Hadithi: Roho ya paka. (Ben R. Mtobwa)

nameless girl

JF-Expert Member
Apr 22, 2012
4,195
2,664
1
ILIKUWA ghafla, kama pigo la kisu ambalo lilipenya mwilini na kuujeruhi moyo wa Inspekta Kombora. Kati ya yote aliyoyatarajia jioni ya leo, simu kama hiyo, ya maafa, haikuwamo kabisa akilini mwake. Kwa jumla, ilikuwa kama iliyopigwa muda huu kwa ajili ya kumsimanga au kumdhihaki.
Muda mfupi uliopita alikuwa akiitazama kwa furaha kubwa chati yake ya taarifa za wizi, ujambazi na mauaji nchini. Ingawa tabasamu ni kitu ambacho huutembelea uso wa Kombora kwa nadra sana, lakini leo liliutawala uso huo kwa muda mrefu wakati akiitazama chati hiyo. Furaha iliyotokana na jinsi idadi ya vitendo hivyo ilivyokuwa ikishuka kwa kasi. Ukiacha udokozi mdogomdogo, wizi wa kuaminiana na ule wa kalamu vinginevyo rekodi hiyo ilikuwa ikielekea kwenye sifuri. Wakati wowote Tanzania ingeweza kujitangaza duniani kama taifa pekee ambalo limeushinda kabisa ujambazi.
Kombora alikuwa mtu wa kwanza aliyestahili kuifurahia hali hiyo kwani alikuwa mstari wa mbele kati ya wale wachache ambao huumiza vichwa vyao na kukesha usiku na mchana pindi linapotokea tukio lolote ambalo hutishia usalama wa taifa hili. Hivyo, alichekelea huku akimpongeza kimoyomoyo Waziri wa Mambo ya Ndani, Augustine Mrema, ambaye alisimamia kwa dhati ulinzi wa sungusungu ambao uliwajumuisha raia wenyewe kujilinda usiku. Kombora aliamini kabisa kuwa hilo lilichangia sana kupunguza wizi, uvunjaji wa majumba na mauaji ambayo yalifikia kiwango cha kukatisha tamaa.
Hata hivyo, tabasamu la Kombora lilitoweka. Lile wazo lililokuwa likimpekecha ubongo mara kwa mara lilipomjia tena, wazo la kwamba, kama imefikia hatua ya raia wenyewe kukesha nje wakijilinda, vyombo ambavyo vina jukumu hilo vinafanya nini? Havitoshi? Haviwezi? Havifai? Haviaminiki? Na kama jibu limo katika moja ya maswali hayo kuna umuhimu gani wa kuwa na vyombo hivyo na kuvitengea mamilioni ya pesa kila mwaka?
Akiwa askari mwaminifu, anayeipenda na kuiamini kazi yake Kombora alijisikia haya. Angefurahi zaidi kama idadi hiyo ya matukio ya kijambazi ingekuwa inashuka kutokana na uwezo wa polisi au usalama. Angefurahi zaidi kama raia wote wangelala usingizi wao kwa amani kama ilivyokuwa miaka michache iliyopita. Pamoja na hayo, aliendelea kuifurahia hali ya usalama. Alijiona kama kwamba wanausalama wako mapumzikoni au chuoni wakiandaa mkakati ambao utawafanya warudipo kazini watimize jukumu lao kwa uhakika zaidi.
Ni wakati alipotoka mbele ya jedwali hilo na kuketi juu ya kiti chake pindi ilipolia simu hii na kuupasua moyo wake kwa habari za mauaji. “Unasema unaitwa nani vile?” Kombora aliuliza kwa ukali kidogo.
“Sajini Brashi, mzee. Wa kituo Kikuu… Ni kweli hunifahamu. Lakini mimi nakufahamu…”
Kombora alimkatiza tena, safari hii kwa ukali zaidi, “Kwa nini unipigie mimi? Huna mkuu wako wa kazi? Sikiliza, Sajini. Kama hadi leo hujafahamu taratibu za kazi yako nadhani njoo zako hapa tukupe barua ili urudi tena chuoni.”

“Sivyo, mzee,” upande wa pili ulijibu, kiasi sauti yake ikiwa na hofu. “Naufahamu wajibu wangu. Lakini kuna jambo katika mauaji haya, ambalo nadhani ungependa kuliona kabla ya mtu mwingine yeyote.”
“Jambo lipi hilo?”
“Labda nikuombe uje mara moja. Ni mwendo wa dakika tano tu, mzee…”

***​
PONGWE Hotel ni moja kati ya yale mamia ya hoteli za kitalii ambazo ziliibuka kama uyoga huku na huko nchini, mara baada ya kutangaza ule uhuru wa kiuchumi. Hii ipo katika Mtaa wa Livingstone, Kariakoo. Ina ghorofa sita, vyumba mia na ishirini vya kulala, vyote vikiwa vinajitegemea kwa bafu, choo na mashine ya kurekebisha hewa.
Kwa nje hoteli hii inaonekana kama hoteli nyingine nyingi za mji huu, kana kwamba wajenzi wake walikusudia kumfanya mpitanjia asivutiwe kabisa na majengo, rangi wala mandhari yake. Lakini ndani, hali ilikuwa tofauti kabisa. Utaalamu na utajiri vilijumuishwa kiasi cha kumfanya Kombora, ambaye hapati nafasi ya kutembelea hoteli mara kwa mara, atikise kichwa chake.
Zilimchukua dakika tisa, badala ya tano, kutoka ofisini kwake hadi hapa, hali ambayo ilisababishwa na msongamano wa magari na ubovu wa barabara. Alimkuta Brashi, kijana mwembamba, mrefu, mwenye nywele nyingi aliyevalia kiraia, akimsubiri mlangoni.
“Hadi sasa, zaidi ya mhudumu wa chumba hicho na meneja wa hoteli, hamna mtu mwingine anayejua kilichotokea,” Brashi alimweleza Inspekta akimwongoza ndani. “Ni katika ghorofa ya tano, chumba namba 108.”
Walipita mapokezi ambapo mhudumu wa kike alikuwa akiwakaribisha wageni wanne kwa maneno na tabasamu lililotosha kabisa kuwashawishi wakae hotelini hapo kwa miaka. Kutoka hapo waliingia chumba cha vinywaji. Huko nusu ya viti vyote tayari ilimezwa na wateja walioonekana wachangamfu zaidi kutokana na bia nyingi zilizokuwa wazi mbele yao. Wawili kati ya wateja hao waligeuza nyuso zao kuwatazama Brashi na Inspekta Kombora, waliokuwa katika mavazi yao ya kawaida. Watumiaji hao waliwapuuza mara moja kwa kuwachukulia kama wanywaji wenzao. Brashi alimwongoza Kombora kuifuata ngazi ya kupandia juu.
Mbele ya chumba walichokihitaji walimkuta meneja akinong’ona na mzee mmoja mwenye tumbo nene na uso wa mtoto mdogo ambaye, kwa kumtazama tu, Kombora alifahamu kuwa ni Mchaga. Nyuso zao zilijawa na wasiwasi.
“Karibu mzee,” Meneja aliwakaribisha. “Huyu hapa ni bwana Mmari, ndiye tajiri wa hoteli hii. Nilikuwa nikimfahamisha mkasa uliotukuta.”
Walishikana mikono. Kisha, wote wakaingia katika chumba hicho ambacho kwa mtazamo wa kawaida kilikuwa kama kawaida. Shuka zilitandikwa vizuri kitandani. Juu ya kitanda hicho alilala kifudifudi msichana mwembamba, mweupe, ambaye huhitaji kumtazama usoni ili ujue kuwa ni mzuri. Alivaa nguo zake zote; gauni jepesi, refu japo lilifunua paja moja na kuonekana kutokana na kulala vibaya. Mikono yake laini ilijaa bangili na pete ya dhahabu. Shingoni pia alikuwa na mkufu wa dhahabu ambao ulioana na nywele zake ambazo pia zilibeba rangi ya dhahabu. Kwa kila hali alikuwa msichana mzuri wa kileo.
Angeweza kuwa amelala… angeweza kuwa amejipumzisha. Kombora alimtazama Brashi kama anayetaka ufafanuzi wa hayo.
“Amekufa mzee,” Brashi alijibu swali hilo ambalo alilisoma katika macho ya kombora. “Amekufa kifo cha kikatili kupita kiasi.”
Kombora hakuelewa. Alimwonyesha hivyo Brashi katika macho yake.
“Labda nikuonyeshe, mzee,” alisema akimsogelea marehemu. “Nikuonyeshe jeraha mzee?” Kombora alipotikisa kichwa kukubali, Brashi alichukua kitambaa cha meza ndogo kando ya kitanda hicho na kukifunga katika mkono wake wa kushoto. Kisha, akautia mkono wake tumboni mwa marehemu na kumgeuza taratibu huku akiyafumba macho yake na kusema taratibu, “Jiandae kwa mshituko.”
Kwanza Kombora hakuelewa. Ilikuwa kama anaota ndoto ya ajabuajabu inayotisha kuliko vitisho vyote. Kisha, akadhani kuwa haoti, bali anatazama sinema ya kuogofya kupita kiasi. Alipotanabahi kuwa hayuko pichani wala ndotoni alihisi alishikwa na kichefuchefu. Hakuhitaji kutapika kwani bwana Mmari alikuwa akitapika badala yake huku akitokwa na sauti ya kilio cha ghafla.
Ilikuwa picha ya kutisha, picha isiyoelezeka wala kutazamika. Yeyote aliyefanya kitendo hiki hakuwa binadamu wa kawaida isipokuwa mnyama. Vinginevyo, hangewezaje kuthubutu? Angewezaje kufikiria hilo?
Bila kujua atendalo, Kombora alijikuta akimshika Sajini Brashi mkono kwa vidole vyake vikubwa na kumbana huku akimuuliza kwa sauti ndogo, “Mimi nahusika vipi na maiti hiyo Sajin? Kitu gani hapo ambacho uliona kitapendeza sana niskikiona?”
Brashi alijaribu kujitoa katika mkono wa kombora. Ilikuwa kama kujaribu kujikwatua toka katika pingu. Badala yake ndiyo kwanza vidole hivyo vilizidi kudidimia katika ngozi yake. Japo maumivu yalikuwa makali, lakini hayakumzuia kushangazwa na nguvu za mzee huyu. “Anakula nini?” alijiuliza akimtazama usoni.
“Kitu gani ulichodhani kitanipendeza hapa?” Kombora aliuliza tena.
“Unaniumiza Inspekta.”
Ndiyo kwanza Kombora akafahamu kuwa alikuwa amemshika Brashi mkono. Akamwachia na kuiona damu ambayo ilianza kutoka katika michubuko iliyosababishwa na vidole vyake. Angeweza kumwomba radhi, lakini hakufanya hivyo. Rohoni mwake, aliona adhabu hiyo ndogo inatosha kabisa kumfunza adabu sajini huyu kwa kosa lake la kuivuruga amani na starehe aliyokuwa nayo moyoni kwa siku chache zilizopita bila misukosuko ya kutisha.
Kumwita hili atazame maiti hii iliyokuwa katika taswira ya kutisha kupita kiasi, maiti ambayo haitamtoka akilini wala katika ndoto zake, kwa muda mrefu bila sababu ya maana, aliona ni ufedhuli wa hali ya juu. Alimkazia Brashi macho akifikiria adhabu ipi ya pili ambayo ingemfaa zaidi.
Brashi hawezi kuwa mbumbumbu kiasi hicho. Hawezi kuwa mtu pekee nchini na duniani ambaye hafahamu kuwa Kombora alikuwa akiongoza idara maalumu na pekee ambayo hushughulikia yale masuala mazito na yanayotishia usalama wa serikali na taifa, si masuala madogomadogo, ya kawaida ambayo yangeweza kushughulikiwa na polisi wa kawaida.
Kana kwamba anayasoma mawazo yake, Sajini Brashi alisema, “Samahani sana Inspekta, nilidhani wewe na Joram Kiango mna aina fulani ya uhusiano. Sijui namna yoyote ya kumpata Joram, ndipo nikaona nikuarifu wewe kabla ya kulipeleka suala hili kwa wakuu wangu ambako linaweza likatangazwa ovyo au kupuuzwa. Kama nimekosea, Inspekta, naomba radhi…”
“Sijakuelewa Joram anahusika vipi na huyu marehemu?” Kombora aliuliza, moyoni akitetemeka kidogo kwa jibu atakalopata.
“ Yawezekana huyu marehemu ni Nuru, yule mwenzi na mpenzi wake Joram Kiango. Kama ndiye…”
“Hukuona mzee?” Brashi alikatiza mawazo yake. “Hukuona? Basi nitalazimika kumfunua tena marehemu.”
“Kuona nini?”
Kombora alijaribu kumzuia, lakini alichelewa. Tayari alikwishamgeuza maiti chali. Kombora alilazimika kulitazama tena jeraha hilo.
Bado lilikuwa halitazamiki. Utalitazamaje jeraha ambalo lilikuwa zaidi ya jeraha? Pale ambapo palitakiwa kuwa na uso wa msichana huyo, toka sikio hadi sikio, na paji la uso hadi kidevu, badala yake palikuwa na shimo la kutisha lililokuwa limekula nyama zote na kuacha mifupa mitupu. Pale yalipostahili kuwepo macho, pua, midomo na ulimi sasa yalikuwa mashimo ambayo yaliacha wekundu wa nyama na damu uonekane kiasi cha kutisha zaidi ya fuvu lolote la binadamu.
Safari hii, akitazama kwa makini zaidi, Kombora aliweza kubuni kilichokula nyama hiyo. Kama si biological weapon ya kisasa zaidi ambayo inatoa wadudu wadogo na wengi sana ambao wanashambulia nyama ya binadamu kwa dakika kadhaa kabla ya kufa, basi ni aina kali sana ya asidi ambayo ilimchoma binti huyo uso mzima na kuacha mifupa mitupu.
“Unaona mzee?” Brashi alimzindua.
“Nini?”
“Tazama hapa,” alielekeza mkono wake pale ambapo palistahili kuwa kinywa, ambapo sasa palikuwa na meno yaliyotokeza kana kwamba yanalia au yanacheka. Kombora aliinama na kuchungulia. Ndipo alipoweza kukiona kipande cha karatasi kilichokuwa kimelazwa humo kinywani. Kilikuwa na maandishi. Kombora aliinama na kuyasoma.
“TUNAMTAKA JORAM KIANGO”
Kombora aliyasoma kwa mara ya pili kabla hajaupata ujumbe huo. Alipoupata aliingiza mkono wake mfukoni na kutoa kitambaa. Akakizungushia katika vidole vyake na kuvididimiza humo kinywani hadi alipofikia hicho kipande cha karatasi. Alikichukua na kukizungushia katika kitambaa hicho na kisha kukitia mfukoni mwake.
Baada ya hapo alimgeukia Brashi na kumwambia, “Sikia sajini, umefanya kazi nzuri. Wanamtaka Joram Kiango. Tutampa ujumbe wao.” Alimkazia macho kabla hajaendelea, “Sasa unaweza ukaendelea na taratibu zako zote, kama kawaida. Tafadhali nitaomba unipe taarifa kamili ya upelelezi wenu juu ya mauaji haya mara mtakapokuwa tayari. Sawa?”
Brashi alitikisa kichwa.
“Na unajua sajini? Sikio la mtu yeyote nje ya chumba hiki lisisikie kuwa mauaji haya ni salamu tu kwa Joram Kiango. Nataka iwe siri, tafadhali.”
“Bila shaka Inspekta.”
“Ngoja nikuonyeshe,” alisema akiinama tena kitandani na kumshika maiti.

***​
HADITHI ilikuwa fupi na nyepesi. Kwa jina aliitwa Sofia Ali, mzaliwa wa huko Dodoma, wilayani Mpwapwa. Alikuja Dar es Salaam kama ilivyowatokea wasichana wenzake wengi wa hirimu yake. Amemaliza shule darasa la saba hana kazi wala mchumba. Jirani, mke wa bwana fulani huko Dodoma mjini anatokea na kumshahuri wafuatane naye mjini kumtunzia nyumba. Mshahara? Mia tano kwa mwezi. Chakula bure, malazi bure, nguo alizochoka nazo mama mwajiri bure, Akatae? Kama wengi wengine Sofia alijikuta yuko mjini.
Maji ya bomba ya mara kwa mara, chai ya maziwa kila asubuhi, chakula chenye viungo vyote; pamoja na ile dokoadokoa ya vipodozi vya mama ilifichua kiumbe mrembo aliyejificha katika umbo lile lililochakaa la Sofia Ali.
Badala yake, miaka miwili baadaye, aliyesimama mbele ya mama mwajiri alikuwa Sofia mwingine kabisa, Sofia aliyewiva, Sofia aliyejaza, Sofia ambaye alimfadhaisha baba mwenyenyumba na kumtisha mama. Matokeo yake Jumapili moja alipewa tiketi ya kurudi Mpwapwa. Kufanya nini? Kazi basi.
Hakurudi Mpwapwa. Akafuate nini? Jembe na mpini wake? Amwachie nani starehe za sinema na muziki ambazo ndio kwanza alikuwa ameanza kuzionjaonja? Rafiki yake aliyekuwa akiishi Tambuka Reli, ambaye alikuwa ameanza kujitegemea baada ya kupitia mkondo huohuo, alimpokea.
Chumba chao chenye upana wa futi tano kilibeba kitanda chao cha futi tatu na majukumu yote ya jiko, ghala; na mengineyo. Ungewatembelea mchana wakati wa joto, huku moshi ukiwaadhibu, usingekosa kuwahurumia. Lakini waone jioni, wakati tayari wameoga, wamevaa na kujitengeneza usingekosa kujiuliza kwa nini hawajatokea wachumba wakawaoa.
Mwaka mmoja baadaye, Sofia alikuwa Sofia hasa. Hata shoga zake walianza kumchukia kwa wivu. Hakujali, kwani alikuwa na marafiki wengi wa kiume kuliko wa kike. Na ni hao ambao aliwahitaji. Wakati huo hata jina alianza kulibadili. Badala ya Sofia sasa alijiita Soffy. Na alipenda sana baba yake aitwe Ally badala ya Ali. Hata lugha yake ilianza kubadilika. Katika kila sentensi alijikuta akiweka walau neno moja la Kiingereza. Hakujua kilipotokea hicho Kiingereza chake Lakini alikuwa na hakika nacho.
Sofia alifanya kosa. Mimba iliingia bila taarifa wala hiyari. Bwana hakumjua wala hakuhitaji mtoto. Alimeza vidonge mimba ikafa. Miezi miwili baadaye mimba ya pili ilimkamata. Hii haikusikia vidonge. Miezi mitatu, minne, mitano! Kila mtu alianza kumshuku. Elfu tatu zilimaliza kazi. Daktari mmoja asiye na huruma, alifanya kazi hiyo na kutupa mtoto anakokujua. Sofia aliponea chupuchupu. Baada ya miezi mitatu ya maumivu, afya yake ilimrudia. Mji wa Dodoma akauona nuksi. Huyoo, akaingia Dar es Salaam.
Dar ilimlaki juujuu. Rafiki yake mmoja wa Kinondoni, akijua kuwa umbo la Sofia lingemwongezea riziki, alimkaribisha kwake na kumwonyesha mji. Madisko ya Lang’ata na Ushirika yaliwakoma. Madansi ya DDC na Friend’s Corner yaliwatambua. Mabaa ya Sky Way na Kilimanjaro, yaliwaheshimu. Mabwana walikuwa tele, wa kila kabila na kila rangi. Sofia hakujua kumkataa mtu. Ni yeye aliyeanzisha msemo wa “… Ni pochi yako tu.”
Jioni ya leo alikuwa katika Hoteli ya Sky Way, ndipo alipomwona yule kijana mrefu, mnene, ambaye alikuwa akinunua vinywaji kwa fujo kuliko mtu mwingine yeyote hotelini hapo. Na mifuko yake bado ilionekana kuwa imetuna. Wasichana wengi waliokuwa wakimzengeazengea walipewa bia na kufukuzwa toka mezani pake. Sofia hakuwa mtu wa kuomba bia. Yeye huitwa au kufuatwa. Alimtupia jicho moja tu kijana huyo na kuona tayari ameimeza ndoano yake. Hakukosea kwani dakika mbili baadaye alianza kuletewa bia, oda ya kijana huyo. Na dakika kumi baadaye tayari waliketi pamoja, na kuanza kushikanashikana.
“Unasemaje?
“Pochi yako tu, darling.”
“Kiasi gani?”
“Hata wewe? Nilidhani umesoma, brother.”
Maongezi yao yaliishia katika kimojawapo cha vyumba vya hotelini. Baada ya nusu saa ya vilio na vicheko vya uongo na kweli Sofia alipokea “pochi” yake. Wakati akijiandaa kuondoka kijana huyo alimshika mkono na kumwambia, “Unajua Soffy, ni tamaa tu iliyonifanya niamue kuanguka nawe. Kwa kweli, nina rafiki yangu mpenzi, mwenye kitita cha pesa, kuliko hiki changu ambaye amenituma hapa Sky Way kumtafutia mwanamke mzuri. Kweli, hata hizi pesa nilizokuwa nikizinywa ni zake, kama hujachoka nikupeleke.”
“Kuchoka!” Sofia alicheka. “Nani aliwahi kuchoka kupokea pochi? Kama una wivu, I can understand, kama huna nipeleke.”
Kisha, Sofia alishituka na kusita kidogo wazo jipya lilipomjia. “Huyo, rafiki yako, What is his name?” aliuliza.
“Jina simfahamu.”
Why! Ni binadamu kweli?”
“Sema, maana mambo ya siku hizi you can’t understand. Mimi sijachoka kiasi cha kumvulia underware yangu mnyama.”
Kijana huyo alicheka. “Unadhani mimi ni crazy kiasi hicho? Huyo ni mtu mwenye hadhi na heshima zake. Naamini hujapata kukutana na mtu mzito kama huyo.”
Bado Sofia alisitasita kidogo. “Jina humjui. Wewe mwenyewe unaitwa nani, honey?”
“Niite Ram Shog.”
“Na huyo friend wako yuko wapi?”
Alipomalizia kuvaa, Ram alimshika mkono Sofia na kumwambia, “Twende nikupeleke. Amepata chumba katika Hoteli ya Pongwe.”

***​

AKIWA mgeni katika hoteli hiyo, Sofia alivutiwa mara tu baada ya kushuka toka katika teksi iliyowaleta. Ram akamwongoza hadi mapokezi ambako aliomba ufunguo wa chumba namba 108. Walipanda ngazi hadi ghorofani ambako walifungua na kuingia hadi chumbani.
“Itabidi umsubiri,” Ram alimwambia Sofia ambaye alikwishajitupa juu ya kitanda na kujilaza. Usingizi wa pombe ukamchukua.
Hakuamka tena hadi majuzi, meneja wa hoteli alipojaribu kumwamsha na, hatimaye, Sajini Brashi alipomgeuza na kukutana na uso ule ambao aliokutana nao.
 
endelea kuleta mambo tunakusubiria......!!!
 
Mkuu jana peterchoka Hiki kitabu jana nimekikuta maeneo ya posta mpya.. Sema nikanunua mtambo wa Mauti na Jumatatu nakwenda kukinunua hiki... Jana nimesoma Mtambo wa Mauti nikahisi Kueukaruka kwa Utamu na Hisia
 
Mkuu jana peterchoka Hiki kitabu jana nimekikuta maeneo ya posta mpya.. Sema nikanunua mtambo wa Mauti na Jumatatu nakwenda kukinunua hiki... Jana nimesoma Mtambo wa Mauti nikahisi Kueukaruka kwa Utamu na Hisia
posta mpya mtaa gani huo maana hivi vitabu adimu sana mtaani, inabidi tuvizie humuhumu
 
peterchoka pale kwenye sanamu la askari ukifika iwapo unatoka njia ya posta angalia upande wako wa kushoto utaona kituo cha tax kabla ya new africa hotel lakini upande ule ule utaviona pale....
 
au kama unatoka st joseph ipite new africa hotel and casino upande wako wa kulia utaona tax nenda na upande ule ule mbele kidogo utaviona vimepangwa vizuri.. Vipo vingi sana... Tutarudi na Roho zetu, mtambo wa mauti, roho ya paka. Mikononi mwa nunda, dimbwi la damu na Salamu toka kuzimu. Pia kuna vya watunzi na waandishi wengine
 
basi karibia pale ujichukulie... Jana nilitamani nichukue hata vitatu sema pesa niliyonayo ilikuwa ya mambo mengine
 
Cookies are required to use this site. You must accept them to continue using the site. Learn more…