibadilisha sura katika masuala mengi mengine na hali ikajirudia katika masuala ya EPA, Dowans na kila ufisadi mpya ulipotokea.
Baadhi yetu tulipoiona hatari hiyo kubwa mapema, ilipotoka tu ile ripoti ya Kamati ya Mwakyembe, tuliamua kutumia kalamu zetu kutoa tahadhari tukionya kwamba, kazi iliyofanyika ilikuwa mahususi kwa ajili ya kutoana kafara ndani ya CCM ili kuhalalisha kuendelea kubakia madarakani.

Maoni yetu hayo ambayo kimsingi yalikuwa na lengo la kujaribu kunusuru demokrasia, yakapokewa kwa upinzani mkubwa kutoka miongoni mwa makada madhubuti wa vyama vya upinzani, na hata wale walio ndani ya CCM ambao wakati huo walifikia hatua ya kujidanganya kuwa walikuwa ni kitu kimoja.

Hali hiyo ilisababisha upepo wa kisiasa kwa taifa zima kupunga kuelekea mwelekeo mmoja na kwa bahati tu ukafanikiwa kumfikia mzee wetu, Reginald Mengi, mfanyabiashara mwenye nguvu kubwa ya vyombo vya habari na ambaye kwa miaka mingi amejijengea ushawishi mkubwa katika jamii.

Tukio hilo la Mengi kuingia au kukumbwa na upepo huo ghafla, kukageuka kuwa neema kubwa si kwa CCM na serikali yake tu, bali pia kwa kundi la makada wa chama hicho ambao wengi ni maskini, waliokuwa wameamua kujitoa mhanga kupambana na ufisadi lengo likiwa kukirejesha chama chao katika mstari, kuinusuru serikali yao na kimsingi kujinusuru wao kisiasa.

Katika lile la mwisho la kujinusuru wao wenyewe, wana CCM hawa walijikuta wakihitaji kukingiwa kifua na mtu mwenye nguvu kubwa ya kiushawishi na pengine kifedha wa aina ya Mengi ili kuweza kupona kuliwa na ukali wa makucha ya makada wenzao wenye nguvu kubwa kimtandao na kifedha waliokuwa wameumizwa na matokeo ya ripoti ya Richmond.
Watu wanaowafahamu vizuri Lowassa na rafiki yake mkubwa, Rostam Aziz ambao walikumbwa na tsunami ya Richmond katika mazingira ambayo siku zote walikuwa wakiyaona kuwa ni ya kuonewa, kuhujumiwa na kulipizwa kisasi, walikuwa wakitambua kwamba watu hawa wasingeweza kukaa kimya na kuwaacha wabaya wao kisiasa wakistawi nyuma ya migongo yao.

Huo ndiyo ukawa mwanzo wa mapambano ambao kimsingi sina sababu ya kuuendeleza kwani nimeshauzungumzia sana siku zilizopita.
Ni kwa sababu hiyo basi, ndiyo maana ni rahisi kuona leo hii kwamba, vita ya sasa inayohusisha makundi makubwa mawili ndani ya CCM ambayo wiki hii na iliyopita yamejipambanua, moja likiwakilishwa na Mengi na jingine na Rostam msingi wake si ufisadi hata kidogo, bali maslahi ya kisiasa yaliyojikita katika kuusaka urais wa mwaka 2015.
Ni jambo jema kwangu kwamba, tangu nianze kujadili mada hii, wiki nne zilizopita, wanasiasa, wachambuzi wa mambo na mashabiki wa makundi yote mawili, kwa namna moja au nyingine wameamua kukaa kimya wakifunga mdomo wakihofia kufichuka kwa siri waliyotaka kufa nayo.

Wanafanya hivi si kwa sababu zozote zile, bali kwa sababu ndani ya makundi yote mawili kuna watu ambao wanao uzoefu wa kucheza rafu za kisiasa zinazohusisha maandalizi ya urais kwa mtu ambaye ni chaguo lao kwa wakati wanaokusudia.

Watu hao ambao wana uzoefu mkubwa katika michezo ya namna hii inayohusisha sayansi ya kumaliza wabaya wao ni akina Lowassa, Rostam, Bernard Membe, Samuel Sitta na Dk. Emmanuel Nchimbi.

Ukiwaacha Lowassa na Rostam ambao leo hii wako katika kundi la majeruhi, wengine waliobaki bado ama wako serikalini au ndani ya Bunge.

Wanasiasa hawa kila mmoja ana nguvu ambazo kwa hakika si za kuzipuuza hata kidogo. Hawa wote ni mabingwa wa mikakati na watu ambao nyuma yao wamezalisha wafuasi lukuki wa kisiasa ambao wanashabikia moja ya makundi hayo.

Pasipo kutaja kundi alilo mtu, wanaocheza nyuma ya mabingwa hawa wa harakati wako akina Mengi, John Malecela, Nape Nnauye, Lawrence Masha, Kilango, Makinda, Mwakyembe, Sellelii, Sendeka na watu wengine wengi ambao kila mmoja amepewa kazi muhimu ya kufanya ndani ya kundi husika.

Watu hawa niliowataja, ndio ambao hakuna shaka kwamba leo hii wanaiyumbisha nchi na kuitikisa serikali. Kwa hakika ni watu hawa ambao wamesababisha ama tupewe majina ya sifa au majina ya kashfa. Hawa ndio wako nyuma ya habari kubwa zote zinazohusu vita dhidi ya ufisadi ama wakiunga mkono upande huu au ule.

Wote hawa kwa bahati moja kubwa, bado wanaonekana kuwa na utii ama wa kweli au wa kinafiki kwa Rais Kikwete na kwa hakika CCM. Kwa hakika hawa ndio watu wa kwanza tunaopaswa kushughulika nao.

Kwa hakika wakati tunapotakiwa kuanza kuishughulikia CCM kwa lengo la kuimega vipande viwili au vitatu ili kumuenzi Mwalimu, tunapaswa kuanza kushughulika na watu hawa kwanza.

Niseme wazi kwamba, kwa Rais Kikwete kama anataka kweli kukomesha vita isiyo na tija ya kusaka urais wakati huu, hata kusababisha wananchi kuacha kufikiria kazi na shughuli za msingi za kiuchumi na kijamii, anapaswa kuwaondoa serikalini mara moja, Membe, Masha na Nchimbi.

Katika hili, Kikwete anapaswa kuchukua hatua hizo si kwa sababu ya kutaka kuwaumiza au kuwatenga. La hasha, bali kwa lengo la kulijengea taifa hali ya utulivu, amani na kimsingi msingi bora wa kutimiza ndoto yake ambayo haijafanyiwa kazi kabisa ya kuwaandalia Watanzania maisha bora.

Ndani ya chama chake na kuanzia katika Kamati Kuu, na Halmashauri Kuu, anapaswa kuwachukulia hatua za kinidhamu kichama akina Rostam, Sitta, Membe, Lowassa, Malecela na wote ambao wametufikisha hapa tulipo sasa. Atakuwa amelinusuru taifa. Huko ndiko tunakopaswa kwenda.

Makala hii inapatikana katika tovuti ifuatayo:

Si ufisadi ni urais 2015 (5)
 
Ukisoma makala hizo kwa makini utaelewa KIBANDA ni miongoni mwa waandishi wa habari wachache sana hapa Tanzania wenye uwezo mkubwa , maono na nguvu ya kuchambua hoja na kuziwasilisha kwa wasomaji wake, haya aliyoyandika mwaka 2009 unaweza ukayaona vema sana kwa sasa.
 
Nakupongeza sana mleta uzi. Ki ukweli nikili kuwa sikuwai kusoma makala hizi na sikuwa nikimjua vizuri Kibanda lakini kwa uzi huu nimemfahamu. Kwa makala zake ni vigumu sana kutomuhusisha yule waziri aliyesema kuwa ana maadui wakiwemo waandishi wa habari kwenye uhasama na Kibanda kwani amemtaja mara nyingi mno tena in negative manner. Kiasi flani nimepata picha kwa nini huyu jamaa amefanyiwa hicho alichofanyiwa, lakini kwa kuwa mikono yake ipo salama na jicho moja ni zima pia ubongo haukupata hitirafu basi tumuombee apone haraka aendelee kutujuza mustakabari wa nchi yetu maana anayajua mengi.
 
Ile Tume kama kweli ipo,wangeanza na BM kumkamata na kumhoji kuhusiana na kuteswa kimafia kwa Kibanda,haiingii akilini kabisa kumuacha BM kwa makala kama hizi,BM amechemsha sana kumuumiza Kibanda sababu ya ukweli na mtazamo wake kwenye makundi na ufisadi,BM hataki aguswe au aandikwe?sababu yeye ana mtandao wa kikachero?mbaya sana!Kama ameungana na kaka yake kutengeneza utawala wa kimla,muda utafika mbivu zitajulikana na mbichi zitatengwa!BM anapata wapi nguvu ya kuwatumia Polisi kumuumiza Kibanda?au ana support ya JK?
 
Tunashangaa ni kwanini mpaka leo Dr steve Ulimboka hajawahi kuhojiwa na polisi, kwa hiyo hatutashangaa kama Kibanda
nae hatahojiwa pia, _ Dr. Wilbroad Peter Slaa, CHADEMA's candidate for presidencial elections 2010.
 
Naona mnataka kuhama kutoka chama chetu cha mapinduzi[revolutionary party] kwenda chama cha demokrasia[democratic party] au from analog to digital.
 
mi pia sijawahi soma hizo makala. ukisoma hapo juu membe kweli katajwa vibaya mara kadhaa. halafu kibanda kahama toka magazeti ya mbowe kwenda ya rostam + lowasa. kumsaidia zaidi lowasa toward 2015 dhidi ya membe na wenzake? motive. lakini hata hivyo malafyale kibanda ni mwandishi wa habari aliyeandika makala nyingi za sampuli hii ambazo zaweza kuwa zimeudhi wengine wengi zaidi ya membe. ni vigumu kujua nani ndo kamfanyia hivi. maadui wake ni wengi. anaweza kuwa yeyote.
 
nchi hii ni mali ya wananchi wa tanzania, tujaribu kuangalia njia ya kuwafanya hawa watu wajue pia sisi tuna roho, tusiishie tu kulalamika kwenye mitandao, haitatusaidia
 
Ukiachilia makala hizo hapo juu, Kibanda pia ni blogger mzuri sana. Blog yake ina makala nzuri fikirishi na chokonozi, huenda nazo zimechangia kumwingiza matatizoni. Fuatilia zaidi blog yake na makala zake HAPA
 
Nionavyo mimi hapo ndio mnatoka nje ya ukweli wa movie. kimsingi issue ya LWAKATARE ilikuwa planned A to Z.If you go through it intelligently utabaini yafuatayo.kuna watu wajanja ndani ya ccm walipanga kuihujumu CHADEMA kisiasa ili kuwasadikisha wananchi kuwa CHADEMA ni chama cha KIGAIDI na hivyo kupunguza nguvu za CDM pia kutokuaminiwa tena na wananchi.Nini kilifuata? ilibidi kwanza wapate video hiyo kwa gharama yoyote halafu mtu mmoja prefarrably mwandishi wa habari adhuriwe.mwandishi gani adhuriwe the choice was easy! KIBANDA. Kwanini yeye? ni kwasababu kwa jujuu kila mtu angefikiri CHADEMA wamemfanyia huo unyama kwasababu amehama kutoka gazeti la mtu wa CHADEMA kwenda kwa ROSTAM (CCM). Nani wa kufanya kazi hiyo? they had no option except the intelligency people.kwasababu hawakutaka kuacha alama yoyote kuwa upande wa pili wamehusika ilibidi wawape watu wenye ujuzi wa kuteka, kutesa na hata kuua haraka sana
Na ndio maana usiku wa kutekwa KIBANDA, ludovick alikuwa ofisini kwake kabla hawaja achana. inaonekana huyu alipewa jukumu la kupeleka taarifa kuwa jamaa anafunga ofisi na kwa hakika anaelekea nyumbani ili watekaji wajiandae na wakamilishe shughuli waliyo tumwa bila kuonekana wakirandaranda kwa muda mrefu.tafsiri ya haraka ni kwamba walitaka ile MOVIE ukweli wake uhalalishwe na mateso ya kibanda.hilo lingewezekana, jamaa wangekuwa mpaka leo hii wanapongezana sana everywhere.saa hizi wamebaki wana laumiana kwanini baadhi yao wameteleza m;paka umma wote umejua kuwa ni KAZI YAO NA UONGO WAO.Usisahau mwanzoni walikuwa wanajinasibu kuwa ile ilikuwa ni clip moja kati ya nyingi walizo nazo!! madhali hii imeshindwa kuwasadikisha watu, hizo zilizo baki hawata zitoa tena kwenye mtandao.kitu kingine kinachoonesha kuwa wameshangazwa na ujinga walio ufanya, huta wasikia tena akina mwampamba,tuntemeke, shonza, mwigulu,na nape wakileta umbea wowote kwenye threads za lwakatare na kibanda watakuwa kimyaaaaaa! ndege mjanja kanaswa na tundu bovu.mwigulu chali,wasira chali,rizone chali na masalia wote hawana hamu tena.
 
Nionavyo mimi hapo ndio mnatoka nje ya ukweli wa movie. kimsingi issue ya LWAKATARE ilikuwa planned A to Z.If you go through it intelligently utabaini yafuatayo.kuna watu wajanja ndani ya ccm walipanga kuihujumu CHADEMA kisiasa ili kuwasadikisha wananchi kuwa CHADEMA ni chama cha KIGAIDI na hivyo kupunguza nguvu za CDM pia kutokuaminiwa tena na wananchi.Nini kilifuata? ilibidi kwanza wapate video hiyo kwa gharama yoyote halafu mtu mmoja prefarrably mwandishi wa habari adhuriwe.mwandishi gani adhuriwe the choice was easy! KIBANDA. Kwanini yeye? ni kwasababu kwa jujuu kila mtu angefikiri CHADEMA wamemfanyia huo unyama kwasababu amehama kutoka gazeti la mtu wa CHADEMA kwenda kwa ROSTAM (CCM). Nani wa kufanya kazi hiyo? they had no option except the intelligency people.kwasababu hawakutaka kuacha alama yoyote kuwa upande wa pili wamehusika ilibidi wawape watu wenye ujuzi wa kuteka, kutesa na hata kuua haraka sana
Na ndio maana usiku wa kutekwa KIBANDA, ludovick alikuwa ofisini kwake kabla hawaja achana. inaonekana huyu alipewa jukumu la kupeleka taarifa kuwa jamaa anafunga ofisi na kwa hakika anaelekea nyumbani ili watekaji wajiandae na wakamilishe shughuli waliyo tumwa bila kuonekana wakirandaranda kwa muda mrefu.tafsiri ya haraka ni kwamba walitaka ile MOVIE ukweli wake uhalalishwe na mateso ya kibanda.hilo lingewezekana, jamaa wangekuwa mpaka leo hii wanapongezana sana everywhere.saa hizi wamebaki wana laumiana kwanini baadhi yao wameteleza m;paka umma wote umejua kuwa ni KAZI YAO NA UONGO WAO.Usisahau mwanzoni walikuwa wanajinasibu kuwa ile ilikuwa ni clip moja kati ya nyingi walizo nazo!! madhali hii imeshindwa kuwasadikisha watu, hizo zilizo baki hawata zitoa tena kwenye mtandao.kitu kingine kinachoonesha kuwa wameshangazwa na ujinga walio ufanya, huta wasikia tena akina mwampamba,tuntemeke, shonza, mwigulu,na nape wakileta umbea wowote kwenye threads za lwakatare na kibanda watakuwa kimyaaaaaa! ndege mjanja kanaswa na tundu bovu.mwigulu chali,wasira chali,rizone chali na masalia wote hawana hamu tena.

mtajikanyaga sana lakini maneno yenu ya kizushi kwenye mtandao hayatamwokoa lwakatare na tuhuma zinazomkabili
 
Binafsi nilimjua Kibanda juu juu ila kwa makala zake ni vigumu Membe kumuacha salama.Kiukweli jamaa anaufahamu wa kutosha na siasa za nchi hii.
 
Ukikubali kutumika, basi stick na bwana mmoja
Ukiamua kubadili, ujue na athari zake.

Ndio game lilivyo.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom