Tanzania Daima = CHADEMA
Mtanzania + Mwananchi + Mawio = Lowasa
Umoja wa Ulaya warejea ukoloni mamboleo
¬ Wasimamisha misaada ya maendeleo
¬ Wasaliti washangilia
¬ Serikali yatakiwa kuyashitaki makampuni na mabenki
UMOJA wa Ulaya kwa pamoja na baadhi ya nchi wanachama wake moja moja zimeamua kusitisha au kusimamisha kwa muda utoaji misaada kwa Tanzania kwa madai kwamba haziridhishwi na mapambano dhidi ya rushwa na ufisadi ndani ya serikali ya Rais Jakaya Mrisho Kikwete.
Nchi zilizotajwa ni Sweden, Finland, Norway, Marekani na Uingereza. Ni katika nchi hizi mabenki na makampuni ambayo kwa namna moja au nyingine yanahusika katika mgogoro wa ufisadi wa IPTL yana makao makuu yake. Na ni katika nchi hizo kwamba makampuni yaliyoko kwenye mgogoro yalifungua kesi mbalimbali na kudai mabilioni ya fedha dhidi ya kampuni ya VIP Engineering and Marketing na serikali ya Tanzania kuhusu mambo mbalimbali yanayohusiana na mradi wa kufua umeme wa IPTL na hasa suala la akaunti ya ESCROW. Kiasi cha dola za kimarekani milioni 125 zilikuwa zimewekwa katika akaunti ya ESCROW iliopo Benki Kuu ya Tanzania (BOT).
Tumemuona Balozi wa Uingereza akiamsha bendera nyekundu kwa madai kwamba anatetea maslahi ya Benki ya Uingereza ambayo eti ilinunua madeni ya IPTL na hivyo inadai fedha zilizokua zimewekwa kwenye Akaunti ya ESCROW.
Kampuni ya IPTL lilikuwepo siku zote na benki ya Standard Chartered inajua matatizo yote ya ufisadi yaliyoibuliwa katika Mahakama mbalimbali pamoja na ripoti za maofisa wafilisi wa muda wa kampuni ya IPTL hapa nchini. Ikitokea kwamba IPTL na washirika wake wakatiwa hatiani, je kwa vipi Standard Chartered itakwepa mashtaka?
Katika nyakati tofauti Mahakama za Kimataifa na mahakama za kawaida katika nchi za Magharibi zimetoa hukumu na maelekezo kwa kampuni zinazoshitakiana. Baadhi ya maelekezo ya mahakama ya New York ni yale yanayosema kwamba kesi nyingine zingelifunguliwa Tanzania kwa sababu mahakama yake ina uwezo wa kusikiliza mashauri hayo.