George Kahangwa
JF-Expert Member
- Oct 18, 2007
- 547
- 147
HOTUBA YA SHUKRANI YA KUTEULIWA KUWA MGOMBEA URAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA KWA TIKETI YA CHAMA CHA NCCR-MAGEUZI
1 AGOSTI, 2010
Ndugu viongozi wa kitaifa wa chama chetu,
Ndugu wajumbe wa Halmashauri kuu ya Taifa na Mkutano mkuu wa chama,
Ndugu watanzania wenzangu,
Mabibi na mabwana,
Awali ya yote namshukuru Mungu muumba wa mbingu na nchi ambaye katika wakati tusioujua aliamua kutufanya sisi kuwa raia wa nchi iitwayo Tanzania. Namshukuru pia kwa kutujalia sisi uzima hata tukaiona siku ya leo ambayo ni muhimu sana kwa chama chetu na kwa nchi yetu kwa ujumla. Heshima na utukufu apewe yeye katika yote, amina.
Kwa furaha, heshima na unyenyekevu mkubwa kabisa naomba nikushukuruni sana kwa heshima kubwa mlionipatia leo, ya kuwa mgombea wa kiti cha urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa tiketi ya chama chetu cha NCCR- Mageuzi katika uchaguzi unaotarajiwa kufanyika mwishoni mwa mwezi Oktoba, mwaka huu 2010. Ninapoitafakari heshima hii, naona sina namna yoyote ya kuwashukuru vya kutosha, zaidi ya kuipeperusha vema bendera ya chama chetu, kupambana kufa na kupona hadi kukipatia chama chetu ushindi katika nafasi mliyoniteua kuigombea, na hatimaye kulipa taifa utumishi bora kabisa kwa kutumia akili, nguvu, maarifa na bidii ya kazi.
Watanzania wenzangu,
Naomba nitoe shukrani zangu pia kwa uongozi wa kitaifa katika mambo mengi; kwanza kwa kukubali kunipatia fomu ya chama pale nilipoamua kuomba kugombea urais. Vile vile naushukuru uongozi wetu kwa kufanya maandalizi ya mkutano wetu wa leo na kuufanikisha kwa kiwango cha juu kabisa. Pamoja na shukrani nawapongezeni sana, maana natambua magumu mliyopitia katika kuhakikisha mnakiandaa chama kushiriki vilivyo katika uchaguzi mkuu ulioko mbele yetu.
Nitoe shukrani zangu pia kwa familia yangu, mke wangu mpendwa pamoja na wana na mabinti zetu, jamaa zangu na marafiki, kwa kuniunga mkono kwa dhati tokea nilipoamua kugombea hata sasa ninapopewa rasmi ridhaa ya chama changu. Nasema tena, ahsanteni sana tena sana.
Ni imani yangu kwamba tutaendelea kushirikiana sote tangu sasa hata mwisho wa mchakato mzima wa uchaguzi, na hata baada ya uchaguzi. PAMOJA TUTASHINDA!
Ndugu wanamageuzi na watanzania wenzangu,
Naomba nitumie fursa hii kutoa ujumbe kwa watanzania wote, japo kwa ufupi juu ya yale ninayoyakusudia kuyafanya kupitia serikali tutakayoiunda endapo watanzania mtanipatieni dhamana ya kuwa kiongozi mkuu wa taifa letu la Tanzania.
Kwa muda wa miaka mingi taifa letu limekuwa na mapungufu makubwa katika mfumo wa kiuongozi na kiutawala. Mapungufu hayo yametokana na uwepo wa kanuni na taratibu za kikatiba zisizokuwa na manufaa kwa watanzania wote bali kwa kundi la watu wachache wanaodhani kwamba wao wana hati-miliki ya kuliongoza taifa hili na mawazo yao tu ndio yanayostahili kuheshimiwa na kufuatwa.
Ndugu zangu watanzania, wakati umefika wa kuondokana na katiba inayotambua itikadi ya chama kimoja katika nchi yenye mfumo wa vyama vingi; wakati umefika wa kuondokana na katiba iliyojazwa viraka ambavyo ni matokeo ya watu wachache kutaka kulinda nafasi zao za madaraka; wakati umefika wa kuondokana na katiba na taratibu zinazokifanya chama kinachounda serikali iliyoko madarakani kigeuke kuwa chama dola. Wakati ni huu wa kuachana na katiba inayotoa haki za binadamu kwa mkono wa kushoto na kisha kumnyanganya mtanzania haki hizo kwa mkono wa kulia.
Ni kwa sababu hii natangaza wazi kwamba, endapo watanzania mtanichagua kuwa rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mimi pamoja na serikali ya umoja wa kitaifa tutakayoiunda, tutaanzisha mchakato wa kulipatia taifa hili KATIBA MPYA ndani ya kipindi cha miezi 18; hii itakuwa ni katiba inayotokana na watanzania wenyewe na inayozingatia matakwa yao na maslahi ya kila mwana taifa hili.
Sanjari na upatikanaji wa katiba mpya, punde tu tutakapoingia madarakani, huo utakuwa mwanzo wa kufutwa kwa sheria zote kandamizi, sheria ambazo zinazominya haki za raia, badala yake kila sheria katika nchi hii itakuwa ni ile tu isiyokinzana kwa namna yoyote ile na haki za mwanadamu.
Ndugu zangu watanzania, kwa kadri tunavyoendelea na mchakato huu wa uchaguzi, nitazungumza kwa upana na kwa kina juu ya mipango yetu mbali mbali ya kufanya mageuzi makubwa ya kiuchumi na katika utoaji wa huduma za jamii.
Lakini kwa kuanzia, leo hii ninao ujumbe mfupi kwa ajili ya wakulima, wafanyakazi na wajasiriamali wazalendo wa taifa letu.
Ndugu zangu wakulima, ninyi mlio wadau wakuu katika sekta muhimu sana hapa nchini, sekta ya kilimo. Ninyi ni mashahidi wa jinsi serikali iliyoko madarakani, licha ya mbwembwe nyingi za kisiasa, nahau na misemo, imeshindwa kabisa si tu kuinua maisha ya mkulima, bali kwa miaka takribani hamsini sasa imekosa uwezo wa kuendeleza kilimo hapa nchini. Wakati umefika wa kuifanya hali hiyo kuwa historia.
Nitamke wazi kwamba, mara baada ya kuingia madarakani, serikali nitakayoiunda pamoja na mambo mengine kwa makusudi mazima itaweka utaratibu wa kuwapatia nyenzo na uwezo wakulima ili kuwatoa katika ukulima wa viwango duni, na kuwaingiza katika UKULIMA WA KISASA na wa viwango. Sambamba na hilo tutaanzisha mipango ya kilimo cha umwagiliaji nchi nzima (huo utakuwa mwisho wa kilimo cha kutegemea hali ya hewa), vile vile tutawezesha kufanyika kwa tafiti za kitaalam, zinazolenga kuwapatia wakulima utaalam wa kutosha, mbegu bora, mazao mengi tena yenye ubora wa hali ya juu.
Ndugu zangu wakulima, serikali yangu itafanya kila inaloweza kuwamilikisheni mashamba makubwa, kwa kutambua kwamba hii ndio nyenzo kuu ya mkulima. Hapa tunakusudia kumtajirisha mkulima, maana kama tusemavyo watanzania; ardhi ni mali. Chini ya serikali iliyoko madarakani, ardhi imefanywa kuwa aghali kiasi kwamba mkulima wa kitanzania hawezi kumudu kumiliki shamba lenye ukubwa wa kumuinua kimaisha. Mwisho wa hali hiyo umewadia. Aidha baada ya kukabidhiwa madaraka, nitahakikisha kwamba mkulima anakuwa na uhuru katika uuzaji wa mazao yake, tofauti na ilivyo sasa ambapo wakulima wanabanwa na serikali pasipo sababu za msingi na wananyonywa sana na walanguzi wa mazao. Tumedhamiria kabisa kupanua wigo wa soko la mazao ya shambani; soko la ndani na la nje ya nchi ili kuwaondoa wakulima wetu katika lindi la umaskini.
Ndugu zangu wafanyakazi, naomba kuweka msisitizo katika kauli yangu niliyoitoa hivi juzi kuhusu nia yangu ya dhati ya kuhakikisha serikali nitakayoiunda inasikiliza mara moja kilio cha muda mrefu cha wafanyakazi kuhusiana ma maslahi yenu. Wakati umefika wa kutumia kwa busara pato la taifa ili ninyi wazalishaji katika sekta mbalimbali na watoa huduma kwa jamii muweze kufaidi matunda ya jasho lenu. Wakati umefika wa kuwangoa madarakani viongozi wanaodiriki kuwalipa fadhila kwa kejeli na matusi na hata kuzikataa kura zenu wazi wazi ati kwa sababu mnadai haki yenu ya kuwa na kipato kinachotosheleza. Naamini kabisa hamko tayari kuendelea kuongozwa na serikali ambayo imeyafanya maisha ya mfanyakazi yawe ya tabu na dhiki katika kila hali. Nimetamka wazi na leo narudia tena, punde tu tutakapoingia madarakani kima cha chini cha mshahara hakitapungua shilingi za kitanzania 315,000/­-. Wakati huo huo serikali yangu itaendelea kutathmini hali halisi ya maisha kwa lengo la kuhakikisha kwamba enzi za kumtaabisha mfanyakazi zinafikia kikomo. Waliokaa madarakani kwa takribani nusu karne sasa, hili limewashinda si tu kwa sababu hawana maono ya kulifanya bali wamefungwa na fikra potofu, kwamba anayestahili maisha bora ni mwanasiasa na familia yake.
Ndani ya chama chetu tunatambua kwamba malipo duni kwa wafanyakazi ni sehemu ya uvunjufu wa haki za binadamu, na ni dhambi inayomtia majaribuni mtu ili atende dhambi nyingine ya kukosa uaminifu mahali pake pa kazi. Hatuwezi kuendelea na dhambi hii.
Ndugu zangu watanzania, sote tunajua kwamba kwa muda mrefu taifa letu limepoteza wataalam, wazalendo wanaoshawishika kwenda kuyatumikia mataifa ya kigeni kwa sababu ya serikali kushindwa kuboresha maslahi na mazingira ya kazi hapa nyumbani. Hatuwezi kuendeleza ujinga huo wa kuipoteza raslimali muhimu ambayo ina uwezo wa kuliletea taifa letu maendeleo makubwa ya kiteknolojia, kiuchumi na kijamii. Watanzania wenzangu mlioko nje ya nchi, kaeni tayari, maana wakati umefika wa kuziondoa push factors zilizotufikisha katika tatizo hili.
Ndugu zangu wajasiriamali wazalendo, ninaheshimu na kutambua mchango wenu mkubwa katika ujenzi wa taifa hili. Hata hivyo taifa letu limekuwa na bahati mbaya ya kuwa na viongozi wanaoendelea kuuweka uchumi wa nchi mikononi mwa wa wageni kwa kisingizio cha uwekezaji, na kutusukuma wazawa mbali kabisa na uchumi wa nchi yetu wenyewe. Napenda niseme kwa msisitizo kabisa, kwamba wakati umefika wa kuweka sehemu kubwa ya njia kuu na ndogo za uchumi mikononi mwa wananchi. Huu ndio sisi wanamageuzi tunaouita UWEZESHAJI, yaani, popote litakapozungumzwa suala la uwekezaji, kanuni yetu itakuwa; MTANZANIA KWANZA. Katika hili tutawahimiza watanzania waliowengi kutafuta kwa bidii fursa zozote za kiuchumi hapa nchini na kushiriki kuzimiliki. Sanjari na hilo tutatoa elimu ya kuwajengea wananchi wetu ujasiri na kuwaonesha kila fursa zote zilizopo.
Ndugu zangu watanzania, yapo masuala mengi ya kiuchumi ambayo ninaendelea kuyafanyia maandalizi na kuyaweka katika programu rasmi ambazo serikali yangu itazisimamia. Kimsingi mipango yetu ya kiuchumi italenga pamoja na mambo mengine kuinua thamani ya shilingi ya Tanzania. Binafsi nimekuwa nikisikitishwa sana na kuporomoka kwa kasi kwa shilingi yetu. Sote tumeona wazi jinsi serikali iliyoko madarakani ilivyoshindwa kuifanya shilingi yetu iwe imara na yenye nguvu. Ni aibu tupu kwa taifa letu kuwa na fedha yenye thamani ndogo inapolinganishwa na fedha za nchi ambazo hazina utajiri wa maliasili kama ambao Mwenyezi Mungu amelijalia taifa letu. Ni aibu kubwa kabisa kwamba ndani ya kipindi cha miaka ya kujitawala kwetu shilingi imeporomoka kutoka uwiano wa dola moja ya kimarekani kuwa sawa na shilingi tano, hadi dola hiyo kwa sasa kuwa sawa na shilingi za kitanzania elfu moja na mia tano! Yaliyotufikisha hapo ni mengi, na bila kuyadhibiti tunakoelekea ni kubaya zaidi. Mojawapo ya sababu za jambo hili ni serikali iliyoko madarakani na watangulizi wao kushindwa kuuheshimu utamaduni wetu na kuthamini bidhaa zinazozalishwa hapa nchini. Kwa mfano mdogo tu, tumekuwa na serikali yenye fikra za kijinga kwamba katika nchi iliyojaliwa misitu mingi tunayoweza kuitumia kuvuna mazao mengi zikiwemo mbao bora kabisa na kutengeneza samani za hali ya juu, serikali inaona itumie fedha za kigeni kuangiza meza na viti vilivyotengenezwa kwa vumbi la mbao huko ngambo. Huu ni ujinga uliokithiri.
Ndugu zangu, dunia iko katika uchumi wa ushindani, hatuwezi kuendelea kuwa wasikilizaji na mashabiki katika mashindano hayo. Kwa sababu hiyo serikali yangu italenga kuondokana na uagizaji wa bidhaa kutoka nje pasipo sababu za msingi. Mpango wetu ni kulifikisha taifa katika hatua ya kuwa wapelekaji bidhaa nje kwa wingi kuliko tunavyoagiza (more imports than exports). Hili litafanyika kitaalam sana ili uchumi wetu uwe imara.
Ndugu zangu watanzania, wakati nikuchukua fomu ya kuomba kugombea urais nilitangaza nia yangu ya kuanzisha mpango kabambe uitwao MWANZO WENYE NGUVU. Mpango huo malengo yake ni kujenga taifa lenye uadilifu, lenye afya na lenye watu waliopewa elimu bora kabisa ili tuwe taifa la watu wenye kuleta maendeleo yetu binafsi na maendeleo ya nchi kwa ujumla.
Naomba nirudie kuufanua mpango huu leo, japo kwa ufupi.
Ndugu zangu, katika mpango huu kila mtanzania ni wa thamani kubwa tokea kutungwa kwa mimba yake tumboni mwa mamaye hadi Mungu atakapomtwaa.
Kwa maana hiyo mpango wetu utalenga kushirikiana na akinamama wote, wanaotarajia kuwaleta duniani watazania wenzetu, ili mtoto alelewe vyema akiwa tumboni, ahudumiwe vyema anapozaliwa, ahakikishiwe kupata elimu bora, aepushwe kuishi katika mazingira magumu, na hatimaye ajengwe kimaadili, kiafya na kiakili ili atumie vipaji vyake kujiletea maendeleo binafsi na kulitumikia taifa kwa kiwango cha juu kabisa. Kwa mantiki hiyo mpango huu utapiga marufuku utoaji mimba; utaboresha huduma za mama na mtoto, utashirikiana na familia zote katika malezi, utakomesha uwepo wa watoto wa mtaani, utapambana na tatizo la mfubao wa akili. Kwa maneno mengine, pale palipo mtoto yeyote wa kitanzania na serikali itakuwepo.
Mpango wa mwanzo wenye nguvu, utampeleka kila mtoto wa kitanzania katika shule bora kabisa za awali. Kadhalika tutaifanya elimu ya msingi ijitosheleze, yaani kufanya mhitimu wa elimu hiyo awe na maarifa na stadi za kuendesha maisha yake kwa mafanikio na kulitumikia taifa.
Katika elimu ya juu, pamoja na mambo mengine, tutaondokana na mpango wa serikali ya sasa wa kupuuza kuwapa watanzania udhamini wa kusoma shahada za uzamili na uzamivu. Hatuwezi kuendelea kufurahia kuwa na takwimu za majengo ya vyuo vikuu wakati vyuo hivi havina wataalam wa ufundishaji na utafiti. Natamka bayana, kwamba mara tu baada ya kuingia madarakani serikali yangu itatenga fedha za kutosha kwa ajili ya kuwasomesha watanzania wenye sifa katika viwango hivyo vya elimu, tofauti na ilivyo sasa ambapo serikali inatoa mikopo kwa wanafunzi wa shahada ya kwanza, tena kwa kwa njia inayojenga ubaguzi.
Wataalam wetu wachache mlioko katika vyuo vikuu, tunafahamu jinsi serikali ilivyowalazimisha kuhangaika huku na kule kutafuta fedha za tafiti kwa wafadhili ili mtimize majukumu yenu. Sisi tunawatangazieni mpango wetu wa kuzithamini na kuzitumia tafiti mbalimbali mnazozifanya. Tutafanya hivyo kwa kuwawezesha kinyenzo, kufanya utafiti wenyewe na hatimaye kuwa nanyi bega kwa bega katika kufikisha matokeo yake kwa sekta lengwa.
Ndugu zangu watanzania, lengo kuu la serikali yangu litakuwa ni KUIFUNUA SIRI YA MAENDELEO; yaani kumwendeleza mtanzania mmoja mmoja. Ninatambua kuwa siri hii ya maendeleo haiwezi kufunuliwa sawasawa bila kuwa na kuboresha miundombinu.
Kwa sababu hiyo, tutapania kabisa kuliondolea taifa utaratibu wa kujenga miundombinu ya taifa, matharani barabara kwa vipande vipande. Badala yake tutaanzisha mpango endelevu wa muda mrefu utakaoziweka kwanza barabara zote zinazohitajika katika nchi hii katika mpango unaofahamika kwa watu wote, kisha tutaweka muda (timeframe) ambao bila shaka utakuwa mrefu kidogo, wa lini nchi nzima itakuwa na barabara za uhakika zitakazowezesha shughuli za kiuchumi na kurahisisha utoaji wa huduma za jamii. Awamu ambatano ya mpango huo, itakuwa ni utaratibu usiokoma wa ukarabati.
Ndugu watanzania, mapambano tunayoyaendea ni kuangamiza Ufisadi, umaskini na yale yote ambayo yamekuwa maadui wakuu wa taifa letu. Naamini ilani yetu itazingatia yote hayo. Nami kwa moyo mmoja nitaitangaza kila pembe ya nchi, na hatimaye kwa pamoja tusherehekee ushindi.
Mungu ibariki Tanzania.
Ahsanteni tena na tena
Hashim Rungwe,
Mgombea urais