SEHEMU YA PILI
“Ni kwa sababu ya usalama wake. Halafu hii ni mimba yake ya kwanza, muache akajifungulie kwao” mke wangu akaniambia.
“Sawa. Nimeelewa”
“Utamsafirisha?”
“Ndiyo nitamsafirisha”
“Asante sana. Kwaheri”
Hapo hapo mke wangu akarudi katika hali yake ya kawaida. Akanitazama kisha akaniuliza.
“Mbona tumeketi?”
Ina maana hajui alichozungumza? Nikajiuliza.
“Nilikuwa nakusikiliza wewe” nikamjibu.
“Wanisikiliza mimi?” akaniuliza kwa mshangao.
“Una maana hujui ulichokuwa unazungumza?”
“Sijui, niambie nilikuwa nazungumza nini?”
Nikamueleza vile alivyozungumza.
“Labda nilipandisha shetani” akaniambia.
“Kwani wewe una shetani?”
Sakina akabetua mabega yake.
“Sijui” akasema.
“Hujawahi kupandisha shetani kabla ya leo?”
“Nilishawahi lakini zamani”
“Basi shetani wako amenieleza hivyo”
“Sasa umeelewa nini?”
“Nilichoelewa ni kukupeleka wewe Tabora ukifikisha miezi minane. Mengine sikuyaelewa”
“Labda una mwanamke anayenipiga vita, shetani wangu asingekwambia hivyo”
“Amini kwamba mimi sina mwanamke zaidi yako wewe mke wangu”
“Unajua mashetani wanaona. Asingekwambia hivyo isipokuwa kuna kitu amekiona”
“Labda kama wewe mwenyewe una mawazo hayo. Niliwahi kusikia mashetani husema kile kilicho moyoni mwa mtu”
“Mimi sina mawazo hayo. Kwani niliwahi kukwambia jambo kama hilo?”
“Basi tulale”
“Tusilale, nipeleke maliwatoni (chooni)”
Nikampeleka maliwatoni, tuliporudi tukalala.
Yale maneno ya shetani wa mke wangu niliyazingatia. Ujauzito wake ulipofikia miezi minane nikamsafirisha kwao Tabora.
Makubaliano yetu yalikuwa akae huko hadi atakapojifungua na kumaliza arobaini, ndiyo nimtumie nauli arudi Dar.
Mke wangu alipoondoka kwenda Tabora nikawa mpweke sana. Nikiondoka nyumbani asubuhi mara nyingi kurudi ni usiku. Nikimaliza shughuli zangu mchana ninakwenda kupiga stori na marafiki zangu hadi saa sita usiku.
Siku moja katika pitapita yangu nikakutana na mke wa yule rafiki yangu Machibya. Tulikutana karubu na soko la Ilala. Alikuwa anatoka sokoni.
“Vipi shem?” akaniuliza.
“Poa shem, za kupotea?”
“Nzuri, mwenzangu hajambo?”
Nilijua alikusudia mke wangu, nikamwambia.
“Hajambo lakini hayupo kwa sasa”
“Amekwenda wapi?”
“Amekwenda kwao Tabora kusalimia wazee”
“Atarudi lini?”
“Atachelewa kidogo”
“Sawa shem, haya kwaheri. Nawahi nyumbani nikamuandalie mzee”
“Nisalimie sana”
“Nitakusalimia sana”
Baada ya hapo tuliachana, kila mmoja akashika njia yake. Baada ya siku ile nikawa nakutana na yule msichana mara kwa mara. Alikuwa na mazoea ya kupita kwenye masikani yangu, mtaa wa Arusha ambapo palikuwa na ofisi yangu.
Kila alipopita alikuwa akisimama na kunisalimia. Na mimi humfuata na kusalimiana naye. Mazoea yalipozidi kunoga nikawa namsindikiza hadi nusu njia.
Kuna siku aliniomba namba yangu, nikamwambia mume wake anayo namba yangu.
“Nataka unipe wewe mwenyewe, siwezi kumwambia mume wangu anipe namba yako” akaniambia.
“Kwanini? Mwambie tu atakupa”
“Akiniuliza naitaka namba yako kwa ajili gani, nitamjibu nini?”
“Basi ngoja nikupe”
Nikampa namba yangu.
Aliijaza kwenye simu yake na kuniambia.
“Ngoja na mimi nikupe namba yangu”
Akaipiga ile namba yangu, simu yangu ikaita.
“Namba yangu ndiyo hiyo” aliniambia.
“Unaitwa nani?” nikamuuliza.
“Naitwa Nikole, na wewe unaitwa nani?”
Ilikuwa kama tunajuana sasa, nikamuuliza.
“Kumbe hujui jina langu?”
“Mume wangu ndiye anayelijua lakini mimi silijui, nakuita shem tu”
“Mimi naitwa Macheo”
“Nimefurahi kulijua jina lako”
Akaliandika kwenye simu yake pamoja na namba yangu.
Baada ya hapo tukaagana. Usiku wake akanipigia simu. Ilikuwa saa tatu usiku. Akaniambia.
“Hello Macheo!” Hakutumia tena neno shemeji.
“Oh shem, habari ya saa hizi?”
“Nzuri. Hilo jina la shem linachosha bwana, liache niite Nikole”
Nikacheka kidogo lakini tayari alishanipa wasiwasi. Nilikuwa najiuliza kwanini aniambie vile.
“Mzee yuko wapi?” nikamuuliza ili kutaka kujua kama alitamka vile mbele ya mume wake.
“Ametoka” akanijibu haraka.
Sasa nikapata jibu. Nikamuuliza tena.
“Amekwenda wapi saa hizi?’
“Achana naye. Tuzungume yetu. Unajua kuna kitu nataka nikwambie lakini naomba kiwe ni siri ya mimi na wewe”
Moyo ulinilipuka!
ITAENDELEA