Kakke
JF-Expert Member
- Dec 4, 2010
- 1,883
- 1,482
Kulingana na taarifa iliyotolewa na mwenyekiti wa taasisi hiyo ya TI, Jose Ugaz, takwimu hizo zimelinganisha viwango vya uwajibikaji na udhibiti wa rushwa katika sekta ya umma.
Jana tulichapisha habari kuhusu Tanzania kushuka katika orodha ya nchi zinazofanya jitihada za kupambana na rushwa, baada ya taasisi inayochunguza masuala hayo, Transparency International (TI) kueleza kwamba imeshuka kwa nafasi nane kutoka ya 111 mwaka jana hadi ya 119 mwaka huu kati ya nchi 175 zilizolengwa.
Kulingana na taarifa iliyotolewa na mwenyekiti wa taasisi hiyo ya TI, Jose Ugaz, takwimu hizo zimelinganisha viwango vya uwajibikaji na udhibiti wa rushwa katika sekta ya umma.
Pamoja na Rwanda iliyokuwa katika nafasi ya 49 mwaka jana kushuka hadi nafasi ya 55 mwaka huu, nafasi ya 119 inayoshikiliwa na Tanzania inaonyesha pasipo kuacha chembe ya shaka kwamba jinamizi la rushwa linaiporomosha nchi kwa kasi kuelekea kwenye maangamizi. Ripoti hiyo inaitaja Botswana kuwa nchi inayofanya vizuri zaidi katika Bara la Afrika kwa kushika nafasi ya 31.
Kwa mujibu wa IT, rushwa imekuwa kikwazo kikubwa cha upatikanaji wa haki na maendeleo ya kiuchumi na imepoteza kabisa imani ya wananchi kwa serikali na viongozi wao, hasa kutokana na kukosekana kwa huduma bora za elimu na afya.
Maana yake ni kuwa, jamii ambayo inashindwa kupata elimu bora inayokidhi viwango vinavyokubalika au jamii isiyokuwa na uhakika wa ustawi wake wa kupata lishe bora na tiba, kamwe haiwezi kujikwamua katika maisha duni kwa kuwa chanzo cha hali hiyo ni kujikita kwa mifumo ya rushwa na kutokuwapo kwa utashi wa dhati wa kisiasa miongoni mwa viongozi walio madarakani.
IT inasema pia kwamba chaguzi ambazo watu wanazotumia fedha nyingi kupata madaraka, ni tatizo kubwa linalofanya rushwa ikue zaidi katika jamii.
Hiyo ndiyo hali halisi hapa nchini. Jitihada za wananchi kupata Katiba mpya inayoweza kujenga uadilifu, uwajibikaji na kukomesha vitendo vya rushwa miongoni mwa viongozi zimekwamishwa na mifumo hasi ya kisiasa na kiserikali, hivyo kusababisha kupatikana kwa Katiba Inayopendekezwa isiyotoa suluhisho la maovu hayo.
Wananchi sasa wamegundua kwamba walifanya makosa makubwa kukubali Bunge Maalumu la Katiba liundwe kutokana na wanasiasa na watu wengine wenye masilahi ya moja kwa moja na Katiba hiyo.
Matokeo yake ni kwamba wajumbe hao walifuta vifungu katika Rasimu ya Mabadiliko ya Katiba (iliyotayarishwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba) walivyoona vinagusa au kuhatarisha masilahi yao binafsi.
Walifuta vifungu vilivyomwondolea Rais madaraka makubwa; vilivyosimamia uadilifu wa viongozi; vilivyowapa wananchi madaraka ya kuwawajibisha wabunge; vilivyoweka ukomo wa ubunge; vilivyotaka mawaziri wasitokane na wabunge; vilivyosimamia mgawanyo wa madaraka kwa mihimili ya dola; mikataba ya gesi, mafuta, madini na ardhi kupelekwa bungeni; miiko ya viongozi na mgongano wa masilahi.
Vingine vilivyofutwa ni elimu ya kidato cha nne kwa wabunge; zawadi wanazopewa viongozi kusalimishwa serikalini; na vifungu vingine vilivyolenga kukuza utawala bora na kujenga uadilifu wa viongozi.
Ndiyo maana wananchi wengi wanaona Katiba Inayopendekezwa kama kichaka cha walarushwa na mafisadi. Jambo la kushangaza ni kwamba hata kamati iliyopewa jukumu la kuandika Katiba Inayopendekezwa ilikuwa na wajumbe ambao wametiliwa shaka kwa kuhusishwa na kashfa kubwa kadhaa.
Kupuuzwa kwa mambo yaliyotajwa hapo juu hakutasaidia nchi kuondoka mkiani mwa orodha hiyo ya aibu, badala yake wananchi wataendelea kuteseka.
Chanzo: Tanzania Daima