Joto laanza kupanda kesi ya Mramba

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,319
33,125
WAZIRI wa zamani wa Fedha, Basil Mramba amekiri kuombwa ruhusa na aliyekuwa Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Daud Ballali, kusaini mkataba na kampuni ya Alex Stewart (Asseyers) Government Business Corporation.

Pia amekiri kumwandikia barua Waziri wa zamani wa Nishati na Madini, Daniel Yona, akimweleza kuwa matumizi ya fedha za Serikali mwaka 2003/04 hayakutengewa fungu la kumlipa mkaguzi wa dhahabu (Alex Stewart) na hivyo wakati huo asingeweza kutoa fedha kwa ajili hiyo.

Hayo yalibainika jana katika mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam, katika kesi inayowakabili ya matumizi mabaya ya madaraka na kuisababishia Serikali hasara ya Sh bilioni 11.7, iliyokuwa mbele ya jopo la mahakimu wakazi John Utamwa, Sam Rumanyika na Saul Kinemela.

Kupitia kwa mawakili wao, Hurbert Nyange, Leonard Shahidi, Joseph Tadayo na Peter Swai wanaowatetea pamoja na Katibu Mkuu wa zamani Hazina, Gray Mgonja, washitakiwa hao walikiri pia kuhojiwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru).

Juzi Wakili Mwandamizi Fredrick Manyanda, aliwasomea maelezo ya awali washitakiwa hao na kudai kuwa kabla ya kufikishwa mahakamani walihojiwa na Takukuru na kukiri kutenda kosa, lakini mawakili wa utetezi walikanusha na kudai kuwa wateja wao hawajahi kuhojiwa mahali popote.

Jana mawakili hao wote walikubali kuwa wateja wao walikuwa ni viongozi wenye nyadhifa kubwa serikalini na wanakubaliana kwamba walipaswa kuwa waadilifu, waaminifu na kutimiza wajibu wao kwa mujibu wa sheria.

Yona na Mgonja jana walidai wanakubali maelezo yaliyotolewa na upande wa mashitaka yaliyo kwenye vielelezo namba moja mpaka nane na kwamba walihojiwa na Takukuru, ila hawakutoa maelezo mengine.

Baada ya hapo, washtakiwa hao waliiambia mahakama kuwa wanakubaliana na maelezo yaliyotolewa na mawakili wao na kuyasaini.

Wakili wa Serikali Stanslaus Boniface aliiomba mahakama kuahirisha shauri hilo kwa sababu orodha waliyokuwa nayo mahakamani jana ina mashahidi 25 ila kwa sababu jopo hilo wakati linarekodi maelezo ya awali kwa mujibu wa sheria, walijikuta wakitakiwa kupunguza idadi ya mashahidi, hivyo akaomba iahirishwe ili warudi ofisini kupunguza idadi hiyo kuzingatia uzito wa mashahidi.

Ombi hilo lilikubaliwa na kiongozi wa jopo, Utamwa, na kuahirisha kesi hadi Septemba 22 mwaka huu, upande wa mashtaka utakapotoa idadi ya mashahidi na vielelezo vitakavyotumika na kwamba endapo siku hiyo itaangukia sikukuu ya Iddi, kesi hiyo itaendelea siku ya kazi inayofuata.


Source: http://www.habarileo.co.tz/kitaifa/?n=3637
 
Back
Top Bottom