Mohamed Said
JF-Expert Member
- Nov 2, 2008
- 23,158
- 33,791
View: https://youtu.be/K4wLDhyZc3M
Nimeweka hiyo santuri ya Frank Humplick kama utangulizi.
Nilikuwa napita tu mtandaoni nikakutana na hii santuri ya
Frank Humplick na dada zake wanaimba nyimbo ya Kichagga.
Nimerudi utotoni Moshi ya miaka ya 1950 namuona Frank Humplick
anaendesha pikipiki na nyuma kafunga gitaa lake.
Frank alikuwa mwanamuziki mkubwa pale mjini na kwa hakika Tanganyiika
nzima nyimbo zake zikisikika radioni na santuri zikiuzwa katika maduka
ya muziki.
Frank Humplick amepata kuniambia kuwa alitunga nyimbo za Kichagga
kama hii baada ya kuitwa na Chief Thomas Marealle na kumwambia kuwa
itapendeza watu kusikiliza nyimbo hizo.
Hii ilikuwa miaka ya mwanzoni 1950 na matangazo ya radio yameshaingia
Tanganyika mwaka wa 1952.
Frank Humplick alipata umaarufu mkubwa nyimbo zake zikipigwa Sauti ya Dar es Salaam.
Frank Humplick alikuwa akipiga muziki akiimba na dada zake wawili - Mary Regina
na Thecla Clara.
Frank Humplick alipata umaarufu zaidi pale Peter Colmore alipomshawishi kuja
Nairobi kuendelea muziki wake.
Peter Colmore alimtia Frank Humplick katika bendi Jambo Boys ambayo
wanamuziki wake walikuwa Fundi Kondo, Fadhili William na vijana wengine.
Peter Colmore alikuwa na kampuni akirekodi muziki na alikuwa mtu wa kwanza
Afrika ya Mashariki kurekodi santuri.
Haya alinieleza Peter Colmore nyumbani kwake Muthaiga mwaka wa 1995.
Nina mengi sana niliyokusanya kwa Peter Colmore kuhusu wanamuziki wa
wakati ule kama Mwenda Jean Bosco, Eduardo Masengo na Salum Abdallah.
Kuna nyimbo Mwenda Jean Bosco alimtungia Peter Colmore akiwa Nairobi.
Katika nyimbo hii Bosco anamtaja Peter Colmore na Eduardo Masengo.
Peter Colmore amenihadithia historia yao safari aliyofanya yeye na Masengo
hadi Congo kwenda kumchukua Mwenda Jean Bosco aje Nairobi kuitangaza
Aspro.
In Shaa Allah siku ikipatikana wasaa nitaeleza historia hii iliusababisha Mwenda
Jean Bosco wa Bayeke kutunga, "Shangwe Mkubwa."
View: https://youtu.be/bKwFQ6XINF4
Peter Colmore na Mwandishi 1995
Frank Humplick na Mwandishi