Boniface Mwabukusi ni wakili ambaye pia ni rais wa chama cha wanasheria Tanganyika (
TLS) ambaye amekuwa mstari wa mbele katika kupigania haki za dinadamu, demokrasia na utawala bora.
Josephat Gwajima ni Askofu na mwanzilishi wa kanisa la 'Glory of Christ Tanzania Church' GCTC (Ufufuo na Uzima Ministries), kadhalika ni mwanasiasa ambaye mwaka 2020 alichaguliwa kuwa
mbunge wa jimbo la Kawe kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi CCM, ambaye pia ni mjumbe wa Halmashauri Kuu ya chama hicho Taifa (MNEC).
Siku za karibuni Askofu gwajima amekuwa mstari wa mbele katika kukemea vitendo vya utekaji pamoja na kutoa ushauri wa namna ya kukabiliana na vitendo hivyo. Pia
ameshauri viongozi wa serikali na Chama Cha Mapinduzi (CCM) kutoingia kwenye Uchaguzi mkuu 2025 bila kushughulikia malalamiko yaliyopo miongoni mwa makundi mbalimbali ya wananchi.
Madai
Zipo grafiki zinazosambazwa mtandaoni zikinukuu ujumbe unaodaiwa kuchapishwa na Mwabukusi katika mtandao wa X kuwa ameamua kuachana na chama chake cha NCCR Mageuzi kwa sababu chama hicho kinapanga kumteua Askofu Gwajima kuwa mgombea ubunge jimbo la kawe.
Uhalisia
Ufuatiliaji wa kimtandao uliofanywa na JamiiCheck kwa kutumia utafutaji wa maneno muhimu (Key word search) umejiridhisha kuwa taarifa hiyo si ya kweli kwani andiko lililonukuliwa halijachapishwa na Boniface Mwabukusi, bali ujumbe huo ni wa kutengenezwa na wapotoshaji.
Vilevile grafiki zilizotumika kusambaza taarifa hiyo zimeghushiwa na wapotoshaji kwani hazijachapishwa na vyanzo hivyo (Jambo Tv,
Habari Leo, na
Clouds Media) kama inavyoonekana.
Aidha kupitia ukurasa wake wa Instagram Clouds TV imekanusha grafiki iliyotumia utambulisho wa televisheni hiyo na kwamba haihusiki nayo.
Aidha kupitia ukurasa wake kwenye mtandao wa X, Mwabukusi
amekanusha taarifa hiyo na kwamba si ya kweli akisema yote yaliyoandikwa hahusiki nayo, hatimaye kuwataka wananchi kuipuuza.
"Puuzeni Ujinga Huu. Siyo kweli na yote yakiyoandikwa hayanihusu. Ninamuheshimusana Bishop Gwajima. Mimi Ni Mkristo niliyelelewa na kanisa. Nafahamu na kuheshimu watumishi wa Mungu. Rev. Bishop Gwajima ni Mtu ninayemuheshimu sana.. Ninatambua mapambano yake na hoja zake ninaziunga Mkono."