CHADEMA na CCM ugomvi wao mkubwa kwa Jiji la Arusha ni kuongoza halmashauri hiyo na kutoa meya,
CCM ina madiwani wanane wa kata, madiwani wa Viti Maalumu watatu na wabunge watatu ambapo jumla yao ni 14.
CHADEMA wenyewe wana madiwani watano wa kata, viti maalumu watatu na wabunge watatu, ambapo jumla yao ni 11.
Kama CHADEMA itafanikiwa kurejesha kata zake nne, itakuwa na madiwani wa kata tisa, wabunge watatu na madiwani wa viti maalumu watatu, hivyo kufanya idadi yao kuwa 15, hivyo kuwazidi CCM kwa diwani mmoja.
Idadi hiyo itawafanya wawe na uwezo wa kuongoza halmashauri hiyo na kutoa meya wa jiji hilo, kwani wakiingia kwenye baraza la madiwani wanaweza kumngoa wa CCM na kumchagua wa kutoka chama chao.
CCM wanaweza kulingana na CHADEMA kama watafanikiwa kumshawishi Diwani wa TLP, Michael Kivuyo, kuwaunga mkono kwenye kura za umeya, hivyo pande hizo kila moja kuwa na madiwani 15.
Kama hali itakuwa hivyo, pande hizo mbili zitalazimika kukaa kwenye meza ya mazungumzo kukubaliana utaratibu wa kuongoza halmashauri ya jiji kwa kupokezana kwa kipindi fulani.
Wachambuzi wa masuala ya siasa wamelidokeza Tanzania Daima kuwa uchaguzi wa kesho kutwa utakuwa mgumu zaidi kuliko ilivyowahi kutokea huko nyuma.
Tayari kuna taarifa kuwa idadi kubwa ya viongozi wa CCM wamepiga kambi mkoani humo kuhakikisha wanapata walau kata moja au mbili ili kuendelea kuiongoza halmashauri ya jiji hilo ambalo ni kivutio kikubwa cha utalii.