Kandoro alitumia silaha; MR. II hakutumia silaha

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797

picture-10.jpg

Na Mwandishi Maalum - Imechapwa 16 November 2011

WAKAZI wa Jiji la Mbeya kwa mara ya kwanza wiki iliyopita walishuhudia filamu ya aina yake. Ilikuwa kama kushuhudia mapambano kupitia luninga, mapambano ya wenye silaha na wasio na silaha.

Ilikuwa kama kushuhudia majeshi ya Waisrael wenye silaha kali wakitwangana na Wapalestina wanaotumia mawe na silaha nyingine dhaifu ili kujihami na kulipiza kisasi.

Ndivyo ilivyokuwa katika Jiji la Mbeya. Uongozi wa mkoa, katika juhudi za kuzima vurugu zilizoanzishwa na wamachinga ilipeleka polisi, waliposhindwa haraka ukaita askari wa Kikosi cha Kuzuia Ghasia (FFU), nao waliposhindwa Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) na baadaye Jeshi la Wananchi (JW) ili kuokoa jahazi.


Walifyatua risasi huku wamachinga wakirusha fimbo na mawe. Askari wa serikali walitumia kila aina ya silaha walizokuwa nazo huku wamachinga wakikwepa risasi, maji ya washawasha na mabomu ya machozi huku wao wakirusha mawe.


Ilikuwa vita iliyodumu takriban saa 30 baina ya askari wa serikali wenye mafunzo ya kivita na wafanyabiashara ndogondogo wanaotafuta haki ya maeneo ya kufanyia biashara zao. Mkuu mpya wa mkoa, Abbas Kandoro na mkurugenzi mpya wa Jiji la Mbeya, Wilson Kabwe waliohamishwa kutoka Mwanza, na mkuu wa wilaya Evance Balama aliyetokea Ilala, hawataki kuwaona wamachinga eneo la Mwanjelwa.


Wakatuma mgambo kuwaondoa. Wamachinga wakawa wanagoma. Ikawa balaa. Vipigo, pingu, mahabusu. Wamachinga walikuwa wakiwazunguka askari wa serikali kwa kuhama kutoka sehemu moja kwenda nyingine huku wakichoma matairi na kuziba barabara kwa mawe makubwa hali iliyosababisha barabara za maeneo ya Mwanjwelwa, Kabwe, na Soweto kuelekea Uyole zisipitike.


Ukweli vurugu hizo kubwa ambazo hazijawahi kutokea jijini Mbeya zililizidi nguvu jeshi la polisi na kulazimika kuomba msaada kutoka mikoa ya jirani.

Aliyefanikiwa kutuliza vurugu zile hakuwa kiongozi wa serikali ya mkoa wala askari wazoefu wa vita isipokuwa Mbunge wa Jimbo la Mbeya, Joseph Mbilinyi maarufu kama Mr. II.


Chanzo cha vurugu ni hicho lakini, Serikali ya mkoa wa Mbeya inasingizia siasa. Inadai vurugu hizo zilipangwa muda mrefu na watu waliokuwa wanatafuta upenyo wa kufanya vurugu hizo.


Ushahidi alioshikiliza Kandoro eti ni wingi na ukubwa mawe yaliyowekwa barabarani na idadi kubwa ya matairi yaliyochomwa barabarani. Eti kwake hiyo inadhihirisha kulikuwa na maandalizi ya muda mrefu ya kufanya vurugu. Kwa nini polisi hawakuyatoa kama waliona muda mrefu?


Halafu anajijitetea kwamba vurugu hizo zilitokea wakati mazungumzo yalikuwa yanaendelea kati ya Halmashauri ya Jiji la Mbeya na uongozi wa wamachinga kuhusiana na sehemu wanayoweza kufanyia shughuli zao bila ya kuleta usumbufu kwa watumiaji wengine wa barabara.


Aidha, anadai kuwa hadi vurugu hizo zinatokea tayari kulikuwa na mazungumzo yamefanyika na viongozi wa machinga na jiji na walikubaliana kuwa juzi Jumatatu wangeoneshwa eneo la kufanyia shughuli zao kwa uhuru na bila kuathili shughuli za watu wengine.


Serikali ya mkoa inakwenda mbali na kuhusisha vurugu hizo na masuala ya kisiasa ambapo Kandoro anadai alistushwa na kuchomwa kwa bendera za Chama Cha Mapinduzi (CCM) na kupandishwa kwa bendera za CHADEMA.


Hisia za Kandoro zinahanikizwa zaidi na mabango yaliyokuwa yamebebwa na vijana yakiwa na ujumbe kama "Mbeya ni nchi, Rais Sugu" ambaye anatambulika kwa jina la Joseph Mbilinyi Mbunge wa Jimbo la Mbeya Mjini.


Vilevile, kitendo wananchi kukataa kumsikiliza Mkuu wa wilaya ya Mbeya, Evance Balama ilitafsiriwa pia ni dharau yenye mwelekeo wa kisiasa.


Hasira za vijana hao na kupambana kwao kwa nguvu bila kuchoka dhidi ya polisi hao inadaiwa kuchochewa na vitendo vya unyanyasaji na rushwa na kubambikiwa kesi vinavyofanywa na askari dhidi ya vijana.


Baadhi ya wakazi wa Jiji la Mbeya, wamelishutumu Jeshi kwa kutumia nguvu kupita kiasi katika kukabiliana na vijana waliokuwa wakifunga barabara kwa mawe na kuchoma matairi barabara hali ambayo inadaiwa ilichochea vurugu zaidi baada ya vijana kuona wenzao wakiwa wamekamatwa.


Ufyatuaji ovyo wa risasi za moto na mabomu ya machozi kunadaiwa kusababisha kujeruhiwa kwa watu ambao hawakuwepo katika vurugu. Baadhi ya majeruhi walipigwa risasi wakiwa katika maeneo yao biashara.


Hata hivyo, Kaimu Kamanda wa polisi Mkoa wa Mbeya, Anaclet Malindisa anapinga shutuma hizo akidai kuwa polisi walitumia nguvu kidogo na kwamba kama ingebidi kuongeza nguvu wangefanya hivyo ili kudhibiti vurugu hizo ambazo zilikuwa zimewazidi.


Kamanda Malindisa anatoa maelezo haya kana kwamba wakazi wa Mbeya hawaoni. Katika kudhihirisha kuwa polisi walizidiwa nguvu na vijana waliokuwa wakifunga barabara na kufanya vurugu bila kufanya uhalifu wa kubomoa maduka na biashara kama ilivyozoeleka, polisi walilazimika kuomba msaada kwa JKT na JW ambao kwa kiasi fulani walisaidia kudhibiti vurugu hizo.


Athari za vurugu hizo zilizodumu kwa takribani siku mbili ni kubwa. Kwanza zimesababisha kifo cha mtu mmoja, majeruhi 17 wakiwemo watano kwa risasi za moto na wengine 12 walioumia wakati wakikimbia huku zaidi ya 370 wakikamatwa na polisi kwa kuhusika katika vurugu hizo.


Pili vurugu hizo zimekuwa na athari za kiuchumi na kijamii. Kwa takriban siku mbili biashara na shughuli nyingine za kiuchumi zilisimama huku kukiwa hakuna mawasiliano kwa njia ya barabara kati ya katika ya Jiji na Uyole.


Jambo lililowazi ni kwamba mbinu za kutuliza ghasia zimempandisha chati Mr. ii. Huyo ndiye alifanikiwa kuzima vurugu hizo kwa kauli siyo silaha.

Akihutubia maelfu ya watu waliokusanyika katika kituo cha mabasi cha Kabwe, Mbunge huyo na msanii mkongwe wa muziki wa kizazi kipya, alisema kwamba vurugu hizo zinapaswa kuwa fundisho kwa polisi kuwa matatizo ya wamachinga si ya kuyaendesha kisiasa bali yanahitaji kuyamaliza kisayansi kwa hali ya juu.

"Nyinyi ni raia wema mlioamua kuacha kukaba na kuzunguka kutwa nzima na kamba mkiuza, ni vema mkapewa nafasi mkasikilizwa kwa kuwa mnatafuta riziki kwa njia halali" alisema Mr. ii katika mkutano huo huku akishangiliwa kwa nguvu na maelfu ya vijana waliojazana katika kituo hicho.


Kichekesho ni kwamba wakati mkuu wa mkoa ambaye ni mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama aliamua kuagiza Jeshi la Ulinzi kuwarushia magruneti wananchi na mkuu wa wilaya kupuuzwa, Mr. ii hakutumia silaha.


Hiyo imetafsiriwa na baadhi ya watu kuwa serikali ya mkoa ilishindwa kulimaliza suala hilo kwa njia sahihi na kwamba jambo hilo limesaidia kumjenga kisiasa Mr. ii ambaye alitumia muda mfupi kumaliza mgogoro huo kidiplomasia.



 
The key to successful leadership today is influence, not authority... More Power to U Mr. II - That show us whose a TRUE LEADER...



 
Siku zote mwanafunzi mtukutu, mwalimu mbaya ndiye mzuri kwake; na kinyume chake. Watu hushabihiana na huelewana kutokana na tabia na matendo yao.
 
Back
Top Bottom