Wakuu kuna matumaini gani hapa?
Hatma ya Kenya mikononi mwa Annan, Mkapa, Graca
*Viongozi wa dini wapinga mkutano wa ODM
*Wasema kipaumbele kwa sasa ni mazungumzo
*Wanajeshi wa Uganda wadaiwa kuingia Kenya
NAIROBI, Kenya
JUKUMU la kuhakikisha kuwa amani inarejea nchini Kenya sasa limeachwa mikononi mwa Katibu Mkuu mstaafu wa Umoja wa Mataifa, Bw. Kofi Annan, Rais mstaafu wa Tanzania, Benjamin Mkapa na mke wa Rais mstaafu wa Afrika Kusini, Bibi Graca Machel.
Tayari Bw. Annan amewatahadharisha mahasimu wawili wa kisiasa nchini Kenya, Rais Mwai Kibaki na kiongozi wa ODM, Bw. Raila Odinga, kuachana na vikwazo vitakavyokwamisha mazungumzo hayo yatakayosimamiwa na Jopo la Watu Maarufu wa Afrika.
Bw. Annan ambaye ni mshindi wa Nishani ya Amani ya Nobel ya mwaka 2001, ametoa tahadhari hiyo huku Marekani kwa upande wake, ikitoa mwito kwa viongozi hao kufanya mazungumzo ya ana kwa ana ili kurejesha utulivu nchini mwao.
"Sisi tunadhani ni muhimu kwa Rais Kibaki na Bw. Odinga, kukutana ana kwa ana bila masharti na kuzungumza jinsi ya kumaliza mgogoro uliojitokeza baada ya uchaguzi kwa njia ambayo itajali maslahi ya watu wa Kenya," alisema Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, Dkt. Jendayi Frazer.
Marekani pia ilitoa mwito wa kuheshimu utawala wa sheria na haki ya wananchi kukutana na pia kuwapo kwa uhuru wa vyombo vya habari.
"Hatukupendelea mtu wakati wa uchaguzi. Tuliunga mkono juhudi za kuwa na uchaguzi ulio wazi na wa haki. Kwa ujumla mchakato wa upigaji kura kwa amani na utulivu na hasa idadi kubwa ya wapiga kura waliojitokeza, vilionesha ushindi kwa watu wa Kenya, lakini udanganyifu katika matokeo ulitibua kila kitu," lilisema Taifa hilo kubwa.
Kauli hizo zimetoka huku ODM ikitoa notisi ya siku tatu ya kufanya mikutano yake nchini kote kesho kutwa, huku Serikali nayo ikiupigamarufuku, lakini pia ni wakati ambao Serikali iliendeleza msimamo wa kupiga marufuku matangazo ya moja kwa moja ya televisheni.
Dkt. Frazer alisisitiza kuwa upo ukweli, kwamba Wakenya wanaamini tatizo lililopo linaweza kutatuliwa kwa pande hizo mbili kugawana madaraka.
Aliongeza: "Pande zote mbili hazina budi kuelewa upungufu uliojitokeza katika kuhakiki kura, hali ambayo ilisababisha kukosekana uhakika wa matokeo ya mwisho na zinatakiwa pia kuchukua hatua za kumaliza ghasia na kurejesha heshima kwa utawala wa sheria, lakini pia na haki za binadamu."
Kauli hiyo ya Marekani ambayo safari hii ilionekana kuwa nzito kulinganisha na ya awali iliendelea: "Hii ni pamoja na kurejesha uhuru wa vyombo vya habari na wa kukutana kwa amani.
"Tunaamini kwamba watu wa Kenya wameshabaini wazi kuwa suluhisho linaweza kupatikana katika kugawana madaraka, kukomesha vurugu, upatanishi na makubaliano ya kuwa na ajenda mahususi kwa ajili ya mabadiliko ya Katiba na uchaguzi".
Bw. Annan, ambaye anatarajia kuanzia alikoishia Rais wa Ghana, Bw. John Kufuor ambaye ni Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika, amewataka Serikali na Upinzani kufikiria maslahi ya Wakenya na kuonesha nia, uongozi na ukomavu.
Alisema wataunda sekretarieti itakayoliwezesha jopo hilo kufanya kazi yake vizuri katika kumaliza matatizo na kuirejesha Kenya katika hali ya kawaida.
Akizungumzia ziara ya Rais Kufuor nchini Kenya, Bw. Annan alisema ilikuwa muhimu sana kwani angalau imeonesha mabadiliko kwa kiasi fulani.
Vyombo vya habari nchini Ghana, viliripoti kuwa Bw. Annan atachukua muda mrefu kidogo nchini Kenya tofauti na alivyokaa Rais Kufuor ambaye alitumia siku mbili tu.
Katika siku hizo mbili, Rais Kufuor aliweza kuwashawishi viongozi hao wawili kukubali kufanya mazungumzo, ziara hiyo ilifanyika sambamba na ya viongozi wastaafu wa Afrika, Bw. Mkapa wa Tanzania, Dkt. Kenneth Kaunda wa Zambia na Bw. Ketumile Masire wa Botswana na Dkt. Frazer.
"Majadiliano ya kisiasa si tukio la mara moja, ni mchakato ambao unaweza kuchukua muda mrefu au mfupi, kutegemea na ushirikiano kutoka kwa viongozi," Bw. Annan alisema baada ya kukutana na Rais Kufuor.
"Huu nauona kama wajibu mkubwa kwangu na nitauchukulia kwa uzito mkubwa pia katika kurejesha utulivu na kumaliza haraka matatizo ya kibinadamu katika nchi hiyo," alisema.
"Hatuendi pale kupeleka suluhisho ila tutafanya kazi pamoja na pande zinazohusika na hatimaye tutafikia suluhisho muhimu na la muda mrefu," alisema.
Viongozi wa kidini nchini Kenya wamepaza sauti zao tena za kutaka mazungumzo ya amani yafanyike, wakiamini kuwa ndilo suluhisho pekee la matatizo hayo.
Kanisa Katoliki kwa upande wake, limepinga mkutano wa ODM na kutaka viongozi wakae mezani kujadili amani.
Kadinali John Njue, alisema juzi kuwa kutokana na vifo vya watu wengi na uharibifu wa mali uliofanywa, njia pekee ya kuondokana na hayo ni mazungumzo.
"Nchi imo katika hali mbaya hivi sasa, hivyo kuitisha mikutano kama hiyo ni sawa na kuongeza mafuta kwenye moto ambao tayari umewaka," alisema Kadinali Njue.
Jijini Nairobi, maaskofu 33 wa Kanisa la kianglikana la Kenya, waliwataka Rais Kibaki na Bw. Odinga kujitokeza kushiriki mazungumzo ya amani.
"Watu hawana budi kuingia katika mazungumzo. Machungu mengi yametokea. Mikutano itazidisha machungu haya, kwani itasababisha uporaji madukani tena. Itasababisha upotevu wa maisha ya watu," alionya Askofu Benjamin Nzimbi.
Viongozi wa kidini kutoka jamii ya Wakalenjin nao waliunga mkono kufanyika kwa mazungumzo na kuwaomba Wakenya waombee amani.
Nao viongozi walio chini ya mwavuli wa Chama cha Maendeleo ya Jumuiya ya Emo, walisema katika taarifa yao: "Tumetiwa moyo na juhudi mbalimbali za viongozi wa kimataifa na wa ndani ya nchi na maombi kutoka kwa watu wengi duniani kote wanaotaka kuwaona Wakenya wakiishi maisha ya amani na maendeleo kama ilivyokuwa awali."
Wanajeshi wa Uganda
Katika hatua nyingine, kuna madai ya kuonekana wanajeshi wa Uganda wakivuka mpaka kuingia Kenya.
Wakazi wa maeneo ya Busia walidai juzi kuwa baadhi ya wanajeshi wa Uganda walionekana mjini hapo na Port Victoria karibu na Mto Suo.
"Wamesambaa katika mpaka huku wengine wakishika doria katika Ziwa Victoria," alisema mwalimu wa sekondari wilayani Budalang'i.
Kwa mujibu wa Mbunge mteule wa Nambale, Bw. Chris Okemo, baadhi ya askari hao wameingia katika eneo huru la mpakani kuelekea Busia upande wa Kenya.
"Tumepokea taarifa, kwamba kuna wageni ambao malengo yao hayajulikani na wanaonekana katika makundi. Bado tunafanya uchunguzi wa madai hayo," alisema.
Naye Mbunge mteule wa Bondo, Dkt. Oburu Oginga, alidai kwamba watu waliovalia sare za kijeshi za Uganda walionekana katika kisiwa cha Mageta juzi jioni wakiwa makundi makundi.
"Kundi la kwanza lenye askari 12 wanaozungumza Kiswahili kibovu lilifika kisiwani Mageta saa 11 jioni Ijumaa na kuomba waelekezwe njia ya kwenda pwani mwa Usenge na Uhanya," alisema Bw. Oginga.
Alisema aliiarifu Polisi mjini Bondo baada ya askari zaidi kufika Mageta saa mbili baadaye.
"Tuna wasiwasi na wageni hawa wa kijeshi katika eneo hili. Wananchi wana hofu," alisema Bw. Oginga. Hata hivyo Kamanda wa Polisi wa Nyanza, Bibi Grace Kaindi, alikanusha madai hayo.
"Huo ni upuuzi. Haiwezekani majeshi ya kigeni yaingie nchini wakati hatuna vita na mtu yeyote," alisema.
"Tuna sheria ambazo zinaweza kutusaidia kushughulikia tishio lolote la usalama jimboni. Wananchi hawana budi kupuuza uvumi kuhusu wanajeshi wa Uganda kupiga kambi mpakani mwa Kenya katika Ziwa victoria," alisema uchunguzi wa Polisi ulibaini kutokuwapo watu wa aina hiyo.
Wanajeshi kama hao walidaiwa pia kuwasili Bungoma, wakiwa katika mabasi sita.
Kumekuwapo na wasiwasi nchini Uganda dhidi ya Rais Yoweri Museveni kujihusisha na mgogoro wa uchaguzi uliotokea nchini Kenya.
Rais Museveni alikuwa Mkuu pekee wa nchi katika eneo la Afrika Mashariki kumpongeza Rais Mwai Kibaki kwa ushindi wake.
Viongozi nchini Uganda wamekanusha wanajeshi wake kuvuka mpaka na kuingia Kenya.
Mshauri wa Rais Museveni wa mambo ya habari, Bw. John Nagenda, jana alikanusha madai hayo sambamba na msemaji wa Jeshi la Uganda, Kapteni Paddy Ankunda, ambaye alisema wanajeshi pekee wa Uganda walioko Kenya ni wanaotoa mafunzo katika Chuo cha Kijeshi cha Karen jijini Nairobi.
Umoja wa Makanisa
Naye Rashid Mkwinda,anaripoti kutoka Mbeya kwamba Umoja wa Makanisa nchini umewataka viongozi wa kisiasa wa Kenya kumrejea Mungu iwapo watashindwa siasa kwa njia ya amani na utulivu na kukomesha mauaji yaliyosababishwa na mzozo wa kisiasa nchini humo.
Wakizungumza katika kongamano la maombi ya kuombea amani nchini katika uwanja wa Sokoine jijini hapa jana viongozi hao walisema kinachoendelea nchini Kenya kinaweza kuiathiri jamii ya watu wa Afrika kutokana na ukweli kwamba nchi hizi zina uhuhusiano wa karibu kijamii, kiuchumi na kisiasa.
Akitoa tamko la maaskofu hao Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya maombi hayo, Askofu John Mwela, kutoka Kanisa la Anglikana alisema Kanisa limepokea kwa masikitiko mgogoro unaoendelea nchini, ambao kwa vyo vyote vile uhusiano wa mgogoro huo unaweza kuenea katika jamii ya Afrika Mashariki.
Askofu Mwela alisema mara nyingi migogoro inayosababisha maafa na mauaji katika jamii huwaathiri akina mama na watoto ambao hawana hatia hivyo ni muhimu kwa viongozi wa kisiasa kumrejea Mungu, ili kuepusha maafa ya aina hiyo.
Kwa upande wake, Mwalimu na Nabii wa Kanisa la Anglikana kutoka Kenya, Bibi Margrethy Aduol ambaye alipokea msaada wa sh. 680,000 kutoka Umoja huo kwa ajili ya kusaidia walioathirika na mzozo wa kisiasa nchini mwake, alisema maombi ya amani kwa nchi za Afrika ni muhimu.
Waangalizi EAC
Naye Glory Mhiliwa anaripoti kutoka Arusha, kwamba waangalizi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) katika uchaguzi mkuu wa Kenya uliofanyika mwishoni mwa mwaka jana, wamependekeza kiitishwe kikao cha wakuu wa nchi za EAC kujadili masuala ya amani, usalama na utawala bora unavyoendelea sasa nchini humo.
Mapendekezo hao yamo katika taarifa ya waangalizi hao wa Jumuiya ya Afrika waliokuwa wanafuatillia uchaguzi mkuu wa Kenya iliyotolewa jana katika makao makuu ya Jumuiya ya Afrika Mashariki mjini hapa
Walieleza kuwa mkataba wa EAC unatoa mwongozo kwa marais wa nchi za Jumuiya kuchukua hatua kwa nchi mwanachama ambayo inakiuka utawala bora na masuala ya amani.
Walieleza kuwa marais wa EAC hawana budi kuchukua jukumu la kuhakikisha mchakato wa kuelekea katika upatikanaji na suluhisho la mgogoro nchini humo unaanza.
Walipendekeza pia wote ambao wamekuwa chanzo cha machafuko ya kisiasa Kenya yaliyosababisha mamia ya watu kufa na wengine kukimbia makazi yao wafikishwe kwenye vyombo vya sheria na kushitakiwa
"Uchunguzi kuhusiana na uhesabuji wa kura ufanyike na endapo itabainika kwamba ofisa yeyote wa Tume ya Uchaguzi ya Kenya(ECK) alihusika basi awajibike," ilieleza sehemu ya taarifa hiyo.
Waangalizi hao pia wamewataka viongozi wa vyama vya siasa nchini humo kuwasihi wafuasi wao kusitisha vurugu na badala yake uitishwe mdahalo wa pamoja wa kutafuta ufumbuzi wa mgogoro uliojitokeza nchini na kutaka pia vyombo vya Dola kuacha matumizi ya nguvu za kupita kiasi kwa waandamanaji.
Kwa upande wa uchaguzi, waangalizi hao walibaini kwamba kuhesabu na kutangazwa kwa matokeo ya kura za urais kulicheleweshwa na hivyo kuwa chanzo cha mtafaruku mkubwa uliosababisha machafuko.
Waangalizi hao walieleza kwamba kucheleweshwa kwa matokeo hasa kutoka eneo moja ambalo mgombea mmoja wa urais ana nguvu zaidi kulizua tetesi kwamba matokeo yao eneo hilo yalipangwa.
Katika taarifa yao hiyo pia walieleza kuwa Mwenyekiti wa ECK Bw. Samuel Kivuitu, alishindwa kudhibiti mchakato wa kuhesabu kura na baadaye kutangazwa kwa matokeo.
Kutoka na dosari mbalimbali zilizofanywa na Mwenyekiti wa Tume hiyo waangalizi hao walieleza kuzua utata wa uwezo na umakini wake katika Tume.
EAC ilituma waangalizi 13 ambao ni wabunge wa Jumuiya hiyo kutoka Uganda na Tanzania na maofisa waandamizi wa Sekretariati ya Jumuiya hiyo wakiongozwa na Bw. Mike Sebalu ambaye ni mbunge wa Afrika Mashariki kutoka Uganda. (The Standard/Waandishi Wetu)
Source: Gazeti la Majira, 14 Jan 2008.
Hatma ya Kenya mikononi mwa Annan, Mkapa, Graca
*Viongozi wa dini wapinga mkutano wa ODM
*Wasema kipaumbele kwa sasa ni mazungumzo
*Wanajeshi wa Uganda wadaiwa kuingia Kenya
NAIROBI, Kenya
JUKUMU la kuhakikisha kuwa amani inarejea nchini Kenya sasa limeachwa mikononi mwa Katibu Mkuu mstaafu wa Umoja wa Mataifa, Bw. Kofi Annan, Rais mstaafu wa Tanzania, Benjamin Mkapa na mke wa Rais mstaafu wa Afrika Kusini, Bibi Graca Machel.
Tayari Bw. Annan amewatahadharisha mahasimu wawili wa kisiasa nchini Kenya, Rais Mwai Kibaki na kiongozi wa ODM, Bw. Raila Odinga, kuachana na vikwazo vitakavyokwamisha mazungumzo hayo yatakayosimamiwa na Jopo la Watu Maarufu wa Afrika.
Bw. Annan ambaye ni mshindi wa Nishani ya Amani ya Nobel ya mwaka 2001, ametoa tahadhari hiyo huku Marekani kwa upande wake, ikitoa mwito kwa viongozi hao kufanya mazungumzo ya ana kwa ana ili kurejesha utulivu nchini mwao.
"Sisi tunadhani ni muhimu kwa Rais Kibaki na Bw. Odinga, kukutana ana kwa ana bila masharti na kuzungumza jinsi ya kumaliza mgogoro uliojitokeza baada ya uchaguzi kwa njia ambayo itajali maslahi ya watu wa Kenya," alisema Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, Dkt. Jendayi Frazer.
Marekani pia ilitoa mwito wa kuheshimu utawala wa sheria na haki ya wananchi kukutana na pia kuwapo kwa uhuru wa vyombo vya habari.
"Hatukupendelea mtu wakati wa uchaguzi. Tuliunga mkono juhudi za kuwa na uchaguzi ulio wazi na wa haki. Kwa ujumla mchakato wa upigaji kura kwa amani na utulivu na hasa idadi kubwa ya wapiga kura waliojitokeza, vilionesha ushindi kwa watu wa Kenya, lakini udanganyifu katika matokeo ulitibua kila kitu," lilisema Taifa hilo kubwa.
Kauli hizo zimetoka huku ODM ikitoa notisi ya siku tatu ya kufanya mikutano yake nchini kote kesho kutwa, huku Serikali nayo ikiupigamarufuku, lakini pia ni wakati ambao Serikali iliendeleza msimamo wa kupiga marufuku matangazo ya moja kwa moja ya televisheni.
Dkt. Frazer alisisitiza kuwa upo ukweli, kwamba Wakenya wanaamini tatizo lililopo linaweza kutatuliwa kwa pande hizo mbili kugawana madaraka.
Aliongeza: "Pande zote mbili hazina budi kuelewa upungufu uliojitokeza katika kuhakiki kura, hali ambayo ilisababisha kukosekana uhakika wa matokeo ya mwisho na zinatakiwa pia kuchukua hatua za kumaliza ghasia na kurejesha heshima kwa utawala wa sheria, lakini pia na haki za binadamu."
Kauli hiyo ya Marekani ambayo safari hii ilionekana kuwa nzito kulinganisha na ya awali iliendelea: "Hii ni pamoja na kurejesha uhuru wa vyombo vya habari na wa kukutana kwa amani.
"Tunaamini kwamba watu wa Kenya wameshabaini wazi kuwa suluhisho linaweza kupatikana katika kugawana madaraka, kukomesha vurugu, upatanishi na makubaliano ya kuwa na ajenda mahususi kwa ajili ya mabadiliko ya Katiba na uchaguzi".
Bw. Annan, ambaye anatarajia kuanzia alikoishia Rais wa Ghana, Bw. John Kufuor ambaye ni Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika, amewataka Serikali na Upinzani kufikiria maslahi ya Wakenya na kuonesha nia, uongozi na ukomavu.
Alisema wataunda sekretarieti itakayoliwezesha jopo hilo kufanya kazi yake vizuri katika kumaliza matatizo na kuirejesha Kenya katika hali ya kawaida.
Akizungumzia ziara ya Rais Kufuor nchini Kenya, Bw. Annan alisema ilikuwa muhimu sana kwani angalau imeonesha mabadiliko kwa kiasi fulani.
Vyombo vya habari nchini Ghana, viliripoti kuwa Bw. Annan atachukua muda mrefu kidogo nchini Kenya tofauti na alivyokaa Rais Kufuor ambaye alitumia siku mbili tu.
Katika siku hizo mbili, Rais Kufuor aliweza kuwashawishi viongozi hao wawili kukubali kufanya mazungumzo, ziara hiyo ilifanyika sambamba na ya viongozi wastaafu wa Afrika, Bw. Mkapa wa Tanzania, Dkt. Kenneth Kaunda wa Zambia na Bw. Ketumile Masire wa Botswana na Dkt. Frazer.
"Majadiliano ya kisiasa si tukio la mara moja, ni mchakato ambao unaweza kuchukua muda mrefu au mfupi, kutegemea na ushirikiano kutoka kwa viongozi," Bw. Annan alisema baada ya kukutana na Rais Kufuor.
"Huu nauona kama wajibu mkubwa kwangu na nitauchukulia kwa uzito mkubwa pia katika kurejesha utulivu na kumaliza haraka matatizo ya kibinadamu katika nchi hiyo," alisema.
"Hatuendi pale kupeleka suluhisho ila tutafanya kazi pamoja na pande zinazohusika na hatimaye tutafikia suluhisho muhimu na la muda mrefu," alisema.
Viongozi wa kidini nchini Kenya wamepaza sauti zao tena za kutaka mazungumzo ya amani yafanyike, wakiamini kuwa ndilo suluhisho pekee la matatizo hayo.
Kanisa Katoliki kwa upande wake, limepinga mkutano wa ODM na kutaka viongozi wakae mezani kujadili amani.
Kadinali John Njue, alisema juzi kuwa kutokana na vifo vya watu wengi na uharibifu wa mali uliofanywa, njia pekee ya kuondokana na hayo ni mazungumzo.
"Nchi imo katika hali mbaya hivi sasa, hivyo kuitisha mikutano kama hiyo ni sawa na kuongeza mafuta kwenye moto ambao tayari umewaka," alisema Kadinali Njue.
Jijini Nairobi, maaskofu 33 wa Kanisa la kianglikana la Kenya, waliwataka Rais Kibaki na Bw. Odinga kujitokeza kushiriki mazungumzo ya amani.
"Watu hawana budi kuingia katika mazungumzo. Machungu mengi yametokea. Mikutano itazidisha machungu haya, kwani itasababisha uporaji madukani tena. Itasababisha upotevu wa maisha ya watu," alionya Askofu Benjamin Nzimbi.
Viongozi wa kidini kutoka jamii ya Wakalenjin nao waliunga mkono kufanyika kwa mazungumzo na kuwaomba Wakenya waombee amani.
Nao viongozi walio chini ya mwavuli wa Chama cha Maendeleo ya Jumuiya ya Emo, walisema katika taarifa yao: "Tumetiwa moyo na juhudi mbalimbali za viongozi wa kimataifa na wa ndani ya nchi na maombi kutoka kwa watu wengi duniani kote wanaotaka kuwaona Wakenya wakiishi maisha ya amani na maendeleo kama ilivyokuwa awali."
Wanajeshi wa Uganda
Katika hatua nyingine, kuna madai ya kuonekana wanajeshi wa Uganda wakivuka mpaka kuingia Kenya.
Wakazi wa maeneo ya Busia walidai juzi kuwa baadhi ya wanajeshi wa Uganda walionekana mjini hapo na Port Victoria karibu na Mto Suo.
"Wamesambaa katika mpaka huku wengine wakishika doria katika Ziwa Victoria," alisema mwalimu wa sekondari wilayani Budalang'i.
Kwa mujibu wa Mbunge mteule wa Nambale, Bw. Chris Okemo, baadhi ya askari hao wameingia katika eneo huru la mpakani kuelekea Busia upande wa Kenya.
"Tumepokea taarifa, kwamba kuna wageni ambao malengo yao hayajulikani na wanaonekana katika makundi. Bado tunafanya uchunguzi wa madai hayo," alisema.
Naye Mbunge mteule wa Bondo, Dkt. Oburu Oginga, alidai kwamba watu waliovalia sare za kijeshi za Uganda walionekana katika kisiwa cha Mageta juzi jioni wakiwa makundi makundi.
"Kundi la kwanza lenye askari 12 wanaozungumza Kiswahili kibovu lilifika kisiwani Mageta saa 11 jioni Ijumaa na kuomba waelekezwe njia ya kwenda pwani mwa Usenge na Uhanya," alisema Bw. Oginga.
Alisema aliiarifu Polisi mjini Bondo baada ya askari zaidi kufika Mageta saa mbili baadaye.
"Tuna wasiwasi na wageni hawa wa kijeshi katika eneo hili. Wananchi wana hofu," alisema Bw. Oginga. Hata hivyo Kamanda wa Polisi wa Nyanza, Bibi Grace Kaindi, alikanusha madai hayo.
"Huo ni upuuzi. Haiwezekani majeshi ya kigeni yaingie nchini wakati hatuna vita na mtu yeyote," alisema.
"Tuna sheria ambazo zinaweza kutusaidia kushughulikia tishio lolote la usalama jimboni. Wananchi hawana budi kupuuza uvumi kuhusu wanajeshi wa Uganda kupiga kambi mpakani mwa Kenya katika Ziwa victoria," alisema uchunguzi wa Polisi ulibaini kutokuwapo watu wa aina hiyo.
Wanajeshi kama hao walidaiwa pia kuwasili Bungoma, wakiwa katika mabasi sita.
Kumekuwapo na wasiwasi nchini Uganda dhidi ya Rais Yoweri Museveni kujihusisha na mgogoro wa uchaguzi uliotokea nchini Kenya.
Rais Museveni alikuwa Mkuu pekee wa nchi katika eneo la Afrika Mashariki kumpongeza Rais Mwai Kibaki kwa ushindi wake.
Viongozi nchini Uganda wamekanusha wanajeshi wake kuvuka mpaka na kuingia Kenya.
Mshauri wa Rais Museveni wa mambo ya habari, Bw. John Nagenda, jana alikanusha madai hayo sambamba na msemaji wa Jeshi la Uganda, Kapteni Paddy Ankunda, ambaye alisema wanajeshi pekee wa Uganda walioko Kenya ni wanaotoa mafunzo katika Chuo cha Kijeshi cha Karen jijini Nairobi.
Umoja wa Makanisa
Naye Rashid Mkwinda,anaripoti kutoka Mbeya kwamba Umoja wa Makanisa nchini umewataka viongozi wa kisiasa wa Kenya kumrejea Mungu iwapo watashindwa siasa kwa njia ya amani na utulivu na kukomesha mauaji yaliyosababishwa na mzozo wa kisiasa nchini humo.
Wakizungumza katika kongamano la maombi ya kuombea amani nchini katika uwanja wa Sokoine jijini hapa jana viongozi hao walisema kinachoendelea nchini Kenya kinaweza kuiathiri jamii ya watu wa Afrika kutokana na ukweli kwamba nchi hizi zina uhuhusiano wa karibu kijamii, kiuchumi na kisiasa.
Akitoa tamko la maaskofu hao Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya maombi hayo, Askofu John Mwela, kutoka Kanisa la Anglikana alisema Kanisa limepokea kwa masikitiko mgogoro unaoendelea nchini, ambao kwa vyo vyote vile uhusiano wa mgogoro huo unaweza kuenea katika jamii ya Afrika Mashariki.
Askofu Mwela alisema mara nyingi migogoro inayosababisha maafa na mauaji katika jamii huwaathiri akina mama na watoto ambao hawana hatia hivyo ni muhimu kwa viongozi wa kisiasa kumrejea Mungu, ili kuepusha maafa ya aina hiyo.
Kwa upande wake, Mwalimu na Nabii wa Kanisa la Anglikana kutoka Kenya, Bibi Margrethy Aduol ambaye alipokea msaada wa sh. 680,000 kutoka Umoja huo kwa ajili ya kusaidia walioathirika na mzozo wa kisiasa nchini mwake, alisema maombi ya amani kwa nchi za Afrika ni muhimu.
Waangalizi EAC
Naye Glory Mhiliwa anaripoti kutoka Arusha, kwamba waangalizi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) katika uchaguzi mkuu wa Kenya uliofanyika mwishoni mwa mwaka jana, wamependekeza kiitishwe kikao cha wakuu wa nchi za EAC kujadili masuala ya amani, usalama na utawala bora unavyoendelea sasa nchini humo.
Mapendekezo hao yamo katika taarifa ya waangalizi hao wa Jumuiya ya Afrika waliokuwa wanafuatillia uchaguzi mkuu wa Kenya iliyotolewa jana katika makao makuu ya Jumuiya ya Afrika Mashariki mjini hapa
Walieleza kuwa mkataba wa EAC unatoa mwongozo kwa marais wa nchi za Jumuiya kuchukua hatua kwa nchi mwanachama ambayo inakiuka utawala bora na masuala ya amani.
Walieleza kuwa marais wa EAC hawana budi kuchukua jukumu la kuhakikisha mchakato wa kuelekea katika upatikanaji na suluhisho la mgogoro nchini humo unaanza.
Walipendekeza pia wote ambao wamekuwa chanzo cha machafuko ya kisiasa Kenya yaliyosababisha mamia ya watu kufa na wengine kukimbia makazi yao wafikishwe kwenye vyombo vya sheria na kushitakiwa
"Uchunguzi kuhusiana na uhesabuji wa kura ufanyike na endapo itabainika kwamba ofisa yeyote wa Tume ya Uchaguzi ya Kenya(ECK) alihusika basi awajibike," ilieleza sehemu ya taarifa hiyo.
Waangalizi hao pia wamewataka viongozi wa vyama vya siasa nchini humo kuwasihi wafuasi wao kusitisha vurugu na badala yake uitishwe mdahalo wa pamoja wa kutafuta ufumbuzi wa mgogoro uliojitokeza nchini na kutaka pia vyombo vya Dola kuacha matumizi ya nguvu za kupita kiasi kwa waandamanaji.
Kwa upande wa uchaguzi, waangalizi hao walibaini kwamba kuhesabu na kutangazwa kwa matokeo ya kura za urais kulicheleweshwa na hivyo kuwa chanzo cha mtafaruku mkubwa uliosababisha machafuko.
Waangalizi hao walieleza kwamba kucheleweshwa kwa matokeo hasa kutoka eneo moja ambalo mgombea mmoja wa urais ana nguvu zaidi kulizua tetesi kwamba matokeo yao eneo hilo yalipangwa.
Katika taarifa yao hiyo pia walieleza kuwa Mwenyekiti wa ECK Bw. Samuel Kivuitu, alishindwa kudhibiti mchakato wa kuhesabu kura na baadaye kutangazwa kwa matokeo.
Kutoka na dosari mbalimbali zilizofanywa na Mwenyekiti wa Tume hiyo waangalizi hao walieleza kuzua utata wa uwezo na umakini wake katika Tume.
EAC ilituma waangalizi 13 ambao ni wabunge wa Jumuiya hiyo kutoka Uganda na Tanzania na maofisa waandamizi wa Sekretariati ya Jumuiya hiyo wakiongozwa na Bw. Mike Sebalu ambaye ni mbunge wa Afrika Mashariki kutoka Uganda. (The Standard/Waandishi Wetu)
Source: Gazeti la Majira, 14 Jan 2008.