Jamani hii imekaaje jk AOMBA MIALIKO

Jan 16, 2007
721
176
H@ki Ngowi: Matumizi Mabaya ya Jina la Mheshimiwa Rais Kwenye Matangazo na Mialiko Mbalimbali

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Ofisi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, imekuwa ikipokea mamia kwa mamia ya mialiko ya kumwomba Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete kushiriki katika shughuli mbali mbali za wananchi ziwe za maendeleo, ama za sherehe, ama za kidini ama nyinginezo.

Ofisi ya Rais inaiona mialiko hiyo kwa Mheshimiwa Rais kuwa jambo zuri na jema linaloonyesha mahusiano mazuri kati ya Mheshimiwa Rais na wananchi. Ofisi ya Rais inawaomba wananchi, taasisi na vikundi mbali mbali kuendelea kutuma mialiko yao ya kumwomba Mheshimiwa Rais kushiriki katika shughuli zao.

Kutokana na mialiko hiyo, tokea kushika uongozi wa nchi yetu Mheshimiwa Rais ameshiriki katika mamia ya shughuli zikiwamo za kufungua miradi ya maendeleo – kama vile miradi ya elimu, miradi ya afya, miradi ya barabara na miundombinu mingine, harambee za kuchangisha fedha kwa ajili ya kutekeleza miradi mbali mbali nchini na shughuli nyingine nyingi za kuleta maendeleo ya wananchi. Miradi hiyo imebuniwa na kutelekezwa na taasisi na watu wa madhehebu mbali mbali ya kidini, Kiserikali na taasisi zisizokuwa za Kiserikali.

Ofisi ya Rais inachukua nafasi hii kuwapongeza watu ambao wamebuni na kufanikisha miradi hiyo. Ofisi ya Rais pia inapenda kuwathibitishia wananchi, kwa mara nyingine tena, kuwa Mheshimiwa Rais Kikwete anafurahishwa na ushiriki wakati katika uzinduzi wa miradi hiyo. Ataendelea kufanya hivyo bila kuchoka kwa sababu maendeleo ya wananchi ni jambo lililoko moyoni mwake na ni jadi ya imani yake ya kisiasa.

Mheshimiwa Rais kwa kadri muda na nafasi yake ilivyoruhusu amekubali kushiriki katika shughuli hizo za wananchi. Utaratibu uliopo ni kwa waombaji kupeleka baura za maombi kwa Katibu wa Rais, Ofisi ya Rais, Ikulu ama kufikisha maombio hayo kwa Katibu wa Rais kupitia Wizara husika.

Ofisi ya Rais kwa kuzingatia ratiba ya shughuli za Rais ndiyo yenye dhamana ya kutoa majibu kwa waombaji kama inawezakana Mheshimiwa Rais kushiriki katika shughuli aliyoombewa ama haiwezekani, kutegemea na nafasi ilivyo katika ratiba ya shughuli za Mheshimiwa Rais. Ni baada ya kupokea majibu na uthibitisho kutoka Ofisi ya Rais, ndipo mwombaji anaweza kutoa matangazo kuhusu kushiriki kwa Mheshimiwa Rais kwenye shughuli waliyompangia kufanya, na siyo vinginevyo.

Tunasikitika kusema kwamba katika siku za karibuni wamejitokeza baadhi ya watu na taasisi ambazo zinakiuka kwa makusudi utaratibu huo uliowekwa na hivyo kutumia vibaya fursa ya kumwomba Mheshimiwa Rais kushiriki katika shughuli zao wanazopanga kuzifanya.
Watu hao na taasisi hizo zimekuwa zikitangaza katika vyombo vya habari ushiriki wa Mheshimiwa Rais kwenye shughuli zao hata kabla ya maombi yao hajajibiwa na Ofisi ya Rais na kupata ridhaa ya Mheshimiwa Rais. Wengine wamekuwa wanatoa matangazo yanayosema Mheshimiwa Rais atashiriki katika shughuli zao wakati hata mwaliko wenyewe haujatumwa kwa Mheshimiwa Rais au Ofisi yake.

Huu ni ukiukwaji wa taratibu na ni matumizi mabaya ya jina la Mheshimiwa Rais. Tunawasihi wanaofanya hivyo waache tabia hii mara moja na badala yake wafuate utaratibu uliowekwa. Ni makosa kutangaza ushiriki wa Mheshimiwa Rais kwenye shughuli yoyote kabla ya kupata majibu na uthibitisho wa kushiriki wake kutoka Ofisi yake.

Hakuna shaka kuwa sote tunafahamu kwamba Mheshimiwa Rais Jakaya Mrisho Kikwete ni kiongozi anayependa sana kushiriki katika shughuli zote za wananchi zenye kuwaletea maendeleo, na ataendelea kufanya hivyo bila kusita wala kuchoka. Tunachowaomba ni kwa waombaji wa fursa hiyo ya Mheshimiwa kushiriki katika shughuli zao, kufuata utaratibu uliowekwa.

Mwisho.
Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu,
Dar es Salaam.
28 Februari, 2011
 
Back
Top Bottom