Gareth Frank Bale: Lulu ya Soka kutoka Wales

Damaso

JF-Expert Member
Jul 18, 2018
1,590
2,088
Gareth Bale, mchezaji wa soka kutoka Wales, mara nyingi huonekana kuwa ni moja ya hazina kubwa katika ulimwengu wa kandanda, haswa kutokana na ustadi wake wa kipekee, uimara, na uchezaji thabiti uwanjani umemfanya kuwa mtu wa kuheshimika sana katika mchezo wa soka. Ni ngumu kuzungumzia mafanikio ya Bale bila kumtaja mwamba Harry Redknapp ambaye ndo alimpokea kutoka Southampton mahala ambapo Bale alionesha makeke yake akiwa na miaka 16 tu, kijana wa miaka 16 aliwashangaza sana watu wa uwezo wake mkubwa wa kufukuza upepo na kuwakimbiza wachezaji wenzake.

bale.jpg


White Hart Lane ndipo alipoisugua vyema nyota yake na dunia ikamfahamu kijana mmoja kutoka Wales ambaye alikuwa ni ball dancer utadhani hautaki vile mpira, Bale aliufanya mchezo wa mpira uwe mtamu sana kama kaimati za Mama Abdul, kumtazama Bale akicheza ni kama unatazama game ya PS2 vile, kuanzia mwendokasi pamoja na mwamko wae wa kiuchezaji, kama unadhani Bale anaboa akicheza mpira basi kamuulie Marc Batra ambavyo alikimbizwa utadhani amesimama vile, Bale alifungulia turbo kama vile Max Verstappen akiwa kwenye mashindano ya Formula One.

bale2.jpg


Nikipewa kazi ya kutaja mawinga bora zaidi ndani ya Ligi Kuu ya Uingereza basi Bale lazma apate heshima yake, katika lile kundi la kina Cristiano Ronaldo, Mohamed Salah, Ryan Giggs , Eden Hazard, David Beckham pamoja na Robert Pires basi nitaweka nomino ya Gareth Frank Bale.

Ni Bale ambaye Ulaya alikuwa ni mwiba wa ajabu kwa timu kutoka mashirikisho mengine. Inter Mila wao walionja utamu na uchungu wa kucheza na winga kisheti, katika ligi ya mabingwa wa msimu wa 2010/11 Bale aliwacharaza Inter Milan vizuri na hat trick yake, Spurs ikiwa na hatari kubwa sana ambayo ndani yake ilikuwa na kina Peter Crouch na fundi wa mpira Roman Pavlyuchenko, nilijisemea kimoyo moyo kuwa mpira ni mchezo wa kikatili sana mara baada ya kumuona Júlio César akiwa haamini namna Bale alivyoweza kumtungua mabao matatu.

bale3.jpg


Bale nikukumbushe kuwa goli lako la pili kwenye ushindi wenu dhidi ya Manchester United wa magoli 3 kwa 2 ulikuwa ni ushindi wa heshima sana kwa Spurs kwani ulikuwa ni ushindi wa kwanza kwa Spurs katika Uwanja wa Old Trafford toka mwaka 1989. Vijana wa Sir Alex Fergusson wakina Ryan Giggs, Michael Carrick, Nani, Paul Scholes, pamoja na Shinji Kagawa wakatoka uwanjani wakiwa hawaamini kama Spurs imevuruga mipango.

p1hgaitytfdAW0cuf8.jpg


Jitihada na mapambano ya kijana fundi wa soka, yote haya yalitosha kumtoa mate Papa Perez ambaye alizama kwenye kibubu na kuweka pesa ili apate huduma ya mwamba huyu pale Los Blancos, mwezi Septemba 2013 basi Bale akavunja rekodi na akawa ni mchezaji ghali zaidi duniani kipindi hicho, kwa hakika Madrid waliona almas iliyotiwa nakshi na dhahabu ikionesha utamu wa soka ndani ya Uingereza.

GettyImages-96362415.jpg


Bale aliwasili Santiago Bernabeu akakutana na mafundi wenzake, wachezaji kama vile, Cristiano Ronaldo and pamoja na Karim Benzema ambao nao walikuwa kwenye viwango safi sana, Bale akapewa uzi wake na hapo kukazaliwa utatu mtakatifu maarufu kwa jina la BBC yaani Bale, Benzema pamoja na Cristiano, kumbuka hapo timu za Barcelona na Atletico Mardid waliona moto wa utatu huu kutoka Los Blancos.

GettyImages-963257930.jpg


Bale alitia jitihada kubwa na kushiriki katika kuipatia mafanikio makubwa klabu ya Real Madrid, akaiheshimisha jezi namba 11 ambayo iliwahi kuvaliwa na wachezaji wakongwe kama Michael Owen Arjen Robben pamoja na Ronaldo de Lima, wataalamu wa mpira watakwambia kuwa jezi hii ni jezi ya mahaba huko Uhispania walikuwa wakiitaja jezi ya Bale wa maneno ya “el viento del amor”, mataji matano ya UEFA Champions League pamoja na Mataji matatu ya Ligi Kuu ya Uhispania La Liga sio kitu cha kawaida kwa timu zingine kufikia kiwango hiki, ila kwa vijana wa Perez, Los Blancos ilikuwa ni kama kumsukuma Mlevi pale mlima kitonga au kula roast kutoka kwa Chef Nusret Gökçe mzee baba wa Salt Bae.

p1hgaigx2nvplcf0cuf8.jpg


Ukiwa na miaka yako 33 ukautangazia Ulimwengu kuwa umestaafu kucheza soka la kulipwa, kwa hakika ulijeruhi mioyo ya watu wengi, lakini ukatubariki kwa kufunga bao safi sana kwenye fainali ya kombe la MLS huko Marekani, yaani kifupi ulituonesha ubora wako, mfupa ulimshinda simba basi Fisi ukaupiga jino moja na kuwalaza chali Philadelphia Union, tulifurahi huku mioyo yetu ikiumia kwani hatutokuona tena ukiwatoa ulimi nje watu kama kina Marc Batra.

1027199-19054977-2560-9023.jpg


Umeacha alama kubwa katika soka haswa ndani ya Wales, taifa ambalo lilikuwa na ukame mkubwa wa kushiriki Kombe la Dunia toka mwaka 1958 ila Bale ukiwa kama Nahodha ukawapa furaha Wales na kuwapeleka Qatar ingawa mliishia kwenye makundi ila shughuli pevu ulituonesha, Bale ambaye ulimuadabisha vyema sana golikipa wa timu ya taifa ya Marekani, Matt Turner, mchuma mzito sana ambao uliwafuta machozi mashabiki wa soka wa Wales.

GettyImages-963257665.jpg


Asante sana Gareth Bale, umetupatia raha na furaha sana katika Ligi Kuu ya Uingereza na Uhispania, heshima yako! Shikamoo Bale! sitosahau ile bicycle kick yako uliyowachapa Liverpool!

parents-of-wales-gareth-bale-debbie-and-frank-in-the-stands-2CHA10K.jpg


Asanteni sana Frank, na Debbie Bale kwa kutuletea chuma hiki duniani! Asante sana Harry Redknapp kwa kuwa mwalimu wake bora na kumpa nafasi Bale kuiosha nyota yake!

White Hart Lane, na Santiago Bernabeu zitakukumbuka milele! Ishi sana Mwamba!
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom