HADITHI: Mimi ni Mwenye Dhambi, Nisamehe Mungu

HADITHI: Mimi ni Mwenye Dhambi, Nisamehe Mungu

Kanungila Karim

JF-Expert Member
Joined
Apr 29, 2016
Posts
20,746
Reaction score
25,672
MIMI NI MWENYE DHAMBI, NISAMEHE MUNGU 1
MTUNZI: NYEMO CHILONGANI
SIMU: 0718 069 269
MAHALI: DAR ES SALAAM
INSTAGRAM: nyemochilongani

Mwenyekiti wa Chama cha Vijana cha Casfeta (Christian Ambassador Students Fellowship Tanzania), Samuel Mpelele alikuwa akiendelea kuhubiri katika mkutano wa Injili uliokuwa ukifanyika katika Uwanja wa mpira wa Chekereni.

Huo ulikuwa mkutano wa Injili ulioandaliwa na vijana waliookoka mkoani Kilimanjaro. Watu walikuwa kimya uwanjani hapo huku wakimsikiliza Samuel ambaye alikuwa akitiririka jasho jingi huku akiendelea kuhubiri mahali pale.

Kila mtu alikuwa akiingiwa na maneno yale ambayo alikuwa akiyaongea katika mkutano ule kwa kutumia kipaza sauti kilichoonganishwa na spika kadhaa zilizokuwa katika uwanja huo. Samuel alionekana kujawa na nguvu za Mungu, kadiri alivyokuwa akihubiri na ndivyo ambavyo watu walizidi kupiga makofi huku wengine wakianza kulia.

Huo ulikuwa ni mkutano wa pili kuandaliwa na wanafunzi wa Chama cha Casfeta mkoani Kilimanjaro, mkutano ambao ulikuwa ukiongozwa na mwenyekiti wa chama hicho mkoani hapo, Samuel Mpelele, mwanafunzi aliyekuwa akisoma katika shule ya Uhuru hapo Kilimanjaro. Watu waliokuwa wakimsikiliza ambao hawakuwa wameokoka, siku hiyo wakaokoka kwani maneno ambayo alikuwa akiongea mahali pale yalionekana kumgusa kila mmoja.

Samuel Mpelele alikuwa mtoto wa mchungaji Christopher Mpelele wa Kanisa la Praise and Worship lililokuwa Mwenge jijini Dar es Salaam. Kwa sababu alizaliwa katika familia iliyomjua Mungu, familia iliyomcha Mungu, Samuel akajikuta akimuabudu Mungu maishani mwake huku wazazi wake wakiwa muongozo mkubwa katika maisha yake.

Mara nyingi Samuel alikuwa akielekea kanisani na kumuona baba yake akihubiri, moyoni alifurahi kupita kawaida, nae akaanza kujisikia msukumo wa kufanya kama ambavyo baba yake alivyokuwa akifanya kila alipokuwa madhabahuni. Katika kipindi hicho, kumuona mtu akiwa anahubiri ndicho kilikuwa kitu ambacho kilikuwa kikimfurahisha mno maishani mwake.

Maisha ya Samuel yakawa ni kwenda kanisani na kumuomba Mungu aweze kuonekana katika maisha yake tu. Moyoni mwake alikuwa akijisikia wito kabisa kwamba nae alitakiwa kuwa kama baba yake kuhubiri madhabauni.

Mchungaji Mpelele tayari aliiona karama ya uhubiri aliyokuwa nayo mtoto wake, alichokifanya ni kuanza kumpa ushirikiano katika kila kitu juu ya karama ambayo alikuwa nayo.

Huo ulikuwa ni wakati ambao Samuel alikuwa darasa la saba, alipomaliza shule, matokeo yake hayakuwa mazuri na hivyo kupelekwa katika shule ya Sekondari ya Uhuru iliyokuwa mkoani Kilimanjaro. Huko, Samuel akajiunga katika Kikundi cha Casfeta, kikundi kilichoanza kumuweka karibu na watu wengi ambao walikuwa wakimuabudu Mungu katika maisha yao shuleni pale.

Shule hiyo ilikuwa ni ya mchanganyiko, kulikuwa na wanafunzi ambao hawakwenda kanisa na wala hawakujua makanisa yalikuwa sehemu gani, kuna wanafunzi wengine ambao walikuwa wakielekea kanisani kila siku katika maisha yao lakini hawakuweza kubadilika, bado walikuwa wakiendelea kuvuta sigara na kunywa pombe pamoja na kufanya starehe za aina mbalimbali.

Ukiachana na hao, kulikuwa na Waislamu ambao wengi wao hawakuwa wakienda msikitini, tena mbaya zaidi wengine wakiwa watoto wa maustadhi wakubwa katika mikoa waliyotoka.
Wao pamoja na watoto wa wachungaji na viongozi wa makanisa mengine ndiyo waliokuwa wakiongoza kwa fujo na tabia chafu shuleni hapo.

Ukiachana na hao, kulikuwa na wanafunzi wengine waliokuwa Waislamu safi. Walikuwa wakielekea misikitini kuswali swala tano. Maisha yao yalikuwa tofauti na maisha ya watu wengine, walikuwa wakiishi kipole sana, hawakuwa wagomvi, walimheshimu kila mtu, kila wakati, walikuwa wakiongea maneno ya dini huku wakiwataka hata watu wengine wabadilike na kumuabudu Allah.

Kwa kifupi, shule ile ilikuwa na watu waliochanganyika ila kwa watoto wa wachungaji na maustadhi ndio ambao walikuwa wakiongoza kwa maovu shuleni pale.

Wao hawakupenda dini, walijiona kuzaliwa katika familia ambazo zilikuwa zikiijua dini, hivyo nao wakajiona kuwa hata kama wasingekwenda kanisani au msikitini, maisha yao yalikuwa na ulinzi wa kutosha.
Walimu hawakuyapenda maisha waliyokuwa wakiishi vijana hao, mara kwa mara walijitahidi sana kuwarekebisha lakini maneno yao hayakusaidia chochote kile, bado vijana hao waliendelea kuwa hivyohivyo.

Shule nzima, watoto wa viongozi wa dini ndio waliokuwa wakitenda yale waliyotakiwa kuyatenda kama wazazi wao. Kwa upande wa dini ya kikristo alikuwepo Samuel au Sam kama alivyojulikana, mtoto wa mchungaji wa Kanisa la Praise and Worship lililokuwa Mwenge jijini Dar es Salaam pamoja na Sadiki Hamidu, mtoto wa Ustadhi Hamidu ambaye alikuwa imamu katika msikiti wa kichangani uliokuwa Magomeni jijini Dar es salaam.

Wawili hao ndiyo waliokuwa mifano mizuri ya kuigwa shuleni hapo huku walimu wakiwataka wanafunzi wote kuishi maisha kama jinsi watu hao wawili walivyokuwa wakiishi. Wanafunzi hawakuonekana kuelewa, kila siku walikuwa wakivuta bangi huku matendo ya ngono yakiwa ya hali ya juu kupita kawaida.
“Inasikitisha sana Sadiki kila ninapowaona vijana wenzangu wa Kikristo wakiwa wanafanya matendo machafu kama wafanyayo,” Samuel alimwambia Sadiki huku akionekana kuwa na huzuni.

“Wewe ni kama mimi Samuel. Waislamu tunatakiwa kuswali swala tano kwa siku na kufuata nguzo tano za Kiislamu lakini wenzangu hawataki kufuata kama Allah anavyotaka tufanye. Inaniuma sana Samuel,” Sadiki alimwambia Samuel kwa sauti ya unyonge. Wawili hao walikuwa pamoja japokuwa walikuwa viongozi wa dini tofauti. Wao ndio waliokuwa chachu kubwa ya kuwafanya watu waliokuwa na dini tofauti kuwa pamoja zaidi.

Shuleni hapo hakukuwa na mitafaruku ya kidini, hakukuwa na mtu ambaye alikuwa akiidharau dini ya mwenzake, kila mtu alijiona sawa na mwenzake mbele za Mungu. Bado Samuel alikuwa akiendelea kuhubiri, watu walionekana kumkubali kupita kawaida, kila wakati watu walikuwa wakitikisa vichwa vyao kuonyesha ni jinsi gani walikuwa wakimkubali Samuel aliyekuwa akiendelea kuhubiri. Mara baada ya mkutano kumalizika, akawaita watu ambao walitaka kufanyiwa maombezi, akawafanyia maombezi na mkutano kufungwa.

Hayo ndio yalikuwa maisha yake shuleni hapo. Kila siku alikuwa akimuabudu Mungu na kumuomba usiku na mchana, alimtegemea Mungu zaidi ya alivyowategemea wazazi wake katika maisha yake.
Taaluma yake darasani wala haikuwa mbaya, ilikuwa ikiridhisha sana kiasi kilichomfanya kuwa miongoni mwa wanafunzi kumi ambao walikuwa wakifanya vizuri shuleni hapo.

“Unapaswa kubadilisha maisha yako na kumfuata Yesu Kristo Catherine,” Samuel alimwambia Catherine, msichana aliyekuwa akimuoneshea hisia za kimapenzi toka zamani shuleni hapo.
“Nimeshindwa mchungaji. Nimeshindwa kabisa,” Catherine alimwambia Samuel kwa sauti ya chini iliyosikika kimahaba.

“Kwa nguvu zako kamwe hautoweza. Muache Mungu ayabadilishe maisha yako. Unapoelekea si sehemu ambayo Yeye anataka wewe uende,” Samuel alimwambia Catherine.
“Kwa hiyo nifanye nini mchungaji?”
“Muombe sana Mungu akubadilishe.”
“Na kama nikishindwa kubadilika?”
“Mungu ashindwi kitu au labda uwe haujaamua moyoni mwako. Ukiamua, Mungu ashindwi kitu chochote katika maisha yako,” Samuel alimwambia Catherine.

Hayo ndio yalikuwa maneno ambayo kila siku Samuel alikuwa akimwambia Catherine juu ya maisha yake. Catherine alikuwa akijitahidi sana kuishi katika maisha ya kutotenda dhambi lakini bila kulazimishwa, mara kwa mara alijikuta akitenda dhambi.

Kuna kipindi kikafika, Catherine akajiona kushindwa kabisa kuuzuia moyo wake hasa pale ulipoamua kumuingiza Samuel. Akazidi kumpenda mvulana huyo na kumhitaji kupita kawaida. Japokuwa Catherine alikuwa akijua fika kwamba alikuwa akimpenda Samuel lakini aliogopa kumfuata na kumwambia ukweli juu ya mapenzi aliyokuwa nayo juu yake, hivyo akaamua kubaki na dukuduku moyoni mwake.

Siku zikaendelea kukatika mpaka kufika kipindi ambacho Catherine akajiona kushindwa kujizuia kabisa, akaona hakuwa na jinsi na wala asingeendelea kubaki kimya, hivyo akaamua kumfuata Samuel kwa lengo la kumwambia ukweli bila kujali Samuel angemchukuliaje.

“Unasemaje?” Samuel aliuliza huku akionekana kutokuamini.
“Ninakupenda mchungaji.”
“Ndio maana kila siku nakwambia muombe sana Mungu kama unataka ayabadilisha maisha yako. Bila Yesu ni kazi bure maishani mwako Catherine,” Samuel alimwambia Catherine.
“Nakupenda Samuel.”
“Hilo ni pepo. Njoo kwenye ibada yetu ya maombezi saa kumi jioni uje uombewe. Hilo ni pepo la uzinzi,” alisema Samuel, muda huo walikuwa darasani.
Samuel hakuridhika, alichokifanya ni kumfanyia maombi Catherine. Hiyo wala haikubadilisha kitu chochote kile, bado moyo wa msichana huyo ulikuwa kwenye mapenzi kwa Samuel.
“Ninashindwa Samuel,” alisema Catherine baada ya maombi.
“Unashindwa nini?”
“Kuacha kukupenda.”

“Haiwezekani. Haujataka kumruhusu Yesu kuingia moyoni mwako Catherine.”
“Nimemruhusu ila bado ninakupenda. Kadiri siku zinavyozidi kwenda mbele nazidi kukupenda Samuel,” Catherine alimwambia Samuel kwa sauti ya chini iliyojaa mahaba.
“Ngoja niendelee kukufanyia maombi” Samuel alisema huku akisimama.
“Ila usiniguse tena. Nifanyie maombi hivi hivi bila kunigusa” alisema Catherine, Samuel akashangaa.
“Kwa nini?”
“Unaponigusa......”
“Kuna nini?”
“Nasikia vijidudu vikinitembelea mwilini mwangu. Mwisho wa siku napata tabu hasa niwapo kitandani peke yangu usiku,” alisema Catherine.

Samuel akanyamaza kwa muda na kuanza kumwangalia Catherine usoni, uso wa Samuel ukaonekana kubadilika kama mtu ambaye alikuwa akimuona kiumbe fulani cha ajabu machoni mwake. Alichokifanya ni kuanza kumfanyia maombi Catherine bila kumgusa kama ambavyo alivyotaka iwe.

Hayo ndio yalikuwa maisha ambayo yaliendelea shuleni hapo, bado Catherine alionekana kuwa karibu na Samuel, kila siku alikuwa akitaka kufanyiwa maombi na Samuel lakini kamwe hakuweza kubadilika. Moyo wake ulionekana kuwa mgumu kubadilika, hakumruhusu Mungu kuubadili moyo wake, mapenzi yalikuwa yakimtesa kupita kawaida.

“Vipi mchungaji?” Sadiki alimuuliza Samuel katika kipindi ambacho alikuwa akionekana kuwa na mawazo.
“Mungu anahitajika sana kuyabadilisha maisha ya wanafunzi shuleni hapa. Kuna wengine wanatumiwa na shetani katika kutujaribu watumishi wa Mungu. Ila kamwe tutasimama imara” Samuel alimwambia Sadiki.
“Umekwishajaribiwa?” Sadiki alimuuliza.
“Ndio. Kuna yule msichana Catherine huwa kila siku anakuja, ishu yake ileile, nimfanyie maombi ila moyo wake hajauweka tayari kumpokea Yesu” Samuel alimwambia Sadiki.
“Pole sana ndugu yangu ila maisha yako hayatofautiani na mimi,” Sadiki alimwambia Samuel.
“Kwa nini?”
“Unamjua yule Mariamu msichana tunayesoma nae kidato cha tatu?” Sadiki aliuliza.
“Mariamu yupi? Wapo watatu darasani.”
“Yule mweupe.”
“Ninamfahamu.”
“Huwa kila siku ananitaka, mara kwa mara ananiandikia barua za kimapenzi,” Sadiki alimwambia Samuel.
“Mungu wangu!”
“Ndio hivyo. Jana tu alikwenda kuninunulia kanzu mpya pamoja na kofia kama zawadi” Sadiki alimwambia Samuel.

“Haya ni majaribu na inapaswa tuyashinde. Mungu wetu hashindwi” Samuel alimwambia Sadiki.
“Ndio hivyo. Ninapenda niendelee kumcha Allah katika maisha yangu. Sipendi kumpa ibilisi ruhusa ya kuyachezea maisha yangu. Namcha Allah si kwa sababu wazazi wangu wanamcha Allah, hapana, ninamcha Allah kwa sababu ninatakiwa kumcha Allah kwani Yeye ndiye muongozo wa maisha yangu” Sadiki alimwambia Samuel.

Hayo ndio yalikuwa majaribu yao ya kila siku. Mara kwa mara wasichana hao walionekana kama kutumwa na shetani kwa ajili ya kuwajaribu katika maisha yao. Japokuwa walikuwa wakiwaepuka sana lakini kila siku walimuomba Mungu aweze kuwashindia katika vita hivyo ambavyo kwao vilionekana kuwa vigumu sana, walihitaji msaada wa Mungu kuyashinda majaribu hayo ambayo kwao yalionekana kuwa makubwa zaidi ya uwezo wao.

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 02

Wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Uhuru wakazidi kubadilika kadiri siku zilivyozidi kwenda mbele. Vilevi vilikuwa vikiingizwa shuleni hapo kinyemela pasipo uongozi wa shule kufahamu kitu chochote kile.
Kutokana na asilimia kubwa ya wanafunzi waliokuwa wakisoma shuleni hapo kuwa wa kutwa waliokuwa wakiishi nyumbani, mara nyingi waliwachukua wenzao wa bweni na kuwapeleka katika kumbi za starehe nyakati za usiku.

Idadi kubwa ya wanafunzi walikuwa wakiondoka usiku na kwenda katika kumbi za starehe, hakukuwa na mwalimu yeyote ambaye alikuwa akifahamu kile kilichokuwa kikiendelea mahali hapo kutokana na walimu wawili tu waliokuwa wakibaki shuleni hapo kulala mapema sana.

Walinzi ndio waliokuwa wakicheza mchezo mzima ambao ulikuwa ukifayika kwa wanafunzi. Wao ndio waliokuwa wakiwaruhusu wanafunzi kutoroka shuleni hapo na kuingia mitaani huku wakihongwa kiasi fulani cha fedha.

Wanafunzi wa kike hawakuweza kujizuia, huko walipokwenda walikuwa wakifanya ufuska na hata wakati mwingine kujiuza kutokana na kutokuwa na fedha za kutumia shuleni. Kadiri siku zilivyozidi kwenda mbele na ndivyo ambavyo shule ile ilivyozidi kuharibika kiasi ambacho hata wazazi wengi ambao watoto wao walikuwa shuleni pale kuanza kuingiwa na hofu. Taaluma za wanafunzi zilishuka chini kila siku jambo lililowashangaza hata walimu wenyewe.

Hapo ndipo walimu walipoonekana kugundua kitu. Kiranja, John Gilipa ambaye alionekana kuwa mnoko shuleni hapo akaenda kuwaambia walimu juu ya kile ambacho kilikuwa kikiendelea nyakati za usiku.
Hatua ya kwanza ambayo ilichukua uongozi wa shule ni kumkamata mlinzi na kumfikisha katika kituo cha polisi kwa yale aliyokuwa akiyafanya, kupokea fedha na kuwaruhusu wanafunzi usiku kwenda katika kumbi za starehe zilizokuwa mitaani.

“Unasema ilikuwaje jana usiku?” Mwalimu wa zamu alimuuliza Kiranja mkuu, John ambaye alikuwa ameleta kesi ofisini hapo.
“Kitanda changu kilimwagiwa maji, tena nahisi ndoo zaidi ya tatu,” John Gilipa alijibu huku akionekana kuwa na hasira.
“Nani aliyefanya hivyo?” Mwalimu wa zamu, Salumu Issa aliuliza.
“Sijui.”
“Wewe unamuhisi nani?”
“Simuhisi mtu yeyote. Ila nadhani bweni zima linahusika,” alisema John.
Siku hiyo ikaonekana kuwa mbaya kwa wanafunzi ambao walikuwa wakiishi katika bweni alilokuwa akiishi kiranja mkuu, John. Mchana wote walikuwa wakipewa adhabu huku wakichapwa fimbo za uhakika na kutakiwa kuwataja watu ambao walikuwa wamehusika katika kulimwagia maji godoro la John lakini hakukuwa na mtu aliyesema kitu chochote kile.

Visa havikuisha, mara baada ya adhabu ile wanafunzi wakaonekana kumkasirikia John kitendo ambacho wengi hawakutaka kuongea nae. John akaonekana kuwa mpweke, wavulana wa shule nzima walikuwa wamemtenga, ni Samuel na Sadiki tu ndio ambao walikuwa wakiongea naye. Aliishi shuleni pale kama mkimbizi, mtu ambaye hakuwa na amani yoyote ile.

Kila siku godoro lake lilikuwa likimwagiwa maji jambo lililomfanya kulipeleka godoro lake ofisini kwa walimu, asubuhi alikuwa akilipeleka ofisini na usiku alikuwa akilichukua na kwenda nalo bwenini kulala. Shuleni, aliendelea kuwa na maisha ya unyonge jambo lililoishusha kiwango chake katika taaluma.
“Hata kama dunia nzima itakutenga, hata kama wazazi wako na ndugu zako watakutenga, jua kwamba kamwe Mungu hawezi kukutenga endapo utamtumikia,” Samuel alimwambia John ambaye alionekana kuhitaji msaada.

“Najiona kuwa katika wakati mgumu sana mchungaji. Wakati mwingine natamani kujiua” John alimwambia Samuel.
“Kujiua! Unadhani hilo litakuwa suluhisho la tatizo lako? Unadhani kujiua kutakufanya kupumzika kwa amani? Ukijiua utakuwa umeua na adhabu yako itakuwa ni moto wa milele. Hautakiwi kufanya kitendo kama hicho. Muachie Mungu” Samuel alimwambia John.
“Sawa. Ila kwanza nataka kuokoka. Nataka kumpa Mungu maisha yangu” John alimwambia Samuel.
“Hakuna tatizo” Samuel alimwambia John na kisha kuanza kumuongoza sala ya toba
.
****
Kila siku Sadiki alikuwa mtu wa kushinda na kitabu kitakatifu cha Qur-an akijisomea bwenini kwake juu ya kitanda huku mkononi akiwa na Tasbihi yake ambayo ilionekana kumpa nguvu ya kuendelea kusoma kitabu kile. Maishani mwake, hakukuwa na kitu ambacho alikuwa akikipenda kukifanya kama kuswali.
Kila siku alikuwa akifanya ibada bwenini au hata msikitini. Sadiki hakuonekana kuwa radhi kupita muda wa swala bila kuswali. Kufanya swala ndio ilikuwa sehemu ya maisha yake shuleni hapo, kila alipokuwa akihitajika kufanya swala alikuwa akifanya kama kawaida.

Wanafunzi wa dini ya Kiislamu ambao walikuwa wakitaka kuyabadilisha maisha yao, Sadiki ndiye alikuwa mtu pekee ambaye alikuwa akiwapa mafunzo mbalimbali kuhusiana na dini ya Kiislamu pamoja na mambo mengi mema ambayo alikuwa amefanya Mtume Muhammad S.A.W.

Kwa sababu maisha yake yalionekana kuwa matakatifu, hata wanafunzi ambao walikuwa wakiyapokea mafundisho yake nao walikuwa wakijitahidi kuishi maisha kama aliyokuwa akiishi Sadiki. Muda mwingi, mavazi ya Sadiki yalikuwa ni kanzu nyeupe zilionekana kung’aa sana katika kila kipindi ambacho alikuwa akizivaa.

“Jumaa Qareem,” Sadiki aliwaambia wanafunzi wenzake waliokuwa wamekaa nje ya bweni wakipiga stori.
Kila mmoja akakunja uso, mtu kama Sadiki au Samuel hawakuwa watu ambao walihitajika katika shule hiyo, wanafunzi shuleni hapo walionekana kutamani kuendelea kuishi maisha ambayo walikuwa wakiyaishi, maisha ya uchafu ambayo hayakupendeza hata machoni mwa mwanadamu.

Kitendo cha Sadiki na Samuel kuzipenda dini zao na kupenda sana kuabudu vilikuwa vitu pekee ambavyo vilikuwa vikiwakasirisha wanafunzi wengi mahali hapo.
“Ananikera huyu jamaa,” alisema mwanafunzi mmoja aliyekuwa akijulikana kwa fujo shuleni hapo, Chepuo.
“Hahaha! “ Wenzake wote wakaanza kucheka.
“Yaani kuna huyu jamaa na yule mwenzake, wananikera sana, kila ninapowaona natamani kuwaua,” Chepuo aliwaambia wenzake.

“Wapotezee tu. Hawana jipya hao.”
“Haiwezekani. Acha leo niende kuyamwagia maji magodoro yao,” alisema Chepuo huku uso wake ukionekana kuwa na hasira juu ya watu hao.

Chepuo alikuwa mwanafunzi wa kidato cha tatu, mwanafunzi aliyekuwa na fujo kuliko wanafunzi wote shuleni hapo. Kwake, hakuwahi kushika Biblia wala Qur-an , alikuwa akizichukia dini zote kupita kawaida.
Alijijua kabisa kwamba wanafunzi wengi wa shuleni hapo walikuwa wakimuogopa, hivyo alitaka kuigawa shule hiyo. Alitamani wanafunzi wengi wawe katika kundi lake ambalo angeliongoza kuleta fujo za mara kwa mara shuleni hapo pamoja na migomo isiyokuwa na sababu yoyote ile.

Kutokana na kutopenda dini yoyote ile, ikawa sababu kubwa ya kuwachukia Samuel na Sadiki shuleni hapo. Kila alipokuwa akiwaona, hasira za waziwazi zilikuwa zikimkaba kooni mwake huku kila siku maombi yake yakiwa ni kumtaka Mungu awaue watu hao ambao walionekana kuwa chukizo mbele za uso wake zake.

Usiku ukaingia, wanafunzi wakaanza kwenda darasani kusoma kama ambavyo ratiba ilivyokuwa ikisema. Katika kipindi hicho, Chepuo alikuwa darasani pamoja na marafiki zake. Kama kawaida, hakuwa akisoma zaidi ya kupiga stori za mitaani na wenzake ambao walikuwa wamemzunguka. Maisha, kwake yakaonekana kuwa si lolote lile, elimu ambayo alitakiwa kuipata mahali hapo haikuonekana kuwa na faida yoyote ile katika maisha yake ya mbele.

Hakujali kitu chochote kile, yeye ndiye aliyekuwa akiwaongoza wanafunzi wengi kufanya maovu mpaka kuanzisha kikundi chake kilichokuwa na wanafunzi ishirini ambacho alikuwa akikiita ‘Black Ninja’.
Black Ninja ndilo lilikuwa kundi la kihuni ambalo kazi yake kubwa lilikuwa ni kufanya fujo shuleni hapo. Kila siku walikuwa wakiwafanyia fujo wanafunzi wengine na hata katika kipindi kingine kutoka na kwenda katika shule ya Majengo, Northern Highland, Majengo na shule mbalimbali kufanya fujo. Wanafunzi ambao walikuwa katika kundi hilo walionekana kuwa wachochezi wakubwa katika kuifanya shule hiyo kutawaliwa na mambo ya ajabuajabu.

Chepuo ndiye alikuwa kiongozi wao ambaye kila siku kazi yake ilikuwa ni kuhakikisha kwamba kila kitu kinakwenda sawa. Hakuonekana kuridhika na idadi ya wanafunzi ambao walikuwa katika kundi hilo, akazidi kuwaongeza wanafunzi wa kiume na wa kike huku muonekano wao ulionekana kuwa kama watu waliopinda.

“Niandalieni ndoo mbili kubwa za maji. Nataka vitanda vyao usiku wa leo viwe mabwawa ya kuogelea,”Chepuo aliwaambia wenzake. Kwa haraka sana bila kupoteza muda vijana wawili wakasimama na kisha kuelekea nje ya darasa lile kwenda kuandaa ndoo mbili kubwa ambazo zilitakiwa kuwa na maji. Baada ya dakika ishirini, vijana wale wakarudi darasani mule.

“Vipi?” Chepuo aliwauliza.
“Tayari.”
“Mmeziweka wapi?” Chepuo aliuliza
“Katika mlango wa kuingilia bwenini.”
“Bweni lipo wazi?”
“Hapana. Limefungwa.”

Hapohapo Chepuo akasimama na kisha kutoka nje. Safari yake ikaishia katika darasa la kidato cha tatu B na kumwambia kiranja wa bweni kumpa ufunguo wa bweni lile. Japokuwa hakuwa akitakiwa kumpa mwanafunzi yeyote ufunguo wa mlango wa bweni lakini kwa Chepuo, kiranja yule akajikuta akimgawia.
Chepuo akatoka darasani humo na moja kwa moja kuelekea bwenini. Alipozikuta ndoo zile mlangoni, akaufungua mlango na kisha kuzibeba na kuingia nazo ndani.

Alichokifanya ni kuchukua ndoo moja na kumwagia katika kitanda cha Samuel na ndoo nyingine kumwagia katika kitanda cha Sadiki. “Leo watalala chini mbwa hawa” Chepuo alisema na kisha kuondoka bwenini hapo huku akimrudishia ufunguo ule kiranja wa bweni.

Ilipofika saa 4:00 usiku, kengele ikagongwa na hivyo wanafunzi kutakiwa kwenda mabwenini mwao. Kama kawaida yao, Samuel na Sadiki wakaanza kuelekea bwenini huku wakiongea kwa furaha bila kujua kwamba magodoro yao yalikuwa yameloanishwa maji dakika kumi zilizopita.

Chepuo hakuonekana kuwa na wasiwasi, muda wote alionekana kuwa na furaha juu ya kile ambacho alikuwa amekifanya bwenini. Yeye na wenzake wakaanza kuelekea bwenini. Macho yake hayakutoka kwa Samuel na Sadiki ambao walionekana kutokuwa na wasiwasi wowote ule.

Mpaka wanaingia bwenini, Chepuo alikuwa akiwaangalia huku wenzake wakiona ni kitu gani kingetokea mara baada ya watu hao kugundua kwamba magodoro yao yalikuwa yameloanishwa na maji. Walibaki wakiwaangalia, Samuel na Sadiki wakapanda katika vitanda vyao na kisha kulala.

Chepuo hakuamini kile ambacho alikuwa amekiona, hakuamini kama kulikuwa na watu ambao wangeweza kulala huku magodoro yakiwa yameloanishwa maji. Alichokifanya ni kumtuma kijana mmoja ambaye alikuwa mmoja wa wanachama wa kundi lake la Black Ninja kwa ajili ya kwenda kuhakikisha.

“Hebu kaangalie kama bado yameloa,” Chepuo alimwambia kijana yule ambaye alikwenda na baada ya sekunde kadhaa kurudi.
“Vipi?” Chepuo aliuliza.
“Mbona hayana maji.”
“Unasemaje?” Chepuo aliuliza huku akionekana kushtuka.
“Hayajaloa hata kidogo” Kijana yule alijibu.
Chepuo hakutaka kubaki mahali hapo, alichokifanya ni kwenda kuhakikisha yeye mwenyewe kujionea kama kile alichoongea kijana yule kilikuwa cha kweli au uongo.

Akafika katika kitanda cha Samuel, alipoligusa godoro, lilikuwa kavu kabisa. Hakuishia hapo, akaelekea mpaka katika kitanda cha Sadiki na kisha kuligusa godoro, nalo lilikuwa kavu kabisa jambo lililomfanya kupiga kelele ambazo ziliwashtua watu wote.

“Uwiiiiiii...kuna watu wachawi humu sijapata kuona,” Chepuo alisema kwa sauti kubwa na kuendelea:
“Kuna watu wachawi humu...kuna watu wachawi humu bwenini,” Chepuo alisema.
Tukio lile likaonekana kumchanganya mno, hakuamini kama magodoro yale hayakuwa yameloana na wakati yeye ndiye alikwenda na kuyamwagia maji usiku huo.

Akili yake kwa wakati huo haikuonekana kuwa sawa, ule ulionekana kuwa muujiza mkubwa. Alichokifanya ni kuanza kuelekea katika kitanda chake, alipoligusa godoro lake, lilikuwa limeloanishwa na maji mengi.

“Nani amemwagia maji godoro langu?” Chepuo aliuliza kwa hasira.
“Hata sisi hatujui kwani magodoro yetu pia yamemwagiwa maji,” Kijana mmoja alisema baadhi ya vijana wa kundi la Black Ninja ambao walikuwa humo wakiwa wamesimama kutokana na magodoro yao kuloanishwa na maji.

Mpaka kufikia hatua hiyo Chepuo alichanganyikiwa zaidi, godoro la Samuel na Sadiki hayakuwa yameloanishwa na maji na wakati alikuwa ameyamwagia maji. Godoro lake pamoja na magodoro ya vijana wenzake waliokuwa katika kundi la Black Ninja yalikuwa yameloanishwa maji. Haikutokea kwa Black Ninja ambao walikuwa katika bweni lile tu, bali hata wale waliokuwa katika mabweni mengine, nao magodoro yao yalikuwa yamemwagiwa maji, mmwagaji wa maji yale katika magodoro yale hakujulikana kwani katika kipindi ambacho walikuwa wakijisomea darasani, mabweni yalikuwa yamefungwa na funguo.

Je nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 03

Asubuhi ya siku iliyofuata, kila mtu aliyesikia taarifa kuhusiana na kile ambacho Chepuo alikuwa amekifanya bwenini cha kuloanisha maji magodoro ya Samuel na Sadiki lakini hayakuwa yameloana zaidi ya godoro lake pamona na vijana wake,walikuwa wakicheka. Hakukuwa na mtu ambaye alikuwa akiamini kama kile kitu kweli kilikuwa kimetokea au Chepuo alikuwa ametunga tu.

Asilimia kubwa waliamini kwamba kweli kile kitu kilikuwa kimetokea kutokana na muonekano ambao alikuwa nao Chepuo katika kila kipindi alichokuwa akiwangalia Samuel na Sadiki.
Baadhi ya wanafunzi wakawaogopa, tayari walijua fika kwamba katika kila hatua ambayo watu hao walikuwa wakiishi shuleni hapo, Mungu alikuwa akiwaangalia katika maisha yao.

Kwa upande mwingine, kasi ya Catherine na Mariamu wala haikuweza kupungua, kila siku walikuwa wakijiona kuwa na uhitaji wa kuwa na wavulana hao waliokuwa wamesimama imara katika misingi ya dini zao.
Kila mmoja alikuwa akimfuata mtu wake kwa nyakati tofauti, katika vipindi ambavyo walikuwa wakikaa darasani kujisomea na hata wakati wa kula chakula.

Walikuwa na wakati mgumu, Samuel na Sadiki walionekana kuwa na misimamo imara katika dini zao. Wanafunzi wengi walikuwa wakitamani kuishi maisha kama ya watu hao wawili waliyokuwa wakiishi lakini hiyo ikaonekana kuwa ngumu katika maisha yao.

Kuishi maisha kama ambayo Samuel na Sadiki walivyokuwa wakiishi ilimaanisha kwamba ilitakiwa uache kila kitu kichafu ambacho kilikuwa kikiendelea katika maisha yako.
Kama wewe ulikuwa mtu wa wanawake au wanaume basi katika ulitakiwa kuachana nao na hata kama wewe ulikuwa mtu wa kutoroka usiku na kuelekea disko pia ulitakiwa kuachana na mambo hayo yaliyokuwa magumu kuachika kwa baadhi ya wanafunzi ambao walikuwa shuleni hapo.

“Nataka nikununulie vitafunio leo,” Ilisikika sauti ya Mariamu akimwambia Sadiki. “Inshallah...! Mwenyezi Mungu akujalie....nashukuru sana. Ila naomba ninunue mimi mwenyewe,” Sadiki alimwambia Mariamu aliyekuwa akimwangalia macho yaliyojaa mahaba.

Mariamu hakuishia hapo, alijua fika kwamba Sadiki alikuwa amemkatalia kumnunulia vitafunio hivyo kitu alichotaka kufanya ni kumlazimisha kufanya kile alichokuwa akikitaka mahali hapo. Alipoona Sadiki amechukua chapati, kwa haraka haraka akatoa kiasi cha fedha cha chapati tatu na kisha kumgawia muuzaji.

Sadiki alitaka kuzuia jambo hilo lakini kwake ikaonekana kuwa ngumu kwani tayari Mariamu alikuwa amekwishamuwahi. Siku hiyo, Sadiki hakuonekana kuwa na amani, kila alipokuwa akimwangalia Mariamu, binti huyo mrembo naye alikuwa akimwangalia jambo ambalo liliyafanya macho yao kugongana kila wakati.

Kwa wote wawili, kitendo kile kikaonekana kuwa na madhara fulani, moyo wa Sadiki ukaanza kuyumba kidogo lakini akajitahidi sana kuuweka sawa ili kusiweze kuharibika kitu chochote kile. Kwake, tayari alijiona kama kutaka kuangukia dhambini jambo ambalo kamwe hakutaka kuliona likitokea katika maisha yake.
“Huyu ibilisi naona anataka kunizidi nguvu” Sadiki alijisemea macho yake yalipogongana na macho ya Mariamu, macho mazuri mithili ya mwanamke aliyekula kungu.

Tayari Sadiki akaanza kujiona wa tofauti, alichokifanya ni kuinuka na kisha kuelekea bwenini. Alipofika huko, hatua ya kwanza ilikuwa ni kuchukua kitabu Kitakatifu cha Qur-an na kuanza kukisoma. Japokuwa alikuwa ameanza kukisoma kitabu hicho mahali hapo, mawazo yake yalikuwa yakimletea picha ya Mariamu katika kipindi ambacho alikuwa akiangaliana nae.

Ukiachilia vitu hivyo, naye shetani akaanza kumuingizia picha za ajabu ajabu kichwani mwake. Mara taswira yake ikaanza kumuona Mariamu akiwa amesimama mbele yake huku akimchekea, mara akaonekana akivua nguo zake na kubakia na nguo ya ndani tu. Mawazo hayo hayakuishia hapo, ghafla yakabadilika na kujikuta yupo chumbani na Mariamu huku wote wakiwa watupu.

Mpaka kufikia hatua hiyo, Sadiki akashtuka kutoka katika lindi la mawazo hayo machafu na kisha kuchukua Tasbihi na kuivaa shingoni. Japokuwa akili yake ilimfanya kuhisi kwamba kufanya kitu kama kile kingeweza kumsaidia lakini hakuambulia kitu, bado shetani alikuwa akiendelea kumletea taswira za ajabuajabu kichwani mwake.
Kadri siku zilivyozidi kwenda mbele na ndivyo ambavyo hali yake ilivyozidi kubadilika zaidi na zaidi. Katika kipindi cha kwanza kila mawazo machafu yalipokuwa yakimjia alikuwa akijitahidi sana kujizuia lakini baadae akajikuta akishindwa kufanya hivyo.

Japokuwa hakutaka kumpa nafasi moyoni mwake, akashangaa kuona akianza kuyaruhusu mawazo juu ya Mariamu, mawazo yale ambayo yalikuwa yakimuonyeshea kuwa kitandani pamoja na Mariamu ndio ambayo yalikuwa yameanza kumtawala katika kipindi hicho. Baada ya mwezi mmoja, nguvu za Mungu ambazo alikuwa nazo Sadiki zikatoweka kabisa mwilini mwake.

Akamruhusu shetani kuzichezea hisia zake na mwisho wa siku akajikuta akihitaji kusoma na Mariamu katika darasa la kidato cha nne hasa katika kipindi ambacho wanafunzi wa kidato cha nne walikuwa wamemaliza shule mahali hapo. Kusoma kwao wawili huko ndipo ambapo kukaanzisha mambo mengine.
Mikono ya Sadiki ikaanza kuwasha, ikaanza kuhitaji kuushika mwili wa Mariamu, na bila hiyana yoyote, mtu ambaye alikuwa akijuliakana kama Ustadhi shuleni hapo, Sadiki akaanza kuyachezea mapaja ya Mariamu jambo lililomuweka kwenye hali nzuri ambayo hakuwahi kuipata kabla.

Hapo ndipo akili yake ilipofunguka kwa kuona kwamba kila siku alikuwa akijitahidi kutofanya kitu kile na wakati kilikuwa kizuri. Aliendelea kuyachezea mapaja ya Mariamu mpaka akaanza kuuhisi mwili wake ukianza kutembelewa na vidudu fulani, Sadiki akashindwa kujizuia. “Sasa unataka kufanya nini? Mbona unafungua mkanda wa suruali yako?” Mariamu aliuliza huku akijifanya kutokujua kitu kinachotaka kutokea.

“Hakuna mtu, darasa zima tupo peke yetu, tatizo nini?” Sadiki aliuliza huku akiendelea kuufungua mkanda kwa kasi ya ajabu, tayari hamu ya kufanya mapenzi ikawa imekwishamuingia.
“Hapana Sadiki. Hapa darasani, siwezi kufanya hivyo,” Mariamu alimwambia Sadiki ambaye akaonekana kunyong’onyea.

“Kwa nini sasa? Mbona mahali hapa pako salama kabisa,” Sadiki alimwambia Mariamu.
“Sehemu hii si salama Sadiki. Muda wowote wanafunzi wanaweza kuja.”
“Waje huku! Kufanya nini?”
“Kwani huku wanafunzi huwa hawaji?”
“Mara mojamoja sana. Form four washamaliza shule na kuondoka,” Sadiki alimwambia Mariamu.
“Hata kama. Hii skendo ustadhi.”
“Hilo si tatizo. Skendo si kitu cha kushangaza. Ni jambo la kawaida tu kama kumchungulia mwanamke bafuni,” Sadiki alimwambia Mariamu.

Sadiki alimuona Mariamu kama anamchelewesha, alichokifanya ni kuanza kumshikashika mapaja yake kwa mara nyingine tena. Katika kipindi hicho, Sadiki alionekana kusahau kwamba shuleni pale alikuwa akiheshimika sana kutokana na ushika dini ambao alikuwa nao, alionekana kusahau kabisa kama mwezi mmoja uliopita alikuwa mtu wa kuswali swala tano, kitu ambacho alikuwa akikitaka mahali hapo ni kufanya ngono na Mariamu ambaye kwa kipindi kirefu sana alikuwa akijipendekeza kwake.

“Siwezi....” Mariamu alisema na kisha kuifunika sketi yake na kuanza kutoka nje.
Sadiki akaonekana kushtuka, hakuamini kama Mariamu angeweza kuondoka darasani mule na kumuacha akiwa katika hali ile. Sadiki akainuka na kusimama, akajikuta akirudi tena kitini na kutulia kwani tayari alionekana kuwa tofauti.
“Mungu nisamehe,” Sadiki alisema kwa sauti ya chini.

Hiyo ndiyo ilikuwa siku ya kwanza kwa Sadiki kumuacha Mungu kimatendo, kuanzia hapo akaanza kumnyemelea Mariamu na hatimae mwisho wa siku kufanikiwa kutoroka nae na kwenda nje ya shule. Huko, wakafanya sana ngono, Sadiki akalipizia mara zote ambazo alikuwa akijifanya mtakatifu mbele za Mungu.
Huo ndio ukawa mchezo wao, mara kwa mara walikuwa wakiendelea kwenda huko na kuuufanya mchezo ule. Unafiki mbele za macho ya binadamu ukaendelea kufanyika.

Hakuacha kuvaa kanzu, hakuacha kuvaa kofia ya Kiislamu, hakuacha kutembea na Tasbihi, kila siku alikuwa akivaa mavazi hayo lakini moyoni alikuwa mzinifu mkubwa. Kasi zake za kwenda msikitini zikaonekana kuanza kupungua. Kila alipokuwa akiulizwa, sababu ilikuwa ni kujiandaa na mitihani ya mwisho wa mwaka kumbe ukweli ulikuwa ni kwamba alikuwa ameanguka dhambini. Mara kwa mara alikuwa akijitahidi kuomba msamaha kwa Mungu juu ya kile ambacho alikuwa akikifanya lakini kesho yake alikuwa akimchezea mapaja Mariamu na hatimae kufanya mapenzi.
Kila kilichokuwa kikiendelea kilionekana kuwa siri kubwa, Sadiki hakutaka mtu yeyote afahamu kile kilichokuwa kikiendelea kati yake na Mariamu.

Kufanya ngono kulipozidi sana, baadhi ya wanafunzi waliokuwa kwenye kundi la Black Ninja wakaonekana kufahamu hasa mara baada ya mara kadhaa kumfuma Sadiki akiwa na Mariamu wakitoka nje ya shule na kutokomea kusipojulikana. “Lazima niwaharibie. Halafu nasikia hata Samuel ndio zake hizo kwa yule Catherine. Lazima niwaharibie” Chepuo, kiongozi wa kundi la Black Ninja aliwaambia wenzake.
****
Mabadiliko ambayo yalikuwa yakitokea kwa Sadiki pia yakaanza kutokea mpaka kwa Samuel. Naye, taratibu akaanza kupiga stori sana na Catherine kitu ambacho wakati mwingine kilikuwa kikimsahaulisha na muda ambao alikuwa ameupanga wa kufanya maombi binafsi. Catherine akaanza kuuteka moyo wake, naye, akaanza kujiona akikosa nguvu katika kumtumia Mungu. Muda wa kwenda kwenye maombi binafsi alikuwa akijisikia uchovu mwingi mpaka wakati mwingine kulala. Mara kwa mara usiku alikuwa akiota ndoto za mbaya, alikuwa akiota akifanya mapenzi na Catherine, msichana ambaye alikuwa akimhitaji toka zamani.

Taratibu, nao mchezo wao ukaanzia katika kipindi ambacho walikuwa wakila chakula cha mchana. Mguu wa Samuel ulipougusa mguu wa Catherine bahati mbaya, kijotojoto alichokipata jumlisha na baridi lile la Kilimanjaro, akajihisi kabisa kuwa mtu wa tofauti. Alichokifanya, mara kwa mara akawa anaugusisha tena mguu wake miguuni mwa Catherine huku akiupandisha juu jambo ambalo likamfanya baadae kuanza kuupandisha zaidi na zaidi mpaka kufika mapajani.
Kwa sababu kulikuwa na meza katikati yao, hakukuwa na mwanafunzi ambaye alishtukia mchezo ambao ulikuwa ukifanyika kwa wawili hao kwani walionekana kuwa katika hali ya utulivu sana.

Mguu ule ukafika katika mapaja ya Catherine na hatimae kupitiliza kabisa. Shetani akaonekana kumshinda nguvu kwa wakati huo. Yule shetani ambaye mara kwa mara alikuwa akimkemea, katika kipindi hicho alionekana kuwa mjanja zaidi yake. Huo nao ukawa mwanzo wa kila kitu katika maisha ya wawili hao, kuchezeana ndio ikawa sehemu ya maisha yao shuleni hapo. Kadri siku zilivyokuwa zikizidi kwenda mbele, ulinzi wa Mungu hakuwa nao tena maishani mwake, aliamua kumuacha Mungu, nae Mungu akamuacha. Hapo ndipo maisha ya ngono yalipofunguliwa zaidi. Samuel akaanza kutoka sana nje ya shule pamoja na Catherine na kisha huko kufanya ngono. Huko ndipo ambapo wakakutana na Sadiki ambaye alikuwa pamoja na Mariamu, wakaungana pamoja na kuwa watu wanne. Toka walipozaliwa hicho ndicho kikawa kipindi chao cha kwanza kuwa na wanawake, hivyo wakatokea kuwapenda sana Mariamu na Catherine.

Wakawa wakitoka na kuelekea mjini na kisha kununua vinywaji mbalimbali isipokuwa pombe na kuanza kunywa. Kutokana na Catherine kuwa mnywaji mzuri wa pombe, akaanza kuwafundisha wenzake namna ya kunywa pombe hizo.
Kwa siku za kwanza zilionekana kuwa chungu lakini kadri walivyokuwa wakiendelea kunywa, uchungu ule ukaanza kupotea. Wazazi wao walikuwa wakiwaamini kupita kiasi, kila mwezi walikuwa wakiwatumia fedha za matumizi lakini kwa bahati mbaya, fedha zile zilikuwa zikiishia kwenye ulevi wa siri ambao ulikuwa ukiendelea maishani mwao. Walimu hawakujua kile ambacho kilikuwa kikiendelea kwa watu hao, kila siku walikuwa wakiwaamini kupita kawaida.
Hata katika kipindi ambacho Samuel alikuwa akiomba ruhusa kwa walimu ya kubaki usiku na wanamaombi kwa ajili ya kuomba, walikuwa wakimkubalia.

Alikuwa akibaki nao na kufanya nao maombi, ila walipokuwa wakimaliza, wanafunzi wengine ambao walikuwa wanamaombi walipokuwa wakiondoka kwenda kulala, alikuwa akibaki na Catherine japo kwa dakika thelathini na kisha kufanya ngono darasani. “Siku hizi kidogo unajitahidi nami naanza kufika ninapopahitaji,” Catherine alimwambia Samuel mara baada ya kufanya mapenzi.

“Usijali. Kuna kipindi kitakuja nitatumia hata saa moja,” Samuel alimwambia Catherine.
“Ila hivi itakuwaje kama walimu watajua?” Catherine aliuliza.
“Watajuaje sasa?”
“Si unajua dunia haina siri?”
“Najua. Dunia haina siri ila shule ina siri,” Samuel alimwambia Catherine.
“Mmmh! Unajiamini sana mpenzi.”
“Hilo usijali. Hakuna kitakachoharibika hapa,” Samuel alisema kwa kujiamini.
Watu ambao walikuwa wakiaminiwa kuwa wacha Mungu shuleni hapo nao wakawa wameharibika. Sadiki hakuwa mtu wa kuswali tena, hakuwa mtu wa kuvaa kanzu mara kwa mara, msikitini alikuwa akipitiliza hata wiki mbili bila kwenda huko.

Maisha yake, shetani alikuwa akizidi kuyatawala, alimruhusu shetani kuchukua nafasi katika moyo wake, akamuachana Mungu, nae Mungu hakuwa na shaka, akamuacha. Kilichotokea kwa Sadiki ndicho kile kile ambacho kilikuwa kimetokea kwa Samuel. Kwenda ibadani na kufanya maombi ikawa ni kwa mazoea, hakufanya kwa sababu alikuwa na msukumo wa kufanya hivyo bali alifanya kwa sababu alikuwa amekwishazoea kufanya ibada na maombi.

Mapenzi ndicho kitu ambacho walikuwa wakikifikiria sana kwa wakati huo, hawakujali kitu chochote kile, hawakujali kama baadae kuna mambo mabaya ambayo yangeweza kutokea katika maisha yao, kitu ambacho walikuwa wakikijali katika kipindi hicho ni kufanya kile ambacho mioyo yao ilikuwa ikiwataka wafanye.

Itaendelea kesho.
 
SEHEMU YA 04

Chepuo akaonekana kuwa na hasira. Alijua kwamba shule nzima ilikuwa ikiwaamini watu hao ambao kwao walionekana kuwa watakatifu kuliko wanafunzi wote shuleni hapo. Chepuo alikuwa akikasirikiwa na walimu kutokana na tabia zake mbaya zilizoonekana kuwachosha walimu hao. Kitendo cha kuambiwa kila siku kwamba ailitakiwa aige tabia kama za Samuel au Sadiki kilionekana kumkasirisha sana.

Moyo wake ulikuwa na chuki kubwa kwa watu hao kiasi ambacho hata kuwaona tu alikuwa akijisikia vibaya. Kwa kipindi kirefu sana alikuwa akitamani kitu kimoja, alijua fika kwamba walimu walikuwa wakiwaamini sana watu hao wawili, sasa alitaka kuwaharibia kwa walimu ili wasiweze kuaminika tena.

Katika kipindi ambacho aliletewa taarifa kwamba hata Samuel na Sadiki walikuwa wakitoka boda hakuonekana kuamini kabisa, kwake, kitu kama kile kilionekana kutokuwezekana hata mara moja. Japokuwa alikuwa hawapendi kabisa watu hao lakini kila siku moyoni mwake alikuwa akiwakubali, utakatifu ambao watu hao walikuwa nao hata yeye mwenyewe kuna kipindi kingine alikuwa akiwaogopa.

“Unasemaje?” Chepuo aliuliza huku akionekana kutokuamini.
“Ndio hivyo. Yaani hata mchungaji na ustadhi nao wanatoka boda kama sisi,” Mrisho, mwanafunzi aliyekuwa kwenye Kundi la Black Ninja alimwambia Chepuo. “Kwanza unapoongea na mimi kuhusu hao mbwa hebu usiwaite hayo majina uliyowaita,” Chepuo alimwambia Mrisho.

“Sawa.”
“Hebu nieleze juu ya jambo hili. Inawezekana vipi?” Chepuo aliuliza.
“Huo ndio ukweli kiongozi. Samuel na Sadiki nao wameanza kwenda boda,” Mrisho alisema.
Chepuo hakutaka kuamini moja kwa moja, kama ambavyo Mrisho alivyoona basi nae alitaka kuhakikisha juu ya kile ambacho kilikuwa kinaendelea katika maisha ya watu hao wawili.
Siku ambayo wanafunzi walikuwa wakipendelea kwenda nje ya shule ikawaida, kama kawaida Chepuo na wenzake wakaanza kuelekea katika njia za kutokea nje ya shule, sehemu ambayo asilimia kubwa ya wavulana walikuwa wakiitumia.

Chepuo akatoka mpaka nje ya shule na kisha kwenda sehemu kujificha. Katika usiku huo alitaka kuona kile ambacho Mrisho alikuwa amemwambia kuhusiana na Samuel pamoja na mwenzake, Sadiki kuanza tabia za kwenda nje ya shule huku wakiwa na wasichana. Chepuo aliendelea kujificha, siku hiyo hakuwa radhi kwenda disko mpaka pale ambapo angepata ukweli juu ya kile ambacho alikuwa ameambiwa.

Saa 6:20 usiku, akaanza kuwaona Samuel na Sadiki wakitoka katika uzio wa shule kwa kuruka ukuta kama walivyokuwa wakifanya wanafunzi wengine na kuanza kuelekea katika upande mwingine huku wakiwa na wasichana wawili.
Chepuo hakuamini kile ambacho alikuwa akikiona mahali hapo, hakuamini kama hata Samuel na Sadiki nao walikuwa wameanza tabia za kutoka nje ya shule kama wanafunzi wengine. Huo ukaonekana kuwa ushahidi tosha kwa Chepuo kwamba hata katika kipindi ambacho angeamua kuwachafua basi asingepata kazi kubwa.

Siku iliyofuata, asubuhi na mapema Chepuo akaanza kuwaambia vijana ambao walikuwa katika kundi la Black Ninja juu ya kile alichokuwa amekiona usiku uliopita. Wanafunzi wengi hawakuamini, bado Samuel na Sadiki waliendelea kuonekana watakatifu katika macho yao. Hata jambo hilo lilipofikishwa kwa walimu, kwanza wanafunzi ambao walipeleka jambo hilo ofisini wakaadhibiwa kwa kuwa walionekana kupeleka taarifa za uongo kwa ajili ya kuwachafua watu ambao walikuwa wakijuliakana kwa utakatifu shuleni hapo.

Tetesi hizo hazikuishia hapo, bado zilikuwa zikiendelea kusikika zaidi na zaidi kiasi ambacho walimu nao wakataka kuhakikisha kile ambacho kilikuwa kikiendelea. Muda ulionekana kuisha katika kipindi hicho. Mitihani ya mwisho wa mwaka ikawa imekwishafika na hivyo Samuel na Sadiki kutulia na kuanza kujisomea huku wakiacha tabia za kwenda boda. Walimu wakajitahidi kuwaweka wapelelezi wao kwa ajili ya kuwafanyia kazi ya kuwapeleleza watu hao lakini mwisho wa siku Samuel na Sadiki wakaonekana kusingiziwa.

“Nimejua tu kwamba hizi zitakuwa tetesi za kutaka kuwachafua watumishi wa Mungu,” Mwalimu mkuu, Massawe aliwaambia walimu wenzake. “Unajua mara ya kwanza niliposikia uzushi huu nilishtuka sana. Niliuhisi mwili wangu ukitetemeka sana,” Mwalimu Agness aliwambia walimu wenzake.

Mpaka shule inafungwa, bado Samuel na Sadiki walionekana watakatifu kupita kawaida. Katika siku ya kuondoka kuelekea nyumbani, Samuel na Sadiki wakaanza kuleta visingizio kwamba walitakiwa kwenda kwa ndugu zao hapo Moshi jambo ambalo wala halikuonekana kuwatia wasiwasi walimu.

Kwa Mariamu na Catherine, wao wakajifanya wanakwenda Arusha kwa ndugu zao huku malengo yao yakiwa ni kukutana sehemu na kisha kutumia usiku mzima pamoja katika hoteli yoyote ile.
Kila kitu walichokuwa wamekipanga kikaonekana kukamilika bila matatizo yoyote yale. Wakakutana Moshi mjini na kuelekea Kibororoni ambapo huko wakachukua vyumba katika hoteli na kulala na wasichana wao.
“Nashangaa kwa nini nilikuwa nikipitwa na mambo haya,” Samuel alimwambia Catherine.
“Mambo gani?” Catherine aliuliza huku akiwa amemlalia Samuel kifuani.
“Haya ya kulaliwa kifuani na binti mrembo kama wewe. Yaani sijui nilikuwa nachelewa vipi kuyajua,” Samuel alimwambia Catherine.

“Tatizo ulijifanya kuwa mtu wa dini sana.”
“Hilo ndilo kosa lenyewe. Unajua baba yangu ni mchungaji, mama yangu nae kiongozi wa kanisa, basi tabu tupu. Raha kama hizi unafikiri ningezitoa wapi?”
“Mmmh! Pole yako.”
“Asante sana.”
Usiku huo hawakulala, walikuwa wakifanya mapenzi tu. Kilichokuwa kikitokea kwa Samuel na ndicho kilichotokea kwa Sadiki katika chumba cha pili.
Kila mtu katika alikuwa na msichana wake, hawakutaka mambo ya kuingiliana. Japokuwa katika kipindi cha zamani muda wa kuondoka shuleni walikuwa wakiondoka na vitabu vyao vya dini kama Qur-an na Biblia, katika kipindi hicho walikuwa wameziacha shuleni.

Kwa wakati huo dini ikaonekana kuwaendea kushoto, hakukuwa na mtu yeyote ambaye alikuwa akikumbuka kwamba alikuwa ametoka katika familia ambazo zilikuwa na msimamo mkubwa wa dini, vitu ambavyo walikuwa wakivijali ni kula raha na wasichana hao tu.

Walikaa katika hoteli hiyo kwa siku moja na ndipo walipoamua kuanza safari ya kuelekea Dar es Salaam. Ndani ya basi, kila mmoja alikuwa amekaa na msichana wake, walikuwa wakibusiana na kushikana hapa na pale.
Mioyo yao kwa wakati huo ilikuwa imejaa dhambi, walionekana kumsahau Mungu ambaye aliwapa bahati ya kuzaliwa katika familia ambazo zilikuwa zimewapa misingi ya dini maishani mwao.

“Tukifika Dar es Salaam ndiyo itakuwa mwisho wa kuonana Sadiki?” Mariamu alimuuliza Sadiki.
“Yaani huko ndipo ambapo mapenzi yatazaliwa upya. Itatupasa kufanya kitu kimoja,” Sadiki alimwambia Mariamu.
“Kitu gani?”
“Tuanze kwenda tuisheni kule Mchikichini ili tuwe tunaonana kila siku,” Sadiki alimwambia Mariamu.
“Hakuna tatizo. Ungemwambia Samuel na Catherine basi ili tuwe wote,” Mariamu alimwambia Sadiki.
Kwa haraka bila kuchelewa Sadiki akamuita Samuel na kumpa taarifa juu ya kile walichokuwa wamekipanga na Mariamu ambacho kilitakiwa kufanyika mara watakapofika jijini Dar es salaam. Hakukuwa na mtu aliyepinga, jambo lile likakubaliwa na kila mtu kwa sababu waliona kwamba lingewafanya kuwa karibu zaidi.
****
Maisha yao yalikuwa yamekwishabadilika kabisa, kitu ambacho walikuwa wakikifikiria katika kipindi hicho ni kufanya mapenzi na wapenzi wao tu. Nyumbani hawakutulia, mara kwa mara walikuwa wakionana na wapenzi wao ambao walikuwa wakiwavutia kila aliyekuwa akiwaangalia. Kasi zao za kwenda msikitini na kanisani hawakuwa nazo tena, walikuwa wakimtumikia shetani bila kujitambua. Wazazi wao wala hawakuwa na wasiwasi, bado walikuwa wakiendelea kuwaamini watoto wao kwa kuona kwamba ni masomo ndio ambayo yalikuwa yamewaweka bize kwa wakati huo mpaka kutokwenda katika nyumba za dini.

Kila mwisho wa wiki walikuwa wakielekea ufukweni kwa ajili ya kula raha na wapenzi wao hao. Katika kipindi hicho, walikuwa wakichukia ibada kupita kawaida. Hayo ndio maisha ambayo waliamua kuishi katika, kupenda starehe ndogondogo za hapa na pale.

“Umebadilika sana Samuel. Tatizo nini mtoto wangu?” bi Magreth alimuuliza mtoto wake, Samuel.
“Nimebadilika! Nimekuwaje mama? Mbona najiona kuwa kawaida tu,” Samuel alimwambia mama yake.
“Hapana Samuel. Kipindi cha nyuma haukuwa hivi. Siku hizi hata kanisani hautaki kwenda. Kwa nini?” bi Magreth alimuuliza Samuel.
“Huwa ninakwenda tuisheni mama, sasa hivi ninaingia kidato cha nne, nisiposoma sana, nitafeli,” Samuel alimwambia mama yake, Bi Magreth.

“Tuisheni mpaka jumapili muda wa ibada?” bi Magreth aliuliza kwa mshangao.
“Ndio mama. Masomo yamekuwa mengi sana na magumu,” Samuel alimwambia mama yake.
Mabadiliko ambayo alikuwa nayo Samuel yakashindwa kujificha, bado yalikuwa yakionekana waziwazi machoni mwa wazazi wake ambao kila siku walikuwa wakiendelea kumsisitizia kuelekea kanisani na kusali. Kutokana na kuingia katika maisha ya kumtumikia shetani, hata ibadani kulionekana kuwa kugumu kwenda jambo ambalo lilimfanya baba yake, mchungaji Mpelele kumuita na kumuweka kikao mara kwa mara.
“Umeanza kumtumikia shetani?” Mchungaji Mpelele alimuuliza Samuel huku akionekana kuwa na hasira.
“Hapana baba.”
“Kumbe unamtumikia nani siku hizi?”
“Namtumikia Mungu.”
“Mungu huyu huyu wa Ibrahim, Isaka na Yakobo au mungu mwingine?” Mchungaji Mpelele alimuuliza Samuel.
“Huyu huyu wa Ibrahim, Isaka na Yakobo.”
“Hapana. Kama unamtumikia Mungu huyu, utakuwa umekosea sana, Mungu huyu tunayemtumikia huwa hatumikiwi kama ambavyo unamtumikia Samuel,” mchungaji Mpelele alimwambia Samuel.
“Ninamtumikia Mungu huyuhuyu,” Samuel alimwambia baba yake, mchungaji Mpelele.
“Kwanza siku hizi kanisani hauendi. Kweli au uongo?” Mchungaji Mpelele aliuliza.
“Kweli.”
“Kwa nini?”
“Naingia kidato cha nne baba, nakuwa bize na masomo,” Samuel alimwambia baba yake, mchungaji Mpelele.
“Usitake kunitania. Hivi Mungu na masomo nani bora?”
“Mungu.”
“Nisikilize Samuel. Utaweza kusoma usiku na mchana, ukakesha katika maisha yako yote ukisoma, ila kumbuka kwamba bila Mungu, unakesha bure mwanangu. Kusoma sana si kufaulu, unaweza ukasoma sana na usifaulu ila ukimtumikia Mungu hata usiposoma sana, utafaulu kwani yeye anajua kila kitu, atakufanya usome muda mchache lakini vile ambavyo utavisoma ndivyo ambavyo vitakavyotoka katika mtihani yako,” Mchungaji Mpelele alimwambia Samuel.
“Naomba unisamehe baba.”
“Haujanikosea mimi, umemkosea Mungu muumba Mbingu na Nchi. Nenda mbele zake na umuombe msamaha,” Mchungaji Mpelele alimwambia Samuel.

Japokuwa mchungaji Mpelele alikuwa ameongea maneno mengi kwa kijana wake, Samuel lakini wala hakuweza kubadilika kabisa, maisha ya anasa yakaonekana kumteka kabisa. Kila siku alikuwa akionana na Catherine na kuendelea na maisha yao kama kawaida yao, maisha ya kwenda ufukweni na sehemu nyingine za starehe.
Maisha ambayo alikuwa akiishi Samuel yalikuwa ni sawa na maisha ambayo alikuwa akiishi Sadiki. Katika kipindi hiki mapenzi yakaonekana kumteka Sadiki, hakutaka kabisa kwenda katika nyumba ya ibada, msikitini kuswali.
Ile kasi yake ya kwenda msikitini kila siku katika kipindi cha nyuma, kwa wakati huo ikaonekana kupungua kabisa mpaka kufikia kipindi kutoweka kabisa.

Sadiki akachukia ibada za msikitini, msikiti kwake ukaonekana kama jela, sehemu ambayo ilionekana kuwa si nzuri kwa kijana kama yeye. Kanzu nyingi ambazo alikuwa akipenda sana kuzivaa katika kipindi hicho alikuwa amezifungia kabatini na kuanza kuvaa majinzi pamoja na fulana ambazo aliziona kuwa nzuri. Baba yake, Ustadhi Hamidu alijitahidi sana kuongea nae lakini hakuonekana kuelekea kabisa. Kila siku alikuwa akitoka na kujifanya kuelekea tuisheni kumbe alikuwa akienda kuonana na Mariamu wake ambaye alikuwa akitumia muda mwingi kuwa pamoja nae.

Maisha yake yakaonekana kuzidi kuharibika kadri siku zilivyozidi kwenda mbele, hofu ya Mungu ikaonekana kutoweka moyoni mwake, alikuwa akijifanyia vitu ambavyo alikuwa akitaka kuvifanya kwa wakati huo, vitu ambavyo havikuwa vikitakiwa kufanyika na mtu aliyekuwa akimcha Mungu. “Maisha yako yamebadilika sana Sadiki, umeanza kuwa firauni sasa,” Ustadhi Hamidu, Imamu wa msikiti wa Kichangani alimwambia mtoto wake, Sadiki.

“Hapana baba, mbona naishi maisha kama zamani,” Sadiki alimwambia baba yake, Ustadhi Hamidu.
“Usinidanganye. Siku hizi hata msikitini hautaki kwenda. Ijumaa iliyopita nilikwambia twende kwenye Maulidi, ukanipiga piga chenga weee ukanipotea,” Ustadhi Hamidu alimwambia sadiki.
“Nilikwenda baba ila sikuongozana nawe.”
“Usitake kunidanganya. Hivi wewe mtoto siku hizi una nini? Kwa nini hautaki kumuabudu Allah? Hivi kuna nani ambaye unamuabudu zaidi ya Allah?” Ustadhi Hamidu alimuuliza Sadiki.
“Namuabudu Allah.”

“Labda Allah mwingine lakini si Allah ninayemfahamu mimi, labda si Allah ambaye alimuongoza Mtume wetu, Mohammad S.A.W katika kila njia njema maishani mwake. Kwa sasa umekuwa kama Firauni Sadiki. Badilisha maisha yako, usipobadilisha, utapotea,” Ustadhi Hamidu alimwambia Sadiki.
Wazazi wote wa pande zote mbili walionekana kuumia, mabadiliko mabaya ambayo walikuwa nayo watoto wao yalionekana kuwaumiza kupita kawaida.
Walijua fika kwamba watoto wao walikuwa wamebadilika na kuziacha njia ambazo walitakiwa kuzifuata, walionekana kuvutiwa na dunia pamoja na mambo yake ya anasa ambayo yakaonekana kuwapoteza zaidi endapo wangeendelea kuyatumikia.

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 05

Siku ziliendelea kukatika mpaka siku ambayo wanafunzi walitakiwa kurudi shuleni. Kila mmoja alionekana kukasirika kwani walijua fika kwamba kila kitu ambacho walikuwa wakikifanya nyumbani basi kingeweza kufanyika kisiri shuleni ili kuwazuia wanafunzi wengine wasijue kile ambacho kilikuwa kikiendelea katika maisha yao. Samuel na Sadiki walikuwa wamezoeana sana na wapenzi wao kiasi ambacho kilionekana kuwa ngumu kuwatenganisha, kuwakataza wasikae pamoja katika kipindi cha kujisomea au kula. Ukaribu wao ule ndio ambao ukawafanya wanafunzi wengine kugundua kwamba kulikuwa na kitu ambacho kilikuwa kikiendelea kwa wanafunzi hao.

Kwa kuwa shule ilikuwa ikitumia umeme, nyakati za usiku ambazo umeme ulikuwa ukikatika, walikuwa wakishikana sana huku wakibadilishana mate kwa kipindi kirefu. Mpaka jenereta linawashwa, tayari walikuwa wamechezeana vya kutosha jambo ambalo liliifanya miili yao kushikwa chachu kubwa ya kufanya mapenzi. Kutoroka hakukukoma, mara kwa mara walikuwa wakitoroka pamoja kuelekea nje ya shule ambapo huko kama kawaida yao walikuwa wakifanya vitu vyao vingi vya ngono na mambo mengine. Kwa sababu walikuwa wamejifunza kunywa pombe, wakajikuta wakinunua vilevi hivyo siku za mwisho wa wiki na kunywa taratibu.

Walimu walipopelekewa kile ambacho kilikuwa kikiendelea katika maisha ya wanafunzi hao, bado waliendelea kutokuamini kabisa kwani watu hao waliendelea kuwa watakatifu katika macho yao kutokana na unafiki ambao walikuwa wakiwaonyeshea kila walipokuwa wakijua wanaangaliwa na walimu hao.

“Astaghafilullah! Yaani mimi nitembee na msichana?” Sadiki aliuliza huku akijifanya kushtuka mara alipoitwa ofisini na kuulizwa juu ya Mariamu.
“Ndio. Tumeletewa kesi kwamba unatembea na Mariamu tena wakati mwingine mnaruka ukuta na kwenda boda,” Mwalimu Michael, mwalimu wa nidhamu alimwambia Sadiki.
“Hii ni kashfa nzito sana kwangu mwalimu. Siwezi kuongea neno lolote baya kwa watu ambao wanaeneza habari hiyo. Ninachotaka kusema ni kimoja tu kwamba Allah ninayemuabudu anayaona maumivu ninayoyasikia moyoni mwangu. Atanilipia tu,” Sadiki alimwambia mwalimu Michael.

Maneno yake pamoja na mshangao mkubwa wa kinafiki ambao alikuwa ameuonyesha mahali pale ukawafanya walimu kuendelea kuamini kwamba yale yalikuwa ni maneno ambayo yalikuwa yameanzishwa na wanafunzi ambao walionekana kuwa na chuki juu ya Sadiki na walifanya hivyo kwa kuwa walitaka kumuharibia kwa sababu alikuwa mtumishi wa Mungu.

Walimu hawakuishia hapo, walichokifanya ni kumuita Samuel na kumuuliza kuhusu tetesi ambazo walikuwa wamezisikia kuhusiana na Catherine, kama ilivyokuwa kwa Sadiki, nae Samuel akajifanya kushtuka kupita kawaida kana kwamba alikuwa ameambiwa taarifa nzito ya uongo masikioni mwake.

“Yesu wangu! Mimi nifanye hivyo? Sasa kutakuwa na maana gani ya kuwa Mwenyekiti wa Casfeta mkoani Kilimanjaro? Kutakuwa na umuhimu gani wa kumuomba Mungu nyakati za usiku, kutakuwa na umuhimu gani wa kwenda kanisani?” Samuel aliuliza maswali mfululizo.

Hakukuwa na mwalimu ambaye alionekana kuuamini uvumi ule kutokana na wahusika kuruka kupita kawaida. Kadri siku zilivyozidi kwenda mbele na ndivyo ambavyo uvumi ule ulivyozidi kusikika zaidi na zaidi jambo ambalo liliwafanya baadhi ya walimu kuanza kufuatilia wao wenyewe ili kuhakikisha kwamba ulikuwa ni uvumi au kweli.

“Mkitaka kufuatilia ninyi wenyewe hamuwezi kuwaona,” Chepuo alikuwa akiwaambia walimu ofisini.
“Kwa nini tusiweze?”
“Kama wanaondoka saa saba za usiku, mtaweza kuwaona?” Chepuo aliuliza.
“Kwa hiyo tufanye nini ili tuweze kuwaona?’
“Nipeni simu.”
“Eeeh! Sasa simu ya nini tena?”
“Si ili nikiwaona niwapigie mje kuhakikisha.”
“Mmmh!”
“Nini tena?”
“Hatukuamini Chepuo. Usije ukaiuza hata simu yenyewe. Mtu mwenyewe dakika moja mbele wewe,” mwalimu Michael alimwambia.
“Basi milele hamtoweza kuujua ukweli. Huu ni mwezi wa nane kumbukeni, miezi miwili baadae wanafanya pepa halafu wanasepa,” Chepuo aliwaambia walimu.
“Sawa. Ngoja tukupe simu halafu utuambie wakiondoka usiku,” mwalimu mkuu, Massawe alimwambia Chepuo na kumkabidhi simu ambayo hakuwa akiitumia.
Katika kipindi hicho, walimu walikuwa wamejaribu kwa kiasi kikubwa kufuatilia lakini hawakuweza kufanikiwa mpaka pale ambapo wakaonekana kuhitaji msaada kutoka kwa Chepuo, mwanafunzi ambaye alionekana kutokuwa na nidhamu shuleni pale.

Kutokana na chuki kubwa ambayo ilijengeka moyoni mwa Chepuo juu ya Samuel na Sadiki, moja kwa moja akaomba kupewa kazi ya kuwahakikishia walimu juu ya zile tetesi ambazo zimekuwa zikiendelea kusikika kwa zaidi ya miezi saba.
Walimu hawakuwa na jinsi, katika kipindi hicho walikuwa wakitaka kujua ukweli juu ya kile ambacho kilikuwa kikiendelea katika maisha ya Samuel na Sadiki, walitaka kuufahamu ukweli kwamba wawili hao walikuwa wakitoroka shuleni hapo na wasichana au la.

Chepuo akapewa kazi hiyo, akapewa simu ndogo ya Nokia Obama kwa ajili ya kumpigia mwalimu Michael ambaye alikuwa akilala shuleni hapo katika kipindi ambacho angewaona Samuel na Sadiki wakitoka nje ya shule pamoja na wasichana hao.

Chepuo akaonekana kufurahia, hakuamini kama kwa wakati huo walimu walikuwa wamemuamini mpaka kumpa kazi hiyo. Kwanza alipofika bwenini, hakutaka kumwambia mwanafunzi yeyote juu ya simu ambayo alikuwa amepewa, alitaka kufanya kila kitu kimyakimya kwani alijua fika kwamba kama angeamua kuwaambia wanafunzi wengine ambao walikuwa katika kundi lake la Black Ninja basi siri ingeweza kuvuja.

Siku ya Jumamosi usiku wa saa saba, kama kawaida yake Chepuo akainuka kutoka kitandani na moja kwa moja kuelekea katika kitanda cha Samuel huku wanafunzi wakiwa wamelala. Akaanza kupapasa kitandani pale, hakukuwa na mtu yeyote. Chepuo hakuishia hapo, alichokifanya ni kuelekea katika kitanda cha Sadiki, nae hakuwepo kitandani hapo.
Moja kwa moja akili yake ikamwambia kwamba wawili hao tayari walikuwa wametoka bwenini na kuelekea boda kama kawaida yao. Kwa kasi ya ajabu akaanza kuvaa nguo zake na kisha kuelekea nje ya bweni hilo. Hakutaka kuchelewa, akaanza kuelekea sehemu ambayo wanafunzi walikuwa wakiitumia sana kutorokea kwenda nje ya shule.
“Wewe nani?” Ilisikika sauti ya mlinzi nyuma yake. Chepuo akageuka.

“Haaaaa! Kumbe mwana. Inakuwaje?” Mlinzi alimwambia Chepuo mara baada ya kumgundua.
“Poa. Hivi Samuel na Sadiki wametoka leo?” Chepuo aliuliza.
“Yeah! Kama kawaida wametoka na malaya wao. Mbona umewaulizia hivyo?” Mlinzi aliwauliza huku tayari akiwa amekwishapewa fedha kama kutunza siri ya watorokaji shuleni hapo.
“Watumishi wa Mungu wale,” Chepuo alimwambia mlinzi.
“Acha utani.”
“Kweli tena. Yule Samuel ni mchungaji na Sadiki ni ustadhi wa shule,” Chepuo alimwambia mlinzi ambaye alionekana kushangaa.
“Kama na wewe unataka kwenda boda nenda tu ila si kuniambia maneno mengi ya uongo,” mlinzi alimwambia Chepuo.
“Kweli tena mpwa. Unafikiri nakudanganya! Uliza shule nzima.”
“Duuh! Kama ni kweli kumbe hata mimi naweza kuwa Ustadhi mwamba,” mlinzi alimwambia Chepuo.
“Ndio hivyo. Umewaona wameelekea wapi?”
“Wamekwenda upande wa kulia bila shaka watakuwa wakielekea kule kwenye Ukumbi wa Manyasa”
“Basi poa. Cha msingi toka maeneo haya. Muda wowote ule ticha anaweza kuja,” Chepuo alimwambia mlinzi.
“Poa poa. Usijali.”
“Aminia. Nipe gwala,” Chepuo alisema na kisha kugongeshana mikono na mlinzi na kuondoka mahali hapo huku simu aliyopewa na walimu ikiwa mfukoni mwake.
Kwa harakaharaka Chepuo akapita katika uwazi mkubwa ambao ulikuwa umetengenezwa na wanafunzi kwa ajili ya kutorokea na kutokea nje ya shule ile.

Hakutaka kubaki mahali hapo, alichokifanya ni kuanza kuelekea katika ukumbi wa muziki ambao wanafunzi wa shule mbalimbali walikuwa wakipenda sana kukutania usiku ambao walikuwa wakitoroka shuleni kwao.
Siku hiyo, Chepuo hakujisikia kwenda nje ya shule kwa ajili ya kufanya mambo yake, siku hiyo alijisikia kuelekea huko kwa sababu alitaka kuwahakikishia walimu kwamba wale watu waliokuwa wakiwaamini hawakuwa watakatifu kama ambavyo mioyo yao ilivyokuwa ikifikiria juu yao.

Ukumbi wa Manyasa uliokuwa Moshi mjini uliendelea kutoa burudani ya muziki kwa kiingilio cha shilingi elfu tatu tu. Watu walikuwa wamejazana ndani ya ukumbi huo, wanafunzi kutoka katika shule mbalimbali kama Majengo, Huru, Northern Highland pamoja na shule nyingine walikuwa wakifika ndani ya ukumbi huo kwa wingi sana.
Burudani ya muziki bado ilikuwa ikiendelea ndani ya ukumbi huo huku asilimia kubwa ya watu ambao walikuwa ndani ya ukumbi huo wakiwa wanafunzi wa shule mbalimbali hapo Moshi Mjini.

Wanawake ambao walikuwa wakijiuza hawakukosa mahali hapo, biashara yao bado ilikuwa ikiendelea kama kawaida. Wateja walikuwa wakifika kwa wingi, walikuwa wakiwanunua na kisha kufanya nao ngono katika vyoo vya ukumbi huo au hata katika sehemu ambazo zilikuwa na giza.

Chepuo akafika katika ukumbi huo, siku hiyo hakutaka kuongea na mtu yeyote yule jambo ambalo lilimfanya kuvua fulana yake na kukifunika kichwa chake huku akibaki na kaoshi pamoja na suruali mwilini mwake. Alipofika mlangoni, akatoa kiasi ambacho kilikuwa kikihitajika na kisha kuingia ndani ya ukumbi ule wa Manyasa.

Macho ya Chepuo hayakutulia sehemu moja, yalikuwa yakiangalia huku na kule, alikuwa akiwatafuta wabaya wake ndani ya ukumbi ule. Watu walikuwa wakicheza kifujofujo, Chepuo akaanza kupiga hatua kuelekea katika sehemu ambayo ilikuwa na kigiza, sehemu ambayo watu ambao hawakutaka kujulikana walikuwa wakiitumia sana kukaa na wasichana wao.

Alipofika karibu na sehemu ile, akaanza kuangalia katika vikochi kadhaa ambavyo vilikuwa mahali pale. Macho yake yakatua nyusoni mwa watu ambao alikuwa na uhakika kwamba walikuwa wabaya wake. Chepuo hakutaka kuonekana kuwa na presha, alichokifanya ni kusogea na kuanza kuwaangalia vizuri.

“Ndio wenyewe,” Chepuo alisema huku akiachia tabasamu pana.
Mpaka kufika kipindi hicho akawa na uhakika kwamba watu ambao walikuwa wamemfanya kufika katika ukumbi ule alikuwa amekwishawaona jambo ambalo lilimfanya kuanza kuwafuatilia kwa karibu sana, hakutaka awapoteze machoni mwake.

Samuel na Sadiki walionekana kutokuwa na habari kabisa, walikuwa wakishikanashikana na wapenzi wao, Catherine na Mariamu bila kujua kwamba Chepuo alikuwa ndani ya ukumbi ule akiwaangalia tu. Matendo ya kimalavidavi yalionekana kuwatawala mahali pale, walikuwa wakinyonyana mate huku wakishikana katika maungo yao ya siri. Kutokana na kofia ambazo walikuwa wamezivaa vichwani mwao ili kuwafanya kutokugundulika na watu mbalimbali ndizo ambazo zilionekana kuwa ulinzi kwao machoni mwa watu wengine.

Watu ambao walikuwa wakijulikana kama watumishi wa Mungu kwa walimu wao, watu ambao walikuwa wakiaminika kwamba ni watakatifu kwa walimu wao, katika kipindi hicho walikuwa ndani ya ukumbi wa Manyasa, ukumbi mkubwa ambao ulikuwa ukisifika kwa kutoa burudani kabambe ndani ya mkoa wa Kilimanjaro. Saa 9:17 usiku ndio ulikuwa muda ambao Samuel na wenzake wakainuka mahali pale kwa ajili ya kuondoka ukumbini hapo. Chepuo alivyoona hivyo, kwa haraka sana akatoka nje ya ukumbi na kisha kwenda kujibanza sehemu huku macho yake yakiwa katika mlango wa kutokea katika ukumbi ule.

Akawaona Samuel, Sadiki, Catherine na Mariamu wakiwa wanatoka nje ya ukumbi ule. Kwa haraka sana akaanza kuelekea katika sehemu ambazo zilikuwa na bodaboda na kisha kuchukua moja ambayo ilimpeleka mpaka nje ya shule yao. Akamlipa dereva na kisha kuchukua simu yake na kisha kuanza kumpigia mwalimu Michael.
“Pokea simu basi kabla hawajafika,” Chepuo alijisemea mara simu ilipoanza kuita. Simu iliendelea kuita mpaka kukata, Chepuo akaamua kupiga tena, simu ile ikaanza kuita mpaka ikapokelewa.
“Hallow....” Sauti ya mwalimu Michael ilisikika kichovu.
“Ticha unalala utafikiri umekufa,” Chepuo alimwambia mwalimu Michael.
“Kuna nini? Mbona usiku sana?”
“Toka nje basi uje kuhakikisha kwa macho yako.”
“Kuhakikisha nini?”
“Kwamba watumishi wa Mungu nao wamekwenda kwenye klabu ya usiku” Chepuo alimwambia mwalimu Michael.
“Watumishi gani?”
“Samuel Mpelele na Sadiki Hamidu,” Chepuo alijibu.
“Upo wapi wewe?”
“Njoo huku nyuma ya jiko la shule.”
“Sawa.”
Simu ikakatwa, tabasamu pana likaanza kuonekana usoni mwa Chepuo kwa kuona kwamba siku hiyo ndio ingekuwa siku ambayo kila kitu kingekwenda kujulikana kwa kila mtu kwamba Samuel na Sadiki walikuwa wakitoka usiku na kwenda katika klabu za starehe pamoja na wasichana.
Ndani ya dakika tatu, mwalimu Michael akatokea sehemu ile huku akiwa amevaa bukta na koti kubwa. Macho yake yalipomuona Chepuo amesimama karibu na tundu kubwa la ukuta, akaanza kumfuata.
“Wapo wapi?” Mwalimu Michael aliuliza.

“Usiwe na presha ticha, wewe subiri tu utawaona,” Chepuo alimwambia mwalimu Michael.
Ndani ya dakika ishirini, baadhi ya wanafunzi wengine wakaonekana wakianza kuingia ndani ya eneo la shule hiyo akitokea katika ukumbi wa starehe wa Manyara. Kila mwanafunzi ambaye alikuwa akitokea mahali hapo, alikuwa akiwekwa pembeni kwa ajili ya kuandikwa majina na baadae kupewa adhabu.
Waliendelea kusubiri zaidi na zaidi lakini watu ambao walikuwa wakiwasubiria mahali hapo wala hawakutokea jambo ambalo lilimshangaza sana Chepuo.

Ilipofika saa 10:15 alfajiri, mwalimu Michael akaonekana kuchoka kuvumilia, hapohapo akaamua kwenda katika bweni ambalo Samuel na Sadiki walikuwa wakilitumia, alipoingia ndani, moja kwa moja akaelekea katika vitanda ambavyo walikuwa wakilalia, akawakuta wakiwa wamelala usingizi mzito.

“Mmmh! Sasa mbona wapo humu?” mwalimu Michael alijiuliza huku akionekana kushangaa.
Hakutaka kubaki mahali hapo, alichokifanya ni kuanza kuondoka kuelekea nje ya bweni lile na kisha kumfuata Chepuo kule alipokuwa pamoja na wanafunzi wengine. Alimpomfikia, akamuita pembeni na kisha kuanza kuongea nae.
“Una uhakika kwamba Samuel na Sadiki walitoka nje ya shule usiku huu?” Mwalimu Michael alimuuliza Chepuo.
“Nina uhakika. Nimewaona mimi mwenyewe kwa macho yangu ndani ya ukumbi wa Manyasa,” Chepuo alisema huku akiapa.

“Unavyoona watakuwa wamerudi au watakuwa bado nje ya shule?” Mwalimu Michael alimuuliza.
“Bado watakuwa nje ya shule, hawajapitia hapa,” Chepuo alijibu.
“Sawa. Ila kwa nini kila siku umekuwa mtu wa kuongea mambo ya uongo juu ya watumishi wa Mungu?” Mwalimu Michael alimuuliza Chepuo.
“Uongo gani tena ticha?”
“Kwamba watu hawa wameanza kwenda kwenye kumbi za starehe.”
“Ila kweli wamekwenda kwenye kumbi za starehe.”
“Mbona nimewaona bwenini wamelala,” mwalimu Michael alimwambia Chepuo maneno ambayo yalionekana kumshtua.
“Unasemaje?” Chepuo aliuliza huku akionekana kushtuka.
“Nimewakuta bwenini wamelala.”
“Haiwezekani. Hawajapita hapa, utakuwa umechanganya vitanda ticha,” Chepuo alimwambia mwalimu Michael huku akionekana kutokuamini.

Hapo hapo wakaanza kuondoka kuelekea katika bweni lile na kisha kuingia ndani. Wakaanza kuelekea katika vitanda vile na kumuonyeshea Chepuo kwamba Samuel na Sadiki walikuwa wamelala. Ili kuhakikisha juu ya kile ambacho alikuwa akimwambia, akawaamsha, ni kweli walikuwa wenyewe ambao walionekana kuwa na usingizi mzito.
“Umeamini?” mwalimu Michael alimuuliza Chepuo.

“Imekuwaje? Mbona pale hawakupita?” Samuel aliuliza huku akionekana kushangaa.
“Wewe ni muongo. Asubuhi nitakuadhibu kwa adhabu ya kuchimba shimo la takataka. Kosa lako kubwa ni kuwasingizia watumishi wa Mungu ili wafukuzwe shule, kosa lako la pili ni kuniamsha wakati nikiwa naota njozi nzuri,” mwalimu Michael alimwambia Chepuo ambaye alikuwa amebaki na mshangao mkubwa huku swali likibakia kichwani mwake, walipitia wapi watu wale kuingia shuleni.

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 06

Bado Samuel na Sadiki walikuwa wakiendelea kuleta unafiki mbele ya macho ya walimu. Muda mwingi walikuwa wakionekana wakiwa na vitabu vyao vya dini jambo ambalo liliwafanya walimu kujua kwamba bado watu wale walikuwa watakatifu kama katika kipindi cha nyuma.

Kutokwenda sana kanisani na msikitini kukaonekana kuanza kuwatia hofu walimu lakini mara baada ya Samuel na Sadiki kuligundua hilo, wakajirudi na kuendelea kufanya kama kile ambacho walikuwa wakikifanya katika siku za nyuma.
Mara kwa mara Samuel alikuwa akionekana ameshika Biblia huku akiisoma kwa muda mwingi. Usiku, kama kawaida alikuwa akifanya maombi na hata wale wanafunzi ambao walikuwa wakisumbuliwa na magonjwa mbalimbali shuleni hapo alikuwa akiwafanyia maombezi.

Matukio hayo na mangine yakaongeza upofu machoni mwa walimu, waliweza kuwaficha kabisa juu ya kile ambacho kilikuwa kikiendelea mioyoni mwao, Kwa Sadiki, kama kawaida yake alikuwa akivaa kanzu, muda mwingi alikuwa akishika Tasbih na kujifanya Shekhe mkubwa ambaye alikuwa akimtumikia Mungu.
Kilemba kikubwa kilikuwa kichwani mwake, alikuwa akionekana kama mtu ambaye alikuwa akimuabudu Mungu kwa moyo mmoja. Katika swala zote tano za siku, Sadiki alikuwa akihudhuria lakini bado mambo yake machafu yalikuwa yakiendelea katika maisha yao.

Siku zikaendelea kukatika huku maisha yale yakiendelea zaidi na zaidi. Kikafika kipindi, kipindi ambacho Mungu hakutaka kuona watu hao wakiendelea kufanya vitu kwa kujificha na kuleta unafiki mbele za walimu ambao walikuwa wakiwaona kuwa watakatifu, watu waliokuwa wakimuabudu Mungu kwa moyo mmoja.

Siku ya jumamosi ya tarehe 7 mwezi wa 9 ikaonekana kuwa mbaya kwao hasa mara baada ya ukaguzi kufanyika katika mabegi ya wanafunzi wote kwa lengo la kutaka kuwatambua wanafunzi ambao walikuwa na simu katika shule hiyo.
“Kuna wengine wanatumia simu shuleni hapa. Kama mnavyojua haturuhusu kitu hicho ndani ya shule hii, tena sio hii tu bali hata shule nyingine za Serikali,” Mwalimu mkuu aliwaambia walimu katika moja ya vikao vya walimu shuleni hapo.
“Nini kifanyike mkuu, tuweke wapelelezi?” Mwalimu Mkuu msaidizi aliuliza.

“Hakuna. Kamwe hatutakiwi kuwaamini wanafunzi kuwapeleleza wanafunzi wenzao, hiyo ngumu. Jumamosi hii ya leo ndio tutataka tufanye upekuzi katika mabegi yao yote bwenini, tutagundua tu,” Mwalimu mkuu aliwaambia walimu wezake. Kile ambacho kilikuwa kimezungumziwa mahali pale ndicho ambacho kilitakiwa kufanyika tena kwa haraka sana. Ilipofika saa 10:00 jioni, kengele ikagongwa, wanafunzi wote wakahitajika kwenda sehemu ya kukutania.
Kila mwanafunzi alibaki akijiuliza juu ya kitu gani ambacho kilikuwa kikiendelea. Uwepo wa walimu ndani ya shule hiyo hasa katika siku ya Jumamosi ilionekana kuwashangaza sana, mbaya zaidi walikuwa wametumia zaidi ya saa moja kuwa katika kikao chao ofisini.

Siku hiyo, mwalimu mkuu hakuonekana kuwa katika hali ya kawaida, ndita zilikuwa zikionekana usoni mwake. Wanafunzi wakajipanga mstalini na walimu kufika mahali hapo. Kitu cha kwanza, mwalimu mkuu akachukua fimbo na kisha kuelekea mbele kabisa ya wanafunzi wale. Hata kabla hajaongea kitu chochote kile akaanza kuwaangalia wanafunzi waliokuwepo mahali pale, wanafunzi walionekana kuhofia sana kwani mwalimu mkuu hakuonekana kuwa katika hali ya kawaida kabisa.

“Tumechoka,” Ilisikika sauti ya mwalimu mkuu, sauti iliyojaa utetemo fulani, sauti ambayo ilizidi kuongeza hofu mioyoni mwa wanafunzi wale.
“Wanafunzi wote wapo hapa?” Mwalimu mkuu alimuuliza kaka mkuu, John Gilipa.
Kwa haraka haraka John akaanza kuwaangalia wanafunzi mahali hapo, alipoona kila mwanafunzi mtukutu ambao walikuwa wakijificha wapo mahali pale, akamuangalia mwalimu mkuu ambaye bado alionekana kuwa katika hali isiyo ya kawaida.
“Ndiyo.”
“Una uhakika?”
“Labda niangalie katika mabweni mwalimu,” John alimjibu mwalimu mkuu na kisha kuanza kuelekea katika mabweni yale na baada ya dakika moja kuja na wanafunzi ambao walikuwa mabwenini ambao asilimia kubwa walikuwa viongozi, wakatakiwa kujumuika na wanafunzi wengine.

“Kuna nini tena? Moyo wangu umejawa na hofu sana,” Samuel alimuuliza Sadiki kwa sauti ya chini.
“Mmmh! Sijui. Hata mimi sina amani kabisa. Ngoja tuwasikilize,” Sadiki alimwambia Samuel huku akiwa amevaa kanzu pamoja na kilemba kichwani.
“Kuna watu leo hii tunakwenda kuwaandikia barua za kurudi nyumbani kwao kama adhabu na baada ya wiki mbili kuja na wazazi wao,” Mwalimu mkuu aliwaambia wanafunzi ambao bado walionekana kuwa na hofu na kisha kuendelea:
“Hatujui ni wangapi. Inawezekana akawa mmoja au inawezekana wakawa mia moja, hatujui,” Mwalimu mkuu alisema na kuendelea.
“Kuna watu wanatumia simu kificho, kuna watu wanatumia pombe kificho, leo hii tutakwenda kuwafahamu tu. Tutaanza kupekua katika kila begi la mwanafunzi na sehemu nyingine, ukikuta umeitwa katika bweni lako, nenda kwa haraka sana” Mwalimu mkuu aliwaambia wanafunzi ambao idadi kubwa walionekana kuwa na wasiwasi.
“Mungu wangu!” Sadiki alisema huku akionekana kushtuka.
“Nini?”
“Kuna pombe.”
“Wapi?”
“Kwenye begi langu na lako.”
“Unasemaje?”
“Jana nilinunua viroba, nimeviweka kwenye begi langu na kifuko kimoja kukuwekea katika begi lako kama ulivyoniambia” Sadiki alimwambia Samuel.
“Unasemaje?”
“Ndio hivyo.”
“Hapana. Uliweka kwenye begi?”
“Ndio.”
“Kwa nini usingeweka ndani ya magodoro kama tunavyofanya kila siku?”
“Sijui kwa nini sikufanya hivyo,” Sadiki alimwambia Samuel.
“Kwa hiyo tufanye nini?”
“Sijajua. Ila ngoja tuwasikilizie. Mungu tusaidie sisi watumishi wako,” Sadiki alisema huku kijasho chembamba kikianza kumtoka.

Walimu wakaingia katika mabweni na kisha upekuzi kuanza. Wanafunzi walionekana kutokuwa na amani kabisa, wengi wao walionekana kuwa na wasiwasi mwingi nyusoni mwao. Kama ilivyokuwa kwa wanafunzi wengine na ndivyo ilivyokuwa kwa Samuel pamoja na Sadiki ambao walikuwa wakitokwa na vijasho vyembamba nyusoni mwao.
Tayari waliona kwamba siku hiyo ndio ilikuwa siku ambayo kila mwanafunzi angekwenda kufahamu ukweli kuhusiana na tetesi zile ambazo kila siku zilikuwa zikisikika masikioni mwao. Macho yao yalipotua nyusoni mwa Mariamu na Catherine, nao walionekana kutokujiamini kabisa.

Baada ya dakika tano, mwanafunzi mmoja baada ya mwingine akaanza kuitwa bwenini jambo ambalo liliwaongezea hofu kupita kawaida. Walimu walichukua muda wa saa moja kuangalia mabegi ya wanafunzi shuleni hapo huku zaidi ya wanafunzi themanini wakiwa wameitwa mabwenini mwao.

Mpaka upekuzi unamalizika, tayari walimu walikuwa wamekuta pombe kali, sigara, simu pamoja na vitu vingine ambavyo havikutakiwa kuingizwa shuleni hapo. Kitu cha ajabu ambacho kiliwafanya Samuel na Sadiki kushtuka, hawakuwa wameitwa bwenini jambo ambalo liliwafanya kuona kwamba kila kitu kilikuwa fresh. “Mbona hatujaitwa! Au ulivificha sana?” Samuel alimuuliza Sadiki.

“Sijajua kwa nini. Ila nafikiri Mungu bado yupo pamoja nasi. Yaani kama tukisalimika leo hii, hakika nitamrudia Allah kwa kuona kwamba bado ananipenda,” Sadiki alimwambia Samuel. Mara baada ya wanafunzi ambao walikuwa na vitu ambavyo havikuwa vikiruhusiwa kuingizwa shuleni kupelekwa ofisini, wengine wakaruhusiwa kuondoka mahali hapo. Kitu cha kwanza ambacho walikifanya Samuel na Sadiki ni kuelekea katika bweni lao na kisha kufungua mabegi yao, Pombe hazikuwepo.

Kila mmoja akabaki kuwa na wasiwasi, ilikuwaje pombe zikosekane ndani ya mabegi yao huku wakiwa hawajaitwa na walimu? Kila mmoja alikosa jibu jambo ambalo liliwafanya kutulia kuona ni kitu gani ambacho kingeendelea mahali hapo.
Saa mbili usiku, wakaitwa ofisini, tayari wakajua kwamba pombe zile zilikuwa zimeonekana na hivyo kuchukuliwa. Moja kwa moja wakaelekea katika ofisi ya mwalimu mkuu ambaye mpaka katika kipindi hicho siku hiyo bado alikuwa shuleni hapo.

“Funga mlango,” Mwalimu mkuu, Massawe alimwambia Sadiki ambaye alikuwa wa mwisho kuingia. Wakamsalimia mwalimu mkuu lakini wala hakuitikia salamu zile, alibaki akiwaangalia kwa muda na kisha kuingiza mkono katika kidroo kidogo cha meza yake na kisha kutoa viroba vya Konyagi na kisha kuweka juu ya meza yake. Sadiki na Samuel wakaonekana kuwa na wasiwasi zaidi, tayari wakaonekana kugundua kwamba walimu walikuwa wamekwishagundua kilichokuwa kikiendelea.

“Hivi nani ana ujasiri wa kuniambia kwamba yeye ni Mtumishi wa Mungu?” lilikuwa swali la kwanza aliloliuliza mwalimu mkuu, swali ambalo halikupatiwa jibu lolote lile.
“Swali gumu. Samuel, wewe ni mtumishi wa Mungu? Unaishi kama Yesu alivyotaka tuishi?” mwalimu mkuu alimuuliza Samuel ambaye alibaki kimya, akayageuza macho yake usoni mwa Sadiki.
“Sadiki, wewe ni mtumishi wa Mungu? Unaishi kama Mtume Muhammad alivyotutaka tuishi?” mwalimu mkuu alimuuliza Sadiki ambaye wala hakujibu kitu chochote kile.

Siri ya kipindi kirefu ambayo ilikuwa imefichika siku hiyo ikaonekana kugundulika. Kuanzia siku hiyo, maisha yao yakawa ya unyonge sana jambo ambalo likawapelekea kutokusoma kabisa. Hakukuwa na siri tena, wanafunzi wakajua ni kitu gani ambacho kilikuwa kimeendelea katika maisha yao, wakaanza kudharauliwa kwa kuonekana kwamba walikuwa wakileta unafiki shuleni hapo.

Kila walipokuwa wakipita walikuwa wakidhihakiwa, walikuwa wakikasirika lakini hawakuwa na la kufanya. Uongozi wa shule haukutaka kuwarudisha nyumbani kwani waliona kwamba kilikuwa kimebakia kipindi kichache sana kabla ya wanafunzi wa kidato cha nne kufanya mitihani yao ya mwisho. Mpaka kipindi cha mitihani kinafika, wote walikuwa katika hali mbaya. Kutokana na kutosoma, wakajikuta wakiiona mitihani ile kuwa migumu kupita kawaida. Wiki mbili za mitihani zilipomalizika, wakaondoka shuleni hapo huku wakiwa wamemaliza shule na aibu kubwa.

“Tumemtenda Mungu dhambi,” Samuel alimwambia Sadiki katika kipindi ambacho walikuwa ndani ya basi wakirudi Dar es Salaam.
“Najua Samuel. Kuna kipindi kingine nabaki nikijuta kwa nini nilimruhusu shetani kunitawala maishani mwangu, sijui kingetokea kitu gani kama baba na mama wangejua kilichoendelea,” Sadiki alimwambia Samuel kwa sauti ya unyonge.
“Nitamrudia Mungu kwa mara nyingine tena, naamini nitasimama” Samuel alimwambia Sadiki.
“Sijui kama nitaweza. Moyo wangu umefadhaika sana, moyo wangu umekuwa na unyonge mkubwa kupita kawaida na sidhani kama nitakuwa na nguvu ya kumrudia Allah. Siwezi Samuel,” Sadiki alimwambia Samuel ambaye alikuwa akimwangalia tu kwa mshangao.

“Mungu anasamehe Sadiki,” Samuel alimwambia Sadiki.
“Najua. Mungu anasamehe sana lakini najiona kutokuwa na nguvu ya kumrudia, moyo wangu umekata tamaa kwa kila kitu maishani mwangu,” Sadiki alimwambia Samuel huku uso wake ukionekana kukata tamaa.
“Kwa hiyo unataka kumtumikia shetani?”
“Hapana. Sijamaanisha hivyo.”
“Kumbe umemaanisha nini?”
“Kuishi kivyanguvyangu.”
“Sikiliza Sadiki. Katika maisha yetu kuna mambo mawili tu katika kutumika. Kama ukishindwa kumtumikia shetani basi ni lazima utamtumikia Mungu na kama ukishindwa kumtumikia Mungu basi ni lazima utamtumikia shetani. Hauwezi kuishi kivyako vyako kama unavyosema. Utamtumikia shetani tu,” Samuel alimwambia Sadiki.

Siku hiyo ndani ya basi walikuwa wakiongea mengi sana. Kila mmoja alionekana kuwa mnyonge, mioyo yao ilikuwa ikiwasuta juu ya yale ambayo walikuwa wameyafanya katika maisha yao. Kitendo chao cha kuacha kumtumikia Mungu kikaonekana kuwaharibia kabisa taswira ya maisha yao ya mbele.

Waliona kila kitu kikiwa kimeharibika maishani mwao. Japokuwa walikuwa wamefanya mitihani ya Taifa ya kidato cha nne lakini walikuwa na uhakika wa asilimia mia moja kwamba wangekwenda kufeli mitihani ile kutokana na kutumia muda mwingi kufanya starehe na wasichana wao ambao walikuwa wamepanda basi tofauti na hilo.
“Nimeshafeli mtihani Samuel,” Sadiki alimwambia Samuel.

“Wewe ni kama mimi tu. Nimefeli pia. Tena nilifeli hata kabla mitihani haijafanyika,” Samuel alimwambia Sadiki.
“Tuangalie mbele yetu, naomba tusahau yaliyopita,” Sadiki alimwambia Samuel.
“Unavyoona tufanye nini tena?”
“Tutafute shule mapema za kuendelea na elimu ya kidato cha tano na sita,” Sadiki alimwambia Samuel.
“Itakuwa safi kama tutasoma shule moja Sadiki. Wewe ni rafiki yangu wa karibu sana, ningependa tuendelee kuwa pamoja zaidi na zaidi,” Samuel alimwambia Sadiki.
“Usijali. Nadhani shule ambazo tunatakiwa kwenda ni za mikoani tu,” Sadiki alimwambia Samuel.
“Hapana. Huko tutapotea sana Sadiki. Ni bora tusome shule za Dar es Salaam tu ili tuwe karibu na uangalizi wa wazazi wetu,” Samuel alimwambia Sadiki.
“Sitaki kuwa karibu na wazazi wangu Samuel.”
“Kwa nini?”
“Watakuwa wakinilazimisha kwenda msikitini.”
“Sasa hautaki kwenda tena msikitini?”
“Nimekwishakwambia kwamba sitaki kumtumikia Allah tena. Bora niishi na maisha yangu,” Sadiki alimwambia Samuel.
“Hapana Sadiki, unachokisema si sahihi kabisa. Maisha bila Mungu hayana kitu kabisa. Kumbuka kwamba hata Mtume Mohammad asingekuwa anamtumikia Mungu asingefika pale alipofika. Alifika pale kwa sababu alikuwa akimtumikia Mungu katika maisha yake na Mungu akaamua kumuinua. Unaposema kwamba hautaki kumtumikia tena Mungu unakosea sana Sadiki,” Samuel alimwambia Sadiki.
“Nimekata tamaa Samuel,” Sadiki alimwambia Samuel kinyonge.
“Huu ndio muda ambao Mungu anataka tumrudie ili aweze kutuinua tena,” Samuel alimwambia Sadiki.
Safari nzima walikuwa wakiyazungumzia maisha yao. Walijua fika kwamba walikuwa wamefanya mambo mengi sana ambayo hayakuwa yakimpa Mungu Utukufu na hivyo walijiona kuwa na sababu ya kuomba msamaha na hatimae kuishi kama zamani.

Kwao, Mungu akaonekana kuwaaibisha sana. Kwao, Mungu alionekana kutopenda wao kuishi maisha ya kinafiki na hivyo alitaka shule nzima ijue kile kilichokuwa kikiendelea katika maisha yao ili iwe hata fundisho kwa wanafunzi wengine ambao walikuwa wakibaki shuleni pale.
“Mungu ameamua kutuaibisha,” Sadiki alimwambia Samuel.
“Hii ni kwa sababu tulikuwa tukileta unafiki. Mungu hapendi unafiki, Mungu hapendi tusimame mguu moja kwake mmoja kwa shetani, anataka tusimame miguu yote kwake tu au kwa shetani na si kusimama katika falme mbili tofauti. Kupitia aibu tuliyoipata shuleni, Mungu ametaka tujifundishe kitu kimoja,” Samuel alimwambia Sadiki.
“Kitu gani?”
“Kwamba Yeye ndiye Muweza wa kila kitu na kipindi chote alikuwa akichukia maisha ambayo tulikuwa tukiyaishi. Katika maisha yangu yote sitoweza kuisahau aibu ambayo imetukuta shuleni katika kipindi hiki Sadiki. Nitaendelea kukumbuka maishani mwangu mpaka nakufa,” Samuel alimwambia Sadiki.

Basi lilichukua masaa nane mpaka kuingia jijini Dar es Salaam ambapo wakakodi bajaji ambayo ilianza kumfikisha Samuel Mwenge na kisha kumpeleka Sadiki Magomeni alipokuwa akiishi.
Samuel alionekana kuwa mnyonge. Katika kipindi ambacho alikuwa akifungua geti la nyumbani kwao, moyo wake ukaongezeka upweke, maneno ya mistari mingi ya Biblia ambayo ilikuwa imeandikwa mlangoni ikaonekana kumchoma kupita kawaida.

Akaufuata mlango na kisha kusimama. Hakutaka kuingia, akabaki mlangoni pale na kisha kuanza kufikiria maisha yake ya shule na aibu ambayo alikuwa amekumbana nayo. Moyo wake ulikuwa kwenye maumivu makali, kwa wakati huo alikuwa akijuta kwa kuubadilisha moyo wake na kumtumikia shetani kwa nguvu zote. Alisimama mlangoni pale kwa muda wa dakika mbili nzima na ndipo akaufungua mlango. Ghafla katika hali ambayo hakuitegemea akakutana na wazazi wake pamoja na ndugu zake wengine ambao walikuwa wameshika maua na kisha kuanza kumwagia huku wakiwa katika nyuso za furaha.

“Supriseeeeeee,” Wote walisikika wakisema kwa sauti ya juu iliyomshtua Samuel.
Samuel alionekana kushtuka sana, badala ya kufurahia kile ambacho alikuwa amekutana nacho mahali hapo, bado uso wake ukaonekana kuwa na huzuni jambo ambalo likawafanya wazazi wake, mchungaji Mpelele pamoja na mama yake, Bi Magreth kumsogelea huku wakionekana kushangaa.

“Kuna nini tena?” Mchungaji Mpelele alimuuliza Samuel ambaye akaliweka begi lake chini na kisha kuanza kulia.
Kila mmoja akaonekana kushtuka, hawakuelewa ni kitu gani ambacho kilimfanya Samuel kuanza kulia. Hapo ndipo walipoanza kumbembeleza na kisha kuanza kumfanyia maombezi ambayo yalichukua kwa zaidi ya dakika tano.
“Kuna nini Samuel?” Mchungaji Mpelele alimuuliza Samuel.
“Nimemtenda Mungu dhambi,” Samuel alijibu.
“Umemtenda Mungu dhambi?”
“Ndio baba. Nimekuwa nikimtumikia shetani shuleni,” Samuel aliwaambia.
“Hebu subiri kwanza. Imekuwaje?” Mchungaji Mpelele alimuuliza kijana wake, Samuel ambaye akaanza kuelezea mengi ambayo yalitokea shuleni.
Kila mmoja alionekana kushtuka, hawakuamini kama Samuel angeweza kufanya kile ambacho alikuwa amewaelezea mahali hapo. Ilikuwa ni stori ambayo ilimgusa kila mmoja, Samuel, kijana ambaye alikuwa akitarajiwa kuwa mtumishi mzuri wa Mungu hapo baadae tayari alikuwa ameanguka dhambini, dhambi ya uzinzi ilikuwa imemwelemea.
“Mungu anasamehe kama tu utaomba msamaha kwa kila ulichokifanya. Mungu wetu ni mwingi wa rehema,” Mchungaji Mpelele alimwambia Samuel na kisha kuanza kumuongoza sala ya toba.

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 07

Sadiki akaonekana kukata tamaa, tayari moyo wake ulikuwa umenyong’onyea kupita kawaida, alijiona kutokuwa na nguvu kuwa kama katika kipindi kilichopita. Maisha ambayo alikuwa ameishi shuleni kificho, maisha ya kumtumikia shetani yakaonekana kumuumiza kupita kawaida, aibu ambayo alikutana nayo shule ndio ambayo ilionekana kumdhoofisha kupita kawaida.

Katika kipindi hicho hakufikiria kuwa mtu wa dini kama alivyokuwa zamani, alitamani kuishi maisha ya peke yake, maisha ya kutokumuabudu Allah na maisha ya kutokumtumikia shetani. Kila wakati Sadiki alikuwa akionekana kuwa mnyonge. Baba yake, ustadhi Hamadi hakupenda kumuona mtoto wake akiwa katika hali hiyo jambo ambalo mara kwa mara alikuwa akimuuliza lakini Sadiki akaonekana kuficha.

Msikitini hakuwa akienda tena, hakuwa akivaa kanzu tena na wala hakupoteza muda wake wowote kusoma kitabu kitakatifu cha Qur-an . Aliamua kwa moyo mmoja kuishi maisha yake, kwake, mambo ya dini yakaonekana kumuendea kushoto.

Kadri siku zilivyozidi kwenda mbele na ndivyo ambavyo chuki kubwa na msikiti ilipokuwa ikimuingia. Hakupenda kuuona msikiti wowote ule, hakupenda kuwaona waislamu wenzake wakiwa wamevaa kanzu na kuelekea msikitini. Maisha ambayo alikuwa akiishi kwa wakati huo yalikuwa ni maisha ya tofauti kabisa.
“Umebadilika. Umebadilika Sadiki, hata msikitini hautaki kwenda. Kwa nini?” Mzee Hamidu almuuliza Sadiki ambaye alibaki kimya kwa muda.

Swali hilo likayarudisha mawazo yake nyuma kabisa katika kipindi ambacho alikuwa shuleni, kipindi ambacho alikuwa akileta unafiki mbele ya macho ya watu kwa kujifanya mtu wa dini na wakati alikuwa akifanya mambo mengi gizani yakiwepo ulevi pamoja na uzinzi.

“Sipendi kwenda msikitini” Sadiki alimwambia baba yake, ustaadhi Hamidu ambaye alionekana kushtuka.
Kwanza akaanza kumwangalia mtoto wake mara mbili mbili huku akionekana kutokuamini kile ambacho alikuwa amekisikia kutoka kwake. Hakujua ni kitu gani ambacho kilikuwa kimetokea kwa mtoto wake mpaka kuamua kusema maneno yale huku akionekana kuwa na ujasiri mkubwa kiasi kile.
“Unasemaje?” Ustaadhi Hamidu aliuliza huku akionekana kushtuka.
“Sitaki kwenda msikitini” Sadiki alijibu kwa kujiamini.
“Kwa nini?
“Sitaki kutumia falme mbili tofauti. Mimi ni mwenye dhambi baba, sitaki kuwa mnafiki kwa mara nyingine tena” Sadiki alimwambia baba yake ambaye alionekana kutokumuelewa.
“Kuna kitu gani kimetokea?”
“Nimekuwa nikiishi maisha ya kumtumikia shetani kwa kipindi kirefu baba, naomba nipumzike, sitaki kuwa mnafiki maishani mwangu. Nimeshindwa kumuabudu Allah” Sadiki alimwambia baba yake, ustadhi Hamidu.

Maneno yakaonekana kuwa kama mwiba mkali moyoni mwa Ustadhi Hamidu, hakuamini kama kijana wake angeweza kutamka maneno yale kwa kujiamini kiasi kile. Akabaki akimwangalia mara mbili mbili huku akijiona kama mtu ambaye alikuwa akiota. Katika maisha yake yote ustadhi Hamidu alikuwa akijitahidi kumlea mtoto wake, Sadiki katika maisha ya kumcha Allah ili baadae aje na kuwa ustaadhi mkubwa kama ambavyo alivyokuwa. Katika kipindi cha nyuma aliona kila kitu kikienda kama alivyokuwa akitaka kiwe hasa mara baada ya Sadiki kuhudhuria mafundisho mengi ya Kiislamu ambayo yalikuwa yakimhusu Mtume Muhammad S.A.W.

Kwa wakati huo Sadiki akaonekana kubadilika, hakuonekana kuipenda tena dini, hakuonekana kumpenda Allah, alionekana kumsaliti mtume Muhammad S.A.W na wakati katika kipindi cha nyuma aliahidi kwamba kamwe asingeweza kuishi maisha ya dhambi kwani lengo lake kubwa lilikuwa ni kuja kuwa Mufti nchini Tanzania. Maisha ya dhambi ambayo alikuwa ameishi shuleni yalionekana kubadilisha kila kitu katika kipindi hicho, alikuwa akiichukia sana dini, hakutaka kujihusisha nayo hata mara moja. Ustaadhi Hamidu bado alikuwa amechanganyikiwa kupita kawaida, maneno ambayo alikuwa ameongea mtoto wake yalionekana kumchanganya kupita kawaida.

“Umeingiliwa na nini Sadiki? Kwa nini umekuwa hivyo?” Ustaadhi Hamidu alimuuliza mtoto wake, Sadiki.
“Kwa nini niwe mnafiki baba? Kwa nini nimtumikie Allah na shetani kwa wakati mmoja baba. Haiwezekani, haiwezekani kabisa” Sadiki alimwambia baba yake. Huo ndio uamuzi ambao Sadiki alikuwa ameupanga kwa wakati huo, hakutaka kutumikia falme mbili kwa wakati mmoja kwani kwa kufanya hivyo alikuwa akijiona kufanya kitu kibaya katika maisha yake. Maisha ya kumtumikia shetani yakaanza rasmi. Sadiki hakutaka kwenda msikitini kuswali hata mara moja, vitabu vyote vitakatifu vya Qur-an ambavyo vilikuwa chumbani kwake akavitoa na kuviweka katika chumba cha wazazi wake.

Picha mbalimbali zilikuwa na jumbe nyingi za kumtukuza Allah ambazo alikuwa amezibandika katika ukuta chumbani kwake akazitoa na kisha kuzipeleka chumbani kwa wazazi wake. Katika kipindi hicho hakutaka kujihusisha na kitu chochote cha dini maishani mwake, alitaka kuishi maisha mapya, maisha ambayo hakutakiwa kwenda msikitini au kujihusisha na kitu chochote kuhusiana na dini

“Ni heri niwe hivi kuliko kuwa mnafiki” Sadiki alijisemea bila kujua kwamba katika kipindi ambacho unapoamua kumuacha Mungu maishani mwako nae hukuacha ili uendelee na maisha yako.

Siku ziliendelea kukatika kama kawaida. Mara kwa mara Samuel alikuwa akionana na Sadiki ambaye alionekana kukata tamaa kuhusiana na kumrudia Mungu na kutengeneza mambo yake kama ilivyokuwa katika kipindi cha nyuma. Wazazi wake wakaonekana kukata tamaa lakini kamwe hawakusita kuomba dua kwamba siku moja Sadiki arudi kule alipotoka.
Katika kipindi hicho, bado hakuwa akielekea msikitini, madrasa ambayo alikuwa amekabidhiwa katika kipindi cha nyuma akaamua kuachana nayo. Maisha ya kuishi bila kufanya ibada au kusoma kitabu chochote cha dini ndio yalikuwa maisha ambayo alikuwa ameamua kuishi kwa wakati huo.

Moyo wake haukujuta kabisa kutokana na hatua ambayo alikuwa ameichukua katika maisha yake, moyoni mwake, aliona kila kitu kuwa sahihi kabisa. Ustadhi Hamidu hakutaka kukata tamaa kwa mtoto wake, mara kwa mara alikuwa akimsisitiza kumrudia Mungu lakini jambo hilo bado lilionekana kuwa gumu kwa Sadiki ambaye alionekana kuzidi kubadilika.

Kutokana na kupita kipindi kirefu cha mwezi mmoja bila kunywa pombe, Sadiki akaanza tena kunywa pombe kwa kujificha kwani hakutaka wazazi wake wamgundue kwamba alikuwa ameingia katika ulevi wa pombe. Mara kwa mara alikuwa akijificha sehemu na kisha kunywa kiasi fulani cha pombe na kusha kutafuna Big G ambazo zilikuwa zikimletea harufu fulani mdomoni mwake na kuipoteza harufu ya pombe ile.

Sadiki hakuishia hapo, bado aliendelea kubadilika zaidi na zaidi mpaka pale ambapo akaanza kutumia mirungi. Kila siku alikuwa akikusanya mirungi mingi ambayo alikuwa akiletewa na rafiki wake wa Kiarabu na kuanza kuitafuna kama mbuzi huku akisindikizia na Big G. Kadri siku zilivyozidi kwenda mbele na ndivyo ambavyo Sadiki alizidi kubadilika zaidi na zaidi na kuwa mtu wa tofauti na jinsi alivyokuwa kabla.

“Mmmh! Mbona unatafuna majani kama mbuzi?” Mama yake, Bi Aisha alimuuliza katika kipindi ambacho alimkuta akila mirungi.
“Hapana mama” Sadiki alisema.
“Sasa hiyo ni nini? Au ndio hiyo mibangi yenu?” Bi Aisha alimuuliza Sadiki ambaye wala hakujibu kitu zaidi ya kuondoka mahali hapo.

Bi Aisha akaonekana kushindwa kuvumilia, alichokifanya mara baada ya mumewe, ustadhi Hamidu aliporudi kutoka msikitini kuswalisha akampa taarifa kuhusiana na majani ambayo alikuwa akiyala Sadiki. Ustadhi Hamidu akaonekana kufahamu dhahiri kwamba majani ambayo mke wake alikuwa akiyazungumzia ilikuwa ni mirungi. Alichokifanya huku akionekana kuwa na hasira, akaanza kuelekea katika chumba cha Sadiki.

“Umeanza kula mirungi ndani ya nyumba yangu” Ustadhi Hamidu alimwambia Sadiki huku akionekana kuwa na hasira.
“Yaani unafanya upumbavu wako mwingi unaonekana kutokutosheka mpaka kuja kula mirungi ndani ya nyumba yangu. Yaani mimi baba yako ni Imamu mkubwa hapa Magomeni halafu eti leo ndani ya nyumba yangu unaingiza mirungi. Sadiki...Sadiki....” Ustadhi Hamidu alimwambia Sadiki.

Moyo wa Ustadhi Hamidu ulikuwa kwenye maumivu makali kupita kawaida. Mabadiliko ambayo alikuwa ameyaonyesha mtoto wake, Hamidu katika kipindi kichache yalionekana kumuumiza kupita kawaida. Kwake, aliyachukulia hayo kuwa sehemu ya majaribu kwa kuona kwamba Mungu alitaka kumjaribu kupitia mtoto wake na hivyo kupunguza kufanya mambo ya ibada.

“Tatizo nini baba?” Sadiki alimuuliza baba yake huku akiendelea kula mirungi ile.
“Unaniuliza tatizo nini! Tatizo haulioni Sadiki? Hauoni wewe kula mirungi ni tatizo kubwa?” Ustadhi Hamidu alimuuliza Sadiki.
“Mbona unanilalamikia sana baba kana kwamba nimekuchukulia mkeo?” Sadiki alimuuliza baba yake swali ambalo lilionekana kumkasirisha sana ustadhi Hamidu.
“Unasemaje?”
“Umenisikia vizuri sana. Kila mtu na stimu zake bwana, kama wewe stimu zako kuswali sisi wengine stimu zetu kula mirungi na kunywa pombe” Sadiki alimwambia baba yake.
“Unanijibu majibu yako ya kipumbavu!!!!”
“Sikiliza baba, kula mirungi siyo tatizo na ndiyo maana Mungu kauweka mmea huu uendelee kukua. Kama ingekuwa ni tatizo, Mungu asingeruhusu mmea huu ukue, nashangaa unavyonimaindi, ungekuwa wewe ndiye Mungu, nadhani hata ngano usingeiotesha kwa kudai kwamba zinatengenezwa pombe,” alisema Sadiki, maneno hayo yakamkasirisha zaidi baba yake.

Ni kweli katika maisha yake ustadhi Hamidu alikwishawahi kudharauliwa mara nyingi na vijana wengi lakini kwa dharau ambazo alizionyesha mtoto wake mwenyewe, Sadiki siku hiyo zilionekana kuwa dharau kubwa ambazo hakuweza kuamini. Ustadhi Hamidu hakusema kitu, alichokifanya ni kutoka ndani ya chumba kile huku machozi yakianza kumlenga machoni mwake.

Moyoni alijisikia akihukumiwa kutokana na kushindwa kumdhibiti Sadiki kutokana na tabia ambayo alikuwa ameianza ya kula mirungi. Hilo likaonekana kuwa pigo kubwa moyoni mwake, kila alipokuwa akielekea msikitini kuswalisha, moyoni mwake kulikuwa kukija sauti ambayo ilikuwa ikimdhihaki kwa kitendo cha kushindwa kumzuia mtoto wake kutumia vilevi mbalimbali.

Baada ya kipindi fulani, mtaa wa Magomeni mapipa wakafahamu kwamba Sadiki alikuwa amebadilika. Watu wengi wakaonekana kushtuka, kitendo cha Sadiki kubadilika na kuwa namna ile kilionekana kumshtua kila aliyekuwa akisikia.
Hawakuamini kama mtoto wa Imamu wa msikiti mkubwa wa Kichangani alikuwa amebadilika na kuwa vile alivyokuwa, hawakuamini kama mwalimu wa Madrasa ya Nur- Munira Sanoor iliyokuwa Magomeni alikuwa amebadilika na kuwa mlevi. Watu wengi wakaanza kuamini kwamba ushirikina ndio ambao ulikuwa umesababisha mpaka Sadiki kuingia katika maisha yale.

Watu wengi wakaanza kumfuata ustadhi Hamidu na kumshauri kwamba ilikuwa ni lazima aende akaonane na mganga yeyote mkubwa kwa ajili ya tatizo lile lakini ustadhi Hamidu hakutaka kukubaliana nao kabisa. Katika maisha yake hakutaka kumwamini mganga zaidi ya Allah, katika maisha yake hakutaka kuweka tumaini lake kwa mwanadamu yeyote yule.

Siku zikaendelea kukatika mpaka kufikia kipindi ambacho matokeo ya kidato cha nne yalipotoka. Kama ambavyo walivyotarajia ndivyo ambavyo ilivyokuwa. Samuel na Sadiki walikuwa wamepata sifuri katika mitihani yao jambo ambalo likaonekana kuwa aibu kwa wazazi wao ambao walikuwa ni watu wa ngazi za juu ambao walikuwa wakiheshimika katika dini zao.

“Umefeli sana. Yaani umefeli sana Sadiki” Ustadhi Hamidu alimwambia Sadiki kwa sauti ya majonzi.
“Kawaida tu mzee” Sadiki alijibu.
“Kawaida?”
“Ndio. Kwani Tanzania nzima nimefeli peke yangu? Halafu kufeli hakumaanishi kwamba sikuwa nikisoma, upepo tu haukuvumia kwangu” Sadiki alimwambia baba yake, ustadhi Hamidu.
“Badilika Sadiki. Allah si binadamu mpaka umchezee namna hiyo” Ustadhi Hamidu alimwambia Sadiki.
“Nibadilike! Nitabadilika vipi na nibadilike kuwa nani?” Sadiki aliuliza.
“Kuwa mtu mwema kama zamani”
“Kwani sasa hivi mimi sio mtu mwema? Kwani nimeua? Kwani nimebaka? Kitu gani kinakufanya kusema mimi si mtu mwema?” Sadiki aliuliza huku akimwangalia baba yake usoni.
“Kuwa kama zamani. Acha ulevi Sadiki”
“Baba unaonekana kuwa si muelewa kabisa. Kama pombe zingekuwa zinamfanya mtu kuwa mbaya basi serikali ingepiga marufuku uuzaji wa pombe hapa nchini, na kama mirungi inamfanya binadamu kuonekana kuwa mbaya basi natumaini hata Mungu asingeweza kuiotesha ardhini hapa duniani. Nadhani vitu hivi vinaonekana kuwa bora na ndio maana serikali imeacha kampuni mbalimbali zitengeneze pombe na hata Mungu kaacha mimiea hii ya mirungi iendelee kuota kwa ajili ya kutufaidisha” Sadiki alimwambia baba yake.
Katika kipindi cha miezi kadhaa toka Sadiki arudi kutoka shuleni alikuwa amebadilika na kuwa mtu mbaya sana. Muda mwingi alikuwa akijifungia chumbani kwake akitafuna mirungi pamoja na kunywa pombe. Ustadhi Hamidu alikuwa amezungumza nae mpaka kuchoka lakini Sadiki hakuonekana kubadilika kabisa.
“Ni lazima aende shule tena” Ustadhi Hamidu alimwambia mkewe, Bi Aisha.
“Mmmh!” Bi Aisha aliguna.
“Unaguna nini tena mke wangu?”
“Ataweza kusoma huyu?”
“Kwa jinsi alivyo, kusoma ngumu sana” Ustadhi Hamidu alimwambia mke wake.
“Kama hatoweza kusoma, kwa nini tumpleke shule?” Bi Aisha aliuliza.
“Kwa sababu atoke maeneo ya nyumbani. Ninaamini atakapokuwa huko ataweza kuchana hata kutafuna mirungi yake na kunywa pombe. Cha msingi tumtafutie shule ya bweni ambayo itakuwa na ulinzi mkali” Ustadhi Hamidu alimwambia mke wake.
Huo ndio uamuzi ambao ulikuwa umefikiwa. Mara baada ya Sadiki kuona kwamba alikuwa akitarajiwa kurudishwa shuleni hapo ndipo alipoanza kuwasiliana na rafiki yake, Samuel na kuanza kuongea nae ili kama ingewezekana basi waende kusoma shule moja.
“Ila mimi nimebadilika Sadiki, namshukuru Mungu kwa kunibadilisha” Samuel alimwambia Sadiki.
“Sikiliza Samuel, tunachokiongea hapa si mabadiliko, tunaloongea hapa ni kwenda kusoma shule moja. Mabadiliko yako hayanihusu” Sadiki alimwambia Samuel.
“Najua ila natakiwa kukuambia ukweli Sadiki”
“Sawa. Nimekuelewa. Niambie, itawezekana au manake wote tushafeli” Sadiki alimuuliza Samuel.
“Hakuna tatizo” Samuel alijibu.

Kama walivyokuwa wamepanga na ndivyo ambavyo ilivyokuwa. Baada ya miezi kadhaa, wakaanza kusoma kwa ajili ya kurudia mitihani yao katika shule ya Makongo huku wote wakiwa wamelilia kutaka kuweka katika hosteli za wanafunzi wa vyuo mbalimbali zilizokuwa Kinondoni.

Kitendo cha kuruhusiwa kwenda kusoma katika shule hiyo pamoja na kukaa hosteli yalionekana kuwa makosa makubwa sana. Katika kipindi cha kwanza Samuel alionekana kuwa na msimamo mkali sana kwa kudhani kwamba tayari alikuwa amemrudia Mungu na hivyo alikuwa akiishi Kitakatifu.

Katika kipindi cha wiki moja tu cha kukaa na Sadiki tayari kiu ya mambo yale ambayo alikuwa amewaambia wazazi wake kwamba alikuwa ameachana nayo ikaanza kumkaba. Kila alipokuwa akimuona Sadiki akinywa pombe huku akimtambia kwamba alikuwa akikosa utamu na radha iliyo bora duniani, akajikuta akitamani kunywa pombe kwa mara nyingine tena.
Maisha ambayo alikuwa akiishi zamani ambayo alisema kwamba alikuwa ameachana nayo yakaanza kurudi tena, Samuel akarudia kunywa pombe na kisha kufundishwa namna ya kutafuna mirungi kitu ambacho alipokizoea kilionekana kumpa stimu zaidi na zaidi.

Katika maisha yao ndani ya hosteli ile yakaonekana kuwashangaza hata wanachuo ambao walikuwepo ndani ya hosteli ile. Samuel na Sadiki wakaonekana kupenda sana starehe kuliko vitu vingine mahali hapo. Sadiki akawa mtu wa kunywa pombe kwa sana na mirungi huku Samuel akiingia katika tabia nyingine, kutembea na wanawake mbalimbali shuleni.
Matendo yao yakaonekana kuwashangaza hata walimu, wanafunzi hao ambao walikuwa wameletwa shuleni hapo kwa ajili ya kusoma na mwisho wa siku kurudia mitihani yao ya kidato cha nne walionekana kuwa na maisha ya ajabu ambayo yalikuwa yakimshangaza kila mtu.

Si kila siku walikuwa wakifika shuleni pale, mara nyingi walikuwa wakikaa chumbani wakinywa na kuvuta sigara mfululizo pamoja na kutafuna mirungi ambayo walikuwa wakiletewa na waarabu ambao waliwafanya kuwa kama wateja wao wakubwa.

“Badilikeni bwana...mnatuzingua na maisha yenu” Cosmas, kijana ambaye walikuwa wakiishi nae ndani ya chumba kimoja aliwaambia.
“Tuweje sasa?” Samuel alimuuliza Cosmas.
“Kama watu wengine mahali hapa. Yaani kwa tabia zenu kila mtu anawashangaa na ndio kwanza mpo sekondari” Cosmas aliwaambia huku akionekana kukasirika.
“Mbona wewe hubadiliki”
“Nibadilike kwa lipi?”
“Kwa kumvua sketi Halima” Samuel alimwambia Cosmas.
“Hivi unafikiri mapenzi nayashobokea sana kama wewe unavyoyashobokea kwa kutembea na mademu wengi, hiyo sio sifa, mademu ni watu wa kupita tu na kamwe siwezi kuwashobokea. Siwezi kubadilisha kama nguo, mmoja ananitosha na si kama wewe” Cosmas alimwambia Samuel.
“Nisikilize Cosmas. Ishu si kuwa na demu mmojammoja tu, ishu ni kuwa muaminifu. Unaweza wewe kuwa muaminifu halafu demu unayempata sio mwaminifu” Samuel alimwambia Cosmas.
“Mimi ni mwaminifu na hata Halima ni mwaminifu pia. Hatuna matatizo katika mahusiano yetu” Cosmas alimwambia Samuel.
“Usiusemee moyo. Una uhakika Halima ni mwaminifu? Unajiamini kwa kumuwekea dhamana demu? Toka lini demu akawekewa dhamana?”
“Nina uhakika. Halima ni msichana anayejitambua sana, ni msichana ambaye anaelewa mapenzi ni nini na si kama wasichana wako unaowachukua ambao unawatoa Uwanja wa Fisi” Samuel alimwambia Cosmas.
“Sasa hizo dharau Cosmas” Sadiki alimwambia Cosmas ambaye alionekana kama mtu mwenye hasira.
“Ukweli ndio huo. Mademu anaowachukua rafiki yako wote wachafuwachafu tu” Cosmas alimwambia Sadiki na kisha kuinuka mahali hapo na kuondoka.
Samuel alibaki kimya huku akionekana kuwa na hasira. Hakujua ni kitu gani ambacho alitaka kuongea mahali hapo, baada ya sekunde chache, akasimama na kisha kuanza kutembea tembea ndani ya chumba kile huku akionekana kutokuamini kama maneno yale ambayo yalisikikika masikioni mwake yalikuwa yametoka mdomoni mwa Cosmas.
“Watu hawa dawa yao moja tu” Samuel alimwambia Sadiki.
“Ipi?”
“Kutembea na demu wake na kisha kujipiga picha kadhaa” Samuel alimwambia Sadiki.
“Hahaha! Hayo mambo nakuachia wewe player...sisi wengine mademu zetu pombe na mirungi tu” Sadiki alimwambia Samuel huku akitafuna mirungi.
“Ngoja nimuonyeshee jinsi mchezo unavyokuwa” Samuel alimwambia Sadiki.
“Shida ni kutembea na Halima tu?”
“Ndio maana yake. Nataka nitembee nae na kisha nimuonyeshee picha ili aache dharau”
“Utaanzaje kutembea nae?”
“Kazi ndogo tu. Halima udhaifu wake upo sehemu moja tu” Samuel alimwambia Sadiki.
“Sehemu gani?”
“Pombe. Anapenda sana pombe. Ngoja nimuonyeshee kazi” Samuel alimwambia Sadiki huku akionekana kupania kile ambacho alikuwa amekiongea mahali pale.
“Ila Halima si anakujua?” Sadiki aliuliza.
“Hanifahamu wala nini, hajawahi kuniona japo sisi tumekuwa tukimuona kila siku” Samuel alimwambia Sadiki.
“Sasa umjuaje kama anapenda pombe?”
“Si huwa unamsikia bwana wake anavyosema kwamba demu wake mnywaji mzuri wa pombe, wewe niachie mimi kaka” Samuel alimwambia Sadiki.

Itaendelea kesho.
 
SEHEMU YA 08

Samuel alikuwa amedhamiria kufanya kile alichokuwa akitaka kukifanya. Shauri mbalimbali ambazo walikuwa wakipewa na Cosmas pamoja na kumsifia msichana wake, Halima kwamba alikuwa mwaminifu vilikuwa ni vitu vilivyomuumiza sana moyoni mwake na kutamani kumuoneshea Cosmas kwamba msichana hakutaka kupewa uaminifu wa asilimia mia moja wala kumsifia kama alivyokuwa akifanya.

Siku ambayo alikuwa amepanga kuanza kazi kwa Halima ikafika. Cosmas alipokuwa akielekea bafuni kuoga ndicho kikawa kipindi ambacho Samuel akaichukua simu ya Cosmas na kisha kuchukua namba ya Halima na kuihifadhi katika simu yake.

B4 Tayari alijiona kukamilisha kila kitu, kitendo cha kupata namba ya simu ya Halima kilionekana kuwa nusu ya ushindi.
Walikuwa wakimfahamu sana Halima, udhaifu wake wa kupenda pombe ndio uliowapa uhakika kwamba Samuel angeweza kukamilisha kufanya kile ambacho alikuwa akitaka kukifanya kutokana na kuwa na fedha za kutosha huku nae akipenda sana kunywa pombe.

“Wewe ni nani?” Ilisikika sauti ya Halima simuni ikimuuliza Samuel ambaye alimpigia simu.
“Unaongea na Paul,” Samuel alimjibu Halima.
“Paul, ndiye nani?” Halima aliuliza simuni.
“Mvulana anayesoma CBE.”
“Umeipata wapi namba yangu?” Halima aliuliza.
“Nimeinunua. Nimetoa kiasi cha shilingi elfu kumi na tano kwa ajili ya namba yako tu. Nahitaji kukuona, itawezekana Halima?” Samuel alimuuliza Halima.
“Haiwezekani,” Halima alisema na kukata simu.

Samuel akaonekana kusikitika sana, hakuamini kama msichana huyo angeweza kukata simu bila kumsikiliza shida yake. Tayari jambo lile ambalo alikuwa amelipanga pamoja na rafiki yake, Sadiki likaonekana kuwa gumu kufanyika, wote kwa pamoja walikuwa na hamu kubwa ya kuumiza moyo wa Cosmas ambaye alikuwa akimuamini sana msichana wake.
Samuel hakuishi hapo, kila siku alikuwa akipata kazi kubwa ya kumpigia simu Halima. Mara nyingi simu ilikuwa ikiita bila kupokelewa na kama ilitokea kupokelewa, basi alikuwa akipokea msonyo mmoja na kisha simu kukatwa.

Samuel hakutaka kukata tamaa, kila siku ndoto yake ilikuwa ile ile tu, kutaka kumuingiza Halima katika mikono yake ili apate nafasi ya kumuumiza Cosmas na kumuonyeshea kwamba wanawake hawakutakiwa kuonyeshewa uaminifu wa hali ya juu kama alivyokuwa akifanya kwa msichana Halima.

Siku zikaendelea kukatika, Samuel hakukoma kumpigia simu Halima. Mara kwa mara tena kila siku alikuwa akimpigia simu Halima lakini hali ilikuwa ile ile. Hapo ndipo Samuel akapata wazo jipya, wazo ambalo aliliona kufaa sana, akaanza kuandika meseji nyingi na kumtumia.

Samuel alijua fika kwamba meseji zote zile ambazo alikuwa akizituma Halima alikuwa akizipokea na kuzisoma. Hata kama alikuwa akizifuta lakini bado alikuwa amekwishazisoma na kujua ni uhitaji gani ambao Samuel alikuwa akiutaka kutoka kwake.

Mwezi mzima Samuel alikuwa akiendelea kumtafuta Halima na kumuingiza katika himaya yake. Kwa kiasi fulani meseji ambazo alikuwa akimtumia zikaonekana kuanza kumbadilisha Halima. Kwa sababu zilikuwa ni kati ya meseji zenye kugusa moyo na zilizoonyesha uhitaji mkubwa, Halima akaonekana kuanza kubadilika kwa kuanza kupokea simu na kumsikiliza Samuel alikuwa na shida gani.

“Kwa nini unataka kuonana nami Paul?” Halima aliuliza.
“Ninataka kuongea nawe Halima. Kuna tatizo hapo?” Samuel alimuuliza.
“Ndio. Kuna tatizo.”
“Tatizo gani?”
“Tena sio tatizo, kuna matatizo.”
“Matatizo gani?”
“Sina muda.”
“Hilo siyo tatizo. Naomba uniambie tatizo Halima” Samuel alimwambia Halima.
“Huwa sipendi kukutana na watu nisiowafahamu.”
“Kwa sababu gani?”
“Basi tu huwa sipendi.”
“Acha uoga Halima. Kukutana na watu usiowafahamu ndio mwanzo wa kuwafahamu. Nadhani marafiki zako wote ambao uliwahi kukutana nao kwa mara ya kwanza haukuwa ukiwafahamu, si ndio hivyo?” Samuel alimuuliza halima.
“Yeah!”
“Na baadae ukaja kuwafahamu, si ndio hivyo?”
“Yeah!”
“Basi nadhani hilo si tatizo, hata nami utakwenda kunifahamu tu.” Samuel alimwambia Halima.
Japokuwa Samuel alikuwa akitumia sana vilevi lakini akili yake katika kufanya mazungumzo ilikuwa na uwezo mkubwa sana. Ushawishi wake mkubwa ambao alikuwa nao maishani mwake ulikuwa na uhakika wa asilimia kubwa ya kubadilisha mambo mengi sana katika akili ya mtu. Kitendo cha Halima kukubali kumsikiliza Samuel kwa muda wa dakika mbili tu, tayari akaonekana kuwa mtu ambaye hakuwa na tatizo lolote lile.
“Lakini kwa nini unataka kuonana nami Paul?” Halima alimuuliza Paul.
“Nahitaji kukufahamu zaidi. Nimejaribu kukutafuta kwa muda wa mwezi mzima Halima, hivi kama nisingekuwa na umuhimu wa kuonana nawe si ningeachana nawe Halima. Hebu wakati mwingine naomba uuthamini uvumulivu wangu ambao nimejiwekea juu yako, mwezi mzima halafu bado unataka kunikatalia! Hiyo ni dhambi Halima” Samuel alimwambia Halima.

Katika kila neno ambalo alikuwa akiongea mahali hapo lilikuwa likiubadilisha moyo wa Halima na kumfanya kukubaliana nae. Tayari kwa maneno yake ambayo alikuwa akiyaongea, kwa majibu yake ambayo alikuwa akiyajibu, moyo wa Halima ukaonekana kubadilika, kiu ya kutaka kuonana na mvulana huyo na kuongea nae ikaonekana kuanza kumshika.
“Ok! Tutaonana nikimaliza mitihani,” Halima alimwambia Samuel.
“Mnaanza lini hiyo mitihani?”
“Wiki ijayo.”
“Mbona mbali sana Halima. Yaani unataka kuniweka na presha wiki nzima na wakati nilikuwa na kiu ya kuonana nawe kwa mwezi mzima. Tafadhali Halima naomba usinifanyie hivi,” Samuel alimwambia Halima kwa sauti ya kipole.
“Nina mitihani Paul.”
“Najua. Ila sidhani kama kuonana nawe kwa dakika ishirini kutakufanya kufeli au kutosoma. Naomba tuonane hata kesho,” Samuel alimwambia Halima.
“Kesho?”
“Ndio. Kwani kuna tatizo hapo?”
“Yeah! Kesho nitakuwa bize sana.”
“Masaa ishirini na nne?”
“Bado sijajua.”
“Naomba unisikilize Halima. Kwenye masaa ishirini na nne ambayo ni sawa na dakika 1440 ninahitaji dakika 20 tu za kukutana nawe na kuongea. Nakuomba Halima,” Samuel alimwambia halima huku akijaribu kuiweka sauti yake katika huruma.
“Sawa. Dakika ishirini tu,” Halima alimwambia Samuel.
“Nitakuwa mwaminifu katika hilo,” Samuel alimwambia Halima.
Hapo ndipo walipopanga kuonania. Kwa Samuel hakutaka kuonana na Halima katika sehemu tofauti na baa kwa kuamini kwamba kama wangeonana katika sehemu hiyo basi ilikuwa ni lazima kwa Halima kunywa pombe jambo ambalo lingempa urahisi wa kutaka kufanya kile alichokuwa akitaka kukifanya.
“Nakwenda kuonana naye pale Kijitonyama Bar usiku wa leo” Samuel alimwambia Sadiki.
“Acha utani.”
“Siwezi kukutania. Huyu mjinga atalia na kunichukia milele,” Samuel alimwambia Sadiki.
Samuel hakutaka kuchelewa, kwa sababu walikuwa wamepanga saa mbili ndio muda wa kuonana na kuongea, akajitahidi kufika kabla ya muda husika. Saa moja na nusu tayari alikuwa katika baa hiyo ambapo akaagiza pombe na kisha kuanza kunywa taratibu huku akimsubiria Halima.
Saa 2:17 usiku, Halima akaonekana kusimama pembeni mwa baa ile huku akiangalia huku na kule. Samuel akaiwasha simu yake na kisha kuuinua mkono wake ulioshika simu na mwanga kuelekea kule alipokuwa Halima, Halima alipouona mwanga huo, akaanza kusogea mahali pale. Samuel akasimama.
“Karibu Halima,” Samuel alimkaribisha Halima huku akimvutia kiti na kutulia.
“Asante. Samahani Paul, sina muda mrefu wa kukaa hapa,” Halima alimwambia Samuel.
“Usijali, sitochukua muda wako mrefu,” Samuel alimwambia Halima.
Hapo hapo bila kupoteza muda wowote ule Samuel akamuita mhudumu na kisha kumtaka kumsikiliza Halima alihitaji kinywaji gani. Mhudumu akafika mahali pale na kutakiwa kumsikiliza halima.
“Naomba Fanta,” Halima alimwambia mhudumu.
“Unakunywa soda? Acha utani Halima. Hebu agiza vinywaji vya watu wazima bwana. Toka lini mtu mzima akanywa soda,” Samuel alimwambia Halima huku akijichekesha.
“Naomba Kilimanjaro,” Halima alimwambia mhudumu huku akitoa tabasamu.
“Tunahitaji nyama ya kuchoma pia” Samuel alimwambia mhudumu yule ambaye aliondoka mahali hapo.
Wote wakabaki wakiangaliana mahali hapo, hakukuwa na mtu ambaye aliongea jambo lolote lile, macho yao yalionekana kama kutamaniana. Alichokifanya Samuel ni kuchukua chupa yake na kisha kupiga fundo moja na kukiweka vizuri kiti chake.
“Nashukuru kwa kuja,” Samuel alimwambia Halima.
“Usijali,” Halima alimwambia Samuel.

Huo ndio ukawa mwanzo wa mazungumzo yao, katika kipindi chote hicho walikuwa wakiongea mambo mengi. Halima hakuonekana kumfahamu Samuel japokuwa Samuel alikuwa akimfahamu Halima kutokana na kumuona mara kadhaa akiwa pamoja na Cosmas.

Ndani ya dakika kumi ya mazungumzo yao wakaonekana kuzoeana sana kana kwamba walikuwa wamefahamiana kwa zaidi ya mwaka mzima. Kila mmoja akajitahidi kuonyesha uchangamfu kwa mwenzake, kila mtu akajitahidi kumuonyeshea mwenzake kwamba alikuwa akijali sana ukaribu wao huo.

“Unaongea sana Paul,” Halima alimwambia Samuel
“Hahaha! Ila sikushindi wewe. Natumaini utakuja kuwa mwanasiasa baadae,” Samuel alimwambia halima.
“Hapana. Sipendi kuwa mwanasiasa.”
“Basi utakuwa mwandishi wa habar,i” Samuel alimwambia Halima na kisha wote kuanza kucheka.
Wakazidi kuongea zaidi, wakala na kunywa mahali hapo. Kwa kipindi fulani Halima akaonekana kujisahau kabisa, akasahau kwamba alikuwa na mpenzi wake.

Japokuwa alikuwa amemwambia Samuel kwamba wangetumia muda wa dakika ishirini tu kuongea lakini wakajikuta wakitumia muda zaidi na zaidi mahali hapo. Samuel hakutaka kuishia hapo, chupa ya pombe ya Halima ilipokuwa ikiishia, aliagiza nyingine na kuendelea kunywa. Waliendelea kuyafurahia maisha mpaka katika kipindi ambacho Halima akaonekana kutokujiweza, chupa kadhaa za pombe ambazo alikuwa amekunywa zikaonekana kumlewesha kupita kawaida.

“Umelewa?” Samuel alimuuliza Halima huku akimshika mkono.
“Sijalewa,” Halima alijibu huku akijifanya kuwa imara.
“Hahaha! Kama haujalewa basi tuendelee,” Samuel alimwambia Halima na kisha kuendelea kuhitaji pombe zaidi.

Katika kipindi chote hicho Samuel alionekana kuwa makini, alikuwa akiagiza pombe lakini hakuwa akinywa kama alivyokuwa akinywa siku nyingine. Taiming yake muda wote ilikuwa ni kumvizia halima alewe na kisha kufanya kile ambacho alikuwa akitaka kukifanya. Ilipofika saa tano usiku, Halima akaonekana kutokujiweza, mwili wake ukakosa nguvu kabisa. Alichokifanya Samuel ni kumchukua na kisha kuondoka nae mahali hapo huku akiwa amemshikilia kiuno. Akaita bajaji na kisha kuondoka katika eneo la baa hiyo huku Halima akionekana kutokujielewa kabisa.

“Wapi braza?” Dereva wa bajaji alimuuliza Samuel.
“La Vista Inn.”
“Ile ya Magomeni au Sinza?”
“Twende ya Magomeni,” Samuel alimwambia dereva wa bajaji.

Hapo hapo safari ya kuelekea katika hoteli hiyo ikaanza. Moyoni mwa Samuel alikuwa akijiona kuwa na uharaka mkubwa sana wa kukamilisha kile ambacho alikuwa amekipanga kwa wakati huo. Kitendo cha Cosmas kumtambia kila siku kwamba msichana wake, Halima alikuwa mwaminifu sana kilionekana kumkera kupita kawaida. Walichukua dakika kumi mpaka kufika katika hoteli hiyo ambapo Samuel akalipa fedha na kisha kukabidhiwa ufunguo wa chumba namba 23. Akaanza kuondoka na Halima kupanda ngazi mpaka kufika kwenye korido ambayo ilikuwa na chumba hicho.

Katika kipindi chote hicho Halima hakuwa akijitambua, kiasi kikubwa cha pombe ambacho alikuwa amekunywa kilionekana kumlewesha kupita kawaida. Walipofika chumbani, Samuel akamlaza Halima kitandani na kisha kuanza kumvua nguo moja baada ya nyingine huku Halima akiwa ametulia tu. Alimvua nguo zote mpaka kumuacha mtupu na ndipo nae akaanza kuvua nguo zake. Alipojiona amekuwa mtupu, akachukua simu yake ambayo ilikuwa na uwezo mkubwa wa kupiga picha na kisha kuanza kumpiga picha Halima.

Kwa kuwa hakuwa akijitambua kitandani pale, hata picha mfululizo ambazo alikuwa akipigwa huku akigeuzwa huku na kule hakuonekana kutambua chochote kile. Samuel hakuridhika, alichokifanya ni kumpigia simu Sadiki na kisha kumpa kile kilichokuwa kikiendelea chumbani pale.

“Umefikia wapi?”
“Hahaha! Chezea pombe wewe. Pombe sio chai kaka,” Samuel alimwambia Sadiki.
“Unanitia presha. Umefikia wapi?” Sauti ya Sadiki ilisikika simuni.
“Yupo hoi kitandani. Ngoja nikutumie picha zaidi ya themanini kupitia whatsApp,” Samuel alimwambia Sadiki na kisha kuanza kumtumia sadiki picha alizokuwa amempiga halima kitandani pale.

Siku hiyo hiyo ndio ilikuwa siku ambayo Samuel akafanya sana mapenzi na Halima kitandani pale huku bado akiwa amelewa kupita kawaida. Alijipiga picha mbalimbali huku akiwa kifuani mwa Halima. Japokuwa kitendo kile kilionekana kuwa kama udharirishaji kwa mwanamke lakini kwake yeye wala hakuonekana kulijali hilo, kitu ambacho alikuwa akikifanya mahali hapo kama kumuonyeshea Cosmas kwamba alikuwa na uwezo wa kulala na mwanamke yeyote ambaye alikuwa akimtaka bila wasiwasi wowote ule. Mara baada ya kufanya nae mapenzi zaidi ya dakika themanini, akalala pembeni ya Halima.

Asubuhi ilipofika, Samuel akaamka na kisha kuelekea bafuni. Akaagiza supu iletwe ndani ya chumba kile pamoja na chai, vyote vikaletwa. Baada ya muda fulani, Halima akaamka kutoka usingizini. Kitu cha kwanza, akaanza kushangaa mahali ambapo alipokuwa katika, akaanza kuangalia huku na kule, hakuonekana kupafahamu mahali hapo. Alipoangalia pembeni, macho yake yakatua usoni mwa Samuel. Hapo ndipo Halima alipoonekana kurudiwa na kumbukumbu. Hata kabla hajauliza kitu chochote kile, akajifunua shuka lake, alikuwa mtupu. Akashtuka kupita kawaida, hakutaka kubaki hapo, akauchukua mkono wake na kuuingiza sehemu zake za siri, akagundua kwamba alikuwa amefanya mapenzi jambo ambalo lilionekana kumshtua.

“Paul,” Halima aliita huku akionekana kubadilika.
“Naam mpenzi.”
“Tumefanya mapenzi?”
“Ndio mpenzi. Kuna tatizo?” Samuel alijibu na kisha kuinuka na kuanza kusogea kitandani pale.

Uso wa Halima tayari ukaanza kubadilika mahali pale, akaonekana kuanza kuingiwa na chuki moyoni mwake juu ya Samuel ambaye alionekana kutokuwa na wasiwasi hata kidogo. Hapo ndipo Halima alipoonekana kujutia hatua ambayo aliichukua ya kunywa pombe kupita kiasi katika kipindi ambacho alikutana na Samuel.

“Kwa nini tumefanya mapenzi? Kwa nini tumefanya mapenzi Paul?” Halima aliuliza huku akionekana kuwa na hasira.
“Kwa sababu ninakupenda Halima. Umekuwa msichana muhimu sana katika maisha yangu. Mara kwa mara nimekuwa mtu wa kukuhitaji sana. Nilikuwa radhi kupoteza muda mwingi kwa ajili yako Halima, nilikuwa naisubiria nafasi hii katika kipindi kirefu sana kilichopita:
“Leo imeonekana kuwa nafasi kubwa sana kwangu. Nakupenda Halima” Samuel alimwambia Halima huku tayari akiwa amekwishafika kitandani pale na kumkumbatia.

Maneno ambayo mara kwa mara Samuel alikuwa akiongea mahali hapo yalionekana kuwa faraja sana kwa Halima ambaye alikuwa akiyasikiliza. Kwake, tayari alimuona Samuel kuwa mtu ambaye alikuwa na mapenzi ya dhati, mtu ambaye alikuwa tayari kufanya kitu chochote kwa ajili yake katika maisha yake.

Japokuwa katika kipindi cha sekunde chache kilichopita alikuwa na hasira lakini akajikuta hasira zote zikianza kutoweka, maneno matamu ambayo alikuwa akizidi kuyaongea Samuel mahali hapo yalionekana kuipoteza hasira yote ambayo alikuwa nayo moyoni mwake dhidi yake.

“Sikufanya makusudi baby, nilikuwa nimevutiwa nawe toka kitambo. Jana usiku tulilewa sana, nikashindwa kuzizuia hisia zangu juu yako hasa mara baada ya kuuona uzuri wa umbo lako. Kama nimefanya makosa naomba unisamehe,” Samuel alimwambia Halima.

Japokuwa ilikuwa ni siku ya kwanza kwa Halima kulala na Samuel lakini akaonekana kuanza kumuamini mwanaume huyo. Hata jina lake halisi hakuwa akilifahamu lakini kwa sababu Samuel alikuwa mtu wa maneno mengi, akajikuta akikubaliana nae. Wakakumbatiana kitandani hapo huku Halima akiendelea kutokwa na machozi, kilichotokea, wakaanza kunyonyana ndimi zao na mwisho wa siku kuanza kufanya mapenzi kwa mara nyingine tena.

Kwa Samuel jambo lile likaonekana kuwa kama ushindi moyoni mwake. Kufanikiwa kufanya mapenzi na Halima mahali pale kilionekana kitendo cha ushindi ambacho alikuwa akikitaka sana kifanikiwe katika maisha yake. Lengo lake kubwa si kwamba alikuwa amevutiwa sana na Halima, hapana, lengo lake lilikuwa ni kutaka kumuumiza sana Cosmas kwa kumuonyeshea kwamba kama mwanaume haukutakiwa kumuamini sana mwanamke.

Kitendo kile kilichukua zaidi ya saa moja na ndipo wakanywa chai. Hawakutaka kutoka chumbani humo siku hiyo, walikuwa wakiongea mengi huku wakifanya mapenzi mara kwa mara. Kwa Samuel, hakutaka kuwa mkweli hata mara moja, kwa sauti ya unyenyekevu ambayo alikuwa akiitumia masikioni mwa Halima ilionekana kuuficha ubaya ambao alikuwa nao.

“Una mpenzi?” Lilikuwa swali ambalo lilitoka mdomoni mwa Samuel.
“Yeah! Ninaye,” Halima alijibu huku wote wakiwa watupu kitandani pale.
“Unampenda kama unavyonipenda?” Samuel alimuuliza.
“Sijui nijibu nini.”
“Kwa nini?”
“Sijui mpenzi.”
“Mpenzi wako anaitwa nani?” Samuel alimuuliza.
“Anaitwa Issa,” Halima alitoa jibu ambalo lilionekana kumshtua Samuel.
“Anaitwa nani?”
“Anaitwa Issa. Ninampenda sana na ninaamini nae ananipenda pia,” Halima alimwambia Samuel.
Hapo Samuel akaonekana kugundua kitu. Akagundua kwamba Halima hakuwa mwaminifu kwa Cosmas japokuwa Cosmas alikuwa akitamba sana kila siku. Halima hakuwa msichana mwenye mpenzi mmoja, hata Cosmas ambaye mara nyingi alikuwa akitamba kwamba alikuwa peke yake kumbe nae alikuwa ni mwanaume wa pembeni tu.
Samuel akaonekana kuwa na uhakika zaidi kwamba mwanamke hakutakiwa kuaminiwa hata mara moja. Kwa Halima, tayari alionekana kuwa mtu ambaye alimfanya kuwa na uhakika juu ya kile ambacho alikuwa akifikiria siku zote. Huo haukuwa mwisho wake, aliendelea kufanya mapenzi zaidi na zaidi.
“Na wewe una mpenzi?” Halima alimuuliza Samuel mara baada ya kufanya tena mapenzi.
“Sina. Demu wangu alikuwa pombe tu,” Samuel alimwambia Halima.
“Kwa nini hukutafuta msichana?”
“Basi tu. Unajua hapo kabla nilikuwa na msichana, aliniumiza sana na kuahidi kwamba nisingeweza kuwa na msichana tena. Kuanzia hapo, demu wangu akawa pombe, tukawa tunapenda, tunalala wote au wakati mwingine namuweka kwenye friji alale peke yake. Tunapenda mpaka sasa,” Samuel alimdanganya Halima uongo ambao ulimfanya kuanza kucheka.
“Nimekuelewa,” Halima alimwambia Samuel.
“Kwa hiyo inamaanisha kwamba kuanzia leo sisi ni wapenzi?” Samuel alimuuliza Halima.
“Wewe unaonaje?”
“Mbona unaniuliza kimitego sana. Unatakiwa kunijibu Halima,” Samuel alimwambia halima.
“Nadhani. Sisi ni wapenzi ila ni wapenzi wa siri. Nina mpenzi wangu, Issa, sitaki siku ajue kwamba nina mvulana mwingine,” Halima alimwambia Samuel ambaye akaonekana kuelewa.

Siku hiyo ndio ilikuwa siku ambayo Samuel akaanzisha uhusiano wa siri na Halima. Kila mmoja kwa kipindi hicho alimuahidi mwenzake kwamba angempenda siku zote. Kwa Samuel, maneno yote ambayo alikuwa akimwambia Halima wala hakuwa akimaanisha hata kidogo, alikuwa amedanganya sana.

Hakuwa na mapenzi yoyote kwa Halima, kitu ambacho alikuwa akikitaka kutoka kwa msichana huyo ni kufanya nae mapenzi na kisha kujipiga picha na mwisho wa siku kumuonyeshea Cosmas ambaye alikuwa akimuamini sana Halima.
Waliendelea kukaa ndani ya chumba kile mpaka ilipofika jioni muda ambao wakaagana kwa mapenzi motomoto huku wakipeana mabusu mfululizo na kisha kuondoka kila mtu kuelekea alipokuwa akiishi huku wakiahidiana kuendelea kuwasiliana zaidi.

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 09

“Nisikilize,” Samuel alimwambia Sadiki ambaye alikuwa akimsikiliza.
“Niambie ilikuwaje.”
“Yule demu anaabudu sana pombe.”
“Kwa hiyo ikawaje?”
“Nikamnywesha sana pombe mpaka akawa hajiwezi.”
“Duuh!”
“Yeah. Baada ya hapo nikampeleka katika hoteli yetu ile.”
“Ipi? La Vista Inn?”
“Kama kawa. Baada ya hapo, kilichoendelea ndio nikakituma kwa simu yako,” Samuel alimwambia Sadiki.
“Wewe noma kaka.”
“Ndio hivyo. Ninachokitafuta ni heshima tu. Nataka kifike kipindi watu tuanze kuheshimiana,” Samuel alimwambia Sadiki.
Muda wote Samuel alikuwa akijisifia kwa Sadiki mara baada ya kutoka kufanya mapenzi na Halima. Kwake, alijiona kuwa mshindi kwa kutekeleza kile ambacho alikuwa amekipanga kukitekeleza katika kipindi cha nyuma.
Kitendo cha Cosmas kujitamba kwao kwamba mpenzi wake alikuwa mwaminifu na asiyeyebabaika na vitu vidogovidogo kama wasichana ambao alikuwa akiwachukua Samuel ndicho kitu ambacho kilimfanya Samuel kutumia mwezi mzima kumtafuta Halima mpaka pale ambapo alifanikiwa kumpata na kufanya nae mapenzi huku ushahidi akiwa nao simuni.
“Ila kuna kitu kingine nimekijua,” Samuel alimwambia Sadiki.
“Kitu gani?”
“Demu ana jamaa yake mwingine anaitwa Issa,” Samuel alimwambua halima.
“Umejuaje?”
“Aliniambia.”
“Kwa hiyo hata Cosmas nae anachunwa tu?”
“Hiyo ndio maana yake.”
Wote wakabaki wakicheka. Kila mmoja alionekana kuwa na furaha kupita kawaida, kitendo cha Samuel kufanikisha kutembea na Halima kilionekana kumfurahisha kila mmoja mahali hapo. Walikuwa wakipiga strori wakicheka na kugongesheana mikono. Hata katika kipindi ambacho Cosmas aliingia ndani ya chumba kile, bado walikuwa wakicheka tu.
“Karibu mgeni,” Samuel alimkaribisha Cosmas huku akicheka jambo ambalo lilionekana kumkasirisha Cosmas.
“Kuwa na nidhamu basi Samuel. Wakati mwingine ujinga unakuwa sio ishu,” Cosmas alimwambia Samuel ambaye bado alikuwa akiendelea kucheka.
“Tatizo lake anapenda kuchukua wanawake wachafu huyu ndio maana anaonekana kuwa hana nidhamu,” Sadiki alimwambia Cosmas.

Katika kila kipindi ambacho walikuwa wakimwangalia Cosmas walikuwa wakicheka tu. Kitendo kile cha kutembea na Halima kiliwafanya kumdharau sana Cosmas kiasi ambacho walimuona kuwa si lolote lile. Thamani yake kwao ikashuka sana, wakamuona kama mtu mshamba ambaye alikuwa akimuwekea dhamana msichana kwa asilimia mia moja.
Hayo ndio yalikuwa maisha yao ya kila siku. Japokuwa wazazi wao walikuwa viongozi wa dini lakini wao walikuwa wakiishi maisha ya tofauti sana. Bado walikuwa wakilewa sana jambo ambalo liliwafanya hata wanachuo waliokuwa wakiishi katika hosteli hiyo kuwalalamikia sana na mwisho wa siku kuamua kuwafukuza katika hosteli hiyo.

Hawakubadilika hata kidogo, walichokifanya baada ya hapo ni kwenda kupanga chumba mitaani na kufanikiwa kupata chumba kilichokuwa mtaa wa Tandale Kwa Mtogole. Huko, maisha yao yakaonekana kubadilika zaidi, wakakutana na watu wengi ambao walikuwa wakitumia pombe, watu ambao walikuwa wakivuta bangi kwa wingi, nao wakaingia katika mfumo huo.

Maisha yao yakazidi kubadilika zaidi na zaidi, hawakutaka tena shule japokuwa kila siku wazazi wao walikuwa wakijitahidi sana kuwatumia fedha kwa kuamini kwamba watu hao walikuwa wakiendelea kusoma. Tabia zao wakaambukizana. Sadiki akamfundisha Samuel kutumia mirungi huku Samuel akimfundisha Sadiki namna ya kuwachukua wanawake mbalimbali mtaani.

Wote wakaanza kubadilisha wanawake. Kwa sababu walikuwa na fedha nyingi ambazo walikuwa wakitumiwa mara kwa mara na wazazi wao, wanawake wakaanza kuwababaikia na kisha kuanza kufanya nao mapenzi. Maisha kwao yakaonekana kuwa kitu kingine kabisa, hawakutaka kujithamini kabisa, walikuwa wakifanya vile ambavyo waliviona kustahili kuvifanya kwa wakati huo.

Huko Tandale ndipo ambapo wakampata mtu mmoja ambaye alikuja kuwa rafiki yao sana, huyu alikuwa Tenende. Tenende alikuwa mmoja wa vijana ambao walikuwa wakisifika sana katika mtaa wa Tandale kutokana na tabia chafu mbalimbali kama uporaji, uvutaji bangi pamoja na vitu vingine. Watu wengi waliokuwa wakiishi Tandale walikuwa wakimhofia Tenende ambaye maisha yake yalikuwa yakitawaliwa na uchafu mwingi.

Huyo ndiye ambaye alikuja kuwa rafiki yao wa karibu, Tenende ndiye ambaye walikuwa wakimtumia katika kuwanunulia bangi na kuwaonganisha kwa watu wengine ambao walikuwa watumiaji wazuri wa vilevi kama bangi na madawa ya kulevya. Japokuwa walikuwa wakivuta bangi na hata kutumia vilevi vingine lakini Samuel na Sadiki walikuwa wakionekana kuwa wasafi muda wote, walikuwa wakivaa vizuri huku wakijitunza kadri walivyoweza jambo ambalo lilikuwa liwavutia wasichana wengi kwao.

“Kuna UKIMWI,” Sadiki alimwambia Samuel.
“Nakumbuka. Kwani wewe ulishasahau hilo?”
“Hapana. Tunatakiwa kujikumbusha mara kwa mara kuhusiana na jambo hilo kwamba UKIMWI upo na unaua,” Sadiki alimwambia Samuel.
“Nafahamu. Siwezi kusahau hilo. Mtoto Joah vipi?” Samuel alimuuliza Sadiki.
“Yupo freshi. Jana mama yake alizingua lakini natumaini leo atakuja kama kawaida,” Sadiki alimwambia Samuel.
Kila kitu ambacho kilikuwa kimepita katika maisha yao ya nyuma kwa wakati huo kilikuwa kimesahaulika, Wakaonekana kusahau kwamba wazazi wao walikuwa wamewaandaa kwa kipindi kirefu sana na kuja kumtumikia Mungu kama ambavyo wao walivyofanya.

Anasa za dunia zikawateka, hawakukumbuka kitu chochote kwa wakati huo, kile ambacho walikuwa wakikikumbuka ni kuendelea kutumia vilevi kadri walivyoweza. Wazazi wao walikuwa wakiendelea kuwatumia fedha kwa kujua kwamba watoto wao walikuwa wakiendelea kwenda shule kama kawaida. Matendo ambayo walikuwa wakiyafanya hayakuwa yakitambulika na wazazi wao. Japokuwa hawakuwa wakiwaamini sana lakini kwa kitendo cha kuwaachia waende kupanga katika hosteli kilionekana kama kuwapoteza kabisa.

“Kuna bonge la mchongo,” Tenende aliwaambia katika kipindi ambacho aliwaletea bangi.
“Mchongo gani?”
“Khaled amerudi jana.”
“Khaled! Ndiye nani?”
“Jamaa ambaye anafanya kazi na mabosi wakubwa hapa Tanzania,” Tenende aliwaambia.
“Mabosi gani?”
“Kumbe mlikuwa hamjui! Kuna jamaa anaiwa Khaled, jamaa ana fedha chafu, yaani ana fedha mpaka anapagawa,” Tenende aliwaambia.
“Unazidi kutuchanganya. Ndiye nani huyo?” Sadiki aliuliza.
“Jamaa ambaye anachukua mizigo hapa anaipeleka huko bara la Asia,” Tenende aliwaambia.
“Bado unatuchanganya,” Samuel alimwambia Tenende.
“Dah! Naona kama hamnielewi. Ishu ipo hivi, jamaa anatengeneza sana fedha kwa kupeleka poda barani Asia. Alitaka nami nijiunge nae, nilipokwenda kwa wakubwa zake, wakanitoa nduki,” Tenende aliwaambia.
“Poda ndio nini?” Samuel alimuuliza Tenende.
“Poda ni madawa ya kulevya Samuel,” Sadiki alimwambia Samuel.
“Kwa hiyo Khaled amepata fedha kijingajinga. Hivi sasa anatengeneza sana fedha huwezi amini. Alipeleka mizigo kadhaa tu, nae sasa hivi kawa bosi,” Tenende aliwaambia huku akionekana kuwa na shauku ya watu hao kuingia katika uuzaji huo.
“Ok! Vizuri,” Sadiki alimwambia Tenende.
“Sasa nyie vipi? Hamtaki kupata fedha?” Tenende aliwauliza.
“Kwa njia hii ya uuzaji?”
“Yeah! Unatengeneza fedha sana.”
“Sasa kwa nini usingetengeza wewe?”
“Mabosi wake walinikataa.”
“Kwa nini walikukataa.”
“Eti ningekimbia na mizigo yao kwani waliniona kuwa mlevi sana,” Tenende aliwaambia.

Muda mwingi Tenende alikuwa akiongea kuhusiana na Khaled huku lengo lake likiwa ni kuwataka Sadiki na Samuel wakubaliane nae na hatimae waingie katika uuzaji wa madawa ya kulevya na kisha kujiingizia fedha kwa kuamini kwamba kama watu hao wangeingia na kupata fedha basi hata yeye pia angeweza kupata fedha.

Kutokana na Tenende kuongea sana kuhusiana na Khaled tena ikiwa mara kwa mara, hapo ndipo walipokubaliana kwamba kulikuwa na umuhimu wa kukutana na Khaled na kisha kuanza kuzungumza nae. Tayari maneno mengi ya Tenende pamoja na sifa ambazo alikuwa akizitoa kuhusiana na Khaled zilionekana kuwaingia vilivyo mioyoni mwao.
Hiyo ikaonekana kuwa furaha kwa Tenende, hakutarajia kama watu hao wangeweza kukubaliana nae na hatimae kutaka kuonana na Khaled ambaye alikuwa akisifika kwa fedha katika kipindi hicho. Walichokifanya ni kutaka kuonana nae kwa haraka sana kwani nao pia walikuwa wakitamani kuwa na fedha za kutosha kwa ajili ya kufanya mambo yao mengine ikiwa pamoja na kufungua biashara kubwa.

Hapo ndipo safari ya kuelekea Kijitonyama kuanza. Muda mwingi Tenende alikuwa akiongea kuhusiana na Khaled, kwake kwa wakati huo alikuwa akitumia muda mwingi kumlemba mtu huyo. Samuel na Sadiki wakawa na hamu ya kuonana na Khaled ambaye sifa zake zilikuwa zimemwagwa sana mdomoni mwa Tenende. Hawakuchukua muda mrefu sana, wakafika katika nyumba moja kubwa ya ghorofa ambayo ilikuwa na mlinzi nje na kisha kuanza kumuulizia Khaled.

“Yupo. Mna shida gani?” Mlinzi aliwauliza huku akiwaangalia kwa zamu.
“Tuna maongezi nae,” Tenende alijibu.
“Haiwezekani,” Mlinzi aliwaambia.
“Kwa nini bosi?”
“Hawa wengine wanaweza kuingia, ila wewe itakupasa ubaki hapa,” Mlinzi alimwambia tenende.
“Kwa nini mimi nibaki?”
“Muonekano wako. Unaonekana unaweza kuiba hata vijiko humu ndani,” Mlinzi aliwaambia huku akifungua geti na kuwaambia Samuel na Sadiki kuingia ndani.
“Sasa bro mimi ndio niliowaleta hao wana kuja kuonana mpwa wangu. Inakuwaje unanizuia?” Tenende alimuuliza mlinzi ambaye alikuwa akijiandaa kufunga geti.
“Hiyo ndio ilivyo kaka.”
“Ila mimi ndio mshika ramani. Hao watafikaje?” Tenende aliuliza.
“Bro, huyo ndiye mtu muhimu sana kwetu. Yeye ndiye alitumwa kutuita,” Samuel alimwambia mlinzi.
“Ila si mnaona jinsi alivyokuwa. Watu kama hawa hawahitajiki ndani ya nyumba hii,” Mlinzi aliwaambia Samuel na Sadiki

kuhusu Tenende ambaye alikuwa akionekana vibaya kutokana na bangi kumharibu na kumuweka katika hali ya uchafu.
Baada ya kuongea sana na mlinzi mahali hapo ndipo alipokubali kumruhusu Tenende kuingia ndani ya nyumba hiyo. Muonekano wake bado haukuwa mzuri kabisa. Mlinzi akawaambia wasubiri mahali hapo karibu na mlango wa kuingilia sebuleni na kisha yeye kuelekea ndani na kumpa taarifa Khaled kuhusiana na ugeni ambao ulikuwa umefika mahali hapo.

Mlinzi akarudi na kisha kuwakaribisha ndani mpaka sebuleni. Nyumba ilionekana kuwa na thamani sana katika macho yao. Ilionekana kuwa moja ya nyumba ya kisasa ambayo kweli alitakiwa kuishi mtu ambaye alikuwa na kiasi kikubwa cha fedha. Macho yao yalikuwa yakiashangaa tu mandhari ya nyumba ile, walikuwa hawaamini kama kungekuwa na binadamu ambaye angekuwa akiishi ndani ya nyumba ile ambayo ilionekana kuwa na mvuto mkubwa.
Wakatulia kwenye makochi makubwa. Macho yao hayakutulia hata kidogo, walikuwa wakiangalia huku na kule. Zuria kubwa la manyoya liliwafanya kujisikia vizuri kabisa miguuni mwao. Walitulia katika makochi yale sebuleni pale mpaka katika kipindi ambacho Khaled akafika sebuleni hapo.

Kitu cha kwanza akaanza kuwaangalia watu ambao walikuwa wamefika mahali hapo. Vijana wawili walionekana kuwa wageni wakubwa machoni mwake, ni Tenende tu ndiye ambaye alikuwa akimfahamu mahali hapo. Khaled hakuonekana kujali, alichokifanya ni kuwasalimia na kisha kukaa katika kochi jingine.
“Nimewaleta hawa,” Tenende alianzisha mazungumzo.
“Wakina nani?”
“Washikaji zangu pande za kitaa,” Tenende alimjibu Khaled.
“Ok! Umewaleta wa kazi gani?”
“Mambo yetu yale.”
“Mambo gani?”
“Yale ya kupaa paa na ndege.”
“Sijakuelewa Tenende.”
“Si yale ya unga wa sembe mkuu,” Tenende alimwambia Khaled ambaye hakuonekana kujisikia vizuri katika hilo.
“Ok! Nimekuelewa. Hebu njoo huku mara moja,” Khaled alimwambia Tenende na kisha kumtaka kumfuata kule alipokuwa ameelekea ukumbini.
“Mbona unaonekana kuwa kama mtoto wewe,” Khaled alimwambia Tenende huku akionekana kubadilika.
“Kivipi?”
“Sasa hawa ndio wakina nani?”
“Washikaji nao wanataka kufanya biashara ya madawa,” Tenende alimwambia Khaled.
“Huu ni upumbavu Tenende. Unajua unaweza kuwaita polisi na kuniletea matatizo.”
“Lakini bosi si.....”
“Hakuna cha lakini. Hili linaweza kuwa tatizo kwangu. Je wakiwa polisi unafikiri itakuwaje?”
“Hawa sio polisi. Ni wana ambao kila siku nipo nao kitaa tunafanya yetu.”
“Umeanza kufahamiana nao kipindi gani?”
“Huu mwezi wa tatu sasa.”
“Bado muda ni mfupi sana. Angalia Tenende na mambo yako naomba usiyafanyie mbele ya macho yangu. Umesikia?”
“Nimesikia bosi.”
“Na hata watu wako iwe mwanzo na mwisho kuwaleta watu nisiowajua ndani ya nyumba hii. Tumeelewana?”
“Tumeelewana.”
Khaled akaondoka mahali pale na kisha kuelekea sebuleni. Hakutaka kuongea kitu chochote kile, alichokifanya ni kuchukua chupa ya maji ambayo alikuwa ameiacha sebuleni pale na kisha kuondoka mahali hapo na kuelekea chumbani kwake. Samuel na Sadiki nao hawakuongea kitu chochote kile, walibaki wakimwangalia Khaled ambaye alikuwa akiondoka mahali hapo.
Huku akionekana kuchoka, Tenende akarudi na kisha kukaa kwenye kochi. Hakuonekana kuwa na furaha kana kwamba kulikuwa na kitu ambacho kilikuwa kimetokea kule ambapo aliitwa na Khaled.
“Vipi?” Samuel aliuliza.
“Amekaza.”
“Kivipi?”
“Twendeni tu,” Tenende aliwaambia huku akisimama.
Hakukuwa na mtu ambaye alibaki mahali hapo, tayari waliona kwamba kile kitu ambacho walikuwa wamekifuata mahali pale kikiwa kimeshindikana kabisa. Pamoja na hayo yote kila mmoja alitaka kufahamu ni kitu gani ambacho Khaled alikuwa ameongea na Tenende kule alipokuwa amemuita.
“Hebu tuambie amesemaje,” Sadiki alimwambia Tenende walipokuwa njiani wakirudi.
“Nimeongea nae.”
“Tunajua. Amesemaje?”
“Amezingua kinoma.”
“Kivipi?”
“Amesema nisiwalete watu tena ndani ya nyumba yake kwani anajua kwamba inawezekana ninyi mkawa polisi,” Tenende aliwaambia.
“Dah! Kwa hiyo ishu imebuma?” Samuel alimuuliza.
“Yeah!” Tenende alijibu.
Kila mmoja akaonekana kunyong’onyea mahali pale. Kitendo cha Khaled kukataa kufanya kazi pamoja nao kilionekana akuwakata maini kabisa. Wakawa wakirudi nyumbani lakini hawakuonekana kuwa na amani. Katika kipindi hicho, kila moja alikuwa na kiu ya kufanya biashara ile ambayo ilionekana kulipa kupita kawaida, kila mmoja katika kipindi hicho alikuwa na hamu ya kupata fedha nyingi katika kipindi kichache.
“Kwa hiyo ndio basi tena?” Sadiki aliuliza.
“Nadhani.”

Ile kwao ikaonekana kuwa bahati ambayo ilikuwa imefutika machoni mwao. Kitendo cha kuiona nyumba ambayo alikuwa akiishi Khaled pamoja na magari ambayo yalikuwa yameegeshwa katika eneo la nyumba yake tayari wakajua kwamba biashara ile ya kuuza madawa ya kulevya ilikuwa ikilipa sana. Kiu kubwa ya kufanya biashara ile ikawa imewashika lakini hawakujua ni kwa namna gani wangeweza kufanya biashara ile.

Kwa sababu Khaled hakuwa ameonekana kuwakubali, walipofika nyumbani maisha yao yakaendelea kama kawaida. Mara kwa mara walikuwa watu wa kuingiza wanawake ndani na kufanya nao mapenzi, maisha ya anasa yalizidi kuwatawala kila siku. Walikuwa wakinywa pombe na kuvuta bangi huku kila siku wakila mirungi kama kawa yao.
Samuel hakutaka kuachana na Halima, mara kwa mara msichana huyo alikuwa akija nyumbani hapo na kisha kufanya nae mapenzi kiasi ambacho kikafika kipindi akachoka kabisa, akahitaji kumuacha kwani kama angeendelea nae kila siku ingeweza kuwa tatizo hapo baadae.

“Kwa hiyo utamuacha vipi?” Sadiki alimuuliza.
“Kazi rahisi sana. Ni kama kumsukuma mlevi katika mteremko wa mlima,” Samuel alimwambia Sadiki.
“Kivipi sasa?”
“Ngoja nimtumie bwana wake zile picha.”
“Nani? Issa?”
“Hapana. Issa simjui. Nataka nimtumie Cosmas.”
“Unadhani hiyo itasaidia?”
“Sana tu. Asilimia mia moja,” Samuel alijibu.
Samuel hakutaka kuchelewa, alichokifanya siku hiyo ni kumtumia Cosmas picha kadhaa ambazo zilimuonyesha akifanya mapenzi na Halima. Samuel hakuonekana kujali kwamba Cosmas angejisikiaje katika kipindi hicho, kitu ambacho alikuwa akikijali zaidi ni yeye kuachana na Halima tu.

Picha zile zilionekana kumuumiza Cosmas kiasi ambacho kikamfanya kumtafuta Samuel na kisha kuonana nae Tandale. Ugomvi mkubwa ukatokea, Cosmas alionekana kuwa na hasira kupita kawaida, hakuonekana kuamini kama Samuel angeweza kufanya kitu kama kile hasa kwa msichana ambaye alikuwa akimpenda.
“Tatizo nini sasa? Demu wako malaya na nilikwambia usimwamini mwanamke. Umeona?” Samuel alimwambia Cosmas ambaye alikuwa ameshikwa na wanaume kadhaa kutokana na fujo ambazo alikuwa amezileta mahali hapo.
“Nitakuua,” Cosmas alisema kwa hasira.
“Sikiliza Cosmas. Demu wako mchafu sana na ndio maana nimeamua kuachana nae. Ulikuwa unatamba sana kwamba demu wako mwaminifu, ana uaminifu gani sasa, yaani nilimpata kirahisi sana kama kumsukuma mlevi kwenye mteremko,” Samuel alizidi kuongea maneno ambayo yalmfanya Cosmas kupata hasira zaidi.
“Nimesema nitakuua.”
“Unataka kumuua msela kisa demu? Wewe wa wapi?” Sadiki aliuliza huku akicheka kidhihaka.
“Achana nae bwana. Demu mwenyewe demu basiii, demu mwenyewe mchafu tu,” Samuel alimwambia Sadiki huku akiingia ndani.

Maneno yale yakaonekana kumtia hasira Cosmas ambaye alikuwa akitamani kuachiwa na watu ambao walikuwa wamemshika mahali hapo na kisha kumfuata Samuel ambaye aliingia chumbani pamoja na Sadiki. Watu ambao walikuwa wamemshika mahali hapo wakaanza kumpoza huku wakimwambia aondoke mahali hapo.

Idadi kubwa ya watu tayari ilikuwa imekusanyika mahali hapo huku kila mmoja akitamani kushuhudia watu hao wakipigana. Cosmas hakutaka kubaki mahali hapo, alichokifanya ni kuondoka huku akionekana kuwa na hasira kali moyoni mwake kwani kitendo cha Samuel kutembea na msichana wake, Halima kilionekana kumuumiza kupita kawaida.
Kidogo lile likaonekana kuwa suluhisho, mara baada ya siku kadhaa, Halima akafika nyumbani hapo na kisha kuamua kuachana na Samuel kwa madai ya kumdhalilisha. Hicho ndicho kitu ambacho alikuwa akikitaka sana Samuel, hakubisha wala kugoma, akamkubalia Halima kwamba huo ndio ulikuwa mwisho wa uhusiano wao wa siri.

Maisha hayakubadilika hata mara moja, bado yalikuwa yakiendelea kama kawaida. Kila siku walikuwa wakiendelea kuvuta bangi ambazo walikuwa wakimtuma Tenende kwenda kuzinunua kwa watu ambao walikuwa wakiziuza pamoja na mirungi ambayo ilikuwa ikiuzwa na watu wachache ambao walikuwa wakitoka Manzese kuja Tandale. Hakukuwa na mtu ambaye alikuwa akikumbuka ibada kwa wakati huo. Maisha yao yalionekana kubadilika kwa asilimia mia moja. Hawakutaka kwenda kanisani wala msikitini, hawakutaka kusoma Biblia wala Qur-an , kitu ambacho walikuwa wakikitaka katika muda huo ni kuendelea kuishi katika maisha yale kama kawaida.

Siku ziliendelea kukatika huku nazo wiki zikiendelea kusonga mbele mpaka katika kipindi ambacho Tenende akawaletea habari ambayo kwao ikaonekana kuwa njema kwamba Khaled alitaka kuwaona siku ya kesho. Kila mmoja hakuonekana kuamini, tayari waliona kwamba walikuwa wamepata nafasi ambayo walikuwa wakiitaka katika kipindi hicho, kitendo cha Khaled kutaka kuwaona tayari kikawapa uhakika kwamba wangeweza kuingizwa katika mtandao wa uuzaji wa madawa ya kulevya na hivyo nao kupata fedha kama ilivyokuwa kwa Khaled.

“Kitu kimetiki,” Samuel alimwambia Sadiki huku akionekana kuwa na furaha.
“Bado kwanza. Tutasema kimetiki mpaka tutakapokabidhiwa mzigo,” Sadiki alimwambia Samuel.
“Lakini si umeona mawingu! Au umezisahau dalili za mvua?” Samuel alimuuliza Sadiki.
“Najua. Ngoja kwanza mpaka tuanze kupeleka mzigo,” Sadiki alimwambia Samuel.
Siku iliyofuta, wakaanza kuelekea nyumbani kwa Khaled. Hawakutaka kuelekea huko pamoja na Tenende kutokana na kuambiwa kwamba walitakiwa kufika mahali hapo peke yao. Njiani, kila mmoja alionekana kuwa na furaha, tayari wakaanza kuona utajiri ukinukia katika maisha yao. Mara baada ya kufika getini, wakaruhusiwa kuingia.
“Ni kweli mnataka kufanya biashara hii?” Khaled aliwauliza huku akivuta sigara kubwa.
“Ndio.”
“Sidhani,” Khaled aliwambia.
“Kweli. Tunataka kuifanya biashara hii,” Samuel alimwambia Khaled.
“Kitu gani kimewavutia katika biashara hii ambayo inaonekana kuwa na majanga makubwa na ambayo polisi wanaitolea macho sana?” Khaled aliwauliza.
“Tumependezwa nayo kuifanya kwa sababu tumegundua nyuma yake kuna mafanikio makubwa,” Samuel alimjibu Khaled.
“Kwa hiyo mnaamini kwamba mtapata fedha na kuwa matajiri?” Khaled aliwauliza.
“Ndio.”
“Msipopata?”
“Tutaendelea kupigana nayo mpaka tupate,” Sadiki alitoa jibu lililowafanya wote kucheka.
“Nisikilizeni kwa makini. Biashara hii ni biashara ya hatari sana ambayo kila mtu anatamani sana kuifanya. Ukiwa serious katika biashara hii utaingiza fedha sana lakini ukiwa upo upo tu haueleweki, hautofanikiwa, mbaya zaidi utakamatwa na kufikishwa polisi,” Khaled aliwaambia.
“Kwa hiyo umakini ndio unaohitajika?”
“Hiyo ndio maana yangu. Ukiwa makini utapata kile unachokitaka lakini usipokuwa makini utaweza kuingizwa hata gerezani,” Khaled aliwaambia huku akinywa juisi.
“Tutakuwa makini,” Samuel alimwambia.
“Kila mmoja anapotaka kuanza kufanya biashara hii husema hivyo lakini mara anapoanza kuifanya, anasahau kile alichokisema kabla ya kuanza biashara hii” Khaled aliwaambia.
“Kuna kingine zaidi?” Samuel aliuliza.
“Ndio. Tamaa.”
“Kivipi?”
“Vijana wengi hukimbia na mizigo kwa kujiona kwamba watafanikiwa lakini mwisho wa siku tunawapata na kuwaua huku maiti zao tukisafirishia madawa hapa hapa Afrika,” Khaled aliwaambia.
“Tumekuelewa.”
“Sawa. Kuna mengi nitakuwa nikiwaambia kuhusiana na biashara hii kabla ya ninyi kuanza biasha hii chini yangu. Ninyi mtakuwa wafanyakazi wangu. Nyie ndio mtakuwa mkisafirisha mizigo kwenda mikoani na hata nchi nyingine hapa hapa Afrika,” Khaled aliwaambia.
“Hilo sio tatizo. Inawezekana tukafika mpaka Ulaya,” Sadiki aliuliza.
“Ulaya! Ulaya ni kama Kariako mara unapoanza kufanya biashara hii. Kote huko mtafika, ila kwa sababu bado hamjafahamu jinsi ya kuifanya biashara hii, tuanze hapa hapa Afrika, mkiwa makamanda wa kuaminika, mtaanza kwenda Ulaya. Ninawahakikishia, safari zenu kumi za kwenda Ulaya, msipotajirika, basi mtakuwa mmerogwa,” Khaled aliwaambia.
“Tutatajirika vipi na wakati sisi tutakuwa wafanyakazi wako?” Sadiki aliuliza.
“Mtanifanyia kazi kwa kipindi fulani ila katika wakati huo nanyi inawapasa kufahamu njia mbalimbali, msitegemee kunifanyia kazi milele. Nanyi pia mnaweza kutajirika na kisha sisi kwa sisi tukawa tunafanyiana biashara. Hamuoni kama hiyo ni hatua mojawapo ya maendeleo?”Khaled aliwauliza.
“Kweli.”
“Hiyo ndio inavyokuwa. Mimi nilikuwa na mfanyakazi fulani anajiita Zinja. Alinifanyia biashara hii kwa uaminifu mkubwa na baada ya miezi kadhaa akaanzisha biashara yake, ninafanya biashara pamoja na yeye, yaani tunauziana. Hivi ndivyo biashara inavyokuwa,” Khaled aliwaambia.
“Ok! Tumekuelewa.”
“Sawa. Cha mwisho sasa.”
“Kipi?”
“Siri. Hamtakiwi kuonyesha mabadiliko yoyote mitaani. Kuweni wasiri sana kwa watu wote hasa hasa wanawake,” Khaled aliwaambia.
“Hasa wanawake,” Sadiki alisema huku akicheka.
“Yeah! Najua udhaifu wa vijana. Sketi zinatufanya kutokuwa wasiri sana na ndio maana hata polisi huwatumia wanawake. Kuweni makini katika hilo. Nadhani mwezi ujao tutaanza kazi,” Khaled aliwaambia.
“Hakuna tatizo.”
“Ila yawapasa kufika mahali hapa mara kwa mara kwa ajili ya kuweka ukaribu sana kati yangu na nyie,” Khaled aliwaambia.
“Hakuna tatizo.”
“Basi sawa,” Khaled aliwambia.

Hawakutaka kuendelea kubaki mahali hapo, walichokifanya ni kuondoka huku kila mmoja akionekana kuwa na furaha. Tayari wakayaona maisha yao yakianza kubadilika na kuwa vile ambavyo walitaka yawe. Kila wakati walikuwa wakicheka kwa furaha, tayari wakajiona kuwa matajiri hata kabla biashara ambayo waliambiwa kwamba waifanye hawajaaza kuifanya.

Katika kipindi hicho, hakukuwa na mtu ambaye alikuwa akijua kwamba bado shetani alikuwa akiendelea kuwateka na kuwapoteza zaidi na zaidi, hakutaka kabisa vijana hao wakumbuke kule walipotoka, nguvu zake nyingi katika kipindi hicho alikuwa ameziweka kwa vijana hao ambao alikuwa na kiu kubwa ya kutaka kuendelea kupoteza zaidi na zaidi.

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 10

Khaled alikuwa miongoni mwa watu waliokuwa wakifanya biashara ya magendo ya madawa ya kulevya nchini Tanzania. Hata kabla hajapata nafasi ya kufanya biashara zake yeye kama yeye, Khaled alikuwa akifanya biashara chini ya muuzaji mkubwa wa madawa ya kulevya, mzee Othman ambaye alikuwa akipenda kujiita kwa jina la Zungu kutokana na weupe wake aliokuwa nao.

Kazi kubwa ya Khaled ilikuwa ni kusafirisha madawa kuelekea katika nchi mbalimbali duniani. Hata kabla hajaanza kuyasafirisha madawa katika nchi za Ulaya na Asia, Khaled akaanza na kuyasafirisha madawa hayo ndani ya nchi ya Tanzania pamoja na nchi kadhaa katika bara la Afrika.Khaled akafahamiana na watu wengi, yeye ndiye ambaye alikuwa akiongea na madaktari na kisha kuwalipa kiasi fulani cha fedha na kuwapa maiti ambazo walikuwa wakizipasua tumboni na kisha kuziwekea madawa ya kulevya na kuanza kuyasafirisha katika nchi nyingi hapa Afrika. Katika kipindi hicho cha zamani, polisi hawakuweza kugundua kitu chochote kile, kila maiti ambayo ilikuwa ikisafirishwa ilionekana kuwa maiti ambayo wala haikuwa na matatizo kabisa.

Baada ya kuweka mizizi mikubwa barani Afrika hapo ndipo ambapo alipoanza kutumwa kuelekea katika nchi mbalimbali Ulaya na barani Asia. Uwezo wake wa kusafirisha madawa ulikuwa mkubwa sana na ilikuwa ngumu kugundulika. Katika kipindi hicho kila kitu kilionekana kuwa chepesi, hakukuwa na ulinzi mkubwa sana jambo ambalo lilimfanya Khaled kutokupata tatizo lolote lile.

Malipo makubwa yalikuwa yakifanyika huku yeye akilipwa fedha kidogo mno. Malipo hayo madogo ndio yakaonekana kumkasirisha Khaled. Kwanza alijiona anayahatarisha maisha yake kwa ajili ya mtu mwingine halafu anapewa kiasi kidogo, hapo ndipo alipoamua kuiba baadhi ya madawa na kisha kuyauza yeye mwenyewe.
Mzee Othman hakuweza kugundua kama Khaled alikuwa akiiba baadhi ya pakti za madawa na kisha kuuza kwa manufaa yake mwenyewe. Mpaka katika kipindi ambacho mzee Othman anakuja kugundua, tayari Khaled alikuwa amekwishachuma fedha za kutosha.

“Nitamuua,” alijisemea mzee Othman kwa hasira. Kwa sababu Khaled alikuwa amekwishaacha kufanya kazi kwake huku akiwa amechukua fedha nyingi kupitia biashara ile hapo ndipo mzee Othman alipotaka kumuua Khaled.
Kila siku alikuwa akiwatuma vijana wake kwa ajili ya kukamilisha kila kitu alichotaka kikamilishwe lakini mwisho wa siku vijana wale wakashindwa kutekeleza kile ambacho walikuwa wameagizwa.
“Mmeshindwa wapi?” mzee Othman aliwauliza huku akionekana kuwa na hasira.
“Kila tunapokwenda tunamkosa bosi. Yaani ni kama ana hirizi,” kijana mmoja alimwambia mzee Othman.
“Yaani nashindwa kuelewa mnashindwa sehemu gani. Mbona kazi inaonekana rahisi sana.”
“Huwa anatupotea sana. Sijui inakuwaje.”
“Ninawapeni wiki moja tu nataka mtu huyu auawe,” mzee Othaman aliwaambia.
Bado akili ya mzee Othman ilikuwa imechanganyikiwa. Hakutaka kabisa kumuona Khaled akiendelea kuvuta pumzi ya dunia hii na wakati alikuwa amemfanyia mambo mengi ya wizi wa madawa yake. Katika kipindi hicho alikuwa akihitaji kukiona kitu kimoja tu, kumuona Khaled anauawa na vijana wake.
Siku ziliendelea kukatika lakini wala hakukuwa na taarifa yoyote ile kutoka kwa vijana wake kuusiana na kifo cha Khaled. Huku ikiwa imebakia siku moja kabla ya kutimiza wiki ambayo alikuwa amewapa vijana wake, akajikuta akivamiwa ndani ya nyumba yake na watu kadhaa, aliwaangalia, mmoja alikuwa Khaled.
“Khaled,” mzee Othman aliita huku akionekana kutokuamini.
“Kwa sababu umeshindwa kuniua, nakukuua wewe,” Khaled alimwambia mzee Othman.

Siku hiyo ndio ilikuwa siku ya mwisho ya mzee Othman kuvuta pumzi ya dunia hii, akauawa ndani ya nyumba yake na kisha vijana wale akiwepo Khaled kuchukua kiasi kikubwa cha fedha ambacho alikuwa amekificha na kisha kuondoka mahali hapo. Kuanzia hapo, Khaled akaanza kufanya biashara kwa amani na ndani ya mwezi mmoja tu tayari alikuwa amepata kiasi kikubwa cha fedha. Khaled hakuishia hapo, akaanza kutafuta vijana zaidi wa kumfanyia kazi ya kusafirisha madawa katika nchi mbalimbali. Zoezi lake lilikuwa gumu kwani kila kijana ambaye alikuwa akimpata alikuwa akikamatwa kirahisi na polisi na mizigo yake kupotea kizembe.

Khaled hakujua ni kitu gani kilikuwa kikiendelea, hakujua sababu ambayo iliwafanya vijana wake kukamatwa kizembe namna ile. Alipokaa kwa muda huku akiwa hajui ni kitu gani kilikuwa kikitokea hapo ndipo alipopata jibu ambalo alikuwa na uhakika nalo kwamba ndilo lililosababisha vijana wake wengi kukamatwa kirahisi. Vijana ambao alikuwa akiwatumia, asilimia kubwa walikuwa watumiaji wa madawa ya kulevya kiasi ambacho katika sehemu za kukagulia uwanja wa ndege walikuwa wakikamatwa kirahisi sana. Hiyo ndio ilikuwa sababu kubwa ya Khaled kuachana na vijana hao na kisha kuanza kuwatafuta vijana ambao wala hawakuwa wakitumia madawa ya kulevya.

Kuwapata vijana wa namna hiyo halikuwa jambo jepesi hata mara moja, kila siku alikuwa akihangaika lakini mwisho wa siku hakuwa akimpata mtu yeyote yule. Hakukata tamaa, kila siku alikuwa mtu wa uvumilivu. Alipoona siku zinasogea bila kuwapata vijana hao ndipo akaamua kuwasiliana na Tenende kwa kuamini kwamba mitaani kulikuwa na vijana ambao wangeweza kuyatoa maisha yao kwa ajili ya kufanya kazi hiyo.

Kitu cha kwanza Tenende akataka kufanya kazi hiyo yeye kama yeye lakini Khaled hakuonekana kukubali, kwa Tenende, alionekana kuwa kama vijana wengine ambao walikuwa wakikamatwa kirahisi sana katika viwanja vya ndege. Alihitaji vijana wengine ambao wangeonekana kuwa wasafi na ambao hawajawahi kutumia madawa ya kulevya. Baada ya wiki kadhaa ndipo Tenende akawaleta Sadiki na Samuel ndani ya nyumba yake. Hali ile haikuonekana kumfurahisha kwani alitaka kuonana na vijana hao nje ya nyumba yake kwa sababu ya usalama zaidi. Japokuwa alimkoromea sana Tenende lakini mwisho wa siku alipowaangalia Samuel na Sadiki kwake wakaonekana kufaa sana katika kuifanya biashara ile ambayo kwa kiasi fulani ilikuwa imekwishaanza kuzorota.

“Ninawahitaji. Waambie waje lakini waje peke yao,” Khaled alimwambia Tenende katika kipindi ambacho alikwenda Tandale.
“Unataka kuwaona lini?” Tenende alimuuliza.
“Hata kesho mchana itakuwa poa sana,” Khaled alijibu huku wote wawili wakiwa ndani ya gari lake.
“Hakuna noma. Tutakuja muda huo.”
“Hapana. Waambie waje peke yao.”
“Unamaanisha mimi nisije?”
“Ndio. Ninawahitaji wao peke yao.”
“Ila bosi unanitenga kweli siku hizi.”
“Hakuna tatizo Tenende. Wewe ni mtu wangu wa karibu. Kwanza chukua hii,” Khaled alimwambia Tenende huku akiwa amefungua pochi yake na kumkabidhi kiasi cha shilingi elfu hamsini.
“Shwari. Nitawaambia waje,” Tenende alisema na kisha Khaled kuondoka mahali hapo.
*****
Samuel na Sadiki tayari walikwishajiingiza katika biashara ya uuzaji wa madawa ya kulevya huku wakiwa chini ya Khaled ambaye alikuwa bosi wao. Kitu ambacho kilifanyika kwa wakati huo kilikuwa ni kuanza kupewa ramani pamoja na kila njia ambayo biashara ilitakiwa kufanyika Katika kipindi hicho kila mtu alikuwa na ndoto za kuwa milionea, kila mtu alikuwa akitaka kumiliki kiasi kikubwa cha fedha. Kujiingiza na kuwa miongoni mwa wafanyakazi wa Khaled kwao wala halikuonekana kuwa tatizo hata mara moja, kitu ambacho walikuwa wakikihangalia kwa wakati huo ni fedha tu.

Alichokifanya Khaled ni kuanza kuwatafutia passport. Kitu ambacho alikijua ni kwamba kama angekamilisha suala zima la passport ingekuwa rahisi sana kwao kuanza kusafiri kuelekea katika nchi mbalimbali kwa ajili ya kupeleka madawa hayo ambayo katika kipindi hicho yalikuwa yakiuzwa sana huku njia kali za kukamata wasafirishaji zikiwa bado hazijaboreshwa duniani. Kila kitu kilipokuwa tayari, baada ya mwezi mmoja Khaled akawapa mzigo wa kilo moja kwa ajili ya kuusafirsha mkoani Arusha uliokuwa ukihitajika kupita kawaida. Kwa sababu walikuwa marafiki ambao walikuwa wamezoeana sana hata zaidi ya ndugu, wakaanza kuelekea huko Arusha huku wakiwa na gari aina ya Prado ambayo ilikuwa ikimilikiwa na Khaled.

“Kazi imeanza,” Sadiki alimwambia Samuel.
“Yeah! Kinachohitajika ni uvumilivu tu katika kazi hii na mafanikio yatajileta,” Samuel alimwambia Sadiki ambaye alikuwa akiendesha gari.
“Alisema tuchukue kiasi gani?”
“Milioni mbili kama mzigo utafika salama. Yaani kitendo cha kutoka Dar es Salaam kuja Arusha tayari tuna milioni moja kila mmoja. Hauoni kama huu ni utajiri unatunyemelea?” Sadiki aliuliza huku akiendelea kuendesha gari.
“Huu ni utajiri dhahiri. Umri mdogo unaanza kukamata mamilioni, mitaani watanitafuta ubaya,” Samuel alimwambia Sadiki.
“Hahaha! Bila shaka unamaanisha sketi.”
“Hiyo ndio maana yangu. Ili uonekane una fedha, haina budi kulala na wakina Salome, Christina na mademu wote wakali,” Samuel alimwambia Sadiki.

Bado safari ilikuwa ikiendelea kama kawaida, kila mtu katika kipindi hicho alikuwa akifikiria fedha. Kiasi cha shilingi milioni moja kwa kila mmoja ambacho walikuwa wamepewa kama malipo ya kupeleka mzigo wa madawa ya kulevya Arusha kilikuwa kiasi kikubwa katika maisha yao kutokana na umri wao kuwa mdogo. Katika safari nzima, kila askari wa barabarani ambaye alikuwa akiwasimamisha walikuwa wakimpa fedha, hawakutaka gari lao lipekuliwe kabisa, walitaka kusafiri kwa amani mpaka wanaingia mkoani Arusha.
“Nimewaambia wote teremkeni garini?” ilisikika sauti ya polisi mmoja wa barabarani akiwaambia huku akionekana kumaanisha alichokuwa akikiongea.

“Ila bosi naomba utuelewe, tunawahi msibani,” Samuel alimwambia askari yule ambaye hakuonekana kuelewa kabisa.
Maaskari wa barabarani wengine ambao walikuwa pembeni ya barabara wakaanza kusogea kule gari alilokuwa Samuel na Sadiki lilipokuwa. Tayari waliona kwamba kulikuwa na kitu ambacho kilikuwa kikiendelea mahali hapo. Askari yule wa barabarani alikuwa akiendelea kusisitiza kwamba Samuel na Sadiki wateremke kutoka garini lakini wao hawakuonekana kuelewa kabisa.

“Kuna nini tena?” askari mmoja ambaye alionekana kuwa kiongozi aliuliza mara baada ya kufika mahali pale.
“Hili gari nina wasiwasi nalo. Nadhani watakuwa wamebeba mirungi hawa,” askari yule alimjibu bosi wake ambaye alifika hapo na kisha kuanza kuwaangalia Samuel na Sadiki ambao walikuwa ndani ya gari lile.
“Hamjambo!” askari yule kiongozi aliwasalimia.
“Hatujambo. Shikamoo,” wote walimsalimia.
“Mmebeba nini garini?” askari yule aliuliza kwa sauti ya upole.
“Hakuna kitu. Tunaelekea katika msiba wa mjomba wetu Marangu Kilimanjaro,” Samuel alijibu huku akimkazia macho askari yule.

“Hamjabeba mirungi nyie?”
“Hapana mzee. Hebu tuangalie kwa macho yako mzee, hivi tunaonekana sisi ni watumiaji wa mirungi?” Samuel alimuuliza askari yule.
“Sasa kwa nini mnashindwa kumuelewa anaposema kwamba mteremke kutoka garini?”
“Kumuelewa tumemuelewa ila tulitaka kuongea nae kiutu uzima. Unajua vitu vingine inabidi tuongee kiutu uzima ili tusimcheleweshe na majukumu yake na hata sisi tusichelewe kuwahi msibani,” Samuel alimwambia askari yule.
“Hebu njoo huku tuongee kidogo. Wewe kijana unaonekana kuwa muelewa,” askari yule alimwambia Samuel ambaye akateremka na kisha kumfuata.
Mpaka kufikia hatua hiyo tayari wakajiona kwamba kusingekuwa na kitu chochote ambacho kingeharibika mahali hapo. Kitendo cha askari yule kumuita Samuel pembeni kilionekana kwamba kuwa ushindi kwao. Samuel na askari yule wakaelekea pembeni kabisa ya barabara na kisha kuanza kuongea.
“Mlisema mnaelekea wapi?” askari yule alimuuliza.
“Tunaelekea Marangu Kilimanjaro kwenye msiba,” Samuel alijibu.
“Nani amefariki?”
“Mjomba wetu.”
“Sasa mbona mlikuwa mkimbishia kijana wangu kuteremka kutoka garini?”
“Tatizo muda bosi. Unajua kuna vitu vingine inabidi tumalizane kimyakimya,” Samuel alimwambia askari yule.
“Sasa kwa nini mmebeba mirungi?”
“Hatujabeba mirungi bosi. Hivi kwa kutuangalia jinsi tulivyo nadhifu tunaweza kuwa wala mirungi kweli?”
“Ok! Naona tunapoteza muda wa bure. Tumalizane basi ili muwahi,” Askari yule alimwambia Samuel.
Samuel hakutaka kuremba, aliiona ile ndio kuwa nafasi yenyewe, alichokifanya ni kuuingiza mkono mfukoni na kisha kutoa noti mbili za shilingi elfu kumi na kisha kumgawia. Kwa kasi ya ajabu askari yule akazichukua noti zile na kisha kuziweka mfukoni.
“Nendeni ila kuweni makini barabarani,” askari yule aliwaambia.
Samuel hakutaka kuchelewa, kitu alichokifanya ni kuondoka mahali hapo na kisha kuingia garini na kisha safari ikiendelea. Kila wakati walikuwa wakicheka tu, fedha ambazo alikuwa amempa askari yule kilikuwa kiasi kikubwa cha fedha, fedha ambazo kwa askari yeyote katika kipindi kile asingeweza kuziacha.
“Fedha ni shetani,” Sadiki alimwambia samuel.
“Tena shetani baba lao aisee.”

Safari iliendelea zaidi na zaidi. Mpaka wanaingia Arusha saa tisa alasiri kila mmoja alionekana kuchoka. Walichokifanya ni kwenda kwenye moja ya hoteli na kisha kula chakula, walipomaliza, wakaondoka na kuelekea mjini. Huko, ndani ya hoteli ya Jumanji ndipo walipokutana na bwana Pawasa ambaye alikuwa ameagiza mzigo huo.
Malipo yakafanyika katika benki ya CRDB, kiasi cha fedha cha zaidi ya milioni mia moja na hamsini kikaingizwa ndani ya kaunti ya Khaled na kisha Samuel na Sadiki kuondoka mahali hapo huku mzee Pawasa akimgawia kila mmoja kiasi cha shilingi laki tano.

“Haya ndio maisha tuliyokuwa tukiyataka,” Sadiki alimwambia Samuel.
“Ukiwa na uhakika wa kuingiza kiasi cha fedha namna hii, kuna nini tena? Unataka Mungu akupe nini tena?” Samuel alimwambia Sadiki
“Hakuna cha zaidi. Ila bado nina majonzi” Sadiki alisema huku uso wake ukipoteza tabasamu ghafla.
“Majonzi gani tena?” Samuel aliuliza.
“Unajua kama tunayahatarisha maisha yetu?”
“Najua.”
“Unajua kwamba tunamchezea rais Benjamin Mkapa sharubu?”
“Najua.”
“Hivi kama mtu anaingiza zaidi ya milioni mia moja na hamsini, kweli sisi ni wa kutulipa milioni moja kila mmoja! Hivi kuna uwiano hapo?” Sadiki aliuliza.
“Mmmh! Hilo uliloongea nalo neno. Hakuna uwiano.”
“Kwa hiyo jamaa anaingiza sana fedha halafu sisi tunaoyaatarisha maisha yetu tunapata kiasi kidogo. Hapana. Ni lazima tufanye kitu,” Sadiki alimwambia Samuel.
“Kitu gani?”
“Unaonaje kama tukampindua?”
“Kwa sasa hivi, hilo ni wazo baya sana.”
“Wazo baya! Kivipi?”
“Kumpindua ngumu kwa sababu hatujajua njia ya kuuzia madawa Ulaya. Kwanza acha tujue njia za huko kisha tunampindua. Au unaonaje?”
“Sawa. Hakuna tatizo. Ila kitu hiki kimeniuma sana.”
“Usijali. Tuendelee kuwa wafanyakazi. Tutakapokamilisha kila kitu, tunampindua na kisha sisi kushika uongozi wa biashara hii. Unaonaje hapo?”
“Hakuna tatizo.”

Tayari katika kipindi hicho mioyo yao ikaanza kuingiwa na tamaa ya kuhitaji fedha nyingi. Walikwishaona kwamba biashara ile ilikuwa inalipa kupita kawaida na hivyo waliona lingekuwa jambo jema kama biashara ile wangeifanya wao wenyewe. Kitu ambacho walishauriana, ilikuwa ni lazima wampindue Khaled na kisha wao kushikilia uongozi wa biashara ile.

Hakukuwa na mtu ambaye alijali kama wangeweza kumwaga damu mpaka kumpindua, kitu ambacho wao walikiona kufaa kwa wakati huo ni kumpindua tu Khaled na kisha wao kuwa viongozi wa biashara ile. Hawakuishia hapo, bado Khaled alikuwa akiwatuma katika sehemu mbalimbali nchini Tanzania kwa ajili ya kusafirisha madawa ya kulevya huku akijiingizia kiasi kikubwa cha fedha huku wao wakiingiza kiasi kidogo sana cha fedha.
Kila siku jambo lile lilikuwa likiwaumiza sana mioyo yao, hawakuamini kama kweli Khaled asingeweza kuwaongezea kiasi kikubwa zaidi kwa sababu walikuwa wakiyahatarisha maisha yao.

Wakavumilia kila siku, tayari wateja wakubwa wa madawa ya kulevya nchini Tanzania walikuwa wamekwishawajua, kwa sasa walikuwa wakitaka kuwafahamu wateja na mabosi kutoka katika nchi za Ulaya, hasa katika bara la Asia ili baada ya hapo, basi waweze kumuua Khaled na kuchukua uongozi wa kuuza madawa ya kulevya.

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 11

Mara baada ya kumaliza kidato cha nne katika shule ya Uhuru mkoani Kilimanjaro, msichana Catherine Mushi akarudi nyumbani kwa ajili ya kusubiria matokeo yake ya kidato cha nne. Siku zote katika maisha yake ya nyumbani, Catherine alikuwa mtu wa kuendelea kuwa karibu na Samuel ambaye alionekana kuwa na mapenzi ya dhati kwake.

Ukaribu wao wa kimapenzi ambao walikuwa nao nyumbani ulikuwa ukiendelea kama kawaida jambo ambalo kwao likaonekana kuwafurahisha na kuyakomaza mapenzi yao hayo ambayo katika kipindi hicho yalionekana kuwa juu sana. Katika maisha yake, Catherine hakujutia kitendo chake cha kuwa na Samuel, kwake alionekana kuwa mwanaume bora ambaye angeweza kumhitaji katika kipindi chote cha maisha yake.

Mara kwa mara alikuwa akionana na Samuel huku wakati mwingine wakiongea simuni kama kawaida yao. Hakutaka kupiga hatua za kurudi nyuma, kila siku walikuwa wakitaka kupiga hatua kwenda mbele zaidi katika mahusiano yao ambayo yalionekana kukua kila siku. Katika kichwa cha Catherine bado kulikuwa na kitu ambacho kilikuwa kikimsumbua sana kwa wakati huo, matokeo ya kidato cha nne.

Japokuwa alikuwa huru na mwanaume ambaye alikuwa akimpenda sana lakini bado Catherine hakuonekana kuwa na amani. Matokeo ambayo yalitarajiwa kutoka baada ya miezi kadhaa yalionekana kumsumbua sana kichwa chake. Hakuwa amesoma vya kutosha, maisha ya kutoroka usiku na kwenda katika kumbi za starehe ndio maisha ambayo alikuwa ameishi sana shuleni Uhuru mkoani Kilimanjaro.

Baada ya miezi kukatika na hatima matokeo kutoka, kile ambacho kila siku alikuwa akikitarajia ndicho ambacho kilikuwa kimetokea. Kama ilivyokuwa kwa wenzake watatu, Samuel, Sadiki na Mariamu ndio ambayo ilikuwa imemtokea hata yeye mwenyewe, alikuwa amefeli vibaya. Hilo likaonekana kuwa pigo la kwanza katika maisha yake, lilikuwa ni pigo kubwa na baya ambalo halikuweza kubebeka kwa urahisi moyoni mwake.

Hapo ndipo maisha ya majuto yalipoanza kumkumba. Mara kwa mara alikuwa akijutia aina ya maisha ambayo alikuwa akiishi shuleni kule katika kipindi cha nyuma. Maisha ya anasa ambayo alikuwa akiishi na wenzake ndio ambayo yalikuwa yamemletea matokeo yale ambayo yalionekana kumkasirisha kila mtu nyumbani kwao.
“Yaani mimi napoteza fedha zangu halafu mtoto anakwenda kufanya umalaya tu” Mzee Mushi alimwambia Catherine huku akionekana kuwa na hasira.

“Msamehe, bado anahitaji nafasi zaidi ya kuyarekebisha mambo yake” Mama yake, Bi Maria alimwambia mumewe, mzee Mushi ambaye katika kipindi hicho alionekana kuwa mkali hata zaidi ya mbogo aliyejeruhiwa.
“Wewe ndiye utalifanya hili kichwa kuwa nyanya. Leo hii ametuletea sifuri humu ndani, huyu si ataweza kutuletea hata UKIMWI ndani ya nyumba hii” Mzee Mushi alimwambia kewe, Bi Maria.

“Bado tumpe nafasi” Bi Maria alimwambia mumewe.
“Nafasi. Wewe unafikiri huyu tukimpa nafasi atabadilika, hivi unafikiri hili likichwa likipewa nafasi litabadilika?” Mzee Mushi alimuuliza mke wake huku akiendelea kuwa na hasira.
“Naomba unisamehe baba. Nitabadilika” Catherine alimwambia baba yake.

Kama kumchapa alikuwa amekwishamchapa vya kutosha na katika kipindi hicho fimbo hazikuonekana kubadilisha kitu chochote kile. Kwa sababu mke wake alikuwa akimtetea sana juu ya kile ambacho kilikuwa kimetokea, mzee Mushi hakuwa na jinsi zaidi ya kukubali kumpa nafasi binti yake kwa kuamini kwamba angeweza kubadilika na hatimae kufanya vizuri.

“Nafasi ya mwisho kwako kuingia darasani. Ukishindwa bora uolewe tu” Mzee Mushi alimwambia Catherine.
“Nitajitahidi baba” Catherine alimwambia baba yake.

Baada ya mwezi mmoja Catherine akaanza masomo katika shule ya Mbezi Beach huku lengo lake likiwa ni kuyarudia masomo ambayo alikuwa ameyasoma na mwisho wa siku kurudia mitihani yake. Katika kipindi chote hicho cha kurudia masomo yake Catherine alionekana kuwa makini katika masomo yake, hakutaka kurudia makosa ambayo alikuwa ameyafanya ambayo yalimpelekea kufanya vibaya katika masomo yake.

Kazi ya kusoma kwake ilikuwa imeongezeka zaidi na alitakiwa kupigana nayo vilivyo. Katika upande mmoja alikuwa akiyasomea masomo ambayo alikuwa amefeli lakini kwa upande mwingine alikuwa akiendelea na masomo ya kidato cha tano ili endapo kama atakuja kufaulu mitihani yake basi aweze kuingia moja kwa moja kidato cha sita. Katika kipindi hicho hakutaka kuwasiliana na Samuel, aliona kwamba endapo angewasiliana na mwanaume huyo basi hali ile ya kutokusoma ingeweza kujirudia tena na hivyo kufanya vibaya katika masomo yake. Kichwa chake alikuwa amekituliza katika kusoma, hakutaka kuyapa nafasi maisha ya anasa tena, ndani ya moyo wake alikuwa ameamua kwa asilimia mia moja kwamba alikuwa akitaka kusoma tu.

Ubongo wake ukashtuka na kisha kuanza kujiweka kama zamani. Ubize wa kusoma ambao alikuwa akijipa kila siku ndio ambao ulianza kumfanya kuanza kurudi kama alivyokuwa zamani, kipindi ambacho hakuanza kuishi maisha ya anasa shuleni Uhuru mkoani Kilimanjaro. Walimu wakautambua uwezo mkubwa ambao alikuwa nao Catherine, ulikuwa ni uwezo ambao ulimfanya mara kwa mara kuongoza katika masomo yake.

Wazazi wake wakaonekana kuwa na matumaini kwa binti yao, juhudi ambazo alikuwa akizionyesha katika masomo yake zikaonekana kuanza kuzaa matunda. Kila siku alikuwa mtu wa kujifungia chumbani na kusoma, mambo ya anasa na kutamani kufanya mambo yasiyokuwa na maana akawa ameachana nayo na katika kipindi hicho alikuwa akifikiria kitu kimoja tu, kusoma na kutimiza ndoto zake ambazo alikuwa akiziota kila siku, ndoto za kuwa mwanasheria mkubwa nchini Tanzania.

Mwaka ulipokatika, akamaliza masomo yake aliyokuwa akiyarudia na alipofanya mitihani akawa amefaulu vizuri jambo ambalo lilimfanya kuingia kidato cha sita huku akiwa na alama zote ambazo alitakiwa kuwa nazo katika matokeo yake.
“Naona kama ndoto zangu zinakaribia kutimia Scola” Catherine alimwambia rafiki yake wa karibu ambaye mara kwa mara alikuwa akipenda kusoma nae.

“Kila kitu kitakwenda kutimia, cha msingi ni kuongeza juhudi tu. Mbona unaweza sana tu Catherine” Scola alimwambia Catherine ambaye alionekana kufarijika.
“Nitataka kuwa mwanasheria katika nchi hii” Catherine alimwambia Scola.
“Kama ukipigana na kusoma sana, utakuwa tu, hakuna kinachoshindikana chini ya jua” Scola alimwambia Catherine ambaye aliendelea kusoma zaidi na zaidi.
Catherine akaonekana kubadilika kabisa, shuleni hapo akaonekana kuwa mkali zaidi ya wanafunzi wote ambao walikuwa kidato cha sita. Katika kipindi hicho aliona kusoma ndicho kilikuwa kitu pekee ambacho kingemfanya kutimiza ndoto zake za baadae, ndoto za kuwa mwanasheria nchini Tanzania. Wanafunzi wengi wa kike na wa kiume walikuwa wakivutiwa na Catherine ambapo mara kwa mara walikuwa wakitamani kuwa karrbu nae na kisha kuwafundisha.
Shuleni hapo, wanafunzi wengi waliambiwa kuiga tabia za Catherine ambaye kila siku alionekana kuwa moto shuleni hapo. Catherine hakutaka kuyakumbuka maisha yake ya nyuma ambayo alikuwa amepitia, kitu ambacho alikuwa akikitaka kwa wakati huo ni kuyafikiria maisha yake ya mbele na kutimiza malengo yote ambayo alikuwa amejiwekea moyoni mwake.
“Vipi kuhusu mapenzi?” Fatuma alimuuliza Catherine.
“Mapenzi hayafai katika kipindi ambacho unahitaji muda wa kusoma” Catherine alimwambia Fatuma.
“Kwa nini? Ulikwishawahi kuumizwa nini?”
“Hapana. Namshukuru Mungu kwa sababu mpaka leo sijawahi kuonja maumivu ya mapenzi maishani mwangu” Catherine alimwambia Fatuma ambaye akabaki akiachia tabasamu.
“Mmmh! Sawa. Ila kuna tu alikuwa akitaka kuongea na wewe” Fatuma alimwambia Catherine.
“Nani?”
“Edmund”
“Kuongea na mimi kuhusu nini?”
“Wala sijui au nikuitie umsikilize” Fatuma alimwambia Catherine.

Edmund alikuwa miongoni mwa vijana wa shule ile ambao walikuwa wakivutiwa sana na uzuri wa Catherine. Kila siku Edmund alikuwa mvulana wa kumwangalia sana Catherine ambaye alikuwa akisoma nae darasa moja. Kwa Catherine, katika kipindi hicho hakuwa akiyatamani mapenzi, alijua kwamba mapenzi hayo hayo yalikuwa yamempotezea muda wake mwingi sana na hivyo hakutakiwa kurudi kule alipotoka.

Japokuwa Edmund alikuwa akimpenda sana Catherine lakini moyo wake ulikuwa umejaa woga mwingi. Hakuwa akiamini kama angeweza kusimama na Catherine na kisha kumueleza ukweli juu ya alivyokuwa akijisikia kwamba alikuwa akimpenda sana. Kila siku alibaki kuwa mtu wa kumwangalia Catherine na kumsifia moyoni kwamba alikuwa msichana mzuri ambaye alitakiwa kuwa na mtu kama yeye.

Edmund hakuwahi kumsogelea Catherine na kumwambia ukweli juu ya jinsi alivyokuwa akijisikia. Kwanza alikuwa akimuogopa sana msichana huyo ambaye alionekana kujiamini kupita kawaida. Kila alipokuwa akisimama mbele ya mvulana yeyote yule Catherine alionekana kuwa msichana imara, msichana asiyetetereka hata kidogo jambo ambalo lilikuwa likiwatia hofu wanaume wengi shuleni hapo.

Wale wanaume ambao hawakuwa wakiogopa kitu chochote wakajitoa mhanga na kisha kumfuata Catherine na kumueleza ukweli juu ya jinsi walivyokuwa wakijisikia mioyoni mwao. Kwa Catherine hakuonekana kuwakubali, kila siku katika maisha yake aliyaona mapenzi kutaka kuzima ndoto zake ambazo alikuwa amejiwekea toka alipokuwa kidato cha kwanza. Ni kweli kabisa mapenzi yalikuwa yamechukua nafasi moyoni mwake na hatimae kumfanya kufeli vibaya masomo yake, katika kipindi hicho hakutaka tena kuwa na mwanaume yeyote yule.

“Nayachukia mapenzi” Catherine alimwambia Scola.
“Kwa nini?”
“Yanaweza kukufanya kutokukamilisha ndoto zako” Catherine alimwambia Scola.
“Mmmh! Ila wavulana wengi wanakupenda hapa shuleni” Scola alimwambia Catherine.
“Najua. Mara kwa mara Fatuma amekuwa akiniambia hivyo”
“ Sasa haukuchukua hata hatua?”
“Hatua gani?”
“Kuwa hata na mmojawapo”
“Hapana. Hilo ni jambo gumu sana. Siwezi kuwa na mwanaume yeyote yule shuleni hapa” Catherine alimwambia Scola.
Japokuwa Catherine alikuwa akiendelea kuonyesha msimamo wake lakini wanaume hawakukoma, kila siku walikuwa wakimfuata lakini Catherine hakuonekana kukubaliana na mwanaume yeyote yule. Edmund hakutaka kukata tamaa, japokuwa wavulana wengi walikuwa wakikataliwa na Catherine lakini kila siku katika moyo wake alikuwa na uhakika wa asilimia mia moja kwamba kuna siku msichana huyo, Catherine angekuwa wake na hivyo kufanya mambo mengi kama wapenzi.

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 12

Mchungaji Mpelele hakuelewa ni kitu gani kilikuwa kikiendelea, kila alipokuwa akimpigia simu mtoto wake, Samuel hakuwa akipatikana simuni kabisa. Wasiwasi ukamwingia moyoni mwake kwa kuona kwamba inawezekana kulikuwa na jambo baya ambayo lilikuwa limemtokea mtoto wake. Alipomuuliza mke wake, Bi Magreth, nae alisema kwamba kila alipokuwa akimpigia simu, simu haikuwa ikipatikana.

Jambo hilo likazidi kumtia wasiwasi zaidi hali ambayo likamfanya kushauriana na mke wake waelekee shuleni kwao, Makongo kwa ajili ya kuuliza ni kitu gani ambacho kilikuwa kikiendelea. Katika kipindi hicho, mchungaji Mpelele hakuwa na wasiwasi na mtoto wake kwani katika kipindi ambacho alikuwa akienda kuanza shule kwa ajili ya kurudia mitihani yake, tayari mtoto wake, Samuel alikuwa amekwishaamua kubadilika kwa kuanza kumtumikia Mungu.

Walipofika shule, moja kwa moja wakaanza kuelekea katika ofisi za walimu ambapo wakahitaji kuonana na mwalimu mkuu na kisha kuruhusiwa kuelekea katika ofisi ya mwalimu huyo. Walipoingia, hawakuwa na muda wa kupoteza, wakajitambulisha kama wazazi wa Samuel na walifika mahali hapo kwa ajili ya kumuona mtoto wao, Samuel.
Kwanza mwalimu mkuu akaonekana kushtuka, akawaangalia vizuri, uso wake ukaonekana kubadilika, mshangao wa wazi ukaonekana machoni mwake. Hakuamini kama kweli Samuel alikuwa mtoto wa mchungaji, uso wake ulionyesha dhahiri kushangazwa na cheo cha mchungaji Mpelele.

“Kumbe wewe ni mchungaji?” Mwalimu mkuu aliuliza huku akionekana kushangaa.
“Ndio. Mimi ni mchungaji wa kanisa la Praise And Worship hapo Mwenge” Mchungaji Mpelele alimwambia mwalimu mkuu.
“Dah! Unajua kuna wakati naona kama siliamini hili” Mwalimu mkuu aliwaambia.
“Kwa nini?”
“Kumbe Samuel ni mtoto wa mchungaji?”
“Ndio. Kuna nini? Tunaweza kumuona?” Mchungaji Mpelele alimuuliza mwalimu.
“Hayupo shuleni”
“Hayupo shuleni?”
“Ndio. Huu mwezi wa pili hajafika shuleni hapa” Mwalimu mkuu aliwajibu.
“Unatuchanganya mwalimu. Inakuwaje Samuel kutokuwa shuleni hapa kwa kipindi kirefu namna hiyo?” Mchungaji Mpelele aliuliza.
“Huo ndio ukweli. Ila mbona mnauliza kwa kushangaa sana?”
“Kwa sababu sisi tunajua anakuja shule kila siku”
“Kwani kila anapofika nyumbani huwa anawaambia nini?”
“Hakai nyumbani”
“Sasa mbona na nyie pia mnanichanganya”
“Hakai nyumbani. Alihitaji muda wa kukaa katika hosteli yoyote ile kwani aliamini kwa kufanya hivyo angekuwa makini na masomo” Mchungaji Mpelele alimwambia mwalimu mkuu.
“Duh! Hii kali mchungaji. Ndio kwanza nimeanza kuisikia kwako kwamba mwanafunzi wa sekondari anakaa hosteli” Mwalimu mkuu alimwambia mchungaji Mpelele na Bi Magreth.
“Hatuwezi kuonana na mwalimu wa dini?”
“Wa nini tena mchungaji”
“Inawezekana akawa anafahamu kidogo kuhusu Samuel”
“Kivipi?”
“Kwa sababu Samuel ni mcha Mungu”
“Mcha Mungu! Kuanzia lini?”
“Toka alipoondoka nyumbani”
“Mcha Mungu kivipi tena? Hapo unanichanganya mchungaji”
“Mcha Mungu kama unavyoelewa wewe mwalimu”
“Sidhani kama Samuel alikuwa mcha Mungu kama ninavyoelewa mcha Mungu anavyokuwa. Mcha Mungu huwa hanywi pombe, mcha Mungu huwa afanyi ngono” Mwalimu alimwambia mchungaji.
“Kwa hiyo una maana kwamba Samuel alikuwa akinywa pombe na kufanya ngono?” Mchungaji Mpelele aliuliza huku akionekana kuchanganyikiwa.
“Ndio”
“Shuleni hapa hapa?”
“Ndio”

Majibu ya mwalimu mkuu yakaonekana kuwachanganya wote, wakabaki kimya, kila mmoja akaonekana akifikiria lake kichwani mwake. Hawakuyaamini maneno yale ambayo mwalimu mkuu alikuwa ameyasema mbele yao, hawakuamini kama mtoto wao Samuel alikuwa ameanguka tena dhambini.

Mchungaji Mpelele akaona koti lake la suti kama linampa sana joto, akalivua na kisha kuanza kujipepea kwa kitambaa chake huku kijasho kikiwa kinamtiririka kupita kawaida. Kwa mke wake, Bi Magreth, alikuwa kimya, nae alionekana kuchanganyikiwa kwa kile ambacho alikuwa amekisikia kutoka kwa mwalimu mkuu. Hapo ndipo walipoamini kwamba shetani alikuwa akiendelea kufanya kazi kwa mtoto wao na si kwamba alikuwa amemaliza kazi zake juu yake.

“Haiwezekani” Mchungaji Mpelele alisema huku akionekana kuchanganyikiwa.
“Hatuwezi kuongea na marafiki zake?” Bi Magreth alimuuliza mwalimu.
“Toka aje katika shule hii alikuwa na rafiki yake mmoja tu” Mwalimu alijibu.
“Huyo huyo tunataka kuongea nae”
“Nae ameondoka pamoja nae. Yaani Samuel alipoacha kuja shule tu, hata nae rafiki yake akaacha kuja shule. Natumaini watakuwa pamoja kwa sasa” Mwalimu alimjibu.
“Rafiki yake yupi?”
“Anaitwa Sadiki Hamidu” Mwalimu mkuu alijibu.

Jina hilo halikuwa geni sana masikioni mwao, walikuwa wamekwishawahi kulisikia mara kadhaa kutoka mdomoni wa mtoto wao, Samuel. Mpaka kufikia hatua hiyo, walikuwa na kitu kimoja tu ambacho walikiona kwamba kilitakiwa kufanyika. Wakataka kuonana na wazazi wa Sadiki na kuzungumza nao ili wafahamu kama nao mtoto wao alikuwa kama Samuel au ilikuwaje. Alichokifanya mwalimu mkuu ni kuwataka wote wafike shuleni hapo kesho huku yeye akifanya mawasiliano na Ustadhi Hamidu kumtaarifu kuhusu kuja shuleni hapo.

Walichokifanya mara baada ya kuondoka shuleni hapo ni kuelekea katika hosteli ya St’ Peter ambayo ilikuwa Kinondoni kwa ajili ya kuonana na Samuel ambaye alikuwa amechukua chumba katika hosteli hiyo. Ndani ya gari kila mtu alikuwa akiwaza lake, maneno ambayo aliongea mwalimu mkuu yalionekana kumchanganya kila mmoja.

“Ila naona ni kama kitu kisichowezekana” Bi magreth alimwambia mume wake, mchungaji Mpelele.
“Kwa nini?”
“Kweli Samuel anaweza kuyarudia maisha ambayo alikuwa akiishi kipindi cha nyuma?”
“Anaweza. Mtu husimama na kuanguka pale ambapo anasimama mguu upande. Shetani ana nguvu sana, sisi kama wanadamu hatuwezi kupigana nae na ndio maana tunasema vita vyetu vya nyama na damu” Mchungaji Mpelele alimwambia mke wake, Bi mage.

Baada ya dakika kadhaa wakafika nje ya jengo la hosteli ya St Peter ambapo wakateremka na kisha kuanza kuusogelea mlango wa kuingia katika jengo lile. Walichokifanya mara baada ya kuingia ndani ya jengo lile ni kuwafuata wanachuo kadhaa ambao walikuwa wamekaa pembeni kwa lengo la kuwauliza.

“Dah! Hao watu toka mwezi uliopita walitimuliwa hapa” Kijana mmoja miongoni mwa vijana hao aliwaambia.
“Waliwatimua! Kisa nini?”
“Walikuwa na tabia chafu sana. Walikuwa wakipenda sana kunywa pombe, kula mirungi, kuvuta sigara mpaka kuleta wanawake ndani” Kijana huyo alijibu.
“Unamaanisha mambo hayo alikuwa akiyafanya Samuel?” Mchungaji Mpelele aliuliza huku akionekana kutokuamini.
“Ndio. Samuel Mpelele pamoja na rafiki yake, Sadiki Hamidu” Kijana yule alijibu.
“Baada ya kutoka hapa watakuwa wameelekea wapi?”
“Hatujui. Labda angekuwepo rafiki yao waliyekuwa anakaa nao chumba kimoja angekuwa anafahamu”
“Rafiki yao nani?”
“Huyu anaitwa Cosmas ila bahati mbaya nae mwenyewe alihama mahali hapa” Kijana yule aliwaambia.
Akili zao zikazidi kuchanganyikiwa zaidi. Hapo wakaonekana kuamini kwamba kijana wao alikuwa amepotelea katika mikono ya shetani na yalihitajika maombi zaidi kwa kumrudisha tena. Wote wakaonekana kukata tamaa, hawakuamini kama kijana wao, Samuel angeweza kupotealea katika mikono ya shetani kwa mara nyingine tena.

Usiku hawakulala vizuri, hawakuwa na amani mioyoni mwao, kitu ambacho walikuwa wakikitaka ni kufahamu mahali ambapo mtoto wao alipokuwa katika kipindi hicho. Nusu saa kabla ya kulala, wakashikana mikono na kisha kuanza kuomba. Sala yao kwa Mungu ilikuwa moja tu, kumrudisha Samuel nyumbani hapo na kumbadilisha kwa mara nyingine tena.
****
Siku iliyofuata saa tano asubuhi wakaanza safari ya kuelekea shuleni hapo kwa ajili ya kuonana na wazazi wa Sadiki ili kujua ni kitu gani ambacho kilikuwa kikiendelea. Walipofika shuleni hapo, moja kwa moja wakaanza kupiga hatua mpaka katika ofisi ya mwalimu mkuu. Walipoingia, ukiachana na mwalimu mkuu, macho yao yakatua kwa ustadhi Hamidu ambaye alikuwa amevalia kanzu huku akiwa na kofia ya kiislamu pamoja na Tasbih mkononi mwake huku mke wake, Bi Aisha akiwa amevalia baibui kubwa nyeusi ambayo ilikuwa imemfunika mpaka miguu yake huku kichwani akiwa amejisitiri na kilemba kilichoonekana kumpendezesha sana.

“Karibuni” Mwalimu mkuu aliwakaribisha mara baada ya kuingia ndani ya ofisi ile.

Moja kwa moja wakakaa vitini na kisha mwalimu mkuu kuanza kutoa utambulisho mahali hapo na kisha kuanza kuelezea kila kitu ambacho kilikuwa kikiendelea katika maisha ya watoto wao. Ustadhi Hamidu na mkewe hawakuonekana kushtuka sana hali ambayo iliwaonyesha kwamba walikuwa wakifahamu baadhi ya mambo ambayo yalikuwa yakiendelea kwa mtoto wao. Japokuwa hawakuonyesha mshtuko mkubwa lakini nyuso zao zilionyesha kuumizwa na kile ambacho kilikuwa kimetokea kwa kijana wao.

“Mtoto wangu alimkataa Allah! Sina uhakika kama Allah ataendelea kuwa nae” Ustadhi Hamidu alisema huku akionekana kukata tamaa.
“Usiseme hivyo ustadhi” Mwalimu mkuu alimwambia ustadhi Hamidu.
“Huo ndio ukweli. Tumeshangaa sana, hatujui ni mahali gani ambapo Sadiki alikuwa amejikwaa, hatujui kama ni yeye ndiye chanzo au kuna sehemu sisi kama wazazi tulifanya makosa. Mabadiliko yake yamekuja kwa haraka sana” Ustadhi Hamidu aliongea huku akionekana kuwa na maumivu makali moyoni.
“Hiyo ni sawa na Samuel. Yaani tuliona amebadilika bila kujua ni kitu gani kilikuwa chanzo cha mabadiliko yake” mchungaji Mpelele aliwaambia.

Kila mmoja akaonekana kukata tamaa na mtoto wake, hakukuonekana kuwa na dalili za watoto wao kurudi katika maisha kama ambayo walikuwa wakiishi zamani, maisha ya kumtumikia Mungu. Mara baada ya maongezi mafupi hapo ndipo mchungaji Mpelele alipowaambia kile ambacho aliambiwa katika hosteli ya St Peter kwamba vijana wao hawakuwepo katika hosteli ile kwani walikuwa wamefunkuzwa.

Ustadhi Hamidu pamoja na mkewe, Bi Aisha wakaonekana kuchanganyikiwa, maneno ambayo aliongea mchungaji Mpelele yakaonekana kuwachanganya zaidi kwani waliona kwamba mtoto wao, Sadiki alikuwa ametoweka moja kwa moja na kujiingiza katika maisha ya mitaani. Mioyo yao ikazidi kuumia zaidi na zaidi, katika kipindi hicho, wazazi wa pande zote mbili wakaonekana kuumizwa kupita kawaida, tayari waliona kwamba shetani alikuwa amewazidi nguvu watoto wao na hatimae kujiingiza katika maisha ya anasa moja kwa moja.

Siku hiyo ikaonekana kuwa mbaya kwa wazazi wa pande zote mbili, walibaki wakiwa na huzuni sana huku mioyo yao ikizidi kumuomba Mungu awalinde watoto wao na mwisho wa siku waje kumtumikia Mungu kama ilivyokuwa katika kipindi cha nyuma.

Walipoondoka mahali hapo, wakajiahidi kuanza kuwatafuta watoto wao huku wakiwa wamebadilishana namba za simu kwa ajili ya kufanya mawasiliano pale ambapo wangesikia kitu chochote kile kuhusiana na watoto wao juu ya mahali walipokuwa katika kipindi hicho.

“Allah! Naomba uniangalie mtumishi wako. Hili pigo ulilompiga Sadiki ni kubwa sana. Naomba umsamehe kwa kila kitu na kumrudisha kundini na aendelee kumtangaza Mtume Mohammad S.A.W” Ustadhi Hamidu alisema huku akiangalia juu, alionekana kukata tamaa na kuonekana katika hali ambayo alimtegemea Mungu tu.

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 13

Bado biashara ya kuuza madawa ya kulevya ilikuwa ikiendelea kama kawaida huku Khaled akiendelea kuwatuma katika nchi mbalimbali barani Afrika hasa katika nchi ambazo zilikuwa katika ukanda wa Mashariki. Kila siku walikuwa wakiifanya kazi ile ambayo kwao ikaonekana kuwa nyepesi kabisa.

Madawa ya kulevya yalikuwa yakisafirishwa na kiasi kikubwa cha fedha kuingizwa katika akaunti ya Khaled ambaye alikuwa akizidi kutanuka kibiashara zaidi nchini Tanzania. Baadhi ya polisi ambao walikuwa wanafiki walionekana kuiangusha Serikali, mara kwa mara walikuwa wakipokea rushwa njiani na kuyaruhusu madawa kupita bila tatizo lolote lile. Kwa sababu Khaled alikuwa na mnyororo mkubwa wa kufanya biashara zake, alihakikisha kwamba vijana wake hawapati tatizo lolote lile njiani jambo ambalo lilimfanya kufanya biashara bila vizingiti vyovyote vile.

Katika kipindi chote ambacho walikuwa wakiendelea kusafirisha madawa ya kulevya, akili zao zilikuwa zikifikiria kitu kimoja tu, kumpindua Khaled katika kipindi cha baadae mara baada ya kuanza safari za Ulaya na kufahamiana na wateja wote ambao walikuwa wakinunua madawa yale ya kulevya.

Hilo ndilo dhmuni ambalo lilikuwa mioyoni mwao, unyonyaji ambao alikuwa akiufanya Khaled kwao waliuona kuwa mkubwa sana kwani walikuwa wakiyahatarisha maisha yao kupita kawaida. Hawakumeza madawa, usafirishaji wao ulikuwa ni wa kawaida sana hasa katika kipindi hicho cha zamani, kipindi ambacho madawa wala hayakuwa yakisafirishwa kwa wingi sana.

Kila siku maongezi yao yalikuwa ni kumzungumzia Khaled, bado walikuwa na tamaa ya kumiliki biashara nzima ambayo Khlaed alikuwa akiifanya, kitendo cha kuona fedha nyingi zikiingizwa ndani ya akaunti ya Khaled zikaonekana kuwatamanisha kupita kawaida. Bado walikuwa wakiendelea kufanya kazi kama kawaida lakini akili zao zilikuwa zikifikiria dhuluma tu. Wote kwa pamoja walikuwa wakihitaji kuwa na fedha nyingi, wawe na utajiri mkubwa ambao ungewafanya kuwa huru kufanya kila kitu ambacho walitakiwa kukifanya.

“Lazima tumuue” Sadiki alimwambia Samuel.
“Hilo lilikwishapita tangu kitambo. Au kama una jingine” Samuel alimwambia Sadiki.
“Na lazima tuchukue utajiri wake. Yaani fedha zake ziwe zetu. Au hilo wazo baya?” Sadiki alimuuliza Samuel.
“Wazo zuri sana. Kitendo cha kumuua tu kinamaanisha kwamba tunataka kila kitu kiwe chini yetu. Ni lazima tufanye hivyo” Samuel alimwambia Sadiki.
“Tumekwishaanza kujua michongo yote ya hapa Afrika. Unazikumbuka namba za bwana Khusa yule mzee wa Afrika Kusini?” Sadiki alimuuliza Samuel.
“Yeah! Nilichukua mawasiliano yake”
“Na yule mzee Pokwane wa pale Zimbazwe?”
“Wote nilichukua mawasiliano yao. Yaani kwa kifupi, watu wote ambao tulifanikiwa kwenda kuwauzia madawa nilichukua mawasiliano yao” Samuel alimwambia Sadiki.
“Basiiii. Hicho ndicho kilikuwa kitu cha muhimu sana. Cha msingi kuna safari hizo za Ulaya, Asia na Brazil inabidi tuzizoee pamoja na kuwafahamu watu kadhaa wanaohusika na madawa hapa nchini” Sadiki alimwambia Samuel.
Akili zao zilikuwa zimekwishabadilika kabisa. Walikuwa wakiendelea kufanya biashara ya kuuza madawa si kwamba walikuwa wakipenda kuifanya kwa sababu ilikuwa ikiwapatia fedha ila katika kipindi hicho walikuwa wakitaka kufanya kitu kimoja tu, kumdhulumu Khaled madawa yale na kisha kumuua.

Kwa jinsi tamaa ya fedha ambayo ilikuwa imewaingia mioyoni mwao wala hakukuwa na woga kabisa wa kumuua mtu yeyote yule, walichokuwa wakikiangalia kwa wakati huo kilikuwa ni fedha tu. Kila siku walikuwa wakiongelea fedha, tena hawakuwa wakiongelea kiasi kidogo cha fedha, walikuwa wakiongelea mamilioni ya fedha.
“Ninawaamini sana” Khaled aliwaambia mara baada ya kuhitaji kuongea nao.

“Asante bosi kwa kutuamini. Unajua tumefanya kazi pamoja nawe kwa mwezi wa sita sasa, haujatuangusha, umekuwa ukitulipa kiasi kizuri cha fedha, hatuna shaka juu ya hilo” Samuel alimwambia Khaled huku moyo wake ukiwa tofauti na maneno ambayo alikuwa akiyaongea kipindi hicho.

“Safi sana. Mmekuwa mkijitoa sana kwa ajili yangu. Ni kweli kwamba katika kipindi cha nyuma nilitamani sana kuwa na wafanyakazi kama ninyi, kila siku nilikuwa naomba Mungu kuwa na wafanyakazi kama ninyi, mwisho wa siku, amejibu maombi yangu kwa kuwaleta mahali hapa” Khaled aliwaambia huku akionekana kuwa na furaha.

Hapo hapo Khaled akasimama na kisha kuelekea kwenye jokofu na kuchukua pombe kali ya John Walker na kisha kurudi mezani pale, akachukua glasi ambazo zilikuwa mezani na kisha kuanza kuwamiminia pombe ile. Katika kipindi chote hicho uso wa Khaled ulikuwa ukionyesha furaha, kwake, Samuel na Sadiki walionekana kuwa wafanyakazi bora ambao alitakiwa kuwa nao katika kipindi kirefu sana.

Kwa sababu alikuwa binadamu, hakuweza kufahamu kile ambacho kilikuwa kikiendelea katika mioyo ya watu hao ambao alikuwa akiwaamini kupita kawaida. Hakujua kama ndani ya mioyo ya watu hao walikuwa wakifikiria kumdhulumu mali zake na kisha kumuua na kuiacha biashara ya madawa ya kulevya mikononi mwao.
“Hiki ndicho kipindi ambacho nilikuwa nakisubiria kwa hamu sana” Khaled aliwaambia huku akionekana kuwa na furaha.
“Kipindi gani bosi?” Samuel Alimuuliza.
“Kipindi cha nyie kwenda barani Ulaya” Khaled aliwaambia.
“Sawa sawa. Na sisi hiki ndicho kipindi ambacho tulikuwa tukikisubiria kwani tunaamini kama tutafanikiwa kupeleka mizigo huko, utaingiza kiasi kikubwa na sisi wadogo zako kutuangalia kwa jicho la tatu” Samuel alimwambia Khaled.
“Sawa sawa. Unalosema ni kweli kabisa. Ila naomba kabla hamjakwenda huko, kuna mzigo nata mpeleke nchini Kenya” Khaled aliwaambia.
“Hakuna tatizo. Tutakwenda tu. Unataka tupeleke lini?” Samuel alimuuliza.
“Kesho kutwa. Cha msingi jiandaeni. Ni mzigo mkubwa ambao unahitaji uangalizi mkubwa sana” Khaled aliwaambia.
“Usijali mkuu”
****
Kila siku Edmund alikuwa akijisikia kuwa wa tofauti moyoni, alikuwa akitamani sana kuongea na Catherine na hatimae amwambie kile ambacho alikuwa akijisikia moyoni mwake. Kwake, Catherine alionekana kama malaika aliyekuwa na uzuri wa tofauti, kila alipokuwa akimuona mapigo yake ya moyo yalikuwa yakidunda kupita kawaida.

Mara kwa mara alikuwa akipanga kwamba siku hiyo ilikuwa ni siku ya kumwambia Catherine juu ya alivyokuwa akijisikia lakini kitu cha ajabu, siku hiyo ilikuwa ikipita bila kutamka neno lolote lile. Katika maisha yake, hakuzoea kabisa kuongea na msichana yeyote yule, hakuwahi kumtongoza msichana yeyote, kwa kifupi, Edmund alikuwa bikira wa kiume.
Mapenzi juu ya Catherine yalikuwa yakimtesa kupita kawaida, katika kipindi hicho ndicho ambacho alipata kufahamu kwamba mapenzi yalikuwa yakitesa sana moyoni hasa pale ambapo ulikuwa ukimpenda mtu ambaye wala hakuwa na habari na wewe. Kila siku akawa mtu wa kuumia tu, Catherine alizidi kuonekana mzuri machoni mwake jambo ambalo lilikuwa likimvutia zaidi na zaidi.

Wanaume wengi walikuwa wakiendelea kujitosa kwa msichana huyo lakini hakuonekana kumkubalia mtu yeyote jambo ambalo lilizidi kumuogopesha Edmund kwa kuona kwamba kulikuwa na uwezekano hata yeye mwenyewe angeshindwa kumuingiza Catherine katika mikono yake. Watu ambao walikuwa wakimfuata Catherine walikuwa watu wenye uwezo mkubwa kuongea, walikuwa watu ambao kila walipokuwa wakisimama na msichana walionekana kuwa na ushawishi mkubwa, ila hao watu wote kwa Catherine wakaonekana kuwa si kitu jambo ambalo lilimfanya Edmund kuona kwamba kama angekwenda yeye, pia mambo yangekuwa vile vile.
“Nitamfuata tu” Hayo yalikuwa maneno ambayo mara kwa mara yalikuwa yakitoka mdomoni mwa Edmund lakini hakuwa akiyatendea kazi.

Siku ziliendelea kukatika mpaka zilipofikia siku za mwisho za kufanya mitihani ya taifa ya kidato cha sita. Kama kuvumilia Edmund alikuwa amevumilia vya kutosha na katika kipindi hicho aliona bora kulipasua jipu ambalo kwake lilionekana kuiva. Alichokifanya wiki moja kabla ya kuanza mitihani ni kuanza kumfuata Catherine ambaye alikuwa amejikalia darasani akijisomea.

Kadri Edmund alivyokuwa akipiga hatua kumfuata Catherine na ndivyo ambavyo mapigo yake ya moyo yalivyokuwa yakizidi kumdunda zaidi na zaidi huku kwa mbali kijasho chembamba kikianza kumtoka. Mpaka anamfikia Catherine katika sehemu ile amliyokuwa amekaa, alionekana kuhofia kupita kawaida.
“Mambo!” Edmund alisalimia huku kwa mbali akionekana kutokujiamini.
“Safi. Karibu” Catherine alimkaribisha Edmund ambaye akajitahidi kuonyesha tabasamu usoni mwake.
“Asante” Edmund alimwambia Catherine.

Mpaka kufikia mahali hapo Edmund akaonekana kuishiwa maneno, akabaki kimya huku akijifikiria ni neno gani ambalo lilitakiwa kufuata baada ya hapo, hakujua ni maneno gani matamu ambayo yalitakiwa kutoka mdomoni mwake na kusikika masikioni mwa Catherine. Kichwani alikuwa akiendelea kujifikiria, kwake tayari ugumu ukaanza kuonekana kwa kuona kwamba kazi ya kuongea na msichana ilikuwa kubwa sana.

“Nakupenda” Edmund alijikuta akisema baada ya ukimya wa muda mrefu kidogo.
Catherine akaonekana kushtuka, kwanza akaacha kazi ya kusoma na kisha kuyapeleka macho yake usoni mwa Edmund. Catherine alionekana kupigwa na mshangao, neno ambalo lilitoka kinywani mwa Edmund likaonekana kumshtua kupita kawaida, alichokifanya ni kutoa tabasamu.

“Umesemaje?” Catherine alimuuliza Edmund huku akionekana kushtuka.
“Nakupenda” Edmund alijibu.
“Kivipi? Kama rafiki? Nakupenda pia” Catherine alimwambia Edmund.
“Hapana. Ninakupenda, ninamaanisha nimeangukia katika mapenzi yako” Edmund alimwambia Catherine.
“Upo sawa kweli leo Edmund?”
“Nadhani nipo sawa zaidi ya siku zote”
“Hapana. Haupo sawa”
“Kwa nini?”
“Kwa hicho ulichoniambia”
“Kwani kigeni masikioni mwako?”
“Hapana, si kigeni ila kwa mtu kama wewe, ni kigeni kabisa na sikutarajia kukisikia” Catherine alimwambia Edmund.
Kwanza Edmund akabaki kimya. Alijua fika kwamba alikuwa ameharibu kwa kumwambia Catherine moja kwa moja juu ya kile alichokuwa akijisikia moyoni mwake ila kwa wakati mwingine alijiona kutakiwa kumwambia zaidi Catherine kwa kuamini kwamba angeweza hata kufanikiwa kumteka msichana huyo ambaye alikuwa akiutesa sana moyo wake.
“Kuna tatizo mimi kukupenda?” Edmund alimuuliza Catherine.
“Hakuna tatizo”
“Sasa mbona umeshtuka?”
“Umekuja moja kwa moja”
“Najua. Huwa nisingependa niongee maneno mengi sana na kuanza kutoa ahadi nyingi ambazo ningeshindwa kuzitimiza mara tu ungekubali kuwa pamoja nami. Sitaki uwe pamoja nami kwa sababu ya maneno yangu na kinafiki yatakayokuonyesha kukujali au kukuthamini, nisingependa uwe mpenzi wangu kwa sababu nimekuwekea ahadi ambazo ningeziona kutoweza kuzitimiza maishani mwangu, nimekwambia moja kwa moja, nisingependa kuongeza neno wala kupunguza neno” Edmund alimwambia Catherine.
“Mmmh! Sikujua kama upo hivi”
“Kivipi?”
“Una maneno mengi”
“Hapana. Ninajaribu kukwambia ukweli tu” Edmund alimwambia Catherine.
Kadri alivyokuwa akiongea na Catherine na ndivyo ambavyo alikuwa akipata ujasiri zaidi na zaidi mpaka kufikia kipindi ambacho akajiona kuwa huru kuzungumza neno lolote kwa msichana huyo mrembo. Edmund hakutaka kutoka nje ya mazungumzo, kila alichokuwa akikiongea mahali hapo kilikuwa kikihusiana na mapenzi, maneno ambayo yakaonekana kuwa tofauti masikioni mwa Catherine, hayakuonekana kuwa kama maneno ya wavulana wengine ambao aliwaona kumfuata kitamaa.
“Naomba nikufikirie” Catherine alimwambia Edmund mara baada ya kuona kabanwa kotekote.
“Nahisi haitokuwa rahisi kunifikiria katika kipindi kama hiki. Tuna mitihani mbele yetu, utaweza kunifikiria na wakati huo huo unatakiwa kufikiria mitihani?” Edmund alimuuliza Catherine.
“Ni ngumu kupanga maamuzi ya haraka Edmund”
“Najua. Ila na ni ngumu kuamua kunifikiria na majibu yako kuwa ya kuniumiza. Naomba uniambie hapa hapa, nataka kufahamu kama upo tayari kuwa na mimi au la” Edmund alimwambia Catherine.
“Nitakujibu simuni. Namba yangu si unayo hapo?”
“Hapana”
“Basi ichukue” Catherine alimwambia Edmund huku akimgawia simu.
Siku hiyo ndio ilikuwa siku ya kwanza kwa wawili hao kuongea kuhusiana na mahusiano ya kimapenzi. Japokuwa Catherine alionekana kuwa mgumu kwa wanaume wengine lakini kwa Edmund akajihisi kuwa wa tofauti kabisa, akahisi mapenzi yakianza kujitokeza moyoni mwake. Kwa sababu Edmund alikuwa amekuja moja kwa moja bila kuzungumza maneno mengi,

Catherine akapata uhakika kwamba mwanaume huyo alikuwa na mapenzi ya dhati kwake kiasi ambacho akaamua kumkabidhi moyo wake usiku wa siku hiyo katika kipindi ambacho walikuwa wakiongea simuni. Japokuwa walikuwa wameahidiana kwamba mapenzi yao yangekuwa siri, wkajikuta wakigundua kwamba mapenzi yalikuwa ni kikohozi, tena kikohozi kizito kwani ndani ya wiki hiyo hiyo, wanafunzi wengi wakafahamu kwamba wawili hao walikuwa kwenye mahusiano ya kimapenzi jambo ambalo liliwashangaz wengi kwani Edmund alionekana kuwa muoga wa wanawake.

“Naomba unipende katika kipindi chako chote cha maisha yako” Catherine alimwambia Edmund kwa sauti ya chini katika kipindi ambacho walikuwa wakijisomea, siku moja kabla ya kuanza mitihani ya Taifa ya kidato cha sita.
“Usijali. Nitakupenda katika maisha yangu yote, nakuhakikishia hakuna kitakachotenganisha upendo wangu kwako zaidi ya kifo” Edmund alimwambia Catherine bila kufahamu ni kitu gani kingetokea katika maisha yao ya mbele, hakukuwa na mtu aliyejua kama maisha yao ya mbele ya mahusiano yale yangekuwa ni machozi na maumivu yasiyokwisha mioyoni mwao.

Mapenzi yalikuwa matamu kama ungempata mtu asiyeweza kukusaliti, ila kwa mahusiano yao, kuna mambo mengi yangeweza kutokea, mambo ambayo kwao hawakuwa wakiyafahamu kwa sababu tu yalikuwa mbele ya muda, endapo wangeyafahamu, kusingekuwa na mtu ambaye angetamani kuwa katika mahusiano ya kimapenzi.
 
SEHEMU YA 15

Mitihani ya kidato cha sita ikafanyika huku Catherine na Edmund wakiwa kwenye mapenzi ya dhati. Katika kipindi hicho wote wawili walionekana kuwa na furaha sana kwa sababu ndio kwanza mapenzi yao yalikuwa machanga na hivyo walikuwa na mambo mengi ambayo walikuwa wameyabakiza kuyafanya katika maisha yao ya mahusiano ya kimapenzi. Mpaka mitihani inakwisha, mapenzi yao hayakuishia shuleni tu bali yaliendelea mpaka nyumbani. Kichwani mwa Catherine, hakumkumbuka tena Samuel, mwanaume ambaye alikuwa pamoja nae katika miaka miwili iliyopita. Katika kipindi hicho alijiona kuanza upya maisha ya mahusiano pamoja na Edmund ambaye alionekana kuwa na mapenzi ya dhati kwake.

Edmund akaona kama anachelewa jambo ambalo lilimfanya kuwaambia wazazi wake juu ya Catherine ambaye kadri siku zilivyozidi kwenda mbele alikuwa akizidi kuvutia zaidi na zaidi machoni mwa kila mwanaume ambaye alikuwa akimwangalia. Ile figa ambayo alikuwa nayo katika kipindi cha nyuma ikaonekana kuongezeka, figa nzuri ambayo ilimdatisha kila mwanaume ndio ambayo ilikuwa ikiupendezesha zaidi mwili wake mpaka kufikia hatua ya kila mwanaume ambaye alikuwa akimwangalia kumkazia macho.

“Mnapendana?” Baba yake Edmund, mzee Zilikana aliwauliza.
“Tunapendana sana” Edmund alijibu na wote kuachia tabasamu.
“Malengo yenu ya baadae ni kufikia ndoa au ni mahusiano ya kupita tu?” Mzee Zilikana aliwauliza.
“Hii ni moja kwa moja mpaka ndoa” Edmund alijibu.
“Ila mbona kila swali unajibu wewe tu Edmund, hebu mpe nafasi Catherine nae tuisikie sauti yake ikijibu swali” Mzee Zilikana alimwambia Edmund.
“Nitampenda mpaka pale kifo kitakapotutenganisha” Catherine alimwambia Edmund.
“Vizuri. Kuweni makini katika maisha yenu, magonjwa mengi kwa sasa, hamtakiwi kuwa na tamaa ya vitu vidogo vidogo” Mzee Zilikana aliwaambia.
“Hilo si tatizo”
“Ila kuna kingine amesahau kuwaambia” Mama yake Edmund, Bi Elizabeth aliwaambia.
“Kipi tena?”
“Mnatakiwa kwenda kupima kwanza mjue afya zenu kabla ya mambo mengine kuendelea” Bi Elizabeth aliwaambia.
Maneno yale hawakutakiwa kuyapuuzia hata mara moja, kila mtu alikuwa akijiamini kwamba hakuwa ameathirika lakini kwa sababu wazazi wao waliwataka kwenda kupimwa damu zao, wakaamua kwenda kupima na majibu yalipotoka walionekana kuwa wazima kabisa.

Majibu hayo yakawa furaha kwao, japokuwa hapo kabla walikuwa wakihofia lakini kwa kiasi fulani walikuwa na uhakika kwamba kila kitu kilikuwa salama kabisa.Siku zikakatika na wiki kusogea mpaka kufika kipindi ambacho matokeo ya kidato cha sita yalipotoka. Kwa wote wawili walikuwa wamefanya vizuri jambo lililowapelekea kuchaguliwa kujiunga na chuo Kikuu cha Dar es salaam huku Edmund akichaguliwa kujiunga na chuo cha Dodoma.

Kwa kiasi fulani hiyo ikaonekana kuwanyong’onyeza sana, hawakutaka kutengana kwa umbali mkubwa kiasi hicho, kila siku walikuwa wakitaka kuwa pamoja zaidi na zaidi ili uhusiano wao uendelee kukua zaidi na zaidi. Hali ambayo ilikuwa imetokea hawakuwa na jinsi nayo, walichokifanya ni kutengana na kila mtu kuendelea na masomo kama kawaida.
Kwa Catherine maisha hayakuonekana kuwa na furaha hata mara moja, kitendo cha kuishi mbali na mpenzi wake alikiona kuwa ni mateso makubwa, mateso ambayo hakuwa akitamani yamfikie hata siku moja katika maisha yake. Kwa kiasi fulani mawasiliano hayo yakawafanya kujiona wapo karibu sana. Kila siku walikuwa wakizungumzia kuhusu mahusiano yao, hawakutaka kukaa muda mrefu bila kuzungumza. Mara kwa mara usiku Catherine alikuwa akijifunika shuka kitandani na kisha kuanza kuwasiliana na mpenzi wake huyo ambaye kwake alimuona kuwa mtu muhimu katika maisha yake.

“Leo ningetaka unionyeshee ni kwa jinsi gani unanipenda” Sauti ya Catherine ilisikika.
“Ungependa nifanye nini kwa ajili yako?” Edmund aliuliza.
“Unibusu”
“Nikubusu wapi?”
“Popote pale”
“Sawa, hakuna tatizo. Ngoja nikubusu kwenye unyayo wako” Edmund alimwambia Catherine huku akiachia tabasamu kana kwamba Catherine alikuwa mbele yake.
“Mmmh! Jamaniiiii”
“Nini tena mpenzi?”
“Unibusu kwenye unyayo?”
“Yeah! Si umekataa kuniambia nikubusu wapi”
“Naomba unibusu kwenye lipsi zangu” Catherine alimwambia Edmund.
“Umenikumbusha mbali sana mpenzi”
“Wapi?”
“Siku ya kwanza nilipoanza kuzibusu. Zilinipa msisimko wa ajabu sana, miguu ilinilegea kabisa, mapigo ya moyo yalikuwa yakidunda sana. Bado nusu nife” Edmund alimwambia Catherine kwa sauti ya chini.
“Mmh! Basi usifanye hivyo tena, sitaki kukupoteza mpenzi wangu”
“Hapana. Usifanye hivyo. Acha niendelee kama kawaida. Hivi inamaana mpaka mwezi wa sita ndio tutaonana?” Edmund alimuuliza Catherine.
“Yeah!”
“Hivi kwa nini vyuo vilianzishwa hapa duniani? Yaani huyu aliyeanzisha mambo ya vyuo bora asingezaliwa tu” Edmund alimwambia Catherine.
“Kwa nini?”
“Amenifanya nitengane na mpenzi wangu, barafu wa moyo wangu, mwanamke ninayempenda sana” Edmund alimwambia Catherine.
Katika usiku huo walikuwa wakiongea mambo mengi sana. Kwa mtu mwingine endapo angeyasikia yalionekana kuwa maneno ya kawaida na kijinga sana lakini kwa wao wawili walikuwa wakiyafurahia kupita kawaida. Kila wakati walikuwa wakicheka cheka tu, kila mmoja alikuwa akijisikia raha sana kuongea na mpenzi wake katika usiku huyo.
Katika chuo Kikuu cha Dar es Salaam, msichana Catherine alikuwa akionekana kuwa mrembo miongoni mwa wasichana wengi ambao walikuwa wakisifika kwa urembo chuoni hapo. Umbo lake zuri pamoja na macho yake yaliyotafsiriwa na wavulana kuwa macho ya kuita vilikuwa miongoni mwa vitu ambavyo vilikuwa vikiwavutia wanaume wengi kutamani kuwa nae.

Kiuno chake kizuri ambacho kilikuwa kimejigawa vilivyo, kifua chake kidogo kilichoitwa cha saa sita pamoja na sura yake nyembamba navyo vilikuwa miongoni mwa vitu ambavyo vilionekana kuwatoa udenda wanaume wengi chuoni hapo. Idadi kubwa ya wanaume walikuwa wakitaka kuwa na Catherine ambaye alionekana kutokuwa na mpango na mwanaume yeyote zaidi ya mwanaume wake ambaye alikuwa akimpenda kwa moyo mmoja, Edmund ambaye alikuwa akisoma katika chuo kikuu cha Dodoma, UDOM.

Japokuwa Catherine alikuwa akiwakatalia wanaume wengi chuoni hapo lakini wanaume hawakuonekana kukoma kabisa, kila siku walikuwa wakimfuata Catherine kwa maneno matamu na ya kuchombeza lakini kwa Catherine hakuonekana kujali kwa sababu maneno yale wala hayakuwa mageni masikioni mwake.

Hapo ndipo ambapo wanaume wale wakaamua kutafuta mbinu nyingine ili mladi msichana huyo aweze kuingia katika mikono yao. Wakaanza kufungua pochi kwa kuamini kwamba msichana huyo angezitetemekea fedha zao lakini hali haikuonekana kuwa kama walivyotarajia, mapenzi ya dhati na uaminifu wake kwa mpenzi wake vilikuwa ni zaidi ya fedha ambazo walikuwa wakija nazo wanaume kama chambo ya kumakatia.

Wanaume hawakujua ni kwa jinsi gani wangeweza kumuingiza msichana huyo katika mikono yao, kila njia ambazo walikuwa wakizitumia zikaonekana kugonga mwamba jambo ambalo liliwakatisha tamaa wanaume wengi. Catherine akaonekana kuwa msichana wa tofauti sana katika chuo kile, wasichana wengi wazuri ambao walikuwa wakisoma chuoni hapo walionekana kuwa radhi kuzipandisha juu sketi zao kwa wanaume katika kipindi ambacho walikuwa wakionyeshewa fedha lakini kwa Catherine hali ilionekana kuwa tofauti sana.

Hakuwa akienda katika pati yoyote ya usiku ambazo marafiki zake walikuwa wakimtaka kwenda pamoja nae, hakuwa akienda disko kwa ajili ya kuiburudisha nafsi yake katika kipindi ambacho marafiki zake walikuwa wakienda huko, yeye, alikuwa akipenda kushinda katika chumba alichokuwa akiishi pamoja na marafiki zake hapo hapo chuo.

“Au huyu msichana ameokoka?” Msichana mmoja alimuuliza mwenzake kuhusiana na Catherine.
“Wala hajaokoka. Kwanza sijawahi kumuona akienda kanisani, cd zake ambazo mara nyingi huwa anazikiliza ni zile zilizojaa nyimbo za kidunia. Wala hajaokoka kabisa” Msichana mwingine alijibu.
“Sasa mbona amekuwa hivi?”
“Nadhani kwa sababu ya msimamo wake tu”
Hiyo ndivyo ilivyokuwa chuoni hapo, wasichana wengi walikuwa wakifikiri kwamba Catherine alikuwa ameokoka kutokana na aina ya maisha ambayo alikuwa akiishi chuoni hapo kumbe hali ilikuwa tofauti kabisa. Katika kipindi chote toka amalize kidato cha nne hakuwahi kwenda kanisa, katika siku ambazo alianza kufanya mapenzi na Samuel shuleni ndicho kilikuwa kipindi cha mwisho kukanyaga miguu yake kanisa.
Msimamo wake mkubwa ambao alikuwa amejiwekea katika maisha yake ndio uliwafanya watu wengi kujua kwamba msichana huyo alikuwa miongoni mwa watu waliokuwa wameokoka, watu ambao hawakutaka kabisa kufanya dhambi. Kwa mtazamo, Catherine alionekana kuwa mtu wa dini japokuwa ukweli ulikuwa ni kwamba dini aliyokuwa nayo ilikuwa imempitia kushoto kabisa.
“Leo kuna sherehe ya kuzaliwa ya Pedeshee Sam” Jamala alimwambia Susan, msichana ambaye alikuwa akiishi ndani ya chumba alichokuwa akiishi Catherine.
“Mmmh! Sipati picha huko jinsi mambo yatakavyokuwa. Itafanikia katika jumba lake lile lile la kifahari?” Susan aliuliza huku akionekana kushtuka.
“Kama kawaida. Kutakuwa na mambo mengi sana usiku wa leo. Kama vipi twende, kiingilio hakuna, ni bure kabisa” Jamala alimwambia Susan.
“Lazima niende, nadhani naweza nikapata hata fedha kidogo za kusogeza siku. Wewe vipi Catherine?” Susan alisema na kisha kumgeukia Catherine ambaye alikuwa kitandani na kumuuliza.
“Kuhusu nini?”
“Kwenda kusherehekea na Pedeshee sam. Au hautaki?” Susan alimjibu na kumuuliza.
“Hapana. Siwezi” Catherine alitoa jibu lililomfanya Susan kupiga hatua kukisogelea kitanda alichokuwa amelalia.
“Mbona unakuwa hivyo Catherine? Yaani kila siku umekuwa mtu wa kukaa ndani tuuu na hautaki hata kutoka kwenda sehemu mbalimbali. Usifanye hivyo, wakati mwingine uwe unatoka, yaani hata kutupa kampani sisi wenzako. Urafiki gani huo, kila siku unataka kututenga. Wewe unapotuambia twende na wewe sehemu yoyote ile tunakwenda nawe, haijalishi iwe nzuri au mbaya, ila wewe tukikwambia uongozane nasi, hautaki, sasa urafiki gani huo? Kwani ukienda huko tutakupa mwanaume? Kwani ukienda huko tutakulazimisha unywe pombe? Kwani tukienda huko tutakulazimisha ucheze muziki? Hapana, tutachohitaji ni kampani yako tu, nasi tujue kwamba tuna rafiki ambaye anatujali na kutusikiliza kama sisi tunavyomsikiliza” Susan alimwambia Catherine.
Susan hakuishia hapo, aliendelea kuongea maneno mengi ambayo yalimaanisha kumpa lawama Catherine kwa kile ambacho alikuwa akiwafanyia. Maneno yale yakaonekana kuwa mwiba moyoni mwa Catherine ambaye baada ya dakika kadhaa akakubaliana nao kwenda katika sherehe ya kuzaliwa ya huyo mtu ambaye alikuwa akijiita Pedeshee Sam, mwanaume ambaye alijulikana kuwa na fedha nyingi katika wakati huo, mwanaume ambaye alikuwa kivutio kwa wanawake wengi, hasa wanavyuo.
****
Katika mwezi huo wa nane, nchi ya Malaysia ilikuwa yenye baridi kali, watu wengi ambao walikuwa wametoka katika nchi mbalimbali barani Afrika katika kipindi hicho walikuwa wakivaa makoti mazito au masweta ambayo yalikuwa na uwezo wa kuzuia baridi lile. Walipoteremka kutoka katika ndege ile, moja kwa moja wakaanza kupiga hatua kuelekea katika jengo la uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Kuala Lumpur uliokuwa katika jiji hilo kubwa la Kuala Lumpur.

Mpaka katika kipindi hicho walichoanza kupiga hatua katika ardhi ya nchi ya Malaysia hawakujua ni kitu gani ambacho walitakiwa kukifanya kwa kuona kwamba kama wangeendelea kwenda na abiria wale basi wangeishia katika sehemu ya kuchunguzia mabegi na hatimae madawa yao ya kulevya kukamatwa na hivyo kuingia matatizoni.

Huku wakiwa wamebakiza hatua kumi kabla ya kuingia katika mlango wa kutokea katika sehemu ambayo wangetakiwa kuyaacha mabegi yao madogo kuungana na makubwa na kisha kuchunguzwa, wakatolewa katika mstari wa abiria wale na watu ambao wala hawakuwa wakiwafahamu na kisha kupelekwa pembeni.
“Are you Samuel and Sadiki (Nyie ni Samuel na Sadiki)” Mwanaume mmoja kati ya wanaume watatu ambao waliwavuta pembeni waliwauliza huku wakiwaangalia.

“Yeah” Samuel alijibu.
“Lets go this way (Twendeni njia hii)” Mwanaume huyo aliwaambia na kisha kuanza kuondoka nao. Wakaingia ndani ya jengo la uwanja wa ndege na kutokea katika sehemu iliyokuwa na mlango wa V.I.P na kisha kupitishwa.
Kila kitu ambacho kilikuwa kikiendelea kilionekana kuwa katika mchongo mkubwa ambao ulikuwa umechezwa na matajiri tu ambao walikuwa wakihusika na uuzaji wa madawa ya kulevya. Khaled alionekana kuwa mwanaume ambaye alikuwa na mtandao mkubwa, mtandao ambao ulimfanya kupanga mbinu mbalimbali na wakuu wa nchi nyingi nje ya Afrika. Mara baada ya kufanikiwa kuvuka salama, wakachukuliwa mpaka katika gari na safari kuanza.

Wote walionekana kushangaa, hawakuamini kama kulikuwa na kazi sana kuvuka katika uwanja wa ndege namna ile, ndani ya mioyo yao waliona kwamba kama wangeanza biashara hiyo basi wangefanikiwa kuifanya kwa wepesi kupita kawaida. Ndani ya gari, wote walikuwa kimya, mabegi yao hawakutaka kumwachia mtu yeyote ayashike, walikuwa wameyashika vilivyo na hawakutakiwa kuyaachia.

Huku safari ikiendele, macho yao walikuwa wameyaelekeza nje huku wakiangalia mandhari mazuri ya jji la Kuala Lumpur kwa jinsi ulivyokuwa ukionekana. Idadi kubwa ya watu ambao walionekana kuwa bize kufanya mambo yao ilikuwa ikionekana kuwashangaza sana. Katika barabara hiyo ya Mupush 23 kulionekana kuwa na idadi kubwa ya watu ambao walionekana kuwa kama kwenye maandamano kiasi ambacho magari ambayo yalikuwa yakitumia barabara hiyo kutembea kwa mwendo wa taratibu sana.

Barabara hiyo ilikuwa ikielekea mpaka Kajang, sehemu ambayo watu waliokuwa wakiishi huko walikuwa matajiri wakubwa. Kutoka uwanja wa ndege mpaka Kajang walichukua zaidi ya dakika arobaini na tano na ndipo wakaweza kuingia ndani ya jumba moja kubwa na la kifahari ambalo lilionekana kukamilika kwa kila kitu. Kulikuwa na bwawa kubwa la kuogelea, kamera nyingi za CCTV pamoja na walinzi ambao walikuwa wamezagaa katika kila pembe ya nyumba hiyo huku mikononi mwao wakiwa na bunduki.

Kwa mtazamo tu, tayari walikwishafahamu kwamba mtu ambaye alikuwa anamiliki jumba lile alikuwa mtu mwenye fedha ambaye alikuwa akiuza sana madawa ya kulevya na alionekana kutokuwa mtu mwenye huruma hata kidogo. Bunduki ambazo zilishikwa na walinzi wale zilionekana kuwatisha kupita kawaida.

Wakaingia hadi ndani ya jengo la nyumba ile kubwa na kisha kutulia. Macho yao hayakutulia sehemu moja, yalikuwa yakiangalia katika kila kona ya sebule ile walipokuwa. Muonekano mzuri wa sebule ile ukaonekana kumvutia kila mtu mahali pale kiasi ambacho mioyo yao ikatamani sana na wao kuanza kuuza madawa yao wenyewe na si kuwa wafanyakazi wa Khaled.

Baada ya dakika kadhaa, mwanaume mmoja ambaye alikuwa na ndevu nyingi akatokea mahali hapo. Kwa heshima wakasimama na kisha kumsalimia. Mwanaume yule alionekana kuwa mwenye furaha tele, hakuamini kama mfanyabiashara mwenzake, Khaled angeweza kukamilisha ishu yote kuhusiana na biashara ya madawa ya kulevya.
Kitu alichokifanya mzee yule ni kujitambulisha kwao kwamba alikuwa ni mzee Carlos, mtu ambaye alikuwa akisifika sana nchini Malaysia kwa kufanya biashara nyingi za magendo kwa kuwa viongozi wengi wa serikali walikuwa mikononi mwake.

Mzee Carlos alikuwa tajiri mkubwa sana nchini Malaysia, tajiri ambaye alikuwa akisifika sana kutokana na wema wake wa kuwasaidia watu waliokuwa katika matatizo mbalimbali. Mzee huyu alikuwa akimiliki kampuni nyingi ambazo zilikuwa zikimuingizia fedha nyingi, ukiachana na kampuni hizo, pia alikuwa na viwanda vingi ambavyo vilikuwa vikitengeneza pombe pamoja na vinywaji vingine.

Kuhusiana na kilimo, mzee Carlos alikuwa akimiliki mashamba mengi ya mpunga pamoja na mazao mengine ambayo kila siku yalikuwa yakiendelea kumuingizia kiasi kikubwa cha fedha. Mzee Carlos hakuishia hapo, yeye ndiye alikuwa mtu pekee ambaye alikuwa akimiliki zaidi ya hoteli saba ndani ya nchi ya Malaysia, Mongoria, China na Indonesia.
Jina la mzee Carlos lilikuwa kubwa ndani ya nchi ya Malaysia, kila raia wa nchi hiyo alikuwa akimfahamu mzee huyo ambaye kadri siku zilivyokuwa zikizidi kwenda mbele na ndivyo ambavyo alivyokuwa akizidi kupata utajiri zaidi na zaidi. Heshima yake ikaongezeka. Alichokuwa akikifanya kila siku ni kuongeza biashara zake nyingine ambazo zilionekana kumuingizia kiasi kikubwa cha fedha na kuzidi kuweka heshima.

Japokuwa mzee Carlos alikuwa akifanya biashara nyingi za kihalali lakini katika upande wa pili alikuwa na biashara nyingine ambayo ilikuwa ikimuingizia kiasi kikubwa zaidi, biashara hii ilikuwa ni madawa ya kulevya. Mara kwa mara mzee Carlos alikuwa akinunua madawa ya kulevya kutoka kwa wafanyabiiashara wengi kutoka katika nchi nyingine, wauzaji ambao alikuwa akiwalipa kiasi kikubwa cha fedha ambacho kilimfanya kuvutiwa na kila mfanyabiashara wa madawa yale.

Alifahamiana na Khaled katika kipindi kirefu cha nyuma, kipindi ambacho alikuwa nchini Iraq na kisha nae kuomba kufanya nae biashara ambayo aliamini ingezidi kumuingizia kupita kawaida. Kwa Khaled hilo wala halikuonekana kuwa tatizo kabisa, kwake kufanya biashara na wafanyabiashara mbalimbali duniani kulionekana kumuingizia kiasi cha fedha kupita kawaida.

Mara kwa mara Khaled alikuwa akiyapata madawa yake ya kulevya kutoka Brazil na Mexico ambayo kila alipokuwa akija nayo Tanzania, nae alikuwa akiyasafirisha kwa watu wengine. Katika kipindi cha kuyasafirisha madawa ya kulevya kutoka katika nchi hizo hakuwa akitumia ndege kwa sababu alikuwa akichukua mzigo mkubwa, usafiri pekee ambao alikuwa akiutumia ulikuwa ni meli.

Ukaribu wao ukaongezeka na kuwa wafanyabiashara ambao walikuwa wakiuziana madawa ya kulevya kiasi ambacho wakaonekana kuaminiana kupita kawaida. Vijana wengi ambao walikuwa wakifanya kazi kwa Khaled walikuwa wakifahamiana na mzee Carlos ambaye hakutaka kusikia wala kuambiwa kuhusiana na Khaled ambaye alikuwa amefanya nae biashara kwa zaidi ya miaka mitano.

Siku hiyo alikuwa amekutana na vijana wengine, vijana ambao walikuwa wametumwa na Khaled kumpelekea madawa ya kulevya, vijana ambao kwa kuwaangalia tu walionekana kuwa wajanja. Muda mwingi mzee Carlos alikuwa akitabasamu, kila alipokuwa akiwaangalia alikuwa akijisikia uhuru na amani kwa kuona kwamba vijana wale wangeweza kuendesha biashara ya Khaled kama alivyokuwa akisisitiza.

“Khaled aliniambia kuhusu ninyi, mnaonekana kuwa vijana hodari ambao hamuonekani kuwa wazi kumtaja bosi wenu. Vizuri sana” Mzee Carlos aliwaambia huku akitoa tabasamu.
“Hakuna haja ya kumtaja hata kama tutakuwa katika hali ipi. Yeye ndiye ambaye anatufanya tuwe hivi tulivyo, tumejitoa kufanya kazi kwa asilimia mia moja” Samuel alimwambia mzee Carlos ambaye alionekana kufarijika.
“Vijana wengine huwa wapumbavu sana, yaani wakibanwa kidogo tu, wanazungumza kila kitu. Watu kama hao hawafai kufanya biashara hii” Mzee carlos aliwaambia huku bado tabasamu lake likiendelea kubaki usoni mwake.
“Kamwe hatuwezi kumtaja wala kumsaliti. Yeye ni bosi wetu na milele atakuwa bosi wetu” Sadiki alisema huku akionekana kumaanisha kile alichokuwa akikisema.

Hiyo ndio ilikuwa safari yao ya kwanza kutoka nje ya bara la Afrika kwa ajili ya kuuza madawa ya kulevya. Kuanzia hapo, wakaanza kupewa safari mbalimbali za kusafirisha madawa. Katika kila safari ambayo walikuwa wakizifanya, walikuwa wakitumia muda mwingi kuzoeana na wateja mbalimbali ambao walikuwa wakifanya biashara na Khaled.
Ndani ya miezi nane, walikuwa wamekwishazoeana na wafanyabiashara wengi ambao walikuwa wakihitaji madawa ya kulevya. Majina yao yakaanza kuzoeleka katika masikio ya wanunuaji wa madawa ya kulevya. Samuel na Sadiki hawakuonekana kuwa na haraka, katika kipindi hicho walikuwa wakiendelea kuwazoea watu mbalimbali.
Katika safari zote za nchini Brazil na Mexico ambako walikuwa wakienda kwa ajili ya kuchukua madawa ya kulevya, Samuel na Sadiki walikuwa wakiendelea kufahamiana na watu mbalimbali huku lengo lao katika kipindi hicho likiwa ni lile lile, kuzijua njia zote ambazo walitakiwa kuzitumia katika kipindi ambacho wangeanza kazi ya kuuza madawa katika nchi mbalimbali duniani.

Samuel na Sadiki wakajikuta wakizidi kupata jina hata zaidi ya bosi wao ambaye alikuwa akiwatuma kila mwezi, wakafanikiwa kusafiri katika nchi nyingi duniani, ulinzi ambao walikuwa wakiwekewa katika viwanja mbalimbali vya ndege ulionekana kuwatosha sana, kwao, walijiona kuwa kama wafalme ambao walitakiwa kuheshimika katika kila sehemu ambazo walikuwa wakikanyaga.
“Mwaka umepita. Yaani bado tu tunatakiwa kusubiri zaidi?” Sadiki alimuuliza Samuel.
“Wewe unaonaje?”
“Nahisi kama tutachelewa vile. Kwa nini tusikamilishe kila kitu kwa kipindi hiki?”
“Kumbuka kwamba hatutakiwi kuwa na haraka hata kidogo. Hii ishu inakuwa mdogo mdogo mpaka kinaeleweka” Samuel alimwambia Sadiki.
“Kwa hiyo tuendelee kusibiri zaidi?”
“Hapana. Kama kusubiri tumekwishasubiri. Tukifika, tuhakikishe tunakamilisha kila kitu” Samuel alimwambia sadiki.
“Sasa tumuue kwa kifo gani?”
“Tutajua huko huko tukirudi Tanzania” Samuel alimwambia Sadiki.

Huo ndio ulikuwa mpango ambao walikuwa wameupanga kwa wakati huo, kitu ambacho walikuwa wakikihitaji ni kumuua Khaled na kisha kuiweka biashara ile chini ya mikono yao. Kitendio cha kuagizwaagizwa sana na Khaled kilionekana kuwachosha kupita kawaida, mbaya zaidi walikuwa wamekwishagundua kwamba Khaled alikuwa akiingiza kiasi kikubwa sana kupitia biashara zile ambazo alikuwa akiwatuma kupeleka au kuchukua madaya ya kulevya.

Katika kipindi hicho wakaonekana kuchoka, hawakutaka tena kusafirisha madawa kwenda katika nchi yoyote ile, kitu ambacho walikuwa wakikitaka katika kipindi hicho ni kumuua Khaled na wao wawe mabosi wa biashara ile ambayo ilikuwa ikiingiza sana fedha. Wakaweka makubaliano juu ya mpango wao huo ambao ulikuwepo vichwani mwao toka zamani kwamba ilikuwa ni lazima wamuue Khaled na mambo mengine kufuata. Kwa wakati huu hakukuwa na mtu ambaye alilipinga hilo kwani kama kutumika chini ya mikono ya Khaled walikuwa wametumika vya kutosha na sasa waliona kuwa muda wao wa ukombozi.

Waliposhuka katika ndege ya Qatar wakitoea nchini Urusi kupeleka madawa, moja kwa moja wakaingia katika gari la Khaled ambalo liliika mahali hapo na kuwachukua huku kukiwa na dereva ambaye walikuwa wakifahamiana nae sana. Ndani ya gari, hawakuongea kitu chochote kile, muda wote walikuwa kimya huku kila mmoja akifikiria lake. Vichwa vyao vilikuwa vikifikiria mauaji ambayo walitakiwa kuyafanya katika kipindi ambacho wangekuwa nchini Tanzania, mauaji ambayo yangewafanya kupanda daraja la juu zaidi, badala ya kuitwa wafanyakazi basi wangeweza kuitwa mabosi.

Je, wataweza kumuua Khaled?
 
SEHEMU YA 16

Kila kitu ambacho walikuwa wakitamani kuwa nacho katika kipindi hicho walikuwa nacho kupitia mauaji na dhuluma ambayo walikuwa wameifanya. Kwao, fedha zikaonekana kuwa kila kitu, biashara ya madawa ya kulevya ambayo walikuwa wakitaka kuimiliki ikaonekana kuanza kuwa yao. Wafanyabiashara wengi ambao walikuwa wakishirikiana na Khaled katika kuuza madawa ya kulevya wakaonekana kuwa na huzuni kupita kawaida, hawakuamini kama mtu wao ambaye walikuwa wakifanya nae biashara alikuwa amekufa katika ajali ya gari, ajali ambayo ilionekana kuwa ya kizembe kupita kawaida.

Kwa kuwa Khaled hakuwa na ndugu, Samuel na Sadiki ndio ambao wakawa wamiliki wa biashara hiyo na kila kitu ambacho Khaled alikuwa akimiliki. Kama alivyowafanyia Khaled, nao wakatafuta vijana ambao walikuwa tayari kuwafanyia biashara ile kwa kuwasafirishia katika nchi nyingine. Kuwapata wala haikuwa kazi kubwa kutokana na vijana wengi kupenda kufanya kazi haramu na kuingiza fedha za haraka haraka, wakawapata vijana wawili, Joram na Ignas ambao walijitolea kufanya biashara pamoja nao.

Hao ndio vijana ambao walikuwa wakiwasafirisha kuelekea katika nchi nyingine na kisha kufanya biashara ya madawa ya kulevya ambayo waliamini kwamba ingewaingizia fedha nyingi kupita kawaida. Vijana wale wakawafundisha mambo mengi juu ya kusafirisha madawa ya kulevya katika nchi nyingine huku wakiwaahidi kuwa nyuma yao kwa kuwatengenezea mazingira yote mazuri ya kufanyia kazi.

Biashara haikusimama, kila siku walikuwa watu wa kuwa bize kuwasiliana na wafanyabiashara wenzao kutoka katika nchi mbalimbali. Katika kipindi hiki ndicho ambacho waliamua kuongeza matawi zaidi ya kusafirishia biashara yao kwa kutambua makosa ambayo Khaled alikuwa akiyafanya, wao wakaamua kuyatatua makosa yale jambo ambalo liliwafanya kuendelea zaidi katika biashara hiyo.

Kila kitu ambacho walikuwa wakikihitaji walikuwa wamekwishakipata, ndani ya miezi minne tayari walikuwa na fedha nyingi na bado walikuwa wakiendelea kuingiza fedha kama kawaida yao. Wakawa wanaishi maisha ya starehe, maisha ambayo yalikuwa yakijumusiha kwenda kwenye viwanja vya starehe pamoja na kulala na wasichana huku kila mmoja akiwa makini kutumia kinga.

Maisha yakawa yamebadilika, Samuel na Sadiki hawakuwa watu wa kulala chumba kimoja kama ilivyokuwa zamani kabla ya kuwa wafanyakazi wa Khaled, katika kipindi hiki kila mmoja alikuwa na maisha yao. Nyumba ambayo alikuwa akiishi Khaled wakaamua kuiuza na kila mtu kununua nyumba yake ya kifahari pamoja na magari.

Biashara ile haramu ikaonekana kuwaingizia fedha nyingi jambo ambalo liliwafanya kutajirika kila siku. Hakukuwa na aliyekuwa akikumbuka kwamba katika kipindi cha nyuma walikuwa watu wa dini kupita kawaida, watu ambao wazazi wao walikuwa wakitamani wawe viongozi wa dini katika nyumba za ibada. Maisha ya starehe yakawateka na kuwapoteza kabisa, hawakuzipenda nyumba za ibada hata mara moja, kwa kifupi ni kwamba walichukia kila kitu ambacho kilikuwa kikikufanya kumsifu Mungu.

Siku zikaendelea kukatika mpaka kufika kipindi ambacho wakaamua kujitegemea katika biashara zao. Kwa kuwa walikuwa wamekwishapata mafanikio makubwa, wakagawana na kisha kuanza kufanya biashara kila mtu kivyake. Mafanikio yakazidi kuongezeka, majina yao yakaanza kusikika masikioni mwa watu kwamba walikuwa wakiingiza kiasi kikubwa cha fedha na walikuwa miongoni mwa watu waliokuwa na fedha nyingi nchini Tanzania huku wakiwa na umri mdogo, chini ya miaka ishirini na tano.

Ili kutaka kuwapa upofu watu wengine hasa serikali, wakaamua kuanzisha biashara mbalimbali kama kufungua maduka mengi ya nguo pamoja na kufungua kampuni nyingi ambazo waliamini kwamba zingekuwa zikiwaingizia kiasi kikubwa cha fedha. Watu wakapigwa upofu, hakukuwa na mtu ambaye alikuwa akijua kwamba watu hao walikuwa wakifanya biashara ya madawa ya kulevya, biashara ambayo walikuwa wameanza nayo kitambo.

Baadhi ya watu ambao walikuwa na vyeo vikubwa wakawa katika upande wao kiasi ambacho wala halikuwa suala kubwa kuhusu kusafirisha madawa ya kulevya kwenda katika nchi nyingine. Kwa Sadiki ndiye ambaye alionekana kuchanganyikiwa zaidi katika kipindi hicho, wanawake wakaonekana kumlevya hata zaidi ya Samuel ambaye kipindi cha nyuma alikuwa mtu wa wasichana kupita kawaida.

Kwa kila msichana mrembo ambaye alikuwa akipita mbele yake, Sadiki alikuwa akitembea nae. Katika kipindi hicho alichokuwa na fedha wala hakumuogopa msichana yeyote yule, fedha ikamfanya kujiamini kupita kawaida kiasi ambacho hakuonekana kujali itu chochote kile. Alihakikisha kwamba analala na wanavyuo mbalimbali ambao walikuwa wakivuma sana, alihakikisha analala na wanawake ambao walikuwa wakizipenda sana fedha katika maisha yao, kuhusu kugawa fedha kwa wanawake, Sadiki hakuwa mchoyo, mara kwa mara alikuwa akimwaga fedha alivyotaka.

“Utakufa” Samuel alimwambia Sadiki.
“Hata wewe utakufa” Sadiki alimwambia Samuel.
“Nipo serious Sadiki, utakufa, wanawake hawafai kabisa. Huu ugonjwa unaousikiasikia unaweza kukupata na kuyaona maisha machungu” Samuel alimwambia Sadiki.
“Unazungumzia UKIMWI? Hahaha! Hakuna kitu kama hicho, huu ugonjwa ni wa kutunga tu, wala haupo” Sadiki alimwambia Samuel ikiwa mwaka 2003.
“Sikiliza Sadiki, hakuna kitu cha kudanganya kuhusu ugonjwa huu”
“Hivi toka umetangazwa umekwishawahi kumuona mtu yeyote akiugua ugonjwa huu?” Sadiki alimuuliza Samuel ambaye akabaki kimya kwa muda.
“Mbona wapo wengi tu”
“Hakuna kitu kama hicho”
“Usipuuzie Sadiki”
“Najua. Ila usiamini kitu usichowahi kukiona. Ona na ndio uamini”
“Hayo ni makosa. Hatutakiwi kuishi hivyo”
“Kwani tatizo lipo wapi? Wewe una fedha zako, mimi nina fedha zangu, kuna tatizo hapo?” Sadiki alimuuliza Samuel.
“Fedha si kila kitu Sadiki”
“Umeanza. Kwa hiyo unataka kuniambia nini sasa? Au unataka kuanza kurudi tena kanisani na kisha uanze kuhubiri kama baba yako?” Sadiki alimiiliza Samuel huku akionekana kumshangaa.
“Hapa sizungumzii kuhusu kanisa, sizungumzii kuhusu kuhubiri, hapa ninazungumzia kuhusu UKIMWI” Samuel alimwambia Sadiki.
“Ok! Nimekuelewa baba mchungaji. Nitaacha tabia hii” Sadiki alimwambia Samuel na kisha kusimama, akachukua chupa iliyokuwa na pombe na kuanza kunywa.

Sadiki hakuishia hapo, bado alikuwa akiendelea na tabia yake ya kuchukua kila mwanamke ambaye alikuwa akimuona kumfaa. Samuel alijitahidi kuongea sana lakini mwisho wa siku akaonekana kuchoka jambo ambalo lilimfanya kubaki kimya na kutaka kuona ni kitu gani ambacho kingetokea katika maisha ya baadae. Bado fedha zilikuwa zikiwasumbua, walikuwa na fedha nyingi sana kiasi ambacho wakaamua kufanya sherehe mbalimbali na kisha kuwaita watu na kusherehekea pamoja nao huku wakimwaga fedha kila wakati. Warembo wakaonekana kuwanyenyekea, fedha walizokuwa nazo zikaonekana kuwa ulimbo kwa wasichana wengi, hasa wanavyuo.

Kwa Samuel hakuonekana kupenda wanawake katika kipindi hicho, kama wanawake alikuwa amekwishatembea na wanawake wengi lakini mwisho wa siku hakuona kama kulikuwa na utofauti wowote ule. Ukiachana na hilo, ugonjwa wa UKIMWI ambao ulikuwa ukuvuma kila siku ndio ambao ulionekana kumuogopesha kupita kawaida. Taarifa mbalimbali za habari ambazo zilikuwa zikitangaza kuhusiana na ugonjwa huo zikaonekana kumuogopesha, akatokea kuwahofia wanawake japokuwa alijua kwamba kulikuwa na mipira ya kinga.

“Kesho ni sikukuu yangu ya kuzaliwa. Nahitaji watu wengi wa kuwa mahali hapa” Samuel alimwambia Sadiki.
“Mbona ghafla hivyo?”
“Nilisahau kama ni kesho, nimekuwa bize sana katika kipindi hiki. Naomba unitafutie watu wengi wa kuja kuhudhuria” Samuel alimwambia Sadiki ambaye akachukua simu yake na kisha kuanza kuwasiliana na watu mbalimbali hasa wasichana wengi huku akiwataka kufika katika nyumba ya Samuel iliyokuwa Mbezi Beach, Africana kwa ajili ya kusherehekea katika siku yake ya kuzaliwa pamoja na kuwaita marafiki zao mbalimbali.
“Itakuwa asubuhi, mchana au usiku?” Sauti ya msichana mmoja iliuliza,
“Ile ni sherehe ya siku ya kuzaliwa ya mtu mzima na si ya mtoto. Itafanyika usiku, watoto ndio wanaofanya asubuhi na mchana” Sadiki alimwambia msichana huyo.
Kuhusu kuwaita watu mbalimbali halikuwa tatizo, Sadiki alikuwa akijitahidi kadri ya uwezo wake kuwaita watu mbalimbali katika sherehe ile ambayo ikawafanya watu wengi kufahamu kile kilichokuwa kikienda kutokea siku ya kesho.
“Kama kawaida. Warembo watakuwa wa kumwaga” Sadiki alimwambia Samuel.
“Hakuna noma. Itakuwa poa sana”
“Kila siku nakwambia lakini unanibishia, vitu vingine bila warembo havipendezi kaka” Sadiki alimwambia Samuel ambaye akakubaliana nae.

Siku ya sherehe ya kuzaliwa kwa Samuel ikawadia, watu wakajazana katika uwanja wa nyumba yake kubwa na ya kifahari, wasichana wengi kutoka vyuoni walikuwa ndani ya eneo la nyumba hiyo huku kila mmoja akiwa amejaribu kuvaa na kupendeza kupita wengine. Wapo ambao walikuwa wamevaa sketi fupi ambazo ziliachia mapaja yao nje, wapo ambao walikuwa wamevaa sketi ndefu lakini vifua vyao havikuwa vimestiliwa vilivyo na ukiachana na hao, wapo pia ambao walikuwa wamevaa suruali za jinsi, kila msichana katika kipindi hicho alikuwa amejitahidi kuvaa na kupendeza zaidi ya mwenzake.

Wanaume hawakukosa, nao walikuwepo mahali hapo huku wakiwa wamefika kwa ajili ya kusherehekea pamoja na Samuel ambaye alionekana kuwa na furaha kila wakati. Sadiki alikuwa bize, kila wakati alikuwa akijiweka karibu na wanawake, hayo ndio maisha ambayo aliamua kuishi kwa kipindi hicho, kupenda wanawake kama mchungaji anavyopenda kwenda kanisani.

Muziki ulikuwa ukisikika kwa sauti ya juu huku kila mmoja akiwa bize na vinywaji mikono mwao. Wale ambao walikuwa wakitaka kula, siku hiyo walikuwa huru kula mpaka kusaza, wale ambao walikuwa wakitaka kunywa, bia na soda zilikuwepo mahali hapo, walikunywa mpaka kuacha na hakuna kilichopungua hata kidogo.
Watu waliendelea kuburudika mpaka katika kipindi ambacho Samuel akasimama na kisha kuanza kuongea, maneno ambayo alikuwa akiyaongea mahali hapo yalikuwa ni ya kuwashukuru watu tisini ambao walikuwa wameruhusiwa kuingia ndani ya eneo la nyumba hiyo ya kifahari. Kila alipokuwa akiongea, tabasamu lake pana lilikuwa likionekana usoni mwake.

“Endeleeni kuburudika, mkihitaji vinywaji zaidi, vipo na havitokwisha, mkihitaji vyakula, navyo vipo. Na hata wale ambao watataka kulala mahali hapo, vyumba vipo vya kutosha.” Samuel aliwaambia na kisha kuruhusu sherehe kuendelea zaidi huku watu wakizidi kufurahia kwa shangwe.
Mara kwa mara watu walikuwa wakimsogelea Samuel na kumpongeza kwa kutimiza miaka ishirini na nne. Alionekana kuwa kijana mdogo lakini mwenye fedha nyingi sana, fedha ambazo hakudhani kama ingetokea siku yoyote na fedha zile kumuisha. Kila alipokuwa akipongezwa, Samuel alikuwa akitoa shukrani huku katika mkono wake wa kulia akiwa ameshika chupa moja ya pombe ya John Walker.
“Samuel....” Samuel aliisikia sauti ya msichana ikimuita, akageuka nyuma na kunza kumwangalia.
“Samuel...” Msichana yule aliita huku Samuel akibaki amesimama kwa kutaka kumuona msichana huyo karibu zaidi kwani alikuwa kwa mbali kidogo na mwanga haukuwa mkubwa.
“Catherine...” Samuel alijikuta akiita kwa mshtuko.
Kila mmoja akabaki akiwa ameduwaa, Samuel akabaki akimwangalia Catherine mara mbili mbili huku akionekana kutokuamini kama mtu ambaye alikuwa amesimama mbele yake alikuwa Catherine, msichana ambaye alikuwa akitembea nae katika kipindi alichokuwa shuleni. Samuel akashindwa kuvumilia, akajikuta akimsogelea Catherine na kisha wote kukumbatiana.
“Umebadilika Samuel” Catherine alimwambia Samuel.
“Nimekuaje?”
“Umenenepa na umekuwa na mwili, kumbe mpaka jina umebadilisha?”
“Hapana. Bado naitwa Samuel”
“Mbona nimesikia wakikuita kwa jina la Pedeshee Sam?”
“Fedha Catherine. Zote fedha hizi” Samuel alimwambia Catherine.
Moyo wa Samuel ukaonekana kufarijika kupita kawaida. Ni kweli alikuwa ametembea na wanawake wengi katika kipindi cha nyuma lakini kwa msichana Catherine kwake alionekana kuwa msichana wa tofauti sana, kila alipokuwa akimwangalia Catherine, Samuel alikuwa akijisikia amani moyoni mwake, mapenzi juu ya Catherine ambayo yalikuwa yamesahaulika yakaanza kurudi moyoni mwake, tena kwa kasi kubwa sana.
“Umeolewa?” Samuel alimuuliza Catherine.
“Hapana. Wewe umeoa?”
“Hapana. Nisingeweza kuoa na wakati wewe haukuwepo” Samuel alimwambia Catherine.
“Lakini nasikia una fedha nyingi sana, kwa nini usioe?” Catherine alimuuliza Samuel.
“Hapana, sikuwahi kumuona mwanamke aliyekuwa sahihi katika maisha yangu zaidi yako Catherine. Wewe ndiye mwanamke ambaye uliniingiza katika mapenzi, thamani yako bado kubwa moyoni mwangu” Samuel alimwambia Catherine.
“Kwani bado unanipenda?”
“Nadhani kwa sasa hivi ni zaidi ya nilivyokuwa nakupenda” Samuel alimwambia Catherine.
“Ila umechelewa”
“Kwa nini?”
“Nina mpenzi ambaye anajulikana nyumbani” Catherine alimwambia Samuel.
“Unafikiri inaweza kubadilisha chochote kile?”
“Ananipenda na yupo tayari kufanya chochote kwa ajili yangu” Catherine alimwambia Samuel.
“Ila sidhani kama anakupenda kama ninavyokupenda. Kama nilikupoteza miaka mitatu ya nyuma, kwa sasa hivi sitotaka kukupoteza tena, nitataka kukushikilia vilivyo” Samuel alimwambia Catherine.
“Please Samuel...umechelewa”
“Hapana. Nimekuja muda sahihi. Kama ningekuwa nimechelewa, moja ya kidole chako kingekuwa na pete. Ukiona hauna pete, jua kwamba sijachelewa bali nimekuja muda muafaka” Samuel alimwambia Catherine.
“Ila Samuel nil......”
“Naomba nikuulize kitu. Unanipenda?”
“Samuel...Samuel naom.......”
“Haujanijibu”
“Lakini ni laz.......”
“Naomba uniangalie machoni mwangu” Samuel alimwambia Catherine ambaye akaunyanua kidogo uso wake na kumwangalia Samuel machoni.
“Unanipenda?” Samuel alilirudia swali lake.
“Nina mpenzi Samuel....ananipenda”
“Hilo si jibu Catherine. Unanipenda?” Samuel alilirudia swali lake.
Swali lile likatengeneza kitu cha tofauti moyoni mwa Catherine, hapo hapo akaanza kukumbuka maisha yake ya nyuma ambayo alikuwa ameishi pamoja na Samuel, maisha ambayo yaliwafanya kuwa huru ya kupendana kupita kawaida. Kumbukumbu zile ndicho kilikuwa zaidi ya vitu vyote ambavyo vilimfanya Catherine kuona kwamba kutokuwa na Samuel katika kipindi chote hicho kulikuwa na kitu ambacho alikuwa amekikosa moyoni mwake, kitu ambacho aliamini kwamba hata Edmund hakuwa nacho.

“Unanipenda?” Samuel aliuliza swali ambalo likamfanya Catherine kushtuka kutoka katika lindi la mawazo, alipomwangalia Samuel machoni kwa mara nyingine, hakuongea kitu, akahisi kama kulikuwa na kitu ambacho kilikuwa kikimtamanisha kufanya kitu kimoja mahali hapo, kubadilishana mate na Samuel. Bila kutarajia, huku kichwa chake kikiendelea kukumbuka mambo ya nyuma, akakikuta kinywa chake kikianza kubadilishana mate na Samuel, hiyo ikawa mara ya kwanza kumsaliti Edmund, mwanaume ambaye alikuwa akimpenda kuliko mwanamke yeyote katika dunia hii.
“Nakupenda Samuel” Catherine alimwambia Samuel ambaye alionekana kuwa kwenye furaha kubwa, kwake,
Catherine ndiye alikuwa msichana ambaye alikuwa akimpenda na kumhitaji kuliko wasichana wengine. Alitembea na wanawake wengi ila kwa Catherine, thamani yake haikupungua, bado alikuwa akimpenda kupita kawaida na katika kipindi hicho alijiahidi kumpenda zaidi ya alivyokuwa akimpenda katika kipindi cha nyuma huku akiwa hajui kama katika kipindi hicho msichana huyo alikuwa na kijana Edmund na ndio maana alikuwa akimwambia kwamba alichelewa.

Je nini kitaendelea?
Tuonane kesho.
 
SEHEMU YA 17

Catherine akaonekana kubadilika, moyo wake ukaanza kuingiza kitu cha tofauti sana, kitu ambacho alikuwa nacho miaka mitatu iliyopita na katika kipindi hicho kilikuwa kimerudi tena, mapenzi ya Samuel. Catherine alijua fika kwamba katika kipindi hicho alikuwa na mwanaume mwingine ambaye alikuwa akijulikana sana mpaka nyumbani kwao lakini kwa Samuel alijiona kuwa tayari kwa kila kitu.

Moyo wake ulikuwa umegawanyika pande mbili, kulikuwa na upande ambao ulimhitaji sana Edmund lakini kulikuwa na upande mwingine ambao ulikuwa ukimhitaji sana Samuel, upande huo ndio ambao ulikuwa na nguvu sana moyoni mwake. Kwa Samuel, hakupenda fedha zake, kitu ambacho alikuwa akikitaka ni mapenzi ambayo yalionekana kupotea katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita.

Catherine akaonekana kuwa na furaha zaidi, kitendo chake cha kuwa na Samuel kilionekana kumfurahisha kupita kawaida. Kwa Edmund kukaanza kubadilika, mara kwa mara alipokuwa akipigiwa simu Catherine alionekana kukasirika kupita kawaida, mapenzi yake juu ya Edmund yakaonekana kuanza kupungua kabisa kitu ambacho kilionekana kuwa kama maumivu kwa Edmund.

Catherine alipokuwa akiiona simu ya Edmund ikiingia, alikuwa akiikata na hata wakati mwingine alipokuwa akijisikia kuipokea, aliipokea na kuanza kuongea kwa hasira kwamba asimsumbue kwa sababu alikuwa bize sana katika kipindi hicho. Maneno yale yalionekana kuwa kama msumali wa moto moyoni mwa Edmund, hakuamini kama mpenzi wake wa kipindi kirefu, Catherine, msichana ambaye alikuwa akijulikana mpaka kwao ndiye ambaye alikuwa akimfanyia mambo yale.

Mkoani Dodoma, Edmund hakusoma kwa raha, kila siku alikuwa na mawazo juu ya mpenzi wake, Catherine ambaye katika kipindi hicho alikuwa katika mapenzi ya dhati kwa Samuel, mwanaume ambaye alikuwa wa kwanza kwake kuutoa usichana wake katika kipindi ambacho walikuwa shuleni miaka mitatu iliyopita.

Edmund hakutaka kukata tamaa, kila alipokuwa akiisikia sauti ikimwambia kwamba kulikuwa na uwezekano wa Catherine kuwa na mwanaume mwingine, kwake akaonekana kulipinga hilo kwa nguvu zote. Alimjua vilivyo Catherine, alimjua vilivyo jinsi alivyokuwa akimpenda na kumthamini kuliko mwanaume yeyote yule katika dunia hii.
Hali ile ikaendelea zaidi na zaidi, moyo wake ukaonekana kuungua katika maumivu makali sana lakini Edmund aliendelea kuvumilia tu huku akiamini kwamba mpenzi wake alikuwa bize na hivyo hakuhitaji usumbufu wowote ule. Edmund alipoona kwamba maumivu yanaendelea zaidi moyoni mwake, hapo ndipo ambapo akaamua kuwaambia wazazi wake, Bwana Zilikana na mama yake, Bi Elizabeth.

Kwanza wazazi hao hawakuamini kama Catherine alikuwa amefikia hatua ya kubadilika namna hiyo kiasi ambacho hawakutaka kuyaamini maneno ya mtoto wao, Edmund na kumtaka kuchunguza zaidi na zaidi juu ya mabadiliko ya Catherine. Edmund hakutaka kujali sana, akaufuata ushauri wa wazazi wake lakini hali haikuonekana kubadilika kwa Catherine, aliendelea kuwa vile vile, mapenzi yalikuwa yamepungua moyoni mwake.

Hapo ndipo wazazi hao wakaamua kuanza kuelekea nyumbani kwa wazazi wa Catherine na kuamua kuwaambia kile ambacho kilikuwa kikiendelea katika kipindi hicho. Masikoni mwa Bwana Mushi na Bi Maria kitu kile kilionekana kutokuaminika hata ara moja, hawakuamini kama binti yao angeweza kufanya kama vile ambavyo maneno ya wazazi wale wa Edmund yalivyokuwa yakisema.

“Haiwezekani kabisa” Bwana Mushi aliwaambia huku machoni akionekana dhahiri kutokuamini.
“Huo ndio ukweli” Bwana Zilikana alimwambia.
“Hivi mnayafahamu vilivyo mapenzi ambayo watoto wetu walikuwa nayo juu ya mahusiano yao au mnaongea tu?” Bwana Mushi aliuliza.

“Edmund alipotuambia, na sisi hatukuamini kabisa, ila alipoendelea kutuambia zaidi na zaidi, tukaonekana kumuamini kwa asilimia mia moja” Bwana Zilikana aliwaambia.
Bado mioyo yao ilikuwa migumu kuamini kile ambacho kilikuwa kinaendelea katika kipindi hicho, hakukuwa na mtu ambaye aliamini kwamba Catherine angeweza kubadilika namna ile. Japokuwa Bwana Mushi na mkewa, Bi Maria walikuwa wakimfahamu Samuel lakini kwa wakati huo hakukuwa na mtu ambaye aliamini kwamba Samuel huyo ndiye ambaye alikuwa amesababisha hayo yote.

Kilichofanyika mahali hapo ni kumpigia simu Catherine ambaye alihitajika nyumbani hapo kwa ajili ya wazazi kutaka kufahamu kile ambacho kilikuwa kikiendelea katika mahusiano yao. Ndani ya dakika arobaini baada ya kuongea na Catherine, akafika nyumbani hapo na kisha kuwasalimia wote na kukaa kochini huku kichwani akionekana kufahamu kile ambacho alikuwa ameitiwa mahali pale kutokana na uwepo uliokuwepo ndani ya nyumba ile.
“Nini kinaendelea?” Bwana Mushi alimuuliza binti yake.
“Wapi?” Catherine aliuliza.
“Katika mahusiano yenu” Bwana Mushi alimjibu Catherine.
“Hakuna kinachoendelea”
“Usitudanganye Catherine, mbona mwenzako amekuwa akilalamika kwamba umebadilika sana na si kama zamani?” Bwana Mushi aliuliza.
“Mwenzangu nani?”
“Hivi Catherine unataka kujifanya mtoto kwamba haufahamu kitu chochote kile na ni nani tunayemzungumzia mahali hapa?” Bwana Mushi aliuliza huku kwa mbali akionekana kubadilika.
“Unaniambia kwa mafumbo sana baba kiasi ambacho naonekana kutokuelewa” Catherine alimwambia baba yake.
“Tunaongea kuhusu wewe na Edmund” Bi Vaness akaingilia.
“Hakuna kilichobadilika, mambo yapo kama zamani” Catherine alijibu.
“Hapana. Hebu tuambie kinachoendelea”
“Hakuna kitu baba. Kila kitu kipo kama kawaida” Catherine alimwambia baba yake.
Kila alipokuwa akiulizwa juu ya kitu kilichokuwa kikiendelea Catherine alionekana kutokuwa tayari kuongea hali halisi, macho yake yakaonekana kujaa uongo. Kila alipokuwa akiulizwa zaidi hakuonekana kuwa radhi kuzungumzia kitu chochote kuhusiana na ukweli ambao ulikuwa ukiendelea katika maisha yake ya kimapenzi pamoja na Edmund. Wazazi wakaonekana kugundua kwamba kulikuwa na kitu ambacho kilikuwa kinaendelea lakini Catherine hakuonekana kuwa radhi kusema ukweli.
“Unajua kwamba dunia haina siri hii?” Bwana Mushi alimuuliza binti yake.
“Nafahamu baba. Na ninafahamu kwamba kila chenye mwanzo kina mwisho” Catherine alimwambia baba yake.
“Umemaanisha nini?”
“Hakuna kitu baba. Nadhani natakiwa kuondoka kurudi chuo” Catherine aliwaambia.
Catherine akaonekana kubadilika, hakuonekana kuwa kama alivyokuwa katika kipindi cha nyuma, majibu yake pamoja na muonekano wake vilionekana kuwa vitu viwili ambavyo vilikuwa tofauti kabisa na jinsi alivyokuwa katika kipindi cha nyuma. Wote wakajua kwamba kulikuwa na kitu ambacho kilimtokea Catherine ambaye hakuonekana kuweza kuyaficha mabadiliko ambayo alikuwa nayo. Hawakutaka kumzuia, wakamuacha kuondoka mahali hapo.
“Mmegundua nini?” Bwana Zilikana, baba yake Edmund aliuliza.
“Catherine amebadilika sana” Bwana Mushi alijibu huku akionekana kuwa na mshangao.
“Kuna nini? Waligombana au?” Bi Elizabeth aliuliza.
“Sijui. Yaani sijui ni kitu gani kinachoendelea mpaka hali kuwa hivi...Catherine amebadilika, tena mabadiliko makubwa” Bi Maria alisema.

Huo ndio ukweli uliopo, Catherine alikuwa amebadilika kupita kawaida, mabadiliko yake hayakuweza kujificha, yalikuwa yakijionyesha waziwazi mbele ya wazazi wake kitu ambacho kilionekana kumtia wasiwasi kila aliyekuwa akimwangalia pasipo kujua kwamba katika kipindi hicho Catherine alikuwa katika mahusiano na mwanaume ambaye alikuwa nae katika kipindi cha nyuma, mwanaume ambaye aliutoa usichana wake, Samuel.

Maisha yaliendelea kusonga mbele, Catherine na Samuel wakaonekana kuwa pamoja zaidi, mara kwa mara Samuel alikuwa akiondoka nyumbani kwake Mbezi Beach na kuelekea chuo kikuu cha Dar es salaam kwa ajili ya kumuona mpenzi wak e ambaye alikuwa akimthamini sana, Catherine. Chuoni, kila msichana ambaye alikuwa akimuona Samuel, alimuonea wivu Catherine kwa kuwa na mwanaume kama Samuel, mwanaume ambaye alikuwa akijulikana kuwa na fedha nyingi katika kipindi hicho.

Catherine hakuwa mtu wa kukaa sana chuoni, mara kwa mara alikuwa akiondoka chuoni hapo na kisha kwenda kulala nyumbani kwa Samuel. Maisha yale yaliendelea, wakaanza kuishi kama mume na mke, kila siku walikuwa pamoja nyumbani huku wakifanya kila kitu ambacho mke na mume walitakiwa kukifanya.
“Nataka tuoane” Catherine alimwambia Samuel.
“Wewe unataka lini?”
“Nikimaliza chuo”
“Chuo utamaliza mwaka gani?”
“Bado miaka miwili mbele”
“Duh! Mbona mbali sana?”
“Ndio hivyo, inatubidi tuvumiliane mpenzi” Catherine alimwambia Samuel.
“Hakuna tatizo mpenzi” Samuel alimwambia Catherine.
Kadri siku zilivyokuwa zikizidi kwenda mbele na ndivyo ambavyo mapenzi yao yalizidi kuongezeka zaidi na zaidi. Walipendana mpaka kufikia hatua ambayo iliwashangaza hata watu ambao walikuwa wakiwaangalia. Hayo ndio mapenzi yalivyokuwa, katika kipindi cha kufurahi, unayafurahia mapenzi na kujiona kama malkia au mfalme, ila wakati yanapoamua kubadilika, moyo unanyong’onyea na kuumia, katika hilo, hakukuwa na mtu ambaye alikuwa akilifikiri, kila mmoja aliona kama wangeendelea kuwa pamoja mpaka kifo kiwatenganishe kumbe mambo yalikuwa tofauti na mategemeo yao.
****
Mzee Hamidu akaonekana kuchanganyikiwa, mpaka katika kipindi hicho hakujua mtoto wake, Sadiki alikuwa mahali gani. Kila siku alikuwa mtu wa majonzi pamoja na mke wake, Bi Aisha ambaye wala hakuweza kuficha hisia zake juu ya kutoonekana kwa mtoto wao ambaye katika kipindi cha nyuma waliamini kwamba angekuwa Imamu kama alivyokuwa baba yake, ustaadhi Hamidu.

Maisha katika kipindi hicho yalikuwa yamebadilika kabisa, furaha zikapotea mioyoni mwao, hawakuamini kama Sadiki hakuwa ameonekana kwa takribani miezi mitatu. Kitu ambacho walikiona kufaa ni kuwasiliana na mchungaji Mpelele na kisha kuhitaji ushirikiano wao. Familia mbili zikaungana na hatimae kuanza kuwatafuta watoto wao.

Hawakujua ni mahali gani wangeweza kuwapata lakini walikuwa wakitaka kuiridhisha mioyo yao kwamba nao walijaribu kuwatafuta. Wakaanza kuwaulizia kwa marafiki zao lakini huko wala hawakuweza kupata taarifa juu ya mahali ambapo watoto wao walipokuwa jambo ambalo wakati mwingine liliwafanya kuona kama watoto wao walikuwa wamefariki.
Siku zikaendelea kukatika, mwaka wa kwanza ukakatika na mwaka wa pili kuingia, bado hawakuweza kufahamu sehemu ambayo watoto wao walipokuwa mbaya zaidi hata tetesi hawakuweza kuzisikia.

Mioyo yao ikanyong’onyea kupita kawaida, hawakuamini kama watoto wao hawakuwa wameonekana machoni mwao kwa muda wa miaka miwili. Miezi ikakatika na hatimae mwaka wa tatu kuingia, huku ikiwa imebaki miezi minne kabla ya mwaka wa tatu kumalizika, hapo ndipo walipoweza kuwaona watoto wao. Kwanza hawakuamini ila kutokana na picha ambazo walikuwa wakiziona kwenye magazeti hasa ya udaku, wakakubaliana nazo.

Watoto wao walikuwa wamejijengea majina makubwa na kuwa wafanyabiashara ambao walikuwa wanaingiza kiasi kikubwa cha fedha. Hawakuyaamini macho yao, hali ile ikaonekana kuwatia hofu kupita kawaida. Walichokifanya ni kuitana na kisha kukaa chini na kuanza kuyazungumzia mabadiliko waliyokuwa nayo watoto wao.
“Hapana. Nina wasiwasi” Mchungaji Mpelele alisema huku uso wake ukionekana kuwa na wasiwasi.
“Hata mimi mchungaji nina wasiwasi. Usiku ninaota ndoto fulani fulani kuhusiana na mtoto wangu na huo utajiri wake” Ustadhi Hamidu alimwambia Mchungaji Mpelele.
“Kuna kitu, nahisi watakuwa wameingia kwenye dini inayomuabudu shetani” Mchungaji Mpelele alimwambia ustadhi Hamidu ambaye akaonekana kukubaliana nae.
“Kwa hiyo tufanye nini?” Mchungaji Mpelele aliuliza.
“Cha msingi tuonane nao kwanza” Ustadh Hamidu alimwambia mchungaji Mpelele.
Hicho ndicho kilichofanyika, kwa haraka sana wakaanza kwenda katika kampuni moja ya magazeti ya udaku na kisha kuulizia mahali ambapo Samuel na Sadiki walipokuwa wakiishi. Kutokana na majina yao kuwa makubwa ndani ya jiji la Dar es Salaam, wakafanikiwa kuelekezwa mahali ambapo walipokuwa wakiishi na kisha kuwafuata.

Kila mmoja katika kipindi hicho alikuwa na hamu ya kumuona mtoto wake, vichwani mwao hawakuwa na hamu ya kuziona mali ambazo walikuwa nazo, wao walichokuwa wakikitaka ni kuwaona tu ili mioyo yao ifurahi na kuwa na amani. Hawakuchukua muda mrefu mpaka kufika Mbezi Beach ambapo wakaanza kuelekea katika sehemu iliyokuwa na nyumba ya Samuel. Wakajitambulisha kwa walinzi na kisha kuingia ndani.

Samuel alipowaona, kwanza akashtuka, hakuamini kile ambacho alikuwa akikiona, hakuamini kwamba wazazi wake walikuwa wamemuona mara baada ya kuondoka kipindi kirefu kilichopita. Bi Magreth hakuonekana kuvumilia, alichokifanya ni kupiga hatua na kumfuata Samuel, alipomfikia, akamkumbatia huku akianza kutokwa na machozi.
“Samuel....” Bi Magreth aliita huku akionekana kutokuamini macho yake kwamba siku hiyo alikuwa amekutana na mtoto wake.
“Nipo hapa. Usilie mama” Samuel alimwambia mama yake, Bi Magreth.
Samuel hakuwa na jinsi, japokuwa hakuwa akitaka wazazi wake wafahamu mahali alipokuwa akiishi lakini katika kipindi hicho kila kitu kilikuwa wazi kabisa. Alipoona kwamba hata ustadhi Hamidu alikuwa mahali hapo, akampigia simu Sadiki ambaye ndani ya dakika kumi, akawa mahali hapo huku muonekano wake tu ukionekana kuwa na fedha.
Kama alivyofanya Bi Magreth, Bi Aisha akajikuta akisimama na kwa furaha kumkumbatia mtoto wake. Machoni mwake, Sadiki alionekana kuwa mpya, alionekana kubadilika kupita kawaida. Nae machozi yakaanza kumtoka na kujiona kama alikuwa ndotoni ambapo baada ya dakika chache angeshtuka na kujikuta yupo kitandani.

“Hatimae nimekuona tena” Bi Aisha alimwambia Sadiki huku akiwa amemkumbatia.
“Hata nami nashukuru kukuona mama” Sadiki alimwambia mama yake, Bi Aisha.
Hapo ndipo kikao kikawekwa, familia mbili zikaanza kuzungumzia kile kilichokuwa kimetokea. Kitu cha kwanza kabisa, Samuel na Sadiki wakaanza kuomba msamaha kwa kila kitu ambacho kilikuwa kimetokea kwa kisingizio kwamba hawakupenda kile kilichotokea kitokee katika kipindi cha nyuma. Wazazi wao wakaonekana kuwa waelewa, wakawasamehe kwa moyo mmoja.

“Na vipi kuhusu utajiri huu” Mchungaji Mpelele aliuliza.
“Ni habari ndefu sana baba”
“Ni ndefu ambayo haisimuliki Samuel?” Ustaadhi Hamidu aliuliza.
“Si kwamba haisimuliki ila kwa kifupi ni kwamba tulikuwa tukifanya kazi mgodini kule Arusha” Samuel aliwaambia.
“Ikawaje sasa?”
“Ni habari ndefu sana” Samuel aliwaambia.
“Hebu Sadiki tuelezee wewe” Mchungaji Mpelele alimwambia Sadiki.
“Ngoja aelezee yeye” Sadiki alisema kwa kuona kwamba stori yake na Samuel zingeweza kutofautiana.
“Kuna siku tuliingia mpaka kwenye mgodi kama wachimbaji, tulipofika humo, kifusi kikajifukia. Watu kumi na mbili ambao walikuwa pamoja nasi wakafariki dunia” Samuel aliwaambia stori ya uongo ambayo ilikuwa ikianza kuaminika .
“Ikawaje?”
“Kwa sababu tulikuwa tumepata madini, kule chini tukayachukua madini na kuyaweka mdomoni mwa maiti moja” Samuel aliendelea kuwaambia habari ya uongo.
“Ilikuwaje hapo? Nyie mbona hamkufa?”
“Kule chini mashimo huwa hutofautiana sana. Shimo la mgodi wetu lilikuwa limekwenda chini kama kilometa moja na kisha kuanzishwa mashimo mengine humo humo, mashimo ambayo yalikuwa upande wa kulia au wa kushoto. Katika kipindi ambacho kifusi kilikuwa kinafukia shimo lile, bahati yetu tulikuwa katika mashimo yale ya pembeni, tukanusurika japokuwa nasi tungekufa kutokana na hewa kuwa nzito” Samuel aliwaambia na kuendelea:
“Kwa sababu tulikuwa na tochi, tukaanza kufukua mchanga na hatimae kukutana na maiti zile ambapo tukayachukua madini na kisha kuwawekea midomoni mwao. Ilikuwa inahitaji ujasiri wa hali ya juu lakini kwa sababu tulikuwa tukitafuta fedha, tukajivika ujasiri na hatimae kufanikiwa” Samuel aliwaambia.
“Mmmh! Sasa hayo madini hayakuonekana?”
“Hapana. Sisi tulikuwa majeruhi na tulikuwa tukiangalia kila kilichokuwa kikiendelea” Samuel aliwaambia.
Japokuwa uongo ule ulikuwa ni wa kitoto sana lakini uso wa kinafiki ambao alikuwa akiuonyesha Samuel ndio ambao ukawafanya wazazi kuwaamini kwa asilimia mia moja. Wote wakaonekana kuridhika kabisa, mioyo yao ikaonekana kukubaliana nao bila kuwa na maswali yoyote vichwani mwao.
“Na vipi kuhusu kwenda katika nyumba za ibada? Mnakwenda?” Mchungaji Mpelele aliwauliza.
“Baba ni rahisi sana kwa ngamia kupita katika tundu la sindano kuliko tajiri kuingia Ufalme wa Mbinguni” Samuel alimwambia baba yake.
“Kwa nini?”
“Unapokuwa na fedha unahitaji nini tena? Wakati mwingine ninaona kwamba watu wengi humwabudu Mungu kwa kuwa hawana fedha” Samuel alimwambia baba yake ambaye akaonekana kutokuamini kile alichokisikia.
“Na vipi kuhusu wewe Sadiki?” Ustaadhi Hamidu alimuuliza Sadiki.
“Kama alivyosema Samuel ndio hivyo hivyo” Sadiki alisema huku akiwa ameuinamisha uso wake chini kwa aibu.
“Mnakosea watoto wetu, mnakosea kabisa. Fedha si kila kitu, umaarufu ambao mmekuwa nao si kila kitu katika maisha yenu, hivi vyote ni ubatili tu, unapokufa hauzikwi na fedha zako wala mali zako. Mungu ndiye kila kitu” Mchungaji Kipelele aliwaambia.
“Nadhani niliongea nawe mengi sana Sadiki. Kama ni fedha umekwishapata, huu ndio muda wako wa kumrudia Allah, hakuna muda ulio maalumu, muda wako ni sasa” Ustaadhi hamidu alimwambia Sadiki.
“Ni ngumu baba”
“Kwa nini?”
“Sitaki kuwa mnafiki katika maisha yangu” Sadiki alimwambia baba yake.
“Unatakiwa kumrudia Allah na kumuomba msamaha. Mtume Mohammad S.A.W alitufundisha mengi sana ikiwa pamoja na kumuabudu Allah kwani Yeye ndiye kila kitu. Wakati wako ni huu Sadiki. Saidia watu wenye matatizo mbalimbali, mtolee Allah sadaka kwani hivyo ndivyo Qur-an inavyoagiza” Ustaadhi Hamidu alimwambia Sadiki ambaye hakuonekana kuelewa hata mara moja.

Samuel na Sadiki walionekana kubadilika kabisa, hawakutaka kwenda katika nyumba za ibada kwani waliamini kwamba kama wangeanza kwenda katika nyumba zile za ibada basi iliwalazimu waache kabisa kufanya biashara zao za madawa ya kulevya kitu ambacho wala hawakutaka kuachana nacho. Bado walikuwa wakihitaji fedha zaidi, hawakutaka kabisa kubadilika na kuwa watu wa dini kama ilivyokuwa zamani.

Wazazi wao hawakuwa na jinsi, japokuwa walikuwa wamejitahidi sana kuwaambia maneno mengi kuhusu Mungu lakini mioyo yao ilionekana kuwa migumu sana. Walikaa katika nyumba ile kwa muda wa masaa mawili huku wakiongea hili na lile na kisha kuondoka kuelekea katika nyumba ya Sadiki ambayo wala haikuwa mbali kutoka mahali hapo.
Kama ilivyokuwa kwa Samuel, Sadiki nae alikuwa na nyumba kubwa ya kifahari, nyumba ambayo ilikuwa na kila kitu ndani. Wazazi wake wakaonekana kufurahia lakini maisha ambayo alikuwa akiishi mtoto wao yakaonekana kutia doa furaha ambayo walikuwa nayo mioyoni mwao.

“Mali bila Allah! Hakuna kitu” Ustaadhi Hamidu alimwambia mtoto wake, maneno mbayo aliamini hata kama atakwenda wapi, kuna siku angeyakumbuka tu.

Itaendelea kesho.
 
SEHEMU YA 18

Joram na Ignas bado walikuwa wakiendelea kufanya kazi zao za kusafirisha madawa kama kawaida. Katika kipindi hiki biashara ile ilionekana kusafirishwa kwa njia nyingine kabisa, njia ambayo ilianza kuingia miaka hiyo, kusafirisha madawa kwa kutumia maiti. Maiti zilikuwa zikisafirishwa huku tumboni kukiwa na madawa ya kulevya. Usafirishaji ule ulikuwa ni wa kisasa zaidi ambao walikuwa wameugundua na hakukuwa na mtu yeyote ambaye alikuwa akiufahamu.

Kila walipokuwa nchini Tanzania, Ignas na Joram walikuwa na kazi ya kutafuta maiti na mwisho wa siku kuzisafirisha sehemu husika na huko ndipo ambapo walikuwa wakizipasua maiti zile na kisha kuchukua madawa ambayo yalikuwa yamesafirishwa kwa njia hizo. Ignas na Joram hawakuonekana kuwa na wasiwasi kabisa, kiasi cha fedha ambacho walikuwa wakilipwa walikiona ni kikubwa sana jambo ambalo liliwafanya kufanya kazi ile kwa moyo mkunjufu.
Mwisho wa Ignas na Joram kusafirisha madawa ilikuwa mwaka 2009, mwaka ambao walikamatwa nchini Thailand na hivyo kusafirishwa mpaka Tanzania na kufungwa jela kwa miaka kumi. Hilo likaonekana kuwa kama pigo kubwa kwa Samuel na Sadiki ambao walikuwa wakiwategemea sana vijana wale ambao walikuwa wamekwishapelekwa gerezani na kutumikia adhabu ya kifungo hicho.

Samuel na Sadiki hawakutaka kuangaika sana, walichokifanya hapo ni kuanza kusafirhsa madawa wao wenyewe kwa staili ya kumeza vidonge kadhaa mpaka katika nchi husika. Japokuwa ilikuwa ni jambo hatari lakini katika kipindi hicho hawakuonekana kuwa na jinsi, ilikuwa ni lazima wafanye jambo hilo hili biashara ile isiweze kusimama huku wakiendelea kutafuta vijana wengine.

Kazi ya kusafirisha madawa kuelekea katika nchi mbalimbali kwa njia ya kuyameza ikaonekana kuwa njia rahisi ambayo wala haikuweza kugundulika hata mara moja. Huo ndio ulikuwa mchezo ambao walikuwa wakiucheza, mchezo ambao ulidumu kwa muda wa miezi sita, kipindi ambacho Sadiki akawa na safari ya kutaka kuelekea nchini Ujerumani ndani ya jiji la Munchen kwa ajili ya kupeleka mzigo mkubwa wa madawa ya kulevya ambayo yalikuwa katika kete arobainii ambazo alikuwa amezimeza.

“Huku nitapiga mpunga mkubwa sana kaka. Nikitoka huko, nitakuwa nimeingiza zaidi ya milioni mia nne” Sadiki alimwambia samuel.
“Nakutakia kila la Kheri, fanikisha mpango huo. Ukirudi, na mimi nitaelekea Sweden, kuna mzigo nitatakiwa kupeleka huko. Nadhani hata kazi ya kuwaajiri vijana kwa sasa tupunguze wasije wakatufanyia kama tulivyomfanyia Khaled” Samuel alimwambia Sadiki.
“Hakuna tatizo. Nadhani nikitoka Ujerumani nitaelekea nchini Brazil kuchukua mzigo mwingine na kuupeleka Malyasia na kisha kurudi nchini Tanzania” Sadiki alimwambia Samuel.
“Hakuna tatizo” Samuel alimwambia sadiki.
Siku tatu zilizofuata, Sadiki akaanza safari yake ya kuelekea nchini Ujerumani huku tumboni akiwa amemeza kete arobaini ambazo zilikuwa katika mfumo wa vidonge, kete ambazo zilikuwa na madawa ya kulevya ambayo yalitakiwa kufikishwa nchini Ujerumani.

Ndani ya ndege muda wote Sadiki hakuonekana kuwa na wasiwasi, alikuwa amekwishazoea kumeza kete za madawa ya kulevya na kisha kuzisafirisha barani Ulaya kwa ajili ya kufanya biashara. Hiyo ndio ilikuwa kazi yake, hakutaka kumgawia kijana yeyote kupeleka madawa yale kwa kuamini kwamba vijana wengine wasingeweza kuwa waaminifu kama ambavyo walivyokuwa Ignas na Joram ambao walikuwa gerezani wakati huo.
Sadiki hakula chakula kigumu kwa kuhofia kuleta matatizo tumboni mwake, matatizo ambayo yangesababisha kete zile kupasuka na hatimae madawa yale ya kulevya kutapakaa tumboni mwake na kufa papo hapo. Chakula cha kikubwa kilikuwa ni biskuti chache sana ambazo alikuwa akinywa na maji ili kusaidia kete zile zisiweze kupasuka tumboni mwake.
****
Mwezi wa kumi na mbili kilikuwa ni kipindi kilichokuwa na baridi kali sana katika nchi za Ulaya kiasi ambacho muda mwingi theluji ilikuwa ikionekana mitaani jambo ambalo lilisababisha theluji ile kufunika barabara nzima na hivyo magari maalumu ya kuondoa theluji kupita katika bharabara nzima ili ziweze kuonekana na magari yaweze kupita.
Katika kipindi hicho cha baridi ndicho kilikuwa kipindi ambacho ndege ya shirika la ndege la Fly Emirates ilikuwa ikitua katika jiji kubwa la Munich, jiji lililokuwa Kusini mwa nchi ya ujerumani. Katika kipindi chote hicho ndani ya ndege Sadiki hakuonekana kuwa na wasiwasi hata kidogo, alikuwa na uhakika wa kupita salama kama ambavyo alivyokuwa akipita katika sehemu nyingine.

Baada ya ndege kusimama, abiria wakatakiwa kuteremka na Sadiki pamoja na abiria wengine kufanya hivyo. Koti kubwa lilikuwa mwilini mwake, japokuwa alikuwa akipigwa na baridi lakini wakati mwingine koti lile lilikuwa likimsaidia sana kumkinga na baridi hilo ambalo lilionekana kuwa kali sana katika nchi za Ulaya hasa katika kipindi hicho cha mwezi wa kumi na mbili.

Mara baada ya mizigo kukaguliwa, akaanza kupiga hatua. Kitendo cha Sadiki kuwaona wanaume saba ambao walikuwa wamevaa suti huku wakiwa na hearphone masikioni mwao na maiki ndogo karibu na midomo yao, Sadiki akaonekana kuwa na wasiwasi, hofu ikaanza kumuingia japokuwa hakujua hofu ile ilikuwa imesababishwa na nini.
Akaanza kupiga hatua za kujishtukia kuufuata mlango wa kuelekea nje. Huku akiwa amebakiza hatua ishirini kabla ya kuufikia mlango, akashangaa kumuona mwanaume mmoja ambaye alivaa suti akimfuata na kisha kumsimamisha. Sadiki akaonekana kuhofia kupita kawaida, mwanaume yule alionekana kugundua kitu fulani, alichokifanya mara baada ya kuona Sadiki kasimama, hapo hapo akawaita wenzake wawili na kisha kumchukua Sadiki na kumpeleka katika chumba kimoja kilichokuwa maalumu kwa kufanyia mahojiano na wasafiri ambao walikuwa wakionekana kuwa si watu wa kawaida.

Ndani ya chumba kile kulikuwa na meza moja ambayo wala haikuwa na viti vingi huku juu ya meza ile kukiwa na televisheni pamoja na deki na pembeni kukiwa na baadhi ya mikanda. Kitu walichokifanya watu wale ni kumuondoa wasiwasi Sadiki ambaye wala hakuonekana kuondokewa na wasiwasi ambao alikuwa nao moyoni mwake. Ndani ya chumba kile, akatakiwa kukaa katika kiti kimoja huku wanaume wanne wakikaa katika viti vya tofauti.
Maswali kibao yakaanza kumiminika kichwani mwa Sadiki juu ya sababu ya watu wale kumhitaji ndani ya chumba kile huku wakionekana kumtilia mashaka kupita kawaida. Alichokifanya Sadiki ni kubaki kimya huku akitaka kuona ni kitu gani kingetokea kwani kila alipokumbuka kwamba sehemu alipoyaweka madawa yasingeweza kuonekana, akajipa imani ya kushinda kila kitu mahali pale.

“Samahani. Tunaweza kuangalia passpoti yako?” Mwanaume mmoja alimuuliza Sadiki ambaye akaichukua pasipoti yake kutoka kwenye begi na kisha kumpa mwanaume yule aliyeihitaji, akaanza kuiangalia, alipoona amemaliza, akawapa wenzake ambao wakaiangalia na kisha kumwangalia Sadiki usoni huku tayari wakionekana kumtilia mashaka.
“Umetembea nchi nyingi sana, tena nchi ambazo zimekuwa maarufu katika usafirishaji wa madawa ya kulevya. Wewe ni mmoja wao?” Mwanaume huyo ambaye alijitambulisha kwa jina moja ya Kurt alimuuliza Sadiki.
“Madawa! Hapana. Mimi ni raia safi kabisa. Sijasafirisha madawa yoyote yale” Sadiki aliwajibu huku akijaribu kuitoa hofu usoni mwake.
“Sawa. Ila umetembea nchi nyingi sana Sadiki” Kurt alimwambia Sadiki huku akichukua pasipoti ile na kisha kumrudishia.
“Kawaida tu. Mimi ni mfanyabiashara wa kujitegemea” Sadiki aliwaambia.
“Ok! Hakuna tatizo. Tumekuelewa. Ningependa kukwambia kitu kimoja” Kurt alimwambia Sadiki.
“Kitu gani?”
“Subiri kwanza” Kurt alisema na hapo hapo kuinuka na kutoka ndani ya chumba kile. Wanaume wengine ambao walikuwa ndani ya chumba kile wakaonekana kuwa bize wakipiga stori huku wakitaka kumuonyeshea Sadiki kwamba hawakuwa wakijali sana uwepo wake mahali pale na wakati kwa macho ya wizi walikuwa wakimfuatilia vizuri sana. Kurt alichukua dakika mbili tu, akarudi mahali hapo huku akiwa na jagi lililokuwa na maji pamoja na glasi na kisha kutulia kitini.
“Haya unayoyaona si maji kama maji bali ni dawa iitwa Methrophesium, dawa maalumu kwa ajili ya kupasua kete za madawa ya kulevya ambayo yapo tumboni mwa mtu yeyote” Kurt alimwambia Sadiki maneno ambayo yalionekana kumshtua kupita kawaida na kisha kuendelea.
“Subiri kwanza” Kurt alimwambia Sadiki na kisha kuchukua rimoti na kuiwasha televisheni ile ambayo ilikuwa mezani na kisha kuweka mkanda mmoja katika deki.
“Huu mkanda utakaouona ni wa watu ambao tuliwashuku kuwa wana madawa tumboni na kisha kuwaambia wanywe maji haya yenye dawa hiyo. Kwa hapa ngoja nikwambie kitu kimoja. Kama kweli hauna kete za madawa ya kulevya tumboni mwako, maji haya yenye dawa hayatokuwa na madhara yoyote yale ila kama una madawa tumboni, kete zitakwenda kupasuka na hatimae madawa kumwagika tumboni mwako na kufa huku ukijiona” Kurt alimwambia Sadiki ambaye alionekana kuwa na wasiwasi mwingi.
“Kuna watu walikuwa na madawa ya kulevya ila wakasema hawana, wakanywa na matokeo yake ndani ya sekunde kumi baada ya maji kugusa kete zile, zikapasuka na hatimae madawa kumwagika tumboni na kufa ila kuna wengine ambao walisema hawana, na kweli wakanywa, hakukuwa na kilichotokea na hivyo kuwalipa dola mia tano kwa kila mmoja kutokana na usumbufu ambao waliupata kutoka kwetu. Ngoja nikuonyeshee video kidogo” Kurt alimwambia Sadiki maneno mengi na kisha kumuwekea video ile.

Sadiki akayatuliza macho yake katika televisheni ile na kuwaona watu wakiwa katika chumba kile kile huku wakifanya mahojiano na mwisho wa siku kupewa glasi moja ya maji yale na kunywa. Kuna wengine walikuwa wakitoka salama lakini kulikuwa na wengine ambao walionekana kuangaika huku wakiyashika matumbo yao na hatimae kufa kwa maumivu makali.

“Hao ni baadhi ya watu. Ukinywa maji haya na kuwa mzima, basi tutakulipa dola mia tano kama usumbufu ila kama ukisema hauna, na ukanywa kisha kufa, hiyo utakuwa umejiua kwa uzembe wako. Chaguo ni lako” Kurt alimwambia Sadiki huku akiyamimina maji katika glasi na kisha kumuwekea glasi ile ya maji Sadiki.

Muda wote Sadiki alikuwa akitetemeka tu, kijasho chembamba kikaanza kumtoka kwa kuona kwamba siku hiyo alikuwa amepatikana. Alibaki kwa dakika kadhaa huku akiiangalia glasi ile iliyokuwa na maji. Kila alipokuwa akiyapeleka macho yake katika televisheni ile, watu wengi walionekana kufa mara baada ya kuyanywa maji yale, watu ambao walikuwa na madawa ya kulevya tumboni mwao.

Bila kupenda na bila kushinikizwa, Sadiki akaamua kuiweka mikono yake juu ya meza katika staili iliyoonyesha kwamba alikuwa tayari kufungwa pingu lakini si kuyanywa maji yale, hiyo ilimaanisha kwamba alikuwa na madawa ya kulevya tumboni mwake.

“Uamuzi mzuri” Kurt alimwambia sadiki na kisha kumfunga pingu.
Katika safari zaidi ya hamsini ambazo alikuwa amezifanya katika nchi mbalimbali safari hiyo ndio ambayo ilionekana kuwa mbaya sana kwake, hakuamini kwamba kwa mafanikio makubwa ambayo alikuwa ameyapata siku hiyo alikuwa amekamatwa kilaini sana jambo ambalo alijua fika kwamba kulikuwa na mtu ambaye aliwambia polisi wale kwa ajili ya kumkamata, alijua fika kwamba mtu huyo alikuwa mzee Bill Brug, mzee wa kijerumani ambaye alikuwa akifanya nae biashara ile lakini mara kwa mara alikuwa na wasiwasi nae.

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 19

Katika kipindi ambacho alikuwa amekamatwa Sadiki akaanza kujutia kile ambacho alikuwa akikifanya, kuuza madawa ya kulevya. Moyo wake uliumia kupita kawaida kila alipokuwa akiyakumbuka maneno ya baba yake, mzee Hamidu ambaye kila siku alikuwa akimtaka kumrudia Mungu. Utajiri mkubwa ambao alikuwa nao katika kipindi hicho akauona ukianza kupotea kwa kuamini kwamba ilikuwa ni lazima afungwe jela miaka kadhaa nchini Ujerumani.

Kutokana na tetesi ambazo zilikuwa zikisikika jijini Munich kwamba kulikuwa na Mtanzania ambaye alikamatwa na madawa ya kulevya, balozi wa Tanzania nchini Ujerumani, Emmanuel Kihampa ikambidi kuingilia kati kwa kutaka mtuhumiwa asafirishwe mpaka nchini Tanzania kwa ajili ya kuhukumiwa kwa kosa la usafirishaji wa madawa ya kulevya ambao alikuwa amelifanya.

Haikuwa kazi nyepesi hata mara moja, ilichukua takribani wiki tatu na ndipo kila kitu kilipokamilika na hivyo Sadiki kuanza kurudishwa nchini Tanzania kwa ajili ya kuhukumiwa kwa kile alichokuwa amekifanya. Ndani ya ndege, alionekana kutia huruma, pingu zilikuwa zimefunga mikoni yake huku maneno ya baba yake ambayo yalikuwa yakimtaka kumrudia Mungu yakiwa yanajirudia kichwani mwake.

“Hii laana. Maneno ya baba ndio yamesababisha nikamatwe” Sadiki alijisemea katika kipindi ambacho safari ya kurudi nchini Tanzania ikiendelea kama kawaida.
“Bora niachane na kazi hii kwa sasa” Sadiki alijisemea huku akionekana kumaanisha kile alichokuwa akikisema.
Hicho ndicho kilikuwa kipindi maalumu cha kuyakumbuka maneno ya busara ambayo walikuwa wakiyaongea wazazi wake na kisha kuyapuuzia. Katika kipindi hicho alikuwa akikumbuka kila neno ambalo wazazi wake walikuwa wakimwambia katika kipindi cha nyuma.

Alijuta, moyo wake ulijuta kupita kiasi kutokana na kile ambacho kilikuwa kimetokea huku akiona kwamba kulikuwa na kila sababu za kuachana na biashara ile ya madawa ya kulevya.
Mpaka katika kipindi hicho alikuwa amechelewa mno, kama kuachana na biashara ile alitakiwa kuachana nayo toka katika kipindi cha nyuma lakini si katika kipindi hicho kwani tayari alikuwa amekamatwa na ilikuwa ni lazima afikishwe mahakamani na kuhukumiwa.

Nchini Tanzania Samuel hakutulia, mara baada ya kupata taarifa kwamba rafiki yake ambaye alimchukulia kama ndugu yake, Sadiki alikuwa amekamatwa alionekana kuchanganyikiwa. Kitu cha kwanza ambacho alikifanya ni kuanza kuwasiliana na watu waliokuwa na vyeo vikubwa ambao alikuwa akishirikiana nao katika uuzaji wa madawa ya kulevya na kuwataka wafanye kila linalowezekana kuhakikisha kwamba Sadiki anatoka na kuwa huru tena.

“Itawezekana ila ina mlolongo mrefu sana” Bwana Marko alimwambia Samuel.
“Inaweza kuchukua muda gani mpaka kukamilika?” Samuel alimuuliza.
“Kama mwezi mzima tena hapo tukiwa tumetoa kiasi kikubwa cha fedha” Bwana Marko alimwambia Samuel.
“Kuhusu fedha si tatizo, ishu iliyokuwepo ni yeye kuwa uraiani kwa mara nyingine tena” Samuel alimwambia Bwana Marko.
“Hakuna tatizo. Ila siku nyingine msijali kusafirisha madawa kwenda Ujerumani”
“Kwa nini?”
“Kule ni nuksi sana, watu wa kule hawatupendi watu wenye ngozi nyeusi na ndio maana huwa hatuendi kufanya biashara kule, sijui imekuwaje mpaka Sadiki kwenda kule” Bwana Marko alimwambia Samuel.
“Cha kwanza tuhakikishe huyu mtu anakuwa huru na hayo mengine yatafuata” Samuel alimwambia Bwana Marko.
Mishemishe zao zikaanza mahali hapo, Samuel hakuweza kutulia, alikuwa akiangaika huku na kule ili tu akamilishe kile ambacho kilitakiwa kukamilishwa muda huo. Bwana Marko alikuwa pamoja nae katika kila hatua ambayo alikuwa akiifanya kuhakikisha kwamba Sadiki anaachiwa huru. Kazi haikuwa nyepesi hata mara moja kutokana na polisi kulishikilia sana suala lake.
“Kazi itafanyika. Mna milioni sabini?” Mwanaume mmoja alimuuliza Bwana Marko na Samuel.
“Fedha si tatizo”
“Basi niachieni mimi. Nyie nendeni nyumbani kanyweni kahawa tu” Mwanaume yule alimwambia.
Hapo ndipo kazi ilipoanza, mwanaume yule ambaye hakutaka kujitambulisha jina lake akaingia kazini. Japokuwa kazi kwa wengine ilionekana kuwa kubwa lakini kwake kazi ile ikaonekana kuwa nyepesi sana na ndani ya wiki tatu tu kila kitu kilikuwa tayari na Sadiki kuwa huru kwa masharti mawili tu, asikae ndani ya nyumba yake mpaka miezi sita itakapokwisha na pia asisafiri kwenda nchi yoyote ya Ulaya mpaka miezi hiyo itimie kitu ambacho wala hakikuonekana kuwa tatizo kwake.
“Nashukuru kwa kila kitu. Nilikuwa napotea hivi hivi” Sadiki aliwaambia Samuel na Bwana Marko.
“Kuwa makini siku nyingine” Samuel alimwambia Sadiki.
“Na kitu kingine ni kwamba usijaribu kwenda Ujerumani, kule utapotezwa” Bwana Marko alimwambia Sadiki.
“Nafikiri huu ulikuwa ni mpango ambao ulipangwa. Sirudi kule tena” Sadiki aliwaambia.
Muda wa majuto ukaonekana kupotea tena. Katika kipindi ambacho alikuwa amekamatwa alitamanai kubadilika na kuwa mtu wa dini kutokana na kipindi cha matatizo ambacho alikuwa nacho lakini kwa wakati huo ambao alikuwa ameachiwa huru, akaonekana kusahau kila kitu. Hakurudi nyumbani kwake, kitu ambacho aliambiwa akifanye ndicho alikitekeleza. Hakwenda kuishi hotelini, akaamua kuishi pamoja na Samuel ndani ya nyumba ya Samuel.
Ndani ya nyumba kubwa wakawa wakiishi watu watatu, Samuel, Catherine na Sadiki tu. Tabia yake ya kuchukua wanawake haikuisha, kila siku Sadiki alikuwa mtu wa kubadilisha wanawake kama nguo kitu ambacho kilimkasirisha sana Samuel lakini hakuwa na la kufanya kwani kama kuongea nae alifanya hivyo mara nyingi sana lakini hakukuwa na mabadiliko yoyote yale.

Leo alikuwa akiingia na wanawake wa vyuo, kesho alikuwa akiingia na wafanyakazi na kesho wahudumu wa bar. Sadiki hakutaka kuelewa hata mara moja, alionekana kama mtu ambaye alikuwa akitafuta kitu fulani kutoka kwa wanawake kwani mara baada ya kumpa Zubeda, msichana wa kitanga, Sadiki akatulia, hakutaka tena wanawake.
Hiyo ikaonekana kuwa nafuu sana, mchezo wake wa kuchukua wanawake ukaonekana kuanza kuisha kabisa. Samuel hakujua Zubeda alikuwa akimfanya nini Sadiki mpaka kutulia namna ile, hiyo ilikuwa ni siri ya watu wawili, Sadiki na Zubeda tu.

“Huyu demu noma kaka” Sadiki alimwambia Samuel.
“Kivipi?”
“Kuwa mtoto wa mjini. Nikisema noma najua unajua namaanisha nini” Sadiki alimwambia Samuel na wote kuanza kucheka.
Hiyo ndio ilikuwa siri ambayo alikuwa nayo Zubeda. Kitandani alikuwa mtundu kupita kawaida kitendo ambacho kilionekana kumchanganya sana Sadiki. Mapenzi motomoto ambayo alikuwa akipewa na Zubeda ndio ambayo yakamfanya kuwasahau wanawake wengine. Zubeda alikuwa akiujua vilivyo mchezo ule kiasi ambacho akili ya Sadiki ikaonekana kuchanganyikiwa kupita kawaida.

Ni kweli alikuwa ametembea na wanawake wengi katika maisha yake lakini kwa msichana Zubeda akaonekana kuchanganyikiwa kupita kawaida. Kitandani, Zubeda alikuwa na uwezo wa kila kitu, alikuwa akiweza kukipeleka kiuno chake huku na kukipeleka kule, alipokuwa akitulia, Sadiki alikuwa akihema juu juu kana kwamba alikuwa akitaka kukata roho. Huyo ndiye alikuwa Zubeda, msichana kutoka Tanga barabara ya tisa,msichana ambaye alikuwa akijua hasa kucheza na mwanaume kitandani.

“Umejifunzia wapi mchezo huu?” Sadiki alimuuliza Zubeda.
“Kwa nini umeuliza?”
“Hapana aisee. Yaani kama una mota kiunoni” Sadiki alimwambia Zubeda.
“Usijali. Nilifundishwa sana nyumbani” Zubeda alimwambia Sadiki.
“Kuna siku utaniua, haiwezekani uwe unakwenda huku na kule kama nyigu” Sadiki alimwambia Zubeda.
Hayo ndio yalikuwa maisha yao, kila siku walikuwa wakifanya ngono tu kitu ambacho kiliwafanya kujiona kama walikuwa katika ulimwengu mwingine, ulimwengu ambao uliwafanya kuwa huru kabisa. Sadiki akaonekana kuridhika, hakuwa na haja ya kuwatafuta wanawake wengine na wakati Zubeda alikuwa amejitosheleza kwa kila kitu.

Hiyo ikaonekana kuwa nafuu kwa Samuel, zile mishemishe za wanawake kuingia na kutoka zikawa zimekwisha kwani tayari Sadiki alikuwa amempata mwanamke ambaye alikuwa akimridhisha kwa kila kitu. Japokuwa alikuwa akimuona Zubeda kuwa mwanamke mzuri aliyekuwa na uwezo wa kila kitu lakini nyuma ya pazia Zubeda hakuwa msichana mzuri, alikuwa ni msichana ambaye alivaa sura ya bandia.

Kwa Sadiki, akaonekana kupata lakini ukweli ni kwamba alikuwa amepatwa kwani maisha ya nyuma ya pazia ambayo alikuwa akiishi Zubeda yalikuwa ni balaa, hayo maisha ndio ambayo yalimfanya Zubeda kubadilika kwani afya yake haikuwa sawa, alikuwa ameathirika na kitu ambacho alikuwa akikifanya ni kuusambaza ugonjwa wa UKIMWI kwa wanaume waliokuwa na fedha tu akiwepo Sadiki kwa kuamini kwamba kupitia watu hao, wanawake wengi wangeteketea kama ilivyokuwa kwake.
****
Samuel hakutaka kuachana na biashara zake, mara kwa mara alikuwa akitoka na kuelekea katika nchi nyingine kwa ajili ya kuuza madawa ya kulevya ambayo bado yalikuwa yakimuingizia fedha kupita kawaida. Kila kitu ambacho kilikuwa kikiendelea Catherine hakuwa akikifahamu japokuwa mara kwa mara mpenzi wake huyo alikuwa akimuaga kwamba alikuwa akisafiri kuelekea nje ya nchi.

Mapenzi yao hayakupungua, kila siku walikuwa wakizidi kupendana kupita kawaida. Catherine hakutaka kuwaambia wazazi wake kwamba aliamua kuwa na Samuel, mwanaume wake ambaye alimtoa usichana katika kipindi ambacho walikuwa shuleni Kilimanjaro. Mapenzi yao yakaonekana kuwa siri kwa wazazi wao, hawakutaka wazazi hao wafahamu kile ambacho kilikuwa kikiendelea kwao.

Muda mwingi ambao Samuel alikuwa nchini Tanzania walikuwa pamoja huku wakiyaurahia maisha yao kama kawaida. Catherine hakuonekana kuambiwa chochote kwa mapenzi ambayo alikuwa nayo kwa Samuel, alikuwa akimpenda kupita kawaida. Akamtambulisha Samuel kwa marafiki zake, Catherine bado alionekana kuwa mwanamke aliyekuwa na bahati kwa kumpata mwanaume ambaye alikuwa na fedha nyingi katika maisha yake.

Wivu wa wanawake bado ulikuwa ukiendelea, kila siku walikuwa wakimuonea wivu Catherine ambaye wala hakuonekana kujali. Catherine akapewa gari la kutembelea huku akaunti yake ya benki ikijazwa pesa jambo ambalo liliendelea kuyafanya mapenzi yake juu ya Samuel kuzidi kuongezeka zaidi na zaidi. Katika kipindi ambacho Samuel aliamua kuelekea nchini Australia kwa ajili ya kupeleka mzigo wa madawa ya kulevya, hali nyumbani ikaonekana kubadilika.

Sadiki ambaye alikuwa pamoja na Zubeda akaonekana kuanza kuingiwa na tamaa hasa mara baada ya kumuona Catherine akiwa amevaa kanga moja tu na kuja sebuleni katika kipindi ambacho ulikuwa ni usiku wa saa tano.
Sadiki akabaki akimwangalia Catherine kwa macho ya matamanio, ni kweli kwamba alikuwa akimfahamu vilivyo Catherine lakini kitendo cha kumuona akiwa amevaa kanga moja kukaonekana kumpagawisha kupita kawaida.

Catherine alionekana kuumbika kupita kawaida, hipsi zake zilikuwa tofauti na jinsi ambavyo Sadiki alivyokuwa akifikiria kabla. Kitendo cha kumuona Catherine akiwa na kanga moja tayari kikaanza kutengeneza kitu fulani moyoni mwake.
Tamaa ikamuingia na kuuhisi mwili wake kuwa na hamu ya kufanya mapenzi na Catherine. Sadiki hakuonekana kujali kwamba angeonekana vipi kwa Samuel kitu ambacho alikuwa akikitaka ni kufanya ngono na Catherine tu. Kuhusu wasichana, Sadiki hakuonekana kuwa na wasiwasi nao kabisa, alijua fika kwamba hata kama msichana alikuwa akimpenda mwanaume wake kwa kiasi gani lakini kuna mambo ambayo kama ungefanikiwa kumfanyia basi ungeweza kumteka na kisha kufanikisha lengo lako.

Huo ndio ulikuwa udhaifu wa wanawake ambao ulikuwa ukijulikana moyoni mwake. Alijua fika kwamba kama angekaza basi ilikuwa ni lazima kutembea na Catherine katika kipindi hicho ambacho Samuel alikuwa nchini Australia. Sadiki hakuonekana kuujali urafiki wake uliokuwa kama ndugu baina yake na Samuel, tamaa ambayo ilikuwa imemuingia ilikuwa imebadilisha kila kitu moyoni mwake na kumsahaulisha ukaribu ambao alikuwa nao na Samuel.
Hakujua ni kipi kingetokea endapo angemwambia Catherine na kisha mwanamke huyo kukataa na kumwambia Samuel katika kipindi ambacho angerudi nchini Tanzania. Sadiki akaupiga moyo konde, kitu ambacho alikuwa akikitaka ni kufanya mapenzi na Catherine tu kwani tayari akili yake ilikuwa imekwishachanganyikiwa.

Katika kipindi ambacho Catherine alikuwa akikaa na kanga moja sebuleni Sadiki alionekana kubadilika, kila wakati alikuwa akimwangalia Catherine ambaye alichukulia kila kitu kawaida sana. Sadiki alikuwa na kazi kubwa ya kubadilisha mikao, mara akae hivi, mara akunje nne, yaani kila mkao ambao alikuwa akikaa aliuona kutokufaa. Tabia ile ya Catherine kuvaa kanga moja na kuja sebuleni iliendelea zaidi na zaidi huku kila siku Sadiki akionekana kuumia kupita kawaida. Kila alipokuwa akikaa sebuleni hakuonekana kuwa huru, suruali yake maeneo ya zipu ilikuwa ikija mbele kana kwamba zipu ilitaka kutobolewa. Maisha yakawa kama mateso, alipokuwa akilala chumbani kichwa chake kilikuwa kikimfikia Catherine tu huku wakati mwingine akitamani kumfuata chumbani na kulala nae.

“Hatuwezi kwenda kuangalia muvi leo” Sadiki alimwambia Catherine ambaye alikuwa sebuleni hapo, kama kawaida alikuwa na kanga moja.
“Hapana. Leo najisikia nimechoka sana” Catherine alimwambia Sadiki.
“Sawa. Usijali. Na vipi kuhusu pombe. Hatuwezi kwenda kununua pombe?” Sadiki alimuuliza Catherine.
“Usiku wote huu?”
“Ndio kwanza saa tano. Kwanza hatutakiwi kuhofia kwa sababu tuna usafiri wa kuturahisishia” Sadiki alimwambia Catherine.
“Ngoja nikavae” Catherine alimwambia Sadiki.
“Hakuna noma” Sadiki alimuitikia.

Tayari akili yake ikazidi kufikiria ngono, kitu ambacho alikuwa akikitaka mahali hapo ni kwenda kununua pombe, amnyweshe sana Catherine na kisha kufanya nae mapenzi. Mpango wake huo ukaonekana kufaa sana. Baada ya dakika kadhaa, Catherine akatoka chumbani huku akiwa amevaa sketi fupi ambayo iliyaacha mapaja yake wazi. Kwa nguo ile tu tayari ikaonekana kumpagawisha Sadiki.

“Umependeza sana” Sadiki alimwambia Catherine ambaye akaanza kujiangalia.
“Asante” Catherine alimwambia Sadiki na kisha kuanza kutoka mpaka katika eneo lililokuwa na magari na kisha kuingia ndani ya Prado na kuondoka mahali hapo.
Kichwa cha Sadiki katika kipindi hicho kilikuwa kikifikiria ngono tu. Kila alipokuwa akiyaangalia mapaja ya Caterine pake ndani ya gari alionekana kuchanganyikiwa kupita kawaida. Akili yake haikutulia, mawazo yake yakaanza kumuonyeshea akiwa chumbani pamoja na Catherine, akaanza kumvua nguo na kisha kuanza kufanya nae mapenzi.
“Simuachi leo. Hata kama urafiki na Samuel bora ufe tu” Sadiki alijisemea kila alipokuwa akiyaangalia mapaja ya Catherine kiwizi..

Ndani ya dakika kumi gari likasimama nje ya duka moja la pombe kali lililokuwa Mwenge na kisha kuteremka. Sadiki akaanza kuangalia ndani ya duka lile, chupa nyingi zilizokuwa na pombe kali zilikuwepo mahali hapo. Sadiki akachukua zile pombe ambazo aliziamini kwamba zilikuwa kali sana na kisha kuondoka mahali hapo. Lengo lake ambalo alikuwa amelipanga lilikuwa ni kumlewesha sana Catherine na mwisho wa siku afanye nae mapenzi bila kipingamizi chochote kile. Kwa kuwa alielewa kwamba Catherine alikuwa mtu wa pombe sana, hakuona kama kulikuwa na dalili za mwanaumke huyo kukataa kunywa pombe.

Walipofika nyumbani moja kwa moja Sadiki akalisimamisha gari na kulipaki, akamfungulia Catherine mlango na kisha kuelekea ndani huku wakiwa wameshika mfuko ambao ulikuwa na pombe kali. Walipofika ndani, moja kwa moja wakazifungua na kuanza kuzinywa huku wakipiga stori za hapa na pale.

Sadiki alikuwa ametuliza kichwa chake kwa wakati huo, hakuwa akinywa mara kwa mara kama ambavyo Catherine alivyokuwa akinywa pombe zile. Alipoona kwamba ukimya ulikuwa haufai mahali hapo, akasimama na kisha kuwasha muziki. Ni ndani ya dakika thelathini tu pombe zikaonekana kuanza kumchukua Catherine, akasimama na kisha kuanza kucheza muziki huku akiwa anayumbayumba kama kwamba angeweza kuanguka muda wowote ule.

Sadiki hakutaka kumuacha peke yake, nae akasimama na kisha kuanza kucheza nae huku Catherine akiendelea kunywa pombe. Kichwa cha Catherine hakikuwa na uwezo wa kuhimili pombe zilizokuwa na ulevi mkubwa namna ile, pombe ambazo alikuwa akizipenda zilikuwa ni Kilimanjaro tu na ndio maana ndani ya muda mchache alikuwa hoi.
Catherine akaonekana kuchoka, akajilalia juu ya kochi huku hata chupa ambayo alikuwa ameishika ikiwa pembeni yake, pombe ilionekana kumchukua kupita kawaida. Hiyo hali ndio ambayo Sadiki alikuwa akitaka kuiona, akamsogelea Catherine mahali pale na kisha kuanza kumuasha. Catherine alikuwa aking’ang’ania kuachwa mahali pale, alichokifanya Sadiki ni kumbeba na kisha kumpeleka chumbani.

“Kiulainiiiiiii najilia mambo” Sadiki alisema katika kipindi ambacho alimlaza Catherine kitandani.
Catherine alikuwa amelala chali, miguu ameitanua na hivyo kuyafanya mapaja yake kuwa wazi. Uchu wa kufanya ngono ukazidi kumpata Sadiki, akaona kwamba lilikuwa ni kosa la jinai kumuacha Catherine mahali hapo bila kufanya nae ngono, alichokifanya ni kuanza kumchojoa nguo zake, Catherine hakuwa na kipingamizi kwani pombe zilikuwa zimemchukua sana.

Siku hiyo ndio ilikuwa siku ya kwanza kwa Sadiki kufanya mapenzi na Catherine. Hata Catherine alipoamka asubuhi na kujikuta yupo chumbani kwa Sadiki akajua kwamba Sadiki alikuwa amefanya nae mapenzi kutokana na kutokuwa hata na nguo moja mwilini mwake. Catherine akaonekana kukasirika, akasimama kitandani pale na kisha kuanza kuvaa nguo zake huku akimwangalia Sadiki kwa hasira kitandani pale.

“Sadiki....Sadiki....” Catherine alimwambisha Sadiki ambaye akaamka huku nae akiwa mtupu.
“Ndio umenifanya nini?” Catherine aliuliza huku akionekana kuwa na hasira.
“Samahani Catherine. Tulilewa sana na ndio maana kitu hiki kilitokea” Sadiki alimwambia Catherine.
“Kwa hiyo umenibaka?”
“Hapana”
“Kumbe umefanyaje?”
“Ni pombe zilituchukua sana” Sadiki alimwambia Catherine ambaye akatoka chumbani hapo kwa hasira.
Hapo ndipo ambapo Sadiki akaanza kujutia kile ambacho alikuwa amekifanya kwa Catherine, moyo wake ukanyong’onyea na hatimae kuanza kuufikiria ukaribu ambao alikuwa nao na Samuel, akajiona kuwa msaliti mkubwa katika maisha yake. Hakutaka kuendelea kubaki katika hali hiyo, akatoka chumbani kwake na kisha kuanza kumfuata Catherine chumbani kwake, alipoufikia mlango akaufungua na kisha kuingia ndani. Catherine alikuwa amekaa kitandani akilia, kitendo ambacho alikuwa amefanyiwa na Sadiki kilionekana kumuumiza kupita kawaida, machozi yalikuwa yakitiririka shavuni kwake. Akilini mwake alikuwa akimfikiria mpenzi wake, Samuel ambaye alikuwa amesafiri kuelekea nchini Australia.

Sadiki akaanza kupiga hatua, alipokifikia kitanda nae akakaa kitandani na kisha kumsogelea Catherine na kisha kumvutia kwake na kisha kumkumbatia. Sadiki akatumia nafasi hiyo kumuomba msamaha Catherine ambaye alionekana kuwa kwenye majonzi makubwa.

“Naomba unisamehe” Sadiki alimwambia Catherine ambaye bado alikuwa akiendelea kulia tu.
“Naomba unisamehe Catherine” Sadiki alimuomba msamaha Catherine kwa mara nyingine tena.
Sadiki hakujua ni kitu gani kilichokuwa kikiendelea mwilini mwake, kwa sababu Catherine alikuwa bado amevaa kisketi chake kifupi huku kifuani akiwa na sidiria tu, akauhisi mwili wake ukianza kushikwa na hisia za kutaka kufanya mapenzi. Sadiki alijitahidi kwa nguvu zote kuzizuia hisia hizo lakini akajikuta akishindwa kabisa hali iliyompelekea kuanza kuyashikashika mapaja ya Catherine.

Catherine hakuwa na ujanja tena, hakuonekana kuwa mgumu kwani hata kama angejifanya kuwa mgumu tayari alikuwa amekwishatembea na Sadiki, tayari alikuwa amekwisauona mwili wake wote. Catherine akajikuta akijifuta machozi, Sadiki alipousogeza mdomo wake, wakajikuta wakianza kubadilishana mate na kisha kuanza kufanya ngono kwa mara nyingine tena.

Usaliti ukaendelea kama kawaida, mchezo ule ukaonekana kushamiri ndani ya nyumba ile. Kila siku wakawa watu wa kufanya ngono tu jambo ambalo liliwafanya kuwa huru kupita kawaida. Hapo ndipo ambapo Sadiki akaamua kuachana na Zubeda bila kuwa na sababu yoyote ile. Japokuwa Zubeda alikuwa ameumia sana lakini wala hakuwa na wasiwasi kwani lengo lake tayari alikuwa amelikamilisha, kumuambukiza UKIMWI Sadiki.

“Siku Samuel akija kujua....” Catherine alimwambia Sadiki huku akiwa amemuegemea kifuani.
“Uzuri ni kwamba hakuna atakayemwambia, kwa hiyo hatoweza kujua” Sadiki alimwambia Catherine.
“Hahah! Yeah! Tuombe Mungu asije kujua kwani akijua itakuwa ni balaa mpenzi” Sadiki alimwambia Samuel.
“Niamini, hatokuja kujua” Sadiki alimwambia Catherine na kisha kukumbatiana, kilichofuata, kama kawaida yao, wakaanza kufanya ngono tena.

Itaendelea.
 
SEHEMU YA 20

Nchini Australia Samuel hakuonekana kuwa na furaha hata mara moja, muda mwingi alikuwa akimfikiria mpenzi wake Catherine ambaye alikuwa amemuacha nchini Tanzania. Katika safari hii, Samuel hakuonekana kuwa na amani kabisa, muda mwingi alikuwa akionekana kuwa mnyonge kupita kawaida kiasi ambacho alijua kwamba kulikuwa na tatizo sehemu.

Wasiwasi ukaanza kumkamata kwamba ingewezekana kuwa nae alikuwa akienda kukamatwa katika kipindi hiki kutokana na madawa ya kulevya ambayo alitakiwa kuyasafirisha kuelekea katika nchi nyingine za barani Asia. Mara kwa mara Samuel alikuwa akiongea na mpenzi wake, Catherine simuni, alikuwa akimpenda sana na kumhitaji na ndio maana kila alipokuwa akielekea ilikuwa ni lazima aongee nae na kumjulia hali.
Moyoni mwake bado alionekana kuwa tofauti kabisa, hakujua sababu ambayo ilimfanya kuwa namna ile, ni kweli kila siku mapenzi yake yalikuwa juu ya mpenzi wake lakini katika kipindi hicho akaonekana kuwa na wasiwasi kupita kawaida.

Samuel alikaa nchini Australia kwa siku sita na ndipo alipoelekea nchini Thailand na kisha Mongolia na kurudi nchini Tanzania. Samuel alirudi huku akiwa ameingiza zaidi ya milioni mia tano kwa safari zake ambazo alikuwa amezifanya za kwenda katika nchi hizo kwa ajili ya kusafirisha madawa ya kulevya tu. Utajiri wake haukukoma, kila siku alikuwa akiendelea kuingiza fedha kiasi ambacho mpaka yeye mwenyewe alikuwa akijishangaa. Fedha hazikukoma, alijiona kama mtu ambaye alimiliki kisima kikubwa cha mafuta na hivyo alitakiwa kuingiza fedha kila siku katika maisha yake.

Alipofika nchini Tanzania akaonekana kuwa na amani, kitendo cha kumuona mpenzi wake kwa mara nyingine kilionekana kumpa furaha kupita kawaida. Kila alipokuwa akikaa nae, alikuwa akimmwagia mabusu mfululizo. Samuel hakuonekana kufahamu kitu chochote kile ambacho kilikuwa kikiedelea kwa wakati huo, kwake, aliamini kwamba Catherine alikuwa msichana muaminifu ambaye alikuwa akilitunza penzi lake katika kipindi ambacho alikuwa safarini.
Wote wawili walikuwa wakimuonyeshea unafiki mbele yake jambo ambalo linamfanya Samuel kutokufahamu kitu chochote kabisa, upofu mkubwa ukatawala machoni mwake, uaminifu mkubwa ambao alikuwa amemuwekea Catherine ulikuwa ni kazi bure kwani Sadiki alikuwa amekwishatembea nae na hivyo kumwambukiza ugonjwa wa UKIMWI.
Ndani ya nyumba hiyo walikuwa wakipokezana kufanya mapenzi na Catherine.

Katika kipindi ambacho Samuel hakuwepo nyumbani hapo, Sadiki alikuwa huru kufanya mapenzi na Catherine huku milango ikiwa imefungwa. Katika kipindi ambacho Samuel alikuwa akirudi nyumbani, alikuwa akilala nae chumbani kama kawaida.

Maisha hayo yaliendelea kila siku mpaka kufikia kipindi ambacho Sadiki akaona kwamba ilitosha na hivyo alitaka kuondoka mahali hapo kwani kwa jinsi hali ilivyokuwa ikienda aliona kwamba Samuel alikuwa njiani kugundua kila kitu ambacho kilikuwa kikiendelea kwao.

“Kwa nini unataka kuondoka mahali hapa?” Samuel alimuuliza Sadiki.
“Maamuzi, nimekaa sana hapa”
“Sasa unataka kwenda wapi? Nyumbani kwa wazazi wako uanze kwenda msikitini?” Samuel alimuuliza Sadiki.
“Hapana. Nataka kwenda kuishi hotelini” Sadiki alimwambia samuel.
“Hapana Sadiki. Mbona unakuwa hivi? Kuna nini ndani ya nyumba yangu mpaka unataka kuondoka kwenda kujiingizia gharama zisizokuwa na msingi?” Samuel alimuuliza Sadiki.
“Basi tu. Wakati mwingine najiona kutamani kubadilisha mazingira”
“Au shemeji yako kaanza chokochoko? Manake wanawake nao wakati mwingine wanakuwa wajinga sana” Samuel alimuuliza Sadiki.
“Hapana. Shemeji yupo peace sana ila nadhani natakiwa kubadilisha mazingira” Sadiki alimwambia Samuel.
Samuel hakuwa na jinsi, alichokifanya ni kukubaliana na Sadiki kwamba alikuwa akitaka kuondoka nyumbani hapo na kwenda kuishi sehemu nyingine tena. Alichokifanya Samuel ni kumchukua na kisha kuelekea nae katika hoteli ya New Africa iliyokuwa Posta na maisha yake kuanza huko.

Hiyo ikaonekana kuwa njia nyingine nzuri ambayo ilimfanya Sadiki kutanua sana na Catherine. Mara kwa mara Catherine aliposema kwamba alikuwa akienda chuoni wala hakuwa akifika huko na matokeo yake kwenda katika hoteli ya Kilimanjaro ambapo Sadiki alikuwa akitoka katika hoteli ya New Africa na kisha kukutana huko na kufanya mapenzi.
Hiyo ndio ilikuwa tabia ya Catherine, maisha yale yaliendelea zaidi na zaidi huku Samuel akiwa hafahamu kitu chochote kile kilichokuwa kikiendelea nyuma ya pazia. Kwake, kila siku aliona kwamba Catherine alikuwa na mapenzi ya dhati na wala hakuwa radhi kumtilia mashaka kwa kumuona kwamba alikuwa akitembea na mwanaume mwingine.

“Naona leo umekuja hotelini. Kuna demu mpya nini upo nae?” Ilikuwa ni meseji iliyotoka kwa rafiki yake, Issa, meseji iliyoingia katika kipindi ambacho alikuwa akitaka kuelekea bafuni kuoga.
Samuel akaiangalia meseji ile mara mbili mbili, akataka kuijibu lakini akaona kama angechelewa, alichokifanya ni kumpigia simu Issa ambaye akaipokea na kisha kuanza kuongea huku Issa akionekana kuwa na furaha.
“Unasema nimekuja hotelini! Hoteli gani?” Lilikuwa swali la kwanza ambalo aliuliza Samuel katika kipindi ambacho simu ilipokelewa na Issa.
“Ninaliona gari lako hapa nje ya hoteli ya Kilimanjaro, nikafikiri upo ndani. Au uliliuza?” Issa alimwambia Samuel na kisha kumuuliza.
“Gari gani?”
“Ile Prado yako ya bluu” Issa alimjibu.
“Ile gari nilimpa mpenzi wangu na anaitumia kwa sasa”
“Kwa hiyo ndio umekuja nae hotelini?”
“Hoteli gani? Mimi mbona nipo nyumbani na sijatoka toka asubuhi”
“Mbona naliona gari lako hapa”
“Gari gani?”
“Hiyo Prado”
“Mmmh! Nadhani umeichanganya kwani Catherine yupo chuoni kwa sasa” Samuel alimwambia issa.
“Mmmh! Ila ni gari lako bwana”
“Hebu angalia namba zake”
“Nimeziona. Ni T 2674 TUN. Au sio zenyewe” Issa alisikika.

Samuel akaonekana kushtuka, ni kweli maneno aliyoyaongea Issa yakaonekana kuwa na ukweli, namba za gari ambazo alikuwa amezitaja zilikuwa ni namba za gari lake ambalo alikuwa amempaka Catherine. Hapo ndipo maswali mengi yakaanza kumiminika kichwani kwake juu ya sababu iliyomfanya Catherine kuwa katika hoteli hiyo na wakati ulikuwa ni muda ambao alitakiwa kuwa chuoni.

Japokuwa alikuwa akitaka kuoga, akaamua kuahirisha na kisha kuvaa nguo zake na kuondoka chumbani. Moja kwa moja akalifuata gari lake na kuondoka mahali hapo. Akili yake ikawa imechanganyikiwa, kila alipojaribu kujiuliza swali, hakuwa na jibu lolote lile. Tayari akahisi kwamba kulikuwa na kitu kilichokuwa kikiendelea kwa wakati huo, alitaka kuwahi hapo hotelini hata kabla Catherine hakuondoka kwani kitu ambacho alikuwa akitaka kukifahamu ni kuona Catherine alikuwa na nani katika hoteli hiyo.

“Kwanza ngoja nimpitie Sadiki niende nae, na kama tukimkuta na mwanaume, atanitambua” Samuel alisema huku akiwa amekwishafika Jangwani, alikuwa akiendesha gari kwa mwendo wa kasi kuelekea katika hoteli ya Kilimanjro iliyokuwa Posta. Bado Samuel alionekana kama kuchanganyikiwa juu ya kile ambacho alikuwa ameambiwa na rafiki yake, Issa. Hakuamini kama kweli msichana wake, Catherine angeweza kwenda katika hoteli ya Kilimanjaro na wakati alimuaga vizuri kwamba alikuwa akielekea chuoni. Kadri ambavyo Samuel alivyokuwa akimfikiria Catherine na ndivyo ambavyo alishikwa na hasira zaidi na zaidi kiasi ambacho akaona kweli msichana hakutakiwa kuwekewa dhamana hata mara moja.

Ndani ya dakika kadhaa Samuel akawa amekwishafika ndani ya eneo la hoteli ya New Africa ambapo akateremka na kisha kuanza kuelekea ndani. Kwa wakati huo mwendo wake ulikuwa ni wa haraka haraka, hakutaka kwenda katika hoteli ya Kilimanjaro akiwa peke yake, alikuwa akitaka kwenda na swahiba wake, Sadiki ili aweze kumfumania vizuri Catherine huku shahidi akiwepo pembeni.

Alipofika mapokezi, akamuulizia Sadiki, mhudumu wa pale mapokezini akamwambia kwamba mtu huyo alikuwa ametoka kama dakika arobaini zilizopita. Samuel akaonekana kuchanganyikiwa, tayari shahidi hakuwepo, alichokifanya ni kuchukua simu yake na kisha kuanza kumpigia. Simu ya Sadiki haikuwa ikipatikana kabisa jambo ambalo lilionekana kumtia hasira zaidi.

Alichokifanya Samuel ni kuondoka mahali hapo na kuelekea katika hoteli ya Kilimanjaro. Kichwa chake hakikuweza kufikiria kwamba Sadiki ndiye ambaye alikuwa amesababisha Catherine kuwa ndani ya hoteli ile. Samuel hakuacha kumtafuta Sadiki simuni, alikuwa akiendelea kumtafuta zaidi na zaidi lakini majibu yalikuwa ni yale yale, simu haikupatikana.

Samuel hakutaka kwenda kuliegesha gari lake katika eneo la hoteli ya Kilimanjaro kwa kuona kwamba Catherine angeweza kuliona na kulijua, alichokifanya ni kwenda kuliegesha nyuma ya hoteli ile na kisha kuingia ndani ya eneo la hoteli ile. Kitu cha kwanza alichokifanya ni kuanza kuangalia ndani ya eneo la kuegeshea magari ndani ya hoteli ile, macho yake yakatua katika gari aina ya Prado ambayo alikuwa amemnunulia mpenzi wake kama zawadi.

“Upo wapi?” Samuel alimuuliza Issa simuni.
“Huku kwenye hiki kimghahawa” Sauti ya Issa ilisikika hali iliyomfanya samuel kukata simu na kuelekea huko ambapo akamkuta Issa akimsubiria.
“Umeliona?” Issa alimuuliza samuel.
“Nimeliona ila yeye mwenyewe simuoni” Samuel alimwambia Issa.
“Umemtafuta simuni?” Issa alimuuliza.
“Hapana. Tena umeongea jambo la maana sana. Ngoja nimcheki” Samuel alimwambia Issa na kisha kuchukua simu yake na kumpigia.

Simu ya Catherine ikaanza kuita. Kwanza iliita sana mpaka ikakata. Samuel hakuishia hapo, akarudia kupiga tena, simu ile ikaita na baada ya muda fulani simu kupokelewa na sauti nyembamba ya Catherine kusikika simuni.
“Halllow mpenzi” Sauti ya Catherine ilisikika.
“Hallow baby! Upo wapi?” Samuel alimuuliza Catherine kwa sauti ya upole, hakutaka kumuonyeshea kwamba alikuwa na wasiwasi.
“Nipo chuo”
“Utatoka saa ngapi?”
“Mmmh! Bado sijajua. Nafikiri mpaka saa kumi na mbili jioni” Sauti ya Catherine ilisikika.
“Sawa. Hakuna tatizo. Ukimaliza hakikisha unakuja mpenzi. Nimekwishakumiss mpaka nahisi kufa” Samuel alimwambia Catherine.
“Usijali” Catherine alimwambia Samuel ambaye akakata simu.
Samuel akaonekana kuvimba kwa hasira, hakuamini kama kweli mpenzi wake, Catherine alikuwa amefikia hatua ya kumdanganya namna ile. Akapiga ngumi mezani huku akionekna kuwa na hasira zaidi kiasi ambacho mpaka mishipa ikaanza kumsimama.
“Nikimkuta na mwanaume. Namuua” Samuel alimwambia Issa.
“Ngoja kwanza. Punguza hasira” Issa alimwambia Samuel.
“Nakwambiaje Issa, huyu malaya nitamuua. Nitamuua” Samuel alimwambia Issa.
“Ngoja tusubirie tuone nini kitatokea. Inawezekana kaja kunywa mara moja au kuonana na marafiki zake” Issa alimwambia Samuel.
“Haiwezekani. Atakuwa na mwanaume tu. Atakuwa na mwanaume tu huyu malaya” Samuel alimwambia Issa huku akionekana kuwa na hasira zaidi.
Samuel na Issa wakaendelea kusubiri mahali pale. Kuanzia saa nane mchana mpaka saa kumi na moja bado Catherine hakuonekana kutokea mahali hapo. Ilipofika saa 12:05, Catherine akaonekana akitoka ndani ya hoteli ile, Samuel akasimama na kisha kuanza kumwangalia, alikuwa ndiye yeye.
“Ngoja nimfuate” Samuel alimwambia Issa.
“Hapana. Ngoja kwanza” Issa alimwambia Samuel hali ambayo ilimfanya Samuel kutulia.

Walimuona Catherine akiingia ndani ya gari lake na kisha kuanza kuondoka mahali hapo. Samuel akashikwa na hasira zaidi, akawa katika hali ya kutaka kufanya mauaji tu kwa wakati huo. Kitendo cha Catherine kutoka ndani ya hoteli ile kilimuonyesha kabisa kwamba alikuwa na mwanaume ndani. Issa bado alikuwa akimsisitiza Samuel kuendelea kusubiri na wala hakutakiwa kuchukua uamuzi wa haraka mpaka pale ambapo angefanikiwa kumjua mtu ambaye alikuwa nae ndani ya hoteli ile. Wala hazikupita dakika nyingi, Sadiki akaonekana akitoka ndani ya hoteli ile. Kwanza Samuel hakuonekana kuamini kile ambacho alikuwa akikiona, akaangalia vizuri, alikuwa Sadiki.

Hapo ndipo ambapo picha ikaanza kumjia kichwani kwake, akaonekana kugundua kwamba Sadiki aliomba kuondoka ndani ya nyumba yake kwa kuwa alikuwa akihitaji muda zaidi wa kuendelea kutanua na msichana huyo kwani kama angeendelea kuwepo ndani ya nyumba ile wala asingeweza kupata uhuru.

Samuel hakuishia hapo, aliendelea kufikiria mambo mengi hata juu ya wasiwasi ambao alikuwa nao mara kwa mara alipokuwa nchini Australia juu ya mpenzi wake, Samuel alionekana kukasirika kupita kawaida.
“Sadiki anatembea na Catherine.....Sadiki anatembea na Catherine! Nitawaua!” Samuel alisema huku akionekana kutokuamini.
“Subiri kwanza Samuel. Hautakiwi kuwa na haraka ya kufanya maamuzi” Issa alimwambia samuel.
“Haiwezekani. Ni LAZIMA NIWAUE” Samuel alimwambia Issa huku akionekana kuwa na hasira.
“Sasa ukichukulia uamuzi wa haraka hautoweza kufanikiwa. Pata ushahidi kwanza”
“Ushahidi gani ambao wewe unataka mimi niupate zaidi ya huu? Unataka nipate ushahidi gani tena Issa?” Samuel alimuuliza issa.

Samuel hakutaka kuendelea kubaki mahali hapo, alichokifanya ni kuondoka huku akiwa na hasira kupita kawaida. Chuki ikaonekana kuanza kuchipukia moyoni mwake, alimchukia Sadiki na kumchukia Catherine pia. Upendo wote ambao alikuwa nao juu ya watu hao ukaonekana kupungua na mwisho wa siku kupotea kabisa. Samuel akaingia ndani ya gari lake, kichwa chake kilikuwa kimechanganyikiwa kupita kawaida. Hakuonekana kuamini kile ambacho alikuwa amekiona hotelini. Hakuamini kama urafiki wake pamoja na Sadiki, urafiki mkubwa ambao ulianzia shuleni ungeweza kuleta yale, hakuamini kama urafiki ule ungeishia kwa yeye kuwa na hasira na Sadiki na kutaka kumuua.

Samuel akaondoka moja kwa moja mpaka nyumbani kwake na kisha kutulia chumbani. Akajilaza kitandani, machozi yakaanza kumtoka. Moyo wake ulikuwa kwenye maumivu makali mno, wakati mwingine alijiona kuwa katika njozi na baada ya muda angeamka lakini ukweli ni kwamba ile haikuwa njozi bali tukio halisi ambalo lilikuwa limetokea katika maisha halisi.

Katika kipindi hicho ndipo ambapo mawazo yake yalipomrudisha nyuma kabisa katika kipindi ambacho alikuwa shuleni, kipindi ambacho alikuwa na urafiki mkubwa na Sadiki, siku ambazo alikuwa na uhusiano wa mapenzi na msichana Catherine ambaye alimfanya kumuacha Mungu na kuingia katika maisha ya kumtumikia shetani.

Katika kila kitu ambacho alikuwa akikifikiria mahali hapo kilionekana kumuumiza kupita kawaida, hakuamini kama matokeo ya urafiki wake na Sadiki, uhusiano wake na Catherine ungeishia namna ile. Samuel akaonekana kujuta, akajutia sababu ambazo zilimpelekea kuanzisha mahusiano na Catherine. Ukiachana na hilo, alijutia uamuzi wake wa kuachana na Mungu na wakati alikuwa na nafasi kubwa ya kubadilisha maisha yake.

Huku akiendelea kuwa katika lindi la mawazo, mara simu yake ikaanza kuita, alipoichukua na kuangalia namba, alikuwa Catherine. Kwanza hasira zilizidi kumkamata zaidi na zaidi, hakuamini kama Catherine angeweza kumpigia simu katika kipindi kama hicho. Kitendo cha kuliona jina lake tu kikamfanya kukumbuka kila kitu kilichotokea hotelini. Alichokifanya Samuel ni kujaribu kuzishusha hasira zake na kisha kuipokea.
“Upo nyumbani mpenzi?” Sauti ya Catherine ilisikika.
“Yeah! Umekwishatoka darasani?”
“Ndio. Leo tulikuwa tumebanwa sana na ndio maana nimechelewa kidogo kutoka. Ila usijali, nakuja” Catherine alimwambia Samuel.

“Usijali. Karibu sana laazizi” Samuel alimwambia Catherine na kisha kukata simu.
Samuel akaonekana kukasirika zaidi na zaidi, hasira ambazo alikuwa nazo zikaongezeka maradufu, hakuamini kama Catherine alikuwa akimwambia maneno ya uongo na wakati ukweli wote alikuwa akiufahamu. Alichokifanya Samuel ni kuchukua bunduki yake iliyokuwa kabatini na kisha kuanza kuiangalia.

Siku hiyo hakutaka kuchelewa wala kujiuliza, kitu ambacho alikuwa ameamua ni kumuua Catherine tu. Alitaka kuanza kumuua yeye na mwisho wa yote kuanza upya na Sadiki. Maumivu ambayo alikuwa nayo katika kipindi hicho yakamfanya kuwa na kiu ya kutaka kuua tu, hakutaka kumuacha Catherine aendelee kuishi na wakati alikuwa amemfanyia upuuzi wa kutembea na rafiki yake kipenzi, Sadiki.

Ndani ya dakika thelathini, Catherine akafika ndani ya nyumba hiyo. Kwa kitendo cha Samuel kumuona Catherine ndani ya nyumba yake akaonekana kupandwa na hasira zaidi lakini hakutaka kumuonyeshea dhahiri kwamba alikuwa amekasirika. Alichokifanya ni kumfuata Catherine na kisha kumkumbatia.

Ni kweli moyoni mwake alikuwa na hasira sana lakini ili apate kumuua vizuri Catherine hakutaka kuonyesha hasira zozote zile zaidi ya kumfanyia unafiki wa kumuonyeshea mapenzi ya dhati. Unafiki ambao alikuwa akimuonyeshea Catherine ukamfanya kutokugundua kile ambacho kilikuwa kikiendelea moyoni mwake.
“Ni lazima nikuue” Samuel alikuwa akijisemea kila alipokuwa akimwangalia Catherine ambaye hakuwa akifahamu kitu chochote kile.
Kama kawaida yake Catherine akaingia jikoni kwa lengo la kupika chakula cha usiku lakini Samuel akamkataza, hakutaka apike chakula chochote kile kitu ambacho kilionekana kuwa kigeni kwake.
“Vipi tena?” Catherine alimuuliza Samuel.
“Leo nataka tukale nje ya nyumba hii. Unapenda twende wapi?” Samuel alimuuliza Catherine huku akimsogelea na kisha kumkumbatia kwa nyuma huku mabusu mfululizo yakimtoka mdomoni mwake.
“Popote mpenzi”
“Chagua mpenzi”
“Popote pale. Utakapopapenda wewe basi na mimi nitapapenda” Catherine alimwambia samuel.
Katika kipindi chote hicho uso wa Samuel ulikuwa ukionekana kujawa na tabasamu pana alakini moyo wake ulikuwa tofauti sana. Moyo ulikuwa na maumivu makali sana, kila alipokuwa akimwangalia Catherine alionekana kukasirika kupita kawaida. Alikuwa na kila sababu za kumuua msichana huyo ambaye alionekana kuwa msaliti mkubwa sana katika maisha yake ya mahusiano.

Japokuwa kwa asilimia mia moja alikuwa akitaka kumuua msichana huyo lakini kwa upande mwingine moyo wake ulikuwa ukimkataza kufanya jambo lile kwa sababu lilikuwa na madhara makubwa zaidi. Japokuwa upande huo ulikuwa ukimpa ushauri mzuri lakini kwake ukaonekana kuwa ushauri mbaya sana ambao wala haukutakiwa kufuatwa.
“Kama upo tayari twende” Catherine alimwambia Samuel.
“Nisubiri” Samuel alimwambia Catherine na kisha kuelekea chumbani.
Alipofika chumbani, Samuel akakaa kitandani kwa muda, mawazo yakaanza kumjaa tena kichwani mwake, pande mbili moyoni mwake zikaonekana kushindana kwa wakati huo, Upande mmoja ulikuwa ukimtaka kumuua Catherine siku hiyo lakini upande mwingine wa moyo wake ulikuwa ukimkataza kufanya hivyo. Samuel akaonekana kupuuzia, alichokifanya ni kuchukua bunduki yake ambayo ilikuwa katika kdroo cha kabati lake na kisha kuondoka chumbani hapo.
“Hapana. Hebu ngoja” Samuel alisema mara baada ya kufungua mlango wa chumbani kwake kwa nia ya kutoka, akarudi tena.
“Kumuua kwa risasi noma. Ngoja nimuue kwa sumu” Samuel alijisemea.
Akarudi tena kitandani na kisha kufungua kidroo kile na kisha kutoa sumu aina ya Smothropheum, sumu kali ambayo ilikuwa ikitumika kuulia wadudu, sumu ambayo haikutakiwa kuguswa kwa mikono. Alichokifanya Samuel ni kuitoboa chupa ile na kisha kuimimina sumu ile katika kichupa kidogo, akakifunga na kisha kukiweka mfukoni.

Huo ndio uamuzi ambao aliuwa ameuchukua katika kipindi hicho, kumuua Catherine kwa sumu ile kali ambayo aliamini kwamba isingemchukua hata dakika kumi kupumua. Alipoona kwamba tayari ilikuwa katika kichupa kile, akatoka chumbani mule na kuelekea sebuleni.Catherine alikuwa sebuleni hapo, uso wake ulionekana kuwa na tabasamu kubwa kila alipokuwa akimwangalia Samuel ambaye nae alikuwa akimrudishia tabasamu pana ambalo lilificha hali ambayo alikuwa nayo moyoni mwake.

“Kama kunywa ngoja tuanze kunywa hapa nyumbani. Kule ni kwenda kula tu” Samuel alimwambia Catherine na kumtaka kuelekea jikoni kwa ajili ya kuchukua glasi.
Kitendo cha Catherine kuondoka sebuleni pale na kuelekea chumbani kilionekana kuwa kosa kubwa sana kwani hapo ndipo Samuel alipopata mwanya wa kuweza kuimiminia sumu ile katika chupa moja ya pombe ambayo alitaka kumpa Catherine anywe. Mpaka Catherine anarudi sebuleni pale, tayari Samuel alikuwa amekwishafanya kile ambacho alikuwa akitaka kukifanya.

Unafiki haukumuisha usoni mwake, bado alikuwa akiendelea kutoa tabasamu mbele ya Catherine ambaye alionekana kutokuwa na wasiwasi wowote ule. Alichokifanya Samuel ni kummiminia Catherine pombe iliyokuwa katika chupa ile na kisha yeye kuchukua chupa nyingine ambayo ilikuwa na pombe nyingine.
“Mbona hautaki kunywa pombe hii?” Catherine alimuuliza Samuel mara baada ya kuona anamimina pombe kutoka katika chupa nyingine.
“Hii yako nikinywa silewi. Hiyo kwa ajili ya wanawake kama nyie” Samuel alimwambia Catherine huku akimimina pombe ile katika glasi ile.
Catherine hakujua ni kitu gani kilichokuwa kikiendelea, kitu ambacho alikuwa akikifikiria ni kwamba bado Samuel alikuwa na mapenzi nae na bado alikuwa akiendelea kumuamini kama zamani na wakati mtu huyo kwa wakati huo alikuwa amebadilika kabisa, mapenzi ambayo alikuwa nayo juu yake yalikuwa yamekwishapotea kabisa ndani ya muda mchache kabisa. Catherine akanywa pombe ile.
“Bora ufe, haya ndio malipo yako malaya mkubwa” Samuel alijisemea moyoni huku akimwangalia Catherine ambaye alikuwa akinywa pombe ile.
Wala haukuchukua muda mrefu, Catherine akaanza kusikia kizunguzungu, akalishika tumbo lake na kulalamikia maumivu makali. Katika kipindi ambacho Cathereine alikuwa akilalamika kwa maumivu makali huku akimuomba msaada Samuel, ndio kwanza Samuel alikuwa amekaa katika kochi jingine, kakunja nne huku akiendelea kunywa pombe.
“Nisaidie mpenzi.....tumbo linaumaaaa....nakufa mpenziiiii.....” Catherine alilalamika kwa maumivu makali huku akijaribu kumsogelea Samuel kochini pale.
“Wewe kufa tu. Kila nafsi itaonja mauti” Samuel alimwambia Catherine.
“Nisaidieeeeeee....” Catherine alimwambia Samuel kwa maumivu makali lakini hakuonekana kujali kabisa zaidi ya kuendelea kunywa pombe yake.
“Nani akusaidie malaya mkubwa wewe. Hivi haukujua unacheza na mtu wa aina gani? Wewe kufa tu, yaani hapa wala sijuti kukupoteza mpumbavu mkubwa wewe” Samuel alimwambia Catherine huku akimtoa mkono ambao alikuwa amemshika pajani.
Catherine alikuwa akiendelea kulia kwa maumivu makali, mwili wake ukakosa nguvu na kisha kulala chali chini. Mapovu yaliyochanganyikana na damu yakaanza kutoka mdomoni huku akikipandisha kifua chake juu na chini na baada ya sekunde kadhaa kutulia tuli, alikuwa amekwishakata roho.

Samuel akaonekana kuridhika, tayari mtu ambaye alikuwa akitaka kumuua akawa amekwishamuua. Alichokifanya ni kusimama na kisha kumuwekea kidole Catherine puani kuona kama alikuwa akipumua, hakuwa akipumua. Huku akiwa amesimama na kujifikiria nini alitakiwa kukifanya, ghafla akashtukia honi ikipigwa getini. Kwanza akasimama na kisha kuangalia getini kupitia dirishani, mlinzi akafungua geti na kisha gari kuingia, alipoliangalia, lilikuwa gari la Sadiki.
Samuel hakuonekana kuamini kama alikuwa amerahisishiwa kazi namna ile, alichokifanya ni kuelekea chumbani kwake na kisha kuchukua bunduki yake, akaiweka kiunoni na kisha kurudi sebuleni. Kitu ambacho alikuwa akikitaka mahali hapo kilikuwa ni kumuua Sadiki tu kwani kazi ya kumuua Catherine ilikuwa imekwishafanyika na alikuwa amebakia Sadiki tu.

Samuel akasikia mlango wa gari ukifungwa na baada ya muda Sadiki kuingia sebuleni hapo. Kitu ambacho alikutana nacho ni mdomo wa bunduki ambayo aliishika Samuel. Sadiki akaonekana kushtuka kupita kawaida, hakuamini kama Samuel alikuwa amemuwekea bunduki bila kujua sababu yoyote ile.

“Ingia ndani kimya kimya mpuuzi mkubwa” Samuel alimwambia Sadiki ambaye akaanza kuingia ndani huku akionekana kushangaa.
“Kuna nini tena Samuel? “ Sadiki alimuuliza Samuel ambaye alikuwa nyuma yake huku mdomo wa bunduki ukiwa kichwani mwake.
“Mungu wangu! Samuel umemuua Catherine?” Sadiki alimuuliza Samuel kwa mshtuko mara baada ya kuuona mwili wa Catherine pale chini.
“Ndio nimemuua. Na baada ya dakika chache nakuua na wewe pia” Samuel alimwambia Sadiki ambaye akaonekana kuchanganyikiwa na kugundua kwamba Samuel alikuwa amejua kila kilichokuwa kimeendelea nyuma ya pazia.

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 21

Sadiki alikuwa akitoka kwa machale ndani ya hoteli ya Kilimanjaro. Macho yake yalikuwa yakiangalia huku na kule kwani hakutaka mtu yeyote amuone katika kipindi hicho. Kama kufanya mapenzi na Catherine alikuwa amekwishafanya nae sana na wala moyo wake haukuwa na majuto juu ya kumsaliti rafiki yake mkubwa, Samuel.

Tamaa ya mwili wake juu ya Catherine ilikuwa kubwa sana kiasi ambacho aliona hata kwa namna gani asingeweza kupigana nayo na kuishinda. Kama kumvua sketi Catherine alikuwa amekwishamvua sana na aliamini kwamba angeendelea kumvua hata kama ingetokea siku Samuel angemuona Catherine bado alikuwa na uhakika kwamba angeendelea kumvua sketi msichana huyo.

Akaondoka hotelini hapo na kuelekea New Africa ambapo moja kwa moja akaelekea katika chumba chake na kutulia. Muda wote Sadiki alionekana kuwa na furaha, hakuamini kama alikuwa na uwezo wa kumshawishi msichana ambaye alikuwa na jamaa yake mwenye pesa na kuwa nae. Kwake yeye, Catherine alionekana kuwa msichana mjinga kwa sababu alikubali kutembea nae na wakati alikuwa akifahamu fika urafiki ambao alikuwa nao kwa Samuel.

Kitandani pale alikuwa amejiachia huku uso wake ukiwa na tabasamu pana. Alikaa katika hali hiyo kwa dakika kadhaa, akainuka na kisha kuelekea bafuni ambapo akaoga na kisha kurudi chumbani pale. Baada ya hapo, akaiwasha televisheni iliyokuwa chumbani mule na kisha kuanza kuangalia filamu. Sadiki aliangalia filamu ile mpaka saa moja, akapata wazo ambalo kwake likaonekana kufaa sana.

Akasimama na kisha kuanza kuelekea kabatini, akachukua nguo zake nadhifu na kisha kuzivaa. Kitu ambacho alikuwa akikifikiria mahali hapo kilikuwa ni kumwambia Samuel kwamba walitakiwa waende sehemu kupata chakula usiku huo. Japokuwa alikuwa amemsaliti kwa mpenzi wake lakini Sadiki alikuwa akipenda sana kuwa karibu na rafiki yake huyo ambaye alikuwa akisaidiana nae kwa mambo mengi.

“Daah! Ila moyo unanisuta sana utafikiri mimi ndiye mtu wa kwanza na wa mwisho kufanya haya” Sadiki alijisemea huku akiwa amekwishavaa nguo zake. Saa moja na dakika ishirini akatoka chumbani mule na kisha kuelekea nje ambapo akachukua gari lake na safari kuelekea Mbezi Beach kuanza. Hakutaka kumpa taarifa Samuel kwa kuona kwamba iwe isiwe ni lazima akubaliane nae na kuelekea sehemu fulani kwa ajili ya kupata chakula cha usiku. Moyo wake bado uliendelea kumsuta kiasi ambacho akaanza kujisikia aibu yeye mwenyewe.

“Ikitokea siku akajua sijui itakuwaje! Nadhani hata urafiki wenyewe utakwisha siku hiyo hiyo” Sadiki alisema katika kipindi ambacho alikuwa akiendelea na safari yake huku akiwa amekwishafika Mbezi Beach.
Safari iliendelea zaidi na zaidi mpaka alipofika Africana ambapo akakata kona na kuanza kuingia ndani. Wala hakuchukua muda mrefu akawa amekwishafika katika eneo lililokuwa na nyumba ya Samuel na kisha kupiga honi ambapo mlinzi akatoka, alipoona kwamba lilikuwa gari la Sadiki, akalifungua geti na kuliingiza gari ndani.

“Kumbe yupo na mke wetu” Sadiki alijisemea mara baada ya kuliona gari la Catherine katika eneo la nyumba ile.
Sadiki akalipaki gari lile na kisha kuteremka na kuanza kupiga hatua kuelekea ndani. Kwa sababu alikuwa amekwishaizoea sana nyumba ile na kujiona kama kwake, wala hakupiga hodi, alipoufikia mlango, akaufungua na kuingia ndani. Sadiki akaonekana kushtuka kupita kawaida mara baada ya kuingia ndani na uso wake kukutana na mdomo wa bunduki ambayo alikuwa ameishika Samuel.

“Ingia ndani kimya kimya mpuuzi mkubwa” Samuel alimwambia Sadiki huku akionekana kuwa na hasira.
“Kuna nini tena Samuel?” Sadiki alimuuliza samuel huku akiendelea kuwa na mshangao wa kile kilichokuwa kikiendelea kutokea.
Sadiki hakuwa na jinsi, alionekana kushangaa sana lakini akaamua kufanya kama ambavyo Samuel alivyotaka afanye. Alipopiga hatua mbele zaidi na ndipo macho yake yakatua katika mwili wa Catherine ambaye alikuwa ametokwa na mapovu mdomoni, mapovu ambayo yalikuwa yamechanganyikana na damu.
“Mungu wangu! Samuel umemuua Catherine!” Sadiki alimuuliza samuel kwa mshtuko.
“Ndio nimemuua. Na baada ya dakika chache nakuua na wewe pia” Samuel alimwambia sadiki ambaye akabaki akitetemeka tu.

Samuel akamuamuru Sadiki kukaa kochini, Sadiki akafanya hivyo. Tayari uso wa Samuel ulionekana dhahiri kufahamu kila kilichokuwa kikiendelea, Sadiki alionekana kuchanganyikiwa, tayari alikiona kifo chake kikiwa kimekaribia. Hapo ndipo majuto yalipoanza kumuingia moyoni mwake, hakuamini kama urafiki wake na Samuel leo hii ungekuwa namna hii.

Samuel alionekana kuwa na hasira zaidi. Muda wote alikuwa akimwangalia Sadiki kwa macho yaliyojaa chuki kubwa, kwa jinsi alivyoonekana, kulikuwa na uwezekano wa kumfyatulia risasi muda wowote ule.
“Kwa nini umenifanyia haya?” Samuel alimuuliza Sadiki huku wakiwa wamekaa makochi tofauti.
“Nimefanya nini tena Samuel?” Sadiki aliuliza huku akijua dhahiri Samuel alimaanisha nini.
“Nisikilize Sadiki. Usitake kunifanya mimi mtoto. Najua unajua kabisa jinsi nilivyo, ninapoamua kuua huwa sijifikirii mara mbili mbili” Samuel alimwambia Sadiki.
“Samu........”
“Nadhani tunataniana na haujui kama nipo serious” Samuel alimwambia Sadiki na kisha kuikoki bunduki yake tayari kwa kumfyatulia risasi.
“No..no usifanye hivyo samuel. Ngoja nikueleze ukweli” Sadiki alimwambia Samuel huku akionekana kuwa na hofu.
“Ukweli gani unataka niufahamu? Nimekwishajua ukweli, kuna lipi jipya ambalo unataka nilifahamu? Umetembea na Catherine toka nilipokuwa nchini Australia, ukatembea nae ulivyojisikia, sasa unataka kuniambia ukweli upi? Au unataka kuniambia kwamba leo mlikuwa pamoja pale Kilimanjaro Hotel? Sema unataka kuniambia ukweli upi nisioujua?” Samuel alimuuliza sadiki kwa sauti ya juu huku akiwa ameanza kubadilika.
“Naomba unisamehe Samuel, ni shetani tu ndiye aliyenipitia kufanya haya ila kiukweli kwa jinsi tulivyo sikutakiwa kufanya haya” Sadiki alimwambia Samuel.

“Sadiki..Sadiki...yaani wewe ndiye wa kunifanyia haya? Urafiki wote tuliokuwa nao, mambo mengi tuliyofanya pamoja leo hii umekwenda kunifanyia haya? Nimekufanya nini Sadiki mpaka umeamua kuniumiza namna hii? Urafiki wetu wote tuliokuwa nao, ukaribu wote tuliokuwa nao umekwenda kunifanyia haya...kweli wewe wa kunifanyia haya Sadiki?” Samuel alimuuliza Sadiki kwa uchungu huku akianza kulia.

“Naomba unisamehe Samuel” Sadiki alimwambia Samuel huku akianza kupiga magoti.
“Sadiki, nimeangaika nawe katika mambo mengi mno. Ulipokamatwa nikafanya kila lililowezekana tena kwa kutumia fedha zangu mpaka wewe kuwa huru na wakati ulikuwa unakwenda kupotea. Eti vyote hivyo...yaani vyote hivyo haya ndio malipo yake? Yaani umeamua kunilipa kwa kuniumiza namna hii? Hebu jifikirie hata wazazi wetu wakijua kilichotokea watakuchukuliaje? Au nilifanya makosa kukukaribisha nyumbani kwangu? Au nilifanya makosa kukutoa katika mdomo wa serikali? Hebu niambie nilifanya makosa wapi?” Samuel alimuuliza Sadiki.
“Naomba unisamehe Samuel”

“Unafikiri msamaha unaweza kubadilisha kitu chochote kile? Unafikiri msamaha unaweza kunifanya niwe na furaha tena? Hapana Sadiki. Msamaha hautoweza kubadilisha kitu chochote kile, msamaha hautoweza kuniletea furaha wala kunifariji” Samuel alimwambia Sadiki.
“Naomba unisamehe Samuel. Hapa unavyoniona mimi ni mfu ninayetembea. Nimeathirika Samuel. Naomba unisamehe kwa sababu mimi tayari ni mfu” Sadiki alimwambia Samuel.
“Unasemaje? Umeathirika?”
“Ndio Samuel”

“Kwa hiyo ulitaka na mimi kuniangamiza? Umefanikiwa Sadiki. Hebu niambie, kuna sababu gani ambayo itanifanya mimi nikuache hai, hebu niambie, kuna sababu gani”
“Wewe ni rafiki yangu Samuel”
“Hapana. Rafiki yangu wa dhati hawezi kutembea na mpenzi wangu. Niambie kuna sababu gani ya kukuacha hai. Umetembea na mpenzi wangu, umemwambukiza UKIMWI na mimi pia nimeupata, hebu niambie kuna sababu gani ya kukuacha hai mtu kama wewe?” Samuel alimuuliza Sadiki.

“Naomba unisamehe Samuel” Sadiki alisema huku nae akianza kulia.
Bado Samuel alikuwa na hasira kupita kawaida. Alijua fika kwamba Sadiki alikuwa amemkasirisha sana lakini kila alipokuwa akimwangalia, kumbukumbu za urafiki wao zikawa zinamjia kichwani mwake, akajikuta akiingiwa na roho ya huruma kitu ambacho hakukitegemea.

“Nimekuelewa. Nimekusamehe ila nataka ufanye kitu kimoja” Samuel alimwambia Sadiki.
“kitu gani?”
“Ondoka na mwili wa mpenzi wako. Uchukue mwili huo uondoke nao. Utakapoondoka nyumbani hapa, usirudi tena. Huu ndio uwe mwanzo na mwisho kukanyaga mahali hapa, na kama iktokea siku umekanyaga hapa, nitakuua” Samuel alimwambia Sadiki.
“Nimekuelewa”

“Ukitoka nje, usiondoke na gari lako, tumia gari lake. Umenielewa?” Samuel alimwambia Sadiki.
“Nimekuelewa” Sadiki alimwambia Samuel.
Kitu alichokitaka Samuel kifanyike ndicho ambacho kikafanyika kama kuepuka kesi kwake. Sadiki akaubeba mwili wa Catherine na kisha kutoka nao nje na kuupakiza ndani ya gari la Catherine na kuondoka mahali hapo huku akiwa hajui ni kitu alitakiwa kukifanya juu ya mwili ule.
****

Samuel hakuonekana kuwa na furaha hata mara moja, mawazo yalikuwa yamemkamata kupita kawaida, kila alichokuwa akikifikiria kwa wakati huo kilikuwa kikimuumiza kupita kawaida. Kichwa chake kilikuwa kikimfikiria Catherine, alikumbuka mambo mengi ambayo alifanya nae mpaka katika kipindi ambacho alikutana nae kwa mara ya pili, hakuamini kama angeweza kumsaliti kirahisi namna ile na wakati alikuwa akimpa kila kitu alichokuwa akikihitaji.

Ukiachana na Catherine akaanza kumkumbuka rafiki yake ambaye alimchukulia kama ndugu yake, Sadiki. Moyo wake ukaumia zaidi, kitendo alichokuwa amekifanya Sadiki cha kutembea na msichana wake ambaye alitarajia kuwa mke wake kilimuumiza zaidi. Aliufikiria ukaribu ambao alikuwa nao pamoja na Sadiki, akafikiria mambo mengi ambayo alifanya na Sadiki, akabaki akiwa haamini kama mwisho wa kila kitu ungekuwa namna ile.

Hapo ndipo alipoanza kujuta, maumivu ambayo alikuwa akiyasikia moyoni mwake yakamfanya kukumbuka katika kipindi ambacho alikuwa akimtumikia Mungu. Katika kipindi kile alikuwa na amani, alikuwa na furaha lakini mara baada ya kuingilia mambo ya kidunia kila kitu kikaonekana kubadilika.

Maneno mengi ya nyuma ya wazazi wake yalikuwa yakijirudia kichwani mwake, katika kipindi hicho ndicho ambacho aliyaona maneno yale kuwa ya maana sana tofauti na kipindi kile. Hakujua afanye nini, alijiona kuwa katika wakati mgumu kupita kawaida.

Samuel akabaki katika hali ya mawazo kwa dakika kadhaa, akasimama na kisha kuanza kuzungukazunguka chumbani kule huku akionekana kuwa na mawazo kupita kawaida. Bunduki yake ilikuwa mkononi mwake huku akionekana kuwa na hasira. Ni kweli kwamba hata Sadiki alikuwa ameuumiza sana moyo wake lakini hakuona kama kulikuwa na sababu ya kumuua mtu huyo kwani walikuwa wametoka mbali na walifanya mambo mengi pamoja.

Ukiachana na mambo mengi, tayari Samuel akajijua kwamba alikuwa ameathirika na UKIMWI, ugonjwa ambao hakuwa akiupenda hata mara moja kwa sababu haukuwa na dawa hospitalini. Kwa wakati huo alikuwa akijiona mfu, alijua fika kwamba kulikuwa na siku ambayo angekufa kitandani, tena kifo kibaya ambacho kingempa sana mateso.
“Nisamehe Mungu” Samuel alijikuta akiongea na kisha kutoka nje huku akiwa na bunduki yake mkononi.

Akamuamuru mlinzi afungue geti na kisha kuondoka na gari lake, katika kipindi hicho, safari ilikuwa ni kuelekea nyumbani kwa wazazi wake. Hakuona kama kulikuwa na sababu ya kuendelea kubaki nyumbani kwake na wakati alikuwa katika hali hiyo ya mawazo, alijiona kuhitaji maneno ya faraja, maneno ambayo aliamini yangeweza kumpa nguvu tena.

Kutokana na foleni za hapa na pale, Samuel alichukua dakika arobaini mpaka kufika katika mtaa wa nyumbani kwao, Mwenge. Hata kabla ya kwenda katika eneo lililokuwa na nyumba ya wazazi wake, akalisimamisha gari lake na kuuegemea usukani wa gari lake na kisha kuanza kukumbuka mambo mengi ya nyuma.

Kila kitu alichokuwa akikifikiria mahali hapo kilionekana kumuumiza kupita kawaida. Nyakati za majuto zikafika maishani mwake, alikuwa akijutia kila sababu ambayo ilimfanya kumuacha Mungu na kuishi maisha ya dhambi. Katika kipindi hicho alikuwa akisikia msukumo mkubwa moyoni mwake ukimtaka kutubu juu ya kila kitu kibaya ambacho alikuwa amekifanya, amani ikatoweka moyoni mwake, alijiona kuwa mtu mwenye dhambi kuu ambayo haikuwa ikisamehekea.
“Nimekuja” Samuel aliwaambia wazazi wake mara baada ya kufika ndani ya nyumba hiyo, uso wake haukuonekana kuwa na amani, alionekana kuwa na wasiwasi sana.

“Mbona usiku hivi?” Mchungaji Mpelele aliuliza huku akishangaa, Samuel akaangalia saa yake, ilikuwa saa tatu na nusu usiku.
“Nimemtenda Mungu dhambi” Samuel aliwaambia wazazi wake ambao walikuwa wamekaa kimya.
“Kuna nini Samuel?” Bi Magreth aliuliza.
“Nimemtenda Mungu dhambi mama. Nimekuwa nikiyadharau maneno yenu ambayo mmekuwa mkiniambia katika maisha yangu. Nimekuwa nikiishi katika ulimwengu wa dhambi kipindi chote” Samuel aliwaambia wazazi wake na kuanza kulia.
Hicho ndicho kilikuwa kipindi cha majuto, katika kila chozi ambalo alikuwa akilimwaga mbele ya wazazi wake lilikuwa ni chozi la majuto, chozi ambalo lilisababishwa na mambo mengi ambayo alikuwa ameyafanya katika kipindi cha nyuma.
“Hebu tueleze kwanza, kuna nini?”
Hapo ndipo ambapo Samuel akaanza kuelezea kila kitu ambacho kilitokea katika maisha yake ya nyuma toka pale ambapo aliamua kwenda kuishi hosteli pamoja na Sadiki. Historia ya maisha yake ilionekana kumuumiza kila mmoja, Bi Magreth akashindwa kuvumilia, akabaki akilia tu kwani Samuel alionekana kupotea katika ulimwengu wa dhambi.
“Mungu anaweza kila kitu. Yakupasa kumrudia sasa” Mchungaji Mpelele alimwambia Samuel.
“Hapana baba. Acha niendelee na maisha yangu” Samuel alimwambia baba yake.
“Unayafurahia maisha ya huko?”
“Hapana”
“Unatamani kubaki huko?”
“Hapana”
“Sasa kwa nini usimrudie Mungu?”
“Ni ngumu baba”
“Hapana. Si ngumu kama ukiamua kurudi tena” Mchungaji Mpelele alimwambia Samuel.
Siku hiyo ilikuwa ni siku ya huzuni katia familia hiyo, historia ya maisha ya Samuel ilionekana kuwaumiza kupita kawaida. Mtoto wao ambaye alikuwa amepotea katika maisha ya dhambi akaonekana kupata ugonjwa hatari wa UKIMWI ambao uliendelea kuwa gumzo duniani. Ugonjwa ule ukaonekana kuwa malipo ya kila dhambi ambayo alikuwa ameifanya.
“Acha niendelee kuishi maisha yangu baba. Dhambi zangu zimekuwa nyingi mno” Samuel alimwambia baba yake huku akisimama na kuanza kuondoka mahali hapo.
“Sikiliza Samuel. Neno la Mungu linasema kwamba Hata kama damu zetu zitakuwa nyekundu kama bendera, Yeye atazisafisha na kuwa nyeupe kama sufi” Mchungaji Mpelele alimwambia Samuel ambaye alisimama na kisha kuondoka mahali hapo.

Samuel akaonekana kukata tamaa ya kuendelea kuishi maisha ya kumcha Mungu. Alijua fika kwamba endapo angeokoka na kumrudia Mungu basi biashara yake ya madawa ya kulevya alitakiwa kuachana nayo kwa sababu angekuwa mtu mpya kabisa. Samuel hakuonekana kuwa radhi kuiachia biashara ile ambayo ilikuwa ikimuingizia fedha kila siku, alionekana kuwa bora kufanya jambo lolote lile lakini si kucha kufanya biashara ile ambayo ilimpa fedha ambazo zilimfanya kuwa juu nchini Tanzania.

“Kama kufa acha nife tu” Samuel alijisemea katika kipindi ambacho alikuwa akiingia ndani ya gari na kuondoka mahali hapo huku ikiwa ni saa tano kasoro usiku.
****
Sadiki alionekana kuwa na wasiwasi, kila alipokuwa akiuangalia mwili wa Catherine alikuwa akiogopa kupita kawaida. Katika kipindi hicho alikiona kichwa chake kutokuwa sawa kabisa, usaliti ambao alikuwa ameufanya kwa rafiki yake ukaonekana kumuumiza kupita kawaida. Japokuwa katika kipindi cha nyuma alikuwa akikiona kila kitu kuwa kawaida lakini katika kipindi hicho alikuwa akiona mambo kumbadilikia.

Kama ilivyokuwa kwa Samuel, nae Sadiki akaanza kujutia kwa kila kitu ambacho alikuwa amekifanya katika maisha yake. Kwanza akaanza kukumbuka katika kipindi cha nyuma ambacho alikuwa akimtumikia sana Mungu, alipojitoa katika kila siku maishani mwake kuswali kwa kwenda msikitini na muda mwingi akiutumia kusoma Qur-an kitu ambacho kilikuwa kikimpa nguvu kusimama kwa Mungu na kupata nguvu za kupinga dhambi maishani mwake.

Hakuishia kuyafikiria mambo hayo tu, akaanza kukumbuka katika kipindi ambacho alikuwa akimuona baba yake akisimama mbele ya msikiti na kisha kuswalisha, mawazo yale yalimpa uchungu mkubwa moyoni, alijua fika kwamba baba yake alikuwa na ndoto nyingi za kumtaka yeye kuwa kama alivyokuwa katika maisha ya baadae, alijua fika kwamba baba yake alikuwa akijitahidi kufanya kila liwezekanalo ili aweze kuwa imamu kama ambavyo alivyokuwa lakini ndoto za baba yake zikaonekana kufutika mara baada ya kuangukia katika mapenzi ya Mariamu.

Mapenzi yakamfanya kumsahau Mungu, mapenzi yakamfanya kucha kabisa kuswali na kwenda msikitini, mapenzi yale yakamfanya kutokusoma kitabu kitakatifu cha Qur-an , mapenzi yakaonekana kumpoteza kabisa maishani mwake. Katika kipindi cha nyuma alikuwa akiona faida nyingi za kumtumikia Mungu, alijua kabisa kwamba moyoni mwake alikuwa na amani tele, moyoni mwake alikuwa huru bila ya kuwa na kifungo chochote kile lakini mara baada ya kuchagua kumtumikia shetani, kila kitu kikaonekana kubadilika, kuanzia mwilini mpaka moyoni.

Aliishi maisha ya kuteseka, bangi zikaonekana kumsumbua kupita kawaida, bila bangi hakuwa akijisikia amani moyoni mwake, bila kuvuta bangi hakuwa akijisikia kuwa mtu sawa. Kitendo cha kuangukia katika mapenzi ya Mariamu ndicho ambacho kikamfanya mpaka kuupata ugonjwa wa UKIMWI kutoka kwa msichana Zubeda ambaye alikuwa amefanya nae ngono sana, ugonjwa ambao alimwambukiza Catherine na Catherine kumwambukiza Samuel.

Kila kitu katika kipindi hicho kikawa kimebadilika, uamuzi mmoja wa kumuacha Mungu ukaonekana kumgharimu kupita kawaida. Machozi yalikuwa yakimtoka katika kipindi hicho, alikuwa akitamani sana kuwa na uwezo wa kuzirudisha siku nyuma ili aweze kuyabadilisha maisha yake lakini katika kipindi hicho alionekana kuchelewa mno.
“Nisamehe Allah!” Sadiki alisema huku akilia.

Kwa wakati huo alikuwa akielekea katika ufukwe wa Coco huku lengo lake likiwa moja tu, kuutelekeza mwili wa Catherine pamoja na lile gari. Aliona fika kwamba alitakiwa kufanya jambo lile kwani kwa kitendo cha Samuel kumuacha hai kililimfanya kumuona mtu huyo kuuthamini sana urafiki ambao walikuwa nao na ndio maana hakutaka kumuua kama alivyofanya kwa Catherine.

Alitumia dakika kadhaa mpaka kufika katika ufukwe wa Coco. Alichokifanya ni kuvua fulana aliyokuwa ameivaa na kisha kuanza kufuta alama zote za vidole katika kila sehemu ambayo alikuwa ameishika kwa mikono yake. Alipofuta garini akaanza kuufuta mwili wa Catherine, alipoona ameridhika, akaondoka zake huku akiendelea kulia kama mtoto.

Kila kitu kikaonekana kubadilika, hatua moja tu ya kuingia katika mahusiano ya kimapenzi na Mariamu ikaonekana kubadilisha kila kitu maishani mwake mpaka kumfikisha katika hali hiyo kwa wakati huo. Moyo wake ulikuwa kwenye maumivu makali kupita kawaida, kitu ambacho alikuwa akikitaka katika kipindi hicho ni kuwafuata wazazi wake na kuongea nao kwani hakuona kama kulikuwa na sehemu nyingine ambayo angeweza kupata maneno ya Mungu zaidi ya wazazi wake.

Kutoka Msasani mpaka Magomeni hakukuwa mbali sana, akafika nyumbani kwao na kisha kuingia ndani. Kitendo cha mama yake, Bi Asha kumuona tayari akajua kwamba kulikuwa na kitu ambacho kiliendelea kwa wakati huo. Sadiki hakuonekana kuwa mtu wa kawaida, Bi Aisha hakuzoea kumuona mtoto wake akiwa katika hali ile hata mara moja, alikuwa akilia huku macho yake yakiwa yamevimba sana.

“Kuna nini?” Bi Aisha alimuuliza huku akionekana kuwa na wasiwasi.
“Nimekosa mama. Nimemkosea Allah” Sadiki alimwambia mama yake, Bi Asha ambaye akatoka mahali hapo na kuelekea chumbani, akamuita mume wake, Ustaadhi Hamidu na kuja sebuleni hapo.
Kitendo cha Sadiki kumuona baba yake, maneno mengi ya hekima kama ambayo alikuwa akiambiwa katika kipindi cha nyuma na baba yake yakaanza kujirudia kichwani mwake kama kanda ya redio. Yalikuwa ni maneno makali ambayo yalikuwa yakimuumiza sana kwa wakati huo, maneno yale yalikuwa yakimfanya kujutia sana kila kitu ambacho alikuwa amekifanya katika maisha yake. Sadiki akapiga magoti na kuanza kuomba msamaha.
“Tumekwishakusamehe Sadiki, tumekusamehe kwa kila kitu. Ila kuna nini kimetokea?” Ustadhi Hamidu alimuuliza Sadiki huku akimnyanyua, Sadiki akaishika kanzu ya baba yake na kuinuka.
“Nimemkosea Allah, niliacha kuyafuata maneno ya Mtume Muhammad S.A.W na kufanya mambo ya kishetani” Sadiki alimwaambia baba yake huku akimwangalia usoni na kuendelea kulia zaidi na zaidi.
Muda wote Sadiki alionekana kuumia kupita kawaida. Maisha yake ambayo alikuwa ameishi mara baada ya kujiingiza kwenye mahusiano ya kimapenzi yakaonekana kuharibu kila kitu na ndio ambayo yalimfanya kuwa katika hali hiyo kipindi hicho. Sadiki alijiona kuwa mkosaji mkubwa katika maisha yake, alichokifanya ni kuanza kuwaambia wazazi wake kila kitu ambacho alikuwa amekifanya toka aondoke nyumbani pale.
Historia ya maisha yake ya nyuma ikaonekana kumuumiza kila aliyekuwa akiisikia, kila mmoja akawa na huzuni kupita kawaida. Sadiki akaonekana kupitia katika maisha yaliyojaa dhambi, maisha ambayo yalionekana kumuabudu shetani usiku na mchana. Sadiki hakujiona kama alikuwa na nafasi ya kubadilisha kila kitu maishani mwake na kumrudia Mungu.
“Yakupasa kumrudia Allah” Ustaadhi Hamidu alimwambia mtoto wake.
“Unafikiri nitaweza baba? Kumbukumbu za maisha yangu ya nyuma zitakuwa zikiniumiza sana” Sadiki alimwambia baba yake.
“Unaweza. Allah si kama binadamu, unapomkosea na kuamua kumrudia, anakusamehe na kuwa mtu mpya maishani mwako” Ustaadhi Hamidu alimwambia Sadiki.
“Ila biashara ya madawa ya kulevya itakuwaje?”
“Achana nayo. Hizo ni kazi za ibilisi ambazo amekuwa akikutumikisha bila kujijua. Mrudie Allah nae atakupa biashara nyingi za halali za kufanya” Ustaadhi Hamidu alimwambi Sadiki.
Kwa Sadiki ikawa tofauti na Samuel. Kwake, kila kitu alikiona kikiwa kimebadilika katika maisha yake. Ni kweli kwamba alikuwa amefanya mambo mengi sana ambayo kwake aliyaona kutokustahili kusamehewa hata mara moja, mambo ambayo yalimuumiza kila mtu ambaye angediriki kumwadithia. Katika kipindi hicho alitaka kurudi tena kwa Mungu wake, alitaka kurudi tena na kuomba msamaha kwa kila alichokuwa amekifanya.
“Ukiamua kwa moyo mmoja kumtumikia Allah, atakusamehe dhambi zako na kukufanya mpya” Ustadhi Hamidu alimwambia mtoto wake.
Sadiki akakubali kubadilika, kwa sababu alikuwa amezuiliwa kujihusisha na uuzaji wa madawa ya kulevya kwa miezi sita hilo wala halikuonekana kuwa tatizo, akaamua kuachana na kila kitu kuhusiana na madawa ya kulevya. Akaanza tena kuvaa kanzu kama zamani, akaachana na mambo ya wanawake, akaanza kuswali huku kila siku akilia kila alipokuwa akikumbuka maisha ya nyuma ambayo alikuwa amepitia.
Sadiki alitamani kuoa lakini kila alipokuwa akikumbuka kwamba alikuwa ameathirika hakuonekana kuwa na nguvu za kutafuta mke wa kuoa. Wazazi wake hawakujua hilo, wao walichokuwa wakifahamu ni kuhusiana na uuzaji wa madawa ya kulevya lakini hakutaka kuwaambia kuhusiana na ugonjwa wa UKIMWI ambao alikuwa ameambukizwa na msichana Zubeda.
Maisha yake yakawa yamebadilika, biashara ya madawa ya kulevya akawa ameiacha jumla na kushughulikia biashara nyingine ambazo zilikuwa na uhalali katika uso wa binadamu na mbele za Mungu pia. Sadiki akajitahidi kutoa misaada mbalimbali kwa watu waliokuwa na uhitaji wa kifedha au vyakula.

Huyo ndiye alikuwa Sadiki, akayabadilisha maisha yake kwa ujumla, hakutaka kumkaribisha shetani katika maisha yake, akawa mtu wa kuswali, mtu wa kuhudhuria msikitini na mtu ambaye alitamani sana kuwaambia watu kuhusiana na maisha yake mpaka kufikia kipindi hicho. Japokuwa alikuwa akimtumikia Mungu na kujitoa kwa kuwasaidia watu wengi lakini ukweli ukabaki vile vile kwamba alikuwa ameathirika kwa ugonjwa wa UKIMWI.
****
Watu walionekana kushtushwa na taarifa ambayo ilisema kulikuwa na maiti ya msichana ambayo ilikuwa imetelekezwa katika ufukwe wa Coco huku ikiwa ndani ya gari aina ya Prado. Taarifa zile ziliwashtua watu wengi ndani ya jiji la Dar es Salaam na kadri muda ulivyozidi kwenda taarifa ile ilizidi kuvuma sana.

Nchi ya Tanzania ikaonekana kuingiwa na mambo ambayo mara nyingi yalikuwa yakisikika katika nchi za Ulaya au Marekani. Wasichana wakaonekana kuwa na hofu kwa kuamini kwamba inawezekana muuaji alikuwa ameamua kuwauwa wanawake katika kipindi hicho.

Polisi wakafanya kazi yao kama inavyotakiwa kufanywa na kisha mwili kupelekwa Muhimbili. Simu yake ilipotumika kuwapigia marafiki wachache, ikagundulika kwamba hiyo ilikuwa maiti ya Catherine ambapo wazazi wake, Bwana Mushi na Bi Maria wakapigiwa simu na kutakiwa kufika katika kituo cha polisi.

Hiyo ikaonekana kuwa taarifa mbaya na nzito katika maisha yao, hawakutarajia kupokea taarifa kama hiyo, taarifa ya kifo cha binti yao waliyekuwa wakimpenda sana. Polisi walipochukua maelezo yake, wakamtaka mpenzi wake ambaye alikuwa akijulikana nyumbani, Edmund afike jijini Dar es salaam kwa sababu walikuwa wakitaka kumuuliza maswali kadhaa.

Katika kipindi ambacho Edmund alipewa taarifa juu ya kifo cha mpenzi wake, Catherine akaanza kulia kama mtoto, hakuamini kwamba msichana ambaye alikuwa akitaka kufunga nae ndoa ndani ya kipindi cha mwaka mmoja ndiye ambaye alikuwa ameuawa kinyama.

Alijua fika kwamba uhusiano wake na Catherine haukuwa mzuri lakini hiyo haikuwa sababu ya kumfanya kufikiria kwa Catherine hakuwa mpenzi wake, bado alikuwa akimpenda na kumthamini kama kawaida yake. Ndani ya basi Edmund hakuonekana kuwa na furaha hata kidogo, kifo cha mpenzi wake, Catherine kilikuwa kimegusa kupita kawaida.
“Kipindi cha mwisho kabla ya mahusiano yenu ilikuwaje?” Lilikuwa swali la kwanza ambalo aliuliza polisi huku akimwangalia Edmund machoni mwake.

“Mpenzi wangu alibadilika, alikuwa na mabadiliko ambayo yalitushangaza sisi sote” Edmund alimwambia.
“Unaposema sisi sote unamaanisha nani na nani?”
“Mimi, wazazi wangu na wazazi wake” Edmund alijibu.
“Yaliwashangaza kivipi?”
“Hakuwa akinijali kama ilivyokuwa zamani, hatukuwa tukiwasiliana kama ilivyokuwa zamani, alikuwa amebadilika sana” Edmund alimwambia polisi.
“Ulihisi nini kwa wakati huo?”
“Kiukweli kabisa nilihisi kwamba alikuwa na mwanaume mwingine, mwanaume aliyetokea kuuteka moyo wake zaidi yangu” Edmund alijibu.
“Mara yako ya mwisho kuwasiliana na marehemu ilikuwa lini?”
“Ilikuwa wiki mbili zilizopita”
“Mbona kipindi kirefu hivyo?”
“Kila nilipompigia simu hakuwa akiipokea. Jana tu nilimpigia sana simu, ila mara ya mwisho kuongea nae ilikuwa wiki mbili zilizopita lakini kuhusu kumpigia simu, nimekuwa nikifanya hivyo kila siku” Edmund alimwambia polisi yule ambaye aliandika kila kitu alichoona kustahili kuandikwa.
“Na vipi kuhusu gari?”
“Mmh! Sijui. Ninachokifahamu ni kwamba wazazi wake walimnunulia” Edmund alimwambia polisi yule.
“Hapana. Wazazi wake wamekataa kumnunulia. Haukumnunulia wewe?”
“Hapana. Sijawahi kumnunulia gari” Edmund alijibu.
Polisi walionekana kuchanganyikiwa, swali ambalo walikuwa wakijiuliza ni kuhusiana na gari ambayo alikuwa akiitumia Catherine ambayo alikutwa ndani akiwa ameuawa kwa kunyweshwa sumu. Kilichofanyika ni kwenda mpaka chuoni na kisha kuongea na marafiki zake ambao alikuwa akiishi nao ndani ya chumba chake na ndipo walipomtaja Samuel.
“Alikuwa mpenzi wangu na gari nilimnunulia mimi” Samuel aliwaambia polisi.
“Ok! Ulikwishawahi kugombana nae?”
“Hapana. Alikuwa ni msichana ambaye anajiheshimu na kujua kupenda sana. Ila katika siku za karibuni hakuonekana kuwa na furaha. Mimi kama mpenzi wake nilijaribu kumuuliza kuhusiana na hali yake lakini hakuniambia kitu. Nikaona bora niache tu kwani kuna siku niliamini angeniambia” Samuel aliwaambia polisi.
“Uhusiano wenu ulikuwa ukijulikana nyumbani?”
“Hapana ila ndio tulikuwa tukijiandaa kwenda kujitambulisha kwani mwaka kesho ilitakiwa tuoane” Samuel aliwaambia polisi.
“Ok! Bado tunaendelea na uchunguzi. Tutapakokuhitaji tutakuita” Polisi mmoja alimwambia Samuel ambaye akaingia ndani ya gari lake na kuondoka mahali hapo huku kwa muonekano akionekana kuwa na huzuni sana.
****
Siku zikaendelea kukatika, wiki zikasonga mbele kama kawaida, wote wawili waliendelea kuishi maisha ya kitajiri huku Sadiki akiwa amebadilika kabisa na kumrudia Mungu. Kwa Samuel, hakutaka kumrudia Mungu, kwake, alijiona kuwa na wakati mgumu sana kama angeamua kuachana na biashara ya madawa ya kulevya,. Bado alihitaji kuwa na fedha zaidi na zaidi.
Baada ya miezi kumi toka Sadiki amrudie Mungu, dalili za ugonjwa wa UKIMWI ukaanza kuonekana mwilini mwake. Alianza kwa kutapika na mwili kupungua. Japokuwa alikuwa na fedha lakini kamwe hakutaka kwenda kubadilisha damu Ulaya kama matajiri wengine walivyokuwa wakifanya. Kitu ambacho alikuwa akikisubiria kwa wakati huo kilikuwa ni kifo tu.
Alijua kwamba maisha yake hayakuwa maisha ya mtu mwenye dhambi tena, alijua fika kwamba alikuwa akiishi katika maisha matakatifu kwa wakati huo, alijiandaa kwa kila kitu, hakuonekana kuogopa kifo hata mara moja. Sadiki hakutaka kumficha mtu yeyote, alijua fika kwamba kuna watu wengi wangebadilika endapo wangemuona jinsi alivyokuwa akipungua.
Kwa wazazi wake ilikuwa ni kilio kila siku, hawakuamini kama katika kipindi hicho kijana wao, Sadiki alikuwa katika hali hiyo baada ya kuamua kumrudia Mungu na kuishi kama alivyokuwa akiishi zamani. Kila walipokuwa wakimwangalia, alionekana kuwa katika hali ya majuto mazito, alionekana kuumizwa na maisha yake ya nyuma ambayo alikuwa ameyaishi.
“Huu ndio mwisho wa kila kitu ila ninamshukuru Allah kwa kuweza kunirudisha na kuwa kama nilivyokuwa zamani” Sadiki aliwaambia wazazi wake katika kipindi ambacho alikuwa kitandani.
“Allah ndiye kila kitu, amini kwamba utakapofariki utakuwa umekwenda kupumzika sehemu salama” Ustadhi Hamidu alimwambia mtoto wake huku akionekana kuwa na uso uliokuwa na majonzi tele.
Hakukuonekana kubadilika kitu chochote, ugonjwa wa UKIMWI ulianza kumtafuna pale kitandani. Watu ambao walikuwa wakimfahamu walikuwa wakifika hospitalini pale na kumuangalia, Sadiki alionekana kuwa mifupa mitupu.
Japokuwa alikuwa katika hali hiyo lakini kila siku kitabu cha Qur-an kilikuwa pembeni mwake. Bado tegemeo lake lilikuwa kwa Mungu, bado alikuwa akijiona kufa na kuamini kwamba Mungu alikuwa amepanga kila kitu katika maisha yake.
Tarehe 13/4/2011 ndio ilikuwa siku ambayo Sadiki akafariki kitandani. Alifariki huku akiwa mifupa mitupu, UKIMWI ulikuwa umemtafuna kupita kiasi.
Kwa sababu alikuwa amejitengenezea marafiki wengi Tanzania, watu wengi wakajitokeza kumzika katika makaburi ya Kinondoni, mali zote pamoja na fedha zote ambazo alikuwa nazo akawaachia wazazi wake huku akiwataka kujenga vyuo vya madrasa pamoja na misikiti ambayo itatumika kumwabudu Mungu.
“Mungu akulaze Pahali Pema peponi” Ustaadhi Hamidu alisema katika kaburi la mtoto wake, Sadiki.
****
Ugonjwa wa UKIMWI ukaonekana kuwa kama malipo juu ya kila kitu alichokuwa amekifanya katika maisha ya dhambi, ugonjwa ule ukaonekana kama mshahara wa dhambi zake alizokuwa amezifanya katika kipindi cha nyuma. Mwili ukaanza kupungua, vipele vikaanza kuota huku nywele zikianza kunyonyoka kama kuku aliyewekwa kwenye maji ya moto.
Kila kitu katika maisha yake kikaonekana kubadilika mpaka kikafika kipindi ambacho alikiona ni bora kutengeneza maisha yake na Mungu. Alichokiamua Samuel ni kuwaita wazazi wake na kisha kumuongoza sala ya toba huku akiomba msamaha kwa kila kitu ambacho kilikuwa kimetokea.
Alikuwa na utajiri mkubwa lakini katika kipindi hicho alikuwa akiuacha mikononi mwa watu wengine. Alikuwa na biashara nyingi lakini nazo alikuwa akiziacha. Watu walibaki wakishangaa, kifo cha sadiki kilikuwa kimetokea siku chache zilizopita na leo alikuwa akiumwa Samuel ambaye nae alionekana kukonda kupita kawaida.
“Huu ni mshahara wa dhambi baba” Samuel alimwambia baba yake.
“Tunajua. Ila kwa sababu umeyakabidhi maisha yako kwa Mungu hakuna tatizo” Mchungaji Mpelele alimwambia mtoto wake, Samuel.
“Nimekuwa nikijuta sana katika maisha yangu, mapenzi yakaonekana kuniweka mbali na Mungu, nilianguka dhambini na hatimae nimekuwa hivi. Ni bora ningeendelea kuwa hata masikini lakini moyoni niwe na Mungu kuliko kuwa na mali halafu moyoni uwe na shetani. Inanuma sana baba kupoteza muda wangu kumtumikia shetani” Samuel alimwambia baba yake.
“Mungu anaweza, Mungu ameyabadilisha maisha yako, damu ya Yesu Kristo imeusafisha moyo wako” Mchungaji Mpelele alimwambia Samuel.
“Najua baba lakini najutia maisha yangu, najutia kila kitu kilichotokea katika maisha yangu ya nyuma. Haikutakiwa kuwa hivi” Samuel alimwambia baba yake.
Huo ndio ulikuwa muda wa kujutia kila kitu kilichopita. Baada ya Sadiki kufariki, baada ya mwezi mmoja nae Samuel alikuwa hoi kitandani. Biblia haikumtoka pembeni mwake, akawa mtu wa kusali kila wakati huku akiendelea kuomba msamaha kwa kila alichokuwa amekifanya.
“MIMI NI MWENYE DHAMBI NISAMEHE MUNGU” Samuel alisema huku akiwa ameikumbatia Biblia yake kifuani mwake.
Tarehe 27/6/2011 ndio ilikuwa siku ambayo Samuel akafariki katika kitanda ndani ya hospitali ya Muhimbili. Mauti ilimkuta huku akiwa amekumbatia Biblia kifuani mwake.

Mwili wake ulikuwa umekonda sana, vipele vilikuwa sehemu kubwa ya mwili wake, nywele zake zilikuwa zimenyonyoka kupita kawaida. Katika mazishi yake, wauzaji wengi wa madawa ya kulevya walikuwa wamekusanyika kumzika. Mama yake alikuwa mtu wa kulia tu, hakuamini kama angeweza kumpoteza mtoto wake katika umri mdogo ambao alikuwa nao.
Kila kitu katika maisha yao kikaonekana kufungwa, mali walizokuwa wamezipata zikawa mikononi mwa wazazi wao ambao walizitumia kuwasaidia watu pamoja na kufanya mambo mengine ya maendeleo. Majina yao yalikuwa makubwa nchini Tanzania, historia zao zikabakia kuwa miongoni mwa watu waliokuwa wamefanya biashara ya madawa ya kulevya kwa nguvu zote. Vifo vyao vilieleza kila kitu kwamba ‘MSHAHARA WA DHAMBI NI MAUTI’.

MWISHO.

Hadithi Imekwisha, wenye kujifunza natumaini wamejifunza. Naomba tukutane tena kwenye hadithi nyingine kali na ndefu iitwayo LETS CALL IT A NIGHT. Ni hadithi inayomuhusu msichana Maimatha ambaye ni muimbaji wa nyimbo za Injili na jamaa anayeitwa Henry ambaye ni mwandishi wa habari. Ni hadithi nzuri ambayo itakusisimua, itakufurahisha, kukuliza ila mwisho wa siku, itakufariji.

Hadithi hiyo itakuwa ikikujia kila saa kumi na moja jioni.
 
Back
Top Bottom