Kesi ya viongozi Chadema yaanza kwa vituko

mdau wetu

JF-Expert Member
Apr 20, 2011
548
58
KESI ya kufanya maandamano bila kibali inayowakabili viongozi wa Chama cha Demokrasia na
Maendeleo (CHADEMA) pamoja na wafuasi wao 19, jana ilianza kusikilizwa huku wafuasi wa chama hicho wakiguna na wakati mwingine wakicheka wakati wakili wa Serikali, Edward Kakolaki akisoma maelezo ya makosa wanayoshtakiwa nayo.

Aidha kesi hiyo ilibidi iahirishwe kwa dakika 10 kutokana na mabishano kati ya Mawakili wa Serikali na mawakili upande wa washtakiwa wakiongozwa na Method Kimomogolo kutokana na wakili wa serikali, Kakolaki kukataa kusaini Mashtaka.

Wakili huyo alikataa kusaini mashitaka ambayo wanakubaliana nayo na yale ambayo wameutaka upande wa Serikali kuwathibitishia kwenye hati ya mashtaka yanayowakabili
washtakiwa hao 19, hatua iliyosababisha Hakimu Charles Magesa kuwapa muda ili wamalize tofauti hizo.

Akisoma hati ya mashitaka, Wakili Kakolaki alisema Januari 3 hadi 5, mwaka huu katika Manispaa ya Arusha, Chadema ilikusudia kufanya mkutano wa hadhara viwanja vya NMC vilivyopo Unga Limited na Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Arusha, Samson Mwigamba alimtaarifu Mkuu wa Polisi wa Wilaya (OCD) Zuberi kusudio hilo la kufanya mkutano huo kwa barua yenye kumbukumbu namba CDM/ AR/ W/10/ 2010 na kuanisha njia watakazopitia.

Kakolaki alisema baada ya kumtaarifu OCD njia watakazotumia ilibainika kuwa si sahihi kuruhusu maandamano hayo kwa vile yangeweza kuleta usumbufu kwa wapita njia kwani hali halisi ya miundombinu ya Jiji la Arusha ni finyu na OCD aliwajulisha Chadema kuwa njia walizochagua si sahihi hivyo wapite njia nyingine lakini walikaidi ushauri huo na kupita njia walizopanga awali katika barua yao.

Hakimu Magesa kabla ya kuahirisha kesi hiyo hadi Novemba 25, mwaka huu alilazimika kutoa
maelezo kwa wafuasi wa Chadema kuwa Mahakama ina taratibu zake na lazima ziheshimiwe kwani imezuka tabia ya watu kucheka, kupiga makofi na wakati mwingine kuzungumza wakati mahakama inaendelea.
 
Back
Top Bottom