vukani
JF-Expert Member
- Dec 30, 2009
- 245
- 165
Hebu leo tuangalie mfano huu wa imani kwa kusoma habari hii ya mwanamke aliyekuwa akitokwa na damu, katika kitabu cha Marko 5:25-34.
Nitanukuu
Na mwanamke mmoja mwenye kutoka damu muda wa miaka kumi na mbili na kuteswa mengi kwa mikono ya matabibu wengi, amegharimiwa na vitu vyote alivyo navyo, kusimfae hata kidogo, bali hali yake ilizidi kuwa mbaya. Aliposikia habari za Yesu, alipita katika mkutano kwa nyuma, akaligusa vazi lake; maana alisema, Nikiyagusa mavazi yake tu nitapona. Mara chemchemi ya damu yake ikakauka , naye akafahamu mwilini mwake kwamba amepona msiba ule. Mara Yesu, hali akifahamu nafsini mwake kwamba nguvu zimemtoka, akageuka kati ya mkutano, akasema, Ni nani aliyenigusa mavazi yangu? Wanafunzi wake wakamwambia, Je! Wawaona makutano wanavyokusonga-songa , nawe wasema , Ni nani aliyenigusa? Akatazama pande zote ili amwone yule aliyelitenda neno hilo, Na yule mwanamke akaingiwa na hofu na kutetemeka, akijua lililompata, akaja akamwangukia, akamweleza kweli yote. Akamwambia, Binti, imani yako imekuponya, enenda zako kwa amani uwe mzima, usiwe na msiba wako tena.
Huyu mwanamke alikuwa na hili tatizo kwa miaka 12, ambayo kwa kweli ni miaka mingi sana kuishi na ugonjwa. Na alijaribu kila njia, akitafuta tiba lakini hakuweza kupona.
Hata hivyo kitu kimoja kilichonivutia ni kwamba, pamoja na kuhangaika kwa miaka yote hiyo akitafuta tiba lakini hakukata tamaa, na baada ya kusikia habari za Yesu akaona ni vyema ajaribu huenda atapona, na hakika kutokana na imani aliyokuwa nayo akapona. Bwana yesu asifiwe!
Watu wengi wanadhani kuwa imani ni kama mazingaombe kwamba unaamini tu halafu imani yako inakuletea kila kitu unachohitaji mikononi mwako .
Hii haiwezekani. Iwapo fikra hasi, au matamshi yako ni ya kukata tamaa na hujiamini, imani haiwezi kufanya kazi kwa mtu wa namna hiyo. Kwa nini?
Ni kwa sababu Imani sio kitu kinachofanya kazi papo kwa hapo, bali inahitaji mchakato fulani huku ikirutubishwa na fikra chanya.
Ili imani iweze kufanya kazi ni lazima ipitie katika mchakato ufuatao ndio ufanye kazi:
Uamuzi: Kumbuka kwamba huyu mwanamke alikuwa amejaribu tiba kadhaa wakiwemo madaktari bingwa na maarufu, hakuweza kupona, lakini aliposikia habari za Yesu akafanya uamuzi katika moyo wake kwamba kupitia Yesu Kristo atapona. Huo ni mchakato wake wa kwanza kabisa kuelekea katika kupona.
Imani: katika Marko 5:28 yule mwanamke alisema Nikiyagusa mavazi yake tu nitapona Ile kauli ya kusema Nitapona ni kauli chanya na yenye nguvu na kama tulivyoona kuwa inatoka kwa mwanamke ambaye alikuwa amejaribu tiba kadhaa kwa miaka 12 bila kupona.
Ni katika Matayo 9:20:22 tunaposoma kuwa alijisemea kauli hiyo kutoka moyoni mwake. Hapo ndipo tunapoona kuwa ni kwa jinsi gani imani inavyokuwa na nguvu hata kwa kujisemea moyoni tu, inatosha kufanya jambo liwe.
Kutenda: Katika Marko 5:27, tunasoma kuhusu, mwanmke huyo Alivyopenya katika kundi la watu na kwenda kugusa mavazi ya Yesu Kristo.
Ni kitu gani kilimsukuma hadi akaamua kujipenyeza katikati ya kundi la watu ili tu kugusa mavazi ya Yesu?
Ni kwa sababu aliamini neno la mungu na ndio sababu ya yeye kuchukuwa uamuzi.
Kutenda kile unachokiamini ndio njia sahihi ya wewe kuelekea katika kufanikiwa, haitakiwi kusema tu, hiyo haitoshi.
Ili imani iweze kufanya kazi ni lazima upitie katika mchakato huo ndipo imani iweze kufanya kazi.